Dunia haina usawa

Dunia haina usawa

SEHEMU YA 21

Mapoto na viongozi wengine wa Chama cha Tanzania National Party walichanganyikiwa, hawakuamini kile kilichokuwa kimetokea kwamba waliangushwa vibaya katika uchaguzi ule na wakati walikuwa na idadi kubwa ya watu waliotaka mabadiliko, watu waliojitoa kwa ajili yao, kupambana mpaka tone la mwisho la jasho.

Walikaa ndani ya jengo la makao makuu ya chama chao na kujifikiria walishindwa wapi. Walisikia kwamba waliongoza kwenye mchakato mzima wa kupiga kura mikoani lakini mwisho wa siku wakaambiwa kwamba walishindwa uchaguzi huo.
“How?” (kivipi?) aliuliza Mapoto huku akimwangalia kila mmoja ndani ya chumba walichokuwa.

Hakukuwa na mtu aliyejibu kitu, kila mmoja alichanganyikiwa, hakukuwa na maboksi ya kura za wizi waliyokuwa wameyakamata, walihakikisha kila kona kunakuwa na ulinzi lakini cha kushangaza, walishindwa uchaguzi, walishindwaje? Ilikuwaje? Nini kilitokea? Je, kweli wananchi waliwabadilikia? Kila kitu walichokuwa wakijiuliza mahali hapo, walikosa jibu kabisa.

Wakati kila mmoja akiwa na huzuni mahali hapo tena huku ukimya ukiwa umetawala kwa muda mrefu, mara simu ya Mapoto ikaanza kuita, hakutaka kuipokea kwani alikuwa amechanganyikiwa kupita kawaida, kila mtu alikuwa akimwangalia kwa mtazamo wa kumtaka angalie simu yake kuona nani alikuwa akimpigia, akaingiza mkono mfukoni na kuitoa simu hiyo.

Jina la Bokasa lilikuwa likionekana kwenye kioo cha simu yake. Hasira kali ikamkamata usoni mwake, akamwangalia kila mtu mule ndani na kuwaonyeshea simu ile ambapo wote kwa pamoja wakamwambia kwamba angepokea na kusikiliza mwanaume huyo alitaka kuzungumza naye nini.

“Halo!” aliita mara baada ya kupokea simu hiyo.
“Halo! Pole sana Mapoto. Najua unajisikia vibaya, najua umeumia sana, hizi ni siasa ambazo tunatakiwa kuachana nazo kwa muda na kuziweka akili zetu kukubaliana na kilichotokea,” alisikika Mapoto.

“Niambie nikusaidie nini?”
“Ninataka kuonana na wewe. Ninataka tuzungumze. Tusizungumze kama wapinzani, hebu tukutane na tuzungumze kama Watanzania! Nchi hii ni kubwa, pasipo mimi na wewe kudumisha urafiki, Watanzania watakuwa kwenye hali mbaya sana. Ninataka tukubaliane kitu kimoja,” alisikika Bokasa.
 
SEHEMU YA 22

“Tukubaliane kitu kimoja?”
“Ndiyo!”
“Wewe na mimi?”
“Ndiyo!”
“Inawezekana vipi?”
“Ni kwa sababu sisi wote ni Watanzania, sisi wote ni ndugu. Ninataka tulifanye hili kwa faida ya taifa na si mimi na wewe,” alisema Bokasa.

“Bokasa…”
“Nakuomba Mapoto, naomba nionane nawe. Kuna jambo nataka kulizungumza,” alisema Bokasa.
“Nitaangalia,” alisema Mapoto na kukata simu.
Jambo hilo likazua mjadala mahali hapo, walikuwa kwenye maumivu makali, waliamini kwamba waliibiwa kura japokuwa hawakujua hizo kura ziliibwa kwa mtindo gani.

Kitendo cha Mapoto kutakiwa kuonana na Bokasa kilizua gumzo mahali hapo kwa kuhisi kwamba mtu huyo alitaka kumuua ili kuizima nyota ya upinzani ambayo ilionkana kuwa tishio kubwa.
“Ninahofu watakuua!” alisema katibu wa chama hizo, Bwana John Pondamali.
“Acha tu niende!”

“Sawa. Ila hutakiwi kunywa maji wala chai! Hutakiwi kufanya chochote kile ukifika huko zaidi ya kumsikiliza,” alisema mwenyekiti wa chama hicho, Bwana Edward.
“Sawa. Ila ningependa kwenda na walinzi hata wawili!” alisema Mapoto.
“Haina shida!”

*** Kila mmoja alikuwa na hofu, waliamini kabisa kwamba kulikuwa na kitu ambacho Bokasa alitaka kukifanya, hasa kumuua Mapoto ambaye alionekana kuwa mwiba wa kuotea mbali.
Viongozi wa Chama cha Tanzania National Party walikubaliana naye lakini ilikuwa ni lazima aende huko akiwa na vijana wengine, walihisi kwamba kungekuwa na mchezo mchafu ambao ungeweza kuchezwa kitu ambacho hawakutaka kuona kikitokea.

Aliporudi nyumbani, Mapoto alionekana kuwa na mawazo tele, kichwa chake kiliuma mno, hakuamini kama kweli alikosa urais, alikubalika kila kona, kila alipopita, jina lake liliimbwa, alionekana kuwa tumaini la mwisho kwa wananchi wa Tanzania kwani chama ambacho kilikuwa madarakani kipindi hicho hakikufanya kitu, yeye aliutaka urais kwa kuwa aliamini kwamba angeibadilisha Tanzania kiuchumi na kuifanya kuwa na hadhi kubwa kama ilivyokuwa kipindi cha Mwalimu Nyerere.
 
SEHEMU YA 23

Mkewe, Rosemary akamfuata na kuanza kumfariji kwa kumwambia kwamba kukosa urais si mwisho wa kila kitu, iliwezekana kwamba Mungu alikuwa akimwandaa kwa miaka mitano ijayo na si kwa kipindi hicho, kama alipangwa kuwa mtetezi wa Watanzania, mtetezi wa wanyonge basi ilikuwa ni lazima kutokea hata kama isingekuwa kipindi hicho.

“Hutakiwi kuwa na hofu! Wewe bado ni mtetezi wa wanyonge, naamini Mungu anakuandaa, unachotakiwa kufanya ni kuvuta subira,” alisema Rosemary huku akimwangalia mume wake alioyeonekana kuwa na mawazo tele.

“Naamini mke wangu!”
“Basi jitie nguvu! Bado wewe ni mshindi,” alisema Rosemary.
Moyo wake ukawa na nguvu, akasimama na kumkumbatia mke wake, japokuwa alikuwa na marafiki wengi lakini mkewe ndiye aliyekuwa kila kitu, kwenye matatizo, alikuwa faraja yake, kwenye maumivu ya moyo, alikuwa furaha yake na hata kwenye hasira, alikuwa tabasamu lake.

Wakati hayo yakiendelea, Bokasa akampigia simu Mapoto na kumwambia kwamba wangekutana mara baada ya kuapishwa kwani kulikuwa na mambo mengi waliyotaka kuzungumza kwa faida ya Watanzania kitu ambacho kwa Mapoto hakikuonekana kuwa tatizo lolote lile.
“Dad! What is wrong with you?” (baba! Una nini?) aliuliza Godwin huku akimwangalia baba yake.

“I have nothing! It is time to sleep,” (sina kitu! Ni muda wa kulala) alisema Mapoto.
“Can you read for me a story about rabbit and the Queen Leah?” (unaweza kunisomea hadithi ya sungura na Malkia Leah?) aliuliza Godwin.

“Okey! Let me take you to bed,” (sawa! Ngoja nikupeleke kitandani)
Akambeba Godwin na kumpeleka kitandani ambapo huko akaanza kumsomea kitabu cha hadithi za watoto mpaka pale alipolala na Mapoto kutoka chumbani.

Japokuwa walikuwa na umri mdogo lakini Godwin na dada yake, Irene walikuwa watoto wenye akili sana darasani. Walikuwa na uwezo mkubwa kiasi kwamba hata walimu wenyewe walikuwa wakishangaa.
 
SEHEMU YA 24

Shuleni, hawakuwa wakishika nafasi zaidi ya mbili za juu. Katika kipindi chote walikuwa wakipokezana kushika nafasi ya kwanza. Katika kipindi hiki aliposhika Godwin, kipindi kijacho alishika Irene.
Walikuwa na upinzani mkubwa, walisoma sana kiasi kwamba walimu walihisi kabisa maisha ya mbele ya watoto hao yangekuwa yenye mafanikio makubwa.

Hakukuwa na somo ambalo hawakufanya vizuri, kwenye Hesabu, Kiingereza na masomo mengine walikuwa moto wa kuotea mbali.
Wazazi wao walijisikia faraja, kila walipokuwa wakienda shule kwenye vikao vya wazazi walipokea sifa mbalimbali kuhusu watoto wao jinsi walivyokuwa wakifanya vizuri na kuwashangaza walimu wao.

“They are very bright,” (wana akili sana)
“Are you sure?” (una uhakika?) aliuliza mwalimu mwingine.
“Yes! Apart from their brightness, they speak fluent English,” (Ndiyo! Ukiachana na akili zao, wanazungumza Kiiingereza kizuri sana) alisema mwalimu huyo.
Kila kona shuleni hapo sifa zilikuwa kwa watoto hao, walikuwa na uwezo mkubwa sana darasani, walifanya vizuri katika kila masomo kiasi kwamba kila mwalimu alitamani kuona watoto hao wakiwa watoto wao.

Katika somo la Hesabu, walijua kuhesabu kwa haraka zaidi ya wanafunzi wengine, walikuwa wanafunzi wa kwanza kujua kusoma kuliko wanafunzi wengine. Uwezo wao wa akili uliwachanganya walimu wengi mpaka kujidharau kwa kuhisi kwamba watoto hao hawakustahili kabisa kuzaliwa nchini Tanzania.

Baada ya wiki moja, Bokasa akaapishwa na kuwa rais wa Tanzania. Si watu wote waliofurahi, zaidi ya asilimia themanini ya Watanzania walichukia kwa kuwa waliamini kwamba mtu huyo asingeweza kuwaletea mabadiliko waliyokuwa wakiyataka.

Wengi walilalamika lakini hakukuwa na mtu aliyekuwa na uwezo wa kubadilisha matokeo, Bokasa akawa rais wa Tanzania kitu kilichozungumzwa sana barani Afrika kwamba iliwezekanaje mtu aliyekuwa na mashabiki wengi kama Mapoto akose nafasi hiyo.
“Mkuu! Hali naona si nzuri kwa chama pinzani,” alisema mshauri wa Rais Bokasa.
 
SEHEMU YA 25

“Najua watu wanalalamika sana ila ninachoshukuru hakuna mtu anayejua ni kwa jinsi gani mchezo umechezwa. Ninahitaji kufanya kitu kimoja, kama Mapoto ataendelea kubaki hapa Tanzania, anaweza kujijenga zaidi na kuleta upinzani mkubwa mwaka 2003. Nahisi kuna kitu ninahitaji kufanya,” alisema Rais Bokasa.

“Kitu gani?”
“Nataka nimpe ubalozi nchini Nchini India! Akawe balozi huko, akasahaulike katika vichwa vya Watanzania ili hata mwaka 2003 usiwe wa upinzani mkubwa,” alisema Bokasa huku akimwangalia mshauri wake.

“Ni wazo zuri ila sidhani kama atafurahi kuwa balozi nchini humo,” alisema mshauri huo.
“Wewe unahisi wapi ataweza kukubaliana napo?”
“Marekani!”
“Basi haina shida.”

Rais Bokasa akampigia simu Mapoto na kuomba kuzungumza naye, hilo halikuwa tatizo, kabla ya kwenda huko Mapoto akatoa taarifa kwa viongozi wa chama hicho ambao walimpa vijana wawili na kwenda nao ikulu.

Walipofika, akaomba kukaa naye sehemu, wawe wawili, wazungumze kile ambacho alikuwa amemuitia. Hilo halikuwa tatizo, wakaelekea katika bustani iliyokuwa hapo ikulu na kuanza kuzungumza.

Alimgusia suala lote la kuwa balozi nchini Marekani. Mara ya kwanza kwa Mapoto ilikuwa ngumu kukubaliana naye, hakutaka kuondoka nchini Tanzania, alijua kwamba yeye ndiye angekuwa rais wa nchi hiyo miaka mitano mbele, hivyo alitaka kuendelea kubaki ili ajiimarishe kwa miaka hiyo.

“Mapoto! Najua unatamani, lakini kumbuka kwamba sasa hivi ni kipindi cha kuijenga nchi yetu. Naomba, ninakuheshimu sana, wewe ni kichwa, nimeangalia watu wengi, hawana uwezo kama wako, una akili sana na ndiyo maana nimeamua kukupeleka Marekani na wengine kuwapeleka sehemu nyingine,” alisema Bokasa.
 
SEHEMU YA 26

Alikuwa akimsifia Mapoto, alimfanya kujiona yeye alikuwa mtu muhimu, mwenye akili kuliko Watanzania wote, kumfanya kujiona kwamba hakukuwa na mtu mwingine aliyetakiwa kuwa balozi nchini Marekani zaidi yake.

Hilo likaulegeza moyo wa Mapoto na mwisho wa siku kukubaliana naye, hakujua kwamba kwa kufanya hivyo ndiyo ilikuwa njia moja ya kumpoteza kisiasa, hakuangalia mbele, kwake, kuwa balozi nchini Marekani ilionekana kuwa heshima kubwa.

“Una uhakika hili litakusaidia?” aliuliza mke wake.
“Ndiyo! Naamini kwamba litasaidia. Najua jinsi watu wanavyonipenda, haijalishi kama nitakuwa nchini Marekani au wapi, nitakachokifanya ni kuendeleza mapambano hukohuko na ninakuhakikishia mpaka mwaka 2003 nitakuwa na nguvu hiihii,” alisema Mapoto huku akiwa na uhakika kwa kile alichokuwa akikizungumza.
“Sawa.”

Baada ya siku mbili, Mapoto akatangazwa kama balozi nchini Marekani. Hilo likaibua maneno mengi, watu wakakasirika, wengine wakatukana kwani walijua kabisa kwamba Bokasa alitumia njia hiyo kama kumzima Mapoto kisiasa.

Watu wakamuona Mapoto kama msaliti kwani hawakutaka kuona akiwa balozi, kitendo cha kumpeleka Marekani kingemfanya kutokuonekana, kumdhoofisha kisiasa na hivyo kupotea kabisa.

Maneno mengi mitaani, lawama zote hazikuweza kubadilisha kitu chochote kile kwani baada ya wiki mbili, yeye na watoto wake wakaondoka kuelekea nchini Marekani. Mke wake, Rosemary hakwenda naye, aliendelea kukaa nchini Tanzania akiendelea na kazi yake ya ualimu katika Shule ya Wasichana ya Azania alipokuwa akifundisha.

“Nakutakia safari njema! Usisahau kuendelea kuwafundisha watoto wetu kuhusu kumjua Mungu,” alisema Rosemary wakati akiagana na mumewe katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere.

“Usijali katika hilo.”
“Nakupenda sana mume wangu!”
“Nakupenda pia,” alisema Mapoto, wakakumbatiana na kuagana huku muda wote Rosemary akilengwa na machozi. Alitamani kumzuia mume wake lakini alishindwa kabisa.

Je, nini kitaendelea?
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom