Mdau wa Jamiiforums.com amechapisha maudhui yanayodai kuwa kula mihogo mibichi kunakufanya kuwa zezeta.
Akitetea hoja yake amesema mihogo mibichi ina sumu inayoitwa cyanide ambayo ipo kwa wingi kwenye mihogo michungu na kiasi kidogo kwenye mihogo mitamu, ivyo kula kidogokidogo kunafanya mtu kwa baadaye ashindwe kufikiri vizuri na kupoteza kumbukumbu
- Tunachokijua
- Cyanide ni kemikali (Sumu) inayopatikana kwa namna nyingi, ni hatari kwa afya na inaweza kuua.
Baadhi ya vyanzo vyake ni moshi wa sigara, uunguzaji wa bidhaa za plastiki pamoja na vyakula kama mihogo na Lozi (Almonds).
Mihogo na Cyanide
Tafiti mbalimbali za kisayansi ikiwemo ule wenye kichwa cha habari "Cyanide detoxification in cassava for food and feed uses" wa Padmaja G unathibitisha pasipo shaka uwepo wa Kemikali kwenye baadhi ya aina za mihogo zinazotumiwa na Binadamu.
Kwa mujibu wa vyanzo hivyo, mihogo michungu, michanga pamoja na ile isiyopikwa huwa na kiwango fulani cha kemikali za Cyanide ambacho hutofautiana kulingana na ukanda pamoja na aina ya ardhi ambayo mihogo husika hulimwa.
Madhara ya Kemikali hii hutokana na wingi wa dozi anayopata mhusika, pamoja na muda aliotumia kuingiza mwilini dozi husika. Kifo kinaweza kutokea ikiwa kiasi kukubwa sana cha dozi kisichoweza kuvumiliwa na mwili kitachukuliwa kwa wakati mmoja.
Kemikali hii huwa na uwezo mkubwa wa kuungana na visambaza taarifa (neurotransmitters) vinavyopatikana kwenye ubongo, kitendo ambacho huzuia usambazwaji wa hewa ya kutosha hivyo kusababisha madhara makubwa kwa seli za ubongo ambapo nyingi hufa (cytotoxic hypoxia).
Athari za jambo hili ni kusababisha kifafa, degedege, kupoteza fahamu, maumivu makali ya kichwa pamoja na Parkinson, ugonjwa unaomfanya mhusika akose uthibiti wa misuli na mwendo.
Pia, kwa kuwa usambazwaji wa hewa ya oxygen hupunguzwa, mapafu yanaweza kuharibika pamoja na kupooza kwa mfumo mzima wa upumuaji.
Ni wazi kuwa kemikali hii huathiri uzalishwaji na utendaji kazi wa kemikali za Dopamine kwenye ubongo pamoja na kuua seli zake lakini bado JamiiForums haijapata ushahidi wowote unaothibitisha kuwa inaweza kusababisha uzezeta hivyo madai haya hayana mashiko kisayansi.
Wataalamu wa Afya wamezungumzia pia suala hili kupitia mahojiano maalumu tuliyofanya ambapo wamethibitisha pia kuwa chakula hiki hakiwezi kusababisha uzezeta.
Unaweza kuepuka madhara ya sumu hii kwa kuloweka mihogo kwenye maji walau kwa saa 24 kabla ya kuipika, kutokula mihogo mibichi pamoja na kuikausha kwanza kwenye jua kabla ya kukoboa mihogo kwa ajili ya matumizi ya unga.
Pia soma: KWELI - Baadhi ya Mihogo huwa na sumu inayoweza kuua