Ziara ya Rais Kikwete Hazina na 'Long Room' (leo)

Maxence Melo

JF Founder
Feb 10, 2006
4,230
13,415
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete leo, Jumanne, Machi 15, 2011, ametembelea Wizara ya Fedha (Hazina), ikiwa ni mwanzo wa ziara za kutembelea Wizara mbalimbali kujionea utendaji wa Serikali, kuangalia utekelezaji wa maagizo ya Serikali na yale aliyoyatoa alipotembelea wizara zote mwanzoni mwa mwaka 2006, mwezi mmoja tu baada ya kuwa ameingia madarakani.

Aidha, Rais baada ya kuwa ametembelea Wizara ya Fedha ametembelea Kitengo cha Long Room cha Mamlaka ya Kodi Tanzania (TRA).

Katika mazungumzo na viongozi wa Wizara na taasisi zote zilizoko chini ya Wizara hiyo, Rais Kikwete ameelezea majukumu matatu makuu ya Wizara hiyo kama ifuatavyo:

(a) Kusimamia Kukua kwa Uchumi

Rais Kikwete amesema kuwa wajibu kipaumbele katika miaka mitano ijayo iwe ni kwa Wizara ya Fedha kusimamia na kutafuta njia za kuleta utulivu zaidi katika uchumi kwa kubuni mikakati bora zaidi ya kuhakikisha uchumi wa Tanzania unakua kwa kasi zaidi na hivyo kupunguza umasikini kwa haraka zaidi. Hivyo, Rais amesema kuwa hata Bajeti ya Serikali ni lazima ilenge katika sekta zitakazoharakisha zaidi kasi ya kukua kwa uchumi.

Sambamba na agizo hilo, Rais Kikwete pia ameielekeza Wizara ya Fedha kutafuta njia za haraka na bora zaidi za kupunguza mfumuko wa bei ili kuwapatia wananchi unafuu zaidi wa maisha.


(b) Ukusanyaji Mapato ya Serikali

Rais Kikwete amesisitiza kuwa Hazina ndiyo moyo na roho ya Serikali na kwamba Wizara hiyo isipofanya kazi ya kukusanya mapato ni dhahiri shughuli za Serikali zitaathirika.

Rais amewasifu watumishi wa Wizara ya Fedha kwa kufanya vizuri katika ukusanyaji wa mapato ya Serikali lakini akawataka waongeze juhudi zaidi na wafanye vizuri zaidi. Ameambiwa kuwa mapato ya Serikali yameongezeka kutoka makusanyo ya kiasi cha shilingi bilioni 215 kwa mwezi mwaka 2005 wakati Rais kikwete anaingia maradakani hadi kufikia wastani wa shilingi bilioni 420 kwa mwezi kwa sasa.

(C) Kusimamia Matumizi ya Fedha ya Serikali

Rais Kikwete amesema kuwa jukumu la tatu la msingi la Wizara hiyo ni kusimamia matumizi ya fedha zinazokusanywa akiwakumbusha viongozi hao kuwa fedha za Serikali siyo shamba la bibi na wala makusanyo hayo ya kodi siyo sawa na ubani wa kilioni.

Amesema kuwa fedha za Serikali baada ya kukusanywa ni lazima zitumike vizuri na kwa shabaha zilizokukusudiwa na akaelezea ni sababu hiyo iliyopelekea Serikali kuchukua hatua za kuimarisha usimamizi wa matumizi ikiwa ni pamoja na kuunda nafasi ya Naibu Mhasibu Mkuu wa Serikali kwa ajili ya kusimamia fedha zinazopelekwa kwenye Halmashauri mbalimbali nchini na pia kuanzisha nafasi ya Mkaguzi Mkuu wa Serikali.

(D) Maagizo Mengine Makubwa

(i) Rais Kikwete amesema kuwa moja ya maeneo ambayo bado yana matatizo katika Wizara hiyo ni shughuli ya Manunuzi na ameitaka Wizara ya Fedha kuhakikisha kuwa wanaajiriwa watu wenye ujuzi na elimu ya masuala ya ununuzi lakini ambao pia ni waaminifu.

(ii) Rais Kikwete pia ameitaka Wizara hiyo kukabiliana na tatizo la kucheleweshwa kulipwa kwa mishahara mipya hasa ile ya watumishi wapya katika Serikali. Aidha, amerudia maelekezo yake kuwa Halmashauri nchini haziwezi kuruhusiwa kuhamishahamisha watumishi bila na kuwa na fedha za kulipia uhamisho huo.

(iii) Kuhusu malipo ya mishahara na marupurupu mengine ya watumishi, Rais Kikwete ametaka umakini mkubwa katika kuhakikisha kuwa haki za watumishi zinalindwa na watu hao kulipwa malipo yao ya haki na kwa wakati.

(iv) Kuhusu malipo ya wasataafu wa iliyokuwa Jumuia ya Afrika Mashariki iliyovunjika, Rais Kikwete ametaka wote wanaostahili kulipwa mafao yao na hawajalipwa hadi sasa walipwe, hata kama ni kweli kuwa wengi wa watumishi hao tayari wamelipwa.

(v) Kuhusu mikopo kwa watumishi wa Serikali, Rais Kikwete amesema amefurahishwa na kwamba Wizara ya Fedha inakamilisha taratibu za kuwakopesha watumishi hao, kama wanavyokopeshwa Wabunge. Aidha, ameongeza kuwa Wizara iangalie uwezekano wa hata kuwadhamini watumishi hao ili waweze kukopa moja kwa moja kwenye taasisi za fedha nchini.

(vi) Kuhusu Deni la Taifa, Rais Kikwete amesema kuwa ni jambo la heri sana kuwa Tanzania sasa inakopesheka tena, lakini lazima Wizara ya Fedha itumie uangalifu mkubwa katika kukopa ili Tanzania ijikute inarudi tena katika mazingira yaliyopelekea kuachwa kukopeshwa huko nyuma.


Imetolewa na:

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais
,
Ikulu,
DAR ES SALAAM
.

15 Machi, 2011
 
Ziara hizi ni za kujaza foleni tu mjini na kujionyesha kwamba " i am the president". Hazina manufaa yoyote, aliishazifanya sana huko bandarini, magereza, hazina , ujenzi nk.

Lakini nenda kaangalie usumbufu wa kutoa mizigo bandarini, wafungwa wamejazana magereza miaka kibao bila kesi kusikilizwa, Airport inavyoharibika, mishahara bado inachelewa na kuibiwa, ziara hizi zina manufaa gani?

Huyo Pinda ndiyo kabisaaa..anazunguka mikoani hamna hata tatizo moja analotatua.

Mkuu Max ikulu wakikupa tena press release kama hizi zitie kwenye shreddler.....
 
Mkapa alimkabidhi hazina iliyoshiba, akaitumbua kama hakuna kesho, naamini ziara hii ni mbwembwe tu za kuja kutamba kwenye tv:washing:
 
Nashangaa mwamsifia Mkapa wakati mwajua fika matatizo mengi ya ufisadi yalitokea kipindi chake. Mfano EPA, MEREMETA, NET GROUP, RADA, NDEGE YA RAIS nk..

so sielewi kama issue to personal or hatujui tunachotaka.
 
Issue utekelezaji, na yeye mwenyewe kufuatilia, c lazma aende, coz haka akiwa magogoni, maagizo yanawafikia wahusika, imagne toka aende 2006, zen leo ndio anaenda, ful up gani hiyo? Mkwere kituko kweli kweli after5 yea? Shame on you
 
(iv) Kuhusu malipo ya wasataafu wa iliyokuwa Jumuia ya Afrika Mashariki iliyovunjika, Rais Kikwete ametaka wote wanaostahili kulipwa mafao yao na hawajalipwa hadi sasa walipwe, hata kama ni kweli kuwa wengi wa watumishi hao tayari wamelipwa.
Hii ni tungo tata........................Jk bado haonyeshi kuelewa ya kuwa wengi wa wastaafu wamelipwa kwa mapunjo na ya kuwa si sahihi kudai wale ambao hawajalipwa walipwe...............kauli sahihi ingelikuwa wote ambao wamelipwa kwa mapunjo na ambao hawajalipwa kabisa walipwe mara moja...............................la pili hakuna fedha zilizotengwa na serikali kutekeleza adhma hii.............................

looks like Jk is playing once again some real cheap politics with human souls................................
 
mbona mambo yenyew hata Ruhanjo angeyasema?mishahara mipya tabu je kukopesha wafanya kazi?atuache kidogo.tushamsoma.
 
Kuna faida gani ya ziara kama hizi endapo unazungumza na menejiment pekee? Kama ni taarifa za utendaji anaweza akaagiza aletewe akiwa magogoni badala ya kuleta foleni mtaani.

Angeeleweka kama angezungumza na upande wa pili ili apewe taarifa za upande huo, nasikia alivyokuja long room leo alitaka kuondoka bila kuongea na mawakala, baada ya makelele yao ndipo aliposhuka kwenye gari alilokuwa ameshapanda na kuzungumza na wawili watatu-usanii mtupu!
 
Jk ni mchumi, sasa anaposema watafute njia za kupunguza inflation, anazungumza kwa nadharia, nilitegemea angetumia uchumi wake kushauri njia ipi itumike kupunguza inflation rate lakin jamaa yetu anatoa matumain mahali panapohitaji kutenda. Wakati huu si muda wakupeana matumaini alisha toa matumaini 5yrs ago hakuna alichotimiza aache ukilaza afanye maamuzi magumu.
 
Rais amewasifu watumishi wa Wizara ya Fedha kwa kufanya vizuri katika ukusanyaji wa mapato ya Serikali lakini akawataka waongeze juhudi zaidi na wafanye vizuri zaidi. Ameambiwa kuwa mapato ya Serikali yameongezeka kutoka makusanyo ya kiasi cha shilingi bilioni 215 kwa mwezi mwaka 2005 wakati Rais kikwete anaingia maradakani hadi kufikia wastani wa shilingi bilioni 420 kwa mwezi kwa sasa.

Mapato ya taifa yameongezeka kwa shilingi bilioni 205 tangu mwaka 2005 alipochanguliwa kuongoza taifa la Tanzania. Miaka ya nyuma mapato yaliyokuwa yanakusanywa ya shilingi bilioni 215 kwa mwezi yaliwezesha kujenga miradi mingi ya maendeleo iliyofadhiliwa na mapato yetu ya ndani na miradi imejengwa kwa ufanisi mkubwa.

Inakuwaje mapato yaongezeke mara mbili kisha miradi mingi ya maendeleo isimame? na hakuna mradi mwingine wowote mpya ambao umeanzishwa na serikali yake anaoweza kujivunia.

Tunataka jibu, pesa zetu zinapelekwa wapi?
 
Kumbe anakumbuka kufanya ziara nchini?? mi nilifikiri yupo Ughaibuni anakula gud tym.
Big up Kikwete kwa kuanza kufanya ziara nchini!
 
Ni ziara nzuri sana,nimefarijika sana na ziara hiyo ya mhe. Rais ya kwenda mwenyewe kujionea hali halisi ya long room. Wale jamaa ni wababaishaji wanatakiwa wafanye kazi usiku na mchana ili waweze kukusanya fedha nyingi za serikali, mbona wenzao wa bandarini wanafanya shift tatu kwa siku moja.

Kwa nini TRA wasiajiri watumishi wa kutosha na kuimarisha ulinzi pale long room wakafanya kazi masaa 24 mpaka siku za sikukuu maana pale ni sehemu muhimu sana kwa taifa letu.

Vilevile suala la kulipa kodi mara mbili liangaliwe hasa magari yanayoingizwa toka Zanzibar

:lol:
 
nafikiri alienda kupigwa picha tu, manake yote aliyoyasema/aliyoagiza wanayajua na ndiyo shughuli zao za kila siku
 
JK anaonekana kama anapata nuru ya usoni, haya ni matokeo ya KIKOMBE CHA BABU loliondo.
 
Nashangaa mwamsifia Mkapa wakati mwajua fika matatizo mengi ya ufisadi yalitokea kipindi chake. Mfano EPA, MEREMETA, NET GROUP, RADA, NDEGE YA RAIS nk..

so sielewi kama issue to personal or hatujui tunachotaka.
Hata hivyo hali haikuwa halijojo kiasi hiki. Mfumuko wa bei haukuzidi 5%, mishahara ilishaaanza kutoka kwa wakati, uzalishaji ulikuwa unapanda. Kikubwa zaidi Mkapa alikuwa na majibu yanayojitosheleza siyo kama huyu JK ambaye anaonekana kama hana baraza la mawaziri. Ziara ni za nini kwani hawezi kutoa maelekezo na kupata majibu ya kero kutoka kwa mawaziri wake wakiwa katika vikao vya Baraza la Mawaziri? Tunataka matokeo siyo ahadi na maagizo ya mdomo. Hizi ni siasa tu. JK hana strategy zozote za kumaliza matatizo ya nchi hii.
 
  • Thanks
Reactions: Obe

Similar Discussions

Back
Top Bottom