Tujikumbushe Bungeni mwaka 2006, kutokana na kauli yake aliyoitoa leo kwamba hausiki na RICHMOND.
"Kesho yake, yaani tarehe 1 Aprili 2006 Waziri wa Nishati na Madini, wakati huo Mhe. Dk. Ibrahim Msabaha, (Mb.) akionesha dhahiri kutotaka njia ya international shopping kutumika, akawaita wajumbe wote wa Bodi ya Wakurugenzi ya TANESCO na kuwaagiza wahakikishe kuwa Bodi ya Zabuni ya shirika inawaita tena wazabuni wote waliojitokeza awali na makampuni mengine yoyote yenye uwezo wa kuingiza nchini mitambo hiyo. Aidha, Mhe. Dk. Ibrahim Msabaha, (Mb.) alisisitiza kwa barua kwamba:
"Mshindi wa tenda ya ununuzi wa mitambo mipya atajulikana baada ya idhini ya Serikali kutolewa. Composition ya wajumbe wa TANESCO Tender Board ibadilishwe na kuimarishwa kwa kuwa na wajumbe wenye uwezo na ni pro-active".
Mheshimiwa Spika, ni dhahiri kuwa agizo hili la Waziri lilikuwa batili kwani Sheria ya Ununuzi wa Umma haimpi Waziri mamlaka ya kuingilia uteuzi wa Wajumbe wa Bodi za Zabuni za mashirika yaliyo chini ya Wizara yake. Agizo hilo la Waziri likafuatiwa na uamuzi wa Waziri Mkuu wa kuliondoa suala hilo mikononi mwa TANESCO na kulikabidhi kwa Kamati Maalum iliyokuwa inaundwa na Katibu Mkuu (Hazina), Katibu Mkuu (Nishati) na Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Tarehe 13 Aprili 2006, Mkurugenzi Mwendeshaji wa TANESCO wakati huo, Bw. Adriaan Van De Merwe, akaiondoa TANESCO rasmi kutoka kwenye mchakato huo kwa kumtumia Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini nyaraka zote kuhusu zabuni yenyewe na uchambuzi wote uliofanywa na TANESCO."