Dunia haina usawa

Dunia haina usawa

SEHEMU YA 27

Ndege kubwa ya Shirika la Ndege la American Airlines ilikuwa ikitua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa JFK uliokuwa jijini New York nchini Marekani. Hiyo ilikuwa ni mara ya kwanza kwa Bwana Mapoto kufika katika jiji hilo kubwa la biashara, achilia mbali na Los Angeles, Texas ambapo alikuwa akifika huko mara kwa mara.

Hali ya hewa ilikuwa nzuri, hakukuwa na baridi kali, kulikuwa na dalili ya mawingu huku kwa mbali jua likianza kuzama. Walipoteremka kwenye ndege pamoja na abiria wengine, Mzee Mapoto akaanza kuangalia huku na kule, alilishangaa jiji hilo, lilikuwa kubwa na lililokuwa na majengo makubwa, kwa kifupi lilionekana kuvutia kuliko Los Angeles.

“Karibu sana mkuu,” alisema mwanaume mmoja aliyekuwa mahali hapo kwa ajili ya kuwapokea.
“Nashukuru sana!”
Wakaingia kwenye gari na safari ya kuelekea katika mtaa wa kitajiri wa Lenox Hill kuanza. Muda wote macho yao yalikuwa yakiangalia nje, jiji hilo lilionekana kuwa na mvuto mno na hakuamini kama alikuwa amekwenda kuanza kazi huko.

Alisahau mambo ya siasa kwa muda, akasahau kwamba kulikuwa na watu waliokuwa wakimuhitaji sana nchini Tanzania, kitu alichokifikiria sana kwa kipindi hicho ni namna ambavyo angefanya kazi yake ya ubalozi nchini humo.

Walichukua dakika thelathini mpaka kufika katika mtaa huo ambapo gari likasimama nje ya jumba moja kubwa la kifahari na geti kuanza kujifungua na gari kuingizwa.

Hakukuwa na aliyeamini kama wao ndiyo wangekwenda kuishi ndani ya jumba hilo kubwa. Lilikuwa na bwawa kubwa la kuogelea, bustani iliyokuwa na maua mazuri, mbuga ndogo ya wanyama na sanamu kubwa la Mwalimu Julius Nyerere huku katikati kukiwa na bendera ya Tanzania.

“Karibuni sana,” alisema dereva huyo na kuwafungulia milango.
Huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa maisha yao nchini Marekani. Kila mmoja alionekana kuwa mwenye furaha tele. Bwana Mapoto hakuacha kuwasiliana na mkewe, majukumu makubwa aliyokuwa nayo nchini Tanzania ndiyo yaliyomfanya kutokwenda pamoja naye.
 
SEHEMU YA 28

Mbali na watoto wake aliokuwa nao ndani ya nyumba hiyo, pia kulikuwa na wafanyakazi wake wawili wa kike ambao walikuwa wakisaidia kazi za ndani.
Akaanza kazi huku akimwagiza kijana ambaye alikuja kumpokea kumtafutia shule nzuri kwa ajili ya watoto wake. Hilo halikuwa na tatizo lolote kwani baada ya siku moja tu, akapewa orodha ya shule bora za watoto zilizokuwa hapo New York.

“Kuna hii St. Monica! Ni shule ya watoto ambayo ninaamini ni bora kabisa. Watoto wengi wanaosoma hapo ni wa matajiri na viongozi wa serikali, ni shule inayotoa elimu bora kabisa,” alisema James, kijana ambaye alimwambia afuatilie masuala yote ya shule.

“Kama ni nzuri! Basi acha wakaanze hapo.”
St. Monica haikuwa mbali na mahali alipokuwa akiishi, ilikuwa ni mwendo wa dakika kumi kwa gari. Kila siku James ambaye alikuwa na dereva wake alikuwa na kazi ya kuwapeleka watoto hao shuleni na kwenda kuwachukua mchana.

Siku ya kwanza kuingia shuleni, watoto wengi walikuwa wakiwashangaa, hakukuwa na mtoto mweusi hata mmoja shuleni hapo, wao ndiyo walikuwa watoto weusi wa kwanza kusoma ndani ya shule hiyo.

Watu wengi walikuwa wakijiuliza kuhusu Godwin na Irene, walionekana kuwa watoto wachangamfu ambao kila mmoja alitamani kuzungumza nao. Darasani, hawakuwa wazungumzaji, kila mmoja alikuwa kimya huku wakionekana kutaka kuyazoea mazingira ya shuleni hapo.

Wazazi waliokuwa wakifika shuleni hapo na kuwaona watoto hao, walishangaa, waliwauliza walimu kuhusu watoto hao, ilikuwaje kuanza masomo katika shule hiyo na wakati walikuwa watoto weusi.
“Ni watoto wa balozi!” alijibu mwalimu mmoja.

“Balozi wa nchi gani?”
“Tanzania!”
“Afrika?”
“Ndiyo!”
Walitaka kufahamu mengi kuhusu watoto hao, waliwadharau kwa kuwa hawakuamini kama kungekuwa na mtu mweusi ambaye alikuwa na akili zaidi ya Mzungu.

Siku zikakatika, japokuwa Godwin na Irene walikuwa wageni shuleni hapo, waliyakuta masomo katikati lakini walionekana kuwa hatari sana katika masomo yote.
 
29

Walijua kusoma vizuri Kiingereza, waliweza vizuri sana somo la hesabu kiasi kwamba hata walimu wenyewe walishangaa na kubaki kujiuliza juu ya uwezo waliokuwa nao watoto hao.
“Haiwezekani! Mbona wana akili hivi?” aliuliza mwalimu Wilbert huku akionekana kushangaa.

“Hata mimi nashangaa! Wanaonekana ni hatari sana. Wana akili za kuzaliwa, haiwezekani kwa mwanafunzi kufahamu mambo kama haya, ni mapema mno lakini cha ajabu, wao wanafahamu sana,” alisema mwalimu mwingine huku uso wake ukiwa kwenye mshangao mkubwa.

Huyo ulikuwa mwezi wa kwanza, uwezo wao darasani uliendelea kujionyesha shuleni hapo na hata kipindi cha mitihani ya mwisho wa mwaka kilipofika, waliweza kushika nafasi ya kwanza kitu kilichowachanganya walimu wengi.

“Wamefaulu vizuri sana, zaidi ya wanafunzi wengine,” alisikika mwalimu mmoja, hakuamini kile alichokuwa akikiona.
“Wakina nani?”
“Wale watoto wa Kiafrika!”
“Godwin na Irene.”
“Hebu nione!”
Huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa mabadiliko, shuleni, walikuwa wanafunzi hatari, hata mwaka huo ulipokatika na mwingine kuingia, bado walikuwa moto wa kuotea mbali.

Wale waliokuwa wakiwadharau watu weusi, wakaacha dharau zao kwani watoto hao wawili walizisafisha akili zao na kugundua kwamba si Wazungu peke yao waliokuwa na akili kuliko watu weusi, hata watu weusi wenyewe walikuwa na akili kuliko hao Wazungu.

“Ninaamini kwamba mnaweza kufanya vizuri zaidi ya hapa. Watoto wote mnaosoma nao, hakuna mtoto mwenye akili zaidi yenu. Hebu waonyesheeni kile ambacho Mungu amekiweka vichwani mwenu,” alisema Bwana Mapoto huku akiwaangalia watoto wake.

“Ninataka kuwa mchungaji baba,” alisema Godwin huku akimwangalia baba yake, kila siku katika maisha yake, hakukuwa na kitu chochote alichokuwa akikihitaji kama kuwa mchungaji kama alivyokuwa Reinhard Bonnke ambaye kila siku alimuona kama ‘role model’ wake.

Wakati hayo yote yakiendelea nchini Marekani, nchini Tanzania hali ilikuwa imebadilika, kila mtu alionekana kukata tamaa ya maisha, hawakuamini kama kweli huo ndiyo ungekuwa mwisho wa Bwana Mapoto ambaye aliondoka na kuelekea nchini Marekani ambapo maisha yake yote yangeendelea kuwa huko.
 
SEHEMU YA 30

Watu waliompenda, walimchukia, mioyo yao iliyokuwa na upendo mkubwa juu yake ilibadilika na chuki nzito kuanza kuchipua kwani kwa kitendo cha kumkubalia Rais Bokasa kuwa balozi nchini Marekani kilimaanisha kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wake.

Chama cha Tanzania National Party na viongozi wake wakachanganyikiwa, waliona kabisa kwamba kama Bwana Mapoto angeendelea kuishi nchini Marekani basi uchaguzi wa mwaka 2003 wasingeweza kuchukua, hivyo ilikuwa ni lazima kumlaghai.

“Ni miaka mitano tu, niamini kwamba nitakaporudi nitakuwa na nguvu ileile,” alisema Bwana Mapoto wakati akizungumza kwenye simu na mwenyekiti wa chama chake, Bwana Edward.
“Hapana! Ni kipindi kirefu sana. Naomba ufanye kitu kimoja, andika barua ya kuacha kazi,” alisema Edward.

“Unahisi hilo litasaidia?”
“Ndiyo! Huku kila mtu anakuhitaji wewe, kitendo chako cha kwenda huko ni kujipoteza kisiasa, fanya juu chini, andika barua ya kuacha kazi na urudi huku Tanzania tuje tulisukume gurudumu hili na kuuchukua urais uchaguzi ujao,” alisema Edward.

“Hakuna shida. Nitafanya hivyo!”
Hilo ndilo walilokubaliana lakini kabla ya kufanya uamuzi wowote ule ilikuwa ni lazima kuwasiliana na mkewe na kushauriana kama lingekuwa jambo sahihi kufanya kama alivyoambiwa.

Akampigia simu na kuzungumza naye, alichoambiwa, mkewe naye akamuunga mkono kwamba alitakiwa kuacha kazi kwani kila mtu nchini Tanzania alikuwa akimlalamikia kwa kitendo alichokifanya, aliwasaliti, ili kuwafurahisha ilikuwa ni lazima kuachana na kazi ya ubalozi na kurudi nchini Tanzania.

“Naandika barua leo hiihii…” alisema Bwana Mapoto.
“Sawa.” Hakutaka kuchelewa, akawasha kompyuta yake ya mapajani, bila kupoteza muda akaanza kuandika barua hiyo kwa njia ya barua pepe kwa ajili ya kuituma kwa Rais Bokasa na kumwambia kwamba hakutaka tena kufanya kazi ya ubalozi nchini Marekani, alibadilisha maamuzi yake na kitu alichokuwa akikihitaji ni kurudi nchini Tanzania.
 
mh!!! Jaman sijasema nimekuwa nikimfukuza mwizi kimyaa kimya tu lakin hii c ban hii jaman hata kama cjui ni ban kumetokea nini jaman
 
Loh!!!!! kidogo tuandamane usirudie hako ka mchezo Shunie haunaga shida na mtu halafu mastori zako hazinaga alosto ndo nilikuwa nimeweka kikao cha dharura kwenye serikali ya kichwa changu jinsi ya kujipanga na maandamano
 
mh!!! Jaman sijasema nimekuwa nikimfukuza mwizi kimyaa kimya tu lakin hii c ban hii jaman hata kama cjui ni ban kumetokea nini jaman
Loh!!!!! kidogo tuandamane usirudie hako ka mchezo Shunie haunaga shida na mtu halafu mastori zako hazinaga alosto ndo nilikuwa nimeweka kikao cha dharura kwenye serikali ya kichwa changu jinsi ya kujipanga na maandamano
Asante sana mkuu kwa kujari ubarikiwe
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom