Nitawapa mifano miwili:
1. Mimi nimeoa mwaka 2010 na bajeti ya sherehe peke yake ilikua milioni 12 hivi. (Hiyo ni nje ya pete, suti yangu na mshenga, gauni la bibi harusi, sare za maids 8, nguo za wazazi pande zote, gharama za honeymoon, send off pia nilichangia, na hapo sijahesabu gharama za kabla ya harusi kuanzia kuvikana pete, wazazi kwenda kujitambulisha, wazazi wake kuja kwetu (lazima sherehe) n.k n.k
Ili kuweza kufanikisha harusi hiyo, ilinibidi nihangaike sana ikiwa ni pamoja na kukwangua akaunti yangu benki, kuzungusha kadi za michango kila mahali hadi kwa watu nisiowajua kivile, yaani ilikua tabu kweli kweli. Mimi na ndugu zangu pia ilibidi tuzunguke huku na kule kuomba omba michango, kulia lia, na kujidhalilisha ili tu harusi hiyo ifanikiwe!
2. Rafiki yangu mmoja alioa mwaka mmoja baada yangu. Mimi binafsi alinitaarifu kuhusu harusi siku mbili kabla. Hakufanya vikao, hakutembeza kadi, hakukuwa na sherehe za kuvikana pete, send off wala nini. Siku ya harusi alitualika kanisani ambapo pia walikuepo wazazi wa pande zote, ndugu na jamaa wa karibu wasiozidi 20. Ndoa ilifungwa saa 10 na baada ya hapo alitualika chakula cha jioni kwenye hoteli moja nzuri tu. Hakukuwa na MC, tarumbeta, Mziki, mapambo, matenti, flat screen, wala vikorokoro vingine tulivyovizoea. Watu tulikula, tukanywa na tukafurahi na kupiga picha chache na maharusi. Saa nne kamili kila mtu yupo kwake. Kwa mahesabu ya haraka ile shughuli haikugharimu zaidi ya 2m na rafiki yangu hakuhangaika kabisa.
Leo ni miaka karibu 10 imepita, wote tunaishi kwa furaha na amani. Lakini ninapolitazama tukio lile naona kabisa kwamba kama ningekua najua ninachokijua sasa, ningefanya kama alivyofanya rafiki yangu.