Dunia haina usawa

Dunia haina usawa

DUNIA HAINA USAWA-30

Kila mtu alitaka kufahamu kile kilichokuwa kikitaka kuzungumzwa na Bilionea Kizota. Huyo alikuwa mwanaume mwenye pesa nyingi kuliko wote nchini Tanzania, maisha yake yalikuwa ya siri sana kiasi kwamba kuna watu wengine hawakuwa wakifahamu alifananaje.
Ilikuwa vigumu kumuona katika magazeti, televisheni au sehemu nyingine, alikuwa mzee aliyeishi kisiri sana kiasi kwamba kuna wengine hawakuwa wakiamini kama mzee huyo alikuwa mwembamba, mwenye sura ya kimasikini kuliko vitu alivyokuwa akimiliki.
Baada ya saa moja, tayari waandishi wa habari walikuwa nje ya jumba lake la kifahari lililokuwa Osterbay jijini Dar es Salaam. Haikuwa rahisi kuingia hivihivi, waliambiwa mmoja mmoja kwenda kusimama sehemu moja kulipokuwa na taa ya rangi ya bluu ambayo iliwaonyesha kila kitu walichokuwa nacho.
Nyumba ilikuwa na ulinzi mkubwa sana, waandishi wa habari wote walichunguzwa lakini hakukuwa na mtu aliyeonekana kuwa na silaha yoyote ile. Wakaruhusiwa kuingia ndani na kupelekwa sehemu fulani iliyokuwa na viti pamoja na hema na kuambiwa wasubiri hapo.
Wakatulia na kuanza kufunga mitambo. Walikuwa wakimsubiri bilionea huyo ambaye alikuwa akijiandaa tayari kwa kuzungumza na waandishi hao. Alitaka kuzungumza mambo fulani ambayo yalikuwa ni siri sana, mambo ambayo hakukuwa na mtu aliyekuwa akiyafahamu.
“Bro! Nimefika,” alisema mwanaume mmoja aliyekuwa na kaera, wakati waandishi wa habari wenzake wakiwa wameingia ndani, yeye ndiyo kwanza alikuwa akifika.
“Wewe nani?”
“Mwandishi kaka!” alijibu mwanaume huyo huku akimuonyeshea kamera aliyokuwa ameishika.
“Kutoka wapi? Kitambulisho chako kiko wapi?’ aliuliza mlinzi huku akimwangalia mwanaume huyo.
Hapohapo akachukua kitambulisho na kumuonyeshea mlinzi, kitambulisho kilichomuonyesha kwamba alikuwa mwandishi wa habari kutoka katika Mtandao wa Omen ambao ulikuwa ukitikisa kipindi hicho.
Akaambiwa aende kusimama katika taa ile ya kuwachunguzia watu ili kuonekana kama hakuwa na silaha yoyote ile, akaenda, akasimama na kummulika kisha kuruhusiwa kuingia ndani.
Mwandishi huyo alikuwa Godwin. Alifika mahali hapo kwa kuwa alitaka kufanya kitu kingine kabisa. Alitembea kwa kujiamini, hakuwa na hofu hata kidogo na kila mtu aliyemwangalia, kwa jinsi alivyokuwa alionekana kuwa mwandishi kweli.
Alikwenda mpaka walipokuwa wenzake na kutulia hapo. Baada ya dakika kadhaa, Bilionea Kizota akafika mahali hapo. Kwa jinsi alivyoonekana, alikuwa amekonda, ilikuwa ni vigumu kuamini kama mtu mwenye pesa ambaye siku chache zilizopita alikuwa na mwili wa kawaida leo hii alikuwa vile.
Kichwa chake kilimpa mawazo, kila mwezi alikuwa na uwezo wa kuingiza bilioni tatu lakini kitu cha ajabu kabisa, alikuwa mtu wa mawazo mengi kuliko hata mtu masikini ambaye alilala pasipo kuwa na chakula chochote.
Waandishi wa habari wakaanza kumpiga picha tangu alipokuwa akiingia mpaka alipokwenda kukaa. Godwin hakutulia, kama walivyokuwa wenzake, naye alikuwa akishughulika sawa na wao na kutulia sehemu yake.
Alimwangalia bilionea huyo, alitia huruma, alipoteza mwili wake mkubwa, kwa kumwangalia mara moja, ilikuwa ni vigumu kuamini kama mtu huyo alikuwa bilionea. Akatulia kwenye kiti, kabla ya kuzungumza chochote kile, akaanza kuwaangalia waandishi hao.
“Nimefurahi sana kuwaona mahali hapa. Najua wengi mnashangaa jinsi nilivyopungua. Ndugu zangu, kuna wakati unakaa na kuingiza pesa nyingi lakini hiyo haitoshi kuonyesha kama umefanikiwa,” alisema Kizota huku akiendelea kuwaangalia watu waliokuwa mahali hapo.
“Siamini pesa ndiyo inaweza kumfanya mtu kuwa tajiri. Tajiri pekee ni yule ambaye ana vitu ambavyo pesa haiwezi kununua kama furaha, faraja, amani. Mimi ni masikini, nina pesa lakini haziwezi kununua furaha, kuna haja gani ya kuwa na pesa?” aliuliza Kizota, alivyokuwa akizungumza, alionekana kuwa na jambo kubwa moyoni mwake.
Alizungumza mambo mengi mno lakini mwisho kabisa aliwaambia kile kitu kilichoujaza moyo wake kwamba kuna wakati alitamani kufa, kuondoka katika dunia hii kwa kuwa kuna jambo ambalo halipo sawa kabisa.
“Jambo gani?” alidakia Godwin, hakutaka kuchelewa.
“Siipendi serikali hii, simpendi rais hata kidogo. Ninamchukia kwa sababu yeye ndiye amekuwa chanzo cha mambo yote, yeye ndiye amekuwa sababu ya mimi kukosa furaha,” alisema Kizota, machozi yakaanza kumlengalenga.
“Kwa nini?” Godwin akadakia tena kiasi kwamba mpaka baadhi ya waandishi wakaanza kushangaa kwani hakukuwa na mwandishi wa habari aliyeonekana kujiamini kama yeye.
“Nilitishiwa maisha kwa sababu ya serikali hii. Jana tu Noel alijiuzulu nafasi yake, najua inawezekana kuna kitu kimemtokea ambacho hata mimi kimenitokea. Jifikirie kwa nini yanatokea haya yote? Jibu ni jepesi kwamba rais ndiye anayesababisha haya, bila rais kuwa na serikali ya kipuuzi haya mambo yote yasingeweza kutokea. Kama wananchi wanapata wanachokitaka, unahisi haya yote yangetokea? Kama rais angekuwa siyo muuaji unafikiri haya yote yangetokea? Hakuna kitu kama hicho. Rais ndiye katunyima furaha, katufanya tutekwe. Kama Noel alisema wazi hamuungi mkono rais, hata mimi pia simuungi mkono hata kidogo,” alisema Kizota.
Hakuogopa, moyoni mwake alikuwa na mzigo mkubwa lakini baada ya kufunguka kwa kirefu na kutoa dukuduku lake, moyo wake ukawa na amani, akahisi kama alikuwa ameutua mzigo mzito aliokuwa ameubeba.
Kila mwandishi alikuwa akishangaa, hawakuamini kama bilionea huyo angezungumza maneno kama hayo tena akiwa laivu kabisa. Wengi wakahisi kwamba kungekuwa na kitu kibaya ambacho kingetokea mahali hapo kwani kama kila mtu alikiona kipindi hicho, rais Bokasa asingekubali kuona akichafuliwa, kwa kutumia cheo chake, mabavu yake basi angetuma polisi kwenda huko na kumkamata.
Walichokuwa wakikihisi ndicho kilichotokea, huku bilionea huyo akiendelea kuzungumza na waandishi, magari mawili ya polisi yakafika nyumbani hapo, kwa mwendo wa kijeshi polisi wakaingia ndani na kumkamata mzee huyo ambaye muda wote alikuwa akisema kwamba ilikuwa ni bora kukamatwa kuliko kuendelea kuishi huku akiwa hana amani moyoni mwake.
“Hata kama kufungwa nitakuwa tayari! Ninachokitaka ni kuwa na amani moyoni mwangu tu. Inatosha,” alisema bilionea huyo wakati amechukuliwa na kupandishwa ndani ya gari na kuondolewa mahali hapo.
Waandishi wa habari hawakuwa na nongwa, walichokifanya ni kuendelea kupiga picha kila kitu kilichokuwa kikitokea mahali hapo. Kwa hilo, Watanzania wengi walikasirika, chuki dhidi ya Rais Bokasa ikazidi kuongezeka kwani kwa kile alichokizungumza bilionea huyo kilikuwa kitu cha kawaida, alitoa dukuduku lake na hakutakiwa kukamatwa kama ilivyokuwa imetokea.
“Ila Kizota alikuwa na haki kabisa. Kwani katukana? Kwani kasingizia? Alichokizungumza ndiyo ukweli wa mambo,” alisema jamaa mmoja alipokuwa akizungumza na wenzake maskani.
“Shiiiii! Sasa hivi Usalama wa Taifa kila kona, unaweza kudakwa, hayo mambo kalalamikie chumbani ukiwa na mkeo,” alisema jamaa mwingine, kwa jinsi hali ilivyokuwa nchini, hakukuwa na haja ya kumwamini mtu yeyote yule.
***
Ndani ya siku chache tu, tayari urafiki baina ya Halima na Winfrida ulikuwa mkubwa. Walikuwa wakikutana na kuzungumza mambo mengi, alimpenda msichana mwenzake huyo kwa kuwa alikuwa na sura nzuri, msikivu na aliyeonekana kufahamu mambo mengi mno.
Halima alihisi kwamba alikuwa kwa mtu sahihi, aliamini kwamba Godwin aliyekuwa amezungumziwa ambaye alikuwa mpenzi wa Winfrida ndiye ambaye walikuwa wakimtafuta kwa udi na uvumba.
Baada ya kuzoeana sana ndipo Winfrida akaamua kumkaribisha Halima nyumbani kwake. Hiyo ikaonekana nafuu kwa msichana huyo kwani aliamini kwamba mara baada ya kufika huko angepata nafasi ya kumuona huyo Godwin na kupanga mikakati juu ya kumkamata mwanaume huyo.
Siku ambayo alikwenda nyumbani hapo alishangaa, hakukuonekana kuwa pazuri hata kidogo. Kulikuwa na godoro chini, chumba kibovu na humo ndani hakukuwa na kitu chochote kilichoonekana kuwa na gharama yoyote ile.
Halima alibaki akishangaa, alipoondoka nchini Somalia aliambiwa kwamba mwanaume aliyekuwa akienda kupeleleza huko alikuwa na uwezo mkubwa wa kuchezea kompyuta lakini pia alikuwa amehamisha kiasi kikubwa cha pesa kutoka benki lakini kwa jinsi alivyokuwa akikiangalia chumba hicho, hakikufanana na zile sifa za mtu huyo ambazo aliambiwa.
Akavumilia, alichokitaka ni kumuona mwanaume mwenyewe, alifananaje na alikuwa na uwezo gani hata kwenye kuzungumza. Hilo halikuwa tatizo lolote kwani baada ya saa mbili, Godwin akafika nyumbani hapo, alikuwa ametoka katika mkutano aliouandaa Bilionea Kizota kwa ajili ya kuzungumza na waandishi wa habari.
Alipofika nyumbani hapo na Halima kutambulishwa kwamba alikuwa mpenzi wa Winfrida aliyeitwa Godwin, hakuamini kama kweli mwanaume huyo ndiye ambaye alikuwa akiwasumbua Usalama wa Taifa wa Uswisi, FIS kwani muonekano wake ulikuwa wa kimasikini mno, alichoka na alionekana kutokuwa hata na shilingi mia tano mfukoni.
“Huyu ndiye mpenzi wako?” aliuliza Halima, hakuwa akiamini.
“Ndiye yeye! Yupoje kwani?”
“Mmh! Hakuna kitu! Ni mwanaume mzuri sana,” alijibu Halima.
Alichokifanya msichana huyo ni kuchukua miwani yake ya macho na kuivaa. Ilionekana kama miwani lakini ukweli wa mambo haikuwa miwani ya kawaida bali ilikuwa na kamera ambayo ilipiga picha moja kwa moja na kuzipeleka nchini Uswisi.
Ili kuwapa taarifa wenzake akamwambia Winfrida kwamba alitaka kwenda chooni kujisaidia haja ndogo, alipoonyeshewa, akaelekea huko, alipofika, akavua miwani ile na kuanza kuiangalia, kamera ndogo ikaanza kumpiga.
“Nimefanya kazi kwa kipindi kichache, nimempata Godwin ambaye sidhani kama ndiye yeye,” alisema Halima huku akitumia simu yake aliyoiunganisha na bluetooth ambayo ilipeleka taarifa kupitia miwani ile.
“Ndiye yule uliyempiga picha?”
“Ndiyo! Na pale ndipo anapoishi!”
“Yaani kwenye lile jalala?”
“Kile ni chumba!”
“Hapana! Atakuwa si huyo. Huyo tunayemtafuta ni yule aliyechukua pesa benki, yule ambaye anaisumbua serikali yetu mpaka ya huko Tanzania,” alisikika Bwana Kom.
“Kwa hiyo huyo si yeye?”
“Sijajua! Hebu endelea kuchunguza zaidi, nenda kampige picha zaidi,” alisema Kom.
“Sawa,” aliitikia Halima, hapohapo akaivaa miwani ile, akaufungua mlango, akashtuka, macho yake yakatua kwa Godwin ambaye naye alikuwa mlangoni hapo na dalili zilionyesha kwamba alisikia kila kitu kilichokuwa kimezungumzwa ndani.
“Ooh My Gosh....” alijikuta akisema huku macho yake yakitazamana na macho ya Godwin aliyekuwa amesimama karibu naye kabisa kwenye mlango wa choo.
***
Tangu Godwin alipoingia ndani ya chumba chake na macho yake kutua kwa msichana Halima, akawa na hofu kwamba inawezekana msichana huyo alikuwa mbaya kwani kwa muonekano alioonekana, hakuonekana kama msichana aliyekulia maisha ya Tanzania, ngozi yake, muonekano wake ulimtia shaka kupita kawaida.
Walikaa na kuzungumza, muda mwingi alikuwa akimwangalia Halima kiwizi, bado moyo wake ulikuwa na hofu na msichana huyo, alihisi kabisa kwamba alikuwa mtu mbaya ambaye hakutakiwa kabisa kuwa karibu naye.
Halima alizungumza mambo mengi chumbani pale mpaka alipotaka kuelekea chooni. Haraka sana naye Godwin akaaga kwamba alikuwa akienda nje, alipofika huko, alikuwa akihesabu sekunde huku akikadiria kwamba muda huu Halima alikuwa amekwenda chooni au bado.
“Atakuwa amekwenda, hebu subiri niende,” alisema Godwin.
Hakutaka kuchelewa, haraka sana naye akaelekea chooni kwani hakuamini kama kweli msichana huyo alikuwa ameshikwa na haja kweli au la. Alipofika huko, akanyata na kusogea karibu na mlango na kuanza kuisikiliza sauti ya msichana huyo ambaye alikuwa akizungumza na mtu mwingine kwa simu.
Mazungumzo yote aliyasikia, akapata uhakika kwamba Halima hakuwa msichana wa kawaida kama alivyosema Winfrida, akapata uhakika kwamba msichana huyo alifika mahali hapo kwa ajili ya kumpeleleza na kujua kama alikuwa ndiye yeye au si yeye.
Halima alipotoka chooni, macho yake yakagongana na Godwin ambaye alijifanya kutokujua kitu chochote kile kilichokuwa kikiendelea, alimwangalia msichana huyo, hapohapo akaanza kutoa tabasamu.
“Umemaliza?” aliuliza Godwin.
“Kumalizi nini shemeji?”
“Kujisaidia ili na mimi niingie manake tumbo limeanza kunivuruga,” alisema Godwin huku akiachia tabasamu pana lililokuwa na lengo la kumsahaulisha msichana huyo, asijue chochote kama kweli mwanaume huyo alikuwa Godwin aliyekuwa akimtafuta.
“Nimemaliza!” alisema Halima, akateremka ngazi ndogo na kuelekea chumbani. Godwin akaingia chumbani kwake, moyo wake ulikuwa na hofu, alijua dhahiri kwamba kama asingefanya lolote liwezekanalo basi msichana huyo angeweza kumkamata kizembe sana. Alichokihitaji kwa wakati huo ni namba yake ya simu tu.
Alipokaa kwa dakika kadhaa, akarudi chumbani ambapo akaungana na wasichana hao na kuanza kupiga nao stori. Alimuonyeshea Halima hali ya kumzoea sana, hakutaka msichana huyo awe na hofu yoyote ile, mwisho kabisa wakati akiaga, akamuomba namba ya simu ambapo kwa Halima halikuwa tatizo lolote lile, akamgawia ili kumfanya kuwa karibu naye.
“Amekwisha!” alisema Godwin.
Halima aliyejulikana kwa jina la Angelica akaondoka huku Winfrida akimsindikiza, haraka sana Godwin akachukua kompyuta yake ya mapajani na kuiwasha, alitaka kufanya vitu kwa haraka, kuingilia mawasiliano ya msichana yule.
Akaiingiza namba ile katika kompyuta yake na kisha kuifungua progamu yake iitwayo SpyGd ambayo aliitengeneza yeye mwenyewe na hakuwa ameisambaza sehemu yoyote ile. Akaiingiza namba ile, kompyuta ikaanza kumuonyeshea sehemu iliyoandikwa download ambapo kwa mbele kulikuwa na asilimia zilikuwa zikisogea mbele.
Ilipofika asilimia mia moja, ikabadilika na kujiandika searching, ikaanza kuitafuta simu ile na ilipoipata, ikaanza kuonyesha asilimia nyingine zikipanda huku kukiwa na neno lililoandikwa Hacking process.
Mpaka inafika mia moja, tayari alikuwa na uwezo wa kuingia katika simu ya Halima. Aliangalia meseji zote, aliona mawasiliano yote na kulikuwa na namba moja kutoka nchini Uswisi ambayo alikuwa amepigiwa na kupiga.
Alichokifanya ni kukata mawasiliano baina ya namba yake na namba ile ya Uswisi na kisha kuiingiza namba yake kwa namba ile na kuiiba kisha kuingia Google, akatafuta picha ya mwanaume mweusi kisha kuandika ujumbe kwenda kwa Halima huku akitumia namba ile ya Uswis, ujumbe uliosomeka:
“We have found his picture,” (tumeipata picha yake) aliandika.
Ujumbe huo ukaenda kwa Halima, alipoupata, haraka sana akaandika ujumbe wa kuomba kutumiwa picha hiyo ili aone kama kweli yule aliyekuwa amempata alikuwa ndiye yeye au mwingine.
“Send it to me,” (nitumie)
Hapohapo Godwin akamtumia picha ya mwanaume yule aliyoitoa Google. Ilikuwa picha ya mwanaume mweusi, Halima alipoiona na kuikumbuka sura ya Godwin ambaye alikutana naye, vilikuwa vitu viwili tofauti.
“Is he the one you found?” (ndiye yeye uliyempata?) aliuliza Godwin pasipo Halima kujua kama alikuwa akiwasiliana na mwanaume huyo.
“No! This is another one,” (hapana! Huyu mwingine kabisa) alijibu Halima.
Msichana huyo alichanganyikiwa, alijipa uhakika kwamba hatimaye Godwin alikuwa amepatikana lakini ujumbe wa simu alioupata kutoka nchini Uswisi tena huku ukiambatanisha na picha ya huyo Godwin aliyekuwa akitafutwa, ukamvunja moyo na kuona kwamba kazi kubwa aliyokuwa ameifanya haikuwa na faida yoyote ile.
Huo ndiyo ukawa mwisho wa kuelekea kwa Godwin kwani aliamini kwamba hata kama angekwenda huko na kudumisha urafiki na Winfrida bado kungekuwa na ugumu wa kumpata kwa kuwa yule aliyefikiri kwamba alikuwa Godwin, hakuwa mwenyewe.
Akaiprinti picha ile, akawa nayo kila alipokuwa akienda. Akaanza kumtafuta mwanaume huyo hapo Tandale. Hakujua kama hiyo ilikuwa picha ya mtandao ambayo ilitolea huko nchini Ghana. Kila siku alipokuwa akilala, aliiweka picha hiyo pembeni yake, alikuwa akiiangalia sura ile na kuikariri na kesho yake alikuwa akiingia mtaani na kuanza kumtafuta.
Ilikuwa kazi ngumu, aliuona ugumu mkubwa mbele yake, hakutaka kukata tamaa, aliendelea kupambana kwa ajili ya kuhakikisha anampata mtu huyo na kumkamata kama ilivyotakiwa kuwa.
Wakati Godwin akiwa ameidukua namba ya Bwana Kom kule Uswisi, pia aliidukua namba ya Halima, kwa maana hiyo Kom alipokuwa akimtumia ujumbe Halima, mtu aliyekuwa akijibu alikuwa Godwin na hata alima alipokuwa akimtumia Bwana Kom ujumbe, mtu aliyekuwa akijibu alikuwa huyohuyo Godwin.
“Umefikia wapi?” aliuliza Kom kupitia ujumbe mfupi wa meseji.
“Bado naendelea kumtafuta, nimejaribu kuwashirikisha baadhi ya watu na wamesema kwamba mtu huyo yupo, si mgeni machoni mwao,” alijibu Godwin na kwa Bwana Kom ilionyesha kama Halima ndiye aliyeituma meseji hiyo.
****
Rais Bokasa alichanganyikiwa, hakuamini kilichokuwa kikiendelea kwamba hata yule bilionea mkubwa, Bwana Kizota hakuwa akimkubali na alisema wazi kwamba alikuwa akimchukia kwa kuwa yeye ndiye alikuwa mtu aliyechangia kwa Tanzania kuwa kama ilivyokuwa.
Moyo wake ukawa na hasira kali, hakutaka kuchelea, hapohapo akampigia simu IGP Ng’osha na kumwambia kwamba ndani ya dakika kumi tu alitaka kuona bilionea huyo akikamatwa kitu ambacho kilifanyika ndani ya dakika saba tu.
Mambo yalianza kuharibika, hali ya nchi ilianza kusumbua, ilimuumiza kichwa na kuhisi kwamba watu hao walikuwa wakitumiwa na mtu fulani, alihisi kwamba alikuwa Godwin lakini baadaye akaona kwamba kijana huyo asingeweza kuwatumia watu hao, mkurugenzi wa Usalama wa Taifa na Bilionea Kizota, hakika kilikuwa kitu kisichowezekana.
Kwenye mitandao, kila mtu alikuwa akizungumza lake, watu wengi walifurahi kwani hawakumpenda rais huyo hata kidogo. Wakati mwingine watu waliona hiyo miezi miwili mpaka rais huyo kujiuzulu au kupinduliwa ilikuwa mingi mno, kila mmoja alitamani kuona jambo hilo likitokea hata muda huo.
Hakuwa na kimbilio, aliogopa, wakati mwingine aliitwa na marais wenzake wa Afrika kwa lengo la kwenda huko na kupumzisha akili lakini alikataa kabisa kufanya hivyo kwa kuhisi kwamba kama angeondoka nchini basi angeweza kupinduliwa huku nyuma.
“Bado kuna mambo mengi napambana nayo, siwezi kuja huko, nataka nipambane mpaka nitakapoona mwisho wake nini,” alisema Rais Bokasa.
Huo ndiyo ulikuwa ukweli wenyewe, hakutaka kuondoka nchini Tanzania, aliendelea kubaki huku akisimamia msimamo wake kwamba kamwe asingeweza kuondoka kwani kama angefanya hivyo basi huo ndiyo ungekuwa mwisho wa kila kitu.
Alitamani kuwa rais milele, hakutaka kuachia madaraka kwa kuamini kwamba kwa yale yote ambayo aliyafanya, ingetokea siku moja kutoka madarakani basi angeweza kushtakiwa kwa uchafu wote aliokuwa ameufanya katika kipindi chake cha madaraka.
“Ila nini kitatokea kama siku nikipinduliwa kama anavyosema Godwin kwenye mitandao? Inawezekana amewaandaa watu kwa ajili ya kufanya hivi! Nitafanya nini?” alijiuliza huku akiwa chumbani kwake.
Hapo ndipo alipopata wazo kuwasiliana na mtu aliyeitwa kwa jina la Mikel Ludovic, mwanaume aliyekuwa akiishi nchini Urusi ambaye alikuwa miongoni mwa wanajeshi waliokuwa wakitengeneza mabomu ya nyuklia nchini humo.
Akataka kuonana naye, yaani mwanaume huyo asafiri mpaka nchini Tanzania na kuzungumza naye. Hilo halikuwa tatizo, mwanaume huyo akasafiri na kuingia nchini Tanzania kisiri huku watu wakiwa hawajui kama Ludovic alikuwa nchini.
Wakakutana na kuzungumza mambo mengi, alichokuwa akikihitaji rais huyo ni gesi aina ya nitrogen trioxide iliyokuwa na sumu kali. Alimwambia kwamba alitaka aandaliwe sumu hiyo kwa kuwa alikuwa na kazi kubwa alitaka kuifanya.
“Haina shida. Nitakuletea ujazo wa kutosha kabisa,” alisema Ludovic na kuondoka.
Ulikuwa mpango wa siri ambao alikuwa ameuandaa na mwanaume huyo, hakutaka kitu chochote kile kijulikane kwani hata watu wa hapo ikulu walimuona Mzungu huyo akiingia lakini hakukuwa na aliyejua sababu ya mwanaume huyo kufika nchini na kuonana na rais huyo.
“Hakuna mtu atakayeweza kukaa ikulu. Ama zangu ama zao,” alisema Rais Bokasa huku akionekana kudhamiria hasa kuhakikisha anabaki ikulu mpaka kifo chake.
Ludovic alikuwa ndani ya ndege, moyo wake ulikuwa na furaha tele, katika maisha yake, hakukuwa na kitu alichokuwa akikichukia kama watu waliokuwa na ngozi nyeusi. Alikuwa akitengeneza mabomu ya nyuklia huku kila siku akimsisitiza rais wake kwamba kama inawezekana waende Afrika na kuhangamiza bara zima ili weusi wasiendelee kuwepo tena.
Kitendo cha kuitwa na rais huyo na kuambiwa kwamba alitakiwa kusafirisha gesi kwa ajili ya kufanya mauaji hayo, kwake alikuwa na furaha tele, tena wakati mwingine alimshukuru Mungu kwa kuwa alikisikia kilio chake.
“Hiki ndicho nilichokuwa nikikitaka. Ameagiza ujazo wa lita kumi. Mimi nitamtumia ujazo wa tani moja kabisa. Yaani ikiwezekana nchi nzima aiangamize kwa sumu hiyo,” alisema Ludovic huku ndege ikikata mawingu kuelekea Moscow nchini Urusi.
***
Jenerali Ojuku alikuwa chumbani kwake, kichwa chake kilikuwa na mawazo tele, aliikumbuka familia yake ambayo mpaka kipindi hicho hakujua mahali ilipokuwa. Moyo wake ulijawa na hasira tele, hakuamini kama kweli mwanajeshi yeye, mwenye cheo kikubwa nchini Tanzania ambaye nyuma yake kulikuwa na vikosi vyote vya jeshi alichezewa mchezo kama ule.
Alihuzunika, wakati mwingine alikuwa akisimama na kutembea huku na kule, aliumia moyoni mwake na hakujua ni kitu gani ambacho angefanya ili kuipata familia yake hiyo ambayo kwake ilikuwa kila kitu.
Wakati amekaa hapo, simu yake ya mkononi ambayo ilikuwa mezani ikaanza kuita, hakuifuata na kuipokea, aliiacha iendelee kuita mpaka ilipokata na baadaye kuanza kuita tena. Kwa kuwa ilikuwa ni kelele, akaifuata na kuangalia kioo, hakuiona namba bali maneno yaliyoandikwa ‘Private call’, akaipokea kwani alimjua mpigaji.
“Hallo!” aliita mara baada ya simu kuiweka sikioni.
“Nisikilize kwa makini sana. Leo inaweza kuwa siku yako ya mwisho kwa familia yako kuvuta pumzi ya dunia hii,” alisikika Godwin.
Ojuku akashusha pumzi ndefu, hakukuwa na maneno yalilouchoma moyo wake kama kuambiwa maneno mabaya kuhusu familia yake, akajua kabisa kwamba huyo mwanaume alitaka kufanya kitu fulani, hivyo akabaki akimsikiliza.
“Ninataka ufanye kitu kimoja.”
“Kitu gani mkuu?”
“Uite waandishi wa habari, useme kwamba humuamini rais na hivyo utamtaka aondoke madarakani haraka sana,” alisema Godwin.
“Unasemaje?”
“Una saa tano za kufanya hivyo! Usipofanya, utazikuta maiti za familia yako ufukweni,” alisema Godwin na kukata simu.
“Halo..halo..halo..” aliita Ojuku lakini tayari simu ilikuwa imekatwa.
Hakuamini kile alichokuwa ameambiwa, kwake, aliona mawenge, alichanganyikiwa kupita kawaida kwani katika maisha yake yote hakuamini kama ingetokea siku ambayo angeambiwa maneno kama hayo.
Kwake, familia yake ilikuwa bora zaidi lakini kile alichokuwa ameambiwa kilimchanganya sana kichwa chake. Pale kochini alipokuwa amekaa alipaona kama padogo, akasimama na kuanza kufikiria kwa makini kila neno aliloambiwa.
Hakuwa na jinsi, kama alitaka kuiokoa familia yake alitakiwa kufanya kile alichoambiwa kwani hata alipojifikiria sana, rais huyo hakuwa akipendwa, kila mtu alitamani kuona siku yoyote ile akiondoka madarakani.
Hapohapo akachukua simu na kumpigia Mhariri Mtendaji wa Global Publishers, Saleh Ally na kumwambia kwamba alitaka kuonana na waandishi wa habari kutoka katika Kampuni ya Magazeti ya Global Publishers, baada ya hapo, akavipigia simu vyombo vingine vya habari kwamba alikuwa akitaka kuzungumza nao maneno kuhusu hali iliyokuwa ikiendelea nchini.
Waandishi walipopewa taarifa, haraka sana taarifa hizo zikarushwa katika mitandao ya kijamii ambapo huko kila mtu akabaki na maswali, hali iliyokuwa ikiendelea nchini ilimfurahisha kila mmoja kwani kitu ambacho hawakuwa wakikipenda kuona kikiendelea ni kitendo cha rais huyo kuendelea kuiongoza Tanzania.
“Naye anataka kumkataa rais au?” aliuliza jamaa mmoja.
“Mmh! Kwa Ojuku? Hakuna kitu kama hicho!”
“Sasa kwa nini naye amewaita waandishi wa habari?”
“Labda anataka kuwaeleza kuhusu msimamo wake kwamba jeshi la wananchi litamuunga mkono rais mpaka mwisho,” alisema jamaa mwingine.
“Hebu tusubiri tuone!”
Kila mtu masikio yake yalikuwa huko, watu ambao walikuwa bize na mambo yao, wakaachana nayo na kuanza kusikiliza kile kilichokuwa kikiendelea huko. Mitandao mingi ya habari ikaanza kurusha kila kitu kilichokuwa kikiendelea huko.
Hakukuwa na mtu aliyejua kile kilichokuwa kikiendelea, hata Meja Jenerali naye hakujua kitu chochote kile na hata alipokuwa akimpigia simu mkuu wake kumuuliza kile alichotaka kuzungumza, hakumwambia kitu chochote kile.
Zaidi ya waandishi wa habari themanini walikusanyika katika Ukumbi wa Diamond Jubilee kwa ajili ya kusikiliza kile walichokuwa wameitiwa mahali hapo. Baada ya dakika ishirini, magari ya kijeshi yakaanza kuingia mahari hapo na wanajeshi zaidi ya ishirini wakateremka huku wakiwa na bunduki zao kana kwamba walikuwa wakielekea vitani.
Gari alilokuwa Jenerali Ojuku likasimama, mwanaume huyo akasimama na moja kwa moja kuanza kuelekea katika ukumbi huyo huku waandishi wa habari wakimpiga picha mfululizo na wengine wakichukua video.
Alipofika ndani, akaelekea mahali ambapo paliandaliwa kwa ajili yake na kutulia hapo. Hakuzungumza kitu kwanza, akaanza kuwaangalia waandishi waliokuwa ndani ya ukumbu huo ambapo baada ya dakika kadhaa akaanza kuzungumza.
“Najua nyie wote mtakuwa mnafahamu mambo yanayoendelea ndani ya nchi hii! Ni mambo ya ajabu sana ambayo yaliwapelekea watu wengi kuona kwamba Rais Bokasa ananyanyasa watu na kujiona kwamba yeye ni rais wa milele,” alisema Ojuku, akanyamaza kidogo na kuendelea.
“Hili ni jeshi la wananchi, tunapoona mambo hayaendi sawa, chuki ya wananchi inakuwa kubwa, ni lazima tujiulize ni wapi tumekosea. Nimekaa na kujifikiria na mwisho wa siku kugundua kwamba nchi yetu inapotea, watoto na wajukuu zetu wataishi vipi kama sisi wenyewe hatutotengeneza mazingira mazuri kwa ajili yao?” aliuliza Ojuku na kuendelea:
“Jeshi la wananchi limekaa chini na kuamua kitu kimoja tu kwamba hatumuungi mkono Rais Bokasa na hivi ninavyoongea, ninampa saa moja kukusanya kila kitu kilicho chake ikulu na aondoke haraka sana,” alisema Ojuku.
Kitu ambacho hakikutegemewa na mtu yeyote ndani ya ukumbi ule, waandishi wa habari wote wakaanza kupiga makofi huku wengine wakishangilia. Tais huyo hakupendwa, kila mtu alitaka kuona akiondoka haraka sana madarakani kwani aliiharibu nchi na kujifanya mungu mtu ambaye hakusikia la mtu yeyote yule nje ya ikulu.
Ojuku hakuongea sana, alipomaliza akasimama na kuondoka zake huku nyuma akiacha shangwe ambazo hazijawahi kusikika kabla. Kwenye mitandao, kila mtu alikuwa akizungumza lake, hakukuwa na mtu ambaye hakuunga mkono msimamo wa jeshi la wananchi, kila mmoja alipongeza kwa hatua kubwa ambayo jeshi hilo limeliona, haraka sana waandishi wa habari wakaondoka hapo na kuelekea ikulu, walitaka kupiga picha kila kitu kilichokuwa kikiendelea huko, walitaka kumuona rais huyo akiondoka madarakani kwa agizo la Jenerali Ojuku au kama alishindwa, basi jeshi liingie kumtoa kinguvu.
***
Wiki moja ilipita tangu Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa, Noel kuamua kujitoa kumuunga mkono. Moyo wake ulikuwa umevurugwa na kitu pekee alichokuwa akikisubiria kipindi hicho kilikuwa ni gesi ya sumu ambayo aliiagiza kutoka nchini Urusi ifike na yeye kufanya kile alichokusudia kufanya.
Hakutaka kuondoka madarakani, alilewa, alitaka kuona akiendelea milele na wakati mwingine alikuwa akijilaumu kwamba kwa nini hakufanya yale ambayo wananchi walitakata kuona akiyafanya, alijiona kuwa mjinga, lakini pamoja na hayo yote, hakutaka kuona akiondoka ikulu pasipo kufanya jambo lolote lile.
Akaendelea kuwasiliana na Ludovick ambaye alimwambia kwamba tayari mzigo wa gesi ya sumu ulitumwa kutoka nchini Urusi kwa kutumia meli na muda wowote ule mzigo ungewasili nchini Tanzania.
“Nimekutumia tani nzima,” alisema Ludovick kwenye simu.
“Nashukuru sana kwa kunijali. Nitakuingizia pesa zako,” alisema Bokasa na kisha kuzihamisha pesa kutoka kwenye akaunti yake na kumtumia Ludovick aliyekuwa nchini Urusi kama malipo yake.
Baada ya siku mbili akawatuma vijana wake kwenda nbandarini ambapo huko wakachukua mitundi minne ya gesi na kwenda nayo ikulu. Hakutaka kumwamini mtu yeyote, alitaka kufanya jambo ambalo aliamini kwamba lingeweka historia nchini Tanzania.
Baada ya siku kadhaa kupita na kusikia kwamba Jenerali Ojuku aliita waandishi wa habari kwa ajili ya kuzungumza nao, alijua kabisa kwamba naye alikuwa akienda kwa ajili ya kumkataa kwani kama angekuwa mtu wake, angempigia simu na kumwambia kile ambacho alikuwa njiani kuwaambia waandishi wa habari.
Alifungulia redio na kusikiliza kila kitu na familia yake. Moyo wake ulimuuma kupita kawaida, akaona kwamba alibaki yeye peke yake hivyo alitakiwa kupambana yeye kama yeye. Aliposikia kwamba alipewa saa moja tu kwa ajili ya kuondoka, akaiambia familia yake kwamba walitakiwa kuelekea nje ambapo wangechukua gari na kuondoka zao kwenda uwanja wa ndege.
“Na wewe?” aliuliza mkewe.
“Nitakuja tu! Nitakimbia Kenya. Nyie nendeni kwanza,” alisema Bokasa na familia yake kuondoka.
Ikulu nzima alibaki peke yake, alikuwa akijifikiria namna ya kuanza. Akachukua mitudi ile ya gesi na kuanza kunyunyizia katika kila chumba, alitaka kumuua mtu yeyote ambaye angeingia ndani ya jumba hilo kubwa. Alipulizia kwenye kila chumba na alipomaliza, akachukua simu yake, akaenda kwenye akaunti ya serikali na kuhamisha pesa zote zaidi ya dola trilioni kumi na kuzipeleka katika akaunti yake ya siri nchini Ubelgiji.
“Yeyote atakayeingia, hakika atakufa,” alisema Bokasa, akatoka nje ambapo akachukua gari, likampeleka ufukweni kisiri, akapanda boti na kuanza safari ya kuelekea Mombasa huku akiwa ameacha sumu ya kutosha ndani ya jumba lile.
Baada ya saa moja kutimia, Jenerali Ojuku akawaambia wanajeshi wake kwenda ikulu na kuvamia ili hata kama rais huyo alikuwa ndani ya jumba hilo basi waweze kumchukua na kuondoka naye.
Hiyo ilikuwa ni amri ambayo moja kwa moja ikapokelewa na wanajeshi hao na kuanza kuelekea huko. Walipofika, wanajeshi ishirini wakaanza kuingia ndani huku wengine wakibaki nje.
Wakaingia ndani mpaka sebuleni ambapo hapo wakaanza kuelekea kwenye vyumba vingine. Walipoanza kufungua tu, wanajeshi hao wakaanza kuanguka kama mizigo, gesi kali yenye sumu ikawapata na hivyo kuwapukutisha kama kuku.

Je, nini kitaendelea?
tukutane cku nyingine naamin dadaa angu atakuwa hewani uck mwema
 
DUNIA HAINA USAWA- 31

“This is insane,” (huu ni wendawazimu)
“Boss! We have to wait for a little bit,” (bosi! Tusubiri kidogo)
“For how long?” (kwa muda gani?)
“Atleast two weeks.” ( Hata kwa wiki mbili)
Bwana Kom alichanganyikiwa, hakuelewa ni kitu gani kilichokuwa kikiendelea nchini Tanzania, kwake, Godwin alikuwa mtu mdogo sana ambaye hakutakiwa kutumiwa nguvu kumtafuta lakini kitu cha ajabu, Halima alikuwa mtu wa tatu kutumwa huko lakini hakukuwa na mafanikio yoyote yale.
Hakutaka kusikia jambo lolote lile kwa wakati huo, kitu alichokuwa akikihitaji ni kuona mwanaume huyo akikamatwa tu. Alihamisha kiasi kikubwa cha pesa kutoka katika Benki ya Geneva, kitendo cha kushindwa kumkamata kilimaanisha kwamba wateja wasingekuwa na imani na benki hiyo kubwa duniani ambayo ilikuwa na wateja wengi kipindi hicho.
Aliamini kwamba mtu aliyekuwa akiwasiliana naye alikuwa Halima, kila alipomtumia meseji, alijibu kwa kumwambia kwamba hali ilikuwa ngumu, mategemeo makubwa aliyokuwa nayo ya kumkamata mtu huyo hakuwa nayo tena kwani kila alipokuwa akimtafuta, hakuambulia kitu chochote kile.
Siku zilikatika, hakupata majibu chanya, hiyo ilimsikitisha na wakati mwingine kuona akifanya uzembe mkubwa mno. Alisubiri zaidi majibu kutoka kwa msichana huyo lakini kila siku majibu yalikuwa yaleyale.
Akawasiliana na mkurugenzi wa Benki ya Geneva, alitaka kujua kama akaunti zile zilizohamishiwa pesa hizo zilirudishwa au la, alipowasiliana naye, akaambiwa kwamba hakukuwa na pesa yoyote iliyorudi.
Hilo lilimchanganya, vijana wa IT katika benki hiyo walipambana vya kutosha lakini hakukuwa na mtu aliyefanikiwa, waliziona pesa lakini kila zilipotakiwa kutoka, hazikutoka na mbaya zaidi, baadaye zikahamishwa kwenda nchini Marekani kisha kupelekwa katika akaunti nyingine ambayo hawakuifahamu.
Wakati Bwana Kom akipambana kwa ajili ya kuhakikisha kwamba Godwin anapatikana, Godwin mwenyewe alikuwa akihangaika kumuondoa Rais Bokasa kutoka madarakani. Alihakikisha anaitumia akaunti yake ya Mabadiliko ya Kweli kuhakikisha kwamba Watanzania wanapata taarifa ambazo wasingeweza kuzipata sehemu yoyote ile.
Watu walitembelea huko, kwa siku zaidi ya watumiaji milioni thelathini walikuwa wakiingia kuona ni kitu gani kilikuwa kikiendelea huko. Akaunti ile ilizidi kupata nguvu na watu wengi kutamani kumuona huyo mtu aliyekuwa akiiendesha akaunti hiyo, alifananaje na kwa nini alikuwa akipata data nyingi kiasi kwamba mpaka viongozi wenyewe walikuwa wakishangaa.
Winfrida hakujua ni mwanaume wa aina gani alikuwa naye, alipenda sana kutembelea akaunti hiyo iliyokuwa katika Mtandao wa Kijamii wa Instagram, alipenda kila kitu kilichokuwa kikiandikwa humo lakini hakujua kama mwanaume aliyekuwa naye ndiye aliyekuwa akihusika na akaunti hiyo ambapo alikuwa akiandika kwa kupitia simu yake ambayo aliificha na wakati mwingine kutumia kompyuta yake.
“Nimesikia Jenerali Ojuku anaita waandishi wa habari kwa ajili ya kuzungumza nao, naye kuna jambo anataka kufanya au?” aliuliza Winfrida huku akimwamsha mpenzi wake aliyekuwa amelala.
Haraka sana Godwin akashtuka kutoka usingizini, kitendo cha kusikia kwamba mtu aliyekuwa amezungumziwa alikuwa Jenerali Ojuku, alitaka kusikia kile kilichokuwa kikiendelea. Alimpigia simu kabla na kumwambia kwamba alitakiwa kutokumuunga mkono Rais Bokasa, kitendo cha kuita waandishi wa habari kilimaanisha juu ya kile alichotakiwa kukifanya.
Akawasha kompyuta yake na kuanza kumwangalia, kwa jinsi alivyoonekana, hakuonekana kuwa na amani, moyoni mwake alikuwa na jambo kubwa alilotaka kuzungumza mahali hapo, waandishi wa habari kutoka katika vyombo mbalimbali vya habari walikuwa mahali hapo kwa ajili ya kuripoti kila kitu kilichokuwa kikiendelea.
Alizungumza kwa marefu lakini mwisho wa siku akaweka wazi kila kitu kwamba hakuwa akimuunga mkono Rais Bokasa na alimalizia kwa kumpa saa moja tu la kuondoka ikulu kwani nchi ingekuwa chini ya jeshi kwa siku kadhaa.
Winfrida akabaki akitabasamu, hakuamini alichokuwa amekisikia, kitu ambacho kila siku alimuomba Mungu ni kumuona rais huyo akiondoka madarakani. Alikuwa kiongozi mbaya, aliyetumia kiasi kikubwa cha pesa kwa matumizi yake binafsi lakini pia alihakikisha kila mtu anayekuwa waziri anakuwa na roho ya tamaa kama aliyokuwanayo na ndiyo maana nchi haikusonga mbele, hakukuwa na kiongozi aliyekuwa na uchungu na nchi yake.
Alipomaliza, Godwin akafungua programu yake kwa ajili ya kuangalia simu ya Rais Bokasa, alijua fika kwamba rais huyo alikuwa amepanga mipango siku hiyo kwa ajili ya kukimbia nchi na kwenda sehemu nyingine. Alipoingiza namba hiyo na kuangalia, akaona kitu ambacho kilichomshtua sana.
Akaona mawasiliano yaliyokuwa yakifanyika baina yake na mtu aliyejulikana kwa jina la Ludovick kutoka nchini Urusi. Haraka sana akaingia Google na kuangalia kuhusu mwanaume huyo, alitaka kujua ni nani na alikuwa akijihusisha na jambo gani.
Alichokiona ni kwamba mwanaume huyo alikuwa mtengeneza mabomu ya nyuklia nchini Urusi aliyekuwa na uwezo mkubwa kiasi kwamba hata Marekani wenyewe walikuwa wakimuhofia. Aliyaona mazungumzo yao kwa njia ya meseji, akaingia katika barua pepe yake pia ambapo huko akaona kukiwa na ujumbe kuhusu sumu ya gesi ambayo ilitakiwa kuingizwa nchini Tanzania na kuipulizia katika kila chumba ikulu.
“Mungu wangu! Kumbe sumu iliagizwa tangu juzi!” alisema Godwin huku akionekana kushtushwa na kile alichokuwa akikiona.
Haraka sana akampigia simu Ojuku kwa lengo la kumweleza kile kilichokuwa kimetokea kwamba kama inawezekana akawasiliana na wahusika kuzuia watu kuingia ndani ya ikulu kabla ya watalaamu wa masuala ya gesi kwenda kupulizia gesi nyingine kwa ajili ya kuitoa sumu hiyo.
Kila alipompigia simu Ojuku, haikupokelewa. Hiyo ilimpa presha kubwa, akaona kwamba kama angechelewa basi kungekuwa na waathirika wa sumu hiyo, akavaa nguo zake haraka sana, hakutaka kubaki mahali hapo, piga ua ilikuwa ni lazima kuhakikisha kwamba hakuna mtu yeyote anayeruhusiwa kuingia ndani ya ikulu hiyo.
“Vipi tena?” aliuliza Winfrida, kila alipomwangalia mpenzi wake namba alivyokuwa akibadilisha nguo harakaharaka, hakumwelewa.
“Kuna kitu natakiwa kukiwahi.”
“Kitu gani?”
“Subiri! Nitakuja, nitakwambia,” alisema Godwin, hakutaka kuendelea kubaki chumbani humo, akaondoka kuelekea huko.
Njiani, hakuacha kumtafuta Jenerali Ojuku kwenye simu, kama kawaida mwanaume huyo hakuwa akipokea simu, iliendelea kuita zaidi na zaidi kitu kilichomfanya kutokufanikiwa kwa kile alichokitaka.
“Unajua kuendesha pikipiki kwa kasi kama ndege?” aliuliza Godwin huku akimwangalia dereva bodaboda.
“Hilo wala usijali! Una moyo wa kuvumilia?” aliuliza dereva bodaboda kwa kujiamini.
“Ndiyo maana nikauliza unajua!”
“Ninajua! Hata ukitaka niendeshe kama Air Force One, wewe tu,” alisema dereva huyo.
“Niwahishe Magogoni.”
“Mjini?”
“Ndiyo!”
“Huko wanakataza bodaboda kuingia!”
“Hata kwa malipo ya laki moja bado hutaki kuingia?”
“Kama ni hivyo poa. Kalia mchuma nikisanue,” alisema dereva huyo kwa lugha ya kihuni, Godwin akapanda na kuondoka mahali hapo.
Kasi waliyoondoka nayo kila mtu alishangaa. Muda wote Godwin macho yake yalikuwa kwenye saa yake, muda aliokuwa ametoa Ojuku zilibaki dakika mbili tu kabla ya wanajeshi kuingia ndani ya ikulu hiyo na kumuondoa rais huyo kinguvu.
Hakukuwa na foleni iliyowababaisha, walipenya katikati ya magari, kwa kasi kubwa na hata pale kulipokuwa na mataa kama Magomeni, Fire walipita kana kwamba walikuwa majambazi waliotoka kuiba benki.
Walichukua dakika tano tu mpaka kufika Magogoni ambapo dereva aliposimamisha tu pikipiki yake, Godwin akateremka pasipo hata kuzungumza na dereva huyo. Akaanza kupiga hatua kwenda getini ambapo kulikuwa na wanajeshi zaidi ya ishirini waliosimama wakiwa na bunduki zao.
“Wewe nani? Simama! Hutakiwi kusogea huku,” alisema mwanajeshi mmoja huku akimwangalia Godwin.
“Kuna kitu! Humo kuna sumu!” alisema Godwin huku akisogea kwa kasi.
“Nimesema simama!”
“Huko kuna sumu! Rais ameacha sumu vyumbani,” alisema Godwin huku akiwasogelea wanajeshi wale waliokuwa wakimnyooshea bunduki.
“Paa....paa...paa...” ilisikika milio ya risasi zilizokuwa zimepiga chini, karibu kabisa na miguu yake kumtaka kusimama. Akatii na kusimama.
“Unataka nini? Umetoka wapi? Wewe ni nani?” yalikuwa maswali matatu mfululizo yaliyotoka kwa mwanajeshi mmoja aliyekuwa na kitambaa kilichoandikwa MP mkononi.
“Rais amecha sumu ya gesi, naomba asiingie mtu, huyu rais anataka kummaliza kila mtu atakayeingia humu,” alisema Godwin huku akiwaangalia wanajeshi hao waliokuwa wakimshangaa.
Hata kabla hajaeleza zaidi kile kilichokuwa kimetokea ndani ya vyumba vya ikulu ile, wanajeshi wakashangaa kuwaona wenzao wakianza kutoka nje huku wakikimbia, wengine wakaanza kuanguka huku wakikohoa, damu zilikuwa zikiwatoka midomoni, puani, machoni na masikioni.
Kila mmoja alishangaa, hawakujua kilichokuwa kikiendelea mpaka wanajeshi hao kuwa katika hali hiyo. Wakaogopa, hapohapo Godwin akawaambia kwamba walitakiwa kuondoka katika eneo hilo, ikulu haikukalika, kulikuwa na gesi yenye sumu iliyokuwa imepulizwa humo ndani.
“Sogeeni, sumu inasogea huku. Tokeni huko,” alisema Godwin hali iliyowafanya wanajeshi hao waliokuwa wamesimama hapo getini kusogea.
Waliwaona wenzao wakihangaika, wakiomba msaada, sumu ilikuwa ikiwateketeza, iliwamaliza lakini hakukuwa na mtu aliyesogea, kila mmoja alikuwa akiogopa. Moyo wa Godwin uliuma, hakuamini kama Rais Bokasa angeweza kufanya upumbavu kama ule.
Kwa kuwa yeye ndiye aliyeleta taarifa kuhusu sumu ile, walichokifanya wanajeshi hao ni kumuweka chini ya ulinzi, walitaka kufahamu baadhi ya vitu, yeye alikuwa nani? Alijuaje kama ndani ya ikulu ile kulikuwa na sumu iliyowamaliza wanajeshi wenzao?
“Mimi ni msamaria mwema. Niliweza kubamba mawasiliano ya Rais Bokasa na mtu anayejulikana kwa jina la Ludovick kutoka nchini Urusi,” alisema Godwin.
“Unatudanganya. Utakuwa umehusika katika upandikizaji wa sumu hii ndani ya hii ikulu. Mchukueni, mpelekeni kambini. Ninataka kusikia ukweli baada ya uso wake kupendeza na kuonekana mnene, akikataa, mpeni kaoshi avae,” alisema mwanajeshi huyo kwa hasira, aliposema kwamba uso wake upendeze, alimaanisha apigwe sana mpaka avimbe, na aliposema akutwe amevaa kaoshi alimaanisha kwamba akatwe mikono kama tu hatosema ukweli juu ya kile kilichokuwa kimetokea.
Hapohapo wanajeshi wanne wakambeba msobemsobe na kumuingiza ndani ya gari. Hata kabla gari halijawashwa, tayari alianza kushushiwa mkong’oto hali iliyomfanya kulia kama mtoto, akajua tu kwamba huko alipokuwa akipelekwa, hakukuwa sehemu ya amani hata kidogo.
***
Kila mtu alikuwa na huzuni tele, hawakuamini kile kilichokuwa kimetokea kwamba wanajeshi zaidi ya ishirini walikufa walipokuwa wameingia ikulu. Kila mmoja alishangaa, hakukuwa na mtu aliyejua kama humo kulikuwa na sumu ya gesi, wengi wakahisi kwamba Rais Bokasa aliamua kuweka uchawi wake ambao ulimwangamiza kila mtu aliyeingia ndani.
Kwenye mitandao, kila mtu alikuwa akizungumzia lake, wengi walikasirika, walionyesha hasira zao waziwazi, hawakupenda kuona lile lililotokea, malalamiko yalikuwa mengi mno kiasi kwamba IGP Ng’osha akapiga mkwara kwamba hakukutakiwa na mtu yeyote aliyetakiwa kulizungumzia jambo hilo katika mitandao ya kijamii.
Wakati hayo yakiendelea, hakukuwa na mtu aliyeruhusiwa kuingia ndani ya jengo hilo tena, hali ilikuwa ni ya hatari na baada ya kugundua kwamba humo kulikuwa na gesi, walitakiwa kwanza kuwasiliana nao na watu wa kitengo cha gesi ili kufika mahali hapo na kueleza hiyo ilikuwa ni gesi ya aina gani na ilitakiwa kuondolewa namna gani.
Jenerali Ojuku alikasirika, kuwapoteza wanajeshi wake kwa dakika kadhaa ilimuuma moyoni mwake, alikasirika na muda mwingine alipokuwa akiongea, alionekana kuumia mno. Alitaka kujua mahali Bokasa alipokuwa, hata kama alikuwa amekimbia, ilikuwa ni lazima kumpata na kupelekwa mahakamani na kushitakiwa kwa kile alichokuwa amekifanya.
“Ni lazima atafutwe haraka sana,” alisema Ojuku huku akiwa amevimba.
“Sawa mkuu! Ila kuna mtu tumempata, nahisi naye alihusika katika hili,” alisema mwanajeshi mmoja.
“Yupo wapi?”
“Kambini!”
Hakutaka kuchelewa, hakukuwa na muda wa kupoteza. Hapohapo akaondoka kuelekea kambini. Njiani, alikuwa na hasira, kila kitu kilichotokea kwake ilikuwa ni aibu kubwa kwamba kwa nini katika uongozi wake litokee jambo la kijinga kama hilo? Hakutaka kuona akishindwa, ilikuwa ni lazima kupambana mpaka kuhakikisha kwanza Bokasa anapatikana haraka iwezekanavyo.
Alipofika kambini, akateremka na kuanza kuelekea ndani ya jengo moja ambalo ndipo alipoambiwa kwamba kijana huyo alikuwemo. Wanajeshi wote waliokuwa wakipishana naye walimpigia saluti kama kumuonyeshea heshima. Hakuwa na muda wa kujibu saluti hizo, alichokuwa akikitaka ni kuonana na kijana huyo tu.
Akatembea mpaka katika chumba kimoja kilichoandikwa Goligotha mlangoni, akaufungua mlango, alipoingia, macho yake yakatua kwa Godwin aliyekuwa kwenye kiti. Kwa kumwangalia tu ilikuwa vigumu kuamini kama mtu huyo alikuwa hai au tayari alikuwa amekufa.
Uso wake ulivimba, upande mmoja wa jicho ulikuwa mkubwa, mashavu yake yaliumuka huku damu zikiwa zimetapaa katika uso mzima. Alikuwa ametulia tu tena akiwa uchi wa mnyama. Akamsogelea kijana huyo na kumuinua uso wake, yeye mwenyewe alibaki akisikitika, hakusikitika kwa kuwa alimuonea huruma, alisikitika kwa sababu adhabu zote alizokuwa amepewa, alipewa wakati yeye akiwa nje ya chumba hicho.
“Imekuwaje? Huyu anajua aliyehusika?” aliuliza Ojuku huku akimwangalia Godwin.
“Ndiyo! Tumezungumza naye kirafiki, amesema hausiki na ndiyo maana tukamgusagusa kidogo tu,” alijibu mwanajeshi mmoja aliyekuwa pembeni, yaani pamoja na Godwin kupigwa vile kama adhabu ya kutakiwa kusema ukweli juu ya upandikizaji wa gesi ile ikulu lakini alidai kwamba walimgusagusa tu.
Ojuku alitaka kuzungumza naye, aliamini kwamba Godwin alikuwa akijua kila kitu. Alichokuwa akikihitaji ni kumpata Bokasa ambaye alihisi kwamba hakuwepo nchini kwa kipindi hicho. Akahitaji Godwin achukuliwe na kupelekwa sehemu kwa ajili ya kupumzika kwanza huku wakimfanyia matibabu kidogo ilimradi tu aweze kuzungumza.
Hakutaka kuondoka mahali hapo, ilikuwa ni lazima kuhakikisha kwamba Bokasa anapatikana haraka sana. Akawasiliana na jeshi la anga, maji na nchi kavu, kote huko aliwaambia kuweka ulinzi wa kutosha mpaka mwanaume huyo kukamatwa lakini cha ajabu, hakukuwa na mtu yeyote aliyetoa taarifa kama mwanaume huyo alinaswa sehemu fulani.
Alisubiri kwa saa saba ndipo Godwin akaanza kupata nafuu. Kwanza akapewa chakula, akala kwa tabu, alipomaliza, akachukuliwa na kupelekwa katika chumba kingine kwa lengo la kufanyiwa mahojiano na jenerali mwenyewe.
“Ulijuaje?” aliuliza huku akimwangalia usoni.
“Nilinasa mawasiliano yake kwa njia ya barua pepe. Aliagiza sumu kutoka nchini Urusi kwa mtu anayeitwa Ludovick,” alisema Godwin kwa sauti ndogo.
“Hebu nionyeshe!”
“Sina simu.”
Hilo halikuwa tatizo, akaletewa simu yake ambapo akaingia na kuanza kumuonyeshea barua pepe hiyo. Yeye mwenyewe alishangaa, hakuamini kama rais huyo angefanya kitu cha kipumbavu kama hicho.
Mbali na hiyo, pia Godwin akamuonyeshea barua pepe nyingine zilizokuwa zimeingia humo kwenda kwa rais wa Kenya, Bwana Onyango na kumwambia kwamba alikuwa njiani kuelekea nchini humo kwa ajili ya kujificha kabla ya kuelekea nchini Ubelgiji.
“Yupo njiani kwenda Kenya. Anakwenda kwa njia gani? Hajafafanua kama ni gari, ndege au meli,” alisema Ojuku huku akionekana kuchanganyikiwa.
Tayari alimuona Godwin kuwa kijana mzuri ambaye angeweza kumsaidia kupata vitu vingine. Alichokifanya ni kuagiza kupatiwa matibabu haraka sana kwani kulikuwa na vitu vingi alitakiwa kusaidiana naye.
Akawataka wanajeshi wote wa anga, maji na ardhi kuwa makini kwani iwe isiwe ilikuwa ni lazima mwanaume huyo akamatwe hata kabla hajafika nchini Kenya bila kujali ni kwa usafiri gani alikuwa akiutumia kwenda huko.
Polisi wa barabarani hawakutakiwa kukaa huko, walikaa wanajeshi ambao walikuwa wakipekua kila gari lililokuwa likipita barabarani kuelekea mikoani. Kila kona walipokuwa wakimtafuta mwanaume huyo, hawakuweza kumpata, walishangaa, kama hakuwa ameondoka kwa ndege, sasa kulikuwa na ugumu gani wa kumpata?
“Bado hajapatikana?” aliuliza Ojuku.
“Ndiyo mkuu! Ila tutampata tu kwani mipaka yote imefungwa, hakuna anayeruhusiwa kuingia au kutoka nchini,” alisema mtu aliyekuwa upande wa pili.
“Basi endeleeni kupambana.”

Je, nini kitaendelea?
 
DUNIA HAINA USAWA- 32

Rais Bokasa alikuwa njiani kuelekea nchini Kenya. Ilikuwa saa 1:00 usiku. Alikuwa ndani ya boti yake ya kawaida sana ambayo hakuwa amewaambia watu kuhusu boti hiyo kwa kuamini kwamba kuna siku jambo kama hilo linalotokea lingetokea.
Alimwambia nahodha wake aendeshe taratibu, hakutaka kabisa kugundulika kama yeye ndiye alikuwa ndani ya boti hiyo. Hakukuwa na mizigo, humo, kulikuwa na begi lake ambalo ndani kulikuwa na nguo za mkewe, manukato na wigi, yote ilikuwa ni kuhakikisha kwamba anabadilisha muonekano wake.
Wakati safari ikiendelea, akachukua begi lile, akalifungua, akatoa nguo za mkewe na kuanza kuzivaa. Akachukua wanja, akaupaka, akausafisha uso wake vilivyo na kupaka lipstiki, akavaa viatu vya kike na nguo nyingine kuweka kwenye makalio yake kuonyesha kwamba alikuwa na wowowo.
Alibadilika kwa asilimia kubwa na kwa kumwangalia tu ingekuwa vigumu kugundua kama huyo alikuwa Rais Bokasa akiwa kwenye harakati zake za kuikimbia nchi hiyo. Boti ilikuwa ikiondoka kuelekea mbali kabisa, hawakutaka kupita katika upande wa Tanzania bali walichokifanya ni kuelekea katika upande wa kimataifa kwa ajili ya kusafiri kwa raha bila kubughudhiwa.
Wakati wakiwa wanakaribia katika eneo la kimataifa baharini, wakashtuka kuona boti moja ya kijeshi ikija kwa kasi kubwa kule walipokuwa huku mtu mmoja akisema kwenye kipaza sauti kwamba walitakiwa kusimama haraka sana.
“Tufanyeje?” aliuliza kijana wake.
“Simama! Wakikuuliza, waambie unakwenda kuvua na mama yako. Si uliweka nyavu kama nilivyokwambia?” aliuliza Rais Bokasa.
“Ndiyo!”
“Basi waambie hivyohivyo!”
Hawakuwa na uhakika kama wangeondoka salama, boti ikasimamishwa, haraka sana kijana yule akachukua nyavu na matenga mawili ambayo aliyaandaa kabla na kuyaweka tayari. Ndani ya sekunde kadhaa, boti hiyo ya kijeshi ikawafikia na wanajeshi wawili kusimama, wakarukia ndani ya boti ile.
“Nyie ni wakina nani?” lilikuwa swali la kwanza kutoka kwa mwanajeshi mmoja aliyeshikilia bunguki aina ya Ak-47
“Wavuvi, tunakwenda kuvua na mama yangu!” alijibu kijana yule, kwa jinsi muonekano aliokuwa nao, ilikuwa vigumu kukataa kama hakuwa mvuvi.
“Mama yako yupi?”
“Yule kule,” alisema kijana yule, mwanajeshi alipopiga macho kwa mtu aliyeonyeshea, yalitua kwa mwanamke mrembo, mwenye wowowo ambaye alikuwa ameinama huku akiwa amewapa mgongo, alikuwa akiweka vizuri nyavu.
“Wewe mwanamke!” aliita mwanajeshi huyo. Hapohapo Rais Bokasa akageuka na kuanza kuwaangalia huku akitabasamu.
Kila kitu, kuanzia uso mpaka muonekano mwingine alionekana kama mwanamke fulani mrembo kabisa. Alimuuliza maswali kadhaa huku akiwa amesimama kwa mbali, kwa jinsi alivyokuwa akijibu, sauti yake ya kike haikusikika sana kwani kulikuwa na mawimbi yaliyokuwa yakipiga ambayo yalisababisha kelele mahali hapo.
“Huyu ni kijana wako?” aliuliza mwanajeshi kwa sauti ya juu kabisa ambayo aliamini angeweza kusikika.
“Ndiyo baba! Tunakwenda kuvua kidogo. Wazima lakini? Mbona bunduki tena mpaka mnatutisha? Hatuvui kwa baruti jamani,” alisema Bokasa kwa sauti ya kike.
“Usijali mama! Tunajaribu kuhakikisha ulinzi mahali hapa,” alisema mwanajeshi huyo.
“Nashukuru baba yangu!” alisema Bokasa na mwanajeshi huyo kuondoka.
Akaingia ndani ya boti yao na kuondoka mahali hapo. Macho yake hayakutoka kwa mwanamke yule, alikuwa akimwangalia, hakuamini kama kulikuwa na mwanamke duniani aliyekuwa na umbo matata kama alilokuwa nalo yule aliyemuona ndani ya boti ile.
“Jamani kuna watu wameumbika, nadhani Mungu alipokuwa akiumba, aliacha kazi zake zote na kumuumba yule mama,” alisema mwanajeshi yule.
“Mama gani?”
“Yule aliyekuwa kwenye boti. Amevimba kama kala amira. Mama huyo, katuna katuna kweli, yaani ni shida, yule ukiwa naye ndani, haki ya Mungu unaomba likizo ya mwaka mzima, ukiondoka tu, baba mwenye nyuma kakuibia,” alisema mwanajeshi yule, alichanganyikiwa kiasi kwamba hakujua ni kwa jinsi gani alitakiwa kumsifia mwanamke yule, alimdatisha, mbaya zaidi, hakujua kama yule ndiye mtu waliyekuwa wakimtafuta kwa udi na uvumba. Meli ikaingia katika eneo la kimataifa na safari ya kuelekea Mombasa ikaendelea.
***
Kitendo cha wanajeshi wale kuondoka mahali hapo kilimpa uhakika kwamba wangefika salama Mombasa nchini Kenya na hivyo kuendelea na safari yake ya kuelekea nchini Ubelgiji.
Japokuwa alikuwa mlemavu wa miguu lakini alijitahidi mpaka kujiweka sawa kwa muda kiasi kwamba mwanajeshi yule hakugundua kabisa kilichokuwa kikiendelea.
Hakuonekana kuwa na hofu tena, alikuwa ameingia katika eneo la kimataifa, sehemu ambayo aliamini kwa namna moja ama nyingine asingeweza kukamatwa na mtu yeyote yule, kichwa chake kilikuwa kikifikiria maisha mapya ambayo angekwenda kuishi nchini huko kwani kama kufanya ubaya, aliufanya sana na kipindi hicho kilikuwa ni cha kuondoka na kwenda kuishi huko mbali.
Safari iliendelea kama kawaida, moyo wake ulikuwa na amani tele. Waliendelea na safari huku wakipiga stori nyingi, boti iliendelea na safari na kwa sababu boti hiyo ilikuwa ikikimbia kwa mwendo wa kasi usiku kucha, wakafanikiwa kutumia saa tisa mpaka kufika huko.
Akapokelewa pembezoni mwa Bandari ya Mombasa, vijana wa Rais Onyango wa hapo Kenya, akaanza kuzungumza nao kidogo na kupewa maelekezo kwamba alifuatwa yeye mahali hapo hivyo kukubaliana nao na kuondoka mahali hapo.
Njiani, alikuwa akiwasiliana na rais huyo, alimshukuru kwa kila kitu kilichotokea ila angemshukuru sana kama angemfanyia mipango ya kuondoka na kuelekea nchini Ubelgiji ambapo angeanza maisha mapya kwani tayari alihamisha kiasi kikubwa cha pesa kwenda katika moja ya benki nchini humo.
Walitumia saa kadhaa mpaka kufika Jijini Nairobi ambapo akapokelewa, akalala mahali hapo na kwa sababu Rais Onyango alipanga kusafiri kuelekea nchini Ubelgiji kama moja ya mipango yake ya kumsafirisha Bokasa nchini humo, siku iliyofuata wakaanza safari kuelekea uwanja wa ndege tayari kwa kupanda ndege na kuelekea nchini Ubelgiji.
"Tanzania wanasemaje? Sikupata taarifa yoyote ile," aliuliza Bokasa huku akionekana kuwa mwenye furaha tele.
"Wanarukaruka tu. Hivi kwanza imekuwaje kuhusu ile gesi, na mimi nataka siku niitumie nikizinguliwa nchini mwangu," alisema Rais Onyango.
"Rahisi sana! Kuna mtu nitakupa namba zake, anaitwa Ludovick."
"Yule Mrusi?"
"Ndiyo huyohuyo. Yule jamaa ni shida sana. Yaani anakupa kitu nachulo kabisa, ukiweka tu, mambo yanajipa," alisema Bokasa na wote kuanza kucheka.
"Daah! Huyo jamaa hatari sana!"
"Kwani imekuwaje? Ilijibu? Sikufuatilia habari!"
"Hahah! Wanajeshi ishirini palepale."
"Kweli?"
"Ndiyo! Watu wamemkimbiza rais, halafu wanaogopa kuingia ikulu. Hahaha!" alisema Rais Onyango na kucheka kwa sauti kubwa, hawakuishia hivyo, wakagongesheana mpaka mikono.
Siku hiyo haikuwa kama siku nyingine, taarifa za safari zote za Rais Onyango zilikuwa zikitangazwa katika televisheni mbalimbali lakini kwa safari hiyo, hakukutakiwa mtu yeyote yule afahamu. Ilikuwa ikifanyika kimya kimya na hakukutakiwa kuwa na mwandishi wa habari wa aina yoyote ile.
Baada ya saa ishirini na mbili, ndege hiyo ikaanza kutua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Brussels uliokuwa hapohapo katika Jiji la Brussels. Wakateremka na kuanza kupiga hatua kuelekea katika mlango wa VIP ambapo wakapita pasipo watu wengine kugundua kwamba kwenye msafara ule wa rais huyo kulikuwa na rais mwingine ambaye alikuwa akitafutwa kwa udi na uvumba nchini mwake.
Japokuwa Bokasa alikuwa katika kiti chake cha matairi, hakukuwa na mtu aliyekuwa na hofu naye kabisa kwani huo haukuwa msafara wa kwanza wa rais kuingia nchini humo huku ukiwa umeongozana na mlemavu kama alivyokuwa Bokasa.
Wakatoka nje, wakaingia ndani ya magari yaliyokuwa yakiwasubiri na kuondoka. Mpaka kufika hatua hiyo, Bokasa akawa na uhakika wa kuwa salama maisha yake yote. Hakutaka kabisa kuisikia kuhusu Tanzania, aliichukia nchi hiyo, kwake, ilionekana kama Jehanamu ambapo hakutaka kurudi maisha yake yote.
Wakaelekea katika Hoteli ya Catalonia Grand Place na kuchukua vyumba huko. Maisha yakabadilika, kwa kuwa alikuwa nchini humo alihitaji kununua jumba la kifahari na kuanza maisha yake mapya hapohapo Brussels huku akiisubiri familia yake ambayo aliamini kwamba Rais Onyango angeifanyia mipango ya kwenda kujumuika naye huko alipokuwa.
"Utaishi vipi?" aliuliza Onyango.
"Nitaishi kwa amani na furaha. Niliiba pesa zote za serikali kiasi cha dola trilioni kumi na kukihamishia katika akaunti yangu kwenye benki kuu ya hapo Ubelgiji," alisema Bokasa huku akionekana kuwa na furaha tele.
"Dola trilioni kumi?"
"Ndiyo!"
"Basi wewe ni tajiri namba moja duniani. Ni pesa nyingi sana. Kama Bill Gates ana dola bilioni 89, wewe una dola trilioni kumi, basi wewe ndiye tajiri namba moja duniani," alisema Onyango na wote kuanza kucheka kwa furaha.
Kwa muda wa miezi sita ya misukosuko, hakukuwa na siku ambayo Bokasa alilala kwa amani na furaha kama siku hiyo. Alijiona kuwa bilionea mkubwa, kiasi cha pesa ambacho alikihamisha kutoka katika akaunti ya serikali nchini Tanzania kingemfanya kuyafurahia maisha yake mpaka kifo chake.
Siku iliyofuata hakutaka kubaki hotelini, akaondoka na kuanza kuelekea katika jengo kubwa la benki hiyo, alipofika, akakaribishwa. Wahudumu wa benki walipomuona tu, wakaanza kuzungumza kimya kimya kuhusu yeye, walimfahamu, alikuwa miongoni mwa marais wasiopendwa nchini Tanzania.
Hakutaka kujali, kwa kuwa alitaka kuangalia usalama wa pesa zake zilizokuwa zimeingia siku chache zilizopita, akaandika akaunti yake kwa lengo la kuangalia kama pesa zake zilikuwa salama.
"Mara ya mwisho kulikuwa na kiasi gani?" aliuliza dada aliyekuwa akimhudumia, walimchukulia kama rais wa kawaida.
"Dola trilioni kumi."
"Kweli?"
"Ndiyo!"
Dada yule akabaki akiiangalia kompyuta yake, hakuelewa kama mwanaume aliyesimama mbele yake alikuwa akizungumza kweli au alikuwa akimdanganya kwani kila alipokuwa akiangalia kwenye akaunti ile, hakukuwa na pesa yoyote ile, yaani salio lilisoma 0.00.
"Una uhakika uliweka humu?"
"Sasa dada yangu! Kwa nini nikudanganye? Kwani mimi siijui akaunti yangu?" aliuliza Bokasa huku akimwangalia msichana huyo.
"Sawa. Hebu pita huku kwanza, nisubiri katika kiti kile," alisema msichana huyo.
Hilo halikuwa tatizo hata kidogo, kitu pekee alichokuwa akikihitaji ni usalama wa pesa zake tu, akaondoka na kumsubiri msichana huyo, alipomfuata, akamchukua na kuelekea naye kwa meneja huku akiwa na karatasi kadhaa mikononi mwake.
Wakaelekea katika chumba kilichoandikwa General Manager na kuambiwa kusubiri hapo. Napo, wala hakuleta ubishi, akasubiri huku akiwa na wasiwasi, alihisi kulikuwa na kitu kilichokuwa kimetokea kwani ishu ya kuangalia salio lake katika akaunti yake hakukuwa na ubaya wowote ule.
Baada ya dakika kadhaa, akaitwa na sekretari na kuingia humo huku akikikokota kiti chake cha matairi. Alipofika, muonekano aliomkuta nao huyo meneja ulionyesha dhahiri kwamba kulikuwa na tatizo kubwa lililokuwa limetokea.
"Kabla ya yote! Kuna nini?" aliuliza Bokasa hata kabla ya salamu.
"Usijali! Karibu."
"Sawa. Ila kwanza ninataka kujua, nini kinaendelea kuhusu pesa zangu?" aliuliza huku akimwangalia meneja huyo.
Alionekana kuwa na presha kubwa, kwa kuwa hakutaka kumuona akianzisha ugomvi wowote ule, akampa karatasi ile na Bokasa kuanza kuisoma. Aliisoma taratibu, mapigo ya moyo yalikuwa yakimdunda.
"Hakuna pesa?" aliuliza huku kijasho chembamba kikianza kumtoka.
"Ndiyo kama unavyoona. Una uhakika uliweka katika akaunti hiyo?" aliuliza meneja.
"Ndiyo! Niliweka humu. Pesa zangu zipo wapi? Pesa zangu zipo wapi?" aliuliza huku akianza kulia, wakati akijiuliza swali hilo, ndipo jina la Godwin likaanza kugonga kichwani mwake.
"Huyu ni Godwin! Huyu ni Godwin," alisema Bokasa huku akitetemeka, alijua tu kwamba mchezo huo aliufanya kijana yuleyule aliyemfanyia umafia katika akaunti yake iliyokuwa katika Benki ya Geneva nchini Uswisi. Hata kabla hajazungumza zaidi, hapohapo akaanguka na kupoteza fahamu.
****
Godwin ndiye alikuwa mkombozi wao, yeye ndiye alikuwa na uwezo wa kuwaambia mahali alipokuwa mtu waliyekuwa wakimtafuta. Walimwambia kwamba alitakiwa kufanya kitu chochote kile mpaka kuhakikisha mtu huyo anajulikana mahali alipokuwa.
Hilo halikuwa tatizo kwa Godwin, alichokifanya ni kuanza kucheza na kompyuta yake, haikuwa kazi nyepesi hata kidogo kuipata simu ya mtu huyo kwani kule alipokuwa, hakukuwa na network, hakukuwa na mawasiliano yoyote yale na ni mara chache tu ilikuwa ikija na kutoka.
Huku akiwa na kompyuta yake, majira ya saa mbili usiku ndipo akapata majibu juu ya mahali alipokuwa Bokasa. Mnara wa simu ukasoma kwamba alikuwa baharini akiendelea na safari ya kuelekea Mombasa.
Akawaambia kwamba mwanaume huyo alikuwa safarini kuelekea nchini Kenya, haraka sana Jenerali Ojuku akakipigia simu kikosi chake cha majini ambacho alikiambia kwamba mtu waliyekuwa wakimtafuta alikuwa huko akielekea nchini Kenya.
"Mkuu! Tumezunguka bahari nzima lakini hatukuweza kumuona mtu huyo," alisikika mwanaume mmoja kwenye simu.
"Mna uhakika?"
"Ndiyo mkuu!"
"Kwa hiyo hamkuiona boti yoyote ile?"
"Tuliiona moja tu, kijana mmoja alikuwa akienda kuvua samaki na mama yake," alisema mwanajeshi huyo.
"Alikuwa akienda kuvua samaki na mama yake?"
"Ndiyo!"
"Hivi mna akili nyie? Ni mvuvi gani anaweza kwenda kuvua samaki na mama yake? Hiyo ndiyo boti aliyokuwa huyo rais. Huyo mwanamke mliongea naye?"
"Ndiyo mkuu!"
"Mlimsogelea?"
"Hapana mkuu! Alikuwa bize na kukunjua nyavu!"
"Mmefanya kosa kubwa sana! Huyo alikuwa Bokasa, rudini baharini mkaiangalie tena hiyo boti," alifoka Ojuku na kukata simu kwa hasira.
Alichanganyikiwa, akamwambia Godwin kile kilichotokea kwamba vijana hao walifanya kosa kubwa kuiruhusu boti iondoke na wakati alikuwa na uhakika kwamba ilikuwa ikiendeshwa na mtu waliyekuwa wakimtafuta kwa udi na uvumba.
"Kwa hiyo anaondoka kuelekea Ubelgiji?" aliuliza Ojuku.
"Ndiyo! Kwa maelezo yake aliyokuwa akimwambia Onyango, atakuwa anakwenda huko. Subiri," alisema Godwin.
Wazo likamjia kichwani mwake, akahisi kwamba kama kweli rais huyo alikuwa akikimbilia nchini Ubelgiji ilikuwa ni lazima kuhamisha pesa hivyo ni kuanza kuichunguza simu yake ili kama kweli alikuwa amehamisha pesa basi angepata kila kitu humo.
"Yes! Nilijua tu. Mungu wangu, kakomba pesa zote za serikali! Huyu mpumbavu sana," alisema Godwin huku akiangalia ujumbe wa meseji uliokuwa katika simu ya Bokasa, akamwambia Ojuku.
"Ameiba pesa za serikali?"
"Ndiyo! Dola trilioni kumi. Basi kama ameiba, ngoja tuzichukue pesa zetu. Au unaonaje swahiba?" aliuliza Godwin, alikuwa akiongea kijana zaidi.
"Haina shida, " alisema Ojuku na Godwin kuanza kuifanya kazi hiyo, yaani pesa zote alizoiba kiongozi huyo zilitakiwa kurudishwa haraka sana, tena si pesa hizo tu, hata pesa zake nyingine zilizokuwa humo, zilitakiwa kurudi katika akaunti ya serikali.
"Yes! Nimemuachia balansi ya 0.00, hiyo itamtosha kufanya shopping huko," alisema Godwin huku akicheka, hata maumivu ya mwilini wake hakuyasikia tena.
***
Moyo wa Godwin ukawa na amani, alifanya kazi kubwa ambayo alitakiwa kuifanya kwa kipindi kirefu. Alikaa katika chumba kile alichoambiwa kukaa huku uso wake ukiwa na tabasamu pana, kitendo cha kufanikisha kuzirudisha pesa zile katika akaunti ya serikali kulimfanya kujiona kuwa mkombozi wa Tanzania.
Jenerali Ojuku alipumua huku akionekana kuwa na furaha tele, kitendo cha Godwin kuifanya kazi ile kilimfanya kumuona kijana huyo kuwa muhimu kuliko mtu yeyote yule nchini Tanzania. Akawasiliana na Meja Jenerali na kumwambia kwamba haraka sana wataalamu wa gesi waende ikulu kwa lengo la kutoa sumu ile kitu kilichofanyika haraka sana.
“Cha kwanza sumu itolewe ikulu ndiyo mambo mengine yafanyike,” alisema Ojuku.
Hilo halikuwa tatizo hata kidogo, baada ya saa mbili akapigiwa simu na kuambiwa kwamba watu wale aliokuwa akiwataka kwenda ikulu walikwenda na kufanya kile alichokuwa akikitaka. Akawa na amani zaidi na kuanza kuzungumza na Godwin.
Alitaka kumfahamu kijana huyo, alikuwa nani na kulikuwa na kitu gani kilichokuwa kikiendelea. Godwin hakutaka kumwambia ukweli, akamdanganya kwamba alikuwa mwanafunzi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambaye moyo wake ulikuwa na uchungu wa kuona mabadiliko yakifanyika nchini mwake.
“Safi sana. Kuna kazi nataka unisaidie!” alisema Ojuku.
“Kazi gani?”
Akamwambia kila kitu kilichokuwa kimetokea kuhusu mtu aliyekuwa ameiteka familia yake. Alimwelezea kwa makini kila kitu kilichokuwa kimetokea kwamba familia yake ilitekwa na mtu asiyemfahamu na mpaka kipindi hicho hakujua familia hiyo alikuwa wapi. Alichokiamini ni kwamba Godwin aliyejitambulisha kwa jina la Denis angeweza kumsaidia kwa kile kilichokuwa kimetokea.
Hilo, kwake halikuonekana kuwa tatizo lolote lile, akazungumza naye na kumwambia ampe siku mbili na angemwambia mahali familia yake ilipokuwa kitu kilichomfurahisha mno Ojuku. Godwin hakukaa sana kambini, akaruhusiwa kuondoka, akapakizwa ndani ya gari la jeshi mpaka Magomeni aliposema anaishi na kuteremshwa.
“Nashukuru sana,” alisema Godwin huku akiwaangalia wanajeshi walimpeleka mahali pale.
Baada ya kuhakikisha kwamba lile gari limeondoka, akachukua bodaboda mpaka Tandale ambapo akateremka na kwenda alipokuwa akiishi. Alipoufikia mlango, akafungua na kuingia ndani. Kitendo cha Winfrida kumuona, akasimama na haraka sana akamfuata na kumkumbatia.
Machozi yalikuwa yakimtoka, kwa siku moja hakumuona mpenzi wake huyo, hakujua mahali alipokuwa na hata muonekano aliokuwa nao kupindi hicho ulionyesha dhahiri kwamba alikuwa katika matatioz makubwa kwani uso wake tu ulikuwa umevimba.
“Nini kimetokea?” aliuliza Winfrida huku akimwangalia mpenzi wake.
“Hakuna kitu!”
“Hakuna kitu kivipi na wakati umevimba uso? Niambie ni kitu gani kimetokea,” alisema Winfrida huku akimwangalia mpenzi wake huyo.
Godwin hakumwambia ukweli, aliendelea kusisitiza kwamba hakukuwa na kitu chochote kile cha hatari kilichokuwa kimetokea. Winfrida hakuridhika lakini hakuwa na jinsi, akaachana naye na kuendelea kufanya mambo yake.
Godwin hakutaka kuchelewa, hapohapo akachukua simu yake na kumpigia bilionea Kizito na kumwambia kwamba aiache familia ya Jenerali Ojuku. Si huyo tu bali aliwapigia watu wote waliokuwa wakizishikilia familia za wenzao na kuwaambia waziachie huru kwani kile kitu alichokuwa akikihitaji, tayari kilifanyika.
“Na picha zangu?” aliuliza Kizito.
“Nakuhakikishia hakuna mtu yeyote atakayejua kitu chochote kile, nitakufa na siri hii moyoni,” alisema Godwin.
“Nikupe kiasi gani kwa kukushukuru kwa wema wako? Nikulipe kiasi gani kwa kuitunza siri hii zaidi?” aliuliza bilionea Kizito, kwa jinsi sauti ilivyosikika tu, ilikuwa kama mtu ambaye hakuwa akiamini kilichokuwa kikiendelea.
“Hakuna haja ya pesa. Nakuhakikishia kwamba hakutokuwa na mtu yeyote atakayefahamu kitu chochote kile,” alisema Godwin kwa msisitizo uliomfanya bilionea huyo kumuamini.
Tanzania ikabadilika, haikuwa ile ya huzuni tena, kila kona watu wote walikuwa na furaha tele. Hakukuwa na mtu aliyeamini kwamba hatimaye Rais Bokasa alitimuliwa na nchi yake kuwa mikononi mwa wanajeshi. Amani ikarudi na bila kupoteza muda, Godwin akampigia simu Kambili na kuzungumza naye, akamwambia wazi kwamba uchaguzi mkuu ulitakiwa kufanyika, mawaziri wote wavuliwe nyadhifa zao, na kwenye uchaguzi huo, Chama cha Labour Party kikatakiwa kufutwa haraka sana, msajili wa vyama akapigiwa simu na Jenerali Ojuku na kuambiwa kwamba chama hiko hakikutakiwa kiwepo na hata wale mawazilri wote ambao walikuwa katika utawala uliopita walitakiwa kukamatwa na polisi na kufanyiwa mahojiano maalumu ambayo yangehusu zaidi mali walizokuwanazo.
****
Meneja wa Benki ya Brussels alishangaa, alibaki akimwangalia Bokasa ambaye alikuwa chini, presha ilimkamata baada ya kuambiwa kwamba kwenye akaunti yake hakukuwa na pesa yoyote ile. Akampigia simu sekretari wake ambaye akafika mahali hapo, wote wawili wakasaidiana kumbeba na kumpeleka nje ambapo wafanyakazi wengine wakawapokea na kuondoka naye kuelekea nje kwa ajili ya kumuwahisha hospitalini.
Njiani, hakuwa amefumbua macho, alikuwa kimya huku kila mmoja akiwa na hofu kwamba inawezekana mtu huyo alikuwa amefariki dunia. Safari hiyo ilichukua dakika kadhaa ndipo wakafika hospitalini ambapo moja kwa moja machela ikaletwa, akapakizwa na kuanza kusukumwa kuelekea ndani.
Kila nesi aliyekuwa akimwangalia alibaki akishangaa, walitaka kujua kitu kilichotokea kwa mtu huyo, alikuwa mlemavu, nini kilitokea? Kila aliyejiuliza alikosa jibu.
Akaingizwa katika chumba cha upasuaji na kuanza kufanyiwa uchunguzi mdogo kwa ajili ya kugundua ni kitu gani kilichokuwa kimetokea. Wakampima presha yake, ilikuwa imepanda kwa kiasi kikubwa sana kiasi kwamba walibaki wakishangaa.
“Jamani! Nini kimetokea? Mbona presha imepanda hivi?” aliuliza daktari huku akiwaangalia manesi waliokuwa wameisukuma machela ndani ya chumba kile na kumlaza kitandani.
“Ndugu zake wamemleta, hatujui chochote kile,” alijibu nesi mmoja huku macho yake yakiwa kwa Bokasa aliyekuwa hoi kitandani.
Walichokifanya ni kumuhudumia kwa nguvu zote kuhakikisha wanayaokoa maisha yake. Walipambana kwa nguvu zote, kidogo hali yake ikaanza kupata nafuu kwani baada ya saa moja kuhudumiwa, akayafumbua macho yake, akaanza kuangalia huku na kule na kitu cha kwanza kabisa kilichokuja kichwani mwake ni pesa zake.
“Where is my money?” (pesa zangu zipo wapi?) aliuliza huku akimwangalia daktari aliyekuwa amesimama karibu naye.
“Which money?” (pesa gani?)
“Someone stole my money! Godwin stole my money,” (kuna mtu ameniibia pesa zangu! Godwin ameniibia pesa zangu) alisema Bokasa maneno yaliyomfanya kila mtu kumshangaa.
Bokasa alikuwa akipiga kelele tu ndani ya chumba kile kiasi kwamba kila mtu alikuwa akishangaa. Hawakumjua mwanaume huyo, hawakujua kitu chochote kilichokuwa kikiendelea katika maisha yake, walishangaa, hizo pesa alizokuwa akizizungumzia zilikuwa zipi na aliibiwa na nani?

Je, nini kitaendelea?
 
Haaaahaaaaaaaa nasomaga sana dada angu story nyingi kila cku tena ila sometimes nabanwa kabla sikuwa na account Jf ko nikawa natumia opera ambayo uruhusiwi KUKOMENT
Nilikupa maujanja ahahahah karibu kwa wakongwe
 
ERIC SHIGONGO
DUNIA HAINA USAWA
Ojuku aliambiwa kwamba Bokasa alikuwa nchini Ubelgiji, hakutaka kuona mwanaume huyo akikimbia na kujificha kama ilivyokuwa kwa marais wengine wa Afrika, hivyo akaagiza watu kuondoka kuelekea nchini humo kwa ajili ya kujua mahali alipokuwa na kumkamata.
Hilo halikuwa tatizo, wanaume hao wakaondoka kuelekea huko, walipofika, wakaanza kuulizia sehemu mbalimbali kuhusu mwanaume huyo, walikuwa na uhakika kwamba alikuwa hapohapo Brussels hivyo hawakutaka kutoka kwenda sehemu nyingine yoyote ile.
Walimtafuta kimyakimya tena kwa kuulizia kwa siku mbili mfululizo lakini hawakufanikiwa kitu kilichowafanya kumpigia simu Ojuku na kumwambia kilichokuwa kimetokea. Hilo tayari likaonekana kuwa tatizo, hakujua ni kwa jinsi gani wangeweza kumpata mwanaume huyo.
Wakati akiwa anafikiria sana ndipo jina la Denis likamjia kichwani mwake, hakutaka kuchelewa, hapohapo akampigia simu na kumwambia kilichokuwa kimetokea kwamba iwe isiwe ilikuwa ni lazima kujua mahali alipokuwa Bokasa.
Denis, ambaye ndiye Godwin akaondoka mpaka kambini na kukutana na Ojuku na kuanza kuzungumza naye kwa undani. Alimwambia lengo lao la kumpata Bokasa, kwa yote aliyokuwa ameyafanya nchini Tanzania, alitakiwa kushtakiwa na kufungwa gerezani.
“Watu wetu wapo Ubelgiji, hawajui mahali alipo,” alisema Ojuku.
“Si tatizo. Ngoja nimtafute.”
Kitu pekee alichokifanya ni kuanza kumtafuta kwa kutumia simu yake. Aliingiza namba ya simu yake katika kompyuta yake na kuanza kumtafuta kila kona. Hiyo ilikuwa kazi yake, alizoea kuifanya kila siku hivyo hakukuwa na shida yoyote ile, baada ya dakika chache, akapata majibu kwamba mtu huyo alikuwa katika Benki ya Brussels.
“Atakuwa benki! Una uhakika?” aliuliza Ojuku.
“Simu yake ipo huko, na bila shaka inawezekana alikwenda kwa ajili ya kutoa pesa. Cha msingi watume waende huko, hata kama hayupo basi kutakuwa na watu wanaojua mahali alipo,” alisema Godwin.
“Sawa. Hakuna shida,” alisema Ojuku, hapohapo akachukua simu yake na kuwapigia watu hao na kuwaambia waende katika Benki ya Brussels ambapo walikuwa na uhakika kwamba mtu huyo anaweza kuwa huko.
“Haina shida. Tunakwenda,” alisema jamaa aliyekuwa huko na safari ya kwenda katika benki hiyo kuanza.
***
Kila mtu alitaka kuiona Tanzania mpya, matumaini na furaha ya Watanzania ambayo ilikuwa imepotea mioyoni mwao ikaanza kurudi, mpaka kipindi hicho hakukuwa na kitu chochote kilichobadilika lakini tayari Watanzania waliona tayari wameanza kupata maisha mazuri ambayo kila mmoja alikuwa akiyatamani.
Godwin alifanya kazi kubwa sana kupitia akaunti yake ya Mabadiliko ya Kweli, kila mtu nchini Tanzania alitaka kumuona mtu huyo, alikuwa nani na alikuwa na muonekano gani? Hilo likawafanya watu kutengeneza umoja waliouita ONYESHA SURA YAKO ambao ulikuwa na kazi ya kupanga mikakati ya kuandamana kutaka kumuona mwanaume ambaye alichangia kuiweka Tanzania hapo ilipokuwa, na hata kumuondoa Rais Bokasa madarakani.
Hakukuwa na mtu aliyemjua mtu huyo, kila mmoja alikuwa na hamu, watu wengi waliomba kumuona huku wengine wakienda mbali na kutaka kuona mtu huyo akiwa rais wa Tanzania lakini hilo halikuwezekana, Godwin hakufikiria kuwa rais wa nchi hiyo, kitu pekee alichokuwa anakitamani kila siku ni kumuondoa Bokasa madarakani kitu ambacho alifanikiwa kwa kiasi kikubwa.
Watu hawakuishia kulalamika mitandaoni tu bali baada ya siku kadhaa, wakajikusanya mitaani na kuanza kuandamana maandamano ya amani ya kumtaka Godwin kujitokeza hadharani huku wengine wakitaka hata kuona akizungumza lolote tangu alipoanzia mpaka pale alipofikia.
Kila kitu kilichokuwa kikiendelea, Godwin alikuwa akikifuatilia na wakati mwingine kukusanyika na waandamanaji hao na kuandamana pamoja nao pasipo kugundua kwamba alikuwa miongoni mwao.
“Kesho nitahitaji kuzungumza na watu kupitia akaunti hii, nitasema mimi ni nani, nimeibukaje, nitaeleza kila kitu ila sitohitaji sura yangu ionekane,” aliandika Godwin kwenye mtandao, maneno ambayo kidogo yakawafanya watu waliokuwa wakitaka kuandamana tena kuacha kufanya hivyo.
Kama alivyokuwa ameahidi ndivyo alivyofanya, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kwenda katika Hoteli ya Atriums iliyokuwa Africasana, moja ya hoteli iliyokuwa na ukimya mkubwa, akachukua chumba ambapo humo ndani akaanza kujirekodi video huku akisimulia historia ya maisha yake.
Wakati mwingine alikuwa akilia, hakutaka kuiacha sura yake ionekane, aliiacha ionekane mwisho mdomoni kushuka chini na kuendelea kuhadithia. Alianza tangu siku ya kwanza alipokuwa na ufahamu, aliwaambia watu kwamba yeye alikuwa mtoto wa Mzee Mapoto, mwanasiasa maarufu nchini Tanzania ambaye alitokea kupendwa kuliko mtu yeyote katika ardhi ya Tanzania.
Akaelezea kifo cha baba yake ambaye alichaguliwa kama balozi nchini Marekani, aliwaeleza kwamba hata kifo chake hakikuwa cha bahati mbaya kama watu waliyovyohisi bali nyuma yake kulikuwa na mkono wa Rais Bokasa ambaye alitaka kuitekekeza familia nzima kwa kuhisi kwamba ingemletea matatizo hapo baadaye.
Hakutaka kuficha kitu, alisimulia kifo cha mama yake, ndugu yake, Irene, jinsi alivyokuwa akitafutwa mpaka alipowekwa katika boksi na kutupwa baharini huku akitakiwa kufa ila mtu mmoja aliyeitwa Kihampa hakutaka kuona hilo likitokea.
Akaelezea namna alivyookolewa na wavuvi wa Japan na kupelekwa nchini humo ambapo alisomea kompyuta na kuwa mkali katika Chuo cha Waseda. Alisimulia kila kitu mpaka alipokuwa akihamisha pesa za viongozi, jinsi alivyowasumbua FIS na kuhakikisha kwamba hapatikani.
Hiyo ndiyo ilikuwa siku ya kuwaambia Watanzania kwamba yeye alikuwa nani, kila mtu alishangaa, wengine wakashindwa kuvumilia kwani mateso na shida alizopitia mwanaume huyo hakika hakukuwa na mtu aliyeamini kwamba kuna binadamu angeweza kupitia maisha hayo.
“Nilitaka kulipa kisasi, na kisasi pekee kilikuwa ni kumuondoa madarakani na kuwapa Watanzania nchi yao. Nimefanikiwa sana,” alisema Godwin hali iliyowafanya Watanzania wengi kufurahi.
“Wengi wanasema kwamba nichukue nafasi ya urais. Ndugu zangu, sikuwa na ndoto za kuwa rais, sikuhangaika kumuondoa madarakani Rais Bokasa ili nije kuwa rais, nilifanya hivyo kwa kuwa nilihitaji kuona Tanzania ikiongozwa na mtu sahihi. Kwangu mimi, nadhani Kambili ni mtu sahihi, mtu mwenye uchungu, mtu ambaye anaweza kufanya kila liwezekanalo sisi kufika kule tunapotaka kufika,” alisema Godwin na kuendelea:
“Ninamshukuru Jenerali Ojuku, kuna mengi amepitia ila ninamwambia kwamba kazi yake ilionekana, nilicheza michezo mingi ya hatari, sikucheza kwa lengo baya, nicheza kama njia ya kumsukuma kunisaidia kumtoa rais huyu madarakani, na kweli imewezekana. Nashukuru kwa wote. Hii akaunti haitofutwa, kwa viongozi wote ambao waliweka pesa zao katika akaunti za Uswisi, nimefunga akaunti, na hata wale viongozi wenye pesa hapa Tanzania, nimezuia pesa zao mpaka kesi zao zitakapokwisha. Kufunga akaunti hizo si kazi ya benki tu, nilifanya hivyo ili kuwasaidia. Nashukuru sana. Karibuni kwenye Tanzania mpya,” alimalizia Godwin, huo ndiyo ukawa mwisho wa video yake iliyogawanywa katika vipande thelathini na mbili.
***
“Sir! We have got a video,” (mkuu! Tumepata video) ilisikika sauti kutoka upande wa pili.
“What is it about?” (kuhusu nini?)
“Godwin! He has released a video,” (Godwin! Ametoa video) alisikika mwanaume huyo.
Kitendo cha Bwana Kom kusikia jina la Godwin akasikia moyo wake ukipiga paa. Hakuamini, hapohapo akamwambia mwanaume huyo kwamba amtumie video hiyo lakini akaambiwa kwamba ilikuwa katika mtandao wa Instagram ambapo alipoingia katika Akaunti ya Mabadiliko ya Kweli, akaiona video hiyo.
Haikuwa ya Kiingereza, ilikuwa ni ya Kiswahili kitu kilichomfanya kumtafuta mkalimani ambaye alikuja kumfafanulia kila neno lililozungumziwa katika video hiyo.
Hapo ndipo alipojua ukweli kwamba mwanaume huyo hakuwa mhalifu kama alivyokuwa akihisi bali alifanya hivyo kwa kuwa alikuwa akipambana na viongozi waliokuwa wakiihujumu nchi yao na hata kuzichukua zile pesa zilizokuwa zimeibwa nchini mwao.
Aliposikia kila kitu, akakifuata kiti chake na kutulia, akaegemea na kuweka mikono kichwani mwake. Hakuamini kama alikuwa akipambana na mtu aliyekuwa akiipigania nchi yake na kuwatokomeza mafisadi waliokuwa wakiwanyonya kila siku.
“Make a call to Halima! Tell her to leave him alone,” (mpigie simu Halima! Mwambie amuache) alisema Kom na hapohapo Halima kupigiwa simu.
***
Wakati simu kutoka kwa Kom ilipokuwa ikiingia, Godwin alikuwa akiiona, alijua kwamba kulikuwa na kitu mwanaume huyo alitaka kumwambia msichana huyo. Alichokifanya ni kuiunganisha mpaka kwa Halima ambapo msichana huyo alipopokea, akampa taarifa kwamba alitakiwa kuachana na Godwin kwani kwa kile alichokuwa akikifanya, hakuwa mtu wa kutafutwa na kushtakiwa kwa kuwa kulikuwa na jambo jingine la msingi alilokuwa akilipigania kwa ajili ya nchini yake.
Kwa Halima, hiyo ikaonekana kuwa nafuu, alikuwa amehangaika kwa kipindi kirefu kumtafuta mwanaume huyo lakini hakuwa amempata, kitendo cha kuambiwa kwamba alitakiwa kurudi, akanyanyua mikono na kumshukuru Mungu.
Alikwishawahi kufanya kazi nyingi lakini kwa ile ya kumtafuta Godwin ilikuwa ni ngumu kuliko zote alizowahi kufanya katika maisha yake. Hakutaka kuchelewa, aliona kama Bwana Kom angeahirisha na kumwambia kwamba aendelee kupambana kumtafuta, siku iliyofuata ukawa mwisho wa kukaa nchini Tanzania, akapanda ndege na kurudi zake nchini Somalia kuendelea na majukumu yake mengine.
Kwa Godwin, maisha yalikuwa ni furaha tele, akawa anaendelea kuishi na Winfrida, hakumwambia alikuwa nani, aliishi kisiri, kila kitu kilichokuwa kimetokea alikifanya kuwa siri kubwa mno. Kazi yake ikawa ni kuwasiliana na Kambili, alimwambia kwamba kila kitu kilikuwa tayari na aliamini kwamba baada ya siku kadhaa yeye ndiye angekuwa rais wa nchi hiyo.
“Nashukuru sana,” alisema Kambili.
“Usijali! Ila usifanye kama Bokasa.”
“Sitoweza kufanya. Naomba uniamini! Sitoweza kufanya jambo lolote lile baya. Nimepigana kwa ajili ya nchi hii kwa miaka mingi, nitaonekana sina akili kama tu nitaanza kufanya vitu tofauti na vile ambavyo Watanzania wanavitaka kila siku,” alisema Kambili, aliamini kabisa kwamba alikuwa akienda kuchukua nafasi ya urais kwa kuwa Godwin aliamua kufanya hivyo.
Hakuishia hapo, alichokifanya ni kuwasiliana na Jenerali Ojuku na kumuomba msamaha kwa yote yaliyokuwa yametokea, kuiteka familia yake, halikuwa lengo lake ila alifanya hivyo kwa kuwa alihitaji mabadiliko kwa nguvu kubwa na yote yalifanyika.
“Haikuwa kwa faida yangu, ilikuwa ni kwa faida ya Watanzania, faida ya watoto na wajukuu zako,” alimwambia Ojuku kwenye simu.
“Nashukuru sana. Najua niliumia sana, sikuwa nimelijua lengo lako, si baya, ni zuri ambalo ninaliunga mkono kwa asilimia mia moja,” alisema Ojuku kwenye simu.
“Nashukuru kwa kulifahamu hilo!”
“Ila hutujawahi hata kuonana. Ningependa nimuone huyu shujaa ambaye ameifanya Tanzania kurudi katika heshima yake na kuondokana na udikteta,” alisema Ojuku.
“Tulikwishaonana! Tukazungumza na kufanya mambo mengi sana,” alisema Godwin maneno yaliyomshtua Ojuku.
“Tulishawahi kuonana?”
“Ndiyo! Niliisaidia Tanzania hata kuhamisha pesa za Bokasa alizozituma Ubelgiji,” alisema Godwin.
“Inamaanisha wewe ndiye yule kijana aliyeitwa Denis?”
“Ndiye mimi!”
“Ni kijana mdogo mno!”
“Najua! Ni kijana mdogo lakini mwenye kiu ya kupambana. Nashukuru kwa msaada wako,” alisema Godwin.
“Nashukuru pia. Naomba tuonane japo tule chakula cha mchana!”
“Ningefurahi sana kama ningepata nafasi hiyo. Lakini sina jinsi, hutoweza kuniona tena. Nimefanya kazi ambayo nilitakiwa kuifanya kwa uwezo wangu wote. Popote nitakapokuwa, utakuwa na namba yangu, tutawasiliana, kama kutatokea tatizo lolote lile, naomba uniambie, kama kuna pesa zimeibwa, nijulishe nizirudishe,” alisema Godwin.
“Haina shida. Nakutakia maisha mema!”
“Nashukuru pia kiongozi,” alisema Godwin na kukata simu.
Alimaliza kuzungumza na Ojuku, mtu mmoja wa kipekee aliyetamani sana kuonana naye alikuwa Mchungaji Kihampa. Huyo ndiye aliyekuwa amemuokoa, mtu aliyemuweka kwenye boksi, japokuwa alitakiwa kuuawa lakini mwanaume huyo alimuokoa kwa kumuacaha hai na kuokolewa na Wajapan.
“Ni lazima nimtafute huyu mtu. Ni muhimu sana, siwezi kumuacha,” aliseema Godwin, akasimama na kuanza kujiandaa kwenda kumtembelea mchungaji huyo.
***
Maofisa wa Usalama wa Taifa wakafika mpaka katika Benki ya Brussels kwa lengo la kwenda kumkamata Bokasa ambaye alikuwa akihitajika sana nchini Tanzania. Walipofika hapo, wakataka kuonana na uongozi wa benki hiyo kwani hapo ndani kila walipoangalia huku na kule, hawakuweza kumuona mtu huyo japokuwa mashine yao ya GPS ilionyesha kwamba simu ile ilikuwa humo ndani.
Kuhusu kuonana na meneja wa benki hiyo hakukuwa na tatizo lolote lile, akapigiwa simu na kuambiwa kwamba kulikuwa na watu waliotaka kuonana naye. Wakaruhusiwa na kwenda ndani ambapo moja kwa moja wakaanza kuzungumza naye.
“Sijawaelewa vizuri! Mmesema rais?” aliuliza meneja huyo huku akiwaangalia kwa mshangao.
“Ndiyo! Picha yake hii hapa!” alisema jamaa mmoja huku akimpa picha yya Bokasa.
“Ooh! Kumbe mnamzungumzia huyU! Mmesema kwamba ni rais! Wa wapi?’ aliuliza meneja huku akishangaa na hapohapo kumwambia kwa kifupi kilichotokea.
Hilo halikuwa tatizo, wakaambiwa kwamba mwanaume huyo hakuwa mahali hapo bali aliiacha simu yake ambayo aliihifadhi katika droo ila mwanaume huyo alikuwa hoi hospitalini.
Hawakutaka kuondoka pasipo kumuona hivyo wakaomba kupelekwa huko kwa lengo la kuonana naye. Wakachukuliwa mpaka hospitalini ambapo kwa ruhusa ya daktari wakapelekwa mpaka katika chumba alichokuwa amelazwa.
Walipofika, wakabaki wakimwangalia. Mwanaume huyo alikuwa akitia huruma kitandani pale, alikuwa kimya, alionekana kuwa na hofu kubwa na hapo kitandani alikuwa akipumulia mashine ya oksijeni tu. Walichokifanya ni kumwambia kwamba alikuwa chini ya ulinzi na alitakiwa kusafirishwa mpaka nchini Tanzania kwa ajili ya kushtakiwa kwa kila kitu kilichokuwa kimetokea pamoja na ubadhilifu wa pesa.
“Daktari! Huyu mgonjwa atatakiwa kupelekwa nchini Tanzania haraka sana!” alisema jamaa mmoja.
“Hapana! Ni mapema sana. Mpeni miezi sita kwani bado hali yake si nzuri kabisa,” alisema daktari kiasi kwamba mawasiliano yakafanyika mpaka nchini Tanzania ambapo wakakubaliana kumpa mtu huyo miezi hiyo kwa ajili ya kupatiwa matibabu na hali yake irudi na kuwa kawaida.
“Haina shida! Kwa kuwa ndiyo utakuwa muda wa uchaguzi, mleteni kipindi hicho, ila awe chini ya uangalizi!” alisikika Jenerali Ojuku.
“Haina shida kiongozi!”
***
Tangu Kihampa aliposikia sauti moyoni mwake ikimwambia kwamba alitakiwa kuyabadilisha maisha yake, akaamua kubadilika na kumtumikia Mungu kwa moyo mmoja. Hakutaka tena kushiriki katika mauaji yoyote yale, moyo wake ulibadilika na ni kitu kimoja tu ndicho kilichokuwa kikimfurukuta moyoni mwake, kumtumikia Mungu katika roho na kweli.
Baada ya kumuweka Godwin ndani ya boksi lile na kulitupa baharini huku akiwa ameweka maboya ndani yake, akaondoka, hakutaka kurudi tena na hivyo kumpigia simu Rais Bokasa na kumwambia kwamba huo ndiyo ulikuwa mwisho wake wa kutumikishwa kufanya mauaji mbalimbali.
Akaanza kumuabudu Mungu, akajiunga katika Kanisa la Praise And Worship lililokuwa Tabata Bima. Hakutaka kusikia kitu chochote kile mbali na kumuabudu Mungu, akaanza kuwa mshirika wa kanisa hilo, akajiunga na kikundi cha vijana cha kuhubiri Injili sehemu mbalimbali nchini Tanzania na baada ya miaka miwili ya huduma hiyo akaamua kwenda kusomea uchungaji katika Chuo kilichopo mkoani Dodoma.
Moyo wake ukaendelea kubadilika, akaendelea kumuhubiri Mungu sehemu mbalimbali na alipomaliza kusomea masomo ya kichungaji ndipo akakabidhiwa kanisa lililokuwa Magomeni Mapipa jijini Dar es Salaam.
Hapo ndipo ambapo Godwin alitaka kwenda kwa ajili ya kumshukuru kwa kila kitu alichokuwa amemfanyia, aliamini kwamba bila mwanaume huyo basi angekuwa marehemu kwani alikuwa na nguvu zote za kummaliza lakini kitu cha ajabu kabisa ambacho hata yeye mwenyewe alikishangaa, aliyakuta maboya ndani ya boksi na wakati alitekwa na mtu huyo huku akipewa amri ya kummaliza.
Alipofika kanisani hapo kulipokuwa na ibada iliyokuwa ikiendelea, akaelekea nyuma kabisa ya kanisa na kutulia hapo. Macho yake yalikuwa yakiangalia mbele, kulikuwa na kwaya iliyokuwa ikiimba kanisa hapo lakini macho ya Godwin yalikuwa kwa mchungaji huyo aliyetulia katika kiti chake huku akisikiliza kwaya iliyokuwa ikiendelea kumuimbia Mungu.
Hakuwa na haraka, aliendelea kusubiri mpaka pale ibada ilipokwisha ambapo moja kwa oja akamfuata mchungaji huyo kwa lengo la kuzungumza naye na kumwambia kile kilichokuwa kimempeleka mahali pale.
“Bwana Yesu Asifiwe mchungaji,” alisalimia Godwin huku akimwangalia mchungaji huyo ambaye baada ya macho yake kutua usoni mwa Godwin, alihisi kuwahi kumuona sehemu fulani.
“Amen! Hujambo mtumishi wa Mungu?” aliuliza huku akimwangalia kwa mtazamo uliomaanisha kwamba alitaka kukumbuka mahali alipowahi kumuona mwanaume huyo.
“Nashukuru Mungu ni mzima kabisa.”
Bado mchungaji Kihampa alikuwa akiendelea kukumbuka, kichwa chake kilikuwa kikifikiria mbali kabisa, aliendelea kujaribu kuikumbuka sura hiyo lakini alishindwa kabisa. Alipoona kwamba haikuwezekana, akamuuliza ambapo bila tatizo lolote lile Godwin akajitambulisha.
“Godwin?” aliuliza huku akiendelea kumwangalia vizuri kabisa.
“Ndiyo mchungaji!”
“Godwin yupi?”
“Wa boksi lililotupwa baharini miaka mingi iliyopita,” alisema Godwin.
Maneno hayo ndiyo yakamfanya mchungaji huyo kuanza kukumbuka kila kitu kilichokuwa kimetokea, hakuwa mgeni tena, alimkumbuka, yeye ndiye alikuwa mtu pekee aliyemuokoa katika mauti kwa kumuweka maboya kadhaa ndani ya boksi alilokuwa amefungwa na kutupwa baharini.
Hapohapo Kihampa akamsogelea zaidi Godwin na kumkumbatia, moyo wake ukawa na furaha tena kwani kwa kipindi chote hicho hakuwa na uhakika kama kijana huyo alinusurika baharini kama alivyokuwa amekusudia alikuwa alikuwa amekufa baharini.
Hapo ndipo Godwin alipoanza kusimulia kila kitu kilichokuwa kimetokea, ilikuwa ni stori ileile ambayo aliisikia sana midomoni mwa watu mara baada ya kusoma katika mitandao ya kijamii.
“Wewe ndiye huyu Godwin msumbufu aliyeitoa Tanzania katika mikono ya Bokasa?” aliuliza Kihampa.
“Ndiyo! Ninamshukuru Mungu kwamba nilipambana kwa nafasi yangu, alinipigania sana, na ninashukuru kwa sababu bila yeye nadhani nisingeweza kumkimbia Bokasa,” alisema Godwin huku akimwangalia mchungaji huyo.
Walibaki na kuzungumza mambo mengi mno, walifurahi na kucheka pamoja kiasi kwamba hata baadhi ya washirika wa kanisa hilo walikuwa wakishangaa, hawakuwahi kumuona mchungaji wao akiongea na mtu mmoja kwa kipindi kirefu kama ilivyokuwa kwa kijana huyo.
Walitumia dakika kadhaa na walipomaliza, Godwin akaondoka kurudi nyumbani ambapo huko akawasiliana na Kambili na kumwambia kwamba alitakiwa kujiandaa kwani uchaguzi mkuu ungeitishwa na yeye kuwa miongoni mwa wagombea ambao walitakiwa kugombea, kwa hiyo alitakiwa kuwaahidi wananchi vile tu ambavyo atavifanya katika uongozi wake, asivyoviweza, aachane navyo.
“Haina shida! Ila kuna siku ningependa sana kukuona,” alisema Kambili.
“Usijali! Kuna siku utaniona, tutazungumza sana, ila bahati mbaya hutonijua kama ndiye mimi,” alisema Godwin kwenye simu.
“Kwa nini unataka kujificha kila siku?”
“Kwa sababu vita vizuri ni kupambana na mtu asiyekujua. Nipo kwa ajili ya Watanzania, tukiongea na kuonana mara kwa mara, utajenga urafiki nami, siku ukifanya ujinga, sitokufanya kitu kwa kuwa wewe ni rafiki yangu, ila ili niwe na nguvu ya kukufanya lolote lile, ni lazima nisiwe rafiki yako, ili siku nikikupiga, nimpige mtu asiyekuwa rafiki yangu,” alijibu Godwin.
“Haina shida! Nitahakikisha napambana kufanya kila kitu ambacho Watanzania wengi wamekuwa wakihitaji kutoka kwangu,” alisema Kambili.
“Nashukuru sana.”
Japokuwa hakuwa na cheo chochote kile lakini Jenerali Ojuku alikuwa akimheshimu mno Godwin, kila alipokuwa akimpigia simu, kwa jinsi alivyokuwa akizungumza naye alizungumza kiheshima, alionekana kama kiongozi wake kiasi kwamba kwa lolote lile ambalo angelisema mwanaume huyo angemuunga mkono kwa asilimia mia moja.
Siku zikaendelea kukatika, miezi sita ilipokatika watu wakawa na hamu ya kuingia katika uchaguzi mkuu ambao haukufanyika nchini humo ngazi ya rais kwa takribani miaka kumi na ishirini, kila mtu alitaka kushuhudia kile ambacho kingetokea.
Wagombea waliokuwa wakigombea nafasi hiyo waliendelea kupiga kampeni ya kuzunguka kila kona nchini Tanzania kuhakikisha kwamba wanachaguliwa na kuiongoza nchi hiyo. Kambili hakuwa na tabu, aliamini kwamba jina la Godwin lingeweza kumpa nafasi hiyo na kila alipokuwa akisimama jukwaani, alisema wazi kwamba angeiongoza nchi hiyo kwani hata Godwin alimuamini kwamba anaweza kufanya yale ambayo Watanzania wote wangependa ayafanye kwa miaka mitano ya kwanza.
“Naombeni mnipe dhamana! Nitahakikisha Tanzania mpya inarudi, kama Godwin ameniamini, kwa nini usiniamini? Nawaahidi wote kwamba sitawaangusha,” alisema Kambili alipokuwa akizungumza na wananchi
“Umepita baba!” alisikika mwanamke mmoja akisema kwa sauti.
“Nimepita?” aliuliza.
“Ndiyoooooo!” watu wote waliitikia kwa sa
Kampeni zilikuwa zikiendelea kila siku, katika kila mkoa ambao Kambili alikuwa akisimama na kuzungumza, Godwin alikuwa kwenye umati wa mkutano huo. Hakukuwa na mtu aliyemfahamu, alikuwa akisikia mauoni ya watu mbalimbali na kila mtu ambaye alimzungumzia Kambili, alisema wazi kuwa kura yake ingekwenda kwa mtu huyo kwa sababu tu Godwin alimwamini.
“Nitampa jamaa kura yangu kwa kuwa Godwin amemwamini! Kama Godwin amekukubali, kwa nini mimi nisikukubali? Ni lazima nikukubali kwani yule jamaa ndiye mkombozi wetu,” alisema mwanaume mmoja huku akionekana kuwa na furaha tele.
***
"Mpo wapi?"
"Nairobee! Kuna lolote the big boss?" ilisikika sauti ya mtu mwingine.
"Mnaweza kuja huku Mombasa mara moja!"
"Hakuna shida, tunakuja!"
"Sawa. Nawasubir! Njooni haraka sana hapa white house," alisema mwanaume mmoja.
"Okay!"
Yalikuwa mazungumzo baina ya watu wawili waliokuwa wakiwasiliana kwa njia ya simu. Mmoja alikuwa Mombasa na mwingine jijini Nairobi nchini Kenya. Mazungumzo yao hayakuwa marefu sana, wakakata simu na kila mtu kuendelea na mambo yake.
Mwanaume aliyevalia suti alikaa nyuma ya meza yake katika ofisi yake iliyokuwa ndani ya jumba moja kubwa ambalo kila mtu hapo Mombasa aliliita kwa jina la White House kama ilivyoitwa ikulu ya Marekani. Muda wote mwanaume huyu alikuwa na sigara kubwa aina ya sigar mdomoni mwake, alikaa kwa kujiachia na mezani kwake kulikuwa na mafaili mengi pamoja na cd ambazo ni yeye tu ndiye alijua humo kulikuwa na nini.
Mwanaume huyu aliitwa Stephano Olotu, alikuwa miongoni mwa wafanyabiashara wakubwa nchini Kenya. Alimiliki utajiri wa dola bilioni mbili ambazo zilikuwa ni zaidi ya shilingi trilioni 4, alikuwa na migahawa mingi jijini Nairobi, migodi ya dhahabu na pia alimiliki kisima cha mafuta nchini Nigeria.
Japokuwa alikuwa mfanyabiashara aliyekuwa na mafanikio makubwa na hata kufanya biashara za halali kabisa lakini nyuma ya pazia mwanaume huyo alikuwa na michezo mingi ya hatari. Alijishughulisha na uuzaji wa madawa ya kulevya, maisha yake yalikuwa ni kutanua na wanawake mbalimbali Afrika nzima. Kwa kuwa alikuwa na jina kubwa alilitumia vilivyo kuweka mikakati kabambe kuzoeana na marais wengi ili kuweza kufanya biashara zake za madawa ya kulevya.
Miongoni mwa marais waliokuwa wakipiga naye mishemishe alikuwa Rais Bokasa, alitumia kiasi kikubwa cha pesa kuwekeza nchini Tanzania, huko, aliwatafuta wafanyabiashara wenzake ambao walikuwa wakifanya biashara haramu ya madawa ya kulevya kwa kupitia mgongo wa rais huyo.
Hakuwa akiwafahamu wafanyabiashara hao, Bokasa alikuwa mjanja, alimwambia kwamba mzigo ulitakiwa kufika kwake kwanza na yeye kuwafikishia hao wafanyabiashara wengine ambapo ulipokwisha, alichukua asilimia kumi na tisini ya pesa iliyolipwa kwenda kwa Olotu.
Hayo ndiyo yalikuwa maisha yake. Katika kipindi chote hicho Bokasa hakutaka kumruhusu Olotu kuwafahamu wafanyabiashara wengine aliokuwa akifanya nao biashara hiyo kwani alijua kwamba kama angeruhusu hilo basi kusingekuwa na ulazima wa Olotu kumtafuta na kuwauzia wenzake mzigo mkubwa ambao alikuwa akiutuma nchini humo.
Bokasa aliondolewa madarakani huku akiwa bado hajakabidhi pesa alizokuwa ameuza mzigo mkubwa uliokuwa na thamani ya shilingi bilioni mia tatu. Olotu alichanganyikiwa, hakuamini kama kweli pesa zake asingezipata kwa kuwa tu rais huyo alikuwa ameondolewa madarakani.
Kwa kipindi hicho alihitaji pesa hizo, hakuwa na njia nyingine za kupata mzigo huo zaidi ya kumuuliza Bokasa juu majina ya wafanyabishara aliokuwa akiwauzia kwani alifanya siri lakini kwa hatua aliyokuwa amefikia, hakukuwa na siri tena, alitaka kuambiwa ili awafuate na kudai pesa zake.
Kumpata Bokasa halikuwa jambo jepesi, mwanaume huyo alikuwa nchini Ubelgiji akiendelea kupata matibabu, hakukubali kuona akifa pasipo kumwambia ukweli juu ya mzigo wake hivyo kitu pekee alichokiamua ni kuwasiliana na vijana wake, wasafiri mpaka nchini huko na kumuuliza juu ya wafanyabisahara hao, na kama hataki kuwaambia ukweli basi wamteke, waondoke naye mpaka nchini Kenya ambapo angefanya kitu kimoja tu, kumuua ili kuiridhisha nafsi yake kwa dhuluma aliyokuwa akifanyiwa.
Baada ya saa mbili, vijana wale aliowapigia simu wakafika Mombasa na kuanza kuzungumza nao, aliwaambia hitaji lake kwamba alitaka wao wasafiri mpaka nchini Ubelgiji ambapo huko wangekwenda mpaka katika hospitali aliyolazwa na kumteka huko.
Mipango ikapangwa ndani ya jumba hilo kubwa na hivyo kutakiwa kwenda nchini humo kwa ajili ya kuhakikisha mwanaume huyo anapelekwa haraka sana mikononi mwake na kufanya kile alichotaka kukifanya.
"Hana ulinzi?" aliuliza kijana mmoja, huyo aliitwa Wilson.
"Sijajua! Ila nina uhakika hana ulinzi, atakuwaje na ulinzi na wakati hapendwi? Ninachokitaka ni kujua majina ya wafanyabiashara aliokuwa akifanya nao biashara yangu," alisema Olotu.
"Basi haina shida."
Baada ya siku tatu wanaume wawili, Wilson na Okotee wakaondoka nchini Kenya na kwenda Ubelgiji kwa ajili ya kukamilisha kile walichoambiwa. Hawakuona kama wangepata tabu kwani tayari waliambiwa kuwa Bokasa alikuwa katika Hospitali ya Clinique Saint Jean iliyokuwa katika Jiji la Brussels akiendelea kupatiwa matibabu kutokana na tatizo la presha alilokuwa amelipata.
"Tukifika, ni kumchukua na kurudi naye, sidhani kama tutashindwa. Cha msingi ndege ya rais binafsi iandaliwe kwa ajili ya kuondoka naye," alisema Wilson, kwao, kitendo cha kumchukua Bokasa na kwenda naye nchini Kenya hakukuwa na tatizo lolote lile, ilikuwa ni kama kumsukuma mlevi katika mteremko wa mlima.
Wakati vijana hao wakiwa njiani, alichokifanya Olotu ni kumpigia simu Rais Onyango wa hapo Kenya na kumwambia kuhusu lengo lake. Alimwambia ukweli kuhusu mzigo wa madawa ya kulevya ambao kipindi hicho hakujua uliuzwa kwa wafanyabiashara gani nchini Tanzania, ilitakiwa mtu huyo achukuliwe kutoka Ubelgiji na kupelekwa Kenya kwa lengo la kuwajua watu hao.
"Si tatizo! Unataka nikusaidie nini Olotu?" aliuliza Rais Onyango.
"Ndege yako kwenda kumsafirisha kutoka Ubelgiji kuja huku!" alijibu Olotu.
"Una uhakika ataweza kutolewa hospitalini?" aliuliza.
"Hilo si tatizo!"
"Unajua kama kuna ulinzi huko?"
"Ulinzi gani?"
"Tanzania imetuma ulinzi, kuna watu wanamlinda usiku na mchana mahali hapo."
"Haina shida! Watu niliowatuma ni hatari sana. Hata kama utaweka ulinzi wa Kimarekani, mwisho wa siku tunapata tunachokitaka," alitamba Olotu.
"Basi sawa. Wasiliana nao, waulize siku gani huyo mtu atakuwa mikononi mwao kwa lengo la kumchukua na kumsafirisha!"
"Haina shida. Ila nafikiri baada ya siku tatu. Yaani Jumatano kila kitu kitakuwa sawa."
"Haina shida."
***
Bokasa alikuwa kitandani, aliendelea kupumulia mashine ya hewa ya oksijeni, hakuwa na nguvu kitandani pale na kila muda macho yake yalikuwa yakiangalia huku na kule. Alipewa taarifa kwamba kulikuwa na maofisa wa Usalama wa Taifa ambao walikuwa hapo kwa lengo la kumlinda na kuhakikisha wanasafiri naye kuelekea nchini Tanzania mara baada ya kupata nafuu.
Hakutaka kurudi Tanzania, alitamani kuendelea kubaki nchini humo, alijua dhahiri kile kilichokuwa kikienda kutokea mara baada ya kufika huko. Hakutaka kwenda, hakutaka kuona akifungwa gerezani kwa maovu yote aliyokuwa ameyafanya katika kipindi alichokuwa rais wa nchi hiyo.
Kwa kuwa kulikuwa na kazi kubwa, wakaongezwa maofisa wa Usalama wa Taifa wengine ili wawe wanabadilishana mpaka pale ambapo mwanaume huyo angepata nafuu na kupelekwa nchini Tanzania.
"Doctor! There is something we have to discuss," (dokta! Kuna kitu nataka tujadili) alisikika msichana fulani kutoka kwenye simu, alimpigia simu daktari mkuu wa hospitali hiyo, Dk. Thump.
"Who are you?" (wewe nani?)
"Amanda Kalulu."
"What is it about?" (kuhusu nini?)
"About my uncle!" (kuhusu mjomba wangu)
"Who is that?" (nani huyo?)
"Bokasa!"
Alipolitaja jina hilo tu daktari akajua ni mtu gani alikuwa akizungumziwa. Hakumjua msichana huyo aliyempigia simu ambaye alitaka sana kuonana naye. Hilo halikuwa tatizo, akamwambia kwamba kama inawezekana basi waonane na kuzungumza kuhusu mwanaume huyo.
Baada ya saa mbili wakaonana ndani ya hospitali hiyo na kuanza kuzungumza. Mwanamke mrembo alikuwa katika kiti cha wageni ndani ya ofisi ya daktari huyo, alifika mahali hapo kwa ajili ya kuzungumza naye kuhusu mgonjwa aliyekuwa ameletwa ambaye alisema kwamba alikuwa mjomba wake.
Walikaa na kuzungumza mambo mengi, alimwambia kuhusu rais huyo kwamba alikuwa mjomba wake kabisa na alisikitishwa kwa taarifa ya ugonjwa aliokuwa nao ambao ulisababisha kupelekwa ndani ya hospitali hiyo.
"Lengo lako ni nini?" aliuliza Dk. Thump.
"Tumekaa kama familia na kuamua jambo moja!" alisema.
"Lipi?"
"Kumpeleka mgonjwa wetu nchini Ufaransa. Anateseka na tunaona kabisa matibabu ya hapa si mazuri kama ambavyo yanatakiwa kuwa. Miezi sita ni mingi sana," alisema mwanamke huyo.
Dokta Thump alibaki akimwangalia mwanamke huyo, kwa jinsi muonekano wake ulivyokuwa ilikuwa vigumu mno kugundua kwamba hakukuwa na uhusiano wowote ule baina yake na mgonjwa aliyekuwa amelazwa ila kwa kuwa alikuwa akiongea kwa huruma sana na wakati mwingine machozi kumtiririka, daktari akajihisi hukumu kubwa moyoni mwake.
Wakati wakizungumza, mara simu ya mwanamke yule ikaanza kuita, hakutaka kuchelewa, akaipokea na kuanza kuzungumza na mwanaume wa upande wa pili, kwa jinsi mazungumzo yao yalivyokuwa, ilionyesha kabisa kwamba aliyepiga simu alikuwa ndugu yake ambaye naye alitaka kufahamu hali aliyokuwa nayo Bokasa.
"Ni mgonjwa mno. Kama ndugu tulivyokubaliana, inabidi asafirishwe na kuelekea nchini Ufaransa," alisema mwanamke huyo.
"Sawa. Nakuja na familia yangu kumuona," alisikika mwanaume huyo wa upande wa pili.
Hicho ndicho kilichofanyika, ndani ya nusu saa, mwanaume mwenye ndevu nyingi akafika hospitalini hapo na moja kwa moja kuonana na Dk. Thump huku akiwa na familia yake ya watu sita.
"Kaka anaendeleaje?" aliuliza mwanaume huyo huku akimwangalia Amanda.
"Ni mgonjwa sana, miezi sita ni mingi mno, hatutokuwa tayari kusubiri kipindi chote hicho," alisema Amanda huku akimkumbatia ndugu yake huyo aliyejitambulisha kwa daktari kwa jina la Sebastian Gambole.
Ilikuwa ni vigumu sana kugundua kwamba huo ulikuwa mchezo uliokuwa umepangwa, watu hao walikuwa mahali hapo kwa lengo la kumtorosha Bokasa na kuelekea nchini Kenya ambapo tayari walikutana na Wilson na mwenzake na kupanga ni kwa jinsi gani mwanaume huyo alitakiwa kusafirishwa kuelekea huko badala ya Ufaransa kama walivyokuwa wamemwambia daktari.
Kitu cha kwanza walichohitaji ni kuonana na mgonjwa wao, hilo halikuwa tatizo, wakapelekwa katika wodi ile na kuonana naye ambapo huko wakampiga picha na kumtumia Wilson ambaye alithibitisha kwamba huyo ndiye mtu aliyetakiwa kusafirishwa.
"It is him!" (ndiye yeye!)
"Okay!" (sawa)
***
Ilikuwa kazi ambayo ilitakiwa kufanyika haraka sana kabla ya watu kujua kile kilichokuwa kikiendelea. Walichokifanya mara baada ya kumpiga picha na Wilson kusema kwamba alikuwa ndiye mtu aliyehitajika, wakaondoka hospitalini hapo na kwenda kupanga mikakati ya kumtoa mwanaume huyo katika hospitali hiyo pasipo mtu wale walinzi kutoka Tanzania kufahamu chochote kile.
Mpango waliokubaliana ilikuwa ni lazima wajifanye madaktari ili iwe rahisi kuingia na kuondoka humo na mtu huyo lakini pia kwa Wilson na Okotee walitakiwa kujifanya madaktari waliokuwa wakizungumziwa kutoka nchini Ufaransa ambao walifika mahali hapo kwa lengo la kumchukua Bokasa.
“Na itakuwaje kuhusu Dk. Thump?” aliuliza Amanda.
“Ni kazi nyepesi sana. Kwa kuwa amekubaliana nanyi, hakuna tatizo, kitakachotakiwa ni kumlazimisha kufanya kile tunachokihitaji au vinginevyo tumuue,” alisema Wilson.
“Sawa. Haina shida kama ni hivyo!”
Walitakiw akujiandaa, Dk. Thump hakutakiwa kuhusika, aliambiwa kwamba ndugu wa mgonjwa ndiyo waliokuwa wakishughulikia kila kitu na wao ndiyo waliokuwa wakijia ni hospitali gani mgonjwa wao alitakiwa kwenda.
Hilo halikuwa tatizo, kitu pekee alichokiandaa ni ripoti kuhusu ugonjwa wa Bokasa ambayo ndiyo walitakiwa kupewa madaktari na hivyo kuondoka naye. Ndege ikaandaliwa tayari kwa kuanza safari ya kuelekea nchini Kenya, kitu pekee kilichobaki ni kuona kama kungekuwa na uwezekano wa kuondoka mahali hapo pasipo wale Usalama wa Taifa wa Tanzania kujua kilichokuwa kikiendelea.
“Hivi kile chumba hakina mlango wa nyuma?” aliuliza Okotee.
“Unao! Niliangalia tulipokwenda kumuona, tuliuona mlango wa nyuma,” alisema Amanda.
“Basi itakuwa vizuri kama tukiutumia huo,” alisema Wilson.
Walipanga mipango yao, ilipokamilika, siku iliyofuata Amanda na wenzake walitakiwa kwenda huko kwa ajili ya kukamilisha mipango midogomidogo iliyokuwa imebaki. Walipofika katika hospitali hiyo wakawasiliana na Dk. Sebastian na kumwambia kwamba madaktari kutoka nchini Ufaransa ambao walikuwa wameandaliwa na familia waliwasili nchini humo.
“Nitatakiwa kuonana nao na kuwapa ripoti kuhusu mgonjwa huyo,” alisema.
Hilo halikuwa tatizo, wakasubiri na ilipofika majira ya saa nane mchana, Wilson na Okotee wakaenda mpaka hospitalini hapo na kuanza kuzungumza naye. Walizungumza Kiingereza kizuri kabisa huku wakati mwingine wakichanganya na Kifaransa ili kuvuta uasilia wa kile walichokuwa wakikitaka mahali hapo.
“Ripoti inasemaje?” aliuliza Wilson huku akimwangalia Dk. Sebastian.
“Ana tatizo la presha, hilo tu!”
“Basi sawa.”
Walijifanya kuwa bize kukagua ripoti hiyo na baada ya muda wakamwambia kwamba walitakiwa kumuona mgonjwa wao ili wajue ni kwa namna gani walitakiwa kufanya kazi ya kumsafirisha na kumpeleka nchini Ufaransa.
Walipoingia ndani ya chumba hicho, umakini wao haukuwa kwa mgonjwa, walikuwa wakiangalia mazingira ya chumba hicho na ule mlango walioambiwa kwamba ulikuwa humo. Walipojiridhisha, wakawaambia watu wote watoke ili wamchunguze kwa umakini?
“Mpaka sisi?” aliuliza Wilson.
“Ndiyo! Kila mtu!” alijibu Wilson huku akijifanya kama mtu aliyekuwa makini kwa kile alichokifanya.
Manesi waliokuwa humo, madaktari kutoka katika hospitali hiyo wakatoka ndani, ilikuwa ni lazima wamchunguze mgonjwa zaidi, lakini lengo la kufanya hivyo ilikuwa ni kama kumuandaa kwa safari pasipo walinzi kufahamu chochote kile.
Maofisa wale wa Usalama wa Taifa hawakutakiwa kuingia ndani, ulinzi wao waliufanya nje ya chumba kile, walisimama imara pasipo kuzungumza na mtu yeyote yule, kila kitu kilichokuwa kikiendelea walikuwa wakikiangalia kwa umakini kabisa na hawakuyatilia ulakini kwa kuwa walikuwa wakishirikiana na madaktari wa hospitali hiyo.
Kitendo cha Amanda na wenzake kutoka nje ulikuwa ni mpango ambao uliandaliwa, hawakukaa hapo, wakaondoka mpaka nje ya hospitali hiyo ambapo huko wakaandaa gari lao, wakazunguka kwa nyuma mpaka ulipokuwa mlango ule wa nyuma wa kuingilia ndani ya chumba kile na kuanza kugonga.
Wilson na Okotee wakajua kwamba hao walikuwa watu wao, wakaufungua mlango, wakaanza kukisukuma kitanda kile kupitia mlango ule na kukitoa nje huku Bokasa akiwa kitandani akishangaa, hakupewa taarifa juu ya kilichokuwa kikiendelea, aliona kama kulikuwa na mchezo uliokuwa ukifanyika.
Hawakutakiwa kugundulika hivyo Amanda na mwenzake wakaondoka na kuwaacha Wilson na mwenzake wakiisukuma machela kule nje. Kila mtu aliyekuwa akipishana naye hakuwa na wasiwasi nao, muonekano wao kuanzia mavazi, miwani waliyoivaa ilionyesha kabisa kwamba walikuwa madaktari hivyo kumpeleka Bokasa kwenye gari walilokuwa wamekuja nalo.
Hakukuwa na mtu aliyehoji kitu chochote kile, kitu cha ajabu hata manesi wengine waliokuwa wakikiona kitendo kile waliona ni kawaida sana, imani yao ilikuwa kubwa kwa madaktari hivyo kuhisi kwamba wale walikuwa madaktari wa hospitali hiyo na iliwezekana mgonjwa huyo alikuwa akihamishwa hospitali kwa matibabu zaidi.
Hawakuzungumza kitu, wakaingia ndani ya gari ambapo likawashwa king’ora na kuondoka mahali hapo kuelekea uwanja wa ndege. Kazi hiyo mara ya kwana ilionekana kuwa kubwa mno lakini baada ya kuifanya wakagundua kuwa ilikuwa kazi nyepesi mno ambayo isingeweza kuwasumbua hata kidogo.
“Kumbe ni nyepesi hivi! Haki ya Mungu tumemsukuma mlevi kwenye mteremko wa mlima,” alisema Wilson huku akimwangalia mwenzake kwa furaha kwani kile walichokuwa wamekifanya kilionekana kuwa kitu chepesi kuliko vyote walivyowahi kuvifanya.
Wakati hayo yakiwa yametokea, Dk. Sebastian alikuwa ofisini kwake, kitu pekee ambacho alijua ni kwamba madaktari wake walikuwa wakishughulika na mgonjwa ambaye alikuwa akiandaliwa tayari kwa kusafirishwa na kupelekwa nchini Ufaransa kwa ajili ya matibabu.
Baada ya dakika kadhaa, akaamua kutoka ndani na kuelekea kule. Huko, akaanza kuhisi kulikuwa na kitu kinaendelea kwani alipofika hapo, alishangaa kuwaona manesi wakiwa nje ya chumba kile pamoja na walinzi.
Hilo halikuwa jambo la kawaida, akawasogelea na kuwauliza sababu ya kuwepo hapo nje ambapo walimwambia kwamba wale madaktari walikuwa ndani ya chumba kile wakimwangalia zaidi mgonjwa wao.
“Wapo ndani wakimwangalia mgonjwa wao?” aliuliza Dk. Sebastian huku akiashangaa.
“Ndiyo!”
“Kivipi? Mbona hili ni jambo tofauti sana na utaratibu wetu!?” aliuliza Dk. Sebastian huku akiwaangalia kwa mshangao mkubwa.
Akaufuata mlango kwa lengo la kuufungua, alipofanya hivyo, mlango haukufunguka. Alishangaa, ilikuwaje madaktari hao wawe ndani huku manesi wake wakiwa nje? Ila jambo jingine ambalo lilimshangaza, kwa nini ndugu wa mgonjwa huyo hawakuwa mahali hapo?
“Na ndugu zao?”
“Waliondoka!”
Alipopewa jibu hilo tu akahisi kulikuwa na kitu kilichokuwa kikiendelea, akaugonga mlango, haukufunguliwa, akaugonga zaidi na matokeo yakawa vilevile hali iliyomtia hofu. Hawakuwa na jinsi, kama hali iliendelea hivyo ilikuwa ni lazima kuuvunja mlango, kitu walichotaka ni kujua kilichokuwa kikiendelea ndani ya chumba hicho.
Mlango ukavunjwa na walipoingia, hawakuwakuta madaktari, na mbaya zaidi hata mgonjwa hakuwa akionekana kitandani hapo hali iliyomshangaza kila mmoja.
Wakaitana, kila mtu aliyekuwa akiangalia kilichokuwa kimetokea, alishangaa. Usalama wa Taifa walipopewa taarifa, wakachanganyikiwa hivyo kuanza kuwatafuta watu hao hapo hospitalini. Walikuwa wamekwishachelewa kwani hata walipouliza walinzi wa getini waliwaambia kwamba kuna gari la wagonjwa liliondoka kama dakika ishirini na tano zilizopita.
“Kuna gari liliondoka? Lina namba zipi?” aliuliza Dk. Sebastian! Akili yake iliruka.
“Bel89J0,” alijibu mlinzi.
“Hatuna gari hilo! Ni la hapa hospitali?”
“Hapana! Hilo sikuwahi kuliona. Na tulishindwa kuuliza chochote kwa kuwa tulijua kwamba ni madaktari ambao mlikubaliana nao kumchukua mgonjwa!” alisema mlinzi maneno yaliyomchanganya zaidi Dk. Sebastian.
Hakutaka kukubali, hakukukalika, akachukua simu na kukipigia kitengo cha ulinzi wa barabarani, akawaambia kwamba kulikuwa na tatizo limetokea, gari moja la wagonjwa liliondoka hospitalini huku likiwa na mgonjwa, hawakujua ni wapi lilielekea lakini baada ya kutaja namba zake, akaambiwa kwamba kamera za barabarani zililinasa gari hilo likielekea uwanja wa ndege.
“Unasema?”
“Kamera zinaonyesha hivyo!”
Hakutaka kuchelewa, haraka sana akawapigia simu polisi wa uwanja wa ndege. Alichanganyikiwa, kitendo cha mgonjwa huyo kuibwa hospitalini hapo kilionyesha kabisa kwamba angekuwa kwenye matatizo makubwa na angeweza hata kufukuzwa kazi, alipopiga huko, akaambiwa kwamba gari hilo lilikuwepo kwani liliingia mpaka ndani kabisa ya uwanja huo.
“Hebu lizuieni. Kuna mgonjwa humo ameibwa. Lizuieni,” alipiga kelele Dk. Sebastian huku akivua koti lake tayari kwa kwenda huko uwanjani.

Je, nini kitaendelea?
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom