ila ukweli ni kwamba, kuna msabato yeyote aliwahi kujazwa Roho Mtakatifu akanena kwa lugha kama walivyofanya mitume siku ya pentecost na waamini wa awali waliohubiriwa nao? ukijibu hilo niite, nimekaa paleee.
Kunena kwa lugha huku mnakofanya , Shakarobobokakaaa risikakaaa au unazungumzia vipi ?
Maana Geo Devi, Mackenzie, gwajima, mashimo, mwamposa , nabii Tito, mwingira , na matapeli wote wanaojiita manabii wanaongea hizo Lugha
Ndio kunena kwa lugha unakomaanisha au ?
Maandiko yanasema hivi kuhusu kunena kwa lugha
Mara nyingi kumekuwa na mizozo kati ya muumini na muumini, na kati ya dhehebu na dhehebu juu ya kunena kwa lugha. Yako baadhi ya makanisa muumini asiponena kwa Lugha anaambiwa hana Roho mtakatifu, na hivyo imewapelekea baadhi ya watu kukata tamaa hata ya kusali kisa kaambiwa hana Roho Mtakatifu kwa sababu Haneni kwa Lugha, Jambo ambalo si kweli kwamba mtu asiponena kwa lugha hana Roho Matakatifu, Huo ni uwongo tu.
Nini maana ya LUGHA?
LUGHA: ni mpangilio wa maneno yenye kuleta maana kwa mzungumzaji na msikilizaji. Ina maana kwamba ikiwa mtu ananena maneno lakini hayaleti maana yoyote hiyo sio Lugha bali ni machafuko.
1 Wakorintho 14:10-11
"Yamkini ziko sauti za namna nyingi duniani, wala hakuna moja isiyo na maana. Basi nisipoijua maana ya ile sauti nitakuwa kama mjinga kwake yeye anenaye; naye anenaye atakuwa mjinga kwangu."
Kwa hiyo Lugha sahihi ni lazima ilete maana.
KUNENA KWA LUGHA, ni kutamka maneno ambayo ni mageni/ mapya kwa mzungumzaji au kwa msikilizaji Au ni kuzungumza lugha yoyote ambayo ni ngeni kwa mzungumzaji au msikilizaji.
CHIMBUKO LA KUNENA KWA LUGHA:
Zamani hakukuwa na makabila kama ilivyo siku hizi, Lakini tunapata chanzo cha makabila katika kitabu cha mwanzo sura ya 11, wakati watu walipojenga mnara wa Baberi, na Mungu ili kuzuia ule uasi ikabidi achafue lugha yao na washindwe kuelewana:
Mwanzo 11:7
"Haya, na tushuke huko, tuwachafulie usemi wao ili wasisikilizane maneno wao kwa wao."
Mwanzo 11:9
"Kwa sababu hiyo jina lake likaitwa Babeli; maana hapo ndipo Bwana alipoichafua lugha ya dunia yote; na kutoka huko Bwana akawatawanya waende usoni pa nchi yote."
Kwa hiyo kunena kwa Lugha pia inaweza ikawa ni Machafuko, pindi endapo kuna kuwa hakuna utaratibu maalumu wa kunena au kukosa maelewano katika unenaji wa lugha:
1 Wakorintho 14:27
"Kama mtu akinena kwa lugha, wanene wawili au watatu, si zaidi, tena zamu kwa zamu, na mmoja na afasiri."
1 Wakorintho 14:33
"Kwa maana Mungu si Mungu wa machafuko, bali wa amani; vile vile kama ilivyo katika makanisa yote ya watakatifu."
Na ndio maana Paulo anasema;
1 Wakorintho 14:23
"Haya! Ikiwa kanisa lote limekusanyika pamoja, na wote wanene kwa lugha, kisha ikawa wameingia watu wajinga au wasioamini, je! Hawatasema ya kwamba mna wazimu?"
Sasa wapo watu hunena lugha ambazo hazieleweki kwa wasikilizaji na pia wao wenyewe hawajui wananena nini, ukiwauliza wanadai kwamba hizo ni lugha za Malaika ambazo hata shetani hajui:Ukweli ni kwamba Hakuna lugha ambayo shetani haifahamu na pia tukumbuke kwamba Shetani kabla ya kuanguka alikuwa ni kiongozi wa Malaika Mbinguni na hivyo anafahamu kila kitu. Kwa hiyo hauwezi ukamficha shetani lugha yoyote.
Na ikiwa lugha hizo zinazonenwa ni lugha za Malaika mbona hatuoni manabii wa zamani wakinena kwa Lugha walipotokewa na malaika? Au Yesu mwenyewe mbona hatuoni mahali popote akinena hizo lugha za malaika?
AINA ZA KUNENA KWA LUGHA:
Zipo aina tatu za Kunena kwa Lugha:
1. NI KUNENA KWA LUGHA PASIPO KUTOA MANENO:
Mfano:
Mpo watu kadhaa mahali na mmoja wenu inabidi aombee chakula, Lani yeye hatoi sauti bali anaomba kwa moyoni: Huko ni kunena kwa lugha maana wengine hawaelewi nini kilichoombwa, ijapokuwa muombaji anajua alichokiomba, hapo anakuwa amejifaidisha mwenyewe:
1 Wakorintho 14:2
"Maana yeye anenaye kwa lugha, hasemi na watu, bali husema na Mungu; maana hakuna asikiaye; lakini anena mambo ya siri katika roho yake."
1 Wakorintho 14:16
" Kwa maana wewe ukibariki kwa roho, yeye aketiye katika mahali pa mjinga ataitikaje, Amina, baada ya kushukuru kwako, akiwa hayajui usemayo?"
Mfano mwingine ni:
Hana wakati alipokuwa anamuomba Mungu apate mtoto, alikuwa akiomba kwa moyo pasipo kutamka maneno bali mdomo ulikuwa ukichezacheza, mpaka Eli akasema Hana amelewa:
1 Samweli 1:13-15
"Basi Hana alikuwa akinena moyoni mwake; midomo yake tu ilionekana kama anena, sauti yake isisikiwe; kwa hiyo huyo Eli alimdhania kuwa amelewa.
Ndipo Eli akamwambia, Je! Utakuwa mlevi hata lini? Achilia mbali divai yako.
Hana akajibu, akasema, Hasha! Bwana wangu, mimi ni mwanamke mwenye roho ya huzuni, mimi sikunywa divai wala kileo, ila nimeimimina roho yangu mbele za Bwana."
Mfano:
Hana angekuwa mtu mwingine angeweza kumjibu vibaya Eli, kwa kuambiwa kwamba amelewa, wakati yeye anaomba, na matokeo yake yangetokea machafuko.
2. KUNENA KWA LUGHA KWA SAUTI:
Aina hii ya kunena kwa lugha ni kuzungumza/kuomba kwa lugha yoyote ambayo ni ngeni kwa mzungumzaji au msikilizaji. Aina hii ya kunena kwa Lugha ndio ambayo wakati Fulani inahitaji mtu wa kutafsiri ili kila mtu aliyepo aelewe ni nini Kilichonenwa/kuombwa.
1 Wakorintho 14:27-28
"Kama mtu akinena kwa lugha, wanene wawili au watatu, si zaidi, tena zamu kwa zamu, na mmoja na afasiri. Lakini asipokuwapo mwenye kufasiri na anyamaze katika kanisa; aseme na nafsi yake tena na Mungu."
NOTE:
Kanisa la Korinto lilikuwa ni kanisa lililokuwa linakusanya waumini wa mataifa mbalimbali, kwa sababu Korintho ulikuwa ni mji wa biashara, na hivyo waumini wa Mataifa mbalimbali walipokuwa wakikusanyika Kanisani kwa ajili ya ibada kila mtu alitaka atumie lugha yake kwenye ibada aidha katika kuhubiri au katika kuomba, na hivyo Paulo anawaonya kwamba ikiwa kuna mtu anataka kutumia lugha yake kunena na kanisa, basi ahakikishe yupo mtu atakaye tafsiri hiyo lugha yake kwa watu wengine, lakini kama hakuna mtu wa kumtafsiria basi atulie tu asinene lolote.
3. KUNENA KWA LUGHA NGENI ISIYO YAKO:
Ieleweke kwamba aina ya kwanza na ya pili ya kunena kwa lugha: mnenaji anakuwa anafahamu ni nini anachokinena, bali changamoto inakuwa kwa wasikilizaji, ndio wanakuwa hawaelewi kinachonenwa. Lakini aina hii ya 3 ya kunena kwa Lugha ni kwamba Mnenaji ananena Lugha isiyokuwa yake. Mara nyingi mfumo huu wa kunena kwa Lugha unatokea kwa Nadra na kwa kusudi maalumu, hasa katika kupeleka Injili katika maeneo ya Ugenini:
Mfano:
Ni kile kilichotokea siku ya Pentekoste, Mitume walikuwa Wagalilaya na walipokutanika Walitumia Lugha yao, Lakini wasikilizaji kila mtu aliwasikia mitume wakinena kwa Lugha zao. Ina maana kwamba Roho mtakatifu alikuwa anamtafsiria kila mtu kwa lugha yake mwenyewe:
Matendo ya Mitume 2:6-8
"Basi sauti hii iliposikiwa makutano walikutanika, wakashikwa na fadhaa, kwa kuwa kila mmoja aliwasikia wakisema kwa lugha yake mwenyewe. Wakashangaa wote, wakastaajabu wakiambiana, Tazama, hawa wote wasemao si Wagalilaya? Imekuwaje basi sisi kusikia kila mtu lugha yetu tuliyozaliwa nayo?"
Hivyo lugha zilizonenwa siku ya Pentekoste zilikuwa ni lugha za Mataifa mengine. Ina maana kwamba siku hiyo Kama wewe ni Mchaga ungekuwepo ungesikia mitume wakinena Kichaga, Kama wewe ni Msukuma ungewasikia mitume wakinena Kisukuma, kama wewe ni mnyakyusa Ungewasikia mitume wakinena Kinyakyusa NK. Kwa hiyo wale ndugu mnaotumia Matendo 2 kutetea unenaji wa lugha zisizojulikana mnakosea, Maana lugha walizonena mitume zilijulikana.
KUSUDIO LA KUNENA KWA LUGHA:
Yesu wakati anaondoka aliwaambia wanafunzi wake kwamba:
Marko 16:17
"Na ishara hizi zitafuatana na hao waaminio; kwa jina langu watatoa pepo; watasema kwa lugha mpya."
Ahadi hii Yesu aliitoa baada ya kufufuka, kwamba Wanafunzi wake watasema kwa lugha mpya. Sasa baadhi ya watu hutumia fungu hili kwa kudai kwamba lugha mpya ni Lugha isiyojulikana, Si kweli, maana Ahadi hii ndio ilikuja kutimizwa katika Matendo sura ya 2. Anaposema watasema lugha mpya ina maana gani? Ina maana kwamba Lugha watakazo sema mitume ni Lugha za watu wa Mataifa ya hapahapa Duniani, lakini kwao zitakuwa mpya kwa sababu ndio mara yao ya kwanza kwao kuzinena. : Ina maana kwamba ukisikia lugha yoyote inazungumzwa isiyokuwa ya kwako hiyo ni ngeni kwako au ni mpya, kwa sababu ndio mara yako ya kwanza kuisikia au kuinena.
Je, wao mitume lugha walizosema zilikuwa kweli mpya kabisa hazijulikani Duniani?
Matendo ya Mitume 2:4-8
"Wote wakajazwa Roho Mtakatifu, wakaanza kusema kwa lugha nyingine, kama Roho alivyowajalia kutamka. Na walikuwako Yerusalemu Wayahudi wakikaa, watu watauwa, watu wa kila taifa chini ya mbingu.
Basi sauti hii iliposikiwa makutano walikutanika, wakashikwa na fadhaa, kwa kuwa kila mmoja aliwasikia wakisema kwa lugha yake mwenyewe. Wakashangaa wote, wakastaajabu wakiambiana, Tazama, hawa wote wasemao si Wagalilaya? Imekuwaje basi sisi kusikia kila mtu lugha yetu tuliyozaliwa nayo?"
Ahadi ya Yesu katika Marko 16:17 ndio ilitimizwa hapo, na hapo anasema ; wakaanza kusema kwa lugha nyingine, hizi lugha nyingine ndiyo lugha mpya, ambazo zilikuwa ni lugha za watu wa Mataifa mengine:
Kusudi la Mungu kuruhusu kunena kwa lugha sio kwa ajili ya maburudisho ndani ya Makanisa, bali aliruhusu kunena kwa Lugha kwa kusudi moja tu, la kueneza Injili, Maana Yesu alisema.
Mathayo 28:19
"Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu"
Sasa haingekuwa rahisi Mitume kuzunguka kila mahali kueneza injili, alicho kifanya Mungu aliyakusanya Mataifa kutoka kila kona ya Dunia ili kila atakayesikia injili akaieneze katika Taifa lake. Na hivyo kusudi kubwa la kunena kwa lugha ilikuwa ni kueneza Injili kwa mataifa yote. Maana siku ile ya Pentekoste kulikuwa na Mataifa kutoka kila kona ya Dunia.
Matendo 2:5 inasema:
"Na walikuwako Yerusalemu Wayahudi wakikaa, watu watauwa, watu wa kila taifa chini ya mbingu."
Matendo ya Mitume 2:9-13
"Warparthi na Wamedi na Waelami, nao wakaao Mesopotamia, Uyahudi na Kapadokia, Ponto na Asia, Frigia na Pamfilia, Misri na pande za Libia karibu na Kirene, na wageni watokao Rumi, Wayahudi na waongofu,
Wakrete na Waarabu; tunawasikia hawa wakisema kwa lugha zetu matendo makuu ya Mungu.Wakashangaa wote wakaingiwa na shaka, wakiambiana, Maana yake nini mambo haya? Wengine walidhihaki, wakisema, wamelewa kwa mvinyo mpya."
Kwa hiyo kupitia muujiza huu wa kunena kwa lugha Injili ikafika kila kona ya Dunia.
Baadaye Kanisa la Korintho walianza kunena kwa lugha kama sehemu ya utaratibu wa Ibada kwa kuiga kile kilichofanyika siku ya Pentekoste, na Paulo akawaonya;
1 Wakorintho 14:20-21
"Ndugu zangu, msiwe watoto katika akili zenu; lakini katika uovu mgeuzwe watoto wachanga, bali katika akili zenu mkawe watu wazima.
Imeandikwa katika torati, Nitasema na watu hawa kwa watu wa lugha nyingine, na kwa midomo ya wageni, wala hata hivyo hawatanisikia, asema Bwana."
Kwa hiyo kilichotokea siku ya Pentekoste ulikuwa ni kutimizwa kwa Utabiri wa kupeleka injili kwa mataifa yote, Lakini Paulo anawaambia pia Kunena kwa Lugha ni Ishara kwa wasioamini:
1 Wakorintho 14:22
"Basi, hizi lugha ni ishara, si kwao waaminio, bali kwao wasioamini lakini kuhutubu si kwa ajili yao wasioamini, bali kwa ajili yao waaminio."
Ina maana kwamba hata siku ya Pentekoste kilichowafanya mataifa wamsikilize Petro ni kwa sababu walitekewa baada ya kuwaona wagalilaya wakizungumza lugha zao. Na kupitia ishara hii ya kunena kwa lugha wakabatizwa watu 3000, maana walisikia habari njema kila mtu kwa lugha yake.
NOTE:
Matukio yote ya kunena kwa lugha yalihusisha upelekaji wa injili kwa watu wa Mataifa,
1. Matendo 2:1-12, kulikuwa na watu wa Mataifa.
2. Matendo 10:44-47, kulikuwa na watu wa Mataifa kwa Kornelio.
3. Matendo 19:1-6, Kulikuwa na watu wa Mataifa pale Korintho.
Hakuna mahali mitume walinena kwa Lugha kama sehemu ya Utaratibu wa Ibada, bali kunena kwa lugha kulitumika katika upelekaji wa injili kwa mataifa ili iwe Ishara ya watu kumjua Mungu pindi wanaposikia lugha tofauti zikinenwa.
Kwa hiyo baada ya Kanisa la Korintho kuanza machafuko ya kunena ovyo kwa Lugha Paulo ikabidi awakemee na kuwapa utarabu mzuri, Na niwaombe wale ndugu zangu mnaopenda kunena kwa lugha bila utaratibu, mfuate utaratibu huu, na ikiwa hamfuti hayo ni machafuko ndani ya kanisa.
1. Kila lugha inayonenwa ni lazima ilete maana;
1 Wakorintho 14:7-8
"Hata vitu visivyo na uhai vitoapo sauti, ikiwa ni filimbi, ikiwa ni kinubi, visipotoa sauti zilizo na tofauti, itatambulikanaje ni wimbo gani unaopigwa kwa filimbi au kwa kinubi? Kwa maana baragumu ikitoa sauti isiyojulikana, ni nani atakayejifanya tayari kwa vita?"
Je, lugha zinazonenwa siku hizi makanisani zina maana gani?
2. Anayenena kwa Lugha ni lazima akili yake ifahamu ananena nini.
1 Wakorintho 14:14-15
"Maana nikiomba kwa lugha, roho yangu huomba, lakini akili zangu hazina matunda. Imekuwaje, basi? Nitaomba kwa roho, tena nitaomba kwa akili pia; mtaimba kwa roho, tena nitaimba kwa akili pia."
Je, ni kweli mnaponena akili zenu zinafahamu ulichokuwa ukikinena, au ukimaliza kunena hukumbuki ulichokinena? Ikiwa akili yako haikumbuki ulichokuwa unakinena basi hayo ni machafuko na ni kazi ya roho mchafu,
3. Lugha wanayoinena iwe inaeleweka kwa wasikilizaji:
1 Wakorintho 14:9
"Vivyo hivyo na ninyi, msipotoa kwa ulimi neno lililo dhahiri, neno lile linenwalo litajulikanaje? Maana mtakuwa mkinena hewani tu."
Je, ni kweli lugha zinazo nenwa siku hizi makanisani zipo dhahili kwa watu au (wanazielewa)?
4. Lugha isipoeleweka huo ni ujinga.
1 Wakorintho 14:11
"Basi nisipoijua maana ya ile sauti nitakuwa kama mjinga kwake yeye anenaye; naye anenaye atakuwa mjinga kwangu."
Mfano:
Unafika mahali unaanza kunena kwa Kingereza wakati hakuna hata mtu mmoja kati yao anayejua Kingereza:, wewe unenaye utakuwa mjinga, na wewe utawaona wale unaowanenea ni wajinga maana hawaitikii kile unachokinena.
5. Ikiwa mtu anataka kunena kwa lugha basi awepo mtu wa kutafsiri hiyo Lugha.
1 Wakorintho 14:13
" Kwa sababu hiyo yeye anenaye kwa lugha na aombe apewe kufasiri."
Na kama hakuna mtu wa kutafsiri hiyo lugha basi asinene, maana hakuna atakayemuelewa anachonena:
1 Wakorintho 14:28
"Lakini asipokuwapo mwenye kufasiri na anyamaze katika kanisa; aseme na nafsi yake tena na Mungu."
Je, ni kweli mnaponena kwa lugha kuna mtu wa kutafsiri au kila mtu ananena apendavyo?
Ndani ya Kanisa watu wa kunena wawe wawili au watatu tu. Zaidi ya hapo ni machafuko.
1 Wakorintho 14:27
"Kama mtu akinena kwa lugha, wanene wawili au watatu, si zaidi, tena zamu kwa zamu, na mmoja na afasiri."
Je, ni kweli makanisani siku hizi wananena wawili au watatu?
Haitakiwi Kanisa zima linene kwa Lugha, maana yatakuwa ni machafuko.
1 Wakorintho 14:23
"Haya! Ikiwa kanisa lote limekusanyika pamoja, na wote wanene kwa lugha, kisha ikawa wameingia watu wajinga au wasioamini, je! Hawatasema ya kwamba mna wazimu?"
Kunena kwa Lugha ni karama inayotolewa na Roho Mtakatifu kwa mtu ampendaye, na sio kwa kila mtu ndani ya kanisa ni lazima anene kwa lugha, na hivyo kulazimisha watu wanene kwa lugha au kuwafundisha watu jinsi ya kunena kwa lugha ni makosa makubwa, maana Roho Mtakatifu ndiye anayemfundisha mtu jinsi ya kunena na sio mwanadamu;
1 Wakorintho 12:28-30
"Na Mungu ameweka wengine katika Kanisa, wa kwanza mitume, wa pili manabii, wa tatu waalimu, kisha miujiza, kisha karama za kuponya wagonjwa, na masaidiano, na maongozi, na aina za lugha. Je! Wote ni mitume? Wote ni manabii? Wote ni waalimu? Wote wanatenda miujiza? Wote wana karama za kuponya wagonjwa? Wote wanena kwa lugha? Wote wafasiri?"
NOTE: Ikiwa kanisani haiwezekani watu wote wakawa Manabii au waalimu au waponyaji, inakuwaje leo makanisani mlazimishe kila mtu anene kwa lugha? Kunena kwa lugha ni moja ya Karama kama zilivyo karama nyingine.
1 Wakorintho 12:4, 7-11
"Basi pana tofauti za karama; bali Roho ni yeye yule….Lakini kila mmoja hupewa ufunuo wa Roho kwa kufaidiana.
Maana mtu mmoja kwa Roho apewa neno la hekima; na mwingine neno la maarifa, apendavyo Roho yeye yule;
mwingine imani katika Roho yeye yule; na mwingine karama za kuponya katika Roho yule mmoja;
na mwingine matendo ya miujiza; na mwingine unabii; na mwingine kupambanua roho; mwingine aina za lugha; na mwingine tafsiri za lugha;
lakini kazi hizi zote huzitenda Roho huyo mmoja, yeye yule, akimgawia kila mtu peke yake kama apendavyo yeye."
Kwa hiyo ukiona mtu haneni kwa Lugha ujue Mungu amempa karama nyingine kati ya hizo, inawezekana amepewa karama ya Hekima au Maarifa au Karama ya kuponya NK.
LUGHA YA MALAIKA
Hakuna mwanadamu aliye wahi kuongea lugha ya malaika katika Biblia; bali Biblia inawaonyesha malaika wakiongea na Wanadamu kwa lugha ya binadamu yenye kueleweka kwa wanadamu waliopelekewa ujumbe.
Mfano:
Mwanzo 19:15-22
Malaika wale wawili waliongea na Lutu juu Sodoma na Gomora kwa lugha ya Wanadamu ya kueleweka.
Danieli 9:21-27.
Malaika Gabrieli aliongea na Danieli lugha ya kibinadamu ya kueleweka kwa Danieli. Mifano ni mingi.!!
HITIMISHO:
Ukweli ni kwamba utaratibu wa kunena kwa Lugha unaofanyika katika makanisa mengi yanayojiita ya kiroho ni kinyume kabisa na Biblia, mfumo huo ni wakipagani: Hakuna utofauti na waganga wa Kienyeji. Mganga wa kienyeji ili aiite mizimu yake ni lazima asisimuliwe kwa ngoma na matunguli, kisha huanza kunena kwa lugha za mizimu yake ili ishuke,
Ndivyo ilivyo Makanisani siku hizi ili roho mchafu ashuke ni lazima watu wasisimuliwe kwanza na nyimbo na ngoma, kisha huanza kunena kwa lugha zisizojulikana.
BWANA ATAWARUDISHIA WAKOMBELEWA LUGHA SAFI.
Sefania 3:8-9
"...dunia yote itateketezwa kwa moto wa wivu wangu.
Maana hapo ndipo nitakapowarudishia mataifa lugha iliyo safi, wapate kuliintia jina la Bwana, wamtumikie kwa nia moja."
NOTE:
Mtu akipagawa na mapepo mara nyingi huangushwa chini na kugaagaa huku akipiga kelele, pasipo yeye mwenyewe kujielewa,
Na wanaodai hujazwa na Roho Mtakatifu kwa kunena kwa Lugha vivyo hivyo wengi wao huangushwa chini na kuanza kupiga kelele na kugaagaa chini, pasipo wao wenyewe kujielewa..
Je, utamtofautisha vipi mtu mwenye mapepo na mwenye Roho? Bila shaka wote ni kundi moja hakuna utofauti.
NB:
Haijawahi kutokea ndani ya Biblia Mtu aliye jazwa na Roho Mtakatifu akaangushwa chini, bali waliopagawa na mapepo tu ndio huangushwa chini.
Mtu aliyejazwa na Roho Mtakatifu hatambuliwi kwa kunena lugha zisizojulikana, Bali hutambuliwa kwa tunda la Roho
Wagalatia 5:22-23
"Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria."
Sasa mtu aliyejazwa na Roho Mtakatifu ajipime hapo,na sio kunena kwa Lugha zisizojulikana, maana wapo watu wananena kwa lugha lakini bado matendo yao ni ya mwilini
Wagalatia 5:19-21
"Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi,husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu"
BWANA AKUBARIKI SANA.