Wakala wa Shetani

Wakala wa Shetani

Wakala wa Shetani - 27-

Alipopapasa vizuri, aligundua ile ni Toyota Pick Up, akiwa anajiuliza pale ni wapi, mara umeme uliwaka. Kusekwa alijiona yupo kwenye maegesho ya magari, kabla hajaamua afanye nini aliwasikia watu wakielekea kwenye gari hilo huku wakizungumza.
“Inabidi tuwahi kuondoka muda huu mzigo umefika tangu saa saba.”
“Itakuwa vizuri, Mr Brown alikuwa hana raha kabisa.”

Sauti zile zilimfanya Kusekwa aingie chini ya gari na kujificha, akaendelea kumuomba Mungu. Kuwaka kwa umeme kulifanya eneo lote ling’ae kama mchana na kumfanya Kusekwa aamini lazima atakamatwa kutokana na kuwaona

askari wakipishana kuhakikisha ulinzi unaimarishwa mgodini.

SASA ENDELEA...


Ndani ya chumba cha kukatia viungo vya albino, baada ya umeme kurudi wauaji wale walishtuka kukuta Kusekwa hayupo sehemu waliyokuwa wamemlaza Kusweka.

“Wazee yule mtoto amekwenda wapi?” mmoja alishtuka na kuuliza huku macho yakiwa yamemtoka pima.
“Si alikuwa amelala hapa?” mmoja alionesha kwa kidole alipokuwa amelala Kusekwa.
“Utani huu, au ametoroka?”
“Inawezekana lakini hata akitoroka atafika wapi? Lazima tutamkamata tu.”
“Tatizo si kukamatwa bali kuokoa muda, mtambo bado kidogo ufae, tukimaliza tuanze kumtafuta, kibaya hatujui katokea mlango upi.”
“Mmh! Kazi ipo jamani, kila mtu atoke na mlango wake ili kumtafuta.”

Baada ya kupeana majukumu, waliingia kwenye kazi ya kumtafuta Kusekwa ambaye alikuwa bado yupo chini ya gari akisikiliza mazungumzo ya dereva na mwenzake.

Kila mmoja alikimbia huku akiulizia walinzi kama wamemuona mtoto albino akipita maeneo hayo. Kila aliyeulizwa alisema hajamuona, kila mmoja akapagawa na kujiuliza atakuwa wapi. Wazo la kuwatoroka hawakuwa nalo zaidi ya kufikiria kuchelewa kutekeleza kazi yao kwa muda muafaka.

Waliamini kabisa mtoto huyo lazima angepatikana asubuhi kama hatajitokeza au kumuona sehemu alipojificha. Kusekwa aliiona miguu ya mbaya wake aliyekuwa amesimama karibu yake kabisa akiwauliza wahusika wa lile gari.

“Wazee hamjamuona mtoto albino?”

“Hatujamuona mtu yeyote, tena bahati nzuri tumefika hapa umeme ukiwa umeshawaka lakini eneo hili hatujaona kiumbe chochote, kwani vipi?”

“Kile kitoto kimetoroka, tulikuwa ndiyo tunatengeneza mtambo kwa ajili ya ishu ya bosi.”
“Sasa?”

“Baada ya umeme kuwaka hatukumuona japo tunajua lazima atapatikana.”
“Sasa fanyeni hivi, toeni taarifa kisha endeleeni na kazi ya kuutengeneza mtambo, mnafikiri atafika wapi? Lazima atapatikana tu. Mkianza kumtafuta hamjui mtachukua muda gani na mkimpata ndiyo muanze kazi ya kutengeneza mtambo.
“Hamuoni mtachukua muda mrefu? Lakini mtambo ukitengemaa na akipatikana mtafanya kazi kwa urahisi,” dereva wa gari alishauri.

“Hapo umesema neno, ngoja nitoe taarifa kisha turudi kutengeneza mtambo.”
Maneno yote hayo, Kusekwa aliyasikia na kuendelea kumuomba Mungu japokuwa aliamini kupona ni sawa na ngamia kupita katika tundu la sindano. Aliomba Mungu wasiliondoe gari haraka kwani lazima angeonekana.

Wale watu baada ya kusema hivyo, waliondoka na kumuacha chini ya lile gari. Baada ya kuondoka Kusekwa alimsikia dereva akisema:
“Acha tuwahi, muda umekwenda.”
Kusekwa alihofia kukanyagwa, alitoka chini ya gari kwa tahadhari kubwa, alipoliangalia lile gari aligundua kuwa nyuma lilikuwa na turubai. Wazo la haraka lilikuwa kuingia nyuma ya gari na kujifunika lile turubai huku akimuomba Mungu atoke salama kwenye mgodi wa kifo.

Mara gari lilianza kuondoka, mapigo ya moyo yalikuwa yakimwenda kwa kasi, kama mtu angekuwa karibu yake angesikia jinsi moyo unavyodunda. Gari lilipofika getini, askari alilisimamisha.
“Jamani simameni tukague gari.”

Kauli ile ilimfanya Kusekwa atokwe na haja ndogo kwa wasiwasi, alimuomba Mungu kwa kujua lazima ataonekana. Gari lilisimama na mlinzi alizunguka nyuma ya gari na kuanza kufunua turubai. Alishangazwa na sehemu moja iliyokuwa na mwinuko.

Bila kusema neno, alisogea hadi kwenye mwinuko na kufunua. Alipofunua turubai alishtuka kumuona mtoto albino akiwa nyuma ya gari, akiwa amejifunika turubai lile. Alipigwa na bumbuwazi na kujiuliza yule mtoto mbona yumo kwenye lile gari tena kajificha,

alishangaa kumuona mtoto akimuomba msamaha kwa kukutanisha mikono yake bila kusema neno huku machozi yakimtoka.
Alikumbuka taarifa ambazo alizipata juujuu kuhusu mauaji ya walemavu wa ngozi kwa imani za kishirikina katika mgodi wa Mr Brown. Aliamini kabisa mtoto huyo alikuwa akitoroka. Alishindwa aseme nini, alibaki kumtazama kwa huruma.
Dereva baada ya kuona muda unakatika kwa ukaguzi wa dakika mbili, aliuliza:

“Mzee Kondo mbona unauweka usiku? Umekuta nini naona umeganda?”

“Hakuna kitu, mnaweza kwenda,” alisema huku akirudisha turubai na kumuacha yule mtoto albino kwenye gari.

Alimruhusu dereva ambaye aliondoa gari na kutoka nje ya mgodi bila kujua nyuma ya gari kuna mtu. Kusekwa alimshukuru Mungu

gari kutoka salama mgodini. Gari lilikwenda kwa mwendo mrefu bila Kusekwa kuelewa alikuwa akielekea wapi, akaendelea kujificha kwenye turubai kutokana na upepo mkali. Sehemu moja gari lilisimama, akawasikia wale jamaa wakizungumza.

“Bwana eeh, tuchimbe dawa hapa.”
“Siyo mbaya.”

Kusekwa alitulia wakati watu wale wakiteremka kwenda kujisaidia haja ndogo. Wakati wanaingia kwenye gari ili waondoke,

Kusekwa aliteremka haraka na kuliacha gari liende. Sehemu aliyoshuka ilikuwa ngeni kwake. Kulikuwa na vichaka ambavyo hakuwa na uhakika wa usalama wake.


Itaendelea wiki ijayo.
 
Wakala wa Shetani - 28-


"Bwana eeeh tuchimbe dawa hapa."
"Sawa."
Kusekwa alitulia akijua jamaa wameteremka kwenda kujisaidia haja ndogo, wakati wanaingia kwenye gari ili waondoke, aliteremka haraka na kuliacha gari liende. Sehemu aliyoshuka ilikuwa ngeni kwake. Kulikuwa na vichaka ambavyo hakuwa na uhakika wa usalama wake.
SASA ENDELEA...


baada ya kutoka ndani ya kinywa cha mauti aliamini alikuwa salama, wakati akitafakari afanye nini mara kwa mbali aliona gari likija na kuwasha taa. Kwa woga alikimbia na kujificha nyuma ya kichaka ili wenye gari wasimuone. Gari lilipita bila wale watu kumuona na kumfanya abaki anajiuliza nini cha kufanya.
Baridi ya alfajiri ilikuwa kali lakini kwa Kusekwa haikuwa shida kwa vile furaha ya kubakia hai ilikuwa zaidi ya baridi ile. Kutokana na kiza cha alfajiri ile aliamua kujilaza pembeni ya kichaka ambacho hakujua usalama wake upo kiasi gani.
Pamoja na kutetemeka, alimuomba Mungu kupambazuke ili ajue yupo wapi na afanye nini. Pamoja na kuwaogopa wanadamu lakini aliamini wapo wenye roho nzuri kama Father Joe ambaye alionesha upendo wa hali ya juu. Aliwachukia binadamu kama Mr Brown ambao hujionesha wana roho nzuri usoni lakini moyoni wana roho mbaya zaidi ya nyoka.
Na pia aliamini kabisa Father Joe hajui chochote toka kwa rafiki yake mkubwa, Mr Brown kuwa anawachukua watoto wenye ulemavu wa ngozi na kwenda kuwakata viungo huku akidanganya kawapeleka Ulaya na kumbe Ulaya yenyewe ni kuzimu.
Kutokana na akili yake kufanya kazi na kujua haki ya mwanadamu inapatikana wapi, alipanga kama atapona katika kile kifo basi atakwenda kwenye vyombo vya sheria. Alikumbuka siku moja aliyoelezwa na Father Joe kuwa kila kitu kinaongozwa na sheria na chombo kinacholinda raia ni jeshi la polisi.
Alimuomba Mungu aweze kufika polisi kufichua uovu ule wa Mr Brown, kila alipojaribu kufumba macho, jinamizi la kutaka kukatwa viungo lilimjia na kumfanya akae macho mpaka kunapambazuka.
Kutokana na baridi kuwa kali, ilibidi Kusekwa ajiingize katikati ya kichaka ili kupunguza ukali wa baridi lile. Kwa bahati mbaya, sehemu aliyoingia kulikuwa na nyoka amelala ambaye alimkanyaga. Naye nyoka katika kujitetea alimgonga mguuni.
Kusekwa alishtuka na kupiga kelele za maumivu, wakati huo nyoka alikuwa akikimbia eneo lile kwa kutoa mlio wa kutambaa. Kusekwa alitoka kichakani mbio huku akishikilia mguu na kusogea barabarani.
Baada ya kwenda mwendo mfupi kuondoka eneo la tukio akiogopa kushambuliwa tena na nyoka, alianza kusikia kizunguzungu ambacho kiliongezwa na mwanga mkali wa gari uliompiga usoni na kumfanya aanguke chini, hakujua kilichoendelea.
MIAKA SABA BAADAYE
Ng'wana Bupilipili alikuwa katika Kijiji cha Sangema kwenye kituo cha kuwatunza watu wenye maisha magumu, baada ya kupata hifadhi. Kituoni hapo hapakuwa tofauti na kituo alichokimbia. Shughuli zilikuwa zilezile za kazi za mikono. Kutokana na uzoefu alioupata, alijikuta akipewa kipaumbele na mkuu wa kituo, Mr Harrison kuwa kiongozi na mwalimu msaidizi.
Kutokana na kupewa uongozi alijikuta akipata posho ndogondogo tofauti na kituo cha awali ambacho malipo yake yalikuwa kula na kulala. Alijikuta akifurahia maisha kule, kila siku dua zake zote alizielekeza kwa mwanaye Kusekwa ili Mungu amtangulie na kumkinga na roho mbaya za watu na kumpa maisha marefu.
Aliendelea kuwa mwalimu mwanafunzi pale kituoni, akawa anajifunza asichokijua na kuwafundisha wenzake anachokijua. Kwa kadiri siku zilivyozidi kusonga mbele ndivyo alivyokuwa akiongeza ujuzi wa kazi yake. Siku moja akiwa darasani, juu ya meza ya mwalimu wao kulikuwa na gazeti.
Ng'wana Bupilipili alilichukua lile gazeti na kuanza kulisoma, ndani yake alikutana na picha yake iliyokuwa robo ukurasa, ikiwa na maandishi makubwa; ANATAFUTWA. Chini ya picha kulikuwa na maneno yaliyosomeka: Mtuhumiwa hapo juu anayetambulika kwa jina la Rozalia Bupilipili au maarufu kwa jina la Ng'wana Bupilipili anatafutwa na jeshi la polisi kwa mauaji ya wanakijiji cha Nyasha pamoja na askari wawili. Ni mwanamke hatari sana mwenye mafunzo ya kigaidi. Yeyote atakayemuona atoe taarifa kituo chochote cha polisi. Zawadi nono itatolewa.
Ng'wana Bupilipili alishtuka kuona picha yake kwenye gazeti huku akituhumiwa kufanya mauaji ya kutisha ya wanakijiji wa Nyasha pamoja na askari wawili. Aliamini usalama wake upo mashakani, kwani kwa yeyote atakayebahatika kuiona ndani ya kituo kile lazima atamuogopa na kisha kuripoti polisi na kusababisha akamatwe.
Kwa jinsi ilivyoonesha, gazeti lile lilikuwa la siku ile, hata mkuu wa kituo kile, Mr Harrison alikuwa bado hajaliperuzi. Alipata wazo la kulichana lakini wasiwasi wake ulikuwa mtu yeyote atakayebahatika kuliona gazeti hilo lazima angemtambua. Kwa ajili ya kuhofia maisha yake, alipata wazo la kutoroka eneo lile ili kujiokoa.
Alitoka darasani taratibu na kuelekea chumbani kwake, akachukua vitu muhimu tu na kuondoka eneo la kituo bila mtu yeyote kujua. Alijitanda khanga na kuuficha uso wake kwa sehemu kubwa kisha alikwenda hadi kituo cha basi ambako alipanda gari kuelekea asikokujua, akawa anatafuta sehemu za kijijini zaidi ambazo magazeti hayafiki.
Mr Harrison baada ya kumaliza shughuli zake ndogondogo, alirudi darasani kuulizia wamefikia wapi. Lakini alishangaa kutomkuta mwalimu, ilibidi amuulize kwa wenzake
"Mwalimu wenu yupo wapi?"
"Mmh! Alikuwa anasoma gazeti hapo kisha alitoka nje, huenda amekwenda msalani."
Mr Harison alichukua gazeti lake na kuanza kulisoma taratibu, alipofika kwenye ukurasa uliokuwa na picha ya Ng'wana Bupilipili alishtuka. Aliiangalia ile picha kwa muda kisha akasoma maelezo yake ambayo yalimshtua sana, habari hiyo ilionesha kuwa mwanamke huyo ni hatari sana.
Ili kutaka ukweli, alitoka na lile gazeti hadi kwa wenzake ambao aliwaonesha ile picha, kila mmoja alimtambua Ng'wana Bupilipili. Kwa vile walijua amekwenda msalani, walimsubiri ili wambane na kumuuliza kuhusu uhusiano na ile picha lakini ajabu muda ulizidi kukatika bila kuonekana.
Ilibidi ufanyike msako wa siri kutaka kubaini yupo wapi, lakini hakukuwa na taarifa zozote. Mr Harrison alikumbuka kauli za wanawake waliokuwa kwenye mafunzo kwamba baada ya kusoma lile gazeti alitoka darasani. Aliamini kabisa ni mwenyewe na ameamua kukimbia.


Je, nini kitaendelea? Fuatilia wiki ijayo.
 
Wakala wa Shetani - 29-


ILIPOISHIA:
Ilibidi ufanyike msako wa siri kutaka kubaini Malimi yupo wapi, lakini hakukuwa na taarifa zozote. Mr Harison alikumbuka kauli za wanawake walipokuwa kwenye mafunzo kwamba baada ya kusoma lile gazeti alitoka darasani. Aliamini kabisa ni mwenyewe ambaye baada ya kuiona picha yake ameamua kukimbia.
SASA ENDELEA...


Waliongeza msako kila kona lakini waliambulia patupu. Ng'wana Bupilipili alikuwa ameshapotea eneo lile. Taarifa zile alizirudisha kwa wenzake ambao walipigwa butwaa wasiamini tuhuma zile kuwa zake kutokana na tabia yake ya upole tena yenye huruma na mapenzi kwa watu wote.
Hakuwa mbaguzi, alikuwa akijitoa yeye kwa wenzake ili kutatua matatizo yao, hata kutoa sehemu ya posho yake kuwasaidia wenzake. Japokuwa picha ilifanana kwa asilimia mia, bado shoga zake walisema siyo yeye. Lakini kizungumkuti kikabakia kama siyo, yeye yupo wapi?
Lilibakia fumbo zito vichwani mwao, wasijue Malimi kipenzi chao amekwenda wapi.
***
Kusekwa aliposhtuka alijikuta amelala kwenye kitanda cha kamba, alipozungusha macho alijikuta yupo kwenye chumba cha nyumba ya udongo. Alijiuliza pale ni wapi na amefikaje. Alisikia sauti za watu wakizungumza nje ya chumba.
"Dogo lazima atakuwa ameamka."
"Ngoja nikamcheki."
Kusekwa aliangalia mlangoni na kumuona mtu mmoja akiingia, walipokutanisha macho alisema kwa sauti:
"Ameamka."
"Poa, njoo naye apate uji na viazi inaonekana hajala tangu jana," sauti kutoka nje ilisema.
"Hakuna tatizo, dogo amka," jamaa alisema na kumfanya Kusekwa anyanyuke kitandani.
Alitoka nje ya chumba na kukuta sebuleni kuna watu wengine wawili.
"Hujambo dogo?" walimsalimia.
"Sijambo, shikamooni."
"Marahaba."
Walimpatia uji na viazi vya kuchemsha, baada ya kula, walimuuliza sehemu waliyomuokota amefikaje na alikuwa anatoka wapi. Kusekwa aliwaeleza yote yaliyomkuta baada ya kuamini wale ni watu wema kutokana na walivyomuokoa na kumtunza kama mdogo wao.
Jamaa alishtuka na kumpa pole huku wakimhakikishia kuishi naye maisha mazuri pale na kumtafutia shule yenye usalama. Aliwashukuru kwa kumuokoa na kuwa tayari kumlea. Siku ilipita wakimlea kama mtoto wao kwa kumuonesha upendo wa hali ya juu.
Usiku ulipofika walikwenda kulala na Kusekwa alipewa chumba chake, majira ya usiku wa manane Kusekwa alishtuka usingizi baada ya kuvamiwa na kuzibwa mdomo. Ghafla alisikia maumivu makali mkono wake wa kushoto. Alitaka kupiga kelele lakini mdomo ulikuwa umezibwa.
Alihisi maumivu makali na kupoteza damu nyingi, aliteseka bila msaada wowote huku akijiuliza wenyeji wake wapo wapi mpaka watu wale wabaya wameingia na kumkata mkono. Baada ya kutoka damu nyingi alipoteza fahamu.
Aliposhtuka alijikuta yupo hospitali lakini hakuwa na mkono mmoja, aliangua kilio kitu kilichofanya wauguzi wafike na kumbembeleza. Baada ya kutulia alielezea yote tangu kuchukuliwa na Mr Brown na kukosa kukatwa viungo na siku aliyovamiwa na watu wabaya na kumkata mkono wake wa kushoto.
Kwa vile ilikuwa hospitali ya dini walimpa malezi mazuri ya kumfajiri, aliendelea kuuguza jeraha la mkono. Baada ya siku mbili zilipatikana taarifa kuna watu wamekamatwa na mkono wa albino. Kwa vile Kusekwa alikuwa amekatwa mkono siku chache. Alichukuliwa kwenda kuwatambua watu wale japokuwa aliamini kwa usiku alivyovamiwa asingeweza kuwajua.
Lakini alipofika polisi ilikuwa tofauti na alivyofikiria, watu waliomuokota na kumuahidi kumtunza ndiyo waliokamatwa na mkono wake. Roho ilimuuma na kuona hakuna kiumbe wa kuaminiwa diniani, kama waliomuokota ndiyo waliomtenda.
Alirudishwa hospitali na watu wale walifunguliwa mashitaka ya kukutwa na mkono wa mtu. Kusekwa naye aliendelea vizuri na jeraha lake ambalo kila siku lilionesha maendeleo vizuri. Baada ya kupata nafuu alihamishwa kutoka wodini na kupelekwa kwenye kituo kidogo cha kulelea watoto yatima ambao huchukuliwa na wafadhili mbalimbali.
Alikaa pale kwa mwezi mmoja akitunzwa na kupata mafunzo ya awali ambayo alianza kuyapata kwenye mgodi wa Mr Brown. Siku zote alijenga chuki kwa watu, kiumbe aliyemwamini alikuwa mwanamke peke yake. Lakini wanaume wote aliwaogopa kwa kuwaona wana sura za furaha lakini mioyo yao ilikuwa na nia mbaya kwao.
Alizidi kuwachukia baada ya kuwasikia mganga mkuu na msaidizi wake wakizungumza juu ya wao maalbino kutolewa kafara kwa ajili ya utajiri wa watu. Hakuamini kama kweli Mungu aliwaumba wawe dawa ya utajiri bali viumbe wenye haki ya kuishi kama wengine.
Alijiuliza haki yake itapatikana wapi kwa vile wale wanaoonekana wema mbele ya watu ndiyo haohao walio mstari wa mbele kusaka roho zao kwa udi na uvumba.
Baada ya mwezi kupita huku afya yake ya jeraha ikizidi kuimarika, alipewa taarifa ambazo kwa wengine waliamini ni njema lakini kwake haikuwa hivyo. Walielezwa mfadhili atakuja kuwachukua watoto wawili, mmoja akiwa yeye Kusekwa.
Kilichomshangaza ni kuchaguliwa yeye na mwenzake ambaye alikuwa albino aliyekuwa na umri mdogo kuliko yeye. Alikumbuka jinsi alivyochukuliwa kwenye kambi ya Father Joe na Mr Brown kuwa anakwenda kumtunza kumbe kumtoa roho.
Alitaka kukataa kwenda popote lakini bado hakutakiwa kuonesha kiburi kwa vile kuna watu wenye roho nzuri kama Father Joe. Hakuwa na uwezo wa kukataa kwenda kwa huyo mfadhili. Alikubali kwa shingo upande huku uhai wake akimkabidhi Mwenyezi Mungu.
Siku ya kuja kuchukuliwa ilipofika alikutwa akiwa amejipumzisha kwa vile haikuwa siku ya masomo. Aliliona gari likija, halikuwa geni machoni mwake, baada ya wageni kushuka, jicho lake lilitua kwa hasimu wake mkubwa Mr Brown. Akiteremka kwenye gari akiwa na wapambe wake walewale aliokuja nao kumchukua kwa Father Joe.
Aliamini kabisa Mr Brown hakujua anayemfuata ni Kusekwa, angejua ni yeye asingekuja zaidi ya kuwatuma wapambe wake. Alimuona akitembea kuelekea ofisini kwa mkuu wa kituo kile cha Misheni chenye hospitali kubwa. Moyo ulimlipuka na kujua alichokuwa akikiwaza kilikuwa kimetimia. Mr Brown alikuwa amemfuata kwa kivuli cha wema wa kuwasaidi huku wengi wakijua ni viumbe kama yeye wanapewa upendeleo wa kwenda nje ya nchi kusoma.
Kumbe ilikuwa safari ya kuzimu yenye maumivu makali ya kukatwa viungo bila ganzi, akiwa bado anatafakari, dada mlezi wa kituo kile alimfuata.
"Kusekwa jiandae basi wageni wameshafika, tena una bahati nasikia watu wa aina yenu ndiyo hupata nafasi ya kwenda nje kusoma."


Je, Kusekwa atafanya nini? Usikose jumapili ijayo
 
[h=1]Wakala wa Shetani -30-[/h]ILIPOISHIA:
Aliamini kabisa Mr Brown hakujua anayemfuata ni Kusekwa, angejua ni yeye asingekuja yeye zaidi ya kuwatuma wapambe wake. Alimuona akitembea kuelekea ofisini kwa mkuu wa kituo kile cha Misheni chenye hospitali kubwa. Moyo ulimlipuka na kujua alichokuwa akikiwaza kilikuwa kimetimia, Mr Brown alikuwa amemfuata kwa kivuli cha wema wa kuwasaidia huku wengi wakijua ni viumbe kama yeye wanapewa upendeleo wa kwenda nje ya nchi kusoma.
Kumbe safari ya kuzimu yenye maumivu makali ya kukatwa viungo bila ganzi, akiwa bado anatafakari, dada mlezi wa kituo kile alimfuata.
"Kusekwa jiandae basi wageni wameshafika, tena una bahati nasikia watu wa aina yenu ndio hupata nafasi ya kwenda nje kusoma."
SASA ENDELEA...

Kusekwa hakujibu zaidi ya kutokwa machozi, Sister Anna alimshangaa Kusekwa alikuwa tofauti na Albino mwenzake aliyekuwa na furaha.
"Kusekwa mbona unalia hukufurahia safari hii?"
"Hii dada si safari ya Ulaya bali ya kifo."
"Kusekwa una maana gani?"
"Dada ni hadithi ndefu ya maisha yangu, nimeweza kuruka mkojo nikakanyaga kinyesi."
"Kusekwa una siri gani ya muda mrefu uliyoiweka moyoni mwako?"
"Wee acha, maisha yangu yamezungukwa na shetani wa mauti."
"Ni kweli, sasa hivi mmekuwa akitafutwa sana na watu wabaya kwa ajili ya kuwatoa kafara. Ndio maana tumekuwa makini kuwalinda kwa nguvu zote ndani ya kituo chetu, muda wote mmepewa kipaumbele hata wafadhili wanapokuja ninyi ndio mnaotakiwa kuondoka.
"Huoni wenzako wana miaka miwili hawakupata nafasi hiyo, lakini wewe na mwenzako mmepewa upendeleo. Huyu mfadhili aliyekuja ni mtu tunayemuamini amekuwa akiwachukua watoto wengi hasa wenye hali kama yako na baada ya muda hutuletea taarifa kuwa amewapeleka nje kusoma."
"Dada mpaka sasa mmeshampa watoto wenye hali kama yangu wangapi?" Kusekwa aliuliza.
"Ni wengi hata thelathini wanafika."
"Mungu wangu!" Kusekwa alishika kichwa.
"Kwani vipi mbona unanitisha Kusekwa?" Sister Anna alishtuka.
"Mna dhambi ya kutoa roho ya watu wote hao na kesho kwa Mungu mna la kujibu."
"Kusekwa kwanini unasema hivyo?"
"Wote uliompa Mr Brown sasa hivi ni nyama ya udongo wakiwa na viungo nusu."
"Mungu wangu, unasema kweli! na umemjuaje Mr Brown?"
"Ndio ushangae kumjua Mr Brown, ni kiumbe mbaya kuliko nyoka aliyelaaniwa na Mungu, cheko lake nyuma ameficha madhambi ya damu za watu wasio na hatia. Kama hapa ameua watu zaidi ya thelathini unafikiri vituo vingine wameuawa watu wangapi?"
"Kusekwa unayosema ni kweli?" Sister Anna alizidi kumshangaa.
"Chanzo cha mimi kukatwa mkono kilikuwa yeye, nilikuwa nimepona kwenye kinywa cha mauti na kuangukia kwenye mikono ya viumbe wenye uchu. Nashukuru nimekatwa mkono lakini kwa Mr Brown ningebakia kiwiliwili kisicho na mikono na miguu."
"Wewee!!"
"Dada yangu shangaa ya Musa uyaone ya Firauni."
"Kusekwa, ilikuwaje?"
Kusekwa alimueleza toka alipokuwa katika kituo cha kulelea watoto wenye matatizo, na chanzo cha yeye kuwa pale. Kutokana na historia aliyopewa mama yake alitoroka baada ya kulipa kisasi cha kuua wanakijiji waliomuua baba yake pamoja na kuchukua mali zao kinguvu yakiwemo mashamba na mifugo.
Sister Anna alibakia mdomo wazi huku muda ukiwa umekwenda.
"Lazima nikiri kuwa Mungu mkubwa ndiye aliyeniokoa na mauti yale, nilikuwa nimeshafungwa kwenye mashine tayari kukatwa viungo bila ganzi. Tena kibaya wanaofanya hivyo ni miongoni mwa ndugu zetu tunaoishi nao sehemu moja kutokana na tamaa ya pesa wanakosa utu ndani ya mioyo yao na kututoa uhai wetu ambao hatukupewa kimakosa na Mungu."
Maneno mazito yaliyochanganyikana na kilio yalimfanya sister Anna kutokwa ma machozi bila kujijua, akiwa hajapata cha kumwambia Kusekwa, walishtuliwa na mkuu wa kituo aliyewafuata baada ya kuona wanachelewa.
"Anna unafanya nini, mtoto mmoja tayari huyo unafanya naye nini muda wote niliokutuma?" mkuu wa kituo aliuliza kwa ukali.
"Samahani mkuu, anakwenda kuoga sasa hivi," alimjibu bila kugeuka.
"Kwa vile hajachafuka kambadilishe nguo tu umlete haraka."
"Sawa."
"Haya fanyeni haraka," baada ya kusema vile aligeuka na kuondoka akimuacha Sister Anna akitazamana na Kusekwa. Kama mkuu wa kituo angemuangalia vizuri Anna usoni angegundua kitu, lakini haraka yake ilimfanya afikishe ujumbe kuliko kuwaangalia wahusika.
Sister Anna alikuwa akitokwa na machozi kwa maneno mazito ya Kusekwa juu ya vijana maalbino wengi waliopoteza maisha yao bila hatia kwa kisingizio cha kupelekwa nje ya nchi kusoma. Alimtazama Kusekwa na kukosa cha kumwambia kwani aliamini kabisa hatakubali kuondoka na Mr Brown baada ya kunusurika kwenye kinywa cha mauti.
"Sasa Kusekwa tufanye nini?" Sister Anna alimuuliza Kusemwa.
"Dada Anna mimi huko siendi labda mauti yangu, siwezi kurudi ndani ya kinywa cha mauti."
"Sawa, sasa tutafanyeje na muda unakwenda?"
"Mimi natoroka siendi huko."
"Hata mimi sikushauri uyafuate mauti tena uliyakimbia kwa muujiza wa Mungu , lakini nitamueleza nini mkuu anielewe?"
"Mweleze ukweli wala usimfiche, acha niondoke eneo hili kabla hajaja tena."
Kusekwa alikwenda chumbani kwake na kuvaa nguo nzito na viatu na kuondoka eneo la kambi aliyokuwa karibu msitu wa miti ya asili, iliyopandwa kwa ajili ya kulinda mazingira na kutengeneza vyanzo vya maji.
Kusekwa akiwa amevaa nguo zake za baridi aliingia porini na kuanza kukimbia katikati ya msitu akiwa na mkono wake mmoja lakini alikuwa ameshauzoea.
***
Baada ya Kusekwa kukimbia na kuondoka eneo la kambi ile, Sister Anna alijikuta akitafuta cha kumwambia mkuu wake. Alikwenda taratibu hadi ofisini ambapo mtoto mwingine albino alikuwa tayari ameandaliwa kwa ajili ya kuondoka na Mr Brown.
Mkuu wake alishangaa kumuona Anna peke yake bila Kusekwa.
"Vipi mbona unakuja peke yako?"
"M..mm...," Sister Anna alikosa jibu.
"Vipi! Mbona sikuelewi yupo wapi muda unakwenda si unajua wanakaa mbali?"
Anna alishindwa kujibu na kubakia akitoa macho kama kameza mfupa, kitu kilichomfanya mkuu wake anyanyuke kwa kuwaomba samahani wageni.
"Jamani samahanini, nakuja?"
"Bila samahani," walijibu kwa pamoja.
Alimfuata Anna na kutoka naye nje baada ya kugundua alikuwa na kitu kilichokuwa kikimtatiza kwani haikuwa kawaida yake kuwa vile. Baada ya kutoka naye nje alimuuliza kwa sauti ya upole.
"Vipi mbona hivyo, Kusekwa yupo wapi?"
"Kuna tatizo father!"
Itaendelea wiki ijayo.



Je, nini kitaendelea? Usikose wiki ijayo.
 
[h=1]Wakala wa Shetani - 31-[/h]
Anna alishindwa kujibu na kubakia akikapua macho kama kameza mfupa, kitu kilichomfanya mkuu wake anyanyuke kwa kuwaomba msamaha wageni.
"Jamani samahani, nakuja."
"Bila samahani," walijibu kwa pamoja.
Alimfuata Anna na kutoka naye nje baada kugundua alikuwa na kitu kilichokuwa kikimtatiza, haikuwa kawaida yake kuwa vile. Baada ya kutoka naye nje alimuuliza kwa sauti ya upole.
"Vipi mbona hivyo, Kusekwa yupo wapi?"
"Kuna tatizo father!"
SASA ENDELEA...

"Tatizo! Kusekwa kafanya nini?" Father alishtuka.
"Father kuna makosa makubwa tutakuwa tumefanya bila kujua."
"Makosa gani?"
"Kama ni kweli tutakuwa tumepata dhambi kubwa kwa kutoa roho za albino wasio na hatia."
"Una maana gani kusema hivyo?"
Anna alimueleza yote aliyoelezwa na Kusekwa na uamuzi aliochukua wa kukimbia.
"Anna unasema kweli!?" Father alishtuka sana kusikia vile.
"Ni kweli, Kusekwa amejuaje kama yule Mzungu anaitwa Mr Brown?"
"Hapo si ndiyo nashangaa kusikia hivyo!"
"Inaonekana kumbe maalbino wote tuliokuwa tukimpa na kusema anawapeleka nje kusoma kumbe alikuwa akiwakata viungo kwa imani za kishirikina kwa ajili ya mgodi wake."
"Lakini watakuwa wanamsingizia, mbona hafanani na tuhuma hizo?"
"Kusekwa aliyosema mwanzo si alitueleza kuwa alitoroka katika mgodi, Mr Brown hana mgodi?"
"Anao."
"Na jina siyo lake?"
"Ni lake."
"Basi Father umiza kichwa, la sivyo tutaendelea kuwatoa kafara watoto maalbino huku tukijua kinachoendelea, tutakuwa wauaji."
"Mmh! Hii mpya, sasa tutafanya nini maana jamaa anajua anaondoka na albino wawili?"
"Hakuna cha kujiuliza, mueleze tumesitisha kuwatoa watoto maalbino."
"Atanielewa kweli, mtu nilishamkubalia na mtoto tumeshamuandaa na amemuona?"
"Mimi nafikiri suala la uhai wa mtu si la kufumbiwa macho, kama wewe huwezi niachie mimi nitamueleza. Huoni tuna dhambi ya watoto wote ambao tuliambiwa wamekwenda Ulaya kusoma kumbe ni Ulaya ya kuzimu?"
"Mmh! Ipo kazi."
"Father kama huwezi niachie niwaeleze, roho inaniuma sana kuona watoto wote tuliompa Mr Brown amewaua kikatili kwa kuwakata viungo," Sister Anna alisema kwa uchungu.
"Okay, nimekuelewa niache nikawaeleze kwamba Filipo haondoki."
Baada ya mazungumzo ya siri waliongozana hadi kwa wageni, mkuu wa kituo baada ya kukohoa akasema:
"Samahani kwa kuwaweka kwa muda mrefu."
"Bila samahani," walijibu wote.
"Kutokana na sababu zilizokuwa nje ya uwezo wetu, hatutakupa watoto kwa vile nilipitiwa kuwaeleza kuwa watoto kabla ya kuondoka walitakiwa kuonana na wazazi wao."
"Mkuu mbona unaharibu mambo, si unajua kampuni yangu inahusika kuwapeleka nje watoto wenye ulemavu wa ngozi?" Mr Brown alilalamika.
"Ni kweli, lakini hata watoto wasio na ulemavu wa ngozi nao wanahitaji kwenda nje," Father alisema.
"Ni kweli, lakini wenye ulemavu wa ngozi ndiyo waliopewa kipaumbele kutokana na kusakwa na watu na kuwakata viungo. Hivyo tumewapa kipaumbele wao ili kuwaweka sehemu salama," Mr Brown alitetea hoja yake.
"Sina hakika kama walemavu wanaoonewa huruma ni wa ngozi tu, mbona wapo wengi?" Sister Anna alihoji.
"Huo ni mpango uliopangwa mwakani kuwachukua watoto mchanganyiko."
"Sawa lakini kama nilivyokueleza hawawezi kuondoka bila kuonana na wazazi wao," Father alikataa kuwatoa watoto.
"Wanakuja lini?"
"Hawakusema ila walituma ujumbe lazima waonane na watoto wao."
"Lakini nina siku moja tu, kama vijana hawa ningeondoka nao leo wangeungana na wengine wanane kuondoka keshokutwa, tena wana bahati ya mtende," Mr Brown alizidi kuwatia tamaa.
"Ni kweli, lakini hatuwezi kukiuka kauli ya wazazi wao kwa vile sisi ni walezi lakini wenye haki ni wazazi wao."
"Sasa mkuu, mimi nitakuachia hapa kiasi cha pesa wakija wape ili wasikusumbue."
"Kama pesa hata mimi ningewapa, lakini naheshimu kauli zao kwa vile wao ni wazazi sisi ni walezi tu, hatuna mamlaka ya kwenda kinyume na makubaliano tuliyokubaliana. Mbona waliotangulia tulikupa bila kipingamizi tena wengi kuliko hawa wawili?"
"Kwa hiyo nisubiri mpaka lini?"
"Wakija leo nitakujulisha uje kesho, wakija kesho vilevile nitakujulisha, usife moyo."
"Okay, hatuna jinsi."
Mr Brown aliondoka akiwa amenyongea baada ya kuwakosa wale maalbino wawili, waliingia kwenye gari lao na kuondoka kurudi mgodini. Baada ya kuondoka walibakia mkuu wa kituo na Sister Anna wakijadiliana.
"Father umeona?" Sister Anna aliuliza.
"Nimeona."
"Anataka kutoa pesa ili awanunue watoto, huoni kama ana maslahi nao?"
"Ni kweli."
"Sasa hizi taarifa zifike kwenye vyombo vya dola ili wachunguzwe na wakigundulika wachukuliwe hatua kali."
"Kuna muhimu wa kufanya hivyo, bado siamini kama kweli watoto wote aliowachukua amewaua kwa kuwakata viungo. Kama ni kweli tuna dhambi kubwa ya damu za watoto wale ambao tulijua wapo Ulaya kumbe kuzimu," Father alisema kwa masikitiko.
"Mkuu hili lisilale, ikiwezekana tukaliripoti leoleo."
"Hapana Anna tusifanye papara, nitampigia mkuu wa makosa ya jinai, ni rafiki yangu mkubwa. Atakuja hapa na tutamueleza, yote nina imani atayafanyia kazi."

Je, nini kitaendelea? Usikose wiki ijayo.
 
[h=1]Wakala wa Shetani - 32-[/h]
"Kama ni kweli tuna dhambi kubwa ya damu za watoto hao ambao tulijua wapo Ulaya kumbe kuzimu," Father alisema kwa masikitiko.
"Mkuu hili lisilale, ikiwezekana tukaliripoti leoleo."
"Hapana Anna, tusifanye papara, nitampigia mpelelezi mkuu wa makosa ya jinai ni rafiki yangu mkubwa. Atakuja hapa tutamueleza yote, nina imani atayafanyia kazi."
SASA ENDELEA...

"Kama ni hivyo itakuwa heri."
"Sasa Kusekwa atakuwa wapi?"
"Sijui, nina imani akiwaona wameondoka atarudi."
Kusekwa baada ya kutoka eneo la kambi, aliingia porini. Kutokana na hofu ya maisha yake, alikimbia kwa muda wa saa tatu bila kupumzika. Baada ya kukimbia kwa muda mrefu alijikuta akichoka na kuamua kujipumzisha kwenye mti uliokuwa na hewa safi.
Bila kujielewa, usingizi mzito ulimpitia, alishtushwa na sauti za watu waliokuwa wakizungumza. Alipofumbua macho hakuamini kumuona Mr Brown akiwa na vijana wake mbele yake.
"Bosi huyu si Kusekwa?"
"Ni yeye, mbona hana mkono mmoja?"
"Tumuulize."
Kusekwa baada ya kukurupuka alipokuwa amelala, alitaka kukimbia lakini walimuwahi na kumkamata.
"Vipi wewe mbona upo hapa?" Mr Brown alimuuliza.
Kusekwa hakuwajibu, aliangua kilio cha hofu akiamini bado mauti yalikuwa yakimuandama, pamoja na kuyakimbia kila kukicha tangu alipozaliwa. Mr Brown alijifanya msamaria mwema kwa kumbembeleza.
"Kusekwa usilie, nipo hapa kwa ajili ya kukusaidia, umefikaje huku na muda wote ulikuwa unaishi wapi?"
Kusekwa hakujibu kitu, aliendelea kulia akiwa amekaa chini, pembeni ya ile barabara kulikuwa na bonde kubwa. Kusekwa wazo lake kubwa lilikuwa kujitupia bondeni, aliona heri afe kwa kujitupa bondeni kuliko kukatwa viungo na Mr Brown.
Mr Brown aliagiza achukuliwe na kuingizwa kwenye gari, msaidizi wake alimbeba juujuu ili kumuingiza ndani ya gari. Kusekwa, kwa kutumia mkono wake mmoja alimshika jamaa jichoni nusura amtoe jicho, maumivu aliyoyapata yalimfanya amtupe chini.
Alipofika chini alitimua mbio kuelekea kwenye lile bonde, hawakukubali, walianza kumfukuza ili wamshike. Alikimbia kwa nguvu zake zote ili kujiokoa katika mikono ya wauaji. Mr Brown baada ya kuona Kusekwa amewazidi mbio alisema kwa sauti ya juu:
"Kama anawasumbua mpigeni risasi ya mguu."
Kusekwa kusikia hivyo, alijua mauti yapo usoni kwake, bila kuangalia anaangukia wapi alijitupa bondeni. Kilichoendelea hakujua baada ya kujipiga sehemu na kupoteza fahamu.
Mr Brown hakukubali, aliutaka mwili wa Kusekwa akiwa hai au umekufa, shida yake ilikuwa viungo vilivyobakia. Vijana wake waliingia bondeni kumtafuta. Kutokana na bonde kuwa refu kwenda chini na kutokuwa na njia ya karibu, walisogea mbele kutafuta njia ya karibu kisha kurudi eneo alilojitupia Kusekwa.
Msako ulichukua zaidi ya saa mbili bila kuuona mwili wa Kusekwa. Kutokana na kina cha bonde kuwa na miti, waliamini huenda amekwama kwenye mti. Waliamua kupiga risasi ovyo kwenye miti, kwa bahati mbaya walikuwa na risasi chache hivyo walishindwa kuendelea kupiga.
Kingine kilichowachanganya ni giza lililoanza kuingia, waliamua kuondoka huku wakijipanga kwenda kuwaita vijana walinde eneo lile mpaka aonekane. Walielekea katika gari lao ili waondoke huku Mr Brown akimlaumu kijana wake kuonesha uzembe wa hali ya juu kwa kushindwa kuvumilia maumivu ya makucha ya jicho aliyopigwa na Kusekwa.
"John leo umeniangusha sana."
"Bosi ningechelewa kidogo angenitoa jicho, aliingiza kucha kwenye mboni ya jicho."
"Basi ungempigiza chini ili asikimbie kuliko kumuacha vile na kutufanya tuonekane wazembe kila siku kwa mtu mmoja. Mnaona alitoroka na mikono miwili lakini leo tumekutana naye akiwa na mkono mmoja? Tukimpoteza leo tutakutana na mzoga wake ukiwa umemalizwa viungo vyote, siyo sisi tu tunaotafuta viungo vyao, si mnajua kuna migodi mingapi?"
"Bora iwe hivyo lakini kama ataokotwa na msamaria mwema lazima atatoa siri yetu, mnafikiri kutakuwa na usalama tena kwetu? Lazima serikali itataka kufanya uchunguzi juu ya maalbino wote tuliowachukua kwa kisingizio cha kuwapeleka Ulaya."
"Usemacho ni kweli, lazima tufanye msako wa kufa mtu ili tuhakikishe tunamtia mikononi huyu mtoto la sivyo tutaumbuka," Mr Brown alizungumza akiwa amekunja uso kwa hasira.
"Ni kweli mkuu, kwa nini usipige simu mgodini ili kuleta jeshi litakalolinda eneo hili kuhakikisha huyu mtoto hatoki na kuangukia mikononi mwetu?"
"Ni kweli lakini sehemu hii haina mawasiliano kabisa, mbona ingekuwa hivyo ingekuwa rahisi kwetu?"
"Sasa tutafanyeje na usiku ndiyo unaingia?"
"La muhimu tuwahi kambini tuchukue baadhi ya watu waje hapa. Nimepata wazo jingine, bora niwaache ninyi hapa ili mlinde eneo hili mimi nitaondoka kwenda kuleta vijana wa kulinda, ambao watawapokeeni au mnasemaje?"
"Mkuu wazo zuri sana, hata mimi nilikuwa na wazo kama hilo."
"Okay, mimi niwaache ili niwahi mgodini."
Kabla hajaingia kwenye gari ili aondoke, lilitanda wingu zito lililoashiria kuteremka mvua kubwa. Mara mvua kubwa ilianza kunyesha, wote walikimbilia kwenye gari na kupandisha vioo juu. Mvua iliendelea kunyesha na kulifanya gari lao kuanza kuserereka kutokana na kulisimamisha pembeni ya bonde lile lenye udongo wa mfinyanzi.
Dereva alipoona vile, aliliwasha harakaharaka na kuweka ‘four wheel drive' kuliondoa lakini alikuwa kama ndiyo analiongeza kulitelezesha kwenda bondeni. Ilikuwa ajabu ya mwaka, kila walivyojitahidi kufungua milango ili waruke nje, iligoma kufunguka huku gari likizidi kuelekea bondeni.
Wakati huo, mvua kubwa ilikuwa ikiendelea na kusababisha maporomoko ya maji yaliyotengeneza mto kutoka juu ya mlima. Gari lilizidi kuserereka kusogea kwenye ukingo wa bonde hilo na kumfanya Mr Brown na watu wake waanze kuhaha. Gari lilikosa kizuizi na kuporomoka hadi bondeni, likaangukia kwenye maji yaliyokuwa yamejaa na kwenda kwa kasi.

Je, nini kitafuatia? Usikose wiki ijayo.
 
Wakala wa Shetani - 33-


ILIPOISHIA:
Ilikuwa ajabu ya mwaka, kila walivyojitahidi kufungua milango ili waruke nje, iligoma kufunguka huku gari likizidi kuelekea bondeni.
SASA ENDELEA...


Wakati huo mvua kubwa ilikuwa ikiendelea kunyesha na kusababisha maporomoko ya maji yaliyotengeneza mto kutokea juu ya mlima. Gari lilizidi kuserereka na kusogea kwenye ukingo wa bonde lile na kumfanya Mr. Brown na watu wake kutahayari. Gari lilikosa kizuizi na kuporomoka hadi bondeni na kuangukia kwenye maji yaliyokuwa yamejaa mtoni na kwenda kwa kasi.
Gari lilianza kuzama kwenye mafuriko ya maji yaliyotokea juu ya mwinuko, ilikuwa ajabu mvua kama ile ilikuwa haijanyesha kwa kipindi kirefu.
Haikuwa na tofauti na ile iliyonyesha wakati Kusekwa alipozaliwa.
Kila walivyojitahidi kujitoa kwenye gari walishindwa, maji yaliwafunika na kujikuta walikosa hewa, wote watano waliokuwa kwenye gari walikuwa wakifa pamoja na mkuu wao Mr. Brown.
Mvua iliyokuwa ikiendelea kunyesha ilimzindua Kusekwa aliyekuwa amekwama kwenye tawi la mti. Alipotaka kujigeuza alijikuta akiporomoka kutoka juu ya mti na kuangukia kwenye maji yaliyokuwa yakitembea kwa kasi.
Alipotua, maji yalianza kumsafirisha, alijikuta akipigania roho yake kwa kurusha mkono wake mmoja. Mungu alimsaidia aliweza kukwama kwenye rundo la majani lililokuwa limejikusanya baada ya kutolewa mbali na mvua.
Kutokana na hofu ya kupoteza maisha kumtawala, alijikuta akipoteza tena fahamu. Alilala kwenye majani mpaka alfajiri aliposhtuliwa tena na sauti za wanakijiji waliomuona.
Walimchukua na kumpeleka kwa mjumbe wa nyumba kumi ili apate hifadhi kabla ya kuhojiwa ili kujua amepatwa na masahibu gani. Kusekwa hakuamini kujiona akiwa bado yupo hai kwa yote yaliyomtokea baada ya kukutana na Mr. Brown. Kila dakika aliona miujiza ya Mungu iliyomtoa kwenye kinywa cha mauti.
Baada ya kupatiwa huduma ya kwanza kwa kupewa kifungua kinywa na kupata muda wa kupumzika walimuuliza kwa utaratibu kujua amepatwa na nini.
Kabla hajatoa maelezo yake zililetwa habari kuwa kuna gari limeangukia bondeni. Waliokwenda kulitazama walirudisha taarifa kuwa ndani ya gari wamekuta kuna maiti tano, ya Mzungu mmoja na Waswahili wanne.
Wanakijiji waliungana tena kwenda kuzichukua zile maiti na kuzileta kijijini, Kusekwa pamoja na ugeni wake naye alikwenda kuziona maiti hizo. Mawazo yake yalimtuma huenda ni Mr. Brown japokuwa kwa akili ya kawaida alijua haiwezekani.
Alipofika naye alijipenyeza kwenye kundi la watu, kingine, kilichomshtua ilikuwa kuwaona watoto maalbino zaidi ya kumi wakicheza bila hofu yoyote. Alipojipenyeza alifanikiwa kuziona sura za wabaya wake. Alipoiona maiti ya Mr. Brown aliangua kilio kilichowashtua watu wote waliokuwepo pale.
Mjumbe alimchukua Kusekwa na kumpeleka nyumbani huku akimbembeleza, lakini haikusaidia kitu aliendelea kulia. Alidhani huenda kuna ndugu yake.
"Kijana kuna ndugu yako katika wale maiti?" Kusekwa alikataa kwa kutikisa kichwa.
"Sasa nini kinakuliza?"
"Hao ndiyo walitaka kuniua."
"Kukuua?" mjumbe alishtuka.
"Ndiyo."
‘Kivipi?"
Kusekwa ilibidi aanze kumhadithia maneno mazito ya tangu kuzaliwa kwake. Mjumbe aliona maneno yale hawezi kuyasikiliza peke yake akawaita wakuu wenzake na kumuweka chini.
Kusekwa alielezea safari yake toka kuzaliwa mpaka siku ile aliyofika pale kijijini. Wote waliomsikiliza walishikwa na mshangao wasiamini alichokuwa akikisema.
"Kumbe hawa ni watu wabaya, kwa vile maiti haina adui wazikwe kaburi moja," mjumbe alisema.
Walikubaliana kuwazika Mr. Brown na vijana wake kaburi moja. Baada ya mazishi kikao cha kijiji kilikaa mara moja kupanga jinsi ya kumsaidia Kusekwa na kupeleka taarifa serikalini ili kukomesha mauaji ya walemavu wa ngozi na kufanya uchunguzi kwa taasisi zote zinazojitolea kuwasaidia wasiojiweza.
Mzee mmoja alijitolea kumlea Kusekwa na kumsomesha mpaka mwisho wa elimu yake.
Wakati huo Ng'wana Bupilipili baada ya kukimbia kwenye ile kambi alijikuta akifikia kwenye Kijiji cha Busesa alichopokelewa mwanaye Kusekwa.
Baada ya kufika alipokelewa na mzee mmoja aliyekuwa mjane na kumchukua kama mkewe.
Mpaka mwanaye Kusekwa anafika katika kijiji kile alikuwa na mtoto wa miaka mitatu na mimba juu, mmoja wa watoto wake watatu alikuwa albino.
Siku moja alisikia taarifa za kuokotwa kwa mtoto albino mwenye mkono mmoja. Jina lake na taarifa zake zilimshtua, alipatwa na shauku ya kumjua huyo mtoto.
Alikwenda hadi katika nyumba aliyokuwepo Kusekwa, akiwa na hamu ya kumuona huyo mtoto. Alipofika alimuona mtoto mwenye ulemavu wa ngozi akiwa amekaa akicheza na wenzake.
Alipomuangalia sana mwili ulimsisimka na kuamini kuwa ndiye mwanaye wa kuzaa ambaye wakati huo alikuwa na mkono mmoja.
Alijikuta akitamka kwa sauti.
"Kusekwa."
Kusekwa alishtuka na kugeuka bila kuitikia alimtazama aliyemwita, Ng'wana Bupilipili huku machozi yakimtoka alimwita huku akimfuata.
"Kusekwa mwanangu."
Kusekwa naye bila kujielewa alijikuta akinyanyuka na kwenda kumkumbatia mama yake. Ng'wana Bupilipili alijikuta akilia kwa uchungu hasa baada ya kumuona mwanaye akiwa na mkono mmoja. Watu hawakuamini historia iliyojirudia kwa watu waliopotezana kukutana tena.
Baada ya Ng'wana Bupilipili kumpata mwanaye ambaye hakuwaza hata siku moja kama kuna siku wangeweza kuonana tena, alipiga magoti na kumshukuru Mungu.
"Asante Mungu, umedhihirisha tena kuwa wewe unaweza kufanya kisichowezekana katika akili za kibinadamu. Huu muujiza ulionifanyia mbele yangu ni zaidi ya kumfufua aliyekufa, ni zaidi ya ngamia kupita kwenye tundu la sindano. Asante Mungu, asante baba, asante kwa kudhihirisha kuwa wewe ni mwanzo na mwisho."
Baada ya kushukuru alimkumbatia mwanaye na kuwafanya watu wote waone muujiza ambao Mungu ameufanya kwa yeyote anayemuamini. Alimchukua na kurudi naye nyumbani kwake.
***
Taarifa za kuwepo na migodi inayotumia nguvu za kishirikina kuua albino ili wapate mali nyingi zilipelekwa kwenye vyombo vya dola na kufuatia taarifa zile ambazo hata mkuu wa kambi aliyotoroka Kusekwa alikwisha peleka taarifa kwenye vyombo vya usalama.
Msako mkali ulifanyika katika migodi mingi na watu wote wanaoishi pembezoni mwa machimbo. Wengi walikamatwa na viungo vya albino vilivyokuwa vipo tayari kuuzwa kwa wamiliki wa migodi wenye kuabudu nguvu za giza.
Mgodi wa Mr. Brown ulitaifishwa na serikali na wote waliobakia katika mgodi huo walikamatwa na kufunguliwa kesi za mauaji. Baada ya operesheni iliyovumbua vitu vingi, serikali ilitoa tamko kwa watu wote kuwa makini na wageni wanaotumia njia za dini au uwezo wa fedha zao kuwasaidia watu huku wakifanya hujuma ya kuliteketeza taifa.
Kuanzia siku ile ulinzi uliimarika kwa albino wote. Wageni wote waliwekwa chini ya uangalizi mkali na serikali.
Kusekwa alifanikiwa kusoma akiwa na mkono mmoja na kujiunga cha chombo cha sheria cha kutetea watu wenye matatizo.
Serikali ilimuongezea elimu, sasa hivi ndiye mkuu wa kitengo cha sheria na anapata mshahara mzuri unaomuwezesha kumlea mama yake na kuwasomesha
wadogo zake.
Huu ndiyo mwisho wa riwaya yetu ila lazima tuamini kila mwanadamu ana haki ya kuishi hakuna mtu aliyeumbwa kwa ajili ya kumpatia mwenzake utajiri kupitia damu yake. Imani potofu imesababisha maisha ya wenzetu wenye matatizo ya ngozi kuwa ya wasiwasi na wengine kuongezewa vilema vya maisha au kuuawa.
Uhai wao unaonekana na waovu na kunukia kwa kila mpenda pesa. Kila apataye fedha kwa damu ya mtu huwa wakala wa Shetani ambaye ameamua kuwa mfuasi wakek wa kutenda dhambi kila siku.
Tusifanye hivyo, kila mtu ana haki ya kuishi na kufurahia maisha, siri ya utajiri si kutoa damu ya mtu bali ni kufanya kazi kwa bidii.

MWISHO.

ASANTENI KWA KUNIFUATILIA MPAKA MWISHO NINAWAPENDENI WOTE.

 
asante sana kwa hadithi yenye mafunzo na inayosadifu hali halisi ya maisha ya sasa yenye wimbi la mauaji ya walemavu wa ngozi.
 
Mbona kuna vi2 umeacha? Kiumbe wa ajabu hujamalizia life yake!
 
hadithi ni nzuri ila ungo mwingi mpaka mtunzi kajisahau alianzia wapi kudanganya maana ilivyoanza jitu la ajabu ni kusekwa ambae aliokotwa akiwa na mkono mmoja anadandia miti kama nyani sasa imeisha kusekwa huyo huyo mkuu wa sheria sijui wakati ilitakiwa ifikie ilipoanzia ndio atafute hiyo happy ending asante lkn next time mtunzi awe makini kujua tunasoma na kufuatilia uhalisia wa hadithi
 
Tumesoma ila sijafaham mkuu au ndo tusome tu hadithi ishatungwa?
 
Back
Top Bottom