FEBIANI BABUYA
JF-Expert Member
- Mar 5, 2022
- 1,035
- 1,925
- Thread starter
- #21
STORY: GEREZA LA HAZWASTORY: GEREZA LA HAZWA
STORY WRITER: FEBIANI BABUYA
STORY TELLER: Bux the story teller
UKURASA WA TATU
TULIPO ISHIA UKURASA WA PILI
Alienda kwenye moja ya migahawa bora sana akaagiza chakula cha bei kubwa akiwa anafidia siku alizo teseka, alikula akashiba vizuri baada ya hapo alienda club na kuchukua mwanamke mmoja mrembo sana akawa anakunywa pombe baadae aliingia naye chumbani kupunguza uzito aliokuwa nao ikiwa ni kama kulipiza kwa namna wanawake wazuri walivyokuwa wanamkataa kwa sababu hakuwa na pesa kwenye maisha yake yote basi alijisikia fahari sana siku hiyo. Asubuhi na mapema sana alikuwa ndani ya gari akiwa anaelekea zake kwenye moja ya jiji ambalo kwake ilikuwa ni ndoto kwenda kuliishi.
ENDELEA..................................
Kani kwa mara ya kwanza alikuwa anashuka ndani ya jiji la Dar es salaam ambalo kwake lilikuwa ni geni mno hakuwahi kufika zaidi ya kusikia tu watu wakiwa wanalinakshi kwa uzuri wake wa kuvutia na umaridadi wa maisha ambayo watu waliomo ndani yake huwa wanayaishi kila siku, majira ya jioni wakati kiza kinaanza kuingia taratibu ndio muda ambao alikuwa anashuka stendi. Namba alikuwa nayo kwenye simu yake aliitoa kwenye mfuko wake kwa umakini sana na kuweza kuipiga iliita kwa mara ya kwanza na kukata, ikaitwa kwa mara ya pili kwa muda mrefu ndipo ilipoweza kupokelewa.
“Vuka hiyo lami kwa mbele utaona kuna gari nyeusi ingia humo” maelekezo aliyo yapata ilionekana mtu ambaye alikuwa akimuelekeza alikuwa anamuona moja kwa moja bila wasiwasi wowote ule basi alivuka na kweli hatua kama hamsini kutoka sehemu aliyokuwepo aliona kuna gari moja zuri sana la kifahari mno alisita kwenda ila aliamua kuufuata moyo wake na maamuzi yake, hatua mbili kabla hajafika mlango ulifunguliwa kana kwamba alikuwa akisubiriwa kwa muda mrefu kisha akaingia ndani ya gari. Ndani ya hiyo gari alikuwa amekaa mwanaume mmoja mwenye ndevu ambazo bila shaka zilichongoka na kukaa kwa usahihi kwa matunzo ambayo yalionekana kufanyika kwenye hizo ndevu, mustachi uliipamba sana sehemu ya juu kidogo ya mdomo wake na kuonekana kama alikuwa mhindi flani hivi, Kani ilimchukua kama dakika mbili kuweza kumtambua vizuri mtu ambaye alikuwa mbele yake alikuwa amebadilika mno na wala hakutegemea kama ndiye yule rafiki yake wa miaka mitano huko nyuma ilihitaji umakini wa hali ya juu na kwa mtu ambaye anamjua kiundani sana kuweza kumtambua kwamba ndiye alikuwa yeye mwenyewe.
Alen ndiye mwanaume aliyekuwa ndani ya gari hiyo ya kifahari walikumbatiana kwa furaha sana huku Kani machozi yakiwa yanamtoka kwa miaka mitano ambayo ilikuwa imepita alipitia mambo magumu sana ambayo yalimpelekea mpaka kuipoteza kazi yake.
“Ulikuwa wapi miaka yote hiyo ndugu yangu” Kani aliuliza akiwa anashangaa namna gari hiyo ilivyokuwa ya kifahari mno na hakuwahi hata siku moja kupanda wala kufikiria kama atakuja siku moja kuwa sehemu ya maisha hayo ya kifahari na kuyaishi kwenye uhalisia wake.
“Namba zinasoma kwa kasi kubwa sana ndugu yangu na miaka inazidi kukatika tu lakini wanadamu bado tupo, hilo ni swali ambalo nitakujibu siku nikipata muda ila kwa sasa nilihitaji kukusaidia ujitoe kwenye hiyo hali ya maisha ambayo ulikuwa nayo kwa muda mrefu sana nina imani umepitia shida za kutosha kwa sababu yangu mimi na hilo ndilo limenisukuma sana kuweza kulipa fadhila kwa wema wako ambao siwezi kuusahau kwa namna ulivyo nisaidia wakatii ule hakukuwa na mtu yeyote yule ambaye angeweza kusimama na kunikumbuka, kwa sasa twende sehemu ambayo ndiyo utafikia na utakuwa unakaa halafu kesho nitakupeleka sehemu ukafanye manunuzi ya nguo kidogo uanze kuendana na kasi ya mji” maneno hayo ya Alen Kani hata hakuwa anayasikia vizuri mawazo yake yalikuwa yapo mbali sana kushangaa namna mtu ambaye alikuwa naye kwenye machimbo ya madini miaka kadhaa nyuma leo alikuwa anaongea akiwa siriasi sana maisha yalikuwa yamebadilika mno kwa kiasi kikubwa.
“Ahhhh…. sawa” alijibu kwa kigugumizi, Alen alitabasamu tu kuona hiyo hali alimjua mwenzake huyo kwa ushamba hususani anapofika sehemu ambayo anakuwa haijui kabisa au ni ngeni kwenye maisha yake, alinyanyua gia na kuanza kutoka kwenye hilo eneo kwa spidi ya kawaida ikionekana wazi hakuhitaji kumuumiza mgeni wake.
“Hivi kaka wewe wazazi wako na asili yako kabisa huwa ni wapi?” ni swali ambalo lilionekana kumshtua sana Alen baada ya kuulizwa na Kani walionekana kuwa watu ambao walikutana na kusaidiana tu ila walikuwa hawajuani kiundani sana.
“Sikumbuki sana nilikuwa mdogo mno ila ninacho kijua mimi wakati naanza kujitambua nilijikuta naishi kwenye kituo cha watoto yatima mpaka pale nilipo ona kwamba nina uwezo wa kujitegemea nikaamua kuondoka hiyo sehemu nadhani hata siku ya kwanza niliwahi kukwambia hivyo” Alen alijibu lakini ni wazi hakupendezwa kabisa na hilo swali ilimbidi kufungua muziki taratibu kwenye gari akiwasha skrini ndogo ambayo iliuchukua umakini wa Kani wote na maswali yakawa yameishia hapo. Nusu saa ilipita waliingia Sinza kwenye mjengo ambao haukuwa mkubwa saana ila ulikamilika kwa mtu kuweza kujiita ana maisha mazuri ya kuvutia, mlango ulifunguliwa wakaingiza gari ndani kisha wakafunga geti, muda wote Kani macho hayakubanduka kwenye skrini ambayo ilikuwa ipo mbele ya gari mpaka pale alipokuja kushtuliwa na Alen kwamba walikuwa wamefika mwisho wa safari yao ndipo alipoweza kushuka ndani ya gari wakaongozana mpaka ndani ya nyumba.
“Kani kuanzia leo hapa ni kwako na ndipo utakapokuwa unaishi kwa sasa, yale magari mawili ambayo umeyaona pale nje ni yako yote ila kuhusu wafanyakazi utaamua wewe kama utawaleta au la itakuwa ni juu yako mwenyewe” Kani aligeuka kutoka kwenye mshangao aliokuwa nao wa kushangaa vitu vya thamani vilivyokuwepo ndani ya sebule hiyo na kumwangalia Alen kwa taharuki, hakuwa anaamini kwamba hivyo vitu humo ndani vilikuwa ni mali yake yeye na alikuwa anaruhusiwa kuvitumia kadri atakavyo, alijikuta analegea na kupiga magoti chini akiwa anatoa machozi huyo mwanaume mbele yake hakuwa ndugu, kaka wa kuzaliwa wala hawakutoka sehemu moja ya kuzaliwa ila leo ndiye aliyekuwa kama ndugu yake ndani ya jiji hili, ni binadamu wachache sana huwa wana moyo wa aina hiyo. Alen alimfuata rafiki yake huyo wa machimbo akamnyanyua na kumkumbatia.
“Kama ningekuwa na uwezo ningeurudisha muda nyuma uzaliwe wakwanza kwenye familia yetu kisha nifuate mimi nikuite kaka wa damu kabisa tumbo moja nadhani ningekuwa mwanadamu ambaye ningekuwa nina bahati kuliko binadamu yeyote yule hapa duniani, asante sana kaka” Kani aliongea kwa kumaanisha macho yake yalitoa ishara za msisitizo kuhusu hilo jambo wakati huo alikuwa amekumbatia sofa moja maridadi sana ambalo lilipita kwenye mkono bora wa fundi seremala.
“Hahahahahah Kani bado hujaachaga masiara yako, hivi ni vitu vidogo tu usijali, wewe ndiye binadamu pekee uliuona umuhimu wangu wakati ule mimi ni kapuku sina hata mia mbovu, ukanipeleka mpaka kazini kwako na kunisaidia sana sehemu ya kulala kwahiyo haya ninayo yafanya wewe ndiye unastahili pongezi kwani huenda kama sio wewe mimi leo nisingekuwa hapa” Alen aliongea kwa kumaanisha mashavu ya Kani yalituna kwa cheko kisha akakaa chini akiwa ana furaha sana, kilicho fuata alionyeshwa mazingira yote ya nyumba na namna ya kutumia vitu mbali mbali humo ndani, vyakula vilikuwa vipo vya kutosha kwenye friji alikula sana baada ya Alen kuondoka na kuahidi kwamba angekuja kesho yake kumchukua akabadilike kuanzia mavazi mpaka muonekano.
Sauti za kengele ndizo zilizo weza kumshtua kutoka kwenye usingizi mkali na mnono ambao alikuwa amelala, hakuwahi kwenye maisha yake kulala sehemu nzuri na bora kama hiyo leo ndiyo ilikuwa mara ya kwanza kabisa hakuhitaji kuukosa usingizi huo hata kwa sekunde moja, alimlaani sana mtu ambaye alikuwa amehusika na kuikatisha safari yake ya usingizi, alitoka taratibu sebuleni na kwenda kuufungua mlango, alitabasamu baada ya kumuona Alen akiwa kwenye moja ya suti nzito mno hakuhitaji maelezo mengi alimhitaji watoke sasa akatengenezwe. Walipanda kwenye gari haraka sana wakaitafuta moja ya saloon kubwa Kani alienda kutengenezwa kuanzia uso wake na kufanyiwa masaji na watoto wakike ambao walinona mno, mate yalikuwa hayamkauki mdomoni na aliapia angerudi kuwatafuta, baada ya kumaliza safari yao ilienda kuishia ndani ya Mlimani City ambako walipanga kwenda kununua nguo za kutosha kwa ajili yake. Walifika na kushuka kwenye gari walianza taratibu kutembea kuelekea ndani Alen akiwa ametangulia mbele wakati anayakaribia malango ya kuingilia alijifanya kama anaishika kofia yake vizuri akaikutanisha mikono yake miwili na kuibonyeza kidogo tu saa ambayo ilikuwa kwenye mkono wake ghafla umeme kwenye sehemu zote ambazo zilikuwa karibu na hapo walipokuwa ulikata kwa dakika moja na kurudi haraka sana halikuwa jambo la kawaida liliwashangaza watu wote ambao walikuwa wapo karibu kutokana na sehemu hiyo kuto katika umeme hata kama umeme wa tanesco ungekata basi huwa kuna jenereta za kutosha ambazo huwa zinafanya sehemu hiyo kuwa yenye umeme muda wote.
Baada ya kumalizana na shoping yao ndani ya Mliman City siku ile maisha yaliendelea kama kawaida Kani akijitahidi sana kuwa mwenyeji wa jiji hili na kwa msaada wa rafiki yake Alen haikuwa kazi ngumu sana ilifika sehemu akawa ni mwenyeji kila sehemu japo alikuwa ana maswali mengi sana juu ya maisha ya rafiki yake kwanza alikuwa haelewi Alen alipoteaje ndani ya Arusha na kuja kuwa mtu tajiri kiasi hiki? Alijaribu kujijibu mwenyewe kwamba huenda mwanaume huyu alibahatika kuyapata madini lakini alilipinga hilo kwa sababu ilikuwa sio rahisi mtu kutoka na madini ndani ya yale machimbo na hata siku ambayo rafiki yake huyo aliondoka alikuwa kwenye hali mbaya mno kiasi kwamba asingekuwa na uwezo wa kufanya hicho kitu, swali la pili lilikuwa ni maisha ya mtu huyo kiujumla muda wote ambao alikuwa amekuja ndani ya jiji la Dar hakuwahi kabisa kuijua sehemu ambayo alikuwa akishi Alen lakini swali la tatu hakuelewa kwanini rafiki yake huyo alikuwa anakwepa sana kupiga picha kwenye uso wake na alikuwa makini sana kuweza kulikwepa hilo jambo hata hivyo aliamua kuuachia muda uamue kwa sababu hakuhitaji kulazimisha mambo wakati mhusika yeye mwenyewe hakuwa tayari kabisa kumwambia japo alitamani sana kuyajua majibu ya maswali yake.
“Kani nina imani utakuwa na maswali mengi sana juu yangu kwamba nimeyapataje haya maisha, kwanini sijawahi kukupeleka nyumbani? Muda ukifika utajua kila kitu ila kwa leo nataka kwa mara ya kwanza ukaione familia yangu ili hata siku nikipata tatizo wapate mtu wa kuwafariji” ni maneno ambayo yalimuacha Kani mdomo wazi alitetemeka kidogo hicho ndicho kitu ambacho alikuwa anakiwaza muda sio mrefu kwenye akili yake sasa alijiuliza huyo mtu kwanini amwambie hayo mambo muda huo kwamba alikuwa ameshajua anacho kiwaza? Hakupata jibu.
“Itakuwa ni vizuri sana ndugu yangu maana sijui hata familia ya rafiki yangu mpaka najisikia aibu muda mwingine” alijibu tu kama kujifariji ila kiuhalisia hata alicho kijibu alikuwa hajakijua, Alen alimwangalia kwa umakini sana Kani kiasi kwamba alikuwa ni mtu ambaye alikuwa anayapima macho yake kisha akatabasamu, waliingia kwenye gari na kuondoka kwa mwendo wa taratibu kabisa. Maeneo ya posta pembezoni kabisa mwa bahari ndipo gari ilipo enda kusimama nje ya mjengo mmoja ambao bila shaka mmiliki hakuwa mtu wa kuhesabu pesa kwa mkono lazima mashine ndizo zilikuwa zinafanya hiyo kazi ya kuhesabu ndipo walipoweza kufika, ilikuwa ni miongoni mwa majumba ya kifahari sana ndani ya eneo hilo Kani aliutazama huo mjengo bila kuumaliza alijikuta anameza mate na kikiri moyoni kwamba ukiachana nayeye kudumu hapa duniani ila dunia hii hii ina watu ambao walikuwa wanaishi kweli.
Baada ya kuingia ndani walikaribishwa na tabasamu la mwanamke mmoja mzuri mno ambaye alienda kumkumbatia Alen na kumpiga busu zito kwenye paji lake la uso.
“Welcome back my husband” ni sauti tamu ambayo ilipenya kwenye ngoma za masikio ya Kani na kujikuta akitabasamu akiwa haamini yule rafiki yake kapuku wa machimboni leo alikuwa anapokelewa na sauti nzuri laini kama hiyo mbele yake maisha yalikuwa yanakimbia mno, naye hakunyimwa haki ya kuisikia sauti hiyo baada ya kugutuliwa na sauti
“Karibu nyumbani shemeji” alijikuta anababaika hata kujibu huku akipokea mkono wa mwanamke huyo kabla hajakaa sawa ilisikika sauti yenye kicheko cha kitoto iliyokuwa na furaha sana ikiwa inakuja upande wao.
“Daddy” mtoto wa Alen alikuja na kumkumbatia baba yake kipenzi, ni kitendo kilicho muacha Kani mdomo wazi hakuweza kuamini kama rafiki yake alikuwa amefikia hatua mpaka ya kuwa na mtoto kabisa, alijikuta anainama chini kwa mshangao, kwake dunia ilikuwa ina siri kali ila wanadamu ndio walikuwa wenye siri zaidi ya mifuko iwekwayo ndani ya nguo ya mtu.
Ni mwanzo kabisa ndani ya GEREZA LA HAZWA ukurasa wa tatu tunaweka nukta tupumzike kidogo.
Bux the story teller.View attachment 2356266
Sent from my TA-1053 using JamiiForums mobile app
STORY WRITER: FEBIANI BABUYA
STORY TELLER: Bux the story teller
UKURASA WA NNE
TULIPO ISHIA UKURASA WA TATU
“Daddy” mtoto wa Alen alikuja na kumkumbatia baba yake kipenzi, ni kitendo kilicho muacha Kani mdomo wazi hakuweza kuamini kama rafiki yake alikuwa amefikia hatua mpaka ya kuwa na mtoto kabisa, alijikuta anainama chini kwa mshangao, kwake dunia ilikuwa ina siri kali ila wanadamu ndio walikuwa wenye siri zaidi ya mifuko iwekwayo ndani ya nguo ya mtu.
ENDELEA..................
Walikuwa kama familia moja, ilikuwa ni furaha kubwa sana kujumuika pamoja sasa swali moja lilikuwa limejibiwa kwake bila hata yeye kuuliza kwa kuweza kujua mahali ambapo rafiki yake alikuwa anaishi tena alibahatika kuijua na familia yake kabisa, sasa ilikuwa ni kawaida kwa Kani kwenda kwa Alen siku ambazo alikuwa ana muda wa kutosha kwa sababu mpaka muda huo alikuwa tayari ana biashara zake ambazo Alen alimfungulia hivyo kuna muda ilikuwa inamlazimu sana kuwa busy kusimamia hiyo miradi ambayo ilikuwa imefunguliwa tayari. Ulipita muda mrefu sana akawa mzoefu wa jiji tayari na alikuwa ameanza kijisimamia kwa kila kitu maisha mazuri yakiwa sehemu yake kwa kupitia mgongo wa rafiki yake ambaye alimsaidia miaka kadhaa nyuma kwake wema ulikuwa ni akiba kubwa ambayo ilikuwa imezaa matunda mema.
Siku moja alikuwa anatamani sana kuweza kumshukuru rafiki yake kwa namna alivyo msaidia na kuyabadilisha maisha yake, aliwaza sana kumshukuru yeye tu lakini aliona haitakuwa sawa kwa sababu alihitaji watu wengi waone anavyo shukuru njia pekee kwake ambayo aliona watu wengi wanaweza kuona ni kupitia mitandao ya kijamii ambako huwa wanakutana watu wengi sana hapa ulimwenguni kwa muda mfupi. Alipanga atafanya kila namna ili ampige mtu huyo picha au wapige wote bila yeye kujua kitu chochote kile hivyo alinunua kamera moja nzuri na kubwa akawa ameihifadhi juu ya friji wakati huo alimpigia simu Alen kwamba alikuwa akimhitaji kwa muda huo kulikuwa na dharura ya mhimu sana mwanaume hakuona tabu alikuja kumsikiliza rafiki yake. Kabla hajaenda kufungua mlango aliitegesha kamera yake vizuri kabisa na kwenda kumfungulia mlango Alen baada ya kugonga.
“Kani umeniita ghafla sana umenishtua kuna nini?” Alen aliuliza kama kulikua kuna usalama humo ndani lakini Kani aliiangalia saa yake na kutoa kicheko
“Angalia kuleeeeee” alionyesha kidole wakiwa wapo karibu na ndipo Alen alipo geukia ule upande ambao ulikuwa na kamera yeye hakuweza kujua chochote kile muda huo kamera hiyo alipiga picha za kutosha (kosa kubwa sana).
“Nimekununulia zawadi ya saa hii hapa kaka, nashukuru sana kwa wewe kuwa sehemu ya maisha yangu sijui ningekuwa naishi vipi mpaka leo, sihitaji kujua kwa sasa kwanini ulitoroka hali iliyo nifanya nifukuzwe kazi kwa kusingiziwa kuiba madini na pia nilifungwa kwa muda wa miaka mitatu jela mpaka nilipo onekana sina hatia maisha yangu yalikuwa yameelekea shimoni ila umekuja na kunipa tumaini jipya kwenye maisha yangu asante sana kaka” Kani aliongea kwa uchungu mkubwa sana wakati anamshukuru rafiki yake, ni kweli maisha yake yalibadilishwa sana na mwanaume huyo kwake alidai alimuita hapo ili kumkabidhi zawadi ya saa ikiwa ni kama sehemu ya shukrani kwa kila alicho fanyiwa kwenye maisha yake, Alen alifurahi kiasi chake japo moyoni alikuwa kawaida sana kwake ilikuwa kawaida kwa sababu aliwajua sana binadamu hasa pale unapo onekana wa mhimu kwao basi watakunadi kwa kila aina ya maneno matamu ila sio ajabu hao hao kesho ndio wanakuja kukufanya ujutie kuwafahamu basi aliipokea saa hiyo na kumkumbatia rafiki yake wa ukubwani na kumpiga piga mgongoni.
“Asante Kani” alitamka kwa tabasamu na kutoka humo ndani akawasha gari na kuondoka kwani hata kazi yake ilikuwa haijulikani kabisa hapa mjini. Kani aliufunga mlango na kuanza kushangilia zoezi lake lilikuwa limeenda sawa, aliifuata kamera yake na kuangalia kweli kulikuwa na picha zaidi ya kumi ila kuna picha mbili tu ndizo alizo zipenda yeye, alizihamisha vizuri kwenye simu yake hakuchukua muda alienda moja kwa moja kwenye kurasa za mitandao na kuanza kuzisambaza hizo picha kwa maelezo mazuri sana ambayo yalikuwa yameandikwa kwa mbwembwe.
“MAISHA YANGU YAMEKUWA KAMA HADITHI YA KUFIKIRIKA KWA ZAIDI YA MIAKA 20 ILIYO PITA NIMEISHI NDANI YA JANGWA BILA MAJI ILA MUNGU ALIVYO WA AJABU AKAMTUMA MJA WAKE NA KUJA KUNIPATIA DAWA YA KIU NIKAPONA, SINA CHA KUKULIPA ILA NINASHUKURU KWA KILA KITU ULICHO NIFANYIA KWENYE HAYA MAISHA YANGU ALEN, I LOVE YOU BRO” maneno yalisomeka vizuri kabisa akiwa ameyaweka kwa herufi kubwa ili kwa kila msomaji atakaye iona picha hiyo asiache kuyasoma hayo maelezo. Lengo lake alitaka kumfanya rafiki yake aone ni namna gani alikuwa anathamini na kuheshimu kwa kila alichoweza kufanyiwa, fikra zake alijua atamfurahisha sana Alen kama ataona hicho kitu ila huenda alikuwa anafanya kosa kubwa sana kwenye maisha yake bila yeye kujua na kama angefanikiwa kujua madhara ya hicho alichokuwa anakifanya ni bora angejiua yeye mwenyewe.
Baada ya kuona ameiweka vizuri kama alivyokuwa anahitaji yeye basi aliichapisha na kuiruhusu kwenye mitandao mbali mbali ambayo kwake aliamini kwamba watu wengi wataiona na kumpongeza kwa Kumkumbuka mtu aliyeweza kumtoa mbali. Baada ya kuichapisha picha hiyo ilichukua dakika moja tu kuna alama nyekundu ilitokea kwenye hiyo picha mpaka yeye mwenyewe alibaki anashangaa hakuwahi kuona hicho kitu, baada ya sekunde thelathini tu picha hiyo ilifutika na kwenye kila ukurasa ambao alikuwa ameisasisha ilikuwa imefutika, mawazo yake yaligoma kuamini hicho kitu alihisi huenda alikosea ikamlazimu kurudia tena kuipakia cha ajabu ilikuwa inagoma. Alitaka kutafuta moja ya namba kwenye simu yake apige simu hiyo mahali ili aulizie hicho kitu lakini simu ilikuwa haifanyi kazi kabisa huku akiwa inapiga alama nyekundu, alibaki anatokwa jasho hakuelewa inawezekana vipi maajabu kama hayo kumtokea yeye majira hayo ya usiku wa mapema kabisa hiyo, alivyokuwa anazidi kulazimisha simu hiyo kufanya kazi ilianza kutoa moshi hatimae ilipasuka kwa mlipuko mdogo wa moto ambao uliifanya ibaki nyeusi kabisa na umeme ulizima nyumba yote.
Alikimbilia kufunga mlango ili kama kuna hatari awe salama alijikuta anarudishwa kwenye sofa kwa nguvu hakujua amepigwa na kitu gani kwenye mwili wake alihisi maumivu makali ambayo yalimfanya agugumie kama jogoo lililo ona tetea mbele yake.
“Nani wewe nani wewe, unavamiaje kwenye nyumba za watu aaaaagh” alikuwa anaongea mwenyewe hakusikia mchakacho wala sauti ya mtu yeyeote ambaye alikuwa akimjibu humo ndani. Ghafla taa ziliwaka mbele yake kulikuwa na watu watatu ambao wote walivaa suti zao nyeusi ila hawakuonekana kuwa watanzania kwa mwonekano wao tu ni wazi hawakuwa na uswahili mwingi kama ilivyo kwa wazawa wengine.
“Hey hey mnataka nini nyie watu, kawatuma nani hapa, hey nitawaua mimi” alikuwa akijitetea baada ya kuona mwanaume mmoja alikuwa anasogelea ile sehemu ambayo alikuwa amedondokea yeye hata hivyo hakujibiwa kitu chochote kile, alitaka kunyanyuka akimbie ngumi ilitua kwenye shingo yake akarudi tena chini na kutulia bila kupiga makelele alizimishwa kisha mwanaume huyo akambeba wakamuingiza kwenye gari na kuondoka naye kwa kasi humo na gari yao ambayo walikuja nayo na walikuwa wameiacha nje ya nyumba.
Kani alishtuka kutoka kwenye usingizi mzito shingo yake ilikuwa na maumivu mno, mwanga mkali uliyaumiza macho yake ilimlazimu kuyafumba kisha kuyafumbua tena kwa mara nyingine ndipo alipoweza kuona sakafu nzuri sana na chumba kikubwa chenye kila kitu cha kukifanya kuwa bora kupita maelezo, alishtuka baada ya mbele yake kuwaona wanaume wenye suti nyeusi wakiwa wapo kama watano hivi mmoja wao alikuwa amekaa kwenye kiti ambapo mbele yake kulikuwa na meza ya kioo na meza hiyo ilitumika kuwekewa bastola na kisu kimoja kikali mno. Kwenye mwili wake alikuwa amevalishwa nguo nyeupe ni kama za wafungwa ila zakwake hazikuwa na mistari na namba, akiwa anashangaa na kurudi nyumba kwenye kitanda kizuri alichokuwa amelala alikuwa anajivuta taratibu nyuma mpaka pale alipofika mwishoni kabisa kwa ukuta hakuwa na sehemu ya kwenda tena kuna kijana mwenzie kama yeye aliingizwa humo ndani akiwa amekunjwa vizuri alisukumiziwa mbele hakuulizwa chochote ila alikuwa analia sana na alionekana alikuwa amelia kwa muda mrefu sana, yule mwanaume ambaye alikuwa amekaa kwenye kile kitu aliichukua bastola yake na kuigeuzia upande ambao alikuwa yule kijana bila hata kuangalia wakati huo macho yake alikuwa ameyakaza kwenye uso wa Kani alimmiminia yule kijana risasi kumi na mbili kwenye mwili wake halafu akaonyesha ishara ya mwili wa kijana huyo utolewe kwa mkono wake lilikuwa ni jambo la haraka hicho kitu kilifanyika kwa wepesi mkubwa, Kani alikuwa akitetemeka hakuwahi kushuhudia mtu akiuawa kwenye maisha yake leo kijana mwenzake kichwa chake kiligeuzwa mpira kwa kupigwa risasi nyingi mno aliogopa isivyo kawaida.
“Unaitwa nani kijana?”
“Naitwa Kani”
“Kwenu wapi?”
“Moshi”
“Unamjua huyo uliye naye kwenye picha?” alirushiwa picha kubwa ambayo yeye alikuwa ameipiga kwa siri na Alen mpaka hapo alijua kwamba watu hao waliibeba ile kamera ndiyo maana walikuwa wana hizo picha.
“Ndiyo namjua” alikuwa akijibu jasho likiwa sehemu ya mwili wake.
“Unamjuaje?”
“Ni rafiki yangu”
“Jitahidi kuwa na kichwa chepesi elezea vizuri umemjuaje na unamjua vipi yeye” sauti nzito ilimsisitizia kiasi kwamba hakuwa akiombwa kutoa hayo maelezo ilikuwa ni lazima afanye hivyo kwa sababu ya usalama wake, hakuwa na kitu ambacho angeweza kukipinga ni kwa muda mfupi sana alitoka kushuhudia mwenzake akiuliwa hapo japo hakuweza kujua kama naye alikuwa na kesi kama hiyo ya kwake au kulikuwa na mambo mengine nyuma yake.
“Anaitwa Alen jina lake jina lingine silijui na wala sijui alizaliwa wapi ila ninacho kikumbuka ni jioni moja majira ya saa mbili za usiku nilikuwa nimetoka kwenye harakati zangu za kila siku za kuweza kutafuta mkate ili nipeleke mkono wangu kinywani, wakati nimetoka kuchukua mikate na juisi kwa ajili ya kuimaliza jioni yangu vizuri nikalale kwenye valanda moja ya duka kubwa nilisikia mtu akiwa anaunguruma, mara ya kwanza nilihisi huenda itakuwa ni mlevi ila nilivyo karibia nilikuta kuna mwanaume amejiviringisha akiwa anatetemeka kwa baridi mno kwenye mwili wake, midomo ilimkauka sana ni wazi ulipita muda mrefu sana bila kuweza kuyapata maji. Nilimuamsha na kumuuliza nini lilikuwa tatizo kwake alinieleza kwamba ana njaa kali sana na ndiyo mara yake ya kwanza kuweza kuingia ndani ya jiji la Arusha, ni mwanaume mwenzangu hivyo niliingiwa sana na huruma nikaamua kumpatia kile chakula ambacho nilikuwa nimekibeba kwenye mfuko, alikifakamia mno akanywa na juisi kisha akadai na maji alikunywa yote akapata na nguvu za kuongea.
“Asante sana ndugu yangu hapa kama ungechelewa hata dakika tano tu nahisi nilikuwa ninakufa nilikuwa na njaa kali mno” aliniambia hivyo nikiwa bado namshangaa.
“Kwani nyumbani ni wapi ndugu yangu?”
“Sijawahi kujua chochote mpaka wakati najielewa nilijikuta kwenye kituo cha kulelea watoto yatima huko Dar es salaam hivyo namimi ni yatima lakini nikaamua kuondoka kwenye kile kituo baada ya kuona umri wangu wa kuweza kujitegemea umeweza kufika niliamua kuondoka na kwenda kuyaanza maisha yangu katika kuhangaika ndo nikawa nimeingia kwenye hili jiji la Arusha nina siku tatu hapa sikuwa nimekula chochote namshukuru sana MUNGU kuweza kukupitisha kwenye hii njia ambayo nilikuwa naenda kufa huku watu wote wakiwa wananipita kama hawamuoni mwanadamu mwenzao kabisa” aliongea kwa msisitizo akiwa anamalizia maji ambayo nilimpatia. Kwa sababu niliona ni msakatonge mwenzangu basi nikamchukua moja kwa moja na kwenda naye nyumbani ambako nilianza kuishi naye, mimi nilikuwa nashinda kwenye machimbo ya madini basi nikamuunganisha nayeye akawa anaenda siku moja moja mpaka pale alipo zoea na kuwa mmoja wa wachimbaji kule na hapo alipanga kachumba kadogo ambako alikuwa anakaa pekeyake japo bado tulibaki kuwa karibu sana kama marafiki na tulisaidiana kwa kila kitu mpaka ile siku ambayo aliumwa ghafla sana tukiwa shimoni kuendelea na uchimbaji, nilifanya jitihada za kuweza kumtoa na nilifanikiwa, alipelekwa kwenye hospitali ambapo huko ndiko inako daiwa alipotea mpaka ilipo pita miaka mitano ndipo alipo nitafuta na kuniambia nije DAR, nilifanikiwa kufika salama akanipa maisha mazuri sana akaniunganisha na familia yake lakini nilikuwa natafuta nafasi ya kuweza kumshukuru ndipo nilipo piga picha za siri ambazo leo hii nilikuwa nataka kuzisasisha mtandaoni kutoa shukrani zangu kwake” alitulia baada ya kuwapa maelezo mafupi ya namna anavyo mjua mwanaume huyo.
Hili game ndo kwanza linaanza, ulishawahi kuona mtu wa kawaida anaishi bila kuhitaji kamera yoyote ile iweze kuipata picha yake? Kwanini? Unadhani huyu binadamu Alen ni nani na hawa watu ni akina nani mpaka wanaonekana kumtafuta kwa nguvu zao zote namna hii?.......ukurasa wa 4 unaishia hapa huenda wakati utaamua kutupatia majibu juu ya huyu mchimba madini Alen ni nani hasa na kwanini anaishi kwa kujificha sana hivi.
Bux the story teller.