Vyombo vyetu vya usalama haviwezi kukwepa lawama hizi zinazoelekeza kwao. Wananchi tuna hofu na hatuna imani tena na vyombo hivyo. Kwa mfano, hatujapewa majibu yoyote kuhusu kesi ya Dr. Ulimboka, Mwandishi Daudi Mwangosi, ajali ya gari na sumu ya Dr. Mwakyembe, wizi wa EPA, wanyama walioporwa ndani ya shamba la bibi "Tanzania" na kusafirishwa Qatar, n.k. Majibu aina mbili hutolewa na wasemaji wa vyombo hivyo vya usalama wanapohojiwa: (1) Uchunguzi bado unaendelea, na (2) Kesi bado iko mahakamani, kwa hiyo siwezi kuzungumza lolote kwa sasa kuhusu jambo hilo. Hivi wanadhani Watanzania ni ng'ombe na wala si binadamu wenye akili kama binadamu wengine?
Sasa, maoni yangu, kwa kuwa mchakato wa kuandika katiba mpya unaendelea ni vema tukatumia mwanya huo kufikiria kwa kiina namna ya kuviunda upya vyombo hivyo ili vishabihiane na jina lake "Usalama wa taifa au Usalama wa raia"; la sivyo msemo huo "Usalama wa taifa au raia na mali yake" utakuwa ni istiari (analogy) tu yenye maana usalama wa mafisadi, majambazi, waporaji wa rasilimali za taifa hata kuwanunua viongozi wa dini kwa fedha zao kushiriki katika shughuli za kidini (k.m. harambee).