Hebu weka direct quote, audio au video.
Mpaka sasa haijulikani maneno halisi aliyosema Karume ni yapi.
Nadhani hii habari ina toka hapa....
Karume awakana CUF kweupe
Mwinyi Sadallah
Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar, Rais Amani Abeid Karume, amesema hakuna maamuzi yanayohusu maslahi ya nchi yatakayoamuliwa bila ya kushirikishwa wananchi wake.
Rais Karume aliyasema hayo jana alipokuwa akihutubia mkutano wa hadhara uliofanyika katika uwanja wa Kibandamaiti kufuatia mazungumzo yake ya kumaliza mpasuko wa kisiasa wa Zanziabr kati yake na Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad.
Alisema katika muafaka mpya uliopatikana, hakuna mshindi kwa vile mazungumzo hayo yamezingatia maslahi ya nchi na kuendeleza sera ya CCM ya kudumisha amani na mshikamano kwa wananchi wake.
Tunaamini amani ya kudumu imefika Zanzibar mafanakio haya ni ya vyama vyote na Wazanzibari wote hamna mshindi katika hilo, ushindi huwa katika uchaguzi sio katika suala la amani, alisema.
Alisema katika mazungumzo hayo, hakuna jambo jingine walilokubaliana zaidi ya kuzungumzia misingi ya kudumisha amani na utulivu kwa wananchi wa Zanzibar.
Hakuna jingine katika mazungumzo hayo isipokuwa suala la amani na utulivu lilikuwa na nafasi kubwa na hilo siyo dogo wanaobeza waache, alisema Rais Karume.
Hata hivyo, alisema kama kutakuwa na jambo lolote linalohusu Zanzibar, wananchi ndiyo watakuwa waamuzi wa suala hilo kwa vile viongozi kazi yao ni kuzungumza na siyo kufikia uamuzi.
Rais Karume alisema anaamini wananchi wa Zanzibar hawawezi kukataa jambo lolote lenye maslahi kwa nchi lakini alisema mtu unaweza kukataa pale mwingine atakapoamua kukulazimisha, kula biriani wakati wa asubuhi badala ya chai na vitafunio vyake.
Kama jirani yako atakujia asubuhi na mapema na kukukaribisha chakula cha biriani na akakulazimisha, basi utakataa kwa kuona kuwa kina madhara ndani yake kwa vile biriani huliwa mchana, alisema.
Hata hivyo, hakufafanua zaidi lakini alisema hakumwita Katibu Mkuu wa CUF Ikulu bali alimtolea salamu akiomba kutaka kuonana naye na kumpa nafasi hiyo.
Alisema baada ya kukutana na Maalim Seif Ikulu, alimpa nafasi ya kumsikiliza na kumueleza Baraza Kuu la Uongozi la CUF limeamua kumaliza tofauti za kisiasa na badala yake washirikiane kujenga nchi.
Tumekaa Baraza Kuu la Uongozi tumeona nchi imetulia na maendeleo tumeyaona hivyo tukiendelea kushirikiana maendeleo yataongezeka zaid, alimkariri Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif katika mazungumzo yake.
Rais Karume alisema baada ya kuwasilisha ujumbe huo, Maalim Seif aliomba amuombee dua kwa vile anakwenda kutoa uamuzi mzito mbele ya wanachama wake na kutoa ahadi ya kutekeleza ombi hilo. Pale pale nikamwambia nashukuru kuniambia maneno yako na siku zote nimekuwa nikikuombea dua njema, alisema Rais Karume huku akishangiliwa na wanachama wa CCM.
Hata hivyo, alisema katika mazungumzo yake yaliyofanyika Novemba 5, mwaka huu, Ikulu, hakumpa chai ya maziwa kama ilivyodaiwa na baadhi ya watu, baada ya kufikia uamuzi wa kumtambua kuwa Rais halali wa Zanzibar.
Hakuna chai wala uji bali alikunywa maji glasi moja na mie moja, alisema Rais Karume na kuongeza kuwa wanachama wote wa CUF wamuunge mkono Hamad kufuatia uamuzi wake wa kuamua kusahau tofauti na kujenga umoja wa kitaifa kwa maslahi ya Wazanzibari.
Alisema uamuzi wa Hamad umeleta faida kubwa kwa Zanzibar kutokana na hatua hiyo kuungwa mkono na mataifa mbalimbali zikiwemo nchi wahisani kwa vile upinzani sio ugomvi bali ni kusukuma mbele maendeleo.
Upinzani sio ugomvi, upinzani sio vita bali ni kutofautiana mawazo kwa lengo la kuharakisha maendeleoa kwa wananchi, alisema.
Alisema kimsingi CUF wamekuwa wakimtambua muda mrefu kwa vile wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wamekuwa wakishirikiana na mawaziri katika vikao vya baraza lake tangu kumalizika kwa uchaguzi mkuu wa mwaka 2005.
Awali, Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Saleh Ramadhan Ferouz, alisema Rais Karume amejitahidi kuleta mabadiliko makubwa ya maendeleo katika kipindi cha uongozi wake.
Alisema Zanzibar imepiga hatua kubwa katika ujenzi wa miundombinu ya barabara, bandari ya Malindi, Uwanja wa Ndege pamoja na mradi wa umeme vijijini hatua ambayo itasaidia katika utekelezaji wa mpango wa kukuza uchumi na kupunguza umasikini.
Aidha, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mjini Magharibi, Yussuf Mohammed, aliwataka wanachama wa CCM waiombee dua CCM iendelee kushinda maisha.
Mkutano huo ulikuwa umepambwa na mabango yanayosomeka Tunakupongeza Makamu Mwenyekiti wa CCM, Rais wa Zanzibar kwa hekima, busara zako na uwezo mkubwa wa kusukuma umoja na mshikamano wa nchi yetu.
Aidha, mabango mengine yalisomeka Chagua Chama cha Mapinduzi kwa maendeleo yako, Mchague mgombea wa CCM mwenye sifa achana na wababaishaji, Sera ya CCM ndiyo ukombozi wa umasikini'.
Viongozi wengine waliohudhuria mkutano huo ni Waziri Kiongozi, Shamsi Vuai Nahodha, Naibu Waziri Kiongozi, Ali Juma Shamuhuna na viongozi wengine mbalimbali wakiwemo mawaziri na viongozi wa chama.
NIPASHE