Ukweli mchungu kuhusu namna fedha za wafanyakazi zinavyotafunwa kwa maslahi ya CCM na washirika wake wachache. Hii ni sehemu tu ya hotuba Msemaji wa Kambi ya Upinzani, Wizara ya Kazi na Ajira, Cecilia Paresso.
Watu waliolazimika kusafiri kwenda Dodoma kwenda kutisha na ku-lobby watu ili habari hizi zisiwafikie wafanyakazi kupitia vyombo vya habari, wajibu hoja badala ya kufukia uvundo chini ya zulia.
..........
MIFUKO YA HIFADHI YA JAMII
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni katika kipindi chote cha miaka mitano tumeshauri mambo yafuatayo kuhusiana na mifuko ya hifadhi ya jamii hapa nchini;
1.Kuunganisha mifuko yote ya Hifadhi ya Jamii na kubaki chini ya usimamizi wa Wizara ya Kazi na Ajira lengo likiwa ni kuirahisishia Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Hifadhi za Jamii katika kutekeleza Sheria moja nakuunda vifungu sawa vya kisheria vitakavyosimamia utekelezaji na uendeshaji wa mifuko hii. Tulipendekeza PPF na NSSF iunganishwe na kuwa mfuko mmoja kwa ajili ya Sekta Binafsi vilevile LAPF, PSPF na GEPF iunganishwe na kuwa mfuko mmoja kwa ajili ya Sekta ya Umma.
2. Tumeitaka serikali kuwa na jitihada za haraka kunusuru uhai wa Mifuko ya Hifadhi ya jamii kwa kulipa fedha walizochota kwa ajili ya uwekezaji katika miradi mikubwa kama ambavyo imeonyeshwa katika Ripoti za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa mwaka 2012/2013, 2013/2014 lakini ripoti ya CAG ambayo imetolewa hivi karibuni ya 2014/2015.
Mheshimiwa Spika,Ni kweli kuwa sikio la kufa halisikii dawa. Madeni sugu ya serikali yanatishia uhai wa mifuko ya hifadhi ya jamii nchini huku Mamlaka ya Usimamizi ya Mifuko hiyo (SSRA) ikitoa angalizo kwa serikali kuhusiana na hali hiyo kufuatia kuidai Sh. trilioni 8.43 kuwa hali hiyo inaweza kukwamisha mifuko hiyo kuwalipa mafao wanachama wake, kujiendesha yenyewe na kuwekeza katika miradi mbali mbali.
Mkurugenzi wa SSRA, Irene Isaka alitoa tahadhari hiyo Oktoba mwaka jana mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kwa kuwakutanisha wakurugenzi wa mifuko ya hifadhi ya jamii, Wizara ya Fedha, Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi wa Mkuu wa Hesabu za Serikali, SSRA na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) ambapo alieleza kuwa iwapo serikali itaendelea kukopa na kutopeleka michango ya wanachama wake, mifuko hiyo itaathirika kiasi cha kushindwa kulipa mafao kwa wanachama wake.
?Tuliyonayo, mifuko yetu ni ya pensheni, hasara ni ya mifuko. Mwanachama hatamsamehe mwenye mfuko kwa kushindwa kumlipia, kadri deni linavyoongezeka ndivyo Mfuko unaumia na baadaye kushindwa kulipa mafao yanayotakiwa.?
Mheshimiwa Spika, Kauli hii ni ya msimamizi mkuu wa mifuko ya hifadhi ya jamii ambaye ndiye mwenye dhamana ya uhai wa mifuko hii. Mara kadhaa Kambi ya upinzani imeelezea na kuonya jinsi ambavyo madeni haya ambayo ni pamoja na PPF (bilioni 192), NHIF ( bilioni 107), NSSF ( bilioni 467), PSPF ( bilioni 4.29), LAPF ( bilioni 170) na GEPF (bilioni 6.86) yanavyohatarisha uhai wa mifuko hii.
Si Raisi Kikwete wala viongozi waandamizi wa CCM wenye kuelewa kuwa, hili ni bomu litakapolipuka muda wowote. Ieleweke kuwa hakuna mpinzani yeyote anayepinga miradi ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa chuo kikuu cha Dodoma (UDOM). Tunachokipinga ni kitendo cha Serikali kutumia fedha za wachangiaji wa mifuko kwa miradi yake ambayo ingeweza kutekeleza ipasavyo kwa kutumia fedha nyingine na kama ingefuta misamaha ya kodi, ingepigana ipasavyo kuzuia ufisadi na ubadhirifu kama wa ESCROW, EPA, RICHMOND- DOWANS na/ au kama ingeweza kupunguza matumizi makubwa ya serikali.
Mheshimiwa Spika,
Huwezi kuukataa ukweli kuwa utawala wa awamu ya nne umeshindwa kuipa wizara ya fedha uwezo wa kitaasisi wa kukusanya kodi matokeo yake, serikali inakuwa inakodolea macho fedha za mifuko ya hifadhi ya jamii na hii ni dhambi ambayo haitafutika machoni pa watanzania.
Na sasa tunaelewa ni kwa nini serikali ilikuwa inaishinikiza wachangiaji wa mifuko wasichukue pensheni zao mpaka wafikishe umri wa kustaafu ambao ni miaka 60, kwa kuwa wanajua umri wa maisha ya wa watanzania ni miaka 52. Hatuwezi kuwa na serikali ambayo ina trade-off na ustawi wa maisha ya watu wake, hii ni aibu kubwa!
MFUKO WA TAIFA WA HIFADHI YA JAMII (NSSF)
Mheshimiwa Spika, mfuko wa hifadhi ya jamii, NSSF, ni mojawapo ya mifuko ambayo mbali ya kutoa mafao ya kustaafu na huduma zingine kwa kadri dira na dhima yake lakini bado inajishughulisha katika uwekezaji kwenye miradi mbalimbali ya maendeleo.
Mheshimiwa Spika, Kwa mujibu wa takwimu zilizopo ni kwamba mbali ya kuwekeza kwenye ujenzi wa majengo ya Chuo Kikuu cha Dodoma na Daraja la Kigamboni, pia NSSF ina miradi ifuatayo ya ujenzi wa nyumba;
i. Nyumba 300 za Mtoni Kijichi (PHASE I &II) ?Nyumba hizo zilikwisha uzwa tayari
ii. Nyumba 800-Flats 500 na Villas 300 (PHASE III) ambao umegharimu shilingi bilioni 137.
iii. Mradi wa AZIMIO SATELITE -Kigamboni wenye Nyumba 7160 (Flats &Villas) ?Utagharimu shilingi bilioni 871
iv. Mradi wa Dungu Farm-Kigamboni (Flats 568) Utagharimu shilingi bilioni 140
v. Mradi wa MZIZIMA TOWER nyumba ya Ghorofa 32 unaotarajiwa kumalizika Juni 2017, ambao utagharimu shilingi bilioni 233. Lakini hadi sasa bado mradi haujaanza.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi sio kama inapinga uwekezaji unaofanywa na NSSF, je uwekezaji huo unafanywa kwa kuangalia kipindi ambacho miradi hiyo itarejesha faida za uwekezaji (return on investment)?
Aidha, kwa mujibu wa kifungu cha 3.12 cha mwongozo wa Msimamizi wa Mifuko ya Hifadhi(SSRA) wa mwaka 2003, pamoja na kanuni zake kuhusu uwekezaji salama wa mifuko na marejeo yake ya mwaka 2012 ni kwamba, mifuko inatakiwa kuwekeza asilimia 70 ya mali zake kwenye dhamana (T-Bills) na hati fungani ( T-Bonds), asilimia 25 ya mali zake kwenye Miundombinu, asilimia 30 ya mali zake kwenye mali isiyohamishika (Real Estates).
Je, ni kwa kiasi gani NSSF imefuata Sheria na kanuni kuhusu uwekezaji wake mpaka sasa kwa kufuatia mgawanyo uliotajwa?
Mheshimiwa Spika, NSSF walinunua majengo ya Manji (EPZ-Project) kwa jumla ya shilingi bilioni 47.5 mwaka 2006, kwa mujibu wa taarifa mbalimbali, ni kuwa majengo hayo hayakuwa na thamani hiyo wakati NSSF inayanunua. Pamoja na hayo, mradi huu unasemekana mpaka sasa kutorudisha thamani ya uwekezaji kwa muda. Kambi ya Upinzani Bungeni inahusisha upandishaji huo wa thamani isiyo halisi kuwa ni mojawapo ya mianya ya watendaji wa NSSF kujipatia 10% kwa miradi isiyo na tija.
Aidha, kodi ya mwaka ya Jengo hilo inayotokana na upangaji, haijaweza kuakisi marejesho ya faida ya uwekezaji huo kwa kuwa mradi huo mpaka sasa umeshindwa kurudisha hata nusu ya fedha zilizowekezwa na hivyo kuhatarisha uwezo wa mfuko kutoa marejesho kwa wanachama wake.
Kwa mujibu wa sheria ya SSRA, Benki Kuu ndio mamlaka ya kuhakikisha mifuko inafanya uwekezaji makini, je kwa uwekezaji huu ambao taarifa ya CAG ilisema kuwa unauweka mfuko katika hali ya kuweza kufilisika na hivyo wanachama kukosa mafao, Wizara ya Fedha inatoa majibu gani?
Mheshimiwa Spika, kuonesha kuwa uwekezaji wa NSSF umekuwa ukiongozwa na matakwa ya watu binafsi, kuna jengo la ghorofa 4 lililojengwa Kigoma kwa gharama ya shilingi Bilioni 7 na limekamilika sasa ni miaka 2, lakini hadi muda huu halijapata mpangaji. Kambi ya Upinzani inahitaji kupata majibu ya uhakika kuhusu uwekezaji huu usio na tija ni nini hatma ikiwemo uwajibikaji wa Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Hifadhi kwa kushindwa kuusimamia mfuko ipasavyo?
Mheshimiwa Spika, NSSF imenunua ardhi mikoa kadhaa kwa bei ambayo ni zaidi ya ile ya soko (Inflated price) na mwishowe viwanja hivyo vinakosa wanunuzi. Kambi Rasmi ya Upinzani inaona kuwa NSSF kukataa kuwekeza kwenye dhamana za Serikali na kuwekeza kwenye majengo ni wa kutia shaka na ni mwanya wa watendaji wake kupokea rushwa au makampuni yanayopewa kandarasi za ujenzi ni makampuni yao na hivyo uwekezaji huo kuwanufaisha wao binafsi na si wanachama wa mfuko.
Kambi ya Upinzani Bungeni, inataka majibu ya kina kutoka kwa Wizara juu ya uwekezaji mzima unaofanywa na NSSF bila kufuata Sheria, Kanuni na Taratibu zilizopo kwa kuwa ni dhahiri kuwa uwekezaji mkubwa usio na tija unaofanywa na NSSF unahatarisha kwa kiwango kikubwa uhai wa mfuko huu.