Hadithi: Kisu chenye mpini mwekundu

Hadithi: Kisu chenye mpini mwekundu

Kisu Chenye Mpini Mwekundu -7
RIWAYA: KISU CHENYE MPINI MWEKUNDU
MTUNZI: Ahmed Mussa Mniachi
SEHEMU YA SABA

Alijua wazi kuwa kama angesiki kuwa amechaguliwa na ameshindwa kuuendelea
angecheka sana. Alimchukia sana Mrisho kwani ndiye aliyemuanzishia majina mengi
mabaya darasani lakini hata hivyo majina hayo hayakuenea.
"We Beda unaenda wapi?" Akashituka baada ya kusikia sauti ya mama yake.
"He." Akashangaa baada ya kugundua kuwa alikuwa ameipita nyumba yao hatua
kadhaa. Alikuwa na mawazo mengi kiasi cha kukosa umakini na kutaka kupita nyumba
yao. Alijishangaa hata yeye mwenyewe kwa tukio lile.

* * *

Ulikuwa usiku wa manane. Mvua zilizoambatana na radi na upepo zilikuwa zinanyesha.
Beda alikuwa ametulia kitandani huku akiwa na hofu. Ilikuwa lazima awe na hofu.
Kwanza hakuwa na imani na nyumba yao kama ingeweza kuhimili vishindo vya mvua
ile, pili alisikia nyayo za mtu aliyekuwa anatembea karibu na dirisha la chumba chake.
Hofu ikautawala moyo wake. Nani tena? Alijiuliza Beda kwa sauti iliyojawa na hofu.
Moyo wake ulizidi kupiga kwa kasi. Usingizi ulipotea ingawa alikuwa amejifunika
shuka gubigubi. Ilikuwa lazima ajifunike.
Hisia kuwa kuna watu wanamchungulia kupitia matundu madogo ya nyumba ile
ambayo ilijengwa kwa tope zilizidi kumtia hofu. Wazo la kujifunua ghafla ili kujua ni
kina nani waliokuwa wanamchungulia lilipotea haraka sana.Alitamani sana kuwasha
kibatari lakini hakuthubutu. Alijipa moyo kuwa huenda ilikuwa ni ndoto.
Hakukubaliana kabisa na wazo hilo. Alikumbuka kuwa ni mara ya tatu sasa anashituka
usingizini na kusikia nyayo za mtu nje ya chumba chake.
Sasa haikuwa ndoto tena kwani alisikia dirisha lake likigongwa. Mapigo ya moyo
yaliongezeka kiasi cha kuweza kuyasikia mwenyewe. Liwalo na liwe, akajifunua.
Hakuona mtu wala watu. Akaamua kutoka ndani. Akafungua mlango na kwenda
kushuhudia kilichokua kinamsumbua. hakuna mtu. Akazidi kushikwa na hasira.
"Beda nipo hapa." Akashituka zaidi baada ya kusikia sauti ya kike. Akataka kukimbia.
"Usikimbie mimi Vick." Kweli ilikuwa sauti ya Vick. Alipoangalia vizuri akamuona Vick
akiwa ameegemea ukuta wa nyumba yao. Alikuwa anatetemeka kwa baridi. Hivi ni Vick
kweli au mzimu ule? Aliwaza Beda baada ya kuhisi kuwa ni jambo lisilowezekana Vick
aje usiku wa manane tena wakati kuna mvua, radi na upepo mkali. Kilichomshangaza
zaidi ni jinsi alivyoweza kutoka kwao kwani nyumba yao ilikuwa na geti kali. Akapiga
moyo konde akamsogelea. Bado Vick alikuwa anatetemeka.
"Vick."
"Bee."
"Mbona usiku?"
"Nimekuja kukuletea hela ya ada."
"Umepata wapi?"
"Nimeiba nyumbani."
"Si ungesubiri asubuhi."
"wakinikuta nazo!" Beda akashindwa kujibu. Sauti zao zilikuwa za kunong'ona. Bado
Vick alikuwa anatetemeka kwa baridi. Beda akamshika mkono akaingia naye ndani.
Vick akaingiza mkono wake kwenye sidiria yake ambayo ilikuwa imebeba matiti
madogo machanga akatoa noti za shilingi elfu kumikumi akamkabidhi Beda. Ahsante
sana Vick. Beda alimshukuru Vick kwa moyo wake wote. Kwa kuwa bado allikuwa
anatetemeka Beda akashikwa na huruma. Akamvutia kifuani akamkumbatia huku
akimfunika kwa shuka yake. Jinsi alivyokuwa na furaha ya kupata zile fedha hakuweza
kugundua kuwa yule msichana alilowa.
"Ahsante sana Vick sina cha kukulipa." Aliongea Beda kwa sauti iliyojaa shukrani ya
kweli.
"Nikusindikize?" Aliuliza Beda.
"Hapana nasikia baridi naomba nilale hapa hapa nitaondoka alfajiri."
"wazazi wako wakigundua."
"Usihofu wote wamesafiri, wameenda msibani Mahenge". Hakuwa na chaguo
akakubali Vick alale pale. Vick alikuwa amelowa lakini akalala na nguo zake. Beda
hakuona Shida kwani wakati ule Vick anakoroma Beda hakuweza kulala. Mawazo yake
yalikuwa juu ya maisha ya shule.
Kitu kimoja kikamshangaza. Licha ya kupita kwenye kipindi kigumu na cha matatizo
makubwa kitendo cha kukumbatiwa na Vick kilimpa faraja. Akashangaa, kwanini
kukumbatiwa kumemsahaulisha matatizo kedekede aliyokuwa nayo. Akapuuza na
kujivutia shuka.

* * *

"Vick, Vick… Amka uwahi nyumbani." Alishituka kutoka usingizini.
"Niko wapi?" Alishangaa Vick, Beda akacheka baada ya kugundua kuwa Vick alidhani
kuwa amelala nyumbani kwao. Alizidi kujishangaa baada ya kuona jinsi nguo zake
zilivyolowa.
"Lakini Vick unajua unanishangaza sana."
"Kwani vipi?"
"Umewezaje kutoroka bila kujulikana?"
"Nafikiri nimeshakueleza kuwa wazazi wangu wote wameenda msibani Mahenge"
"Hakuna mlinzi?"
"Hakuna." Alijibu Vick kwa mkato huku akishika komeo la mlango. Akaondoka huku
akimpungia mkono Beda.
Tukio lile lilimfungulia ukurasa mpya Beda. Alikuwa hajawahi kulala kitanda kimoja na
msichana toka apate akili timamu.
Akatembea kwa kunyata hadi kwenye mlango wa chumba cha mama yake. Akatega
sikio pale mlangoni. Akashusha pumzi baada ya kugundua kuwa mama yake alikuwa
anakoroma.
Hajui kitu.
Alifurahia moyoni.
Baada ya kurudi chumbani kwake kitu cha kwanza ilikuwa ni kuhesabu zile noti
alizopewa na Vick.
"Haaa." Alishituka kwa mshangao. Zilikuwa fedha za kitanzania shilingi Elfu sabini.
Hakuamini macho yake kama Vick anaweza kumfanyia mambo mazito namna ile.
Akaruka ruka kwa furaha. Matumaini ya kwenda shule yalikuwa makubwa. Furaha
yake iliendelea mpaka pale aliposhikwa na usingizi.
Beda akaamua kuwa muwazi kwa mama yake, aliamua kumsimulia tukio lote bila
kumficha chochote. Na ndivyo alivyofanya. Mama Beda akajikuta anashindwa
kumkaripia mwanawe kwani kwa kufanya hivyo angelazimika kuwa na fedha za kulipia
karo.
‘Huu umasikini ni chanzo cha mambo mengi.' Aliwaza huku akishindwa kujua iwapo
ashukuru au asikitike kwa tukio lile.

* * *

Asubuhi saa 3.30 ilimkuta mama Beda akiwa katika viunga vya shule ya sekondari
Benjamin Mkapa. Akaelekea moja kwa moja kule iliko ofisi ya waalimu.
Pale ofisini kulikuwa na walimu wachache, wengi walikuwa madarasani. Akawasalimia
wachache waliopo.
"Samahani dada nimekuja kulipa ada ya mwanangu, sijui tunalipia wapi."
"Fuata hiyo korido, kama anaanza nenda ofisi iliyoandikwa HEADMASTER kama
alishaanza nenda upande wakushoto mbele kidogo ya ofisi ya kwanza kuna ofisi
imeandikwa MALIPO." Alimaliza kuelekeza yule mwalimu wa kike.
Akatembea kwa haraka huku kandambili zikipigapiga miguu yake. Akagonga mlango
kwenye ile ofisi iliyoandikwa headmaster.
"Ingia." Alikaribishwa na sauti ya kike. Akafungua mlango. "Habari yako."
"Nzuri dada."
"Mkuu ana mgeni tafadhali msubiri hapo kwenye kiti akiondoka utaingia." aliongea
yule dada ambaye alikuwa anachapa kitu kwenye Kompyuta. Baada ya kuangalia vizuri
akagundua kuwa kulikuwa na chumba kingine mle ndani ambacho kilikuwa na
maandishi mlangoni MKUU WA SHULE. Akakaa kwenye kiti.
Baada ya dakika kumi mlango ukafunguliwa. Akatoka mzee wa makamo ambaye bila
shaka ndiye aliyekuwa anaongea na mkuu wa shule. Yule dada akamuashiria mama
Beda kwa mkono kuwa aingie ndani.
Huku moyo wake ukiwa na furaha akaingia ofisi ya mkuu wa shule. Aipofungua mlango
akamkuta mkuu wa shule akiwa ameenea kwenye kiti cha ofisi ambacho kilikuwa
kinazunguka kama vile vya saluni. Alikuwa ni mzee mweusi mnene mwenye mvi. Uso
wake ulikuwa mpana huku ukibeba mawani ya kusomea.
"Karibu." Sauti yake ilikuwa nzito kiasi ilimtia hofu mama Beda.
"Ahsante, shikamoo."
"Marahaba, enhe nikusaidie nini?" Mama Beda hakujibu badala yake akaingiza mkono
kwenye mfuko wa nailoni ambao ulikuwa mkononi mwake. Akatoa makaratasi
yaliyokuwamo mle ndani akamkabidhi yule mkuu. Mkuu akaweka sawa yale
makaratasi akaanza kuyapitia moja baada ya nyingine. "Mbona umechelewa sana
mama , hii nafasi naona kama imezibwa na mtu mwingine." Lilikuwa ni pigo lingine
akainamisha uso wake. Machozi yakaanza kumtoka. Mkuu wa shule akatulia hadi pale
alipojifuta machozi kisha akaendelea. "Labda uende ofisi ya elimu wilaya wao
wanaweza kukusaidia." Huku akiwa na majonzi mapya akaondoka pale ofisini
hakukumbuka hata kumuaga yule dada aliyempokea.

*****
Gervas Msangi aliinuka kwenye kiti akaanza kupekuwa hapa na pale akitafuta funguo
afunge ofisi. Alihangaika kwa muda wa dakika tano. Hatimaye akaziona. Wakati
anainuka pale kwenye kiti mlango wa ofisi yake ukagongwa. " Vipi bosi mbona kama
unataka kuondoka." Alisikika Zena muhudumu wa ofisi ya elimu. "Eeeh, kwani vipi?"
"Kuna kimeo huko chini unaweza kupata ya bia." "Usinitanie Zena leo nimepigika
kishenzi." Aliongea kwa kiherehere. "Ngoja nikuletee." akafungua mlango na kushuka
chini. Baada ya dakika chache ofisi ya Gervas afisa elimu taaluma ikagongwa. "Ingia."
Alisema huku akijiweka sawa kwenye kiti.
"Habari yako." Alisalimia Gervas baada ya kuona mama Beda amekaa kwenye kiti.
Wazo jipya likapita kichwani kwa Gervas. Aliweza kubaini kuwa huyu mama
asingekuwa na chochote cha kumridhisha. Shetani akamkalia kichwani. Akatabasamu
moyoni kwani mkewe alikuwa amesafiri.
"Enhe. Nikusaidie nini?" Aliuliza. Akampa zile fomu za mwanawe. akamsimulia hatua
zote alizopitia mpaka kufika hapo. Pia akamuelezea sababu zote za kuchelewa
isipokuwa ile ya kukamatwa na polisi.
Pale alipokaa Gervas alikuwa na wazo moja tu. Kweli alitaka kumsaidia huyu mama
lakini na yeye alitaka kukidhiwa haja zake. Tamaa zilimshika zikamhamasisha. Alikuwa
anatafuta namna mzuri ya kumshawishi yule mama ili aweze kukidhiwa haja yake.
Ilikuwa ni kawaida ya afisa huyo kutofanya kazi bure bila kupokea chochote mpaka
pale ofisini akapachikwa jina la mzee wa vimeo. Hiki kilikuwa kimeo kingine mbele
yake. Lakini kwa jinsi alivyo alijua wazi kuwa huyu mama pamoja na umbo na sura
nzuri alikuwa na dalili zote za maisha magumu. Umbo na sura yake vilimvutia. Duh.
Lakini analipa huyu. Ibilisi aliendelea kumpigia matari kichwani.
"Sawa, nimekusikia na nimekuelewa. Nitakutafutia shule nyingine ambayo iko karibu
kabisa na huko kwenu, umesema unatoka Mbagala eeh." Aliuliza baada ya mambo
kadhaa kupita kichwani mwake.
"Ndiyo baba."
"Sawa iko shule moja ya sekondari pale headmaster ni rafiki yangu, tutampeleka huko."
Mama Beda akajawa na furaha.
"Ili tuweze kupanga vizuri nitahitaji kuonana na wewe jioni ya leo kwa sababu huu ni
mpango mgumu kidogo tofauti na unavyofikiri."
"Wapi?"
"Tukutane pale White park Kiwalani"
"Mbona sipajui."
"We ukifika Kiwalani uliza tu iliko white park, ukija hapo nitakusaidia namna nzuri ya
kufanikisha mpango wako maana nataka niifanye kazi yako haraka kwa sababu kesho
kutwa nina safari ya kikazi mkoani.
"Ahsante baba." Alisikika mama Beda huku akiinuka kwenye meza.
Maskini hakujua dhamira iliyojikita kwenye nafsi ya afisa elimu yule.

* * *
Gervas nayeye hana staha anamuwazia Mama Beda maovu….. mama Beda
anatabasamu akijua kuwa huo ni wakati wake wa ukombozi…… nini kitajiri?

ITAENDELEA
 
Samahanini wadau mambo yamekuwa mengi sana kwa upande wangu aisee ndio maana huwa sitokei humu
 
Analyse toka huko gheto bila kukiacha kisu chenye mpini mwekundu.
 
Last edited by a moderator:
Hadithi nyingi huwa haziishi kwa wakati unaostahili nyingine haziishi kabisa'ina boa kichiz
 
Kisu Chenye Mpini Mwekundu -8
MTUNZI: Ahmad Mussa Mniachi
SEHEMU YA NANE

“Tukutane pale White park Kiwalani”
“Mbona sipajui.”
“We ukifika Kiwalani uliza tu iliko white park, ukija hapo nitakusaidia namna nzuri ya
kufanikisha mpango wako maana nataka niifanye kazi yako haraka kwa sababu kesho
kutwa nina safari ya kikazi mkoani.
“Ahsante baba.” Alisikika mama Beda huku akiinuka kwenye meza.
Maskini hakujua dhamira iliyojikita kwenye nafsi ya afisa elimu yule.
* * *
Maridadi ni miongoni mwa nyumba za kulala wageni ambazo zina sifa ya kupokea
wenyeji kuliko wageni. Iko karibu kabisa na reli ya Tazara. Watu wengi hupendelea
kufika hapo nyakati za jioni. Gervas Msangi hakuwa mzoefu sana wa eneo hili lakini
Ijumaa hiyo alijikuta akiwa mmoja wa wateja wa sehemu hiyo ambayo ilikuwa na baa.
Hakuwa mlevi wa pombe, alikuwa na ulevi wake mwingine kabisa. Baada ya kukaa
dakika kadhaa akijiburudisha na soda Gervas aliinuka na kuelekea mapokezi.
“Habari yako dada.”
” Nzuri shikamoo.”
“Ahsante, naweza kupata chumba?”
“Eeh. kulala elfu tano shoo taim elfu mbili.” Akatoa noti ya shilingi elfu tano
akamkabidhi yule muhudumu wa gesti.
“Enhe, jina…”
“Carlos Tevez.”
“Nani.?” Aliuliza tena yule muhudumu kwa mshangao.
“Nimekwambia Carlos Tarimo.”
“Ahaa. Nilisikia Carlos Tevez.” Akacheka kidogo baada ya kugundua ameongopewa.
“Nitarudi baadae kidogo.” Alisema huku akiondoka baada ya kupiga sahihi kwenye
daftari la kusajili wageni. Kabla hajafika mbali akarudi tena.
“Umesema chumba namba ngapi vile.”
“Namba kumi na moja.”
“Unaweza kunipatia funguo.”
“Hizi hapa lakini nakupa tu kwa kuwa nakuheshimu funguo zote zinatakiwa kubaki
hapa receiption iwapo mteja atatoka nje ya eneo letu.” “Poa naenda hapo White parks
nitarudi baada ya muda mfupi.” Akaondoka kwa haraka, alitamani apae.
* * *
Alikuwa na furaha kubwa baada ya kuahidiwa kusaidiwa na afisa elimu taaluma.
“Twende wote mama .” Alisisitiza Beda baada ya kutoa ombi hilo mara ya kwanza na
kukosa jibu. “Kaa hapa nyumbani kwani nauli haitatosha.” Aliongea mama Beda kwa
ukali kidogo.
Akafunga vizuri kanga yake ambayo nyuma ilikuwa na picha ya mgombea wa ubunge
wa jimbo lake. Akahakikisha kuwa amejiaandaa vizuri kadri ya uwezo wake.
Akaondoka na kumwacha Beda pale nyumbani.
****
Beda alikaa kwenye gogo la mnazi akamwangalia mama yake jinsi alivyokuwa
anaondoka kuelekea Kiwalani. Moyoni alitamani sana waongozane lakini kigezo cha
nauli kilichotumiwa na mama yake kilimkwamisha. Mama akatokomea…..
Ghafla, akazibwa uso na mtu asiyemfahamu. Akajaribu kupapasa kwa mikono yake.
“Sele..” hakupatia yule mtu aliendelea kumziba uso.
“Pita….” Bado hakupatia. Mtu aliyemshika akaangua kicheko. Akamtambua.
“Karibu Vick.”
“Ahsante, leo mama hayupo?”
“Mama kaenda Kiwalani.”
“Vipi mpango wa shule.”
“Ndio amefuatilia naona akirudi huko tutapata jibu kamili.” Alijibu Beda huku akisogea
pembeni kidogo ili Vick naye akae.
“Vipi ulifika salama? Maana toka juzi hatujaonana” “Nashukuru Mungu nilifika
salama.”
“Nilikukumbuka sana jana.” Aliongea huku akijishika shika vidole vyake.
“Hata mimi nilikukumbuka.” Aliongea Beda.
“Vile tulivyolala pamoja siwezi kusahau.”
“Utasahau tu.”
“Nitasahau kama utanioa.” Hapo Beda akashindwa kuvumilia akaanza kucheka.
“Tutaoana kweli? Mbona una mawazo ambayo hayaendani na umri wetu?”
“Lazima niwaze kwani ipo siku na mimi nitakuwa mkubwa na chaguo sahihi ni sasa
hivi.”
“Hatutakiwi kufikiria mambo ya ukubwani saa hizi.”
“Si kweli Beda mbona mwalimu anatuuliza ukiwa mkubwa unapenda kufanya kazi
gani, huoni kama anatuuliza mambo ya ukubwani wakati sisi ni wadogo?”
“Kwa hiyo unasemaje?”
“Kama angeuliza unapenda kuolewa na nani ningesema Beda.”
“Kweli unanipenda?”
“Nakupenda sana Beda na natarajia siku moja utakuwa mume wangu.”
“uhhff.” Alishusha pumzi Beda.
“Twende ndani.”
“Kuna nini?” Aliuliza Vick.
“Twende we utaona tu.”
“Mh, haya.” Alisikika Vick huku wakiingia ndani.

* * *

“Kwanini umenileta huku gesti?” Aliuliza mama Beda. “Usiwe kama mtoto mpenzi.”
“Haa. Mimi mpenzi wako?”
“Usijali mimi nitakusaidia tu.”
“Sijahitaji huu uchafu nataka mwanangu asome?”
“Unajua toka siku ile niliyokuona kwa mara ya kwanza nilikupenda sana ndio maana
sikuhitaji chochote zaidi ya penzi lako.”
“Kwa hiyo utanisaidia au hunisaidii?”
“Ukishanipa penzi nitakusaidia.”
“Hilo ndilo sharti lako?”
“Hilo tu.”
“Unaliona dogo, mbona sharti gumu sana.” Alilalamika mama Beda.
Mama Beda alikuwa hataki kabisa kuudhalilisha utu wake.
“Kwa hiyo utanipa hunipi?” Aliuliza Gervas
“Kwani siwezi kukupa fedha badala ya hicho unachohitaji?” Aliuliza.
“Hapana sihitaji fedha, mimi nina fedha zaidi yako” Aliongea huku akimshika shika
kifuani.
“Aah, niache bwana.” Gervas hakuisikia kauli hiyo. Aliendelea kumvua nguo yule dada.
“Niache bwana.” Sauti ilikuwa imefifia.

Ndani ya dakika tano alikuwa na nguo ya ndani tu.
“Hapana hatuwezi kufanya bila kinga.” Alilalamika mama Beda.
“Tukifanya na kinga siwezi kuku saidia.” Aliongea Gervas kwa msisitizo.
“Naomba unijibu swali moja kabla hatujafanya lolote.”
“Uliza nitakujibu.”
“Mkeo yuko wapi?”
“Mke wangu amesafiri amejifungua wiki hiihii hivyo ameenda kwao kupumzika.”
“Naomba utumie kinga basi.”
“Siwezi kula pipi kwenye mfuko.”
“Mh…..” Aliguna mama Beda. Alihitaji msaada…………

Itaendelea......
 
Wakuu naomba mniwie radhi,majukumu yanazidi kuwa mengi kwa upande wangu.
 
Wakuu kukikucha ntaiweka leo,alaf ntajitahidi niwe naitupia kila Ijumaa inshallah
 
RIWAYA: KISU CHENYE MPINI MWEKUNDU

MTUNZI: Ahmad Mussa Mniachi

SEHEMU YA TISA

“Ubwabwa mtamu, amepika nani?”
“Mimi.” Alijibu Beda.
“Mmmm, acha kujisifia amepika mama yako.” Aliongea Vick huku akijilamba vidole
vyake.
“Ahsante kwa chakula kilikuwa kitamu sana.” Aliendelea kumwaga sifa Vick. Beda
hakuongea chochote akatabasamu. “Naona muda umeenda wacha nirudi nyumbani.”
“Hautaki kusubiri umsalimie mama mkwe?” Hapo Vick akacheka mpaka jino la
mwisho likaonekana.
“Nitamwona siku nyingine, wazazi wangu wamerudi leo baba alikasirika alikuwa
anashangaa mbona hela zake zimepungua?”
“Hakukuuliza?”
“Hakumuuliza yeyote ana wasiwasi eti amepoteza kazini.” “Yaani, mama anatamani
sana kuonana na wewe.”
“Usijali ataniona tu kama tutaendelea kuwa hai.” Akajibu huku akimvutia Beda upande
wake. Akamkumbatia. Zilikuwa dakika mbili za hisia kali kwa kila mmoja.
“Kwaheri “
“Akaaga na kuondoka mle ndani huku akikimbia.” Huyo, huyoo….. Akatokomea gizani.
Beda akaanza kuingiwa na hofu baada ya kuona mama yake anachelewa
kurudi.Hakuweza kulala. Mama yake alikuwa mtu wa matukio mabaya, hakuweza
kusahau lile tukio la kuwekwa ndani mwezi mmoja na nusu. Aliogopa sana kwani
hakuamini kama jinamizi la matukio mabaya limeacha kuiandama familia yao.
Alikuwa anaingia na kutoka ndani. Asingeweza kutulia usiku kama ule. Kuna nini tena?
Alijiuliza bila kupata jibu. Aliangalia saa yake ya mkono ambayo mikanda yake
ilishaharibika, ilisomeka saa 4.23 Mama yake alikuwa hajarudi. Akaamua kulala bila
kufunga mlango wa kuingilia pale sebuleni.

* * *
Mama Beda alirudi nyumbani saa 6.30 usiku. Alikuta mlango ukiwa wazi. Akaingia
ndani akiwa amechoka sana. Akachukua ndoo ya bafuni akajaza maji kisha akaenda
kuoga. Alipooga akarudi na kukaaa kitandani. Machozi yakaanza kumtoka. Safari hii
hakulia kwa ajili ya udhalilishaji aliojifanyia, kilichomsikitisha ni adhabu kubwa
aliyompa yule afisa elimu. Yule alikuwa amejitakia mwenyewe mkewe Je. Hilo ndilo
lililomtesa alimuhurumia sana mke wa Gervas ambaye kaenda kujifungua huko kwao.
Fikra zake zikampeleka miaka kumi nyuma. Akakumbuka jinsi mumewe alivyoiaga
dunia. Akakumbuka jinsi alivyomuuguza muda mrefu. Akaanza kulia, alimhurumia
mtu ambaye hamjui, mke wa Gervas Msangi ambaye amemchukulia mumewe.
Akapapasa pale kwenye meza ndogo alikuwa anatafuta kiberiti. Hatimaye akakipata.
Akawasha kibatari, akatembea kuelekea kule lilikokuwa begi la marehemu mumewe.
Ndugu walimsusia kila kitu kwa madai kuwa yeye ndiye alimroga mumewe. Hakuwahi
kutembelewa na ndugu upande wa mume hata siku moja baada ya kifo kile.
Ndugu zake walikuwa Kigoma adha ya usafiri iliwafanya washindwe kuhudhuria hata
mazishi ya mumewe.
Alipekua lile begi akatoa karatasi mbili ngumu za rangi ya kaki. Akasoma karatasi ya
kwanza kisha akaiweka mezani. Akachukua ile ya pili, haikuwa na maelezo tofauti na ile
ya kwanza, tofauti ilikuwa ni majina yaliyotumika. Ile ya kwanza ilikuwa ni ya
marehemu mumewe na ile ya pili ilikuwa ya kwake. Jina Sakina Msomba, Result HIV
Positive. Alikuwa ni muathirika, alikumbuka vema jinsi alivyomuuguza mpaka
mumewe anakufa mikononi mwake. Mumewe hakuwahi kutumia dawa za kupunguza
makali hivyo alikufa mapaema. Alipoenda kuomba ajiunge akaambiwa CD4 zake
zilikuwa zinatosheleza kwa wakati huo hakuhitaji kujiunga. Akaishi hivyo kwa muda wa
miaka yote kumi. Baada ya kupata ile kashikasi ya kukamatwa na polisi hali yake
ilibadilika ikawa mbaya.
Ndipo alipoanza dozi rasmi pale hospitali ya Temeke. Ni siri aliyoijua mwenyewe na
madaktari tu. Leo amemuambukiza Gervas yule afisa elimu aliyekataa kutumia kinga.
Hakuona sababu ya kumueleza ukweli amembembeleza mara nyingi atumie kinga
hakutaka pia alijihisi kama aliyebakwa kutokana na hila aliyotumia afisa yule.
Angefanya nini?
Wazo moja lilimtesa, mke wa Gervas hakustahili adhabu ile. Afanye nini kumuokoa?
Lazima nimuokoe, siwezi kuacha mtu asiyehusika anapata adhabu asiyostahili, yule
mumewe amestahili kwani ilikuwa vigumu kumpeleka PCCB, ningethibitisha vipi kuwa
alihitaji rushwa ya ngono. Aliwaza mama Beda.
Nafsi yake yenye huruma haikutaka kusikia mwanamke mwenzake akipata mateso kwa
sababu ya ufuska wa mumewe. Akalala akiwa na azma ya kumuokoa Mke wa Gervas.
Nitamuokoaje? Ni swali lililopita kichwani mwake kabla hajapitiwa na usingizi.

* * *

Saa 1.30 Beda alienda kwenye mlango wa chumba cha mama yake. Akamsikia akiwa
kwenye mkoromo wa usingizi . Akashusha pumzi kisha akakusanya vyombo
alivyovitumia na Vick akakaa nje akaanza kuosha. Alikuwa na hamu kubwa ya kutaka
kujua nini kimejiri kuhusu mpango wake wa kujiunga na masomo ya sekondari.
Aliendelea kuosha vyombo huku akiimba kwa mluzi. Alipomaliza alivianika kwenye
uchanja kisha akarudi tena ndani. Wakati anaingia ndani akakutana na mama yake
mlangoni. Alikuwa anapiga miayo ya uchovu.
“shikamoo mama .”
“Marahaba ngoja nioge mwanangu tutaongea vizuri nikirudi bafuni.”
Beda aliingia ndani na kusubiri kwa shauku kubwa.
Dakika za kuoga zilikuwa chache lakini Beda aliona kama siku nzima. Siku zilikuwa
zinaenda wenzake walishaanza masomo. Akasubiri mpaka mama yake aliporudi. Mama
yake akaingia chumbani akabadili nguo kisha akaja pale ambapo wenyewe walipatumia
kama sebule. Kulikuwa na mkeka, kiti kimoja na kigoda tu. Beda aliona aibu pale
alipokumbuka sebule alizotembelea kwa rafiki zake. Kidogo ilimshangaza kuona Vick
mtoto aliyetoka kwenye familia yenye uwezo akiyakubali mazingira yale.
“Mama unabadili nguo mwaka nzima.” Alilalamika Beda
“Nakuja Beda mbona una haraka hivi?” Alisikika mama yake akiongea kutoka
chumbani.
“Enhe, imekuwaje huko mama ?” Aliuliza Beda kwa kiherehere baada ya mama yake
kutoka mle chumbani.
“Afisa elimu kanijazia hizi fomu tumebahatika kupata shule ya hapo jirani”
“Lini natakiwa kuanza?” Aliuliza Beda.
“Nikishapeleka hizi fomu nitapata jibu hukohuko.”
Aliondoka pale nyumbani huku akikabiliwa na mtihani mgumu kwa mke wa Gervas.
Atampata vipi ili amweleze ukweli wa mambo. Iwapo atamueleza kweli haitamletea
matatizo. Aliona wazi kuwa kuna hatari ya kushtakiwa kwa kueneza maradhi wakati
anajua wazi kuwa yeye ni muathirika. Lakini kama angeweka wazi kweli angepata ule
msaada? Angeupata vipi wakati Gervas alikataahata fedha. Kwanini Gervas ambaye
kafunga ndoa kanisani atake liwazo lingine nje ya ndoa? Labda haya ni malipo mazuri
ya usaliti. Hapana lazima nimuokoe mkewe, nitajibu nini mbele ya Mungu kama yule
mwanamke atakufa kwa ajili yangu? Alijiuliza maswali mengi bila kupata njia sahihi ya
kumnusuru mwanamke mwenzake.....

ITAENDELEA...
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom