Habari za humu wadau,
Natumai kuwa mko poa na wenye matatizo nawaombea kwa Mungu awaondolee matatizo yao ili waweze kuendelea na mapambano ya kila siku ya kuboresha maisha yao.
Nichukue nafasi hii kuwashukuru na kuwapongeza wale wote waliotumia muda wao kusoma au kufuatilia na kucomment kile nilichokiandika kuhusu story yangu ya kweli ya kuzamia nchini Canada.
Wadau sina haja ya kuwadanganya watu, lengo langu ni kuwaambia watu wanaofikiria kuzamia nchi zilizoendelea (ughaibuni) kwa ajili ya kujipatia maendeleo, na niwaahidi leo kuwa ntawaeleza kila kitu kuhusu maisha ya huku Canada, yaani changamoto zake na Faida zake.
Inaendelea...
Nilifanikiwa kwenda kwenye Interview ni mwendo wa saa 2 kutoka hapa ninapoishi mpaka kwenye Immigration Department Office. Hivyo niliamka alfajiri na mapema nikajiandaa kwenda kwenye hiyo Interview kwakuwa baridi ni kali nilivaa jacket zito na pullover ndani na gloves za baridi na buti za baridi na kofia ya baridi, hivyo niliweza kuihimili baridi.
Nilienda kituo cha basi nikapanda basi then nikashuka nikapanda treni then nikabadilisha treni mpaka nilipofika ilikuwa ni saa moja na nusu na uzuri wa nchi za wenzetu kabla ya kutoka unaangalia katika simu yako unaandika ulipo na unapokwenda inakueleza basi litapita muda fulani mpaka muda fulani utafika mahala fulani na utasubiri muda fulani hapo treni itapita.
Cha ajabu unakuta muda ni uleule, ukichelewa tu imekula kwako kiukweli. Huku muda unathaminiwa kuliko kitu chochote.
Nilipofika kwenye hilo jengo nilikuta Security wa kawaida tu ambao hawakuwa wazungu hivyo walinisachi kisha wakaniruhusu niingie na wakanambia niende kwenye counter nikadaiwa kitambulisho nikawapa kisha wakaichukua wakanipa namba then wakaniambia niende ninyooshe mbele kidogo nikaenda na nikakutana na kama hall kubwa hivi ambapo nilikuta watu wengi sana, Waafrika na Waarabu wengi sana.
Nikawa nasubiri kusikiliza namba yangu ikiitwa na nilisubiri masaa matatu mpaka kuitwa, hivyo niliingia ndani nikakutana na Mcanada mmoja mwanaume akiwa na computer yake na Mwafrica mmoja mwanamke. Yule Mwafrica akajitambulisha Kiswahili akasema yeye ni Mkenya na atakuwa Mkalimani kwaajili ya kesi yangu hivyo nikaulizwa swali "Je, unataka kuwa interviewed kwa lugha gani?" Nikajibu KISWAHILI kwasababu tayari Mkalimani yupo pale kwanini nijifanye mjuaji sana.
Tukaanza Interview ambapo waliniuliza maswali yafuatayo:
1. Je, huyu ni wewe? (Walinipa karatasi inayoonesha Visa yangu ya Marekani). Nilistuka sana kwasababu sikuambiwa kabla. Hivyo nilisema ndiyo.
2. Je, wewe ni raia wa Tanzania? (Nikajibu siyo)
3. Ulipataje Passport ya Tanzania (Nikajibu kuwa nilitengenezewa safari na agent hivyo sijui yeye aliipataje). Kumbukeni wadau Mzungu anaandika kwenye computer yake kila ninachokujibu.
4. Je, ulimlipa nini agent? (Nilimpa dhahabu)
5. Ulipata wapi hizo dhahabu (Nilijibu ni urithi kutoka kwa wazazi wangu)
6. Wazazi wako wako wapi (Nilijibu baba alishakufa ila mama yupo)
7. Mama yako yuko wapi? Nikasema Tanzania.
8. Una mke na watoto? (Nikasema Nina mke na watoto watatu)
9.Mkeo ni Mtanzania? (Nikajibu ndiyo).
Kwa kweli maswali ni mengi mno maana kikubwa walitaka kuthibitisha kuwa mi ni Msomali kweli au nadanganya. Hivyo maswali ni mengi mno.
Uzuri nilikuwa nishapangwa vizuri eneo la Somalia nililotoka na tamaduni za huko. Maswali mengine hata sikufundishwa katika zile karatasi alizonitumia jamaa kwahiyo nilitumia akili yangu ya ziada.
Mwisho waliniuliza, je tukikurudisha Somalia itakuwaje nikawaambia nitaenda kuuawa kwasababu Al Shabab waliwahi kunitaka nijiunge nao nikakataa wakanipiga sana.
Waliniuliza pia, je tukikurudisha Tanzania? Nikajibu "Ntafungwa kwa kosa la kumiliki nyaraka nisiyostahili kumiliki"
Interview ilikuwa ngumu sana yaani mpaka sasa siamini kuwa nitabakishwa au nitarudishwa.
Mbaya zaidi nimejipiga under age kuwa nina miaka 18 na wameamini. Hivyo elimu yangu sijui itakuaje yaani niko shaghala bagala sielewi matokeo yatakuaje?
Baada ya kumaliza Interview karatasi mbili zikatoka kwenye printer nikatia saini zote kisha nakala moja nikachukua mimi moja ikabakiwa. Nikitoka nikiwa na mawazo sana.
Siku ya pili nikawa nimekaa na rafiki zangu tunabadilisha na mawazo nikawaelezea balaa lililonikuta na maswali mazito sana wakaniambia kesi si lolote si chochote ni kutimiza wajibu tu ila hawawezi kukurudisha Bongo maana hawa nchi yao ni nchi ya pili kwa ukubwa duniani na haina nguvu kazi hivyo wanahitaji nguvu kazi. Kwahiyo tulipeana moyo sana.
Baada ya week 1 nililetewa post inayoeleza kuwa ninaruhusiwa kutafuta kazi nikipata kazi ntapewa kibali cha kazi. Kazi ni nyingi mno Canada zinahitaji watu hivyo niliingia kwenye mtandao nikaangalia kazi ninayoitaka kisha nikaomba kazi ya Hoteli KFC. Baada ya siku 2 nikaitwa kwenye Interview nikaenda nikafaulu interview hivyo nikapewa mkataba nikajaza vizuri kisha nikaambiwa nizipeleke Government zikapigwe muhuri.
Hivi tunavyoongea muda huu mimi nafanya kazi huku nikisubiri majibu ya Interview yangu ambapo sijui yatatoka lini? Ila najua ntapewa Negative tu.
Mshahara wangu ni mara 5 ya mshahara niliyokuwa naupata nyumbani. Na bado nipo kambini hivyo sina mzigo wa kodi ila wenzangu washaletewa barua walipe bili ya maji na umeme na malazi, hivyo wamesema bora kutafuta nyumba ya kupanga na ku-share.
Kikubwa ambacho nataka niwaambie ndugu zangu maisha ya nyumbani hayana guarantee wala warranty ila kwa mtu aliyesoma na akafanikiwa kupata kazi ni bora akatulia nyumbani maana kuwa karibu na familia ni bora zaidi.
Tazama leo napata pesa ila nipo mbali na mke wangu na wanangu, sasa haya ni maisha gani?
Na huku sio lele mama na ukifika utakuwa tajiri, hapana! Sivyo hivyo wanavyofikiria wengi. huku ni kazi kazi tu ila malipo mazuri sana. Na utofauti wa nyumbani na huku. Huku elimu bure tena elimu bora na matibabu bora. Usafiri wa umma ni mzuri sana hakuna foleni. Kwa kweli jamaa wamejipanga.
Ushauri wangu kwa vijana wenzangu Njoo huku ikiwa unaona huna elimu na huna mtaji na maisha yako mabovu mno. Yaani hata chakula huna na huoni mwanga nyumbani.
Nimeifupisha stori kwasababu niko busy sana na kazi.
Nawatakia jioni njema.
Nakaribisha maswali kwa anayetaka kujua kuhusu maisha ya kuzamia huku.
Asanteni sana.
Sent using
Jamii Forums mobile app