Binafsi nakunywa pombe mara mojamoja, naweza kupitisha mwezi sijanywa ila nikinywa huwa nalipiza siku ambazo sikunywa kabisa. Hii imenikuta wiki chache zilizopita tulikuwa na event na marafiki tunaotoka sehemu moja, kwenye pombe mbuzi anahusika nilisimamia kitengo.
Nilikunywa mpaka K Vant nikaiona kama soda, nakuja kustuka pombe imenizidi kiasi hata kutembea ilikuwa noma. Sifanyi fujo nikilewa kila mtu alifurahi lakini balaa lipo kwa ndugu zangu kujua kuwa ninakunywa. Busara ilitumika simu yangu nikaicha kwa mtu niipate nikiwa fresh.
Ase nilifanya safari ya saa 1 na nusu peke yangu nikiwa nimelewa na sijui nilifikaje nyumbani, kuja kustuka ni asubuhi niko kitandani tatizo limebaki kwa ndugu zangu. Wakati nimeacha simu kwa rafiki nilipigiwa jamaa akapokea na kuwaambia niko kwenye matatizo ile kitu ilizua taharuki watu hawajalala kuulizia hali yangu maana mimi sikupatikana tena.
Hii kitu imeniweka sehemu mbaya sana hakuna mtu anataka kunielewa tena. Ukweli nimekwama nimeamua kuacha pombe maana naona itanigombanisha na ndugu.
wakati wa Nuhu pia watu walikuwa hivi hivi. walikuwa wanakula na kunywa, wakioa na kuolewa, kifupi ni kwamba walikuwa wanakula bata, hadi siku ilipofika hawakuamini macho yao, na mlango ulishafungwa. Uishi ukijua kuna siku aidha utakufa au Yesu atarudi atakukuta, kama ulikuwa umeokoka utaurithi uzima ila ukifa au unyakuo ukija bado, utapata adhabu. Mungu amekupa nafasi hii leo, ni opportunity ya kubadili maisha yako, mrudie Mungu, onjeni muone ya kuwa Bwana yu mwema, heri mtu yule anayemtumaini Bwana, jaribu tu kuokoka, uone kama ni kubaya, uone kama kweli kunabadilisha moyo na maisha au la, wengi wanaona aibu kuokoka, wengine msingi wao wa kupata pesa umejikita kwenye njia zilizo kinyume na wokovu hivyo wanaona wakiokoka watakata mrija wa pesa, wengine wanaona ni jambo la aibu, Yesu alisema atakayenionea haya mbele za watu nami nitamwonea haya mbele za Baba, atakayenikiri mbele za watu nami nitamkiri mbele za BAba. zitafakarini njia zenu, tafakari halafu chukua hatua. Mungu awabariki.
Luka 17:26 ā 37:
YESU AKAWAAMBIA; Na kama ilivyokuwa siku za Nuhu, ndivyo itakavyokuwa katika siku zake Mwana wa Adamu. Watu walikuwa wakila na kunywa, walikuwa wakioa na kuolewa, hata siku ile Nuhu aliyoingia katika safina, gharika ikashuka, ikawaangamiza wote.
Na kadhalika, kama ilivyokuwa katika siku za LUtu, walikuwa wakila na kunywa, walikuwa wakinunua na kuuza, wakipanda na kujenga; lakini siku ile LUtu aliyotoka Sodoma kulinyesha moto na kibiriti kutoka mbinguni vikawaangamiza wote.
Hivyo ndivyo itakavyokuwa siku ile atakayofunuliwa Mwana wa Adamu. Katika siku ile, aliye juu ya dari, na vyombo vyake vimo ndani ya nyumba, asishuke ili kuvitwaa; na kadhalika, aliye shambani asirejee nyuma. Mkumbukeni mkewe Lutu. Mtu yeyote atakaye kuiponya nafsi yake ataiangamiza; na yeyote atakayeiangamiza ataiponya. Nawaambia, usiku huo watu wawili watakuwa katika kitanda kimoja, mmoja atatwaliwa, mmoja ataachwa. Wanawake wawili watakuwa wakisaga pamoja, mmoja atatwaliwa, mmoja ataachwa. Watu wawili watakuwa shambani, mmoja atatwaliwa mmoja ataachwa. Wakajibu wakamwuliza, wapi Bwana? Akawaambia, ulipo mzoga ndipo watakapokutanika tai.
Soma pia Mathayo 24:37.- 38
37 Kama ilivyokuwa wakati wa Nuhu, ndivyo itakavyokuwa atakaporudi Mwana wa Adamu. 38 Kwa maana siku zile kabla ya gharika, watu walikuwa wakila na kunywa, wakioa na kuolewa, mpaka siku ile Nuhu alipoingia kwenye safina.