VIPEPEO WEUSI: MKAKATI NAMBA 0034
EPISODE 11
GEREZA KUU LA MKOA, MOROGORO.
SIKU YA KWANZA
Ilikuwa yapata saa kumi na mbili asubuhi. Mda mchache uliopita waumini wa kiislamu ndani ya selo walikuwa wamemaliza kuswali na sasa watu walikuwa wamekaa kwenye magodoro wanapiga stori tunasubiri kuja kufunguliwa selo tuelekew yard ili kuanza siku nyingine ndani ya gereza.
Selo yetu ambayo ni 'Namba 2 kubwa' ilikuwa na urefu wa takribani kama mita nane kwa urefu na mita tatu upana.
Jana jioni saa kumi tulivyoingia nilimuona nyapala wa selo amendika mlangoni 53. Akimaanisha kuwa jumla ya wafungwa na mahabusu 53 siku hiyo tumefungiwa ndani ya selo namba mbili kubwa.
Wafungwa na mahabusu wote isipokuwa manyapara tulikuwa tunalalia godoro moja watu wawili. Godoro lilikuwa na ukubwa wa kama inch tatu kwa tank hivi.
Mimi na Godi tulishea godoro moja na staili rasmi ya wafungwa wote kulala ni 'mzungu wa nne'.
Usiku wa jana nilikuwa nimeenda chooni kilichopo ndani ya Selo na kuitoa ile karatasi niliyopewa na Baba Bite. (Kwa mara nyingine, siwezi kamwe kuelezea namna nilivyoitoa).
Nilisoma kilichopo ndani, na ingawa siku kielewa lakini yanipasa kukifanyia kazi kama Baba Bite alivyonieleza kuwa "itanisaidia kusurvive humu ndani."
Toka jana mda tunaingia ndani ya selo nilipomuuliza Godi kuhusu Eric Kaburu, kwa kiasi fulani alikuwa amenichunia na hataki kabisa maongezi na mimi.
Watu walikuwa wanapiga soga kila upande lakini mimi na Godi tulikuwa kila mtu yuko kwenye dimbwi la mawazo.
Nikaona nivunje ukimya.
"Braza naona toka jana nikutajie jina la Kaburu, umebadilika kabisa! Ingekuwa poa ukinidokeza hata kidofo hofu yako ni nini badala ya kuninunia kama mtoto wa kike" nikamueleza kwa sauti ya kihuni Fulani hivi, jela ilikuwa imeanza kunikaa kwenye damu.
"Sitakueleza hofu yangu ni nini, ila nitakuonyesha!" Godi akaongea akiwa serious kweli kweli bila kuniangalia usoni.
"Una maana gani??" Nikamuuliza kwa mshangao.
Hakunijibu chochote akaendelea kukaa kimya tu anaangalia pembeni.
Mara nikamsikia Nyapara wa selo anaongea kama anatangaza kwenye kipaza sauti, "kaa kwenye mstari weweeeeeee, kaa kwenye mstariiiiiii."
Wafungwa wote na mahabusu tukainuka na kupanga mstari kuelekea mlangoni.
Kisha akaja askari magereza akasimama kule mbele mlangoni baada ya kuufungua. Na kama jana jioni tukaanza kuhesabiwa tena kama ng'ombe tunatoka zizini.
"Mda wa mazoezi ya viungo huu na mchakachaka, tukimakiza kabla ya kunywa uji nitakuonyesha kwanini sitaki kumuongelea Kaburu!" Godi akaongea huku anatembea bila kuniangalia mara tu tulipotoka ndani ya selo.
Tukaelekea mpaka kule kwenye yard ya pili, kwenye uwanja mkubwa ambako hakuna TV. Tukawakuta wafungwa wanaolala selo ndogo wote wameshafunguliwa milango na wako yard wanakimbia mchaka mchaka kuuzunguka mwembe.
Utaratibu ni kwamba ukifika tu pale na wewe 'unaunga tela' kukimbia mchaka mchaka. Mbele alikuwa ametangulia askari magereza anaimbisha na wafungwa wanaitikia.
Yule askari alikuwa anaimbisha wimbo ambao ulinikumbusha mbali sana, enzi za utoto.
"Zaina zainaaaaaaa"
"Zainaaaaaaaaaaaa" wafungwa wanaitikia.
"Zainabu wanguuuuuuu"
"Zainaaaaaaaaaaaa" wafungwa wanaitikia tena.
"Mtoto wa kihayaaaaaaaaa"
"Zainaaaaaaa! Lete raha zainaaaaa!!" Wafungwa.
"Ukimuona zainaaaaaaa"
"Zainaaaaaaaaaaa"
"Mtoto ziwa konziiiiiiiii" askari magereza anaweka mbwembwe. Na wafungwa wanaitikia kwa furaha "lete raha zainaaaaaaa."
Mimi, Godi na wafungwa wenzetu tunaolala selo kubwa tulifika pale yard yapata kama saa kumi na mbili na dakika kumi hivi na tukaungana na wenzetu kwenye mchaka mchaka huo kwa takribani dakika ishirini hivi tukizunguka pale yard na kuuzunguka mwembe.
Baa ya hizo dakika ishirini za mchaka mchaka wote tukakusanyika mbele ya ule mwembe ambapo kulikuwa na kama 'kibaraza' hivi kimejengwa kimeinuka juu kidogo na yule askari akapanda pale juu ya kibaraza na kuanza kuimbisha nyimbo za "kijeshi".
Alipokuwa anaimbisha tulikuwa tumejipanga kama vile wanafunzi wako 'assemble' na tulikuwa tunaimba huku tunaruka kama wanajeshi kweli kweli.
Kukupa picha kamili, niseme kwamba naamini umewahi kuona jinsi wanajeshi wale 'makomando' kwenye sherehe za Uhuru pale uwanja wa taifa wakimaliza 'show' yao ya kuvunja mawe kwa kichwa na kulala juu ya misumali (sijui ukomando wa wapi huu?? Kama mazingaombwe!!) Huwa wanapita mbelw ya rais na wageni waalikwa jukwaa kuu wakiruka ruka kama wanakimbia. Basi hicho ndicho nasi tulikuwa tunakifanya hapa jela kwenye haya mazoezi. Tulikuwa tunaruka ruka kama makomando wa uwanja wa taifa huku nyimbo za halaiki zinaimbwa na yule askari magereza.
"Arereeeeeeeeeeee"
"Haiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiii" wafungwa wanaitikia
"Arereeeeeeeeeeee"
"Haiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiii"
"Chini kuna motooooo"
"Kanyagaaaaaaaaaaa" wafungwa wanaotikia.
"Chini kuna motooooooooo"
"Kanyagaaaaaaaaaaaa"
Hiyo mkiimba "kanyagaaaaa" unatakiwa unyanyue mguu juu kweli kweli kama komando kweli. Uzuri mimi ni mtu wa mazoezi kwahiyo nikawa nanyanyua mguu karibu ufike kidevuni.
Wakati huo maaskari wengine wanakuwa wanapita pita huku na huko kuangalia wafungwa wanaotegea. Kwahiyo kila baada ya sekunde chache unasikia "paaaaaaaaahh". Mtu amepigwa "salala" kama wanavyoita gerezani, kofi la haja la mgongoni mpaka unasikia kama ngozi inabanduka.
Nilichokuja kugundua muda huu wa mazoezi ndio moja ya muda unaopendwa sana na wafungwa. Kwani kwa kuangalia tu nyuso za watu walikuwa na furaha na kwa muda mchache walikuwa wamesahau kuwa "hawana maisha" kwa maana ya maisha. Na mimi nikaanza kusikia kifuraha fulani hivi kinaniingia na sikupenda kabisa, lakini nilishindwa kujizuia. Aliyeanzisha huu mfumo wa mchaka mchaka na mazoezi gerezani ni 'genius' anastahili nishani ya heshima. Msongo unaondoka kwa mfungwa bila mwenyewe kutaka.
Baada ya yule askari kumaliza kutuimbisha kijeshi akapanda askari mwingine mfupi hivi mwenye mbwembwe kibao na alivyopanda tu wafungwa wakaanza kushangilia. Huyu askari nilikuja kumfahamu hapo baadae kuw anaitwa jina la utani 'Msauzi' na alikuja kunisaidia sana huko mbeleni kutimiza azma yangu iliyonileta humu gerezani.
Msauzi akaanza mbwembwe zake.
"Wiiiiiiiiiiiiiiiii"
"Waaaaaaaaaaaaaaa" wafungwa wakaitikia.
Akaanza kuimbisha nyimbo zake za "kihuni".
"Ptruuuuuuuuuu wekaaaa"
"Wekaaaaaaaaaaaaa" wafungwa wakalipuka na kujibu kwa sauti.
"Niweke vodaaaaaa??"
"Wekaaaaaaaaa" wafungwa wanaitikia.
"Niweke zeniiiiiiiiiii??"
"Wekaaaaaaaaaaa"
"Niweke tigoooooooo??"
"Aaaaaaaaaaaaaaahh" wafungwa wanakataa kuitikia kwa utani.
Kisha anaanza tena mwanzo. Akaimbisha hizi nyimbo za "kihuni" kwa karibia robo saa, na kwakweli nilisikia raha sana. Umepita mda mrefu tangu nijihisi kufanya "uhuni" walau kidogo. Roho yangu ikasuuzikasijakaa,
Baada ya 'mchaka mchaka' na mazoezi kuisha watu wakaanza kujiandaa kwenda kunywa uji.
Tukarudi mpaka kule jikoni upande wenye selo kubwa. Nikachukua kikombe cha bati kama wenzangu na kupanga foleni, kisha nikawekewa uji wangu wa dona, na ninaposema dona ni dona kweli kweli, uji hata rangi yake sijui ni rangi gani. Chukua njano changanya na nyeusi rangi utakayopata ndiyo hiyo hiyo niliyokuwa naiona kwenye kikombe changu cha uji.
Baada ya kuwekewa uji nikarudi yard namba mbili kule kutafuta sehemu ya kukaa niburudike na kifungua kinywa chabgu huku kichwani nikipanga nifanye mini.
Nilipofika yard kabla sijakaa chani, ghafla nikamuona Godi anakuja kwa kasi pale nilipo.
"Twende" akaongea huku anatembea haraka haraka bila kuniangalia.
"Twende wapi?" Nikamjibu bila kunyanyua hatua hata moja.
Akagueka na kunifata kwa kasi mpaka pale nilipo.
"Uliniuliza kwanini nilikuwa na hofu uliponitajia jina la Kaburu, nikakwambia sitakwambia kwanini Bali nitakuonyesha! So twende nikuonyeshe kwanini sitaki kusikia hill jina" akaongea kwa hasira huku anageuka na kuanz kuondoka.
Nikaweka kikombe cha uji chini na kuanza kumfuata.
Tukaelekea mpaka kwenye ule 'uchochoro' ambao ukipita unatokea yard ya kwanza, uchochoro ambao pia unatumika kama bafu.
Tulipofika hapo akasimama. Tulikuwa peke yetu.
"Umeona pale!" Akanionyesha mahali Fulani ukutani.
"Sioni kitu naona ukuta tu na ukungu wa kijani" nikamjibu. Nilijitahidi kukaza macho ukutani lakini kitu pekee nilichokiona ni ukungu wa kijani uliotokana na watu kuoga mahali hapo.
"Angalia pale juu kidogo"
Nikatazama kwa umakini zaidi. Kuna sehemu ilikuwa na kama alama kubwa nyekundu ambayo imebadilika kiasi na kuwa kama nyeusi kutokana na kukaa muda mrefu.
"Yeah nimeona kama damu hivi nahisi"
"Sio unahisi, hiyo ni damu! Damu ya binadamu" akanijibu huku ananiangalia kwa hasira. "Sogea cheki na hapa" akanionyesha sehemu nyingine kwenye kona ya ukuta inapokutana na ukuta mwingine.
"Umeona hapa?" Akanionyesha.
Sehemu ya chini kidogo kulikuwa na alama kubwa ya kama kitu kimechuruzika ukutani.
"Nahisi ni damu pia"
"Pimbi wewe, sio unahisi! Hiyo ni damu! Damu ya binadamu!" Akanijibu tena huku ananiangalia kwa hasira.
"Unaweza ukanambia kwanini unanionyesha damu za binadamu?" Nikamuuliza kwa hofu.
"Ile damu pale juu maiti ya mfungwa ilikutwa hapa mwaka mmoja uliopita! Inaonekana kuna mtu alimuinua juu juu na kumbamiza Kisogo ukutani mpaka akafa!" Akaongea kwa jazba. "Hiyo damu hapo chini miezi mitatu au minne iliyopita nikiwa humu humu jela, mfungwa mwingine alikutwa amechinjwa na mzoga wake umeegemezwa hapo hapo ukutani!! Unajua wote kosa lao lilikuwa nini?" Akauliza huku amefura kwa hasira.
"Walikuwa na kosa gani?" Nikamuuliza kwa hofu na unyonge.
"Walikuja humu gerezani wakaanza kumuulizia na kuchunguza chunguza kuhusu Eric Kaburu! Na hiki ndicho kilichowapata na kwa mujibu wa magereza waliotemnda hayo mambo 'hawajulikani' mpaka leo hii" Godi alikuwa na hasira mpaka anatetemeka.
"Kwahiyo nakuambia hivi! Kuanzia sasa sitaki unisemeshe wala kunijua jua humu jela! Endelea na using* wako kumuulizia Kaburu sitaki unijue" akaongea kwa hasira huku anaondoka, lakini ghafla akageuka na kunifuata tena kama kuna kitu amekumbuka, "na kwa kuwa umedhamiria kufa wacha nikusaidie! Ukitaka kuonana na Kaburu muda pekee unao weza kumuona ni muda wa uji pekee anakuwa yuko yard ya kwanza! Baada ya hapo huwezi kumuona mpaka muda wa kaba selo.! So nakushauri uende sasa ukajichimbie kaburi" akaongea nan kutoa kicheko cha dharau chenye hasira ndani yake na kuondoka.
Nikabaki nimeduwaa pale nimepigwa na bumbuwazi. Kwa dakika kadhaa sikuweza kutingishika nikabaki nimekodolea macho zile sehemu zenyw damu nilizoonyeshwa na Godi.
Nikakumbuka sentesi yake ya mwisho "ukitaka kumuona Kaburu muda pekee unaoweza kumuona na muda wa kunywa uji anakuwa yard ya kwanza."
Nikajikaza kiume. Nikatembea kutola kwenye uchochoro huo mpaka nikatokea yard ya kwanza.
Niaanza kupepesa macho kumtafuta Kaburu ni wapi alipokaa. Nikamuona ameketi mbele kabisa kwenye yard mahali wanapoangalia TV akiwa amekaa na kikombe chake cha uji mkononi.
Nikakumbuka usia niliopewa na Godi kuhusu jinsi watu walivyouwawa kwa kumfata fata Kaburu na kumuulizia. Nikakumbuka pia maneno niliyoambiwa na kaburu mwenyewe siku ya kwanza tulipoonana alinambia "usije tena hapa kwa usalama wako na wangu."
Nikajiuliza nifanyeje? Niachane na mpango wa kuonana nae na kuzungumza naye? Nikifanya hivyo tabu yote hii niliyoipata mpaka kuingia jela itakuwa na faida gani??
Hapana, nimekula ng'ombe mzima wacha nimalizie mkia.! Liwalo na liwe..
Sikujua niongee nae nini au nitasema kitu gani lakini nikaamua kuwa huu ndio muda wa mimi kumkabiri Kaburu.
Nikatembea kumfuata pale alipo na kusimama nyuma yake.. Kaburu hakugeka ila nilikuwa na hakika alikuwa amehisi nimesimama nyuma yake! Akaweka chini kikombe cha uji.. moyo ukanipasuka!!
Itaendelea Jumanne Ijayo..
13:3+msng