RIWAYA; BOMU
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU 0652212391
Sehemu ya Ishirini na Tatu
Wakati huohuo teksi iliyompakia Martin Hisia ilikuwa maeneo ya Buguruni. Pamoja na dereva teksi kujaribu kukimbiza kwa kasi kila apatapo nafasi, lakini foleni ya haja ilizizima mbio zake mara kwa mara.
Pindi walipokuwa katika foleni hapo Buguruni ndipo simu ya Martin Hisia ilipoingia meseji. Martin aliitoa simu yake mfukoni ili kuiangalia hiyo meseji. Ulikuwa ni ujumbe uliongia kwa njia ya mtandao wa Whatsapp. Martin alifungua whatsapp yake. Akaona ni ujumbe uliongia kutoka kwa mpenzi wake, Felisia. Lakini uliingia kwa mtindo wa 'voice note'. Martin alitoa 'earphone' kutoka katika mfuko wake mwengine wa suruali. Akazichomeka katika simu yake.
Akaanza kusikiliza.
Wakati huohuo kule katika nyumba ya kulala wageni ya Platnumz. Felisia aliomba kwenda kujisaidia chooni nakutoka mle chumbani ambapo walikuwepo wakina Imma Ogbo. Alinyanyuka bila kuomba ruhusa. Alitoka nje ya mlango wa chumba walichofikia. Akakata kushoto akiifuata korido ndefu ambapo ndipo kulikuwa na choo. Mara kwa mara alikuwa anageuka nyuma ili kuona kama kuna hatari yoyote ile ilikuwa inamfuata. Hakuiona hatari, wala harufu ya hatari. Aliingia moja kwa moja bafuni. Akafungulia bomba la maji, akiruhusu maji kutoa sauti wakati yakiingia katika ndoo ya chuma. Sekunde ileile alitoa simu yake mfukoni na kumpigia Martin Hisia. Alisikiliza kidogo, kwa bahati mbaya alikuta simu ya Martin Hisia ilikuwa inatumika. Martin Hisia alikuwa anaongea na simu nyingine.
Hofu dhahiri ilishamiri katika moyo wa Felisia. Aliujua uhatari uliopo kwa kitendo alichokuwa anakifanya. Alifahamu vizuri sana adhabu atakayopewa na Imma Ogbo pindi atakapogundua kwamba alikuwa anamsaliti. Lakini hakuwa na namna, kuungana na Imma Ogbo safari hii ilikuwa ni kuisaliti nchi yake Tanzania. Na yeye hakuwa tayari kwa hilo.
Akiwa anatetemeka kwa woga Felisia alipiga tena simu ya Martin Hisia. Lakini bado majibu yalikuwa yaleyale. Simu aliyokuwa anaipigia ilikuwa inatumika.
Hii ilimpa mawazo mengi sana Felisia. Maana hakujua kwamba Martin aliusikiliza ujumbe wake aliomtumia ama lah. Alitamani Martin apokee simu yake hata sekunde moja na kumjulisha kwamba aliusoma ujumbe wake.
Angejisikia amani..
Alipiga tena simu kwa mara ya tatu.
"Come on Martin pokea simu" Felisia alisema kwa sauti ndogo. Lakini majibu ya simu yalikuwa yaleyale, bado ilikuwa inatumika.
"Hapa sina jinsi. Yanipasa nitoke tu nje. Maana jamaa wasije wakanitilia shaka kwakuwa nimechelewa sana kutoka chooni" Felisia aliwaza. Akafunga lile bomba la maji na kuelekea mlangoni. Alipofika mlangoni na kufungua tu ule mlango, alikutana na jambo la kushtusha sana!!
Felisia alikuwa anatazamana na mdomo wa bastola nyeusi iliyoshikwa imara na mkono wa nguvu wa Immanuel Igbo!!
Kimbembe....
Wakati Felisia akitazamana na mdomo wa bastola, mpenzi wake, Martin Hisia alikuwa anaongea kwenye simu na Daniel Mwaseba. Alikuwa ameshamtumia ule ujumbe uliotoka kwa Felisia. Na Daniel aliituma ule ujjumbe pamoja na namba ya Felisia kwa Mwanasheria mlevi. Ndipo walipoweza kufanikiwa kupafahamu mahali alipo mtumaji wa ujumbe ule. Sasa safari yao ilibadilika, kwa kasi walikuwa wanaelekea Vikindu mahali ambapo waligundua kwamba ndipo alipokuwa Dr Luis.
"Kazi imekuwa rahisi sana. Sikutegemea kwamba tutampata Dr Luis kirahisi namna hii" Adrian alisema.
"Adrian, usiseme kazi ni rahisi. Hatujui Dr Luis yupo katika mazingira gani? Na hatujui tunaenda kupambana na watu wa aina gani? Hapa lazima tujipange kamili ili kuhakikisha tunampata Dr Luis" David alisema.
"Lakini jamani kuna mambo ya kushangaza kidogo juu ya hizi sauti alizotutumia Martin Hisia. Inaonesha kwamba Dr Luis hajatekwa, yupo na watu anaowafahamu kabisa huku naye akishiriki katika mpango wao wa kuulipua ubalozi wa Uganda. Hii ipo vipi?" Daniel aliuliza.
"Hata mimi nimekuwa nikijiuliza swali hilo kichwani mwangu. Lakini hatuna haja ya kuumiza kichwa. Dakika chache zijazo Tunaenda kukutana na hawa watu, na tutajua tu mbivu na mbichi" Adrian alisema.
"Hili swala limekuwa kubwa sana. Uhusika wa rais Abayo katika sakata hili ndo limezidi kulifanya kuwa kubwa. Lakini niahidi tu tutazifukia hila zote za watu hawa na kuziweka hadharani. Tutampata Dr Luis na kumfikisha kwa mheshimiwa rais, na lazima tuziseme hila zake. Pia lazima tuhakikishe ubalozi wa Uganda haulipuliwi abadaan, sambamba na kuwatia mikononi hao majasusi watano wanaokuja kutoka nchini Nigeria.
Pamoja na hayo lazima tuhakikishe tunamkomboa Hannan na familia ya David. Hizo ndio kazi zetu kuu, na nina hakika tutazikamilisha" Daniel alisema kipindi hiko gari yao ilikuwa Kongowe.
Walikuwa wameshapoteana na gari ya kina Mark ambao nao walihisi wanawakimbia wakina Daniel. Kumbe haikuwa hivyo, wakina Daniel walikuwa wamepata misheni ndani ya misheni.
Kwa mwendo wa gari la kina Daniel, Dakika saba tu ziliwafikisha Madafu kutokea Kongowe. Walipofika Madafu walimpigia simu Mwanasheria mlevi ili awape mwelekeo sahihi waliopo wakina Dr Luis.
"Mwanasheria, tupe mwelekeo, tupo Madafu hapa" Daniel alisema.
"Sasa Daniel ninavyoona hapa katika mtandao, hapo Madafu upande wenu wa kulia kuna kituo cha mafuta. Mita chache kutoka kituo cha mafuta upande huohuo wa kulia kuna nyumba ya kulala wageni. Hapo ndipo hiyo simu ilituma ile meseji" Mwanasheria alisema.
"Sawa Mwanasheria nd'o tupo katika kituo cha mafuta hapa, tunaelekea hilo eneo. Vipi hiyo namba iliwasiliana tena na mtu mwengine?" Daniel aliuliza.
"Hapana Daniel. Nimekuwa nikiichunguza namba hii muda wote. Ilijaribu kuwasiliana na namba moja ambayo nayo ilikuwa inaongea wakati akiipigia. Nilijaribu kuichunguza namba hiyo ikiyopigiwa nikagundua imesajiliwa kwa jina la Martin Hisia. Nikachunguza tena huyo Martin Hisia alikuwa anaongea na nani kwa muda huo? Nikagundua anawasiliana na simu iliyosajiliwa kwa majina ya Adrian Kaanan, hivyo nikagundua alikuwa anawasiliana nanyi" Mwanasheria mlevi alisema.
"Pengine huyo mtu alikuwa anataka kumpa taarifa nyingine Martin" Daniel alisema.
"Inawezekana. Maana alijaribu kupiga simu zaidi ya mara mbili"
"Sawa Mwanasheria. Sisi tunaingia kazini. Nitakupigia baada ya kutoka hapa. Tuna kazi kubwa sana kesho asubuhi kama ulivyosikia katika hizo records. Nitakuhitaji ili kuikamilisha hiyo kazi" Daniel alisema.
"Nipo tayari saa yoyote, sehemu yoyote. Mimi ni Mwanasheria..."
"Mwanasheria mlevi" Daniel alimalizia.
Na simu ikakatwa.
Daniel alimwangalia Adrian, kisha akamwangalia David.
"Wanaume, sasa tunaenda kuvamia hii nyumba ya kulala wageni ambayo tuna uhakika yupo mtu anayeitwa Imma Ogbo. Pengine hamumjui vizuri Imma Ogbo. Mimi nimemjua Imma Ogbo kupitia Mwanasheria pindi nilipomtumia zile record alizoturushia Martin Hisia. Katika record zile kuna sauti tatu, ya Dr Luis, mwanamke ambaye ndiye amevujisha siri hii na mwengine ni sauti ya Imma Ogbo. Sisi shabaha yetu ni Dr Luis, lakini tujue kwamba Dr Luis yupo sambamba na kiumbe hatari kinachoitwa Imma Ogbo.
Imma Ogbo ni nani?
Imma Ogbo ni jasusi namba mbili kutoka nchini Nigeria. Licha ya ujasusi Imma ni mlinzi namba mbili wa rais wa Nigeria, rais Abayo. Kupambana na jasusi namba mbili wa nchi kama Nigeria, nchi yenye maelfu ya majasusi na yeye kupewa namba mbili si jambo la kitoto. Kwa Afrika Imma Ogbo anashika namba sita. Mmeona uhatari wa huyu jamaa? Lazima tuwe makini sana ndugu zangu. Ukimwona Imma Ogbo cha kwanza mpige risasi ya kichwa kisha ndo umuhoji!! Nataka leo ndio uwe mwisho wa hila za hawa manyang'au!!!." Daniel alisema huku akiwaangalia wenzie kwa zamu.
Wote waliitikia. Sura zao zikionesha walikuwa na hamu kubwa ya kuingia katika mapambano haya magumu na ya hatari.
"Haya sasa...Twendeni tukaivamie hiyo nyumba ya kulala wageni. Iwe iweje..lazima tuhakikishe tunawatia mkononi Dr Luis na Imma Ogbo!!" Daniel alisema.
Wote watatu, walishuka kwenye gari, wakiwa tayaritayari, na kwa kutumia miguu yao walielekea katika nyumba ya kulala wageni ya Platnumz kuwatia mbaroni watu ambao waliwapachika jina la Manyang'au...
Je wataweza kuwatia mikononi wakina Imma Ogbo? Hili ni swali..wewe nipe jibu