Uchaguzi Biharamulo
* Mwenyekiti CHADEMA akatwa mapanga
* Pikipiki yachomwa moto
Na Suleiman Abeid, Kagera[/B]
IKIWA zimesalia siku mbili kufanyika kwa uchaguzi mdogo katika jimbo la Biharamulo Magharibi mkoani Kagera, damu imemwagika baada ya Mwenyekiti wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Wilaya ya Chato, Bw. Stephen Nyororo (59) kujeruhiwa kwa kukatwa mapanga na pikipiki moja kuteketezwa kwa moto.
Tukio hilo lilitokea juzi saa 10 jioni katika kijiji cha Kagoma kata ya Runazi wilayani Biharamulo baada ya mwenyekiti huyo na wafuasi wengine wawili wa CHADEMA kushambuliwa kwa kipigo na kukatwa mapanga na watu wanaohisiwa kuwa ni wafuasi wa Chama cha Mapinduzi (CCM).
Akizungumza na waandishi wa habari katika wodi namba tatu ya Hospitali Teule ya Wilaya ya Biharamulo, Bw. Nyororo, alisema alifikwa na mkasa huo baada ya vijana wapatao 15 kuwavamia walipokuwa wamekaa chini ya mti wakiongea katika kijiji cha Kagoma.
"Kwa kweli sielewi kwa nini tulishambuliwa, siku hiyo sisi tulikuwa tumekaa chini ya mti na wenzangu wawili tukiongea pale katika kijiji cha Kagoma, ghafla lilipita gari la watu wa CCM akiwemo mwenyekiti wa Taifa wa UWT, Bi. Sophia Simba, alitusalimu kwa ishara yao ya kuweka dole gumba, na sisi tulimnyooshea kumjibu,"
"Lakini baada kama ya dakika kumi hivi lilikuja gari aina ya Land cruiser lenye maandishi ya Serengeti ubavuni, wakateremka vijana watatu na kumwita kijana mmoja tuliyekuwa tumekaa naye, kijana alikataa, ndipo walipoamua kumfuata huku wakihoji kwa nini amekataa kwenda alipoitwa ghafla walianza kumshambulia," alieleza Bw. Nyororo.
Alisema baadaye waliteremka vijana wengine kutoka ndani ya gari hilo huku wakiwa na mapanga waliowafuata na kuanza kuwashambulia kwa fimbo huku wakiwakata mapanga hali ambayo ilisababisha wenzake wawili aliowataja kwa jina moja moja la Bw. Juma na Bw. Goosayi wakimbie.
Bw. Nyororo aliendelea kueleza kuwa baada ya wenzake kukimbia kundi la vijana hao walimfuata yeye alipokuwa amesimama na wakaanza kumshambulia kwa kumkata mapanga sehemu za kichwani na mikononi na kusababisha kujeruhiwa vibaya kiganja chake cha mkono wa kushoto.
"Hii mikono nilikatwa wakati nakinga ili panga lisinikate shingoni ndipo likakata kiganja cha mkono wa kushoto huku wakinipiga fimbo hali iliyosababisha nianguke chini na mmoja wa wale vijana alichukua chupa aliyokuwa nayo na kunipulizia dawa usoni ambayo ilikuwa kali na nikashindwa kuona," alidai Bw. Nyororo.
Alisema baada ya kuona hali hiyo alisimama kwa tabu na kuanza kukimbia ambapo alikimbilia katika ofisi ya mtendaji wa kijiji lakini hata hivyo Ofisa mtendaji aliyekuwa nje ya ofisi yake alimfukuza akimueleza kuwa aondoke eneo hilo kwa vile anaweza kumsababishia vurugu.
Bw.Nyororo ambaye ni Meneja Kampeni wa Mgombea Ubunge katika jimbo la Biharamulo magharibi kwa tiketi ya CHADEMA katika kata ya Nyamigogo, alisema baadae alikimbilia shuleni ambako aliokolewa na mwalimu wa shule hiyo aliyemtaja kwa jina la moja la Mwalimu George.
Alisema baadaye walipiga simu kuomba msaada wa Polisi pamoja na kuwaarifu viongozi wa CHADEMA waliokuwa katika mkutano wa kampeni eneo Runazi ambapo walikwenda katika kituo cha Polisi alikopewa fomu namba tatu na kupelekwa Hospitali Teule ya Wilaya kwa ajili ya kupatiwa matibabu.
Hata hivyo, alisema mbali ya wao kushambuliwa pia vijana hao waliharibu pikipiki moja waliyokuwa wakiitumia kufanyia kampeni ambayo ilichomwa moto na kuteketea kabisa.
Kwa upande wake Kamanda wa Operesheni Uchaguzi Jimbo la Biharamulo Magharibi, Bw. Telesphory Anaclet alikiri kutokea kwa tukio hilo na kwamba tayari Polisi ilikuwa ikiwasaka watu waliohusika.
"Ni kweli tukio hilo limetokea ambapo watu watatu wamejeruhiwa ...tumepeleka vijana wetu wanaoshirikiana na wananchi kuwasaka wahusika pamoja na gari lao lenye namba T.895 ANC ili tuweze kuwakamata," alieleza Kamanda Anaclet.
Kamanda Anaclet alisema gari linalodaiwa kutumiwa na watuhumiwa hao lilikuwa aina ya Toyota Land cruiser lenye rangi nyeupe na nembo ya wanyama na maandishi ya Seregenti ambalo linadaiwa kutoroka mara tu baada ya tukio hilo na kwamba pikipiki moja iliteketezwa kwa kuchomwa moto.
Source: Majira