Kweli kuchangia harusi ya mtu ambaye sio wa karibu kabisa ni ushamba. Unachangia laki unapata kinywaji kimoja maana gharama nyingi za ziada (kukodisha magari ya ajabu ajabu, farasi, n.k.) zinapunguza bajeti za vyakula na vinywaji. Tena mara nyingi "wenyeviti wa idara" (k.m. chakula, upambaji n.k.) wanapata "cha juu" kwa kumleta mhusika anayetoza gharama kubwa kuliko inavyostahili. Nimewahi kuona harusi ambazo kamati ya maandalizi imeweka "sherehe ya kujipongeza" kwa sababu michango ilibaki. Yaani badala ya kuwapa maharusi hiyo baki iwasaidie kwenye kodi ya pango au kwenye ujenzi kama tayari wana kiwanja, kamati inazila hizo fedha. Halafu mwisho wa siku baada ya harusi ya kifahari sa-a-na ndoa inavunjika (wakati mwingine hata mwaka haujaisha). Napendekeza muoaji aite tu marafiki wa karibu, wajomba, mashangazi, na wazazi na ndugu upande wa mume na mke. Jumla ya watu isizidi 50. Na gharama isizidi milioni nne. Mradi picha na video ziwepo basi. Kama gharama ni ndogo hapatakuwepo haja ya kuomba michango mingi. Siku hizi unaweza kujikuta una kadi nne au tano zinataka michango kila mwezi. Na ukimchangia mtu elfu 20 anakudharau. Si afadhali kuacha kuchangia kuliko kutoa pesa kibao kila mwezi kuchangia harusi? Mwisho kabisa:- Kwenye mila za makabila mengi ni watu wa ukoo tu ndio walikuwa wanachanga, na kwenye makabila mengi michango ilikuwa ni vitu vya kusaidia maharusi katika maisha yao yajayo (yaani fenicha na vyombo vya ndani) na sio pesa za kwenda kula na kunywa.