Tunapokumbwa na majanga makubwa duniani nchi zinapaswa kushikamana na kutatua kwa pamoja

ldleo

JF-Expert Member
Jan 9, 2010
1,010
1,034
VCG31N1247100247.jpg

VCG111421789042.jpg

Jumatatu ya Februari 6, dunia iliamka kwa habari mbaya na za mshtuko baada ya nchi za Uturuki na Syria kukumbwa na tetemeko kubwa lenye kipenyo cha richta 7.8, ambalo limesababisha uharibifu mkubwa wa mali, na cha kuhuzunisha zaidi ni kwamba watu takriban elfu 40 katika nchi hizo mbili wamepoteza maisha yao na zaidi ya watu laki 1 kujeruhiwa.

Kwa sasa mataifa kutoka maeneo mbalimbali duniani, ikiwemo China yanakimbizana kupeleka misaada ya mali na uokozi katika nchi hizo.

Ikumbukwe kuwa mara ya mwisho dunia kutikiswa na tetemeko kubwa zaidi ilikuwa mwaka 2011 nchini Japan, ambalo lilikuwa na ukubwa wa Richta 9 na kusababisha tsunami ambayo imepelekea karibu watu 20,000 kufariki dunia. Majanga makubwa kama haya huwa yanatokea kila baada ya muda fulani. Lakini tujiulize dunia imejipanga vipi kukabiliana nayo?

Kama nilivyosema awali nchi mbalimbali sasa zimekuwa mstari wa mbele kuhakikisha zinasaidia kadiri ziwezavyo kutafuta manusura waliokwama kwenye vifusi ili kupunguza idadi isiwe kubwa zaidi. Lakini kama tunavyofahamu kuwa hali ya hewa sasa ni baridi kwa hiyo kuna changamoto mbalimbali wanazopitia waokoaji.

China kupitia Wizara ya Usimamizi wa Hali ya Dharura imepeleka timu yake ya waokoaji yenye jumla ya watu 82 ikiwa na tani 20 za vifaa na sasa inasaidiana na timu kutoka nchi nyingine duniani, kuendelea na zoezi la kutafuta watu usiku na mchana bila kupumzika. Mbali na timu hiyo pia China imepeleka msaada wa fedha.

Ikiwa sasa tupo kwenye enzi ya ushirikiano wa kimataifa, changamoto za kawaida zikiwemo mabadiliko ya tabianchi, magonjwa, na majanga ya asili yanahitaji mshikamano na uratibu wa watu wote duniani. Mfano huu wa mshikamano unaonekana wazi kwenye janga la matetemeko ya ardhi nchini Uturuki na Syria, ambapo ile kauli inayosisitizwa sana na rais Xi Jinping wa China ya kuwa na “jumuiya ya watu wenye hatma ya pamoja” sasa imedhihirika, na kutoa fursa ya kuunganisha tena ulimwengu.

Hata hivyo tunafahamu kuwa kuna baadhi ya nchi bado zimekuwa mwiba kwa Syria iliyoathirika na tetemeko hilo. Na ni jambo lisilopingika kuwa Marekani ni miongoni mwa nchi zinazosaidia nchi hizi mbili zilizokumbwa na tetemeko baya, kwani rais wa Marekani Joe Biden ameahidi kutoa msaada "wa aina yoyote ile" unaohitajika ili kusaidia juhudi za uokoaji.

Ni kweli kutoa ahadi ya hali na mali ni vizuri, lakini msaada mkubwa unaohitajika hivi sasa nchini Syria ni kuondolewa kwa vikwazo ili kuwapa wepesi watoa misaada ya kibinadamu na waokozi kufika maeneo yaliyoathiriwa na tetemeko kwa wakati na pia kutoa msaada wao kwa wakati.

Huu ndio mshikamano ambao tunauzungumzia kwa sasa. Kama kweli Marekani ina nia nzuri ya kuisaidia Syria katika kipindi hiki cha tetemeko, basi inapaswa kuangalia uhai wa watu wa nchi hiyo, ambayo sasa imekumbwa na taharuki huku familia mbalimbali zikisubiri wapendwa wao kuokolewa wakiwa hai.

Wakati Marekani imetuma timu za kusaidia juhudi za uokoaji na kushughulikia mahitaji ya watu waliokosa makaazi katika eneo hilo, cha ajabu ni kwamba imeondoa kabisa uwezekano wa kuwasiliana na serikali ya Rais wa Syria Bashar al-Assad, ambayo sasa inaendelea kutekeleza kazi ya uokoaji na ujenzi mpya wa nchi. Licha ya kwamba washirika wa Marekani wanajitahidi kurekebisha uhusiano na Syria katika miaka ya hivi karibuni, lakini serikali ya Marekani inasisitiza msimamo wake dhidi ya serikali ya Syria.

Lakini juu ya yote, mataifa na mashirika mbalimbali yasiyo ya kiserikali duniani yanaendelea kutoa vifaa vya msaada na kutuma timu za waokozi. Na kwa upande wa watu walionusurika kwenye matetemeko hayo sasa wapo nje wakipigwa na baridi na theluji, hivyo wanahitaji mahema, msaada wa kibinadamu, nguo, maji na chakula. Kwa hiyo tukishikamana pamoja na kuondoa tofauti zetu tutaweza kuwasaidia wale wote waliothirika nchini Uturuki na Syria.
 
Back
Top Bottom