BARD AI
JF-Expert Member
- Jul 24, 2018
- 3,376
- 8,120
Katika ajali hiyo wamo mume na mke waliopeza maisha, mama na mwanaye na nyumba moja ambayo imepoteza watu wanne wakiwemo baba na watoto wake wawili pamoja na mjukuu huku wengine wakiwa ni ndugu wa familia hiyo ya Mrema.
Ajali hiyo ilitokea eneo la Magira Gereza, Kata ya Magira Gereza, wilayani Korogwe, barabara ya Segera - Buiko na kusababisha vifo hivyo pamoja na majeruhi 12 wakati wakisindikiza mwili wa ndugu yao, Athanas Mrema (59) aliyefariki dunia Februari Mosi, kutokea jijini Dar es salaam kuja mkoani Kilimanjaro ndipo walipokutana na ajali hiyo.
Hata hivyo, miili hiyo ya watu 14 inatarajiwa kupokewa kesho Jumapili wilayani Rombo na itahifadhiwa katika Hospitali ya Huruma na Kituo cha afya Karume kwa ajili ya taratibu za mazishi ambayo yatafanyika Jumatatu katika Kitongoji cha Kirungu Mokala, Kata ya Kelamfua Mokala, wilayani humo.
Mmoja wa ndugu wa familia hiyo, Colman Mrema amesema tukio hilo la vifo vya watu 13 ni pengo kubwa kwa familia na halitazibika na kwamba limewaachia majeraha makubwa kwani siyo tukio la kwanza kutokea.
Wakati akizungumza na Mwananchi Digital, idadi ya vifo ilikuwa 13 lakini baadaye jioni ya leo, majeruhi ambaye ni mtoto aliyekuwa amelazwa chumba cha ungalizi maalum (ICU) naye alifariki dunia.
Amesema miaka 10 iliyopita familia hiyo hiyo ya Mrema ilipoteza watu wengine wanne katika ajali eneo la Makanya wilayani Same.
Amesema tukio hilo limeleta sehemu kubwa ya umaskini katika ukoo wao kwani wengi wao waliofariki katika ajali hiyo ni wafanyabiashara na wasomi ambao walikuwa wakitegemewa katika ukoo huo wa Mrema.
"Hili tukio haliwezi kuelezeka ni la kutisha na limeleta sehemu kubwa sana ya umaskini katika familia na ukoo wetu, hili ni pengo ambalo kamwe haliwezi kuzibika kwani ndani yake kuna wasomi, wafanyabaishara, ni tukio lisilo la kawaida," amesema.
Selina Silayo, mmoja wa majirani na familia hiyo amesema tukio hilo ni la kihstoria na kwamba katika mazingira ya kawaida ya kibinadamu ni ngumu kuipokea hali hiyo.
"Hili tukio limetuumiza sana kwa kweli maana leo tumekuja hapa kuzika lakini tumekutana na taarifa nyingine, Mungu aitie familia hii nguvu kuupokea huu msiba maana siyo mwepesi," amesema.
MWANANCHI