Tafadhali mama usiwaue watoto wangu

Tafadhali mama usiwaue watoto wangu

Kanungila Karim

JF-Expert Member
Joined
Apr 29, 2016
Posts
20,746
Reaction score
25,639
SEHEMU YA KWANZA

Hali ya hewa ilikuwa tulivu ingawa kulikuwa na kijua kilichochoma kwa mbali na kufanya hali ya Mwanza iwe na joto kiasi.

Anne alisimama kizimbani mbele ya jaji wa Mahakama ya Rufaa Raphael Mpoki, siku hiyo ya Januari 21, 1998 ilikuwa siku ya hukumu yake na wengi wa watu waliohudhuria mahakamani walitegemea kwa kosa alilolifanya Anne ni lazima angenyongwa.

Miongoni mwa watu waliokuwepo makahamani walikuwa watoto wake wawili, wa kike Nancy na wa kiume aliyetwa Patrick, walikuwa watoto wazuri tena mapacha na siku tano kabla ya siku hiyo walitimiza miaka kumi na mbili lakini miaka waliyoishi na mama yao katika maisha ilikuwa ni miwili tu!

Patrick na Nancy walikosa mapenzi ya mama yao na si mama tu bali pia baba yao aliyefariki dunia katika mazingira ya kutatanisha wakiwa na umri wa mwaka mmoja, yeye hawakumwona kabisa zaidi ya kuiona sura yake katika picha.

Mpaka siku hiyo Anne alikuwa amekaa mahabusu kwa takribani miaka kumi na siku thelathini na saba kamili na aliwaacha watoto wake wakiwa na miaka miwili tu! Patrick na Nancy walikuwa kama watoto wa yatima wakilelewa na mama yao mdogo, Suzanne.

Walimhurumia sana mama yao kwa sababu alikuwa amekondeana sana alivaa nguo chafu na mwili wake ulijaa vipele na ukurutu lakini pamoja na hali hiyo ya uchafu bado alionekana ni mwanamke mwenye sura nzuri na sura yake ilifanana sana na ya mtoto wake wa kike Nancy!

Tofauti pekee kati yao ilikuwa ni rangi ya ngozi zao, Nancy alikuwa mweupe zaidi ya mama yake kwa sababu baba yake Huggins alikuwa Mmarekani mweusi mwenye mchanganyiko wa damu ya kizungu ila mama yake ndiye alikuwa raia wa Sierra Leone aliyehamia Marekani miaka mingi kabla.

Anne alipowaangalia watoto wake wawili waliokuwa wamekaa miguuni kwa mama yao mdogo akiwa amewakumbatia, alilia machozi alisikia uchungu moyoni mwake kufahamu kuwa ni siku hiyo ndiyo ilikuwa ya mwisho kwake kuwaona watoto wake!

“Patrick and Nancy today I’m dying for you!”(Patrick na Nancy leo nakufa kwa ajili yenu!)

“No! Mom don’t die! Please mom we need you mom dont go!”(Hapana mama usife, tafadhali bado tunakuhitaji sana usituache) mtoto mdogo Patrick alipiga kelele mahakamani na kuchomoka mikononi kwa mama yake mdogo na kukimbia akimfuata mama yake.

Kabla hajakifikia kizimba alishikwa mkono na askari na kuanza kuvutwa akirudishwa mahali alipokaa mama yake mdogo. Mawakili waliokuwa wakiendelea na mabishano ya kisheria ndani ya mahakama na hata jaji mwenyewe walikerwa sana na kelele za mtoto Patrick aliyekuwa akilia, ikabidi hakimu aagize Patrick na Nancy pamoja na mama yao mdogo watolewe nje ya mahakama haraka ili kuruhusu mahakama iendelee na kazi yake!

“Hatutaki! Hatutaki! Hatutaki! Tuachieni tumwone mama yetu mara ya mwisho!”Patrick na Nancy walilia wakati askari akiwavuta kuwatoa nje ya mahakama.
****
Hali ilipotulia mahakama iliendelea na kazi yake kama kawaida.

“Mheshimiwa Jaji siamini hata kidogo kuwa mshtakiwa alimuua mama yake kwa sababu marehemu alikutwa nje ya nyumba yake iliyo umbali wa mita elfu moja kutoka nyumbani kwa mshtakiwa, akiwa amechomwa visu, kimoja shingoni na kingine kwenye titi la kushoto. Mheshimiwa jaji kufanyika kwa kitendo hicho haimaanishi kuwa mshtakiwa ndiye aliyefanya na hakuna ushahidi wa kutosha kulithibitisha jambo hilo uliokwishatolewa mbele ya mahakama yako tukufu!”

Mahakama ilikuwa kimya ikimsikiliza wakili Lydia Ishegoma aliyekuwa akimtetea Anne mahakamani, alikuwa ameifanya kazi hiyo kwa miaka kumi na siku hiyo ndiyo ilikuwa siku ya mwisho! Aliamua kumtetea Anne kwa sababu walisoma wote na aliyefanyiwa na mama yake mzazi yalimsikitisha sana kiasi cha kusema hata yeye asingeweza kuvumilia.

“Mheshimiwa Jaji mtu yeyote angeweza kufanya hivyo na kisha kuutupa mwili wa marehemu nje ya nyumba yake na isitoshe visu vyote vilipopimwa na wataalam wa vidole haikuonyesha alama za vidole vya aina yoyote! Jambo linalonifanya niamini muuaji alikuwa mtaalam wa kazi hiyo kuliko anavyoonekana mshtakiwa! Hivyo naiomba mahakama yako tukufu imwachie mshtakiwa huru kwa sababu ameteseka kwa muda mrefu na ni mama wa watoto wawili ambao baba yao alikufa miaka mingi!” Alimaliza wakili Lydia kutoka chama cha mawakili wanawake nchini Tanzania.

Maneno ya wakili Lydia yalionekana kumwingia jaji akilini na ndani ya moyo wake, alijikuta akiingiwa na huruma kwa sababu alishaisikia historia ya jambo lililopelekea Anne kumuua mama yake mzazi!
Alitaka sana kumwachia Anne huru lakini alishindwa atumie kifungu gani cha sheria wakati ushahidi uliokwishatolewa mahakamani uliyoonyesha wazi kuwa Anne ndiye alimuua mama yake.

Huku moyo wake ukiwa umejaa huzuni Jaji Raphael aliigonga meza iliyokuwa mbele yake kuashiria kuwa mahakama ilikuwa inapumzika kwa muda wa dakika tano na alitoka mahakamani kupitia mlango wa nyuma na alikwenda moja kwa moja hadi ofisini kwake ambako aliendelea kuwaza mambo mengi juu ya Anne.

Watu wote ndani ya mahakama baada ya Jaji kuondoka waliendelea na minong’ono kimya kimya wakimwongelea Anne aliyekuwa ndani ya kizimba akilia! Kilichomfanya Anne alie si kingine bali ni watoto wake.

“Bila Patrick na Nancy wala nisingejali kifo changu kwani kufa ni kulala! Aliwaza Isabella.
****
Mwili wake wote ulinuka na alihisi nguo zake kulowana! Inzi wengi walimzunguka na aliwapiga kwa mkono wake kuwafukuza. Anne alijua ni kitu gani kilichokuwa kimetokea, kwani mwaka mmoja kabla ya kutiwa mahabusu alipatwa na ugonjwa wa ajabu, ugonjwa uliomtesa na kumpa fedheha kubwa katika jamii iliyomzunguka, ni ugonjwa huo ndio uliomfanya mumewe na baba wa watoto wake Huggins William kijana wa kimarekani kumwacha na kuanza kuishi na mwanamke mwingine aliyeitwa Delilla.

Ni mwanamke huyo ndiye aliyempa sumu Huggins, mwanaume ambaye Anne alimpenda na kumuua! Mpaka siku hiyo ya hukumu bado Anne aliamini bila kupatwa na ugonjwa huo, Huggins asingemkimbia kwenda kwa Delilla na asingekufa.

“Mimi naona nilichomfanyia mama ni sawa tu! Kwani alichonifanyia yeye mimi yaani niwe namiminika hedhi kila siku kwa miaka kumi! Mama alistahili kifo na kama kuna maisha baada ya kunyongwa kwangu huko ahera ninakokwenda ni lazima nimuue tena! Alinifanyia ubaya mkubwa mno na ninashangaa kwanini Jaji hanihukumu ili nife, acha nihukumiwe nife niende zangu, nina thamani gani hapa duniani mie ni bora kifo!”Aliendelea kwanza Anne.
****
Dakika tano baadaye Jaji alirejea tena mahakamani na mahakama iliendelea.

“Anne!” Jaji aliita kwa huruma lakini Anne alikaa kimya bila kujibu kitu, watu mahakamani walishangaa kuona jaji Raphael Mpoki akiongea kwa upole kiasi kile siku hiyo kwani alikuwa ni jaji aliyeaminika kuwa mkali kupita majaji wote nchini Tanzania.

“Anne!”Jaji aliita tena safari hii akitabasamu, watu wote wakajua ushindi ulikuwa ni wa Anne.

“Naa..m mhe…shimi…wa!” alijibu Anne huku akilia.

“Usilie binti tafadhali niambie kwanini nisikuhukumu kifo kwa mauaji ya kikatili uliyoyafanya kwa mama yako kwa sababu kila aina ya ushahidi kuwa ulifanya tendo hilo!”Jaji alimwambia Anne huku akimwangalia kwa huruma!

Watu wote mahakamani walikaa kimya wakisubiri jibu la Anne, hata watoto wake ambao tayari walisharudishwa ndani ya mahakama pia walikuwa wakisubiri jibu la mama yao, walitaka dunia ibadilike na mama yao asihukumiwe kifo wala kifungo cha maisha, walitaka aachiwe huru ili waonje na kufaidi upendo wa mama! Walikuwa wemechoka kujisikia yatima na kushinda kutwa nzima wakiangalia picha za mama na baba yao!

Anne alijaribu kufungua mdomo ili aongee kitu lakini maneno hayakutoka kwa sababu ya kwikwi iliyokuwa imekaba kooni!

“Sema Anne, sema usiogope ongea na mimi unataka nikufanye nini maisha yako yapo mikononi mwangu?” Alisema jaji Raphael Mpoki lengo lake likiwa ni kumshawishi Anne aombe kuachiwa huru ni hicho tu alichokuwa akisubiri ili amuachie aende zake.

“Mhesh..imi...wa Ja..ji!” Anne alijikaza na kujikuta akiongea ingawa kwa shida na watu wote walikaa kimya kumsikiliza.

“Ndiyo nastahili kifo na ninaomba unihukumu kifo, ninaomba unihukumu kunyongwa lakini kabla sijafa naomba niseme maneno yafuatayo kwa watu waliopo hapa mahakamani! Ndugu zangu ni wengi wananyongwa na ni wengi wameua lakini hawakutakiwa kufanya hivyo , mimi si muuaji ila nililazimika kuua kwa sababu sikuwa na njia yoyote ya kuwalinda watoto wangu, kwa sababu mama yangu aliyenizaa mimi na kunileta duniani alitaka kuwaua wanangu ingawa tayari alikwishawaua watoto wangu wengine wawili, William na Henry!”

Mahakama ilikuwa kimya watu wote wakisikiliza kwa makini maneno ya Anne aliyoyaongea huku akilia.

“Nilipokataa kumpa watoto wangu akaniroga na kunipa ugonjwa wa kupata hedhi kila siku na hivi mnavyoniona hapa niliposimama nguo zangu zote zimeloa na nimekuwa katika hali hii kwa muda wa miaka kumi na moja! Macho yangu ni meupe kwa sababu nimepoteza damu nyingi na sili chakula kizuri gerezani! Na yote haya alinifanyia mama yangu mwenyewe ambaye bila yeye mimi nisingeifahamu dunia, mlitegemea nifanye nini wakati alitaka kuniulia watoto wangu Patrick na Nancy? Ni yeye aliyesababisha kifo cha mume wangu na kuniharibia maisha yangu kwa kweli ilibidi nimuue mama yangu ili kuokoa maisha ya watoto wangu NA SINA LA KUFANYA MHESHIMIWA JAJI NAOMBA UNIHUKUMU KIFO ILI NINYONGWE NIMFUATE MAMA HUKO ALIKO NA NIKIMKUTA NI LAZIMA NIMUUE TENA KWA SABABU AMENITESA SANA NA MARA KWA MARA NAJIULIZA NI KWANINI ALINIZAA!”

Maneno hayo ya Anne yalimfanya wakili wake aliyejua siku hiyo ushindi ulikuwa wao apigwe na butwaa na kujikuta akiziba mdomo wake kwa mikono yake yote miwili, kwa utetezi aliokuwa ametoa alifahamu wazi Anne angeachiwa huru lakini maneno aliyoyatoa Anne pale mahakamani yalimfanya wakili wake atokwe na machozi!

“ANNE WHAAAAT!”(Anne nini?) wakili wa Anne ajikuta akipiga kelele.

“Sorry Lydia I want to die! I’m very sorry for wasting your ten years time trying to defend me in court but God will pay you for me!”(Samahani Lydia nataka kufa, nasikitika kwa kukupotezea muda wako wa miaka kumi ukijaribu kunitetea mahakamani lakini Mungu atakulipia!)

Kwa historia aliyoitoa Anne watu wote mahakamani walijikuta wakimwanga machozi kumlilia Anne, maneno yake yaliwachoma watu wengi, waligundua alifanyiwa unyama mkubwa ambao binadamu yeyote mwenye akili ya kawaida asingeweza kuuvumilia, hata jaji Mpoki pia alikuwa akijifuta machozi kwa sababu ya kulia, maaskari pia walishindwa kuvumilia na kujikuta wakitokwa na machozi.

“Nimesikitishwa sana na historia aliyoitoa na sina la kufanya zaidi ya …………….!” Jaji Raphael Mpoki alijikuta akishindwa kuvumilia na kuangua kilio mbele ya watu wengi waliokuwa mahakamani, watoto wa Anne na mama yao mdogo pia waliendelea kulia machozi, mahakama nzima ilijaa vilio na maaskari walijaribu kunyamazisha mahakama bila mafanikio.

Je nini kitaendelea?
Je Anne atahukumiwa kifungo cha gerezani au atanyongwa?
Je nini kilitokea katika maisha ya mwanamke huyu?
Kuna mambo mengi ya kusisimua, tukutane baadae saa 7 kamili usiku
 
Shigongo huyu, kwenye Ijumaa mwaka 2001 kama sio 2002 ndio ilikuwa inachapwa hii hadithi.
 
SEHEMU YA 02


Anne anabaki akilia tu, ndani ya mahakama hiyo, kuna watoto wake wake mapacha, msichana aliitwa Nancy na wa kiume aliitwa Patrick. Hakimu ambaye alikuwa akisimamia kesi hiyo aitwaye Raphael Mpoki anamuonea huruma Anne, hataki kumuhumu kifo na hivyo kumuuliza alitaka amfanyie nini, cha ajabu, Anne anasema kwamba anachokitaka ni kufa tu na ni kweli alimuua mama yake.
Mahakama inashtuka, wakili aliyekuwa akimsaidia aitwaye Lydia naye anashtuka, haamini kama mteja wake aliyetumia nguvu nyingi kumsimamia anakihitaji kifo kwa gharama yoyote ile.
Kwa uchungu mkubwa moyoni mwake, tena huku akiwa analia kama mtoto, Anne anaanza kusimulia kilichotokea maishani mwake na sababu iliyosababisha kumuua mama yake, historia ambayo ilibadilisha kila kitu.

SONGA NAYO...

1972, kisiwani Kome:

Kabila la Wazinza ni miongoni mwa makabila madogomadogo mkoani Mwanza, watu wa kabila hili hasa huishi wilayani Sengerema na makao yao makuu yakiwa kisiwani Kome na maeneo ya Nyakalilo wilayani humo. Wazinza ndilo kabila la asili wilayani Sengerema ndiyo maana eneo lote baada ya kuvuka tu kwenye kivuko cha Kamanga huitwa UZINZA!

Makabila mengine kama Wasukuma, Wakerewe, Wajita ni wahamiaji tu katika maeneo hayo ili kutafuta maisha baada ya kusikia maeneo hayo yalikuwa na rutuba ya kutosha!

Ukoo wa mzee Kamanzi ulikuwa mkubwa sana katika jamii ya Wazinza na ni ukoo ulioheshimiwa na kuogopwa na kila mtu ndani ya kabila hilo kwani uliaminika kuumiliki mzimu hatari ulioitwa Lutego! Mzimu huo uliua watu, ulimaliza koo mbalimbali na watu waliojaribu kwa namna moja au nyingine kupingana na ukoo huo.

Mtu yeyote aliyefanya maudhi katika ukoo wa Kamanzi alitumiwa mzimu wa Lutego uliwaua ndugu zake wote katika ukoo wake tena mmoja baada ya mwingine mpaka kuumaliza kabisa ukoo huo, katika Nyumba iliyotupiwa mzimu huo viumbe vyote vyenye damu kuanzia watu, mbuzi, kuku hadi sisimizi vilikufa!

Ukoo wa Kamanzi ulitisha! Hakuna mtu aliyethubutu kuigusa familia yoyote katika ukoo huo, mzimu wa Lutego uliokuwepo katika familia hiyo kwa miaka karibu mia tano iliyopita, ukihama kutoka kwa mtu mmoja hadi mwingine kutoka kwa kizazi kimoja hadi kingine.

Ni mwanamke mmoja tu katika ukoo aliyeteuliwa kuishi na mzimu huo ndani ya mwili wake, huyo walimwita Malkia au Maha! Na huyo Maha alipokufa alimwachia mtoto wake yeyote wa kike katika familia yake ambaye mzimu ulimwingia naye alikaa na mzimu huo mpaka mwisho wa uhai wake na alipokaribia kufa alimrithisha mtoto wake mzimu huo.

Mzimu huo ulirithishwa kwa mtu mwingine kwa kumpa hirizi ya chuma ambayo ilitoka yenyewe mwilini kwa Maha aliyekufa kabla ya kuzikwa! Hirizi hiyo alilishwa mtoto aliyechaguliwa kuurithi mzimu huo siku chache baada ya mazishi tena usiku wa manane katika sherehe kubwa iliyofanyika katikati ya ziwa Victoria na watu wengi walioamini uchawi walihudhuria, ilikuwa ni lazima watoto wawili mapacha watolewe kafara kabla Maha hajameza hirizi.

Mrithi wa mzimu huo katikati ya miaka ya sitini na sabini alikuwa Bi Isabella Katikilo, mama huyu aliabudiwa sana na ukoo mzima na alikuwa mwanamke mzuri ambaye ilikuwa si rahisi hata kidogo kufahamu kwamba alitembea mwilini na mzimu uliowaua watu!

Baadaye mama huyo aliolewa na bwana Innocent Mataruma na kuzaa naye mtoto mmoja wa kike wakampa jina la Bibi Anna ambalo baadaye lilikuja kubadilishwa na sista mmoja huko Kome aliyemwita mtoto huyo Anne! Mtoto huyo alikuwa mtoto mzuri na aliyemvutia karibu kila mtu aliyemwona na wengi walipenda kumbeba mtoto huyo.

Wana ukoo walioijua siri ya Isabella Katikilo walimsikitikia mtoto huyo kuzaliwa katika ukoo huo kwani walijua ni yeye ndiye angeurithi mzimu wa Lutego!

Shuleni akiwa na umri wa miaka saba Anne alionyesha uwezo mkubwa sana katika masomo yake, tangu darasa la kwanza hadi la saba alishika namba moja kila siku katika masomo yake, kila mtu aliamini Anne angekuja kuwa mtu mkubwa katika maisha yake!

Alipofaulu mtihani wake wa darasa la saba na kuingia kidato cha kwanza katika Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Ngaza iliyopo mjini Mwanza, hakuna mtu aliyeshangazwa na matokeo hayo kwani hilo lilikuwa ni tegemeo la watu wengi.

Uzuri wa sura yake shuleni ulifanya wanafunzi wengi kumbadika jina la ‘Miss Ngaza’. Alikuwa mrefu, alikuwa na miguu ya kuvutia na alikuwa na umbile zuri la kuvutia kwa nyuma! Kila mtu alimtamani Anne si walimu tu bali hata wanafunzi wa shule jirani ya Nsumba iliyokuwa ya wavulana tupu!

Magari ya matajiri wa Mwanza mjini kila siku ya kutembelea wanafunzi ilipofika, walifurika wakimtaka msichana huyo, lakini hakuna aliyefaulu kuiona nguo ya ndani ya Anne, wasichana wenzake walimshangaa kwanini kwa uzuri aliokuwa nao hakuwa na mpenzi ambaye angemtunza badala ya kuendelea kupata shida ndogondogo shuleni!

“Kwanini usimkubali tu hata Huggins?” Dina rafiki mkubwa wa Anne alimwambia kila siku iliyokwenda kwa Mungu.

“Siwezi Dina, ningependa kuwa na mpenzi lakini siwezi kufanya hivyo!”

“Kwanini lakini?”

“Siwezi kukueleza hata siku moja hiyo ni siri yangu mimi mwenyewe!”
Anne alihitaji sana kuwa na mpenzi lakini maneno aliyoambiwa na mama yake kabla hajaondoka nyumbani yalimtisha!

“Mwanangu Anne usijaribu kufanya mapenzi na mwanaume yoyote katika maisha yako kabla hujanirithi mimi, wewe ndiye mrithi wangu ni lazima uyatayarishe makazi ya nanihii sawa?”

“Makazi ya nani mama?”

“Utakuja kufahamu baadaye ila usijitie najisi bure na siku utakayofanya hivyo mwanaume utakayefanya naye atakufa kifo kibaya sana mbele ya macho yako!” Yalikuwa ni maneno ya mama yake yaliyomtisha mno Anne na kumfanya awaogope wanaume.

Ndiyo aliogopa lakini alipofikisha umri wa miaka 17 akiwa kidato cha tatu mwili wake ulianza kumlazimisha afanye tendo hilo na kujiliwaza.
****
“Anne tangu leo nimekuchagua utakuwa unanipikia chai hapa ofisini kwangu!” ilikuwa ni sauti ya mwalimu mkuu wa shule ya wasichana ya Ngaza aliyeitwa Joseph Lutambi!.

“Sawa mwalimu nakushukuru sana na nitakuwa mwaminifu!” Alijibu Anne.

Hiyo ndiyo ilikuwa tabia ya mwalimu Lutambi, kila mwaka alibadilisha msichana wa kumpikia chai, alimchukua huyu na baada ya kufanya naye mapenzi alimfukuza ofisini kwake na kuchagua tena msichana mwingine! Ofisi yake ilikuwa ni kama nyumba ya wageni ya chapuchapu na ilikuwa na kitanda ambacho yeye alidai ni cha kujipumzisha nyakati za mchana, ukweli ni kwamba hakikuwepo kwa ajili ya kazi hiyo bali kazi ya kufanyia ngono na wanafunzi kila walipomtayarishia chai mwalimu Mkuu ofisini kwake.

Siku zote alimtamani Anne sifa zake alizipata kuwa hakuwa na uhusiano na mvulana yoyote na iliaminika alikuwa bikira!
“Nitamuanza mimi, mimi dume bwana!”
****
Ilikuwa siku ya Ijumaa mchana wakati wa mapumziko ya chakula cha mchana mwalimu Lutambi alimwita Anne ofisini kwake, mvua kubwa sana ilikuwa ikinyesha kiasi kwamba Anne alilowa wakati akikimbia ofisini kwa Mwalimu.

Alipoingia tu ofisini mwalimu alifunga mlango nyuma ya Isabella na kudumbukiza funguo mfukoni mwake.

“Anne leo nataka ufanye kama ambavyo wenzako waliopitia ofisi hii wamekuwa wakifanya!”

“Kwa vipi mwalimu?”

“Ni lazima tulale!”

“Tulale una maana gani mwalimu!”

Kabla mwalimu Lutambi aliyekuwa mrefu na aliyejaza misuli mingi hajajibu swali hilo alimkamata Isabella na kumtupia kitandani!
Akampanua miguu yake kwa nguvu! Mvua kubwa tena ya mawe ilikuwa kinyesha kiasi kwamba sauti ya Anne haikufika nje ya ofisi iliyokuwa imefungwa vilivyo!

“Mwalimu niachie mimi sitaki mchezo huo!”

“Hutaki nini? Wenzako wote wamewezaje uwe wewe?”

“Mwalimu kwangu mimi ni mwiko utapata matatizo!”

“Matatizo gani? Acha yaje tutakabiliana nayo mimi najulikana hadi wizarani siogopi kitu!”

“Siyo hivyo utakufa!”

“Nitakufa? Ataniua nani na mimi ni jiwe!”

“Mwalimu utakufa!”

Ilikuwa kukurakakara kitandani hatimaye mwalimu alifanikiwa kumwingilia Isabella kwa nguvu, alikuwa amembaka msichana yule mdogo na kumharibu.

“Anne kumbe ulikuwa bado?”

Anne hakujibu kitu aliendelea kulia, ghafla mwalimu Lutambi alianguka chini mbele ya Anne, macho yakamtoka na ulimi ukatoka nje urefu wa mkono wa binadamu na kuning’inia chini na mwili wake ulikakamaa ghafla, damu nyingi zikimtoka masikioni, puani na mdomoni, alikuwa amekufa!

Anne alinyanyuka kitandani akiwa katika maumivu makali na damu zikimtoka sehemu za siri alikuwa akilia machozi.

“Unaona sasa mwalimu nilikuambia uache hukunisikiliza!” alisema Anne kwa huzuni.

Je nini kitatokea?
 
SEHEMU YA 03


Anne anakataa kwa kumwambia mwalimu kwamba atakufa. Mwalimu Lutambi anabisha, anajiona mwanaume wa shoka, anamvamia Anne na kuanza kumbaka. Anapomaliza, ghafla anaanguka chini na kuanza kuhangaika, mwisho wa siku, anafariki dunia.

SONGA NAYO...

Pamoja na udhaifu wa kufanya mapenzi na wanafunzi mwalimu Lutambi alikuwa kipenzi kikubwa cha wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Ngaza, hakuwa mkali kwao na alipenda sana kuendeleza taaluma, ni katika kipindi chake cha utawala ndiyo Shule ya Ngaza ilifanya vizuri zaidi kiasi cha wanafunzi kumi hadi ishirini kufaulu kwenda kidato cha tano!

Mwalimu Lutambi hakuwa kipenzi cha wanafunzi peke yake bali pia waalimu wenzake katika shule hiyo, aliishi nao vizuri na alijitahidi kuwatafutia nafasi mbalimbali za masomo ni katika kipindi cha utawala wake, waalimu watano kutoka shule hiyo walipata nafasi ya kuendelea na masomo ya chuo kikuu kuchukua digrii ya kwanza ya elimu!

Hivyo kifo chake cha ghafla kiliwashtua watu wengi, karibu kila mtu shuleni alilia, hakuna aliyejizuia! Familia yake ilichanganyikiwa na mkewe ambaye ndiye alikuwa amejifungua mtoto wao wa kwanza alilia mpaka kupoteza fahamu.

“Mume wangu alikuwa mzima tangu asubuhi wala hakuwa na homa, imekuwaje afe ghafla kiasi hiki?” alilia mwanamke huyo aliyejulikana kwa jina la Rosemary!

Wengi walishindwa kukieleza vizuri kifo cha mwalimu Lutambi na walimu walijiuliza maswali mengi bila majibu maafisa elimu wa mkoa na wilaya walipokuja, nao walichanganyikiwa kwa sababu kuliko na wiki kama moja tu mbele kabla mkutano wa wakuu wa shule haujafanyika.

Anne alikuwa katika wakati mgumu sana, wakati huo tayari alikuwa bwenini akiwa amejifunika na shuka akilia kwa sababu ya maumivu makali aliyokuwa nayo sehemu zake za siri! Mwalimu Lutambi alimjeruhi vibaya mno kiasi kwamba alishindwa hata kusimama wima.

“Hebu nendeni mkamwite Anne bwenini ili aje atueleze alichokishuhudia kabla ya kifo cha mwalimu!” mwalimu mkuu msaidizi aliwaamuru wanafunzi waliokuwa nje ya ofisi yake wakilia na wanafunzi watatu wa kidato cha pili waliondoka wakikimbia kuelekea bwenini ambako walimkuta Anne akiwa kitandani kwake.

“Unaitwa na mkuu wa shule msaidizi”

“Nikafanye nini jamani mimi naumwa?”

“Hata sisi hatujui!”

“Sawa basi nakuja!”

Baada ya kujibiwa wanafunzi waliondoka tena mbio kurudi ofisini ambako waliwakuta walimu wote wamekusanyika wakimsubiri Anne.

Anne aliteremka polepole kitandani kwake na kuanza kuchechemea akielekea ofisini kwa mwalimu, macho yake yalikuwa mekundu kwa sababu ya kulia, alielewa ni kwanini alikuwa anaitwa, alijua walimu walihisi alielewa chanzo cha kifo cha mwalimu Lutambi! Ingawa kweli alifahamu sababu ya kifo lakini hakuwa tayari kuitoa!

Anne alikuwa tayari kufa kwa maumivu ya kubakwa aliyokuwa nayo kuliko kudiriki kufungua mdomo wake kusema maneno aliyoambiwa na mama yake ambayo aliamini ndiyo yalikuwa chanzo cha kifo cha mwalimu, alishindwa kuelewa angelifafanua vipi jambo hilo wakati hata yeye mwenyewe hakuielewa siri ya maneno aliyoambiwa na mama yake.

Kabla hajaingia ofisini alikutana na mwalimu wake wa Biolojia aliyeitwa mwalimu Kassanda, mwalimu aliyeonyesha kushangazwa na mwendo wa Anne.

“Anne vipi mbona unachechemea?”

“Nilijikwaa jana na tayari nina mitoki miwili mapajani hiyo ndiyo inanisumbua!” Anne aliuficha ukweli, hakuwa tayari kusema kitu chochote ambacho kingepelekea kugundulika kwa kilichotokea ofisini.

Kwa taabu alipanda ngazi na kuingia ofisini ambako aliwakuta walimu wote wamekaa duara wakimsubiri, walikuwepo pia maafisa elimu wa wilaya na mkoa, dada mkuu na kaka mkuu, kiti cha Anne kiliwekwa katikati ya walimu wote baada ya salamu walianza kumuuliza maswali wakitaka kujua kilichotokea kabla mwalimu hajaanguka chini na kufa!

“Anne hebu tuambie kilichotokea nafikiri wewe ndiye ulikuwa ukimpikia chai siyo?”

“Ndi….o…mwali….mu!” Anne alijibu kwa shida na alishindwa kuendelea.

“Kilitokea nini mpaka mwalimu akafa?” Afisa elimu alidaka kwa swali.

Badala ya kujibu swali hilo Anne alianza kulia tena walimu wote alijaribu kumbembeleza bila mafanikio, nusu saa baadaye akiwa bado yupo ofisini alitulia na walimu waliendelea kumdadisi ili aeleze kilichojitokeza.

“Hata mimi sijui!”Alijibu jibu la mkato.

“Ndiyo hujui, lakini kilitokea nini kabla?”

“Baada tu ya kumpa chai kabla hata hajainywa alianguka chini akaanza kutokwa damu puani na masikioni, macho yakamtoka na ulimi wake pia ukaning’inia nje, nilishtuka sana nikaanza kupiga kelele nikiomba msaada ndipo mwalimu Malima alipokuja na kumkuta mkuu wa shule ameanguka chini amekufa!

“Uliweka kitu kingine kwenye chai?” Afisa elimu alihoji tena.

“Hakuna kitu zaidi ya sukari na majani mkuu!”

“Kweli?”

“Ndiyo mwalimu!”

Kila kona ya shule ya Ngaza ilifunikwa na vilio, wanafunzi walilia na kugalagala chini wakimlilia mwalimu wao Lutambi, kifo chake kilikuwa cha ghafla sana na kilisababisha mshtuko mkubwa mno miongoni mwao! Jina la mwalimu Lutambi lilitajwa kila sehemu katika vilio vya wanafunzi wake.

Hali hiyo ilimsikitisha sana Anne ambaye pia alishindwa kuelewa ni nini hasa kilimpata mwalimu Lutambi mpaka kufa kifo cha aina ile tena baada ya kumbaka!

“Mwanangu Anne usije ukafanya tendo hilo mtu utakayefanya naye atakufa!” Maneno ya mama yake yalimwijia kichwani.

Pamoja na kuyakumbuka maneno hayo bado alishindwa kuelewa ni kitu gani kilichomuua mwalimu Lutambi, kifo chake pamoja na kwamba alimbaka kilimfanya amwonee huruma mwalimu kwa yaliyompata! Anne alilia akimtupia mama yake lawama nyingi.

****
Ndugu wa marehemu mwalimu Lutambi walishinikiza mwili wake ufanyiwe uchunguzi kabla ya kuzikwa na pia chai iliyokuwa mezani kwake kabla ya kifo ilichukuliwa na kupelekwa kwa mkemia mkuu Dar es Salaam ili kufanyiwa uchunguzi kwani kulikuwa na hisia pengine Anne alimnywesha mwalimu Lutambi sumu! Aliitwa kituo cha polisi kutoa maelezo yake na ilibidi kwa siku nne atiwe ndani ili kuisaidia polisi katika upelelezi wake.

Majibu ya uchunguzi wa mwili marehemu yalipotoka yalionyesha mwalimu Lutambi alikufa kwa ugonjwa wa shinikizo la damu! Ni majibu hayo ndiyo yaliyomweka huru Anne kutoka mahabusu ingawa ndugu wa marehemu hawakuridhika na majibu hayo.

Mazishi ya mwalimu huyo kipenzi cha wanafunzi yalifanyika katika Makaburi ya Nyegezi mjini Mwanza na wanafunzi wa shule zote za jirani ya Ngaza walihudhuria mazishi yake na kufanya idadi ya watu waliokuwepo mazishini kuwa wengi mno.

Anne alijisikia vibaya kila alipoona watu wakilia machozi makaburini, alijua wazi ni yeye aliyesababisha machozi ya watu wote kumwagika alijisikia muuaji ingawa hakufahamu aliua vipi? Hata yeye hakufahamu ilivyotokea ingawa aliamini wazi mama yake alifahamu chanzo cha kifo hicho!

Mwezi mmoja tu baada ya mazishi mwalimu majibu kutoka kwa mkemia mkuu nayo yalirudi na kuonyesha chai aliyokunywa marehemu siku ya tukio pia haikuwa na sumu yoyote kama ilivyodhaniwa! Na wanafunzi waliokuwa wameanza kumchukia Anne wakifikiri alimpa sumu mwalimu wao walifurahi kupata majibu yao na uhusiano wao na Anne aliyetengwa na wanafunzi wenzake ulianza kurejea.

Lakini pamoja na hali hiyo ndani ya nafsi yake Anne hapakuwa na amani hata kidogo, aliendelea kujisikia muuaji kwani alijua wazi kuwa kifo cha mwalimu kilimhusu.

“Nikienda likizo ni lazima mama anieleze ni kwanini mwalimu alikufa na ni kwanini aliniambia nisifanye mapenzi, nitafanyeje mimi wakati mwili wangu unahitaji? Sitakubali nataka kujua!”
****
Miongoni mwa watu ambao hawakuamini kuwa kifo cha mwalimu Lutambi kilisababishwa na shinikizo la damu alikuwa ni kaka yake marehemu, Leonard huyu aliamini sana uchawi na ushirikina, baada ya mazishi alilazimika kusafiri hadi sehemu za milima huko Sumbawanga, kwa mganga mmoja wa kienyeji ili kufahamu vizuri chanzo cha kifo cha mdogo wake na jibu alilopewa na mganga wake maarufu mzee Kipili lilimtia hasira kubwa hasa baada ya kuonyeshwa picha ya Anne katika beseni la maji na kuambiwa ni yeye ndiye alimuua mwalimu si kwa sumu bali kwa uchawi wa kabila la Wazinza.

“Msichana huyo ni malkia mtarajiwa na hatakiwi kufanya mapenzi na mtu mpaka atakapoolewa na ikitokea akifanya hivyo mwanaume atakayefanya naye atakufa! Nduguyo alimbaka msichana huyo ndiyo maana akafa!”

“Kweli?”

“Ndiyo!”

Baada ya kutoka hapo Leonard alikwenda tena kwa waganga wengine watatu na jibu liliendelea kuwa hilohilo na kuamua kurejea nyumbani Mwanza akiwa na hasira zake kifuani.

Jambo la kwanza alilolifanya baada ya kufika Mwanza ni kuwataarifu ndugu zake juu ya majibu aliyoyapata na kila mtu alisikitika sana, hasa mke wa marehemu na jioni ya siku hiyo hiyo Leonard aliivamia Shule ya Ngaza akiwa na panga mkononi na kufanya fujo kwa lengo la kumshambulia Anne na kumuua lakini walinzi wa shule walifanikiwa kumzuia kabla hajafika bwenini kwa Anne na kumuondoa shuleni.

“Weweeeeeee! Unataka uniue mimi nimekukosea nini?” Anne alisema huku akimsonta na kidole.

“Usitembee kabisa mitaani, siku yoyote nitakayokuona nje ya ngome hii nitakumaliza! Huwezi kumuua ndugu yangu hivihivi mchawi mkubwa wewe!” Alifoka Leonard huku wanafunzi wakiwa wamejaa na kushangaa.

Baada ya kufoka Leonard aliondoka zake, kilichosikitisha zaidi siku iliyofuata taarifa zilikuja shuleni wengi walisikitika mzee yule aligongwa na treni na kufa!

Baada ya siku hiyo hisia zilianza kusambaa kuwa Anne pamoja na uzuri wake alikuwa mchawi na akawa anaogopa hata kutoka shuleni kwa vitisho vya ndugu wengine wa marehemu mwalimu Lutambi.
****
Shule ilipofungwa gari la shule lilimchukua hadi kituo cha mabasi ambako alipanda basi la kwenda Sengerema, nyumbani kwao alimsimulia mama yake kila kitu.

“Mama hali ni mbaya sana shuleni!”

“Kwanini mwanangu!”

“Watu wawili wameshakufa kwa sababu yangu!”

“Kwanini ulifanya mapenzi na mtu?”

“Nilifanya lakini si kwa ridhaa yangu mwalimu wangu alinibaka na palepale alikufa! Wa pili ni ndugu yake yeye alikuja shuleni na panga kwa lengo la kutaka kuniua kesho yake tulisikia kuwa aligongwa na treni akafa!”

Anne alieleza kila kitu juu ya yaliyompata na kutaka kujua kutoka kwa mama yake kilichokuwa kikiendelea.

“Siwezi kukueleza kitu hivi sasa mwanangu utafahamu baadaye mimi nikifa ila bado nasema hutakiwi kufanya tendo la ndoa na mtu yeyote yule mpaka baada ya mimi kufa na wewe kuolewa na hutakiwi kumnyoshea mtu kidole, ukifanya hivyo tu mtu huyo atakufa!”

“Mama nini lakini? Hebu tafadhali nieleze kinachoendela nataka kufahamu siwezi kuendelea kuishi hivi!” Anne alijikuta akifoka.

“Hapana Anne nikikueleza sasa hivi nitakufa mimi, sitaki kabisa kutoboa siri hii!”

Anne alilia machozi kwani alitaka sana kufahamu jambo lililokuwa likiendelea mwilini mwake na alikumbuka kumwonyesha kidole kaka yake marehemu mwalimu Lutambi!

“Ndiyo sababu alikufa, jamani mimi nitaishije katika hali hii?”
****
Baada ya likizo yake Anne alirejea tena shuleni na kuendelea na masomo, wanafunzi wenzake walishirikiana naye vizuri ingawa kuna baadhi bado walimwogopa kwa madai alikuwa mchawi ingawa hapakuwa na mtu aliyekuwa na uhakika na jambo hilo.

Pamoja na hayo bado Anne aliendelea kuwavutia na wanaume wengi walioendelea kumsumbua wakimtaka mapenzi kila siku, hata walimu wake hawakumwogopa, hakuna aliyekuwa tayari kuamini kuwa Anne ndiye alimuua mwalimu Lutambi!

Wavulana wengi waliokuja shuleni kuwatembelea wasichana wao walipomwona Anne walishtuliwa sana na uzuri wake na kujikuta wakianza kumfukuzia kwa nguvu na wakati mwingine walipoleta zawadi kwa wapenzi wao na yeye walimletea kama njia ya kumsogeza karibu.

Mmoja wa wavulana waliovutiwa sana na uzuri wa Anne alikuwa Dioniz Edward , huyu alikuwa ni mmoja wa vijana waliojaliwa sura nzuri sana duniani kiasi kwamba wanafunzi wenzake wa Shule ya Nsumba alikokuwa kiranja mkuu walimbandika jina la School HB, wakiamaanisha yeye ndiye alikuwa mzuri kuliko wavulana wote shuleni kwao!

Dioniz alikuwa mpenzi wa Emmaculata, msichana aliyesoma darasa moja na Anne, mara kwa mara alikwenda shule ya Sekondari ya Ngaza kumtembelea msichana Emmaculata ambaye pia alikuwa mrembo kupindukia, ingawa si kama Anne! Kama ni urefu wote walikuwa warefu na kama ni miguu mizuri wote walikuwa nayo na kama ni mianya wote walikuwa nayo!

“Emma kwa kweli ninampenda sana msichana huyu!”

Mwanzoni Emmaculata alifikiri labda alichoambiwa na Dioniz kilikuwa ni utani, lakini alishangaa mwezi mmoja baadaye alipowakuta Anne na Dioniz wamesimama peke yao ufukweni, siku hiyo Dioniz alikuja shuleni bila kumtaarifu Emmaculata na kwenda ufukweni kutanua na Anne!

Emmaculata alilia na kuanza kumvuta Dioniz lakini haikuwezekana kumshawishi kwani alishalewa penzi la Anne! Dioniz alikataa kuondoka.

“It is too late Emma, at the moment I’m in love with Anne!”(Umechelewa Emma kwa sasa hivi nina mapenzi kwa Anne!)

“Kweli Dioniz?”

“Ndiyo!”

“Hebu njoo basi kwanza nikueleza kitu!”

Dioniz aliitikia mwito huo na kumfuata Emmaculata pembeni alipokuwa amesimama huku Anne akitabasamu pembeni!
“Huyu msichana ni mchawi utakufa Dio!”

“I’don’t care, jambo hilo nimelisikia sana lakini najua huo ni uongo mnampakazia ili asifukuziwe!”

“Dio!”

“Nini?”

“Achana naye huyo binti!”

“Haiwezekani tena Emma niache nifanye kitu ambacho moyo wangu unataka!”

Kwa hasira Emma alimfuata Anne na kuanza kumfokea matusi makubwa akimwita mchawi aliyetumia madawa kuvuruga mapenzi ya watu!

“We Emma usinitukane tafadhali!”

“Nini? Fanya unachotaka!”

Anne alipotaka kumsonta Emma kwa kidole chake aliyakumbuka maneno ya mama yake “Siku zote usimsonte mtu yeyote kidole ukifanya hivyo atakufa!”

Baada ya siku hiyo Anne na Emmaculata walinuniana kwa sababu ya Dio! Na mwili wa Anne ulizidi kusisimka na kumfanya atamani kuwa na uhusiano wa kimapenzi na Dio hasa alipowasikia wanafunzi wenzake wakiliongelea tendo hilo bwenini, alitamani sana kuwa na mpenzi lakini aliogopa kuua tena kama ilivyotokea kwa mwalimu Lutambi Lakini baadaye alilazimika kumkubali Dio

“Dio nimekubali lakini mimi na wewe hatutafanya tendo la ndoa ila tutafanya mapenzi ya kiwokovu, tutaongea kubadilishana mawazo lakini siyo ngono!”

“Unaogopa Ukimwi sana eeh!”

“Sanaaaaa, sitaki kufanya mapenzi kabla ya wakati!”

“Mimi bora tu niwe na wewe darling!”

Walikumbatiana na kupigana mabusu! Walipoachiana Dioniz alikuwa akiumwa kichwa ghafla lakini baadaye kilitulia, alipomwambia Anne kuhusu maumivu hayo aliielewa sababu.

Uhusiano wao ulidumu kwa muda mrefu sana na mara kwa mara Dioniz alimtembelea Anne shuleni, Anne pia alifanya hivyohivyo! Katika uhusiano wao hata siku moja hawakuwahi kufanya tendo la ndoa ingawa mara nyingi Dioniz alijaribu kumwomba Anne wafanye hivyo.
****
Ilikuwa ni siku ya mawingu na ngurumo nyingi angani lakini ni siku ambayo muziki mzito ulitanda kila mahali ndani ya ukumbi wa shule ya Ngaza, ilikuwa ni siku ya furaha, wanafunzi wakifurahia wenzao kumaliza kidato cha nne! Wakati huo Anne alikuwa kidato cha tatu akiwa na mwaka mmoja mbele kumaliza masomo yake ya sekondari.

Wavulana kutoka shule za sekondari ya wavulana Nsumba pamoja na Bwiru walikuwa shuleni hapa kucheza muziki na wasichana wa shule hiyo ya wasichana tupu, mmoja wa wanafunzi wa Nsumba waliokuokuwepo shuleni alikuwa ni Dioniz, aliyekuwa amemkumbatia Anne wakicheza bluzi pamoja, wote wawili walilingana urefu! Katika kucheza alimng’atang’ata Anne shingo na kumsemea sikioni jambo lililomfanya Anne ashindwe kuvumilia na kumfanya aanze kumtamani Dioniz.

“Labda leo itakuwa siku tofauti acha tu nijaribu lakini nampenda sana Dioniz nisingependa kumuua!” Anne alijipa moyo.

“Anne kwanini leo tusifanye kumbuka tumevumiliana sana?”

“Kufanya nini Dio?”

“Kwani wewe hujui?”

Ingawa alitamani kufanya hivyo Anne alijifanya kugoma, kitu pekee kilichomtisha kilikuwa ni kumbukumbu za kifo cha mwalimu Lutambi lakini baadaye alikubali.
****
Ilikuwa ni saa sita kamili ya usiku disko lilikuwa limepamba moto Dio na Anne walipotoka nje ya ukumbi na kwenda gizani bustanini ambako waliendelea kutomasa miili yao! Ilikuwa ni siku ya kwanza kwa Anne kusikia raha kama vile akiguswa na mwanaume aliyempenda.

“Lakini kichwa kinaniuma sana!” Dio alisema.

Muda mfupi baadaye Anne ilizidiwa mahaba na kujikuta akilala ardhini na Dionizi alimfuata bila kuchelewa na wote wawili walijikuta akili zao zikipepea angani! Akili za Anne zilirejea aliposhtukia matone ya damu yakimlowanisha begani! Alipomwangalia vizuri Dioniz aliuona ulimi wake ukiwa nje na macho yake yalikuwa yamemtoka! Picha ya marehemu mwalimu Lutambi ilimwijia akilini akajua Dio kafa!

Aliusukuma mwili wa Dio pembeni na kuanza kuutingisha akimwita jina lake lakini alikuwa ametulia.

“Dio! Dio! Dio! Dio!” Anne aliita mara nyingi lakini Dioniz hakutingishika na damu nyingi zilizidi kutoka puani na mdomoni!

“Dioniz umekufa!” Alisema Anne huku akilia mwili wake wote ulitetemeka kwa hofu.

“Sijui nitawaweleza nini wanafunzi wenzake! Ni lazima nitafute njia ya kuuficha ukweli huu kabla haujajulikana!” Aliwaza Anne kisha kuangalia huku na kule!

Baada ya mawazo hayo alitoka mbio hadi bwenini na kulivua shati lake lililokuwa na damu na kuvaa tisheti nyingine iliyokuwa na madoa ya damu aliichoma moto na bila kuchelewa alianza kutembea kuelekea tena bustanini alikomuacha Dioniz.

Alipofikiria kuhusu kuchimbia shimo ili aifukie maiti alishindwa kwa sababu hakuwa na jembe wala koleo, alipoangaza pembeni aliliona shimo la maji ya chooni na kukimbia hadi lilipokuwa na kulifungua.

“Hili linafaa!” Alijisemea mwenyewe moyoni mwake na kurudi hadi maiti ya Dio ilipokuwa na kuanza kuivuta hadi pembeni mwa shimo lile lengo lake likiwa ni kuidumbukiza lakini aligundua isingezama bila kufungwa na kitu kizito, alikimbia hadi jikoni ambako alichukua kamba mbili ndefu akaja na kuifunga na kuidumbukiza shimoni, alipomaliza kazi hiyo alifunika vizuri na kuondoka taratibu kuelekea ukumbini ambako aliendelea kucheza muziki huku akilia machozi.

Je nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 04


Kwa uchungu mkubwa moyoni mwake, tena huku akiwa analia kama mtoto, Anne anaanza kusimulia kilichotokea maishani mwake na sababu iliyosababisha kumuua mama yake, historia ambayo ilibadilisha kila kitu.

Historia ya maisha yake inaanzia shule, huku akiwa hajui kama amepewa uchawi, mama yake anamtahadharish
a kwamba hatakiwi kufanya mapenzi na mwanaume yeyote yule kwani akifanya hivyo mwanaume huyo atakufa.

Mtu wa kwanza kabisa kufa alikuwa mwalimu wake, Lutambi. Anapoitwa na kuhojiwa, anakataa katakata. HAikuishia hapo, anajikuta akimuua mtu wa pili ambaye ni mwanafunzi handome aitwae Dioniz.

Hajui ni nini anachotakiwa kukifanya, akili yake imechanganyikiwa.

SONGA NAYO...

Anne alikuwa mwenye mawazo mengi, machozi yalizidi kumtoka alishindwa kuelewa nini kilikuwa kikitokea katika maisha yake.

“Tayari mtu wa pili amekufa sababu yangu, hivi nini hasa kilichomo mwilini mwangu? Ni mkosi gani nilionao mimi masikini?” alizidi kuwaza Anne.

Anne alijaribu kucheza muziki lakini haukuchezeka, mwisho aliamua kukaa kitini na kuendelea kufikiria jinsi ambavyo angekabiliana na tatizo lililokuwa mbele yake, alijua muda si mrefu Dioniz angetafutwa na wanafunzi wenzake kabla hawajaondoka shuleni na kwa sababu yeye alionekana naye kwa mara ya mwisho ni lazima angetakiwa kueleza mahali alikokuwa. Mawazo hayo yalimfanya Anne ashindwe kuvumilia na kujikuta akilia machozi.

Alipojaribu kumkumbuka Dioniz na kifo chake roho ilimuuma sana, Dioniz kijana mwenye sura nzuri alikuwa ndani ya shimo la maji machafu kutoka chooni, alipowaza hilo roho ilimuuma zaidi! Alijiona ni mkosaji mkubwa mbele ya Mungu!

“Yaani katika umri huu mdogo tayari nimekwishafanya mauaji ya watu wawili?!” aliwaza Anne na kuendelea kulia.

“Dada twende tukacheze!” Mvulana mmoja alisimama mbele ya Anne na kumwomba wakacheze wote.

“Mimi?”

“Ndiyo!”

“Sijisikii vizuri kwani hali yangu si njema nimebanwa sana na mafua”

“Kweli?!”

“Niwie radhi kaka yangu!” Anne alimjibu kijana mmoja wa Shule ya Sekondari ya Nsumba aliyetaka kucheza naye Blues ya Michael Bolton iitwayo “Soul Provider!”

“Hakuna tatizo dada yangu! Nakumbuka nilikuona na HB! Yupo wapi?”

“HB ndiye nani kaka yangu?”

“Dioniz, sisi shuleni humwita HB kwa sababu ya uzuri wa sura yake!”

Moyo wa Anne ulidunda kwa nguvu kufuatia swali hilo, aliuhisi ukichomoka na kuuacha mwili wake, hofu kubwa ilimkumba kwani alijua baadaye angetakiwa kueleza mahali alipokuwa Dioniz! Alikaa kimya akiwa amemkodolea macho mvulana aliyemuuliza.

“Dada sijui kama umesikia swali langu?”

“Umeulizaje kweli kaka yangu? Maana hapa ndani muziki umepamba moto na una sauti kubwa sana!”

“Nilikuuliza kuwa Dioniz umemwacha wapi? Maana mara ya mwisho ulikuwa naye!”

“Ah! Dioniz!...Ah!... Tuliachana naye kitambo na yeye akarudi hapa ndani, mimi nikaenda bwenini labda jaribu kupitapita hapa ukumbini utamuona!” Alijibu Anne huku akitetemeka!

“Ok wewe si ni Anne lakini?”

“Ndiyo!”

“Aisee kwanza nimefurahi sana kukutana na wewe ana kwa ana mimi naitwa Benedict, nasoma darasa moja na Dioniz na lengo langu kuja hapa Nganza lilikuwa ni kukutafuta wewe, lakini bahati mbaya Dioniz ameniwahi kuonana na wewe lakini hakijaharibika kitu! Kwanza kabisa wewe Anne ni mzuri!”

“Ahsante sana Benedict lakini hata wewe ni mzuri pia!”

“Ahsante sana, je, unaweza kuniruhusu nikae na wewe kidogo!”

“Unasemajeee?”

“Hakuna matatizo yoyote kaa tuu!”

Walijaribu kuongea mambo tofauti kuhusu masomo na sherehe nzima iliyokuwa ikiendelea lakini baadaye Benedict alimwekea Anne mkono begani.

“Anne ninakupenda na tafadhali kubali kuwa na mimi na siyo Dio, ninakupenda sana Anne tafadhali usiniangushe!”

“Mungu wangu mwingine tena huyu, nitafanya nini mie? Ee Mungu ni kwanini uliniumba na uzuri huu, halafu nikawa na kasoro hii, nitaendelea kuua watu hadi lini?” Aliwaza Anne na badala ya kufurahi Anne alianza kulia machozi mbele ya Benedict moyo wake ulikuwa bado haujatulia, kifo kilichompata Dio kilikuwa bado kikimsumbua akilini.

“Vipi mbona unalia?”

“Naomba uniache kaka!”

“Haiwezekani Anne ni vizuri unipe jibu zuri kabla sijarudi shuleni!”

“Siwezi kuwa na uhusiano na wewe kimapenzi!”

“Kwanini?”

“Usiniulize kwanini! Kama kweli unajipenda, achana na mimi kabisa na ufuate mambo yako!”Alijibu Anne kwa ukali na kuanza kunyanyuka kuelekea nje ambako Benedict aliendelea kumfuata huku akimbembeleza akubali.

“Najua ni kwa sababu umekutana na Dio mwenye sura nzuri kuliko mimi ndiyo maana unakataa lakini Dio atakuchezea tu ana wasichana wengi sana, mimi nataka kukuoa kabisa kama tutaelewana!”alisema Benedict.

Juhudi za Benedict kumbembeleza Anne ili akubali ziligonga mwamba akaamua kurudi zake ukumbini, Anne naye alikwenda bwenini ambako alipanda kitandani na kuendelea kulia machozi, alishindwa kuelewa nini kingefuata.

Saa moja baadae alishitukia muziki umezimwa Bwaloni, aliponyanyuka na kuchungulia dirishani aliona wanafunzi wenzake wakitoka ukumbini huku wakishangilia na kufurahi, dakika kama mbili hivi baadaye wanafunzi wenzake wakaanza kuingia bwenini.

“Hakyanani ya leo ilikuwa kiboko, sijawahi kuona disco kali kama la leo hili!”

“Hata mimi!” wasichana wawili waliolala vitanda vya chini ya Anne sababu kitanda chao kilikuwa cha deki, waliongea huku wakivua nguo zao tayari kwa kwenda kuoga! Anne alikuwa amejifunika shuka hadi kichwani.

“Hivi viatu si vya Anne!”

“Ndiyo, yupo wapi?”

“Alitoka na yule handsome wa Nsumba naona leo mambo yake safi, aangalie tu asije naye akamuua kama alivyomuua mwalimu wetu Lutambi maana mimi yule huwa simwelewi hata kidogo!” mmoja wa wanafunzi wale alijikuta akitamka maneno yaliyomfikia Anne moja kwa moja chini ya shuka lake na kumuumiza moyo zaidi! Alihisi ni lazima alichokifanya kingejulikana.

Msichana mmoja alinyanyua uso wake kuangalia juu ya kitanda na alishangaa sana kugundua kuwa Anne alikuwepo kitandani!”

“Ha! kumbe yupo sijui kasikia?” alimnong’oneza mwenzake!”

“Kweli?”

“Ndiyo!”

“Lakini hajasikia hebu jaribu kumwita uone kama bado yupo macho!” Alishauri mmoja wa wasichana wale na mwenzake alijaribu kumwita Anne kwa jina lakini Anne hakuitika, alisikia kila kitu lakini aliamua kukaa kimya huku akiendelea kulia!

Machozi yaliendelea kumwagika na kulowanisha mashuka yake, baadaye wasichana wale waliondoka kwenda bafuni kuoga na wengine wengi waliendelea kuingia bwenini wakilisifu disco la siku hiyo!

Anne alipoangalia saa yake tayari ilionyesha saa tisa na nusu ya usiku! Na nje alisikia kelele za wanafunzi wa Nsumba wakimuulizia Dioniz.

“Yuko wapi?”

“Hata sisi hatujui lakini alikuwa na msichana mmoja wa hapa Nganza simkumbuki kwa jina!”

Hofu kubwa iliujaa moyo wake na alizidi kutetemeka, alilala macho yakiwa yameangalia nje ambako aliwaona wanafunzi wakizunguka huku na kule kumtafuta Dioniz bila mafanikio, moyo wake ulidunda kwa nguvu na aliendelea kutetemeka!

“Labda katangulia shuleni?”

“Kwa usafiri gani?”

“Huwezi kujua labda alipata lifti ya mtu yeyote, si mnajua tena Dioniz ni mtu wa usingizi hata muziki huwa hachezi labda aliboreka akaamua kutangulia shuleni cha msingi twendeni tukaangalie kwanza!”

Walimu na wanafunzi waliojitokeza kumtafuta Dioniz walikubaliana akaangaliwe kwanza shuleni kwao, wengi waliamini ni lazima angekuwa shuleni.

Anne aliyasikia vizuri majadiliano yao kutoka kitandani kwake, kauli ya kuamini kuwa alikuwa shule ilimpa ahueni moyoni, baadae alilisikia gari la Shule ya Nsumba likiondoka na moyo wake ukatulia.

Kupotea kwa Dioniz kulikuwa gumzo shuleni Nganza usiku huo, wanafunzi wengi walimfuata Anne kitandani kwake na kumuuliza mahali alikokwenda na Dio usiku lakini jibu lake liliendelea kuwa “Niliachana nae!”
****
Siku iliyofuata ilikuwa ni siku ya Jumapili na kwa sababu ya kuchelewa kulala wanafunzi wengi walichelewa kuamka pia, lakini kwa Anne ilikuwa tofauti aliwahi sana kuamka kabla jua halijachomoza na kwenda moja kwa moja bustanini, kwenye shimo la maji machafu kuangalia kama kulikuwa na dalili yoyote iliyoonyesha kuwa mtu alidumbukizwa ndani ya shimo hilo!

Anne aligundua alama za viatu vyake na mkwaruzo iliyojitokeza wakati akiuburuza mwili wa Dioniz kuupeleka shimoni.

“Hii itaniletea matatizo!” aliwaza Anne na kwa haraka bila kuchelewa alikata tawi la mti na kuanza kufuta alama zote ardhini, alipomaliza aliamua kuchungulia shimoni ili kuona kama mwili wa Dioniz ulikuwa ukielea juu juu!

Kabla hajaufunua vizuri mfuniko wa shimo la maji machafu, ghafla alisikia sauti ikiita jina lake kwa nyuma, alipogeuka alikuwa ni mwalimu wake wa somo la Biolojia, mwalimu Catherine!”

“Unafanya nini hapo asubuhi hii?”

“Ah! Ah! Ah! Unajua... mwalimu!...”

“Nini unachofanya hapo kwenye shimo!?”

Anne alikosa kitu cha kujibu na aligundua wazi kuwa siri yake ilikuwa imeanikwa ni lazima mwalimu wangetaka kujua kilichokuwa ndani ya shimo hilo. Mwalimu alizidi kumsogelea.

“Kuna nini humu shimoni?”

“Hakuna kitu mwalimu!”

“Hebu funua nione?”

Anne aliogopa kufanya hivyo, alihofia mwili wa Dioniz ungeonekana hakutaka hata mwalimu Catherine afunue hakutaka kabisa siri yake ijulikane!

“Hutaki kufunua siyo? Basi nafunua mwenyewe!”

“Hapana mwalimu, tafadhali usifunue hilo shimo”

“Kwanini?”

“Usifunue tu acha mwalimu utapata matatizo.”

“Matatizo gani?”

Mwalimu hakulijali onyo hilo la Anne na kuushika mfuniko wa shimo na kuanza kufunua.

Bila kuchelewa Anne alinyanyua mkono wake wa kulia na kumsonta mwalimu kwa kidole, polepole mwalimu alilegea na kuanguka juu ya sakafu ya shimo akiwa taabani huku mapovu yakimtoka mdomoni na puani.

“Mwalimu unaona sasa, mimi nilikuambia usifunue hilo shimo wewe ukang’ang’ania!”

“Sasa mimi ningefanya nini?” alisema Anne huku akiusogelea mwili wa mwalimu uliokuwa juu!

Anne aliangaza macho huku na kule na kugundua hapakuwa na mtu yeyote aliyekuwa karibu yake, wazo lilimwijia haraka kichwani na alisikia sauti ikimwambia “Na yeye mdumbukize shimoni!”

Anne alilikimbilia jiwe kubwa lililokuwa karibu na kulisogeza karibu kabisa na shimo, alimvua mwalimu khanga alizokuwa amejifunga kiunoni na kulifunga vizuri jiwe lile, kisha akalifunga kiunoni kwa mwalimu Catherine na kwa nguvu za ajabu ambazo hakujua alizipata wapi alimnyanyua mwalimu na kumpitisha katika tundu la shimo lile kisha akalidumbukiza jiwe pamoja naye, mwalimu alizama taratibu akipenya katikati ya maji machafu hadi kupotea kabisa!

Anne bila kupenda alimuua mwalimu Catherine kwa sababu tu alitaka kuificha siri ya mauaji ya Dio! Aliomba Mungu kusiwe na mtu mwingine yeyote aliyeshuhudia akimzamisha mwalimu Catherine shimoni.

“Kama kuna mtu kaona basi nimekwisha kabisa!”

Aliangaza huku na kule lakini hakuona mtu yeyote, mara ghafla jogoo likawika na alikimbia haraka kwenda bwenini ambako aliingia bafuni na kuanza kuoga, alipoyafikiria yote yaliyokuwa yakitokea katika maisha yake alimlaumu sana mama yake.

Alishindwa kuelewa ni nguvu gani iliyokuwa ndani ya mwili wake iliyofanya hata aue kikatili kiasi kile! Hakuamini zilikuwa ni nguvu za uchawi kwa sababu hakuwahi kufundishwa mahali popote! Maji yakiendelea kutiririka na kumlowanisha na kufanya atetemeke ovyo!
Akiwa wima kabla hata kuoga ghafla alishitukia mlango wa bafuni ukigongwa alipofungua walikuwa ni wanafunzi wenzake.

“Anne unaitwa ofisini kwa Mwalimu Mkuu haraka!

“Sawa!”alijua tayari mambo yamekwishaharibika na alihisi kuna mtu alimuona asubuhi ile akimdumbukiza mwalimu Catherine shimoni, mwili wake wote ulitetemeka alitoka mbio bafuni na kuanza kukimbia kuelekea kilipokuwa kitanda chake!

“Hey! Anne mbona unatembea bila nguo!”

“Ha! nimesahau taulo langu bafuni!”Alijibu Anne na kuanza kukimbia tena kurejea bafuni ambako alichukua taulo lake na kulivaa.

Alinyoosha moja kwa moja hadi kitandani kwake ambako alivaa nguo safi na kutoka kuelekea ofisini kwa Mwalimu Mkuu ambako alikuta walimu wote wamekaa wakimsubiri, mkutano ule ulimkumbusha siku alipokufa mwalimu Lutambi. Mmoja wa waalimu alikuwa kutoka Nsumba na alikuwa na watu wengine wawili ambao hakuwafahamu kabisa!

“Mbona unatetemeka Anne!” Mwalimu Mkuu aliuliza.

“Baridi mwalimu, nilikuwa naoga!”

“Baada ya jibu hilo Anne aliwageukia walimu na kuwaamkia.

“Msichana mwenyewe ndiye huyu hapa!” Mwalimu Mkuu alisema.

“Sawa!” Alijibu mwalimu kutoka Nganza

“Kwani kuna nini mwalimu!” Anne aliwauliza. Alijifanya kushangaa ingawa alifahamu kabisa ni kwa nini aliitwa ingawa hakuwa na uhakika ni suala la Diozin au la mwalimu Catherine.

“Eti binti ni wewe ndiye uliyekuwa na Dioniz jana usiku? Ulitoka naye nje?”

Je, nini kitatokea?
Je, mwalimu Catherine na Dioniz watagundulika shimoni?
 
Back
Top Bottom