Kisu Chenye Mpini Mwekundu-5
Sehemu ya tano
"Mh,makubwa.Yunifomu,vifaa vya masomo,ada na nauli juu...."Aliongea peke yake.
"vipi Mama Sanga mbona hivyo?" Aliuliza yule mama mtu mzima.
"Mwenzangu makubwa madogo yana nafuu,eti Beda kafaulu"
"Pole mwaya,majukumu ndo'yanaanza hivyo."Aliongeza yule bibi
"Mwenzangu ndio nimechanganyikiwa hapa hata sijui niingilie wapi."
Maneno ya mama yake yakaanza kumliza tena Beda.Huyu ndiye mtu pekee ambaye angeweza kumsaidia.
"Tangulia nyumbani nakuja" Alisikika mama Beda kwa sauti ya kukata tamaa.
* * *
Mvua kubwa ilikuwa imetulia na kuruhusu watu watoke majumbani mwao.Hali hii ilimuathiri sana mama Beda.Siku hiyo hakwenda kufagia barabara.Siku alizokuwa anapumzika ilikuwa kawaida yake kufanya biashara ndogondogo kama hii ya muhogo.Lakini leo alikuwa ameangukia pua,hakunusa wala hakupumua.Hakuna aliyekuja kununua muhogo zaidi ya watu watatu wa kwanza ambao walikuja kabla mvua haijaanza kunyesha.
Beda Sanga alitoka ndani ya nyumba ile ambayo haikuweza kuwasitiri vizuri kwa mvua kwani ilikuwa inavuja.Akajisogeza karibu na mama yake ili aweze kusikia lolote ambalo lingempa matumaini ya kwenda shule.Alijionea wazi ugumu wa biashara ya mihogo.Aliiona wazi huzuni iliyokuwa kwenye macho ya mama yake.Akukumbuka jinsi mama yake alivyoenda kuomba msaada kwa jirani yao ambaye anauwezo kidogo.
"Mama uliambiwa nini ulipoenda kwa mzee Uwesu?" Ilikuwa kama aliyemtonesha,mama yake hakujibu badala yake akaanza kulia kilikuwa kilio kamili.Huku akiwa katika hali ya kwikwi akaamwomba mwanae amsaidie kunyanyua vyombo warudishe ndani.Hakukuwa na biashara tena.Ilikuwa ni hasara tupu.Beda akaendelea kudadisi mama hakutaka kujibu.Akarudisha fikra jinsi alivyoenda kuomba msaada kwa Mzee Uwesu
"Baba mwanangu amefaulu naomba msaada wa mchango wenu kama inawezekana." Alikumbuka vema maneno hayo mara baada ya salamu
"We mama husinletee uchuro hapa kwani huko mnakofanya uchawi wenu hakuna michango.Kwa taarifa yako nakujua sana kuwa ni mchawi mkubwa hapa mtaani ndio maana huendelei,umemuua mumeo makusudi leo unakuja kutaka msaada kwetu?"
Baada ya maneno hayo Mama Beda akaondoka bila kuaga huku akilia.Hakutaka kabisa kumsimulia Beda mambo yale.
Usiku huo huo pamoja na kilio chake bado hakukata tamaa.Akaenda kwa Diwani wa kata yao.
"Hodi,hodi...." Alibisha hodi nyumbani kwa diwani.
"Karibu.." Sauti ya kike ilijibu kutoka ndani.Akafunguliwa
"Karibu ndani".Akamfuata yule binti ambaye mikono yake ilikuwa imelowa maji,bila shaka alikuwa anaosha vyombo muda huo.
"Karibu ukae." Alikaribisha binti huyo ambae alionekana wazi ni 'house girl'
Akakaa kwenye moja ya sofa za thamani zilizokuwepo pale sebuleni.Akaruhusu macho yake yaisanifu sebule ile.Thamani ya kile kiti alichokalia tu ingetosha kabisa kutatua matatizo yake yote ya ada na vifaa vya shule.Alistaajabu ukubwa na uzuri wa sebule ile.Akastaajabu zaidi kuona samaki ambao walikuwa wanafungwa kwenye kabati maalumu la vioo pale sebuleni.Hakumaliza kuisanifu sebule ile,diwani alifika pale sebuleni.Mzee Athumani Kipande diwani wa kata ya Charambe alikaa kivivuvivu katika moja ya viti vilivyokuwemo mle sebuleni.Alikuwa mzee mfupi mwenye mvi chache,mazingira ya nyumbani alipenda kuvaa sana msuli na kizibao
"Karibu mama" Aliita kwa mazoea tu kwani kiumri alikuwa mkubwa kuliko yule mama aliyekuwa mbele yake
"ahsante,shikamoo."
"Marhaba habari za nyumbani?"
"Nzuri kiasi baba"
"Kwanini kiasi?"
"Ahh." Alijikuta akishindwa kuongea na badala yake akaminyaminya vidole ambavyo vilikuwa vinatoa mlio kama vijiti vidogo ambavyo vilikuwa vinavunjika.Hatimaye akaamua kupasua jipu
"Baba nimekuja unisaidie juu ya swala la mwanangu,amachaguliwa kuijiunga na shule ya sekondari."
"Msaada gani unaihitaji?" Aliuliza diwani.
"Ili aweze kuanza masomo ninahitaji shilingi elfu arobaini kwani tayari mwenyewe ninayo shilingi elfu ishirini.Aliongea mama Beda huku hali ya kujiamini ikiongezeka.
"Aah,samahani mama unajua wiki hii kuna kundi la ngoma za kienyeji linakuja kutoka Botswana kwa hiyo akiba yangu nitaitumia huko mimi na familia yangu maanakiingilio kwa familia yote ni laki nne."Akatulia diwani na kumwangalia mama yule kwa jicho lililokosa huruma.Moyoni mama Beda alilaani sana kauli ile bora hata hasingeambiwa
Akanyanyuka pale kwenye kiti na kumuaga diwani wake.
Hizo zote zilikuwa kumbukumbu za siku mbaya ambazo zinapita katika maisha yake.Alisononeka sana moyoni.Ngalawa ya mawazo ikamfikisha kwenye mawimbi ya siku zile tamu ambazo alikuwa uhusinao mzuri na diwani yule.akakumbuka jinsi alivyoimba na kucheza ili diwani apate ushindi.Kumbukumbu zikamfikisha siku zile zenye ugwadu ambazo alipewa kitenge kipya cha waksi kutoka kwa mbunge mtarajiwa huku wakiongezewa na maji na soda kutoka kwa diwani wao.Akatikisa kichwa.
* * *
Ni siku nyingine saa 7:30 ilimkuta mama Beda akiwa na beseni lake la mahindi ya kuchemsha maeneo ya Mtongani.Ilikuwa ni katika jitihada zake za kuhakikisha Beda anaenda shule.Kidogo siku hii ilikuwa nzuri kwake kwani alibakiza mahindi mawili tu.Akaendelea kuzunguka maeneo ya pale kituo cha magari,hatimaye akamaliza.
Akaanza kuhesabu alichikipata.Ilikuwa ni shilingi elfu kumi na nne na mia saba.Akatoa elfu kumi aliyonunulia mahindi,elfu nne mia saba akaweka kibindoni.Akatembea taratibu kuelekea nyumbani.Hakutaka kupanda gari kwani faida ilikuwa ni ndogo mno.Hatimaye chakara chakara za miguu zikamfikisha Mbagala rangi tatu.Bado mjeledi wa kashfa iliyotolewa na jirani yake uliendelea kumtesa ndani ya nafsi yake.Inamaana hapa mtaani ndio ninavyotafsirika,etu nimemuua mume wangu!Aliwaza na kusikia fundo likiushika moyo wake kwa uchungu
Akatua beseni lake kisha akaingia ndani.Hakujua alifuata nini ndani akaamua kutoka.
Hakugundua njaa aliyokuwa nayo kutokana na fikra nzito alizokuwa nazo.Akakaa chini ya mpera,bado jinamizi la shutuma za jirani yake liliendelea kumuandama.Fikra zake zikamfikisha kwa marehemu mumewe.Hawakuwa na maisha mazuri lakini hasingeweza kushindwa kumlipia ada mwanae.Kitu kikamshika kooni.Akaanza kulia.
"Heheee,mumewe kamuua mwenyewe leo anamlilia." Kicheko cha Mama Suzi mke wa jirani yake kikamzindua.Akageuka na kumwangalia kwa hasira.Mama Suzi ambaye alikuwa anamwaga takataka kwenye kiwanja wa Mama Beda akaondoka huku akishusha maneno ya majigambo."Hunifanyi lolote nimeaga kwetu,umemuweza huyo huyo mumeo."Aliendelea kumwaga maneno ambayo yalimuumiza Mama Beda.Mama Beda alishindwa kuvumilia akaokota chupa ya konyagi akaanza kumfuata jirani yake huyo.Mama Suzi akaanza kukimbia huku akiangusha ndoo ya takataka ambayo aliibeba mkononi.Kwa nguvu zake zote Mama Beda akairusha ile chupa.
* * *
Alitembea taratibu kuelekea kituo cha polisi cha Mbagala Charambe.Hakujua ni nini kimemsibu mama yake hadi akajikuta yupo kituoni.Moyoni alikuwa na mswali mengi sana.Hakujua kwanini furaha kwake kilikuwa kitu hadimu.Hata jambo la kufurahisha yeye lilimtia uchungu.Mfano ulikuwa ni yale matokeo ya mtihani ambayo badala ya kumfurahisha yalimuhuzunisha.Angefurahivipi wakati hakuwa na uhakika
wa kusoma, halafu iweje leo akamatwe yule ambaye kidogo alimpa matumaini.
Alipofika pale mapokezi akamkuta yule bibi mfagia barabara akiongea na askari wa
zamu. Ingawa aliwakuta wakiwa katikati ya maongezi aliweza kuelewa wazi kile walichokuwa wanazungumza.
Kutokana na uzito wa kesi yake ndiyo maana tukaamua kumuhamishia polisi
Changombe.
huyu ndiye mwanae niliyekuwa nakueleza. Aliongea yule mama huku akimkazia
macho yule askari kama anayehitaji msaada zaidi.
Sawa mama lakini sina namna ya kukusaidia kwani suala lake limeshikwa na wazito.
Yule bibi mfagia barabara akamgeukia Beda na kumwangalia kwa sura iliyokosa
matumaini. Yule bibi akatoka mle kituoni lakini Beda hakutoka akaganda palepale
kabla ya kuanza kuongea na askari.
Shikamoo. Alimwamkia askari aliyemkuta pale.
Marhaba unasemaje? Aliuliza yule askari kwa sauti nzito yenye ukali kidogo.
Nimesikia mama yangu yuko hapa nimekuja kumuona.
Umesikia, umemsikia nani? aliongea yule askari kwa sauti iliyojaa dharau na ujivuni.
Nimesikia kutoka kwa majirani. Alijibu
Anaitwa nani mama yako? Aliuliza yule askari
Mrs Sanga. Alijibu Beda.
Ahaa, Yule mama aliyetaka kuua mtu? Swali hilo likamshitua Beda hakuweza
kulijibu.
yule mama kesi yake ni nzito kahamishwa hapa yuko polisi Changombe Aliendelea
kuongea yule askari. Beda akaondoka pale kaunta huku machozi yakimtoka.
Alipofika nje akaangua kilio kikubwa. Kilio chake kikakatishwa na mtu aliyemshika
bega. Alipogeuka akamuona yule bibi ambaye mara nyingi alikuwa anafagia barabara
na mama yake.
Usilie Beda mimi naenda kumuona mama yako huko Changombe,
yatakwisha tu. Yule mama alimbembeleza Beda aache kulia.
Kwani ilikuwaje? Aliuliza Beda huku akifuta machozi yake.
Kulikuwa na ugomvi na yule jirani yenu Mama Suzi, kamrushia chupa kwa bahati
ikamkosa lakini hawakukubali wakaja kumshitaki huku kuwa amedhamiria kuua.
Beda akashusha pumzi kwa nguvu. Ulikuwa ni muendelezo wa machungu katika maisha yake.
* * *
Mbu na harufu za mikojo vilikuwa kero ya aina yake kwa mama Beda ambaye
hakutarajia kupatwa na mkasa kama huo katika maisha yake. Ilikuwa kama ndoto pale
Mama Suzi alipokuja na kuanza kumrushia maneno ya kashfa. Bila kutarajia alijikuta
akiokota chupa na kumrushia. Ilikuwa ni bahati kwa Mama Suzi kwani chupa ilimkosa
na badala yake ikapiga ukutani na kupasuka vipande vipande. Mama Beda alijua
yamekwisha.
Siku ya pili akiwa kwenye maandalizi ya kuchemsha mahindi ndipo aliposhuhudia kile
ambacho hakukitarajia. Askari wawili wakiongozana na mzee Uwesu walifika
nyumbani kwake na kumkamata. Alielezwa wazi kuwa kosa lake ni kujaribu kuua.
Alilia, akalia
Kilio chake kikapotelea hewani, hakuna aliyemjali alionekana punguani.
Amlilie nani. Kwa namna ya kudhalilishwa akafungwa mikono yake kwa nyuma.
Watoto wakamzomea, majirani wakamcheka. Mpeleke akaroge gerezani.
Walichombeza safari yake hiyo. Hakuujua uchawi, hakumjua hata mganga wa kienyeji.
Labda umaskini wake na yale macho yake yaliyobadilika na kuwa mekundu kutokana
na kushinda kwenye jiko la kuni huku akibugia na kulizwa na moshi ule mkali.
Alishakubali matokeo sasa alikuwa anasubiri kudra za mola wake.
Akapokelewa na kiza cha mchana kwenye chumba kidogo ambacho hakina hata
dirisha. Baadae akatolewa bila maelezo yoyote na kupandishwa kwenye gari ambalo
lilimfikisha polisi Changombe. Akawekwa mahabusu. Makazi duni kabisa ambayo
hakustahili kukaa hata mbwa. Hakutamani kuendelea kuishi, dunia aliiona chungu.
Hakujua kama kulikuwa na tofauti kati ya dunia na jahannamu ule moto mkali ambao
unaelezwa kwenye vitabu vitukufu.
Akiwa kwenye lindi la mawazo mlango ukafunguliwa. Akatolewa kwa muda.
Akashangaa baada ya kugundua kuwa ni mchana kweupe. Beda mwanae wa pekee
alikuwa kaunta akihitaji kuongea na mama yake. Alitaka kuongea nini? Ilikuwa ni
vigumu kufahamu kwani mtu na mwanae wakaangua vilio ambavyo vilidhihirisha jinsi
askari wale walivyokosa huruma.
Afande Marwa mrudishe ndani huyo asitupigie makelele hapa.
Sawa afande. Amri ya mkuu ilipokelewa mama Beda akarudishwa tena kwenye
chumba kile kibaya kuliko vyumba vyote alivyowahi kuingia. Akalia, akaliaa
.. Sauti
ikakauka lakini bado kilio kiliendelea. Kama alivyolia kwa sauti akashindwa kusikika
sasa ilikuwa zaidi kwani alilia bila kutoa sauti. Alijua fika siri ya kifo cha mumewe,
kumbukumbu hiyo ikazidisha kilio kisicho na machozi.
* * *
JIFUNZE!
Mwenye pesa si mwenzako na kamwe masikini hathaminiwi katikati ya pesa. Pesa
hubadili mioyo ya wema kuwa miovu, pesa hubadili ndio na kuwa hapana, pesa
hununua utu na mbaya zaidi pesa hiyohiyo hurejesha utu! Isake kwa njia halali, jitume
uwezavyo kuisaka. Ukiipata usiitumie kama fimbo maana utaitumia kuwachapa
wenzako duniani lakini ipo hukumu inakungoja. Nawe utachapwa mara elfu ya
ulivyochapa Duniani!!
©George Iron, 2010
**MAMA Beda matatani, sauti yake inayolia unyonge haisikiki, wenye pesa wamemnyamazisha
..
Nini kitajiri!!! Beda hajui kama ataendelea kusoma ama la!!
ITAENDELEA!!