Annina
JF-Expert Member
- Nov 15, 2009
- 437
- 57
Miaka 2 iliyopita katika pitapita zangu maeneo ya sinza nilikutana na bango lenye ujumbe huu "wakivuta wao sigara, tukivuta sisi bangi". Ujumbe huu ulikuwa umebandikwa kwenye maskani ya vijana wa eneo hilo - maarufu kama kijiweni.
Leo nimeukumbuka usemi huu na nimeutafakari kidogo. Nimewakumbuka vijana wale wa kijiweni, ambao mara nyingi hakuna anaewapatiliza. Kwenye ujumbe huu wanaonekana kukata tamaa, hawaoni kama haki inatendeka na kwamba kuna matabaka ya "wao" na "sisi" - kwamba "wao" wakiiba kutoka hazina wanaombwa na kubembelezwa kurudisha walichoiba na kupongezwa kama vile ni mashujaa -maana ni "sigara", lakini "sisi" tukiiba kuku wa jirani kwa ajili ya kujikimu sheria inachukua mkondo wake maana ni "bangi"!
Wao wakisema uongo ulio dhahiri wanaitwa wanasiasa -sigara, sisi tukitoa maoni yetu tunaitwa wehu na kutakiwa kuthibitisha - bangi! Wao wakituingiza kwenye mikataba mibovu yenye dalili ya rushwa na kuliingiza taifa kwenye janga tunaambiwa ni vijisenti tu na pengine tunasumbuliwa na wivu wa kike - sisi tukichukua rushwa ya 5000/= tunaozea segerea!
Orodha ya wao na sisi ni ndefu... najiuliza kwa matabaka haya tunayoyajenga kwa ari mpya, nguvu mpya na kasi mpya tupo tayari kupokea matokeo yake?