Kwa kifupi kinachoendelea sasa bungeni ni mnyukano kati ya watetea haki kwa upande mmoja na watetea uovu kwa upande mwingine, kati ya watetea maslahi ya wananchi na watetea maslahi ya wateule wachache ndani ya sisiemu (na serikali), kati ya wawakilishi wa wananchi na wawakilishi wa chama tawala (na serikali yake).
Ni mnyukano kati ya wabunge wachache wanaojua shida za wananchi wanaowawakilisha bungeni na wengi ambao wameziba masikio (kwa kujua au kutokujua) na kugeuka kuwa watetezi wa serikali, kati ya 'wachumia tumbo' hata kama wanajiita first class economist na wachumi wa kweli, kati ya wale wanaona rasilimali za nchi na namna zinavyoweza kutumika kama vitega uchumi na 'vibaka uchumi'.
Ni mnyukano kati ya utandawazi na 'mtandaowizi', kati ya uhuru wa kuzungumza na 'uhuni' wa kuzungumza, kati ya wasomi wachache na watu waliowahi kwenda kupasha joto madawati shuleni. Ni mnyukano kati ya nuru na giza, kati ya chumvi na kitu kingine chenye ladha chungu.
Naam, yote haya yapaswa yatokee ili watanzania wajue ya kuwa kile chama walichokiamini (au kuaminishwa) kuwa ni chama cha wakulima na wafanyakazi sasa ni chama cha mafisadi, wahamisha twiga na wauza pembe za ndovu. Chama ambacho tuliambiwa kuwa kinaamini kwamba binadamu wote ni sawa sasa kimebadilika na kuwa 'binadamu wote si sawa' maana kuna wanasisiemu na wapinzani, kuna wanamtwara na wanabagamoyo. Chama kilichosema rushwa ni adui wa haki, sitatoa wala kupokea rushwa, sasa kinasema wagombea wake wote wanatoa rushwa kwenye chaguzi. Ile ahadi ya kuwa nitajielimisha kwa kadri ya uwezo wangu na kutumia elimu yangu kwa faida ya wote, sasa elimu inatumika kwa 'faida' ya chama kwanza.
Hii ni sauti inayopazwa kwa mwito na mshindo mkuu kwa baba, mama, kaka, dada na wadogo zangu kule Namiyonga (Newala), Lumuma (Mpwapwa), Kinalilya (Iramba), Makere (Kasulu), Lubafu (Bukoba), Kabanga (Nzega) au Nkwarungo (Hai) na vijijini kote katika nchi hii, msidanganyike tena kwa pombe, tshirt, kanga au chumvi na kuuza haki zenu za msingi kwa makuwadi wa mafisadi.
Nionapo yote haya, najua kwa hakika mwisho wa mambo yote umekaribia. Naam, hata huo mwisho hauko mbali sana maana naoina Tz mpya yenye tumaini jipya. Naona anguko kuu la sisiemu, naye ajidhaniye amesimama aangalie asije akaanguka. Asomaye na afahamu!!!!!