Tuhuma za kutisha za Dr. Munga Askofu KKKT -DKMS

Tuhuma za kutisha za Dr. Munga Askofu KKKT -DKMS

Status
Not open for further replies.

Mshana Jr

Platinum Member
Joined
Aug 19, 2012
Posts
371,537
Reaction score
860,577
WAUMINI DKMS - KKKT
S.L.P 10
LUSHOTO

03/04/2020


MKUU WA KKKT
S.L.P 3033
ARUSHA
TANZANIA

Salaam katika Jina la Bwana na Mwokozi wetu Kristo!

MALALAMIKO YETU DHIDI YA HUJUMA NA UBADHILIFU WA ASKOFU STEPHEN ISMAIL MUNGA WA DKMS - KKKT

"Kama si BWANA aliyekuwa pamoja nasi, Israeli na aseme sasa," Zaburi 124:1.

Mh. Mkuu wa Kanila la Kiinjili la Kilutheri Tanzania, tunatambua kuwa unayo majukumu mengi ya kuliongoza Kanisa letu la KKKT, pamoja na majukumu haya tunaomba uweke uzito stahiki katika waraka huu tunaokuandikia ili uweze kuinusuru Dayosisi ya Kaskazini Mashariki ya KKKT.

Sisi Waumini wa DKMS - KKKT; ambao majina yet una saini zetu zimo katika barua hii tunapowakilisha wana Dayosisi wengi kwa kuzingatia Kanuni zifuatazo za Katiba ya KKKT - Toleo la Mwaka 2015:
[emoji3581] Kanuni ya VII: G:3,
[emoji818] Kanuni ya VIII: C:2 na 3
[emoji818] Kanuni ya XII:A:1,4,5,7 na
[emoji818] Kanuni ya XIV:A:1,2,3,4,
tumeona ni vema kuleta malalamiko yetu kwenye Ofisi yako, kama kichwa cha habari hapo juu kinavyosomeka.

Mh. Mkuu wa Kanisa, DKMS - KKKT, ina hali ngumu mno kutokana na Uongozi usiofaa wa Askofu Dkt. Stephen Munga, ambaye, bado anang'ang'ania madaraka licha ya muda wake wa kuiongoza DKMS - KKKT kumalizika tokea Mwezi Machi 2020 ( Taz. Katiba ya DKMS - KKKT ya Mwaka 2000: Articles 6: 1c ambayo tumeiambatanisha katika barua hii kiambatisho namba 5), na kuendelea kuingiza Dayosisi ya Kaskazini Mashariki katika mazingira magumu.

Bila ya kumung'ung'unya maneno malalamiko yetu dhidi ya Askofu Stephen Ismail Munga, ni haya yafuatayo;

1. Kuisigina Katiba ya DKMS - KKKT ya Mwaka 2000: articles 6:1c, inayomlazimu Askofu wa DKMS - KKKT kustaafu afikiapo umri wa miaka 65; na hakuna kuongeza ama kuongezewa muda. Hata katika Katiba ya KKKT Toleo la Mwaka 2015 Kanuni ya XIV: A3, inatoa mwongozo. Askofu Stephen Munga amegoma kustaafu na hivyo amejiongezea muda kinyemela bila kupitishwa na kikao chochote cha Kikatiba.

2. Askofu Stephen Munga amesababisha anguko la SEKOMU.

A.Tarehe 20/10/2009, ilitolewa Ripoti ya Ukaguzi wa Fedha za SEKOMU; Bw. Yohana Mnkanda ndiye aliyetoa Ripoti hiyo ambayo tumeimbatanisha kama kiambatanisho namba 6. Ripoti hiyo ilionesha ubadhilifu mkubwa wa Fedha za Chuo, na yeye akiwa kiongozi wa Dayosisi aliifumbia macho kwani Mke wake (Mch. Dkt. Aneth Munga) alihusika katika ubadhilifu huo akiwa Provost wa Chuo hicho.

Dean wa DKMS wa wakati huo Mch. Jonathan Mwamboza aliingilia kati swala la ripoti hiyo, kwamba ifanyiwe kazi, lakini juhudi zake hazikuzaa matunda kwani zilizimwa kwa maelekezo ya Memo toka kwa Askofu Munga ya tarehe 8/10/2009, akitaka jambo hilo liachwe. Memo hiyo tumeiambatanisha kama kiambatanisho namba 7.

Jambo hilo la Dean kutaka kuchukua hatua kutokana na Ripoti hiyo kuligharimu Huduma yake, na kupelekea kuvuliwa Uchungaji kwa barua ya tarehe 24/08/2010, ambayo tumeimbatanisha kama kiambatanisho namba 8.

B. Tarehe 14.12. 2018 Halmashauri Kuu ya DKMS - KKKT, iliunda Tume Maalum, ambayo ilipewa jukumu la kuchunguza matatizo yanayoikabili SEKOMU hata kupelekea Chuo hicho kufikia hali mbaya na hivyo kusitishiwa usajili hadi sasa. Tume hii iliapishwa rasmi na Mwenyekiti wa Halmashauri Kuu Askofu Dkt. Stephen Munga na kuanza kazi rasmi tarehe 17.12.2018 ikizingatia hadidu za rejea ilizopewa na Halmashauri Kuu.

Tume hiyo iligundua ubadhilifu mkubwa mno wa Fedha, na ilitoa mapendekezo kwa Halmashauri Kuu ya DKMS, kuwa wote waliohusika wawajibike, akiwemo Askofu Stephen Munga, Mch. Dkt. Aneth Munga, Msaidizi wa Askofu Mch. Dkt. Eberhart Ngugi, Katibu Mkuu Mch. James Mwinuka ambaye pia ndiye Mwenyekiti wa Kamati ya Fedha ya SEKOMU, na Bw. Geofrey Kingazi ambaye ni Mkurugenzi wa Fedha SEKOMU.

Ripoti hiyo ya Tume Maalum yenye ya kurasa zipatazo 85 ilizimwa na Askofu Munga na wala haikufanyiwa kazi yoyote mpaka sasa.

C. Madeni Makubwa ya SEKOMU
Chuo cha SEKOMU kimeingia kwenye madeni makubwa na kuiweka Dayosisi mahali pabaya sana kutokana na sababu mbalimbali:

i) Udhibiti mbovu wa Fedha.
- Kwa kuwa Chuo hiki kimeongozwa kwa misingi ya kindugu hakuna kuwajibishana katika maswala nyeti ya Fedha. Mf. Vice Chancellor ni mke wa Askofu hivyo japo alionekana kuwa hana uwezo hapakuwa na yeyote wa kumkemea kwa sababu ya masilahi ya kifamilia.

- Mwenyekiti wa Kamati ya Fedha ya Chuo, Mch. James Mwinuka ni mtu wa karibu sana wa Familia ya Askofu.

- Mkurugenzi wa Fedha wa Chuo Bw. Geofrey Kingazi ambaye ni ndugu wa Askofu Munga ndiye Mwenyekiti wa Kamati ya Fedha ya Dayosisi. Kwa mtindo huu Mwenyekiti wa Kamati ya Chuo, ambaye ni Katibu Mkuu hawezi kumuwajibisha Mkurugenzi wa Fedha wa Chuo kwa kuwa naye atawajibishwa na mtu huyo huyo kwenye vikao vya Kidayosisi. Kilichopo hap ani kwamba ukiniwajibisha leo nami nitakuwajibisha kesho nitakapokalia kiti. Kwa maneno mepesi ni kwamba tutunziane siri na kulindana. Hapo ndipo shimo kubwa lililopokea fedha za SEKOMU lilipoanzia.

ii) Askofu Stephen Munga, mara kwa mara alidharau ushauri wa TCU kuhusu namna nzuri ya kuendesha Chuo cha SEKOMU, kwa kufuata Miongozo na Kanuni, za TCU akiendelea kung’ang’ania mke aendelee kuwa Vice Chancellor hata kama hana sifa zitoshazo. Haya yote yalipelekea Chuo hicho kutokidhi vigezo vya udahili, na kuibuka kwa madeni makubwa yanayoikabili Taasisi hiyo na Dayosisi kwa ujumla.

iii) Kuna Deni la CRDB la Sh. 1,300,000,000 (Bilioni Moja na Milioni Mia Tatu) ambalo mpaka sasa halijalipwa. Mwaka 2018 hadi 2019 Uongozi wa DKMS chini ya Askofu Dkt. Stephen Munga, Deni hili liligawanywa kwenye Dinari na Vituo vya Dayosisi kwa viwango kama ifuatavyo:

a) Dinari ya Pwani - Sh. 400,000,000/=
b) Dinari ya Tambarare - Sh. 400,000,000/=
c) Dinari ya Kusini - Sh. 200,000,000/=
d) Dinari ya Kaskazini – Sh. 100,000,000/=
e) Ofisi Kuu ya Dayosisi Sh. 100,000,000/=
f) Vituo vya Dayosisi - Sh. 100,000,000/=
Jumla Sh. 1,300,000,000.

Waumini wa DKMS kupitia Sharika zao na vituo walijitoa kwa moyo kuchangia kuliondosha deni hilo, na kwa asilimia kubwa fedha hiyo ilipatikana; cha ajabu ukisoma katika Ripoti ya TCU kwa SEKOMU; SEKOMU 6 MONTH REPORT, utaona deni hilo lipo na halijalipwa. Swali kubwa letu sisi Washarika wa DKMs ni kwamba je fedha zote tulizochanga zimekwenda wapi?

Mwanzoni mwa mwaka 2019 Askofu Dkt. Stephen Munga na Katibu Mkuu waliitisha harambee maalum ya kuinusuru SEKOMU huko Dar es Salaam. Walioalikwa kwenye Harambee hiyo walikuwa Dkt. Reginald Mengi (Marehemu), Rais Mstaafu Benjamin Mkapa, Waziri Mkuu Mstaafu Edward Lowasa, Wabunge na viongozi mbalimbali. Haijulikani hadi sasa kuwa fedha zilizopatikana kupitia Harambee hiyo zimeelekezwa wapi.

Ripoti ya TCU imeonyesha kwa uchache madeni yanayokikabili Chuo, yakiwemo yale ya TRA, NSSF, WCF, Mishahara ya Watumishi wa Chuo, ambapo Deni hilo linaoneshwa kuwa ni zaidi ya Tsh. Bilioni 2.

Kutokana na madeni hayo, baadhi ya Watumishi wa Chuo hicho wamefungua kesi Mahakamani kudai haki zao ambazo ni fedha nyingi mno kuliko tunavyofikiri. Kwa kuwa kesi hizi ziko Mahakamani hatutapenda kuzungumza mengi hapa.

Miongoni mwa Madeni haya yamepelekea Basi aina ya Coaster lenye namba za usajili T 114 CDT mali ya SEKOMU kupigwa mnada na kuuzwa kwa Sh. 24,000,000/= , baada ya Mtumishi mmoja kushinda kesi dhidi ya Dayosisi. Bado mtumishi huyu anadai fedha nyingi kwa kuwa kiasi cha fedha zilizopatikana kwa mnada wa Coaster hii hakikutosha. Picha ya Coaster hii inaambatanishwa kama kielelezo, (kiambatanisho namba 9)

Tunaambatanisha Ripoti ya TCU kama kiambatisho namba 10; kwani Wana DKMS pamoja na Wachungaji wao wanaaminishwa kuwa hakuna deni lolote.

3. Kuuzwa kwa Kituo cha Mafuta BP Mombo.

Askofu Dkt. Stephen Munga amekiuza Kituo cha Mafuta Mombo kwa Bw. Mziray kwa Sh. 300,000,000/= bila ya idhini ya Halmashauri Kuu ya Dayosisi, na haijulikani Fedha hizo amepeleka wapi. Bw Mziray kwanza alilipa Tsh. 210,000,000/=, na pale atakapokabidhiwa Hati ya eneo hilo angemalizia kiasi kilichobaki. Baada ya kutopewa Hati aliamua kufungua Kesi Mahakama Kuu Tanga, na upo uwezekano wa DKMS - KKKT kuingia hasara ya kumlipa mamilioni ya fedha.

4. Uvunaji wa Misitu ya Dayosisi bila kibali cha Halmashauri Kuu ya DKMS.
Misitu mingi ya Dayosisi imevunwa kwa agizo la Askofu wa DKMS, bila ya Utaratibu bila H/Kuu kuridhia. Misitu hiyo ni ya Magamba, Chatlon, VBS, Bangala na Mponde. Hali ya maeneo hayo ni ya kutisha, na wala haijulikani fedha zilizopatikana katika uvunaji wa Misitu hiyo, Askofu Munga na timu yake wamezipeleka wapi. Shamba la Magundi Korogwe linatakiwa kukaguliwa kama bado linamilikiwa na DKMS.

5. Hali ngumu ya Watumishi katika Dayosisi.

Watumishi wengi katika Vituo vya Dayosisi, mf. Ofisi Kuu ya Dayosisi, Lwandai Sekondari, Bangala Seminari, Vuga Press, Tumaini Hostel, Radio Utume nk wako katika hali ngumu mno. Hawalipwi mishahara yao kwa miezi mingi sasa, hawana tumaini, wanateseka, hawana pa kusemea maana Askofu Munga yu juu ya Halmashauri Kuu ya DKMS, anawaburuza anavyotaka.

Wachungaji walio wengi wanapata maumivu makubwa kwa kukosa posho zao kwa ajili ya michango mikubwa ya fedha ili kuinusuru SEKOMU lakini hawathubutu kusema lolote kwa kuwa Askofu ameshatamka kuwa yeyote atakayenyanyua mdomo kinyume na Askofu atafukuzwa kazi mara moja. Watumishi wa Dayosisi wakihojiwa wataeleza maumivu yao.

6. Hali mbaya ya Vituo katika Dayosisi.

Vituo kama Vuga Press, Lwandai Sekondari, Bangala Seminari, Mbuyukenda, Tumaini, Duka la Vitabu Lushoto, vinapita katika bonde la uvuli wa mauti; na viko hatarini ya kufungwa kama UTC na Gereji ya Lushoto zilivyofungwa kutokana na Uongozi mbovu wa Askofu Munga.

7. Uanaharakati na mapambano.

Askofu Dk Stephen Ismail Munga amepoteza sifa za Kichungaji, huduma yake ameielekeza zaidi katika uanaharakati na mapambano ya kuwaumiza wengine wakati kwake kumemshinda. Tokea alipoingia madarakani alianza kuvuruga Umoja wa Kanisa, aliibadilisha Katiba, KKKT - DKMS, na kuwa DKMS - KKKT, Majimbo kuwa Dinari, na Wakuu wa Majimbo kuitwa Wakuu wa Dinari, ili mradi ajiweke kinyume na Madayosisi mengine ya KKKT. Haya aliyafanya mara tu baada ya kushindwa kwenye kinyang’anyiro cha Ukuu wa Kanisa alipochaguliwa Askofu Dkt. Alex Malasusa. Hivi karibuni pia tumeshuhudia akihamasisha na kushiriki vikao visivyo rasmi vya kuivuruga KKKT kama kile alichokifanya Dodoma Machi 18, 2020. Dayosisi ya Kaskazini Mashariki haijamtuma kufanya hivyo, na hatujui mamlaka hiyo ameitoa wapi na pia ijulikane kuwa gharama za safari hizo anagharimiwa na Dayosisi kinyume cha utaratibu.

8. Kuwasimamisha/ kuwafukuza Uchungaji/ na Utumishi katika Dayosisi. Tokea Askofu Munga aingie madarakani tumeshuhudia akiwasimamisha baadhi ya Wachungaji na Watumishi wa DKMS: mfano:

- Mch. Godfrey Hermann aliyekuwa Dean na Katibu Mkuu, aliyeitumikia DKMS kwa weledi na uaminifu mkubwa, alimfanyia hujuma mpaka Baba huyu akaondoka kwa haraka katika huduma.

- Mch. Jonathan Mwamboza aliyekuwa Dean wa Dayosisi alimfukuza kazi kwa chuki binafsi kwa kuwa tu alikuwa anasimamia ukweli.

- Mch. Dkt. William Kopwe aliyesomeshwa kwa gharama kubwa naye alimfukuza kwa chuki binafsi.

- Mch. Dickson Kihiyo naye amemsimamisha Uchungaji tokea Mwaka 2017, sasa ana miaka 3 anahangaika na familia yake, na wala halipwi stahiki zake kama Kanuni ya ajira na mahusiano kazini inavyoagiza. Baraza la Wachungaji chini ya Uenyekiti wa Askofu Munga lilishakubaliana kuwa Mch. Kihiyo arudishwe kazini, lakini mpaka sasa hajarudishwa.

Tunaambatanisha barua ya kusimamishwa Utumishi kwa Mchungaji Kihiyo kiambatanisho namba 11.
- Bw. Richard Shembilu aliyekuwa Mhazini wa DKMS naye pia alifukuzwa kazi bila ya kufuata kanuni; aliishitaki Dayosisi, ameshinda wakalazimika kumlipa pesa nyingi ambazo bado hawajamaliza.

9. Kuvunja Urafiki wa Kihistoria na Ujerumani
Askofu Dkt. Stephen Munga kwa sababu zake binafsi zikiwemo za kutopenda kukaguliwa na kufuatiliwa juu ya matumizi ya fedha ameamua kuvuruga urafiki uliokuwepo wa miaka mingi na Makanisa ya Ujerumani. Sasa anashinikiza kuiingiza Dasyosisi ihusiane na Dayosisi ya Lund Sweden ambayo inakubali mambo ya Ushoga.

10. Safari binafsi za Dar es Salaam kila wiki
Askofu Dkt. Stephen Munga tangu alipochaguliwa amekuwa na tabia ya kutokukaa ofisini na hivyo kila Jumatatu amekuwa akiondoka kuelekea Dar es Salaam na kukaa huko hadi Alhamisi au Ijumaa. Safari hizi zimekuwa mzigo mkubwa kwa Dayosisi yetu na hatuna mashaka kusema kuwa zimechangia kuiweka Dayosisi yetu pabaya sana kifedha. Ukaguzi wa kina ukifanyika utabaini ni kiasi gani cha fedha alichokitumia katika safari zake hizi binafsi kwa kipindi cha miaka hii 19 ya uongozi wake. Hata pale ambapo watumishi wamekuwa hawana mishahara Ofisi Kuu yeye hajawahi kukosa fedha za kuweka gari mafuta na posho za safari kwa siku hizo. Tunajiuliza maswali magumu kuwa hivi huko Dar es Salaam anakwenda kufanya nini kila wiki?

Mh. Mkuu wa Kanisa, yapo mambo mengi yanayoivuruga DKMS - KKKT chini ya Uongozi wa Askofu Dkt. Stephen Ismail Munga, tumeyaleta hayo machache ili Kanisa litafute njia ya kuikoa DKMS - KKKT toka katika mikono dhalimu.

Nasi tunapendekeza yafuatayo:

I) Askofu Dkt. Stephen Ismail Munga, kwakuwa muda wake wa Uaskofu DKMS umemaliza ajiuzulu mara moja bila ya masharti yoyote.

II) Kwa kuwa muda kwa Askofu umeshapita, asiruhusiwe kufanya kazi yoyote kama Askofu wa DKMS - KKKT, na wala asiwe msemaji wa Dayosisi, na asiruhusiwe kushiriki katika Vikao vya KKKT, viwe ni vya Halmashauri Kuu ama vya Maaskofu kwani hayuko kazini, atambuliwe kuwa ni Askofu mstaafu kama Katiba ya DKMS na ile ya KKKT ilivyoonesha.
III) Iundwe Tume Maalum ya KKKT ichunguze na kukagua fedha na madeni ya SEKOMU, Ofisi Kuu na Vituo vyote vya Dayosisi. Akaunti zote za Dayosisi zikaguliwe ikiwemo ile ya Fedha za Kigeni.

IIII) Akaunti za Askofu Dkt. Stephen Ismail Munga pamoja za Mch. Dkt. Aneth Munga, nazo zikaguliwe.

Mwisho, tumalizie kwa kusema kwamba tumelileta jambo hili mikononi mwako, kwa unyenyekevu mkubwa, ili liweze kushughulikiwa kwa dharura ili kuepusha vurugu ndani ya Dayosisi.

Iwapo Askofu Dkt. Stephen Ismail Munga, atakaidi, tuko tayari kumpeleka Mahakamani.

"Watu wa kusitasita nawachukia, Lakini sheria yako naipenda." Zab 119:113.

Tunawasilisha,

Ni sisi Waumini wa DKMS - KKKT

1.
2.


Nakala kwa:
- Maaskofu wote wa KKKT
- Katibu Mkuu KKKT
- Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya KKKT
- Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani (TZ)
- Msajili wa Taasisi za Dini Tanzania

Jr[emoji769]
 
KKKT nadhani ni dhehebu linaloongoza nchini kwenye migogoro ambayo chimbuko lake ni pesa!

Swali la kujiuliza kwa nini linaongoza kwenye migogoro ya pesa?

Je, viongozi wa kutoka maeneo gani ambao wanakumbwa na migogoro ambayo chimbuko lake ni pesa?

Je, viongozi wake hawa wanajua sana umuhimu wa pesa kuliko wengine?
 
Aingie kwenye siasa basi.. Mbona kilichoandikwa hapo ni facts tupu?
Hii migogoro ya kuwakataa viongozi wenu nyie KKKT ni ya miaka yote, jitafakarini kwanza.

Lakin kwa sisi watanzania wa kawaida Dr. Munga tunamkubali sana na tunajua uwezo wake wa akili,hayo mengine mnayajua nyie wanadayosisi

Sent using Jamii Forums mobile app

Jr[emoji769]
 
Dr. Munga ni kweli alipiga hela yeye na huyo Anneth ambaye ni ndugu yake, na kwanini bado anang'ang'ania madaraka au mamlaka?

Askofu Mkuu yuko wapi?

Inabidi Askofu Mkuu ama baraza la Maaskofu limshughulikie.

Sent using Jamii Forums mobile app
 
Mimi naweza kupinga kidogo, KKKT inao mfumo mzuri wa kiungozi, sio kanisa kama la Gwajima ambaye ana final say kwenye kila kitu kinachousiana na kanisa lake,

Isije ikawa na siasa za kanisani za kikundi cha watu wanaosaka madaraka
 
Sasa wewe Mshana Barua za Kanisa unazileta huku JF ili upate nini? Si hekima ulivyofanya. Hii barua ungeiacha huko ilikotumwa. Kuwa na Hekima kama Yusufu aliposhtukia Mariamu ana mimba bila kuhusiana naye. Unamuabisha Baba Askofu Munga Mtumishi wa Bwana.
 
Status
Not open for further replies.
Back
Top Bottom