Video: Tukio la uvamizi Igunga

TAHARUKI kubwa ilizuka usiku wa kuamkia jana baada ya milio ya risasi na kelele za wafuasi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo kusikika katikati ya viunga vya mji wa Igunga.

Watu walioshuhudia mkasa huo walisema wabunge wawili wa CCM, Esther Bulaya (Viti Maalumu) na Aeshi Hillary (Sumbawanga Mjini) ndio waliofyatua risasi hizo, karibu na Hoteli ya Misana walikofikia viongozi waandamizi na makada wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).

Hata hivyo, habari za kutatanisha zimeonesha kuwa chanzo cha vurugu hizo kimetokana na vijana wa CCM kutaka kuyachoma moto magari mawili ya CHADEMA yanayotumika katika kampeni usiku wa kuamkia jana.

Imedaiwa kwamba vijana kadhaa walionekana wakishuka kutoka ndani ya magari mawili ya wabunge wa CCM waliokuwa wakitoka disko majira ya saa saba usiku na kuelekea yalikoegeshwa magari ya CHADEMA kwa kificho.

Habari zimedai kwamba walinzi wa CHADEMA walioshuhudia tukio hilo baada ya kugundua njama hizo waliyazingira magari mawili ya wabunge hao, yenye namba za usajili T 540 BSZ, Land Cruiser Prado, mali ya Esther Bulaya na T 399 BBV Land Cruiser linalomilikiwa na Aeshi Hillary, na ndipo vurugu kubwa ilipozuka kiasi cha kusababisha matumizi ya risasi.

Mratibu wa Kampeni za CHADEMA katika Jimbo la Igunga, Mwita Mwikabe Waitara, alisema vijana waliokuwa na wabunge wa CCM walivamia hoteli wanayoishi viongozi wa CHADEMA na kutaka kuchoma moto magari mawili ya matangazo yanayotumiwa na chama hicho.

Aliongeza kuwa alikuwa ndani wakati sakata hilo linaanza, lakini baada ya kutoka nje alikuta tafrani hiyo huku gari la Aishe likiwa chini ya ulinzi wa vijana wa CHADEMA.

Aliongeza kuwa baada ya polisi kufika, yeye na vijana wengine wa CHADEMA waliongozana nao hadi kwenye ofisi za polisi kutoa taarifa ya uvamizi huo lakini cha ajabu aliwekwa ndani.

“Esther alikuja pale kituoni huku akiwatukana polisi na kuwaambia polisi eti mimi ndiye niliyekuwa na bastola, nao waliamua kunishikilia kwa muda,” alisema.

Hata hivyo, madai hayo ya CHADEMA yamekanushwa na Mbunge wa CCM, Esther Bulaya, akidai kuwa hakurusha risasi hewani, bali aliyefanya hivyo ni kiongozi wa CHADEMA, Mwita Waitara.

Esther amesema akiwa njiani kutoka matembezini, wakati akikaribia katika Hoteli ya Peak Lodge wanakoishi, alishtushwa kuona gari aina ya Pick up Hilux lililokuwa na bendera ya CHADEMA likimfuatilia.

“Nilikuwa natoka Silent Inn, nikaona gari inanifuatilia kabla sijaingia njia ya kwenda Peak nilikofikia, nikapitiliza kama naenda Singida, bado wakawa wananifuata huku wakilipiga gari langu kwa mawe na risasi,” alisema na kuongeza kuwa baada ya kuona hali hiyo, alilazimika kumpigia simu Mbunge mwenzake, Hillary, aje kumsaidia.

“Nilipompigia mwenzangu akanambia anakuja kunisaidia na amewapigia simu polisi kuomba msaada zaidi, ndipo wale watu wakakimbia porini,” alisema Esther.

Alikana kutumia silaha, badala yake akasukuma lawama hizo kwa Waitara wa CHADEMA. “Aliyerusha risasi ni Waitara. Nimememwona,” alisema Esther alipoulizwa iwapo alimwona mtu aliyekuwa akirusha risasi hizo.

Akizungumzia suala hilo, Mkuu wa Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathmini, Naibu Kamishna wa Polisi, Kamanda Issaya Mungulu, alikiri kutokea kwa vurugu hizo zilizosababisha uharibifu wa mali na mtu mmoja kujeruhiwa.

Kamanda Mungulu alisema vurugu hizo zilitokea kati ya saa saba na saa tisa usiku na kutaja magari yaliyoharibiwa kuwa ni namba T 540 BSZ Land Cruiser Prado mali ya Esther na T 399 BBV Land Cruiser Prado mali ya Aeshi.

Kutokana na tukio hilo la kutatanisha polisi wilayani Igunga imewahoji watu watano wakiwamo wabunge wawili wa CCM, Esther Bulaya, Aeshi Hillary (Sumbawanga Mjini) na viongozi wawili waandamizi wa CHADEMA, Mwita Mwikabe Waitara na John Heche pamoja na Ramadhan Twaha.

CCM yatoa msimamo

Akitoa msimamo wa CCM kuhusu matukio ya vurugu zinazojitokeza tangu kuanza kwa kampeni hizo, Mkurugenzi wa Kampeni wa CCM katika uchaguzi huu, Mwigulu Mchemba, aliwaonya wafuasi na uongozi wa CHADEMA kufuata kanuni na maadili ya sheria za uchaguzi.

“Watanzania wote tunatakiwa kulaani kwa sababu si vitendo vya kiungwana. Tunatoa rai kwa wenzetu waache tabia hiyo, lakini pia kwa vyombo vya dola kuchukua hatua mara moja wakipata ushahidi wa kutosha,” alisema na kuongeza:

“Si kwamba hatuwezi kujibu, kwa takwimu wana CCM Igunga ni wengi kuliko wafuasi wa vyama vingine. Hatutaki kuigeuza Igunga kuwa uwanja wa mapambano wala vita. Leo hii tungeamua kujibu, sidhani kama kuna duka lingefunguliwa,” alisisitiza Mwigulu.

Lissu awaonya Polisi

Naye Mkurugenzi wa Katiba na Sheria wa CHADEMA, Tundu Lissu, alisema Aeshi ndiye aliyetumia bastola hiyo kwenye vurumai hizo, lakini kwa sababu polisi wanafanya kazi kama kitengo cha CCM, wameshindwa kumchukulia hatua.

“Wabunge wa CCM wanatembea na bastola waziwazi na sasa wameanza kuzitumia. Badala ya kumweka ndani Aeshi kama walivyowaweka wabunge wetu wamemwachia na bastola anayo,” alisisitiza Lissu na kuongeza kuwa Jeshi la Polisi linatumika kama mkono wa mabavu wa CCM.

Zitto atikisa Igunga

Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA, Zitto Kabwe, jana alipokewa kwa maandamano makubwa na kusema CCM inaanza kupiga kelele na kufanya vurugu baada ya kuona hatari ya kulipoteza jimbo.

“Jamani CCM wanahaha, wanajua moto wetu hawauwezi ndiyo maana kila kukicha wamekuwa na propaganda za kipuuzi, dawa yao ni kumpa kura mgombea wa CHADEMA, Joseph Kashindye,” alisema huku akishangiliwa na idadi kubwa ya watu waliohudhuria kwenye mapokezi hayo. Zitto alisema kama wana Igunga watamchagua mbunge mbovu, kero za maji, barabara na nyinginezo zitaendelea.

Rage aanza kuchunguzwa

JESHI la Polisi limesema uchunguzi dhidi ya Mbunge wa Tabora Mjini, Ismail Aden Rage (CCM), kuhutubia mkutano wa kampeni za uchaguzi mdogo wa ubunge wa Igunga akiwa na bastola umeanza.

Akizungumza na waandishi wa habari, Mkuu wa Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathmini, Naibu Kamishna wa Polisi, Kamanda Issaya Mungulu, alisema suala la Rage linashughulikiwa kwa makini kutokana na kuwapo kwa sheria za umiliki wa silaha.

“Tumeanza kumhoji kwa nini alifanya hivyo na uchunguzi utakapokamilika, tutatuma kwa wataalamu wa sheria watoe ufafanuzi.

“Watatuambia katika hali ile inakuwaje ili mradi kama mtu anamiliki kihalali na kama mnavyohoji kuwa wananchi watatishika au wanatishika kwa kuiona silaha hiyo,” alisisitiza Kamanda Mungulu.

Hata hivyo, Tundu Lissu ambaye ni Mkurugenzi wa Katiba na Sheria wa CHADEMA amesema ni marufuku kuwa na silaha yoyote katika mkutano wa kampeni kwa mujibu wa Ibara ya 2.2C ya Maadili ya Uchaguzi ya mwaka 2010 ambayo imefanyiwa marekebisho hivi karibuni.

“Leo tumepeleka malalamiko yetu kwa msimamizi wa uchaguzi na CHADEMA tumeomba mgombea wa CCM na chama chake kwa ushahidi huu waondolewe kwenye kampeni hizi kama ambavyo sheria za nchi zinavyoelekeza.

“Hawa wanafikiria kwa kuwa ni chama tawala wanaweza kufanya lolote wanalotaka, tunaomba mwenyekiti wa kamati ya maadili ya jimbo asikilize hili, maana ni lalamiko letu la tatu lakini hatujaitwa kutoa ushahidi wetu.

“Hili la kukalia malalamiko litatupeleka pabaya na sisi hatupo tayari kuona watu wetu wanavamiwa usiku, tunapeleka malalamiko polisi hayachukuliwi hatua,” alisema Lissu.

Hivi karibuni akiwa kwenye Kata ya Igurubi wakati wa mkutano wa hadhara akimnadi mgombea ubunge wa CCM, Dk. Dallaly Kafumu, Rage alionekana akiwa na bastola kiunoni, jambo linalodaiwa ni kinyume cha maadili ya kanuni za uchaguzi.
 
Polisi wanatumikia kafiri ili wapate mradi wao, lakini siku zao zahesabika kitaeleweka tu
 
Wenzao huwa wanaanza kuzeeka mwili ndio zifuate akili sasa CCM wameshazeeka vyote kwa pamoja! kaaazi kweli kweli siasa za uzeeni hizo!
 
Mwigulu Kama alikana kufumaniwa itakuwa hili la bastola na vurugu hawezi kukiri Hilo loss lazima awatupie chadema.
 
Nashauri kuwa this time Viongozi wa CHADEMA wakikamatwa tena na Polisi wa CCM watumie fursa hio kupiga kampeni kwa polisi hao kuwaeleimisha madhara yake, kwa mfano pale alipokamatwa Mwita angetumia fursa hio kuwa"tongoza" polisi hao wahamie CHADEMA.
 
Nashauri kuwa this time Viongozi wa CHADEMA wakikamatwa tena na Polisi wa CCM watumie fursa hio kupiga kampeni kwa polisi hao kuwaeleimisha madhara yake, kwa mfano pale alipokamatwa Mwita angetumia fursa hio kuwa"tongoza" polisi hao wahamie CHADEMA.

Kweli hawa polisi vihiyo wanaitaji elmu
 
Nashauri kuwa this time Viongozi wa CHADEMA wakikamatwa tena na Polisi wa CCM watumie fursa hio kupiga kampeni kwa polisi hao kuwaeleimisha madhara yake, kwa mfano pale alipokamatwa Mwita angetumia fursa hio kuwa"tongoza" polisi hao wahamie CHADEMA.

watendaji wengi wa jeshi la polisi-wale wasio na vyeo hasa wanaotambulika kama PC hawaipendi CCM, lakini viongozi wao kuanzia OCS hadi RPC, wengi ni CCM, kwani wao maslah yao ni mazuri na kwa kuwa siasa za CCM zina nguvu kwa viongozi hao, wanalazimika kutekeleza maelekezo ya CCM kwa kuhofia kunyang'anywa vyeo vyao walivyonavyo-ni mbumbu kiihivyo.

Askari wadogo wanapopewa amri nao wanalazimika kutekeleza, kwani wanaogopa kushitakiwa kijeshi
 
Nashauri kuwa this time Viongozi wa CHADEMA wakikamatwa tena na Polisi wa CCM watumie fursa hio kupiga kampeni kwa polisi hao kuwaeleimisha madhara yake, kwa mfano pale alipokamatwa Mwita angetumia fursa hio kuwa"tongoza" polisi hao wahamie CHADEMA.

mtumba inu nee mbui, polisi njaa zinawaua na uwepo wa nidhamu ya woga lakini wanaijua kweli.
 
Back
Top Bottom