Kwa mujibu wa taarifa toka ITV, Deni la taifa laongezeka hadi kufikia shilingi trilioni sitini na moja nukta nane. Mwaka 2015 deni la taifa lilifikia Shilingi Trilioni 40
========
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti imebaini kuwa deni la taifa limekua kukua kutoka shilingi trilioni hamsini na tatu nukta tatu mwaka 2017 hadi shilingi trilioni sitini na moja nukta nane mwaka 2018 kutokana na mahitaji ya uwekezaji kwenye miradi ya maendeleo na kijamii nchini kwa ajili ya kukuza uchumi.
Akisoma taarifa ya utekelezaji wa majukumu kamati hiyo kwa kipindi cha Januari 2018/19 Mwenyekiti wa kamati Mhe. George Simbachawene amesema deni hilo linajumuisha fedha zilizokopwa na serikali kutoka vyanzo vya ndani na nje pamoja na sekta binafsi kutoka nje ya nchi kwa ajili ya kugharamia miradi ya maendeleo.
Akizungumza na ITV kuhusu taarifa ya uwekezaji wa mitaji ya umma ya Kamati ya Bunge ya Uwekezaji wa Umma, Mwenyekiti wa kamati hiyo Mheshimiwa Raphael Chegeni amesema baadhi ya tasisi na mashirika mengi ya umma yanayowekeza kibiashara hayana mpango mkakati, mpango wa kibiashara na sera ya uwekezaji na kusababisha kushindwa kujiendesha kwa tija.
Wakichangia taarifa ya Kamati za Bunge ya Bajeti na Kamati ya Bunge ya Uwekezaji wa Umma, baadhi ya wabunge wamesema hakuna nchi iliyoendelea kwa kutegemea wafadhili, hivyo wameitaka serikali kuongeza kodi kwa bidhaa zinazoingia nchni, ambazo zinaweza kutengenezwa hapa nchni,ili kuinua bidhaa za ndani.
Chanzo: ITV