TAJIRI MKUU WA MATAJIRI
JF-Expert Member
- Dec 1, 2010
- 5,720
- 10,216
Huu ndio mto LUKUGA, uliochipuka kutokea Ziwa Tanganyika
(Nashindwa kupata kichwa cha habari kinachofaa kubeba maelezo haya)
Mto Lukuga ni kijito cha 'Mto Lualaba' katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) unaochota maji ya Ziwa Tanganyika na kuyamwaga kwenye mto Kongo, kisha Mto Kongo kuyasafirisha na kuyamwaga katika Bahari ya Atlantic. Sio kawaida kwa kuwa mtiririko wa LUKUGA hutofautiana sio tu kwa msimu lakini pia kwa sababu ya mabadiliko ya hali ya hewa ya muda mrefu.
Ziwa Tanganyika hulishwa na mamia ya mito, mito mikubwa zaidi ikiwa ni Ruzizi nchini Burundi, Malagarasi nchini Tanzania, na Lufubu nchini Zambia.
Maji yanayotiririka kuingia ziwani Tanganyika kwa msaada wa mito hii yanazidi yale yanayo tiririka kutoka Ziwani kupitia Mto Lukuga. Lukuga ni sehemu pekee ya ziwa Tanganyika ambayo hutoa maji ziwani na kuyapeleka Mto Kongo.
Kwa mtiririko huo wa maji kutoka Ziwa Tanganyika kuingia Mto Lukuga, huzalishwa kasi kubwa ya upepo, upepo wenye nguvu unaozalisha mawimbi makubwa makubwa ndani ya ziwa Tanganyika, mwelekeo wa upepo husambaratisha vyote vilivyopo ndani ya Ziwa kutokana na shinikizo kubwa la hewa. Hali hii hutokea msimu baada ya msimu.
Ni marufuku boat za usafiri kutembea, wavuvi kwenda kuvua kutokana na kuchefukwa kwa Ziwa Tanganyika kunako sababishwa na upepo wa Lukuga.
Baadhi ya nyakati upepo huambatana na mvua, radi, na hutokea haswa nyakati za usiku. Ni upepo wa Lukuga ambao husambaratisha nyumba zilizopo karibu na Ziwa, husambaratisha na kuivunjavunja mitumbwi ya wavuvi katika mwambao wa Ziwa Tanganyika.
Nyakati za upepo wa Lukuga, ndio nyakati ambazo unatakiwa uchukue tahadhari ya ziada kusafiri ndani ya Ziwa Tanganyika, upepo wa Lukuga mara nyingi huanza kuvuma Mwezi September mwishoni, October, November, December, January na February' Katika miezi hiyo ni lazima Lukuga atatokea kwa kishindo kikubwa.
Kuna mamia ya watu waliopoteza maisha kwa kuzama ndani ya Ziwa Tanganyika baada ya kufanyiwa ambush na upepo wa Lukuga. Vyombo vingi vya usafiri na usafirishaji vimewahi kuzamishwa kwa upepo mkali wa Lukuga.
Huu ndio mto LUKUGA ambao umepelekea Tanzania, DRC na Burundi kuanzisha utafiti ili kuliokoa Ziwa Tanganyika katika kupoteza maji yake.
Katika kupambana na uharibifu wa mazingira katika ziwa Tanganyika, serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na nchi za Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na Burundi zimefanya tafiti katika bonde la Mto Congo ili kubaini athari zinazojitokeza na kuathiri uendelevu katika Ziwa Tanganyika ambalo linamwaga maji yake katika Mto huo jambo linalochangia kupungua kwa kina chake.
Tafiti zilizofanyika zinaeleza kuwa ziwa Tanganyika linapungua kina chake kwa mita 0.8 ambapo mikakati iliyopo ni kuanzishwa kwa ujenzi wa uzio katika Mto Lukuga utakaosaidia kuzuia kupungua kwa kina cha maji Ziwa Tanganyika.
Profesa Preksedis Macro ambaye ni mtafiti kiongozi wa Tanzania alisema utafiti huo utasaidia kutoa fursa za uwekezaji mkubwa katika miradi ya maendeleo ikiwemo nishati kupitia mto Congo na kuwa na matumizi sahihi ya maji na kuzingatia utunzaji wa mazingira.
Utafiti katika mto Congo ulitekelezwa na watafiti wa chuo kikuu cha Dar es Salaam, kwa kushirikiana na vyuo vikuu vya kimataifa kutoka Uingereza, Kinshasa, Congo DRC na Afrika kusini ambao ulianza tangu mwaka 2016 na ulikamilika mwaka 2020.
............
Kwanini Lukuga inahusishwa na mkoa wa Kigoma ilihali ni mto ambao unapatikana nchini Kongo?
Jibu ni kwamba: Mto Lukuga unapita kando ya ukingo wa kaskazini wa Uwanda wa Katanga katika Mji wa Kalemie nchini DRC. Huu ndio mto ambao umepita katikati ya mji wa Kalimie. Kwa kawaida mto huu unachangia 18% ya upotevu wa maji kutoka ziwani.
Ukiwa Kalimie, upepo huvuma kutokea mto Lukuga kuja Ziwani, na kuathiri maeneo mengi ya ziwa ikiwemo Kigoma. Pia itakuchukua masaa 9 kutokea Kalimie hadi mwambao wa Ziwa Tanganyika mkoani Kigoma Bandari ya Sibwesa, sawa na Kilomita 107.03 km ndani ya maji. Kwa hivyo kuna muingiliano mkubwa wa watu wa Kalimie Ville na mji wa Kigoma Tanzania.
Vilevile, inahusishwa Mto Lukuga na watu wa Kigoma kwasababu LUKUGA ni mto maarufu ambao unapatikana nchini Congo na ni miongoni mwa mito 10 ambayo walitoka Wamanyema, mingine ni pamoja na mto Lualaba, Lomami, Kimbi, Mtambala, Lukuti, Lukuga, Nemba, Ulindi, Lwama, na Lwanazi.
Ukisikia Wamanyema wanapaita Ujiji kwa jina la 'Lwama', basi elewa Lwama ni mto mkubwa nchini Kongo.
Ni nani Mtu wa kwanza mkoani Kigoma kupewa jina la 'LUKUGA' ??
Si mwingine ni Dkt. Amani Walid Kabourou - Kinara wa Mageuzi ya Vyama Vingi Nchini. Mwami Kabuyuki, Mwamba wa Kigoma. Mbunge wa kwanza wa jimbo la Kigoma Mjini kuchaguliwa na wananchi baada ya mfumo wa vyama vingi kurejeshwa nchini 1992!
Dkt. Kabourou alifanya kazi moja kubwa kwa watu wa Kigoma, alitufungua macho kuhusu haki zetu. Alikuwa mtetezi mkubwa wa haki za watu wa Kigoma na Tanzania kwa ujumla. Alifungwa jela mara kwa mara kwa kusimamia haki za watu wa Kigoma. Alifanya mikutano mingi na Wananchi kuelimisha watu Kuhusu haki zao kipindi ambacho watu wengi walikuwa kwenye giza nene, katika kipindi ambacho wasomi wengi walikuwa wanajiweka karibu na watawala. Dkt. Kabourou alikwenda katika kila kijiji, mkoa mzima wa Kigoma kufanya kazi ya kutoa elimu ya siasa na kuamsha Wananchi.
Huyu ni shujaa wa Kigoma na Taifa kwa ujumla. Jabali la siasa za mageuzi, upepo (Lukuga) wa kufukuza udhalimu, mwalimu wa Haki, Utu na Demokrasia, Mwanahistoria, na Mlezi. Kwa sifa hizo ndio maana akapewa jina hilo la LUKUGA.