WABUNGE wa Bunge la Tanzania wametaka tuhuma za kuwapo udini nchini ikiwa ni pamoja na ndani ya vyama vya siasa zishughulikiwe kwa kuchukuliwa hatua kuzikomesha. Wakichangia Makadirio ya Matumizi ya Fedha ya Mwaka 2011/12 ya Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora yaliyowasilishwa juzi na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Hawa Ghasia, walisema udini huo ukiendelea kufumbiwa macho, nchi itafika pabaya. Mbunge wa Rombo, Joseph Selasini (Chadema), alisema "mimi ni kiongozi wa Kanisa Katoliki, viongozi wanazungumzia udini na tuhuma kwa baadhi ya vyama vya siasa nashangaa hawachukui hatua. "Kama suala hili halishughulikiwi kikamilifu, huko mbele tutawatazama viongozi kwa mujibu wa dini zao, jambo hili ni baya kuliko maandamano ya Chadema ... kwa nini tuliowapa dhamana hawachukui hatua inaudhi ... Serikali ichukue hatua na suala hili lishughulikiwe haraka". Mbunge wa Mbulu, Mustapha Akunaay(Chadema), alisema suala la udini liliibuka mwaka 1992 kulipoanza mfumo wa vyama vingi vya siasa kwa watu kuchanganya dini na siasa, lakini katika uchaguzi wa mwaka jana hali ilikuwa mbaya zaidi. "Suala hilo limefikia pabaya hadi watu wanaogopa kusimamia dini zao na kulazimika kutoa salamu tatu za Asalaam aleykum, Bwana asifiwe, Tumsifu Yesu Kristo. Serikali iliangalie hilo, ili watu warudi katika hali ya zamani hakukuwa na udini," alisema. Mbunge wa Viti Maalumu, Zainab Kawawa (CCM), alisema "kwa sababu wenzangu wamezungumzia udini mimi nasema udini upo, tumeona Sumbawanga waumini 400 wa CCM wakitengwa na Kanisa Katoliki kwa sababu za kisiasa". Akizungumzia utendaji wa watumishi wa umma, Selasini alisema Watanzania wengi wanaiibia Serikali kwa kutofanya kazi, lakini wanadai mshahara ambapo alifafanua: "unawakuta wanatumia siku nzima kubishana mpira wa Simba na Yanga au wakati wa uchaguzi wanabishania vyama vya siasa, hadi wamegawanyika kwa vyama, mambo haya yanatia aibu watumishi wafanye kazi. "Hata hapa bungeni wapo wabunge wako nje hawafayi kazi, lakini baadaye wanataka mshahara". Alisema, rushwa imekithiri hasa mahakamani na Polisi, lakini Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa(Takukuru) inafumbia macho na kutolea mfano mahindi yanasafirishwa kupitia Himo kutoka nchini kwenda Kenya, huku malori yakisindikizwa na polisi wa pikipiki wakiwa na silaha. Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (Chadema), alisema tatizo la watuhumiwa wa rushwa kubwa kutochukuliwa hatua likiendelea bila kushitakiwa, wananchi watachoka na watachukua hatua ambazo hazijazoeleka. Mbunge wa Viti Maalumu, Fakharia Shomari (CCM), alisema fomu za maadili ya viongozi zinazopelekwa Zanzibar hazifuatiliwi kama zinajazwa ambapo aliongeza: "Jengo la Ofisi ya Makamu wa Rais ni kubwa, wangeomba ofisi ili ofisa mmoja awepo pale kufuatilia kujazwa kwa fomu hizo". Chanzo: Habari leo |