Isingekuwa sawa kwangu kuingia humu na kupita bila ya kuzungumzia habari kubwa iliyopo sasa juu ya ujio wa bonge moja la video la muziki wa Bongo Flava ambayo sio ya waimba muziki wa Naija. Na baada ya kusoma maoni ya baadhi ya watu, nimeona niseme jambo hili kidogo kabla sijaondoka humu.
Binafsi, nahisi sehemu kubwa ya jamii ya Kitanzania haina uelewa wa kutosha kuhusu video za muziki, hudhani ni kuweka tu matukio hata kama hayana maana, wala hayaungani na matukio mengine. Huamini kuwa, ubora wa video ni kuonesha magari ya kifahari na nyumba za kitajiri.
Kama si miongoni mwa watu niliowaeleza hapo juu, hutasita kutoa pongezi kwa video ya Chekecha Cheketua Kiba iliyochezwa kwa mara ya kwanza na kituo cha kimataifa cha runinga cha Trace Urbun, tena kwa namna inayoupa heshima muziki wetu na lugha yetu (swahili).
Kwa heshima zote nakubaliana na video ya Chekecha Cheketua, sio kwa ushabiki au kufuata mkumbo, bali kutokana na malengo ya video kukamilishwa vizuri na timu iliyoitayarisha video hiyo. Umakini wa props, maleba na mapambo ulikuwa ni mkubwa sana kiukweli.
Angalia magari yaliyotumika, angalia redio zilizomo humu ndani. Na sio ajabu Kituo kikubwa kama Trace Urbun kuamua kuipiga kama exclusive, na kupiga mara saba (7) ndani ya saa kumi na mbili (12) za siku moja, ambayo kwa hesabu za haraka, waliipiga kila baada ya saa moja na nusu.
Tueleweshane Kidogo!
Kwa wale waliobahatika kupata nafasi ya kuelimika, naamini watakuwa wakifahamu kuwa muziki ni
fasihi. Na maana ya Fasihi ni utanzu (tawi) wa sanaa ambao hutumia lugha ya mazungumzo/vitendo au maandishi ili kufikisha (kuwasilisha) ujumbe fulani kwa hadhira husika.
Katika kazi yoyote ya fasihi lazima pawepo na ustadi wenye kuleta mvuto fulani kwa hadhira (wasikilizaji/watazamaji au wasomaji) husika. Na ustadi (ufundi) huo unaovutia hadhira ndio huitwa FANI, ambayo hujumuisha mambo kama vile:
- Muundo (mtitiriko/msuko/mpangilio wa matukio/visa)
- Mtindo (mbinu inayotumiwa na fanani ili atofautiane na fanani mwingine)
- Wahusika (watu au vitu ambavyo hutumiwa na fanani katika kazi yake)
- Mandhari (eneo ambalo fanani hulitumia katika kuumba kazi yake)
Vilevile kazi yoyote ya fasihi huwa na
ujumbe na malengo mbalimbali ambayo hukusudiwa yaifikie jamii husika. Yale yote ambayo msanii wa kazi ya fasihi anakusudia yaifikie jamii husika, ndio huitwa
Maudhui (content). Maudhui ya kazi ya fasihi hujumuisha:
- Dhamira
- Ujumbe
- Migogoro
- Falsafa/misimamo
- Mtazamo
Kazi ya fasihi ni kujaribu kusawiri vipengele vya maisha, mahusiano, na hisia za watu katika jamii husika, ambayo huwasilishwa kwa njia ya masimulizi ya mdomo au vitendo. Na
kuna aina kuu mbili za fasihi ambazo ni Fasihi Simulizi na Fasihi Andishi.
Kisa cha kwenye video ya Chekecha!
Nampongeza mwandishi wa script, muongozaji na wawasilishaji kwa maana ya washiriki wote tuliowaona kwenye video hii. Tukirudi kwenye fasihi, maana
(DHAMIRA) ya video hii kuelezea kwa vitendo
'NGUVU YA SANAA YA MUZIKI KWA JAMII'.
Kisa kiko hivi, Kiba anafika kwenye mji usio na maendeleo makubwa na wakazi wake hawako huru kufanya majukumu yao (kutengeneza gari/mke na mume kufunguliana milango ya gari), kufanya wapendacho (kushiriki michezo kama karata/gofu, kusikiliza redio) na kunyimwa haki ya kuzungumza, kwani wako kwenye amri ya kuganda
(MIGOGORO).
Na kwa kawaida amri hutolewa na utawala. Kiba anashangazwa sana na hali hiyo, hivyo kuonesha kuwa ndio kwanza anakutana nayo kwa mara ya kwanza. Moja kwa moja anaamua kuwakomboa kwa kutumia silaha ya muziki (sauti ya kumtoa nyoka pangoni), anawaimbia na wote kuwatoa kifungoni.
Hapa ana lengo la kutueleza
(UJUMBE) muziki unavyoweza kutumika kutatua migogoro (vita/uonevu) mikubwa ya kiutawala na kufanya dunia kuwa huru. Hatimaye kwa kutwa moja tu, mji ulioonekana kutokuwa na watu (mpweke) ukaonekana kujaa watu wakicheza na kushangilia huku wengine wakibaki kuwa mashabiki.
Kuna kitu cha kupongezwa sana nimekiona kwenye video hii, ambacho ni kukwepa kuonesha tabia za Kimagharibi, kama mavazi, uchezaji wa mitindo ya kuhamasisha ngono, na badala yake kuonesha Uafrica wetu
(FALSAFA/MISIMAMO) na taratibu zetu.
Namsifu sana muongozaji wa video hii Meji Alabi kwa kuifanya video isiwe kwenye muonekano wa video za muziki wa Nigeria, na kufanikiwa kuilinda Bongo Flava na zaidi dansa wa Kitanzania, Kellz Mbowe kuwa ndiye dansa aliyeonekana zaidi (ndiye yule aliyefungua boneti ya gari).
Ukirejea maelezo haya utagundua kwamba, kilichofanyika kwenye video ya Chekecha Cheketua kilifuata misingi ya Fasihi kwa umahiri mkubwa, kuanzia Muundo, Mtindo, Wahusika na Mandhari.
Ova