Nimeshitushwa na kauli za mara kwa mara za DPP wetu kuhusu ugumu wa kuishitaki kampuni ya KAGODA. Nimeshitushwa zaidi na matamshi yake yaliyonukuliwa na gazeti la Tanzania Daima la Jumapili, Aprili 12, 2009 kuwa: wamiliki wa KAGODA watafunguliwa mashitaka ikiwa itathibitika kuwa kampuni hiyo haikupewa kazi ya kukusanya madeni na kampuni za nje! Hivyo basi, DPP wetu sasa hivi anahangaika kuzitafuta kampuni hizo huko nje!
Kwa msimamo huo wa kichekesho, mimi najiuliza: DPP WETU NI KIHIYO WA SHERIA, MSANII AU MBABAISHAJI TU? Nashindwa kupata jibu sahihi, maana ushahidi wote wa kumfungulia mashtaka Rostam Aziz na washirika wake upo!!! Kazi aliyojipa DPP wetu si yake ni ya mawakili wa utetezi kuleta ushahidi kuwa KAGODA ilikuwa imetumwa na kampuni fulani ya nje ambayo itaitwa kutoa ushahidi! Anayoyafanya DPP wetu ni upuuzi na mchezo wa kitoto unaotia kichefuchefu, unaowageuza Watanzania wapumbavu wa mwisho duniani. Hivi, nauliza, wamiliki wa makampuni mengine wako mahakamani kutokana na kwamba DPP ana uthibitisho wa makampuni yote kutoka nje? Aliyemwambia DPP wetu kuwa ONUS OF PROOF katika kesi za jinai inamwangukia yeye, ni nani? Huyu kasoma kweli shule, mbabaishaji au msanii ambaye amewekwa hapo kuwahadaa Watanzania?
Katika kesi ya Herniman dhidi ya Smith ya mwaka 1938 ambayo iliamuliwa na Mahakama ya Juu ya Uingereza (House of Lords) na uamuzi wake ukapokewa baadaye na Mahakama Kuu ya Tanganyika kama mwongozo katika kesi ya Ali Mohamed Osman dhidi ya DC Hill, msimamo wa kisheria ni kwamba si wajibu wa upande wa mashtaka kuhakiki kila kipengele cha ushahidi kabla ya kuchukua hatua za kushitaki. Nanukuu:
"... It is not required of any prosecutor that he must have tested every possible relevant fact before he takers action. His duty is not to ascertain whether there is reasonable and probable cause for prosecution. ... there is no obligation to call on the cheat and ask for an explanation in as much as to ask for this may only have the effect of causing material evidence to disappear or to be manufactured ..."
Na kweli kabisa, anachofanya DPP ni kumruhusu Rostam kutengeneza ushahidi na makampuni ya nje! Kwa sisi wazee tuliokaa ndani ya taaluma ya sheria kwa zaidi ya miaka 50 sasa, tunachokiona ni KIOJA! Ili kumfikisha mtu mahakamani, DPP hahitaji kujiridhisha na ushahidi wote, anachohitaji ni ushahidi kiasi unaojenga "reasonable and probable cause to prosecute". Ushahidi wa aina hiyo, tayari DPP Elieza Feleshi anao!
Tanganyika Law Society mko wapi? Wanasheria wa Tanzania mko wapi kuiokoa taaluma yenu ambayo sasa inabakwa? Tofauti yenu na laymen iko wapi?