Tafadhali mama usiwaue watoto wangu

Tafadhali mama usiwaue watoto wangu

SEHEMU YA 05


Mtu wa kwanza kabisa kufa alikuwa mwalimu wake, Lutambi. Anapoitwa na kuhojiwa, anakataa katakata. Haikuishia hapo, anajikuta akimuua mtu wa pili ambaye ni mwanafunzi handome aitwae Dioniz.

Hajui ni nini anachotakiwa kukifanya, akili yake imechanganyikiwa.

SONGA NAYO...

Kifo cha Dioniz kiliwasikitisha watu wengi sana, alikuwa kipenzi cha wanafunzi wengi shuleni kwao na si kwa wanafunzi peke yao bali hata walimu wake!

Lilikuwa ni pigo kwa kila mmoja wao na hakuna mtu aliyekuwa tayari kuamini Dioniz hakuwepo duniani! Wengi waliamini Dioniz alikuwa hai ila alikuwa ametoweka kwenda kusikojulikana na si ajabu Ulaya.

Wanafunzi wa Nsumba hawakuchoka kumtafuta, msako uliendelea usiku na mchana! Polisi nao walilazimika kuleta mbwa wa kunusa lakini hakuna mbwa hata mmoja aliyefanikiwa kuwapeleka kwenye shimo la maji machafu kulikokuwa na miili ya watu wawili.

Kwa siku saba Dioniz aliendelea kutafutwa bila mafanikio yoyote na hakuna mtu aliyehisi mahali alikokuwa wengi walijifariji kwa kusema Dioniz aliondoka shuleni kurejea nyumbani kwao kwa sababu katika kipindi hicho kulikuwa na tatizo ya ada ya shule kwa wanafunzi wengi! Lakini kwanini aondoke usiku? Wengi waliendelea kujiuliza bila majibu na walipofuatilia ofisini waligundua kuwa hakuwa na tatizo la ada ya shule.
***
Katika Shule ya Ngaza aliyosoma Anne hali ilikuwa mbaya pia, Emmaculata aliyekuwa mpenzi wa Dioniz kabla ya Anne kuyaingilia kati mapenzi yao alikuwa bado akimlilia Dioniz, aliamini kabisa Anne alifahamu vizuri mahali alikokuwa. Mara kwa mara alisisitiza upelelezi uzidi kufanyika na Anne abanwe ili aeleze.

Emmaculata hakuamini maneno kuwa Dioniz alipotea, wasiwasi wake mkubwa ulikuwa kuuawa na maiti yake kufukiwa ardhini lakini alipolitoa wazo hilo kwa watu walimbeza na kumpuuzia! Alitamani amuulize Anne lakini alishindwa kufanya hivyo, aliamini asilimia mia moja Anne alikuwa mchawi na angeweza kumfanyia lolote hata kumuua kabisa.
****
Ilikuwa ni siku ya pili Anne akiwa mwenye mawazo mengi juu ya mauaji aliyokuwa ameyafanya! Muda mwingi alikuwa akilia na kumlaumu mama yake, hakupenda kuwa jinsi alivyokuwa alitaka awe na uhusiano na mvulana kama walivyokuwa wasichana wengine, lakini kila mvulana aliyekutaka naye alikufa! Jambo hilo lilimsikitisha sana.

Ni siku hiyo hiyo saa 11:30 jioni taarifa zilipelekwa ofisini kwa mwalimu mkuu msaidizi kuwa mwalimu Catherine hakuwepo kazini kwa siku mbili! Mkuu wa shule msaidizi alituma watu kuangalia kama alikuwepo nyumbani kwake.

“Hatujamkuta, tumekuta mlango wa nyumba yake umefungwa!”
Walimjibu mkuu wa shule msaidizi waliporejea.

“Hakuna mtu yeyote anayeishi naye?”

“Anaishi peke yake ila Mkuyuni kuna mchumba wake!”

“Basi nendeni hukohuko Mkuyuni kwa mchumba wake mkamwangalie si ajabu anaweza kuwa mgonjwa!”

Waliporudi baada ya masaa mawili jibu lilikuwa lilelile kuwa mwalimu Catherine hakuwepo Mkuyuni, mkuu wa shule alipojaribu kudadisi kama alimuaga mtu yeyote hakuna aliyekiri! Alipotafutwa mtu aliyekuwa naye mara ya mwisho jibu lake liliwapa utata!

“Ile siku ya mahafali mimi nilikuwa naye zamu lakini ilipotimu saa kumi na moja alfajiri aliondoka kurudi kwake, sikumwona tena nikafikiri labda amesafiri.

“Uliripoti mahali popote?”

“Ndiyo nilimwambia Wadeni!”

Watu walizidi kuchanganyikiwa walishindwa kuelewa ni nini kilikuwa kimetokea katika shule ya Ngaza, watu wawili kupotea kwa wakati mmoja halikuwa jambo la kawaida.

Habari za kupotea kwa mwalimu zilipoanza kuongelewa shuleni zilimtia Anne simanzi kubwa na kukiongeza kilio chake! Uongozi wa shule ulilazimika kutoa taarifa hiyo kwa polisi ambao mpaka wakati huo walikuwa bado wakiendelea na upelelezi wa kupotea kwa Dio.
****
“Itabidi huyu binti tuondoke naye ili atusaidie katika upelelezi wa suala hili tuna wasiwasi atakuwa anafahamu kitu fulani kuhusu kupotea kwa yule kijana!” mmoja wa maaskari alishauri baada ya Anne kuitwa ofisini kwa mahojiano zaidi.

Anne aliyasikia maneno hayo moja kwa moja hakutaka kabisa kupelekwa kituo cha polisi kama ilivyotokea mara ya kwanza mwalimu Lutambi alipokufa!

“Hiyo ni kazi yenu sisi hatuwezi kuwaingilia hata kidogo!’ Mwalimu Mkuu msaidizi alisema.

“Mfunge pingu upesi tuondoke naye sasa hivi, kituoni atasema tu alipo Dio!”

Bila kuchelewa mmoja wa maaskari aliyekuwepo ndani alinyanyuka na kumtia pingu mikononi Anne aliyekuwa akilia muda wote wa mahojiano na alizidi kusisitiza kuwa hakufahamu mahali alikokuwa Dioniz.

‘Utasema tu ukifika kituoni wewe si ndiye uliyekuwa nae mara ya mwisho!”

“Ndiyo lakini........!” Anne alishindwa kumalizia sentensi yake, kwikwi za kulia zilizidi kumkaba shingoni!

Anne alitolewa ofisini na kuanza kusukumwa na polisi akipelekwa kwenye gari la polisi lililokuwa limeegeshwa katikati ya uwanja wa mbele ya shule, wanafunzi waliokuwa mabwenini walimshuhudia Anne akisukumwa, kelele zaidi zilisikika kutoka ndani ya bweni liitwalo Machame! Bweni alilolala Emmaculata.

“Ni huyo huyo ndiye anafahamu alipo Dio! Mchukueni mchawi mkubwa huyo!”Alipiga kelele kwa nguvu Emmaculata.

Sauti ya Emmaculata ilipomfikia Anne pamoja na kwamba kweli alihusika na kupotea kwa Dio na mwalimu alijisikia vibaya sana moyoni mwake na kujikuta akimchukia Emma kwa mara nyingine.

Anne aliumia kujisikia muuaji, vifo cha Dioniz na mwalimu vilimuuma sana moyoni mwake, hakupenda Dioniz afe na zaidi ya yote mahali alipoficha maiti yake ndipo palipomsikitisha zaidi, Dio alikuwa kijana mzuri mno kutumbukizwa katika shimo la maji machafu tena ya chooni!

Ilikuwa si rahisi kwa mtu yeyote kufikiria kuwa miili wa Dio na mwalimu ilikuwa ndani ya shimo palepale shuleni! Anne alijua isingejulikana lakini bado aliamini kwake ilikuwa si rahisi kulisahau tukio hilo, siku zote za maisha yake angekuwa mtumwa wa siri hiyo jambo aliloliona ni mateso makubwa kwake lakini aliahidi kukaa nalo moyoni hadi kaburini!

Dakika tano baadaye gari liliegeshwa kituo cha polisi na Anne aliteremshwa na kupelekwa moja kwa moja hadi chumba cha upelelezi kilichokuwa na giza nene! Waipoingia, taa ziliwasha na Anne alisukumwa kwa nguvu na kuingia ndani ambako alikalishwa chini, hasira zilimkaba lakini alishindwa kumnyoshea askari kidole chake cha sumu akijua kufanya hivyo kungesababisha aaminike kuwa muuaji.

“Binti kama umefika hapa jiandae kueleza ukweli! Hapa si mchezo dada yangu, ukidanganya tu hutoki salama hebu pumzika kwanza ndio tuanze mahojiano yetu!” Alisema mmoja wa maaskari.

Anne alikaa chini kwa kama dakika ishirini hivi akiwa mwenye wasiwasi mkubwa, muda wote huo alishuhudia vifaa mbalimbali vikiingizwa chumbani yakiwemo mawe mawili makubwa! Aligundua yalikuwa maalum kwa ajili ya kumtesa ili aseme ukweli lakini aliuahidi moyo wake kutofanya hivyo!

“Dada wakati umefika sasa hebu nieleze wazi Dioniz yupo wapi?”

“Dioniz?”

“Ndiyo!”

“Tuliachana naye nje ya ukumbi siku ya mahafali!”

“Nje ya ukumbi? Unanitania siyo? Unaviona vifaa vyote hivi?”

“Ndiyo!”

‘Ni vifaa vya mateso kwa ajili yako usiposema ukweli tu nitavitumia!”

“Hata kama mtanitesa na kuniua kabisa sitakuwa na jibu jingine zaidi ya kusema sikumwona Dioniz, baada ya kuachana naye nilikuwa na mvulana mmoja aliyeitwa Benedict!”

“Una hakika?”

“Asilimia mia moja!”

“Unanidanganya mimi subiri sasa!”

Baada ya kusema hayo afande alichukua kinyundo kidogo na kuanza kumgonga nacho Anne kwenye visigino na magotini! Anne alilia kwa maumivu makali aliyoyapata!

“Jamani mtaniua bure mi sijui kitu chochote!”

“Utasema tu!”

Mateso yaliendelea hadi usiku lakini Anne hakuwahi kukubali kufahamu mahali alipokuwa Dio!

Mwili wake wote ulivimba kila sehemu, ndani ya nafsi yake alijua wazi kuwa kweli alihusika na vifo vya watu hao wawili lakini hakuwa tayari kutoboa siri hiyo kwani alijua huo ndio ungekuwa mwisho wa maisha yake kitu ambacho hakupenda kabisa kitokee! Alikuwa tayari kufa lakini si kutamka mahali mwili wa Dioniz ulipokuwa!

Ilipotimu saa nne ya usiku bila kusema kitu maafande walikusanya vifaa vyao vya mateso na kuondoka wakimwacha Anne amelala sakafuni, lawama zote za mateso yale Anne alimtupia mama yake.
****
Asubuhi siku iliyofuata majira ya saa tano idadi kubwa ya wanafunzi kutoka Shule za Ngaza na Nsumba walifurika kituo cha polisi cha kati mjini Mwanza, waliruhusiwa kwenda kituoni kumsalimia Anne, habari za kupotea kwa Dioniz na mlinzi wa shule ya Ngaza zilikuwa zimesambaa sana Mwanza mjini na katika vitongoji vyake kiasi kwamba watu wengi walitamani kumwona kwa macho Anne aliyetuhumiwa kuhusika na kupotea kwa Dioniz na pia kifo cha mwalimu Lutambi.

Kituoni haikuwa rahisi kwa wanafunzi kumwona Anne moja kwa moja mahabusu alikokuwa lakini walimwomba mkuu wa kituo awaruhusu kuongea na wanafunzi mwenzao walikubaliwa na mkuu wa kituo aliwaagiza maaskari wawili wamtoe Anne mahabusu ili asalimiane na wanafunzi wenzake.

Wanafunzi walitulia wakisubiri Anne atolewe mahabusu, dakika tatu baadaye walimwona mtu aliyevimba uso na viungo vya mwili akitoka katika chumba fulani kilichokuwa karibu na kaunta ya polisi, alipojaribu kutembea peke yake alishindwa na kuanguka chini.
Wanafunzi walipoangalia vizuri waligundua kuwa msichana yule alikuwa ni Anne! Wengi hasa ambao hawakuifahamu siri ya mauaji hayo walidondosha machozi.

Maaskari walimbeba hadi nje ambako alikalishwa kwenye msingi wa kituo! Aliponyanyua uso wake kuwaangalia wanafunzi wenzake Anne alilia machozi! Alitia huruma alikuwa amevimba mno usoni kutokana na kipigo wakati wa kuhojiwa.

“Pole Anne! lakini kweli unajua alipo huyo mwanafunzi wa Nsumba?”

“Hapana Angelina!”

“Mwalimu Catherine je?”

“Hata yeye sijamwona kabisa wananionea bure!”

Emmaculata aliyekuwa miongoni mwa wanafunzi waliokuwa kituoni na aliyasikia maneno hayo na kulazimika kusogea mbele ambako alianza kumzodoa!

“Unaonewa nini wakati huo ndio mchezo wako? Unajua kila kitu huna sababu ya kulia!”

Anne aligeuka kwa huruma na kumwangalia Emmaculata msichana waliyesoma naye darasa moja shuleni kwao na waliwahi kuwa marafiki kabla Dioniz hajajitokeza, hasira kali ilimshika Anne akajikuta akisahau kuwa kidole chake cha shahada kilikuwa ni sumu kali kuliko hata Thiodani!

“Wewe Emmaculata weweeeee!” Anne alimsonta Emmaculata kwa kidole chake huku akiwa amevimba kwa hasira.

Katika hali ambayo wanafunzi wengi hawakuitegemea Emmaculata alianguka chini kama mzoga na kuanza kufuka moshi mwili mzima! Wanafunzi wote walishangaa na wengine walianza kukimbia, Anne aligundua alikuwa amefanya kosa ambalo lingepelekea watu kuamini kuwa kweli alikuwa na nguvu za miujiza ya kichawi zenye uwezo wa kuondoa maisha!

“Hee! Kumbe kweli mchawi?” Ilisikia sauti ikitoka katika kundi la wanafunzi.

Anne alijilaumu kwa kitendo hicho na bila kuchelewa aliwaomba wanafunzi wamshikilie mkono na kumsogeza hadi mahali alipolala Emmaculata akitoka moshi na povu mdomoni kama mtu mwenye kifafa akitupa miguu huku na kule kama mtu aliyekuwa akitokwa na roho.

Anne alipomfikia alimsogezea Emmaculata mdomo karibu na sikio na bila mtu yeyote kuona alimpulizia kiasi kidogo cha pumzi sikioni.
****
Dioniz alikuwa ni mtoto wa tano na wa mwisho katika familia yao na ni yeye pekee aliyekuwa mtoto wa kiume na familia yake ilimtegemea yeye zaidi kuwa mrithi wa mali zote alizokuwa nazo baba yake, wazazi wake walimpa kila kitu alichokitaka na walihakikisha anapata elimu bora ili aweze kuziendesha vizuri shughuli za baba yake akiwa mtu mzima.

Taarifa za kupotea kwa Dioniz ziliwachanganya sana akili wazazi wake, presha ya mama yake ilipanda na kumwangusha chini akazirai, kwa siku saba mama huyo alikaa hospitali akisumbuliwa na ugonjwa mbaya wa kiharusi na alipooza upande mmoja wa mwili wake kwa sababu ya ugonjwa huo.

Walitumia kila uwezo waliokuwa nao kumtafuta Dioniz lakini hawakufanikiwa, walipiga simu kwa kila ndugu lakini hakuna aliyejitokeza na kusema Dioniz alikuwa kwake! Wazazi na ndugu wote walichanganyikiwa na waliposikia taarifa za Anne na hisia zilizokuwepo juu yake walitaka sana wamwone ili awaeleze kama kuna kitu chochote Dioniz alimweleza kabla ya kupotea.

Walipokwenda shule walimkuta Anne amekwishaondoka kwenda kwao Sengerema kwa mapumziko baada ya kutoka mahabusu, haikuwa gharama kubwa sana kwao kusafiri kwenda mpaka kisiwani Kome wilayani Sengerema ambako Anne na wazazi wake waliishi!
Majibu ya mama yake na Anne, Isabella yaliwasikitisha sana wazazi wa Dioniz, yeye alijua wazi kilichokuwa kikiendelea na alijua wasingeweza kufanya lolote.

“Mtoto wenu hajapotea isipokuwa kafa na maiti yake hamtaiona milele! Kwa sababu alimlazimisha mwanangu kufanya naye mapenzi na kuna mwalimu mmoja wa shule hiyohiyo aliwahi kumlazimisha nae akafa kifo kibaya! Sisi sio watu wa kuchezea” Alisema Isabella huku akifoka.

“Nini?” Aliuliza kwa ukali Regnald baba mzazi wa Dioniz.

“Umeshasikia! Na ninawaomba muondoke hapa nyumbani!”

“Mama acha kuwafukuza hao watu bado wanauchungu na mtoto wao!”

“Mimi hiyo sijui!”

“Binti ni kweli yanayosemwa na mama yako?”

“Hata mimi mwenyewe sijui kinachoendelea, huwa inanitokea tu ila mama anaelewa zaidi! Nilimpenda mno Dioniz nisingemuua ilikuwa bahati mbaya” Anne alijibu huku machozi yakimtoka.

Wazazi wa Dioniz waliondoka huku wakilia walipofika mjini Mwanza walichofanya ni kuitafuta familia ya marehemu mwalimu Lutambi na familia ya mwalimu Catherine ambao pia walikuwa na uchungu na kifo cha ndugu yao.

Siku hiyo hiyo usiku kilifanyika kikao na wote walikubaliana kutumia kila walichokuwa nacho kuhakikisha wanapambana na familia ya akina Anne!

“Tutatumia kila tulichonacho kuhakikisha kuwa tunalipiza kisasi, mimi nitakwenda Kigoma, wewe utakwenda Bagamoyo na wewe utakwenda Sumbawanga!” Mzee Regnald aligawa majukumu kwa watu wa familia zote.

Je nini kitaendelea?
Je watu hao wataweza kupambana na Anne na mama yake?
Je ni nini hatima ya kila kitu?
 
SEHEMU YA 06


Kidole cha shahada cha Anne kilikuwa tishio na gumzo kubwa midomoni mwa wanafunzi wote shuleni kwao, kitendo cha Emmaculata kuanguka chini baada ya kusontwa kiliwashangaza wengi na kuwafanya waamini kweli Anne alikuwa na nguvu za kichawi!
Wote waliamini isingekuwa Huggins Martin mwanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Nsumba na rafiki mkubwa wa Dioniz kumwombea Emmaculata angekufa!
‘Bila yule mwanafunzi wa Nsumba kuwepo Emmaculata angekuwa marehemu!”
Huggins alikuwa miongoni mwa wanafunzi waliookoka katika shule yake, yeye ndiye alikuwa kiongozi wa umoja wa Kikristo wa wanafunzi Tanzania(UKWATA) katika shule yao. Huggins alimcha Mungu na alimfanya awe kila kitu katika maisha yake!
****
Huggins alikuwepo kituo cha polisi wakati Anne alipomsonta Emmaculata na kidole chake cha shahada na kwa maneno aliyokuwa ameyasikia juu ya Anne, Huggins alikigundua nini lilikuwa tatizo lake aligundua alikuwa na mapepo mabaya.
Huggins alimshuhudia Anne akihangaika kwa dakika kama tatu bila Emmaculata kushtuka, ndipo alipomsogelea karibu zaidi na kumgusa begani!
“Anne yupo Mungu mwenye nguvu zaidi ya hizo ulizonazo!”
Anne aliduwaa bila kujua ni nini cha kufanya na hakuyaelewa vizuri maneno yaliyosema na Huggins, alimfahamu kijana huyo kama rafiki wa Dio lakini hakukielewa alichokisikia kutoka mdomoni kwake
“Unasemaje?”
“Nakuambia yupo mwenye nguvu kuliko hizo unazotumia!”
“Nani huyo?”
“Mungu wa mbinguni, unahitaji msaada wake!”
Anne alitingisha kichwa kuashiria kuwa alikubaliana na kilichosemwa.
Bila kuchelewa Huggins alinyanyua mkono wake wa kuume na kumwekea Emmaculata aliyekuwa amelala chini kwenye paji lake la uso.
“TOKA KATIKA JINA LA YESU! UKASHIDWE NA UKALEGEE PEPO MCHAFU! MWACHIE KATIKA JIIIIIIINA LA YESU!NASEMA MWACHE HURU!” Huggins alikemea.
Askari mmoja alilazimika kumchukua Anne kwa haraka na kumrudisha mahabusu ambako alifungiwa tena rumande, nyuma yake Huggins aliendelea kumwombea Emmaculata, lakini kabla hajamaliza maombi yake gari la polisi lilifika na Emmaculata akapakiwa ndani ya gari harakaharaka tayari kwa kwenda Hospitali ya Seko Toure kwa matibabu.
Huggins alipanda nyuma ya gari hilo pamoja na wanafunzi wengine wa Shule ya Ngaza waliosoma na Anne pamoja na Emmaculata, njiani aliendelea kumwomba Mungu afungue miujiza, mita chache baadaye kabla hawajafika hospitali walishangaa mwili wa Emmaculata ulipoanza kufuka moshi ambao ulijaa nyuma ya gari na kuonekana kama vile gari lilitaka kushika moto! Ilimlazimu dereva asimamishe gari na kurudi hadi nyuma kuangalia ni nini kilikuwa kimetokea.
“Vipi?”
“Anatoa moshi!”
“Moshi!”
“Ndiyo!”
“Unatoka wapi?”
“Mwilini kwake!”
Dakika tatu baadaye Emmaculata alijitingisha na baada ya kunyanyuka alikaa kitako huku akiwashangaa watu walikuwa ndani ya gari!
“Mnanipeleka wapi?”
“Hospitali!”
“Kufanya nini?”
“Kutibiwa si unaumwa!”
“Naumwa nini?”
“Umeanguka ghafla!”
“Wapi?”
“Kituoni!”
“Ilikuwaje nikaanguka?” Alizidi kuuliza Emmaculata na ililazimu Huggins amsimulie kila kitu kilichotokea, wanafunzi wenzake ndani ya gari walikuwa wakilia, Emmaculata alisikitika sana na kujikuta akilia pia.
“Kwa hiyo basi hakuna haja ya kwenda hospitali tena au?” Aliuliza dereva wa gari la polisi!
“Ahsante Huggins kwa msaada wako kwani bila wewe nisingekuwa hai, Anne alishaniua tayari!”
“Hapana siyo mimi niliyefanya kazi hii ila ni yeye aishie ndani yangu!” Alijibu Huggins.
Walipofika kituo cha polisi Huggins alitaka kuonana na Anne pengine kuliko wanafunzi wengine wote, alijua kabisa Anne alihitaji msaada mkubwa sana kutoka kwake na alikuwa na uwezo wa kumsaidia, alijua wazi Anne alikuwa na mapepo yaliyomsumbua na kumpa mateso maishani.
“Jamani naomba mniruhusu nimwone Anne, ananihitaji sana!” Alisema Huggins kwa sauti kubwa mbele ya maaskari na sauti hiyo ilipenya moja kwa moja hadi ndani ya mahabusu na kumfanya Anne anyanyuke kutoka sehemu aliyokuwa amekaa na kutembea hadi mlangoni ambako alichungulia nje na kumwona Huggins akiwabembeleza maaskari wamruhusu aonane naye!
“Mpaka saa tisa kamili jioni wakati wa kuleta chakula sawa?” Afande alimwambia Huggins ikabidi akubali kusubiri.
Huggins hakutaka kuondoka kituoni kurudi shuleni bila kuonana na Anne, alipotoka nje aliagana na wanafunzi wa Ngaza na wakaondoka kurudi shuleni, Huggins aliamua kusubiri mpaka muda wa mahabusu kuletewa chakula ufike ili aonane na Anne, alitaka kumsaidia na kumwondoa katika mateso aliyokuwa nayo.
****
Muda wa mahabusu kuletewa chakula ulipofika Huggins aliisogelea kaunta ya polisi na kuwaeleza nia yake ya kuonana na Anne.
“Wewe bado upo hapa tu?”
“Ni lazima nimwone!”
“Ni lazima?”
“Hapana ni ombi!”
“Kama ni ombi sawa! Hebu njoo huku ndani uongee naye hapahapa kwenye nondo!”
Huggins alizunguka hadi upande wa pili wa kaunta ambako alipelekwa hadi kwenye mlango wa mahabusu ya wanawake.
“Anneee!” Afande mmoja wa kike aliita na Anne akajitokeza na kuja hadi mlangoni!
“Ninaitwa Huggins nafikiri unanikumbuka vizuri, ni rafiki wa Dioniz na nimeshaligundua tatizo lako, kama ukitoka ndani nitakuja shuleni kufanya maombi na wewe! Kwa sasa chukua hiki kitambaa changu cha mkononi nimekifanyia maombi kitakusaidia!”
“Wewe kijana usimpe kitu chochote huyo huruhusiwi kabisa kufanya hivyo, unataka akitumie kujinyonga? Wee msichana hebu mrudishie haraka hicho kitambaa chake, halafu wewe uondoke tayari umekwishaharibu mambo!” Alifoka afande huyo wa kike.
Bila ubishi Huggins aliingiza kitambaa chake mfukoni na kuanza kutembea kurudi nyuma hatimaye kutoka kabisa nje ya kituo ambako alinyoosha moja kwa moja hadi stendi ya mabasi na kupanda basi la kwenda Nyegezi ambako alitembea kwa miguu hadi shuleni kwao!
Wiki moja baadaye Huggins alisikia Anne aliachiwa baada ya Afisa elimu kushinikiza, lakini Huggins alipokwenda shuleni kwao kumtafuta alipewa taarifa kuwa baada tu ya kutoka aliondoka kurudi nyumbani kwao kupumzika baada ya wanafunzi kuonekana kumtenga.
****
Ndugu na wazazi wa Dioniz, mwalimu Catherine na mwalimu Lutambi walisafiri kwenda sehemu mbalimbali kama walizokubaliana, mwingine alikwenda Sumbawanga, mwingine Kigoma na mwingine Bagamoyo!
Nia yao ikiwa ni kutafuta namna ya kulipiza kisasi kwa familia ya Anne kwa kitendo walichofanyiwa, umoja waliokuwa wameuunda ulikuwa na nia mbaya ya kisasi tena kwa gharama yoyote!
Waliporejea baada ya wiki kila mtu alikuwa na burungutu lake la madawa, zilikuwepo dawa za radhi kuvunjwa njia panda! Palikuwa na dawa za kutupa baharini! Kulikuwa na dawa za kuoga kufukiza n.k! Zote zikiwa na lengo la kuiteketeza kabisa familia ya Anne na wazazi wake!
Kazi ilivyokuwa mbele yao ni kuzitumia dawa hizo ili kutimiza azma yao waligawana majukumu zaidi, na kuondoka na dawa zao tayari kwa kuzitumia usiku wakiwa wamekubaliana kukutana siku iliyofuata, hali ya mzee Edward haikuwa nzuri hivyo alishindwa kuzitumia dawa zake usiku huo nakuwapa wanachama wenzake wazitumie.
“Tukutane tena kesho tujue tumefikia wapi na kazi hii kila mtu atimize wajibu wake usiku huuhuu sawa jamani, ninataka kesho nisikie Anne na mama yake wamekufa sawa?”
“Sawa!” aliitikia mchumba wa Catherine, Laurian.
****
Saa moja kamili siku iliyofuata mzee Edward alikuwa nyumbani kwake akiwasubiri wenzake wafike na kumpa ripoti, lakini hakumwona hata mtu mmoja akitokea! Aliingia wasiwasi, usiku wa siku hiyo hakulala kwa mawazo.
Siku iliyofuata wakati akijaribu kwenda majumbani kwao kuulizia nini kilichotokea alishangaa kukutana na mchumba wa mwalimu Catherine akiwa uchi mtaani huku akiongea peke yake, mzee Edward alishtuka sana na kushindwa kuelewa nini kilichokuwa kimempata lakini hakutaka kusimama, alinyoosha moja kwa moja kwenda nyumbani kwa mzee Lutambi.
Kabla hajafika alishangaa kuona makundi makubwa ya watu! Nyumbani kwa Mzee Lutambi kulionyesha kuwa na msiba! Alishindwa kuelewa kulikuwa na nini.
Alifika na kuulizia, jibu alilolipata lilimchanganya sana akili Bi Nyanda shangazi wa marehemu Mwalimu Lutambi aliyekuwa mmoja wa wanachama alikutwa mtaani akiwa uchi wa mnyama damu zikimtoka puani na mdomoni haikufahamika ni nani alimuua.
Hakuna aliyehisi ni majambazi kwa sababu pembeni ya mwili wake kulikutwa dawa nyeusi, hirizi nyeupe na nyekundu na mwili wake ulijaa chale kubwakubwa! Wengi walidai alikufa katika mazingira ya kishirikina!
Mzee Edward alielewa ni nini kiliwapata! Walizidiwa nguvu na dawa za Anne na mama yake.
Miujiza mingi ilijitokeza chumbani kwake usiku, mara kwa mara alisikia sauti ikimwita nje na akiwa hajui hili wala lile ghafla alishtukia mlango na madirisha yote ya nyumba yake yakifunguka na kitu kama kimbunga kikubwa kikaingia ndani! Hali ilitisha mno ikabidi afumbe macho, alipofumbua macho yake alishangaa kukuta mkewe hayupo! Alisikia sauti ya mkewe akilia nje katika shamba lao la migomba.
Mzee Edward alijaribu kutoka nje kujaribu kufuatilia lakini alishindwa kuwafikia, sauti ya mkewe ilizidi kutokomea mbali zaidi migombani!
“Ni heri basi nife na kumfuata mwanangu Dio!”
****
Mzee Edward hakumwona tena mkewe na kwa wiki mbili nzima alimtafuta kila mahali kwa msaada wa majirani na polisi bila mafanikio! Kila mtu alijua mkewe alichukuliwa msukule, waganga kutoka sehemu mbalimbali za Tanzania walijitokeza ili kujaribu kumrudisha Dioniz na mama yake bila mafanikio yoyote, alitumia kiasi kikubwa cha pesa na alikuwa tayari kutumia pesa zaidi katika kuhakikisha mkewe anapatikana.
“Nimegundua Anne na mama yake si watu wa kulipizwa kisasi kwa uchawi ila kuwafuata mchana mchana na bastola na kuwaua kikatili, hawawezi kuniharibia maisha yangu kiasi hiki, hawezi kunitesa kiasi hiki!” Alijisemea mzee Edward na kunyanyuka sebuleni alipokuwa amekaa peke yake na kwenda chumbani ambako alijitupa kitandani.
Alikuwa amepania kuwa siku iliyofuata aondoke kwenda kisiwani Kome na kulipiza kisasi kwa mkono wake mwenyewe, hakutaka tena kutumia madawa ya kienyeji tena! Alikuwa na hasira kali iliyomfanya atetemeke mwili mzima, kila alipowakumbuka mke na mtoto wake roho ilimuuma sana na aliona hapakuwa na uwezo wa kulipiza kisasi zaidi ya kufanya mambo kwa mkono wake mwenyewe.
Siku iliyofuata asubuhi alichukua bastola yake na kuiweka kiunoni akavaa suruali na koti juu, akatoka nje na kuelekea stendi ya mabasi ya kwenda Sengerema, alitamani sana afike Kome dakika hiyohiyo na kuimaliza kazi iliyokuwa mbele yake!
Hakuwa na kazi nyingine zaidi ya kuwaua Anne na mama yake, alikuwa amedhamiria na alikuwa tayari kwenda kufia gerezani! Hakuamini kama maisha yake yangeweza kuharibika kiasi hicho! Bila mwanae Dioniz na mke wake mzee Edward alikosa maana ya yeye kuishi.
“Lazima niue!”
****
Ilikuwa ni katikati ya usiku Anne na mama yake pamoja na watu wengine wengi walikuwa chini ya mti mkubwa wa mbuyu ilikuwa ni kama sherehe watu wakila na kunywa pombe! Watu wote waliokuwa uwanjani pale walikuwa uchi wa mnyama.
Chini ya mbuyu kulikuwa na kiti kilichokaliwa na aliyekuwa malkia wa sherehe hiyo, huyo alikuwa Isabella mama yake Anne, pembeni yake alikaa msichana mdogo mzuri na mrembo huyo alikuwa Anne, mama yake alikuwa akimwomba Anne msamaha kwa mambo aliyoyafanya katika maisha yake na alimtaka arithi mzimu aliokuwa nao yeye.
“Mwanangu huwezi kukwepa jukumu hili hata siku moja! Mimi nilikataa kama wewe lakini nililazimika kukubali hivyo tafadhali sana usikatae utakufa!”
“Kwanini nife?”
“Hautakiwi kukataa wadhifa huu, baada ya mimi kufa ni wewe utakayerithi!”
“Pale ilihitajika damu ya watu wawili ndiyo maana ukajikuta unaua!”
“Mama sitaki kuua tena, niliumia sana alipokufa Dioniz!”
“Dioniz hajafa yupo hapahapa anahifadhiwa ila katika ulimwengu mwingine, watu wengi hawawezi kumwona ila sisi peke yetu! Bado unampenda Dioniz?”
“Sana mama! Yupo hapa kweli?”
“Ndiyo!” Aliitikia mama yake na kumwita bibi kizee mmoja aliyekuwa akipita karibu na eneo hilo!
“Hebu mlete Dioniz hapa!”
Yule bibi kizee aliyekuwa uchi aliondoka akikimbia mbio kwenda nyuma ya mbuyu mkubwa, Anne alisikia mbuyu ukitingishika kama ulitaka kudondoka!
Aliporejea bibi kizee alikuwa na kijana mrefu, akiwa na mavazi aliyovaa siku ya graduation, Anne hakuamini na kunyanyuka mbio akimkimbilia alipomwangalia kweli alikuwa ni yeye!
‘Oh! My God, Dio....is that you!”(Oh! Mungu wangu Dio ni wewe!) Alisema Anne akimkimbilia Dioniz lakini badala ya Dioniz kuchangamka alikuwa ameinamisha kichwa chake chini na hakutaka kuangalia mbele.
“Dio! Dio! Dio!” Anne alizidi kuita!
“Huyu hawezi kuongea tena amekwishakatwa ulimi!” Alisema mama yake Anne.

Je nini kitaendelea?
Je huo ndiyo mwisho wa kila kitu?
 
SEHEMU YA 07

Mzee Edward alinyoosha bastola yake lakini kabla hajafyatua alishtukia macho yake yakiingia giza, hakuwaona tena na aliamini walipotea kimazingara. Yeye mwenyewe alitetemeka hakutaka tena kubaki kisiwani Kome aliamua kurejea Mwanza mara moja!
Lililomtokea lilikuwa jambo la kutisha sana, alikata tamaa ya kuwapata mke wake na mwanae.
******
Ulikuwa ni usiku wa kutisha sana Anne hakuamini alichokuwa akikiona mahali pale, alikuwa bado hajaamini kama mtu aliyemwona alikuwa ni Dioniz! Kabla hajakaa vizuri alimwona mtu kama mwalimu Catherine akiwa na shoka mikononi akipasua kuni! Alipozungusha macho yake upande wa pili alimwona mwanamke mmoja na alipomwangalia vizuri aligundua alikuwa na mama yake na Dioniz.

“Huyu mama naye kaja huku lini?” Alijiuliza Anne lakini hakupata jibu.

Alikimbia kwenda mahali alipokuwa amesimama Dioniz na kumkumbatia wakaanguka nae hadi chini huku akimmwagia mabusu mfululizo.

“Dioniz nakupenda!” Alisema Anne.

“Anne usitumie maneno hayo hapa si mahali pake! Utaiudhi mizimu yetu”

“Sawa mama lakini ninampenda Dioniz na kwanini ulimuua? Je hatuwezi kumrudisha tena duniani?”

“Hiyo haiwezekani tena mwanangu mtu akishafika huku hawezi kurudi duniani tena, sisi pekee yetu ndio tunaweza kufanya hivyo!”

“Lakini kwa ninavyompenda Dioniz mama ni heri na mimi nibaki hukuhuku niishi naye!”

“Haiwezekani mwanangu anakoishi Dioniz wewe huwezi kukaa kabisa kuna mateso makubwa mno!”

“Nitavumilia mama!”

Muda mfupi baadaye Dioniz, mwalimu Lutambi na mwalimu Catherine pamoja na watu wengine ambao hakuwafahamu wakatolewa eneo lile na kuzungushwa nyuma ya mbuyu ambako bibi mmoja alipiga kelele akiomba ardhi ifunguke na wote walidumbukizwa ndani ya shimo lililotokea chini ya mbuyu na kupotelea ardhini Anne alimlilia Dioniz.

Baada ya tukio hilo la kutisha mama yake alimpiga Anne usoni kwa unyoya wa Jogoo, mazingira yakabadilika wakawa wamerejea katika dunia ya kawaida ambayo Anne aliizoea! Anne aliwaona watu wakitembea kuelekea mahali yeye na mama yake walikokuwa wamesimama wakiwa uchi.

“Mama wale watu watatuona!”

“Wao hawaoni ila sisi ndio tunawaona!”

“Kweli?”

“Kama huamini tukikaribia tuwatishie kwa kuwachoma na miti machoni, kama wakishtuka basi wanaona lakini kama hawaoni basi hawatafumba wala kushtuka!”

Ili kuhakikisha maneno ya mama yake, Anne alipowakaribia alinyanyua kipande cha mwiba na kuanza kuwatisha kama anawachoma machoni lakini watu wale hawakufumba macho wala kushtuka! Anne akaamini kuwa kweli walikuwa hawawaoni akacheka.

Njiani waliendelea kupishana na watu lakini wote waliokutana nao hawakuwaona kwa macho, walipofika nyumbani mama yake aligeuka na kuugusa mlango kwa matako, mlango ukafunguka bila hata kuguswa na mtu! Wote wakaingia ndani na kujitupa kitandani.
*****
Asubuhi kulipokucha Anne alikuwa mwenye mawazo mengi sana juu ya tabia ya mama yake, ni usiku wa siku hiyo ndiyo aligundua kumbe mama yake alikuwa mchawi. Kilichomsumbua zaidi akilini Anne ni vipi Dioniz na mwalimu Catherine walitoka katika shimo la maji machafu ya chooni alikowadumbukiza na kwenda hadi kwao.

Anne na mama yake waliendelea kwenda kwenye sherehe za kichawi kila siku usiku, akiwa katika matayarisho ya kurithishwa Kiti cha Umalkia mara bada ya mama yake kufariki. Hatimaye Anne alizoea na kukubali kuwa mchawi! Alifundishwa kitu na mama yake.
****
Pamoja na waganga wote aliokwenda kwao kumweleza kuwa mtoto wake Dioniz alifariki dunia kichawi bado mzee Edward hakuamini na aliendelea kuwasisitiza polisi wamtafute mwanae na pia mke wake, aliamini Anne na mama yake walikuwa wachawi.

Kitendo cha yeye kuona giza alipotaka kuwashambulia kwa risasi kijijini kwao ndicho kilimfanya aamini Anne na mama yake walikuwa wachawi lakini pamoja na hayo bado aliendelea kuwashinikiza polisi wamtafute Dioniz mpaka apatikane.

Kwa shinikizo hilo msako wa polisi ulikuwa bado ukiendelea tena kwa nguvu kuliko mwanzo lakini Dio hakupatikana, mzee Edward na polisi na hata watu wengine walikata tamaa na kuendelea na maisha yao mambo yote wakimwachia Mungu.

“Yaani mke wangu na mwanangu hawapo tena? Mungu anajua na yeye ndiye atanilipia!”
****
Baadaye Anne alirejea shuleni kuendelea na masomo, shule nzima ilimtenga si wanafunzi tu bali hata walimu pia walimwogopa, hakuna mwalimu ayediriki kumchapa Anne hata kama alikosea kitu! Ni msichana mmoja tu katika shule hiyo aliyetokea kumzoea Anne na kuwa rafiki yake.

Msichana huyo aliitwa Grace mwenyeji wa Morogoro, yeye na Anne walikuwa marafiki wakubwa sana, walisoma pamoja, walikula pamoja na pia kucheza pamoja, wanafunzi wengine katika Shule ya Ngaza walimshangaa Grace na kuna wakati walihisi labda yeye pia alikuwa mchawi.

Kila siku iliyopita Grace alimshauri Anne juu ya kujiunga na UKWATA, Anne alitamani sana kuingia katika umoja huo kusali kitu ambacho hakuwa kukifanya katika maisha yake, lakini aliogopa vitisho alivyopewa na mama yake kuwa siku yoyote ambayo angeingia kanisani angekufa sababu mizimu yao ilizuia!

Siku zote aliendelea kumkatalia Grace bila kumwambia sababu, kila siku iliyokwenda kwa Mungu aliendelea kuteseka na siri aliyokuwa nayo moyoni mwake, hakuwa na mtu wa kumwambia jambo lililomsumbua ingawa moyo wake siku zote ulitamani kufanya hivyo.
“Ipo siku nitaenaweza kusema jambo hili kwa mtu yeyote!” aliwaza Anne.
****
Juni 26 Mkutano Mkubwa wa UKWATA ulipangwa kufanyika katika shule ya sekondari ya Ngaza, Grace ndiye alikuwa muandaaji wa mkutano huo kwa sababu yeye ndiye alikuwa mwenyekiti wa UKWATA katika shule yao, shule zote za sekondari mjini Mwanza zilitegemewa kutuma wawakilishi kwenye mkutano huo.

Kijana Huggins alikuwa miongoni mwa watu waliotegemewa kuhudhuria mkutano huo na na kutoa mahubiri kwa wanafunzi wenzake, hilo lilikuwa moja ya malengo ya Huggins lakini lengo la pili la Huggins lilikuwa ni kumtafuta Anne, msichana aliyetamani kumwona siku zote. Alitaka amwone ili amsadie matatizo yake.

“Safari hii ni lazima nimwone tu!” Aliwaza Huggins.

Kila siku Grace aliendelea kumshawishi Anne pia ahudhurie mkutano huo, maneno ya Grace na yalimwigia lakini bado aliogopa kuingia kanisani!

“Tuna kijana mmoja aitwaye Huggins ni mwanafunzi wa shule ya sekondari ya Nsumba, atakuwepo na atakuwa mahubiri maalum tafadhali njoo usikie habari zake!”

“Huggins?”

“Ndiyo kwani unamfahamu?”

Kabla Anne hajajibu swali hilo kumbukumbu zake zilimrudisha moja kwa moja hadi kituo cha polisi, siku aliyomsonta Emmaculata kwa kidole akaanguka chini,ni Huggins aliyemnusuru baada ya kumwombea maombi maalam!

Kwa siku nyingi sana Anne pia alitamani kukutana na kijana huyo aliposikia alikuwa anakuja hisia za kutaka kumwona zilianza kumwingia tena upya.

“Kweli atakuja au unamwongelea Huggins mwingine?”

“Hapana ni Huggins yuleyule mmoja si ni mrefu mwenye sura nzuri hivi?”

“Sawasawa kabisa Grace!”

“Basi atakuwa hapa 26!”

Walipoachana siku hiyo Anne aliendelea kumfikiria Huggins, sura yake ilimchanganya akili, yeye na Dioniz hawakuwa na tofauti sana! Lakini alipofikiria kasoro aliyokuwa nayo mwilini mwake alisita kwani hakutaka kuua tena!

“Akija nitaonana naye lakini siyo kanisani kwao!”
****
Mkutano ulijaa idadi kubwa sana ya wanafunzi kutoka shule mbalimbali zilizopo mjini Mwanza, ilikuwa ni furaha kupita kiasi, wanafunzi waliimba, wanafunzi walifanya maombi na mambo mengine mengi ya kufurahisha, Huggins alimtafuta Anne bila mafanikio yoyote, Anne alikuwa amejificha hakutaka kabisa kuwa karibu na mkutano ule, aliigopa mizimu yao, kila aliposikia nyimbo za mapambio zikiimbwa alijisikia kupandisha mashetani.

Ndani ya roho ya Huggins aliendelea kusikia sauti ikimweleza amtafute Anne kwani alijisikia kumsaidia, ndipo alipofikia uamuzi wa kumtafuta Grace na kumuuliza.

“Tena nilikuwa naongea naye jana tu ni rafiki yangu sana!”

“Sasa nitafanye nini ili nimpate?”

“Subiri baadaye kidogo tukimaliza mahubiri nitakwenda nikamwite sawa?”

Muda wa mahubiri ulipowadia wanafunzi walitulia kumsikiliza Huggins akihubiri, Anne alikuwa umbali wa kama mita mia nne hivi kutoka mkutanoni akiwa ameinama chini ya mti na vitabu vyake, alikuwa akiusikia mwili wake ukiwaka moto!

Anne alishindwa kuelewa kabisa moto ule uliomuunguza ulitoka wapi, aliungua kama alikuwa ndani ya pipa la maji ya moto! Alikimbia bafuni kujimwagia maji lakini maji ya bafuni hayakutosha na kujikuta akichomoka uchi kuelekea ziwani ambako alijitupa majini na kuanza kuogelea lakini bado maji ya ziwani hayakuupoza mwili wake!

Watu walimwona akikimbia kuelekea ziwani akiwa uchi walimtaarifu mwalimu wa nidhamu ambaye alitoka akiongozana na walinzi pamoja na baadhi ya wanafunzi hadi ziwani ambako walimkuta Anne ndani ya maji akilia kwa maumivu.

“Moto! Moto! Moto! Unaniunguza!” Alimwambia mwalimu.

“Moto upo wapi?”

“Mwilini mwangu mwalimu nisaidieeeeeeeeee!” Anne alipiga kelele kwa maumivu.

Walimkamata na kumtoa majini na kuanza kuongozana naye kwenda bwenini mwalimu mmoja wa kike alitoa khanga aliyokuwa amejifunga na kumfunga Anne kiunoni, kabla hawajafika bwenini upepo ulielekea upande wao na sauti ya kipaza sauti ilisikika vizuri masikioni mwao.

“BABA WA MBINGUNI SHUSHA MOTO! MOTO! MOTO! MOTO !MOTO WA MBINGUNI UMETEKETEZE SHETANI!” Ilikuwa ni sauti ya Huggins.

Kadri moto ulivyozidi kutajwa katika kipaza sauti ndivyo Anne alivyozidi kujirusha huku na kule akidai moto ulimuunguza, walipoingia bwenini sauti iliacha kutaja neno moto na palepale Anne alitulia.

Wakati bado wanajadiliana kitu cha kufanya Huggins alianza tena kupaza sauti yake akimwomba Mungu ashushe moto kumteketeza shetani, Anne alianza kupiga kelele tena.

“Mh!”Mwalimu aliguna.

“Mbona kila mhubiri anapotaja moto ndio Anne anadai kuungua?”

“Hata mimi nashangaa!”

Wakiwa bado wanatafakari hilo ghafla macho ya Anne yalianza kutoka nje na mapovu mengi pia yalitoka mdomoni watu wote waliogopa.

“Jamani mimi nafikiri huyu msichana ana mapepo!”

“Hata mimi!”

Mwalimu, walinzi na wanafunzi waliokuwepo walikubaliana kumpeleka Anne moja kwa moja kwenye mkutano huo!

“Hapana msinipeleke!”

“Kwanini?”

“Nitakufa kabisa!”

“Huwezi kufa huko ndiko utapata msaada!”

“Mama! Mama! Msinipeleke huko!” Alilia Anne

Baadaye alichomoka nakuanza kukimbia kuelekea ziwani, walipomfuata hawakumuwahi walimkuta ameshaingia majini na alizidi kuogelea kuelekea kwenye maji yenye kina kirefu zaidi, wanafunzi walizidi kuogelea kumfuata majini, kabla hawajamfikia Anne alizama majini na alipoibuka hakuwa yeye bali nyoka mkubwa aina ya chatu mwenye vichwa viwili! Wanafunzi na waalimu walikimbia na kutoka majini! Taarifa zilipelekwa kwa Huggins naye alishuka hadi ziwani kila mtu aliamini lile lilikuwa ni pepo.

Bila kuchelewa Huggins alishuka jukwaani na kuongozana na wanafunzi wengine hadi ziwani, mkononi alikuwa na Biblia yake, alipofika alishangaa kuona nyoka mkubwa majini!

“Mh! Huyu alikuwa mtu?”

“Ndiyo ni mwanafunzi mmoja anasoma hapahapa!”

“Anaitwa nani?”

“Anaitwa Anne!”

Alilikumbuka jina lakini hakusema kitu na bila kuchelewa alianza kuteremka kuingia majini, watu wote walimshangaa, alizidi kumsogelea yule nyoka huku akiwa amenyanyua mikono yake juu!
Nyoka alizidi kuvimba kama vile alitaka kumrukia Huggins amuume, watu wote waliokuwepo ziwani waliingiwa na hofu kubwa mioyoni mwao, walijua Huggins angeumwa na nyoka na kufa!

“Toka katika jina la …..!” Aliamuru Huggins huku bado hakukutoka kitu. Na watu wote walikuwa kimya kusikiliza.

“Nakuamuru katika jina la Yesu toka, mwachie kiumbe wa Mungu shetani wewe mwachie nenda nyikani na usirudi tena!” Alizidi kukemea Huggins.

Ghafla katika hali ambayo haikutegemewa na wengi nyoka yule alizama majini na alipoibuka hakuwa nyoka tena bali Anne, akilia machozi, watu wote walipigwa na butwaa.

“Ahsante baba kwa sababu umemweka mtumishi wako huru!” Huggins alisema akiwa amenyanyua mikono yake juu.

“Nisaidie Huggins nimeteseka kiasi kikubwa!”

“Siyo mimi ila ni yeye aishie ndani yangu atakusaidia, upo tayari kutubu?”

“Ndiyo!”

Hapohapo majini alimwangoza Anne Sala ya Toba, alipomaliza wote waliondoka kuelekea juu mahali kulipokuwa na mkutano awali ambako Anne alipandishwa jukwaani na kuanza kutoa ushuhuda juu ya mambo aliyowahi kuyafanya.

“Mama yangu alinifanya mimi mchawi bila kutaka, nasikitika nilisababisha kifo cha mwalimu Lutambi, Dioniz na mwalimu Catherine!” Aliposema tu maneno hayo wanafunzi wa Nsumba waliomfahamu Dioniz walianza kulia machozi.

“Haijalishi alifanya nini, Mungu amemweka huru na sasa yeye ni safi! Haleluya!!

“Ameeni!” Watu wote waliitikia kwa sauti kuu!

Kumbe katika watu waliokuwepo katika mkutano huo wapelelezi wawili walijichanganya, aliposhuka tu jukwaani Anne alifikia mikononi mwa polisi na kutiwa pingu mikono yote miwili.

“Tuonyeshe mahali ulipozika miili ya watu uliowaua umetusumbua sana!”Askari mmoja alimshambulia Anne na kumzaba vibao.

Je nini kitaendelea?
Je Anne ataonyesha mahali watu hao walipo?
 
SEHEMU YA 08


Minong’ono ilitawala kila mahali watu wakijadiliana juu ya kitu ambacho Anne alikisema jukwaani kama ushuhuda wa maisha yake yaliyopita! Watu hawakuamini kama kweli Anne na jinsi alivyokuwa mzuri alikuwa mchawi na ndiye aliyemuua Dio na mwalimu wao Catherine.

Mkutano haukuendelea tena palepale ulivunjika na Anne huku akifuatwa na kundi kubwa la watu aliongozwa na maaskari kupelekwa kituo cha polisi ambako ilibidi aandikishe maelezo yake juu ya nguvu aliyokuwa nayo ndani ya mwili wake iliyomwezesha kuwaua Dioniz na watu wengine akiwemo mwalimu Lutambi na Catherine!

Kwa kila mtu aliyesikia tukio hilo na mpaka walimu wa shule ya Ngaza, ilikuwa si rahisi kuamini kuwa msichana mdogo na mwenye sura ya kuvutia kama Anne alikuwa na nguvu ya kichawi na za hatari kiasi kile, hata askari wa kike WP Jacqulline aliyekuwa akichukua maelezo ya Anne alitetemeka.

“Bila msaada wa maombi ya leo mimi ndiye nilikuwa nimetayarishwa kuwa mrithi wa mama yangu katika uchawi!”

‘Mrithi wa nani?”

“Ni habari ndefu sana ila fahamu tu kuwa kuna mzimu uitwao Lutego, upo katika ukoo wetu ni huu ambao hutumika kutulinda sisi watu na ukoo wote wa mzee Kamanzi! Mzimu huu hukaa ndani ya mwanamke mmoja katika ukoo!”

“Kwa hivi sasa anao nani?”

“Anao mama yangu na baada ya kufa yeye mzimu huo ungeniingia mimi na tangu siku hiyo ningekuwa na uwezo mkubwa mno kichawi na ni mimi ndiye ningekuwa malkia wa wachawi kanda ya ziwa!”

Maelezo hayo ya Anne yalizidi kumtisha WP Jacqulline na maaskari wengine na kuwafanya wawe na wasiwasi zaidi, kwa hofu hiyo hakuna hata askari mmoja aliyethubutu kumpiga Anne, askari aliyemzaba kibao baada ya kumtia pingu kwenye mkutano aliingiwa na wasiwasi mkubwa maisha yake, ikabidi amfuate Anne kumwomba msamaha.

“Nisamehe sana dada yangu!” Alisema baada ya kupiga magoti chini.

“Usiwe na wasiwasi Afande hayo ni ya zamani, hivi sasa mimi ni kiumbe kipya kabisa! Sina tena mambo hayo nimeokolewa na kuwa huru!” Alijibu Anne.
****
Baada ya maelezo hayo Anne alichukuliwa na maaskari na kupelekwa kwenye chumba cha mkuu wa kituo ambako pia alitoa maelezo yaliyomtisha sana mkuu huyo, bila kuchelewa alitoa idadi ya maaskari wapatao sita na gari la kunyonya maji machafu kwenda kuona kama kweli miili ile ilikuwa ndani ya shimo alilodai Anne au la!

“Binti kweli una hakika miili hiyo ipo ndani ya shimo manaake usitupotezee muda wetu bure!”

“Afande hauamini basi twende ukaone!”Anne alisema kwa ujasiri ingawa moyoni mwake alishindwa kuwa na uhakika zaidi kama kweli miili wangeikuta ndani ya shimo la maji machafu au la! Kitendo cha kuwaona akina Dioniz na mwalimu Catherine kisiwani Kome katika moja ya sherehe zao za kichawi zilizofanyika usiku kilimfanya akose uhakika!

“Sina uhakika lakini acha twende tukaone, kama haipo sijui nitawaeleza nini!” Aliwaza Anne.
****
Habari juu ya tukio la mwanafunzi na kukiri kuua watu kichawi na kutumbukiza maiti zao katika shimo la maji machafu zilivuma sana katika maeneo yote ya kuzunguka shule ya Ngaza na hatimaye yalifika shule ya sekondari ya Nsumba, wanafunzi walipopata taarifa kuwa gari la polisi lilikuwa likinyonya maji katika shimo hilo ili kuzitoa hizo wengi walimiminika shuleni hapo kushuhudia tukio hilo la ajabu.

Pamoja na kuwepo na watu wengine idadi kubwa ya watu waliokuwepo walikuwa ni wanafunzi wa shule ya sekondari ya Nsumba, waliokuwa wakilia machozi kumlilia Dioniz rafiki yao mpendwa.

Gari la majitaka lililomilikiwa na jeshi la polisi liliendelea kunyonya maji yote yaliyokuwemo ndani ya shimo hilo ili kuona kama kweli miili ya Dioniz na mwalimu Catherine ilikuwemo ndani ya shimo hilo kama alivyodai Anne.

Watu mbalimbali wakiwemo waandishi wa habari wa vyombo mbalimbali ya habari walikuwepo kushuhudia tukio hilo, walimpiga Anne picha nyingi zisizo na idadi na alijua wazi kuwa magazeti ya siku iliyofuata yangejaa picha na habari zake kwa kichwa cha habari ambacho wangetaka wenyewe.

Anne hakuona aibu wala kujuta moyoni mwake kuitwa mchawi! Hiyo ni kwa sababu hakuwa hivyo tena hayo yote kwake yalikuwa mapito, hiyo ilikuwa historia yeye wakati huo alijisikia ni mtu mpya na mwenye mtazamo wa kimungu zaidi kuliko dunia.

Wanafunzi wa Nsumba wenye hasira walimkuta Huggins akiwa pale na aliwasimulia kila kilichotokea na kuwaomba wawe wavumilivu mpaka mwisho wa tukio hilo, alihofia wangeweza kufanya jambo lolote kwa hasira ya kumpoteza Dioniz.

Maneno ya Huggins hayakusaidia lolote kwani badala ya wanafunzi kuwa wavumilivu waliendelea kumshambulia Anne kwa maneno makali huku wengine wakimmwagia mchanga machoni na kumwita mchawi, wanafunzi wa Ngaza pamoja na polisi walijaribu kuzuia lakini haikuwezekana.

“Tuue wote basi, ulimuua Dio unashindwa nini kutumaliza na sisi kabisa?”

Anne alizidi kulia machozi, Huggins alimhurumia na akamsogelea na kuanza kumfuta machozi yake machoni.

“Jamani! Jamani! Jamani!” Huggins alipiga kelele Huggins akiwaomba wanafunzi wenzake wamsikilize na kweli walitulia ili kusikia alichotaka kusema.

Pamoja na Huggins kuwa kiongozi wa UKWATA katika shule ya Nsumba pia alikuwa kiranja mkuu hivyo wanafunzi walimheshimu sana.

“Wanafunzi wenzangu nawaombeni sana tafadhali msimsumbue Anne kwani hana makosa, yaliyotokea yote si kwa mapenzi yake, tafadhali msimwagie mchanga wala kumwita mchawi, kwa taarifa yenu ndugu zangu hivi sasa Anne ni mpendwa mwenzetu amekwishaamua kumpokea kristo na kufanya ngome yake yaliyotokea nyuma katika maisha yake hayajalishi tena, hebu tushangilie!” Alisema Huggins lakini idadi ya watu walishangilia haikuwa kubwa sana wengi walionekana kutaka kuendelea kummwagia mchanga na kumpiga Anne.

Muda wote Anne alikuwa akilia machozi, alizidi kumlaumu mama yake kwa alichomfanyia, alijilaumu kuzaliwa katika ukoo wa wachawi, katika maisha yake hakutaka kuua lakini tayari alishafanya hivyo bila mapenzi yake mwenyewe!

“Kwa kweli simpendi mama ila nimemsamehe kwa sababu hivi sasa nimeokoka!” Aliwaza Anne.

Wakati hayo yote yakiendelea mpira mkubwa wa gari la maji taka ulikuwa ndani ya shimo ukiendelea kunyonya maji machafu, watu wote walikaa kusubiri maji yaishe ili waone kama kweli maiti zilikuwepo chini.

Dakika ishirini na tano baadaye kazi hiyo ilimalizika na wafanyakazi wawili wa gari hilo walichungulia ndani ya shimo kukagua, macho yao yalipambana na tope zito, hawakuona kitu chochote kile!

Baada ya majadiliano na uongozi wa shule uamuzi ulifikiwa kuwa shimo hilo libomolewe ili maaskari waingie ndani kuangalia vizuri ndani ya tope ili kuona kama kweli kulikuwa na kitu chochote kimejificha humo.

Ilikuwa ni lazima waangalie ndani ili kujua kama kweli yaliyosemwa na Anne yalikuwa kweli au la, Anne alikuwa pale na pingu zake mikononi akishuhudia choo kikipigwa nyundo na kubomolewa, ilipomalizika kazi hiyo maaskari wawili waliovaa mavazi maalum waliingia ndani ya shimo na kwa kutumia chepeo walianza kulichambua tope lililokuwepo chini wakiangalia.

Ghafla chepeo la mmoja wao liligonga kwenye kitu kigumu kilichokuwa ndani ya matope, alipokibinua kilikuwa ni kipande kikubwa cha mgomba, kilichofungwa khanga na alipoivuta khanga aligundua ilifungwa kwenye jiwe kubwa lililokuwepo pembeni.

Muda mfupi baadaye askari huyo huyo alipambana na kipande kingine cha mgomba kilichofungwa kwenye jiwe, alizidi kushangaa!
Walipomaliza kazi hiyo hapakuwa na kitu kingine zaidi ya mgomba ndani ya tope hilo, Maaskari wote walishangaa na kuitoa migomba ile nje!

‘Tumekutana na migomba hii tu hakuna kitu kingine chochote ndani ya shimo hili!”

“Kweli?”

“Ndiyo!”

“Binti uliwatupa wapi mbona hatuwaoni?”

“Niliwadumbukiza humo humo ndani ya shimo! Sijui maiti zao zimepotelea wapi ila hiyo nguo ilikuwa ya mwalimu Catherine!”

Waalimu na wanafunzi wote waliokuwepo pale waliitambua nguo ile, ilikuwa ya mwalimu Catherine na alipenda sana kuivaa baada ya saa za kazi.

Maaskari walizidi kuchanganyikiwa lakini watu wa kanda ya ziwa waliokuwepo eneo lile walielewa migomba ile ilimaanisha kitu gani kuwepo ndani ya shimo hilo, miili yote ya watu waliochukuliwa msukule ilibadilika kuwa migomba.
****
Pamoja na kuwa hapakuwa na ushahidi wa kutosha kuwa kweli Anne aliwaua Dioniz, mwalimu Lutambia na mwalimu Catherine, tendo pekee la kukiri mauaji kilitosha kabisa kumfanya awekwe mahabusu! Huggins alijitahidi kuwaomba askari wasifanye hivyo lakini haikuwezekana kuwazuia walidai hata kama alitubu kwenye mkutano wa dini kisheria alikuwa bado ana kesi ya kujibu na kama ingethibitika alifanya mauaji hayo angehukumiwa kifungo cha maisha.

“Jamani si mmwachie tu kwa sababu ametubu!”

“Hapana hiyo haiwezekani hata kidogo ni lazima akae mahabusu mpaka upelelezi ukamilike!”

Huggins badala ya kufurahia alilia machozi, wanafunzi wenzake walishangaa kuona akimtetea Anne mtu aliyemuua Dio rafiki yao kipenzi.

“Ebwanae na wewe usilete ulokole wako hapa hebu twende zetu shule upesi si umwache akafie lupango, wewe inakuuma nini? Mbona Dio alikufa” Alifoka kijana mmoja.

“Hapana jamani, Anne amekwishatubu hayo ina maana amekwishasamehewa mbinguni na duniani!”

“Mbinguni na wapi?”

“Duniani!”

“Mbinguni sawa lakini duniani, anajidanganya ni lazima akanyee ndoo tu!” alijibu mwanafunzi mwingine.
****
Mkutano wa wanachama wa Lutego ulikuwa umekutana kwa dharura kuliongelea suala la Anne kukiri kuua watu kichawi na kuokoka, jambo ambalo hakutakiwa kabisa kulifanya hata kama angekuwa amewekewa kisu shingoni, hilo lilikuwa mwiko kwa wanachama wote wa chama hicho! Kuamua kwake kumpokea Yesu Kristo lilikuwa kero kubwa sana kwa mama yake na wanachama wenzake ambao hatimaye walidhamiria kunywa damu yake kupunguza hasira zao!

Uamuzi huo kwa maana nyingine ulimaanisha kifo cha Anne, ilikuwa ni lazima afe na damu yake inywewe na wanachama.

“Mtoto huyu kanikosea sana na nitaamuru watu wanywe damu yake sasa hivi kwanini kaenda kuniadhirisha kiasi hicho?” Aliwaza mama yake Anne.

Kikao kizima kilikuwa kimya watu wote wakifikiria ni nani angemrithi malkia kama mtu aliyetegemewa kufanya hivyo alikuwa ameamua kukiasi chama chao na kujiunga na Ukristo!

“Ni lazima Anne afe!” Alipiga kelele mama yake na vibibi vizee vyote viligeuka kumwangalia kwa mshtuko mkubwa! Ilikuwa ni mara ya kwanza kumwona mama yake Anne akiwa katika hali hiyo hawakujua nini kingempata Anne huko alikokuwa.

“Nileteeni damu ya mtoto mchanga hapa upesi!” Haikuchukua hata sekunde mbili damu ikaletwa katika kikombe cheupe.

“Haya nileteeni kipande cha kamba aliyojinyongea mwanamke!” haikuchukua muda mrefu kamba hiyo ikaletwa!

“Naomba mniletee kipande cha sanda ya zeruzeru pamoja na mchanga kutoka kwenye kaburi la mwendawazimu!”

Vitu vyote hivyo alikabidhiwa, alichukua sanda, kamba na kuvichoma moto na majivu yake aliyamwaga katika kikombe cha damu ya mtoto na vyote kwa pamoja alivinywa.

Aliposhusha kikombe mwili wake ulikuwa ukifuka moshi jambo kuwa alikuwa na hasira kubwa sana.

“Nisikilizeni kwa makini leo nimekasirika kupita kiasi na nafikiri nimesikia mambo ambayo Anne ameyafanya huko shuleni kwao, ametusaliti vibaya mno hivyo nimeamua afe hukohuko mahabusu aliko na ninakwenda mwenyewe ninafikiri hatanisumbua, hivyo nitarudi sasa hivi nisubirini”

Baada ya kusema hayo kiti alichokalia kilibaki tupu akawa amepotea ghafla katika kimbunga kilichotokea.
****
Mpaka saa tisa hivi usiku Huggins alikuwa hajapata usingizi, mawazo yake yalikuwa kwa Anne aliyekuwa mahabusu akiteseka, alijishangaa ni kwanini alikuwa amevutiwa kiasi hicho na msichana huyo, kwa mara ya kwanza katika kipindi kirefu alihisi kulikuwa na kitu kilichokuwa kikitokea ndani ya moyo wake.

Huggins alihisi kumpenda Anne, alimhurumia kwa mateso aliyokuwa akiyapata ingawa tayari alishaokoka na kubadilishwa! Usiku huo alikuwa katikati ya maombi akimwomba Mungu amlinde Anne huko mahabusu alikokuwa.

Anne naye mpaka muda huohuo alikuwa akifanya maombi ya toba, alikuwa akitubu dhambi za kuua alizofanya na kumwomba Mungu amtie nguvu zaidi ili aweze kupambana na mzimu wa Lutego ambao alijua kwa vyovyote ungetumwa kwake.

Ghafla akiwa katikati ya maombi hayo alishtukia anasikia kishindo kikubwa sana nje ya mahabusu, wafungwa wote walikuwa wamelala usingizi katika sakafu iliyolowa maji na mikojo! Ni yeye tu aliyesikia.

Baada ya hapo aliendelea kusikia vishindo vikiendelea nje ya mahabusu, Anne alijua ni nini kilikuwa kikitokea nje, alijua huyo alikuwa mama yake na yeye alizidisha maombi akimwomba Mungu ampe ulinzi zaidi, alijua wazi bila ulinzi wa Mungu siku hiyo ndiyo ingekuwa mwisho wake.

Ghafla alianza kusikia sauti ya bundi wengi wakilia nje na sauti ya mtu akiita jina lake ilisikika pia, sauti hiyo ilikuwa ya mama yake alijua alikuwa amekuja kumdhuru kwa sababu ya msimamo wake, Anne alizidi kumwomba Mungu amsaidie katika janga lililokuwa mbele yake.

Baadaye sauti za bundi zilitulia lakini vishindo viliendelea kuwepo mpaka mwanga wa jua ulianza kutokea kwenye kidirisha kidogo kilichokuwa juu ya mahabusu, ilionyesha kuwa tayari kulikuwa kumekucha.

Majira aliyoyakadiria kuwa saa kumi na mbili na nusu hivi alisikia sauti za watu wakipiga kelele nje ya mahabusu.

“Jamani mwanga! Mwanga! Mwanga! Huyu hapa mwanga! Amekuja kuloga kituo cha polisi!” Anne aliisikia sauti hiyo na kujua kilichotokea, mama yake alikuwa ameshikwa wanga kituoni.

Kelele ziliendelea na alianza kusikia kilio cha mama yake na watu wakimpiga, muda mfupi baadaye katika hali ambayo hakuitegemea Anne alishtukia mlango wa mahabusu ukifunguliwa na mama yake akitupwa ndani, alikuwa uchi wa mnyama akiwa amevalia mavazi ya kutisha ya kichawi Anne alipiga kelele kuomba msaada!

“Kuniingiza humu wamenirahisishia kazi!” mama yake alitamka huku akicheka.

Je nini kitaendelea?
Je Anne ataweza kuuawa humo?
 
SEHEMU YA 09


Ni hadithi inayohusu maisha ya msichana Anne na nguvu za giza. Mwanamke mrembo, Anne amefikishwa mbele ya mahakama kwa kosa la kumuua mama yake kwa kumchoma kisu. Kesi yake inakuwa nzito, huku hakimu ambaye alisoma naye akitaka kumtetea kwa kumuweka huru, mwenyewe anasema kwamba anastahili kufa.

Baada ya hapo mahakamani, maisha yaliyopita ya mwanamke huyo yanaanza kuonekana katika simulizi hii. Alipokuwa mdogo, mama yake alipanga kumrithisha umalkia wa uchawi hivyo hakutakiwa kufanya mapenzi na mtu yeyote yule vinginevyo mwanaume atakayejaribu kufanya naye mapenzi atakufa.

Mwalimu wake anapombaka ofisini, anakufa hapohapo, anapofanya mapenzi na mpenzi wake, Dioniz, naye anakufa. Mbali na hao, pia kulikuwa na mwalimu wake, Catherine, naye anakufa.

Maisha yamebadilika, anaua bila kupenda, uchawi unamwendesha Anne. Huku akiwa ameua sana, anakutana na nguvu za Mungu hivyo kuamua kuokoka.

Hiyo hamsaidii kumuepusha na kesi ya mauaji, anachukuliwa na kupelekwa sero akisubiri kesi inayomkabili kwa kumuua Dioniz na walimu wake.

Mara baada ya kuokoka, mama yake anakasirika hivyo kuamua kumfuata hukohuko sero kwa lengo kumuua kwa mikono yake, kisa tu aliamua kuokoka.

SONGA NAYO....

“Ndiyo ni mama yangu lakini there is nothing I can do to help”(Hakuna ninachoweza kufanya kusaidia!) Alitamka Anne huku akitupa mikono yake huku na kule kwa hasira, alionyesha ni kiasi gani alimchukia mama yake, shetani alimwingia na kujikuta akilia machozi kwa hasira, madereva walishangaa.

“Kwanini mmemleta hapa lakini?” Anne alimfokea dereva teksi.

“Amesema yeye ni mama yako na kwa sababu ni mgonjwa tukashindwa kumwacha ukizingatia sisi tunakufahamu!”

“Asanteni sana ndugu zangu lakini ninasikitika mimi siwezi kumpokea huyu mama!”

“Lakini ni mama yako kweli?”

“Ndiyo lakini……!”

“Lakini dada hata kama alikukosea huyu ni mama yako tafadhali tunakuomba umpokee!”

“Nasema haiwezekani!” Anne aliongea akiwa ametoa macho kumwangalia dereva.

“Kwanini?”

“Mimi ninajua kwanini sitaki kumpokea nyinyi hamuwezi kuelewa ni bora mniache niendelee na uamuzi wangu!”

Mama yake Anne, Isabella alikuwa ndani ya gari hajiwezi mwili wake ukiwa umevimba kwa sababu ya kupigwa, ingawa hakueleza ni kwa sababu gani sungusungu walimpiga Anne alijua ilikuwa ni sababu ya uchawi wake na ni hilo hilo ndilo lililomfanya asiwasiliane na mama yake kwa miaka karibu kumi.

“Sasa dada tutafanya nini na huyu mama yako?”

“Kwa kweli mimi sijui labda mmrudishe mlipomchukua!” Alisema Anne bila huruma, ni kweli alikuwa mama yake lakini alimuogopa.

“Na pesa yetu atatulipa nani?”

“Kama ni pesa nitawalipa lakini sipo tayari hata kidogo kumpokea!”

“Basi tulipe hizo pesa zetu sisi tuondoke!”

“Nisubirini!” Alisema Anne na kuondoka kuingia ndani na aliporudi alikuwa na noti ya shilingi mia tano mkononi mwake na kumkabidhi dereva.

Cha kushangaza baada ya dereva kuipokea pesa hiyo alifungua mlango na kuanza kumshusha mama yake Anne kutoka ndani ya gari, alipomfikisha chini alimuamuru kijana aliyekuwa naye aingie ndani ya gari na walianza kuondoka kwa kasi.

“Mama yako huyo hapo chini bwana, hatuwezi kuzunguka nae tuache kufanya biashara utajua mwenyewe la kufanya naye ili mradi amekwishafika kwako!” Alisema dereva wakati gari lake likiondoka.

Anne alimwangalia mama yake na roho ikamuuma kupita kiasi kweli Isabella alikuwa mama yake kabisa, lakini mambo ambayo mama yake alimfanyia katika maisha yake hakuyafurahia hata kidogo kwa sababu hiyo hakuwa tayari kumkaribisha ndani.

Alijua kufanya hivyo lingekuwa kosa kubwa kwani ni lazima mama yake angesababisha madhara makubwa sana kwa familia yake hasa kwa watoto wake wakiwemo mapacha Patrick na Nancy waliokuwa na umri wa mwaka mmoja tu wakati huo.

“Nisaidie mwanangu!” Isabella alilia akimwangalia mwanae Anne usoni, alishangaa kuona mtoto wake hakuwa na huruma kiasi kile lakini kwa aliyomtendea hakuhitaji kumlaumu.

“Mama siwezi kukusaidia sababu tabia na mwenendo wako ni mbaya sana! Hebu nieleze kwanini umechapwa kiasi hiki?”

“Wanadai mimi mchawi!”

“Wanadai?”

“Ndiyo!”

“Yaani hata mimi unaniambia hivyo wakati kila kitu nakielewa cha muhimu mama uache tabia hiyo! Si unaona matatizo yake?”

“Nimekwishaacha mwanangu na ninaomba tu unipokee nyumbani kwako unitibu mpaka nipone!”

“Hapana mama siwezi kufanya hivyo mume wangu hatakubali hata kidogo kwani anaifaha....!” Kabla hajamaliza sentensi yake Anne alisikia mlio wa gari ikitokea upande wake wa kulia alipogeuka lilikuwa gari la Huggins! Alishangaa ni kwanini mume wake alirudi nyumbani muda huo kitu ambacho hakikuwa kawaida yake.

“Vipi honey mbona umerudi saa hizi tena?”

“Nimepigiwa simu kuwa hapa nyumbani kuna mgeni tena ni mgonjwa na umekataa kumpokea!” Alijibu Huggins baada ya kuteremka kwenye gari.

“Ndiyo ni huyu mama yangu! Sitaki kabisa aingie ndani kwetu!”
Huggins aliinama na kumwangalia mama mkwe wake aliyekuwa amelala chini huruma ilimshika moyoni mwake, alijua kilichomfanya mke wake asikubali mama yake aingie ndani!
Aliuogopa uchawi wa mama yake lakini yeye Huggins hakuwa na hofu kwani alijua ile ilikuwa ndiyo nafasi nzuri ya kumbadilisha mama yake na Anne na kumfanya aachane na matumizi ya nguzu za giza!

“Anne mruhusu tu mama aingine ndani tafadhali nakuomba!”

“Haiwezekani! Sitaki! Sitaki Huggins, mimi namfahamu mama!”

“Mwache mama Anne! Yasahau ya zamani wewe sasa unaifahamu nuru lazima uwe tayari kutoa msamaha!” Alisema
Huggins lakini badala ya Anne kukubali alianza kulia machozi.

Huggins aliendelea kumbembeleza mke wake mpaka akakubali na wote wawili walisaidiana kumbeba Isabella na kumwingiza ndani ya nyumba yao na dakika chache baadaye Huggins alitoka na kwenda kumtafuta daktari aliyekuja nyumbani na kuanza kumpa Isabella matibabu.

Baada ya huduma hiyo Huggins aliondoka kurejea kazini kwake na kumwacha mke wake akimhudumia mama mkwe wake kwa chakula, Anne aliyafanya yote hayo akiwa na hofu kubwa, watoto wake wakubwa Frank na William walimuuliza maswali mengi wakitaka kujua Isabella alikuwa nani.

“Ni bibi yenu ndiye mama yangu mzazi!”

Watoto wake walifurahi sana kumwona bibi mzaa mama yao.
******
Ilimchukua Isabella miezi miwili mpaka kurejea katika hali yake ya kawaida na katika muda huo wote Huggins na Anne waliendelea kumpasha mama yaojuu ya Mungu ili ageuke na kuyaacha mambo yake mabaya! Kwa juujuu Isabella aliwakubalia lakini ndani ya moyo wake roho ya uchawi iliendelea kumtawala na pamoja na wema wote aliofanyiwa mpango wake wa kumuua mwanae bado uliendelea.
******
Baada ya Huggins na Anne kuwa wamekaa na mama yao kwa miezi sita bila matatizo, akiwa amewahakikishia kuwa tabia ya uchawi aliiacha, wote walimkubali na kuyasahau ya zamani.

Anne alimsamehe kabisa mama yake ikawa ni familia yenye furaha tena,mama aliishi kwa raha na alikuwa kipenzi kikubwa cha wajukuu zake, ilikuwa si rahisi kuamini Isabella aliwahi kuwa mshirikina.

Kasoro pekee aliyokuwa nayo mama yao ni kutokwenda kanisani! Hakuweza kwenda kanisani kwa sababu siku aliyojaribu kufanya hivyo alipoukaribia mlango wa kanisa alianguka chini akageuza macho na kuanza kutoa mapovu mdomoni.

Kwa siku tano mfululizo Isabella alikuwa kama mwendawazimu akiongea peke yake na kuokota makopo, alitulia baada ya kufanyiwa maombi na wachungaji lakini tangu siku hiyo hakuthubutu kuingia tena kanisani, si kanisani tu bali hata nyumbani hakushiriki ibada yoyote kila mahali lilipotajwa jina la Mungu yeye hakuthubutu kusimama, kila mtu aliamini Isabella bado alikuwa na mapepo.

Huggins na Anne pamoja na watoto wao walimwamini Isabella lakini kumbe hakufaa kuaminiwa, kwani roho yake bado ilijaa uchawi na nia ya kuua! Isabella alichukizwa sana na kitendo cha mwanae aliyetegemewa kuwa mrithi wake wa mzimu wa Lutego kujiunga na Ukristo kitu ambacho hakutakiwa kukifanya.

Hapakuwa na mtu mwingine wa kuurithi mzimu wake isipokuwa Anne peke yake na kila siku iliyokwenda kwa Mungu Isabella alitamani sana Anne aanguke na kurejea katika imani yao lakini haikuwa hivyo.

Hatimaye siku moja baada ya Isabella kuwa amevumilia sana alifikia uamuzi wa kumwita mwanae kwa maongezi siku hiyo Huggins hakuwepo nyumbani.

“Anne nimejaribu sana kuvumilia lakini nimeshindwa na ninaomba niseme wazi nia yangu ya kuja hapa ilikuwa kukuua lakini nilipofika hapa kwa msaada ulionipa niliamua kughairi!”

Moyo wa Anne ulilipuka na kujikuta akikubwa na hofu kubwa,
lakini alijikaza hakutaka kuonyesha udhaifu wa wazi.

“Asante mama!”

“Sipendi hata kidogo kukua mwanangu, lakini wanachama wa Lutego wote walichukizwa sana na kitendo chako cha kuingia katika Ukristo na wote wanahitaji kunywa damu yako, siku zote nimejaribu kujitahidi sana kukutetea lakini siku zote imeshindikana, juzi nilipoongea nao walisema ili wakuache hai ni lazima uache dini yako na urejee na kuwa malkia nitakapokufa!”

“Mama kumbe bado unahudhuria sherehe zenu usiku?” Anne aliuliza kwa mshangao hakuamini kabisa kama mama yake katika siku zote alizokaa nao alikuwa akitoka usiku na kwenda kwenye vikao vya wachawi!

“Hilo usijali kitu cha muhimu wewe eleza unakubali kuacha dini yako au hapana!”

“Mama hiyo haiwezekani tena!”

“Kweli? Shauri yako yatakupata makubwa!”

“Mama lolote na liwe!”

Maongezi yao hayakuendelea tena, yaliishia hapo hapo Isabella alionyesha hasira kali.

Jioni ya siku hiyo Huggins aliporejea kutoka kazini kwake hakuwa mtu mwenye furaha kama siku zilizotangulia, alionekana mnyonge na mwenye mawazo mengi, kwa sababu hiyo Anne alishindwa hata kumweleza kilichotokea siku hiyo nyumbani kati yake na mama yake na alipomchunguza mume wake vizuri usoni aligundua Huggins alikuwa akilia! Anne alishtuka na kumsogelea.

“Vipi tena baba?”

“Nina matatizo makubwa sana mke wangu!”

“Matatizo gani tena?”

“Nimepunguzwa kazi ofisini!”

“Umepunguzwa kazini kwa sababu gani?”

“Hata mimi sijui ila wafanyakazi kama kumi hivi tumepewa barua za kupunguzwa kazi na tutalipwa mafao yetu baadaye!”

“Mh! Unasema kweli au unatania baba Patrick!”

“Kweli ndiyo maana unaona nina hali hii nashidwa kuelewa maisha yetu yatakuwaje!” Alisema Huggins na kuendelea kulia huku mkewe akimbembeleza na kumpa moyo!

“Usilie darling hayo ni majaribu tu, si ajabu Mungu amekutayarishia sehemu nyingine nzuri zaidi!”

“Kweli?” Aliuliza kwa mshangao Huggins ilikuwa si rahisi hata kidogo kuyaamini maneno ya mkewe kwani kutokea kwa jambo hilo kulimaanisha mwisho wa kila kitu!Mwisho wa raha zote na mwisho wa furaha iliyokuwa katika maisha yao.
*****
Wakati Huggins anasimamishwa kazi ulikuwa ni mwezi wa kumi na mbili katikati na hayo yaliyotokea yalikuwa ni jaribu makubwa katika maisha yao, yalihitaji mtu imara kusimama.

Huggins akawa haendi tena kazini akawa mtu wa kushinda nyumbani na familia yake na usiku ulipoingia alilala, hiyo ndiyo ikawa ratiba yake ya kila siku kwa mtu aliyezoea kazi yalikuwa ni mateso makubwa! Watoto wake walimsumbua sana wakimuuliza maswali ni kwanini alikuwa haendi kazini tena, hakuwa na jibu la kuwapa ila maswali hayo yaliuumiza moyo wake sana.
******
Shule zilipofunguliwa Huggins hakuwa na pesa ya ada ya watoto wake kwani mafao yao hayakuwa tayari! Watoto walimsumbua kwa maswali wakitaka kujua ni kwanini walikuwa hawaendi shule wakati wenzao walikuwa wakisoma!

Watoto hakuwakujua tatizo lilikuwa ni ada, Huggins hakuwa na akiba yoyote, akaunti yake haikuwa na pesa, pesa yote aliitumia kununulia shamba sehemu za Nyegezi mwezi mmoja kabla ya kupunguzwa kazi! Alishindwa kuelewa angepata wapi pesa za kulipa ada ya watoto wake.

Ni usumbufu wa maswali ya watoto wake yaliyomfanya asiwe anashinda nyumbani na kurudi usiku watoto wakiwa wamelala ni mke wake aliyempa ushauri wa kuuza gari lao ili wapate pesa za kulipa ada ya watoto ! Huggins hakuwa mbishi mbele ya mke wake ilibidi aliuze gari lao na pesa iliyopatikana aliwalipia watoto wake ada katika shule ya kimataifa, waliyokuwa wakisoma na sehemu nyingine alilipa pango la nyumba yao lililokuwa limekwisha.

Watoto walianza kwenda shule lakini bado waliendelea kumsumbua baba yao na maswali zaidi, kila jumapili walimuuliza gari lilikuwa wapi waende kanisani kuna wakati walikataa kwenda kanisani kwa kutumia daladala wakitaka gari la baba roho ya Huggins ilizidi kuuma zaidi, alitamani yaliyokuwa yakitokea yawe ndoto lakini uliendelea kubaki ukweli.

Watu wengi kanisani waliyaelewa matatizo yake na walimpa pole wakifikiri ingesaidia lakini ndiyo alizidi kumfanya achanganyikiwe zaidi mwisho alianza kuona aibu mbele ya waumini wenzake taratibu akaanza kupunguza safari zake za kwenda kanisani mke wake peke yake na watoto wakawa wanahudhuria misa kila Jumapili, Anne alimshauri Huggins arejee kanisani lakini haikuwezekana.

Kitendo hicho cha Huggins kilimfanya mke wake awe analia machozi na alilia zaidi siku Huggins aliporudi nyumbani akiwa amelewa pombe chakari, hakuwahi kumwona Huggins akiwa amelewa katika maisha yao ya ndoa hiyo ndiyo ilikuwa siku ya kwanza na alijua wazi kuwa mumewe alikuwa amevurugikiwa.

“Huggins umeanza kunywa pombe?”

“Ni lazima nipumzishe mawazo mke wangu nitachanganyikiwa!”

“Upumzishe mawazo kwa pombe badala ya kufunga na kuomba?”

Huggins hakunywa pombe tu bali alianza pia tabia ya kuwa anampiga mke wake na kusumbua watoto! Ilibidi Anne apeleke taarifa hizo kwa wazazi wake na Huggins ambao pia walijaribu kumshauri mtoto wao bila mafanikio tabia ya Huggins ilizidi kuwa mbaya.

Huggins alipoteza imani kwa Mungu katika muda mfupi tangu alipopunguzwa kazi, alishindwa kuelewa hayo yalikuwa majaribu ambayo ilikuwa ni lazima ayapitie, akawa mlevi kupindukia na watu wengi walishangazwa na mabadiliko hayo na kuna wakati akawa analala katika baa na kurudi asubuhi.

Hali hiyo ilimvunja moyo sana Anne naye pia akawa haendi kanisani tena, imani katika familia yao ikapotea na uwepo wa Mungu ukaisha! Mama yake Anne aliifurahia hali hiyo kwa sababu jina la Mungu likawa halitajwi tena katika familia yao, shetani akatawala kila kona ya nyumba! Kwake huo ndio ulikuwa wakati mwafaka wa kufanya kazi yake iliyomleta mjini.
******
“Mwanangu Anne hili sasa ni ombi la mwisho, jana tulikuwa kwenye kikao cha Lutego, wazee wametaka damu yako na nilipokataa sana walisema wanataka damu ya watoto wako wawili!”

‘MAMAAAA! UNANITAFUTA NINI? NINAAMINI NI WEWE UMENIHARIBIA NDOA YANGU NA UCHAWI WAKO!”

“Unasemaje?”

“Tena nasema ondoka kwangu leo hii nitakuitia polisi!”

“Unanifukuza Anne?”

“Ndio mama na ninajuta kukukaribisha hapa nyumbani!”

“Naondoka lakini cha moto utakiona!”

Siku hiyo hiyo mama yake alikusanya mizigo yake na kuondoka, ilikuwa yapata saa tisa za jioni na Huggins aliporejea saa sita usiku Anne alimsimulia kila kitu kilichotokea na kumwambia mama yake alikuwa ameondoka kurejea Kisiwani Kome.
“Heri mama yako ameondoka labda ndiye anayenitia mikosi hii?” Alisema Huggins.

Waliongea mengi baadaye walipitiwa na usingizi, masaa matatu baadaye walizinduliwa na kelele ndani ya chumba chao walipofungua macho kulikuwa na mwanga mkali kupita kiasi, wote waliogopa na miili yao ilitetemeka.

“Baba Patrick nini?”

“Hata mimi sijui!”

Hali hiyo ilidumu kwa dakika ishirini ilipotulia walikwenda kwenye chumba cha watoto na kujikuta wakilia walipowakuta watoto wao wawili Frank na William wakiwa wamening’iniza vichwa pembeni mwa vitanda vyao damu zikiwatoka puani na mdomoni! Walikuwa wamekufa.

“MAMAAAAA KWELI UMEUA WANANGUUUU!” Anne alipiga kelele.

“Ni mama aliyewaua?” Huggins aliuliza.

Je nini kitatokea?
 
SEHEMU YA 10


KWA kawaida wazazi wengi huwa na upendeleo fulani kwa baadhi ya watoto wao, mzazi anaweza kuwa na watoto kumi lakini akawa anampenda zaidi mtoto mmoja au wawili kati yao pamoja na kuwa wote ni watoto wake, katika familia nyingine hali hufikia mpaka watoto wengine kuelewa kabisa kuwa mtoto fulani ni kipenzi cha baba au mama na wengine sio!

Hivyo ndivyo pia ilivyokuwa kwa Huggins, alikuwa na watoto wanne lakini kati ya watoto hao aliwapenda sana Frank na William, hawakuwa watoto wake tu bali marafiki zake wakubwa, ingawa umri wao ulikuwa mdogo ni wao waliomwambia aache tabia mbaya ya kunywa pombe kwa wingi na kurudi nyumbani usiku na wakati mwingine kumsumbua mama yao.

Ni watoto hao kipenzi wa Huggins, ndiyo walikuwa wakining’inia darini damu zilichuruzika sakafuni.

“Patrick na Nancy wako wapi?” Huggins alimuuliza mke wake.

“Wako kitandani wamelala!”

“Hawajashtuka?”

Wangeshtuka wangelia!”

Aliendelea kujibu Anne huku akilia.
****
Ghafla bila kutegemea kibunga kikubwa na cha ajabu kiliibuka nje ya nyumba yao.

“Anne ni nini hiki lakini, nini kimetupata jamani? Mbona mimi sielewi”

“Huggins huyu ni mama tu hakuna mwingine na anafanya hivi kwa sababu ninamemwasi na kujiunga na Ukristo!”

“Kweli ni mama yako?” aliuliza tena Huggins kwa mshangao.

“Nakuambia hakuna mwingine huyu ni mama tu na nguvu zake za giza na ndiye kawaua watoto wetu Frank na William!”

“Hivi kweli Frank na William wamekufa ehe?”

“Nina hakika watoto wetu wamekufa Huggins!” Aliitikia Anne huku akilia.

Pamoja na yote aliyoyaona kwa macho yake bado Huggins hakuamini kama kweli watoto wake walikuwa wamekufa, alichofanya ni kutafuta kitu cha kukanyagia ili apande juu na kuhakikisha kama kweli Frank na William walikuwa wamekufa au la!

Alipata kiti kirefu na kukisogeza karibu na mahali mwili wa Frank ulipokuwa ukining’inia lakini kabla hajapanda ili kuangalia alisikia sauti ya kutisha ikitokea dirishani kwao.

“Anne mwanangu ni mpaka ukubali cha dini yako ndipo tutaacha kuiteketeza familia yako na sasa bado wewe, mpaka tutainywa damu yako na usithubutu kuyasema mambo haya kwa watu!”

Walipoisikiliza vizuri sauti hiyo waliigundua ilikuwa ni sauti ya Isabella mama yake Anne, ni sauti hiyo ndiyo iliyomfanya Huggins aamini maneno aliyoyasikia kwa mke wako.

“Uchawi wa mama yako ndiyo umeua watoto wangu Frank na William?” alisema Huggins huku akimsogelea Anne.

Katika hali ya kushangaza ambayo Anne hakuitegemea kabisa alishtukia mumewe akimkaba na kuanza kumpiga vibao, ngumi na mateke bila huruma.

“Huggins kwanini unanipiga?”

“Utanieleza kwanini wewe na mama yako mmewaua watoto wangu!”

Anne alijaribu kadri ya uwezo wake kujitoa mikononi kwa Huggins lakini alishindwa kabisa, aliendelea kulia akiomba msaada wa majirani kwa sababu ya mvua kubwa iliyokuwa ikinyesha hakuna jirani hata mmoja aliyeisikia sauti yake na kumfanya Huggins aendelee kutoa kipigo kwa mkewe bila huruma. Kilio cha Anne kiliwaamsha Nancy na Patrick na kuwafanya nao waanze kulia na kuzidisha kelele.

“Yaani uchawi wenu ndiyo umeua watoto wangu wapendwa? Wewe na mama yako mtawala watoto hawa nyama!” Huggins alisema kwa hasira.

“Siyo hivyo mume wangu ni mama pake yake, mimi nisingeweza kuwaua watoto niliowazaa mwenyewe! Niliwapenda mno Frank na William hata wewe unajua!

“Haiwezekani, umewatoa wanangu sadaka kwani mimi sijui wachawi mnavyofanya!”

Radi ilipiga kila mahali lakini Huggins hakuogopa, alitembea gizani huku mvua ikinyesha na kuyachukua machozi yote yaliyotiririka kutoka machoni pake, moyo wake uliuma mno!
****

Anne alibaki pake yake ndani akiwa amelala sakafuni hajiwezi kwa kipigo alichopewa, damu nyingi ilimtoka puani na kuilowanisha blauzi yake, Huggins alimuumiza sana na hakuamini kama ni yeye aliyemfanyia ukatili huo.

Hali ndani ya chumba chake ilitisha, giza lilitanda kila mahali sababu umeme ulikatika muda mfupi baada ya mvua kuanza kunyesha, kila wakati picha ya watoto wake wakining’inia darini ilipomwijia kichwani alipiga kelele kwa woga.

Baadaye ilimbidi anyanyuke na kupapasa mezani kwake ambako alichukua kiberiti akawasha mshumaa akachukua pamba ambazo alizitumia kuziba pua ili damu isiendelee kutoka zaidi, alipomaliza kazi hiyo aliuzima mshumaa kwa sababu hakutaka kuiona miili ya watoto wake ikining’inia darini.
****
Kama saa mbili hivi asubuhi Anne alisikia mlango wa mbele ya nyumba yake ukigongwa, alifikiri labda ni Huggins alikuwa amerudi kwa sababu tangu alipoondoka usiku wa manane mvua ikinyesha hakurudi tena.

Alinyanyuka na kujikongoja hadi mlangoni ambako alifungua mlango, tofauti na alivyofikiria mtu aliyekuwa mlangoni hakuwa Huggins bali akinamama wawili wa nyumba za jirani.

“Mama Patrick vipi tena mbona damu nyingi kiasi hiki zimechuruzika nje? Kuna nini humu ndani? Mmechinja mbuzi nini?” aliuliza mmoja wa majirani hao kwa utani.

Badala ya Anne kujibu swali hilo aliangua kilio! Kitendo hicho ndicho kilichowashtua majirani hao na kuwafanya waanze kudadisi.

“Mama Patrick nini? Hebu tueleze tafadhali? Una tatizo gani?”

“Ni mambo makubwa mno na sijui nianzie wapi kuyaeleza!”
“Nini?”

“Ingieni wenyewe humo ndani mkaangalie!”

Bila kusita majirani wale walimpita Anne pembeni na kuingia ndani walifuata michirizi ya damu hadi sebuleni hawakuona kitu!

“Mbona hatuoni kitu?” Mama Mariam alisema kwa sauti.

“Angalieni darini!” Anne alipaza sauti iliyochanganyika na kilio.

Kauli hiyo ya Anne iliwafanya majirani wale wanyanyue shingo zao kuangalia juu, alichosikia Anne kutoka ndani ya nyumba kilikuwa ni kilio huku akinamama hao wakikimbia kurudi nje, walimpita Anne na kusimama.

“Anne watoto wako wamepatwa na nini?”

“Nimewaeleza ni stori ndefu sana!”

“Na mumeo yupo wapi!”

“Aliondoka usiku kwenye safari!”

“Ni nini hasa kilichotokea mpaka watoto wakatundikwa darini?”

“Majambazi walituvamia” Anne alidanganya.
****
Hapakuwa na jambo la kufanya zaidi ya majirani kwenda kutoa taarifa polisi, kila mtu aliyeona miili hiyo darini alilazimika kumuuliza Anne juu ya kilichotokea lakini jibu lake lilikuwa majambazi.

Polisi walipokuja wakiambatana na daktari waliishusha miili ya Frank na William darini na kuibeba miili ya marehemu kwenda nayo Hospitali ya Sekotoure ambako ulifanyika upasuaji kuichunguza vizuri miili hiyo.

Baada ya kuchunguza kufanyika miili ilihifadhiwa chumba cha maiti wakati majibu yakisubiriwa, wazazi wa Huggins walishapata taarifa na walikuwa miongoni mwa watu waliofurika hospitali kutaka kujua ukweli.

Siku iliyofuata majibu yalitoka na yalionyesha kulichoua watoto kilikuwa ni kupasukakwa mishipa kichwani lakini kitaalamu haikuweleweka ni kitu gani kilichowapandisha darini ingawa Anne alielewa.

Baada ya majibu hayo majirani wakiongozwa na baba ya Huggins mzee Martin William waliruhusiwa kuchukua miili ya marehemu kwenda kuzika.
****
vifo vya Frank na William viliwachanganya akili sana wazazi wa Huggins, walishindwa kuamini kama ni majambazi kweli walioua watoto ila walilazimika kukubali kilichosemwa na Anne, walichukua Patrick na Nancy na kuwahamishia nyumbani kwao.

“Hivi baba yao yupo wapi?” mzee Martin aliuliza.

“Aliondoka usiku!

“Kwenda wapi?”

“Hakuniaga!”

“Hakukuaga kwanini? Je wakati anaondoka watoto walishafariki au la!”

“Walishafariki!”

“Sasa kwanini aliamua kuondoka?”

Anne alikosa jibu na kubaki kimya na baadaye aliangua kilio.

“Baba acheni kwanza kuniuliza maswali hivi sasa mimi bado nimechanganyikiwa!”

lilikuwa ni ombo la msingi na baba wa Huggins alielewa alikuwa amevuka mpaka kuuliza maswali kwa mtu aliyefiwa.

“Samahani sana mwanangu ni sababu ya uchungu!”

Baadaye Anne alihitajika kituo cha polisi kutoa maelezo juu ya tukio hilo bado msimamo wake uliendelea kuwa huo huo kuwa alivamiwa na majambazi usiku walikuja kulipa kisasi.
****
Mazishi hayakufanyika siku hiyo sababu Huggins hakuwepo na watu wote waliamini Huggins alikuwa safarini, ilibidi mazishi yaahirishwe hadi siku iliyofuata ambayo Anne alidanganya kuwa mume wake angeweza kurudi kutoka safarini.

Kulipokucha asubuhi watu walianza kukusanyika msibani, kijana mmoja aliwashangaza waombolezaji alipoleta taarifa kuwa alimwona Huggins asubuhi hiyo akiwa amefunga taulo kiunoni akipiga mswaki nyumbani kwa mwanamke mmoja aliyejishughulisha na biashara ya kuuza pombe za kienyeji aina ya gongo.

“Hakyanani nimemwona Huggins nyumbani kwa Delila!”
Alisisitiza kijana huyo.
“Nani labda umemfananisha!”

“Nina uhakika nimemwona kama hamuamini nendeni mkahakikishe!”

“Kweli?” baba yake Huggins mzee Martin aliuliza kwa mshangao ilibidi vijana watano wa mtaani waamriwe kwenda kuhakikisha, waliporudi dakika kumi na tano baadaye jibu lao liliwashangaza wazee na kuanza kuhisi vifo vya watoto wao havikuwa vya kawaida.

“Tumemkuta nyumbani akiwa amelewa vibaya mno, tukampa taarifa za vifo vya watoto wake lakini amekataa kuja!”

“Mna hakika mliyemwona kweli ni Huggins?” aliuliza baba yake na Huggins Mzee Martin.

“Ndiyo baba ni yeye!”

“Haya twendeni nikahakikishe mwenyewe sasa hivi!” Alisema mzee Martin na vijana kama ishirini hizi waliongozana nae hadi nyumbani kwa Delila, Huggins alipomwona baba yake alianza kulia.

“Mwanangu vipi?”

“Baba mke wangu na mama yake wamewaua watoto wangu!”

“Akinanan?”

“Mke wangu na mama yake!”

“Wamewauaje?”

“Kichawi na simtaki tena yule mwanamke ni mchawi nimemwambia awale nyama!”

“Mh! Huggins unayosema ni kweli?

“Ni kweli baba!”

“Siamini hata kidogo twende kwenye msiba wa watoto!”

“Baba niache tafadhali niache baba!” Huggins alikataa katakata pamoja na kubembelezwa na baba yake kwa masaa matatu!
****
Taarifa za kugoma kwa Huggins zilisambaa mioyoni mwa majirani ikabidi watu wengi wajae nyumbani kwa Delila wakijaribu kumshawishi Huggins akubali.

Taarifa hizo kuliwaudhi sana wakazi wa mtaa huo ambao mara nyingi walifiwa na watoto wao kimazingara na kujikuta wakimbebesha Anne lawama zote juu ya vifo vilivyotokea mtaani hapo, akimama waliokaa nae ndani walitoka nje na kumwacha chumbani peke yake na maiti mbili za watoto wake.

“Anajifanya mlokole kumbe ni mchawi!” Sauti hiyo ilimuumiza sana moyo Anne.

“Hatuwezi kuzika maiti ya mtu aliyeua watoto wake mwenyewe!” alisema kiongozi wa mtaa.

Maneno hayo yaliwafanya wananchi waanze kusambaa kurudi majumbani kwao baba na mama yake Huggins walishindwa kuondoka na kumwacha Anne peke yake na maiti.

“Mama hebu tueleze ukweli nini kimetokea?”

Anne aliendelea kulia machozi huku akizidi kuzikumbatia maiti za watoto wake zilizokuwa pembeni yake.

“Baba ninawapenda sana watoto wangu nisingewaua!”

“Sasa ni nini kimewaua?”

“Ni mama yangu, alitaka damu za wajukuu zake ili zikanywewe na wachawi wenzake siyo mimi wazazi wangu naonewa bure!”

Ilibidi Anne achukue sana kuwaeleza wazazi wa Huggins juu ya mzimu na jinsi ulivyorithiwa kutoka kwa mwanamke mmoja hadi mwingine na pia alieleza jinsi ambavyo mama yake alimlazimisha yeye kuacha Ukristo ili awe mrithi wake atakapokufa.

“Mwanangu kama ndio hivyo hatuwezi kukusaidia shauri yako, utabaki na miili ya watoto wako utawala nyama!” Alisema baba yake Huggins kwa hasira.

“Baba!” aliita Anne lakini mzee Martin hakujibu kitu alimnyanyua mke wake na wote walianza kutoka nje ya nyumba.

“Mama!” Anne aligeuka na kuanza kumwita mama yake Huggins lakini naye pia hakuitika wote walitoka nje na kuingia ndani ya gari lao na kuondoka, mbele walikatisha nyumbani kwa Delila na kumkuta mtoto wao akiwa amelewa chakali, Huggins alipomwona mama yake alianza kulia tena kwa uchungu akiita majina ya watoto wake.

“Mama, amewaua watoto wangu!”

“Pole sana mwanangu Mungu anayafahamu yote haya na atakupa faraja!”

walimbembeleza kuondoka naye lakini alikataa alichofanya ni kuwaomba wamtunzie watoto wake.
****
Mawingu yalikusanyika angani jioni ya siku ya jumapili baadaye mvua yenye radi kubwa ilianza kunyesha na kusababisha giza kila mahali, umeme ulikatika tena na kufanya kuwa kiza kabisa!

Katika hali kama hiyo Anne alikuwa ndani ya nyumba yake katikati ya maiti mbili za watoto wake katikati ya maiti mbili za watoto wake machozi ya uchungu yaliendelea kumbubujika, watu wote walishamkimbia mpaka wakati huo alikuwa haamini hata kidogo kama dunia ilikuwa imemgeukia kiasi kile, yote hayo kwa sababu ya mama yake, aliwatingisha watoto wake akifikiri yaliyotokea yalikuwa ndoto na labda wangeweza kurejewa na fahamu, ukweli haukubadilika.

Asubuhi siku iliyofuata pia hakuna mtu aliyefika nyumbani kwake, Anne aliendelea kukaa peke yake na maiti za watoto wake akilia, hakuna mtu aliyefika kumpa pole, alitamani Patrick na Nancy wangekuwepo kumfariji lakini bibi na babu yao waliwachukua!

Alikaa hivyo hivyo kwa siku ya nne na maiti zilianza kutoa harufu.

Je nini kitaendelea?
Je Anne ataweza kupigana vipi na hali hii tena akiwa peke yake?
 
SEHEMU YA 11

Saa 12:45 asubuhi ya siku ya Jumatano ikiwa tayari ni siku ya tano tangu Anne asusiwe watoto na majirani zake pamoja na ndugu wote baada ya kuaminika kuwa aliwaua mwenyewe kichawi, alikuwa ndani nyumba yake akilia, mume wake hakuwepo alimkimbia baada tu ya watoto wake kufariki katika mazingira ya kutatanisha.
“Hivi kweli Isabella ni mama yangu mzazi? Hivi ningekuwa mtoto wake kweli angenifanyia ukatili huu? Hapana si mama yangu na mimi nitamuua, ni lazima afe, kama siyo leo kesho na kama si kweli wiki ijayo lakini ni lazima Isabella afe tu!” Alisema Anne huku akilia.
Harufu ilisambaa mtaa mzima na kuwaghasi watu wengine, baadhi ya majirani walitamani kwenda kumsaidia Anne lakini waliogopa kwa kitisho walichokipata kutoka kwa uongozi wa mtaa kuwa yeyote ambaye angejitokeza na kwenda nyumbani kwa Anne kumsaidia pia angetengwa!
Kauli hiyo ilizidi kuwafanya majirani wote wabaki ndani ya nyumba zao kama vile hakukutokea kitu mtaani kwao. Taarifa za mateso hayo ya Anne ziliwafikia waumini wa kanisa la Praise And Worship ambalo Anne na Huggins walisali kabla ya kuasi na kuacha kwenda kanisani, habari hizo za Anne kufiwa ziliwasikitisha sana waumini wenzake.
Kuna hata waliolia kanisani habari hiyo ilipotangazwa, kanisa zima waliazimia kwenda kumsaidia Anne katika mateso yake.
“Pamoja na kwamba ameasi kuja kanisani lakini bado ni ndugu yetu tu katika bwana ni wengi waliasi na baadaye kurudi tena kanisani, ni lazima tumsaidie Anne!” Alisema mchungaji Aaron Mugabiro aliyekuwa kiongozi wa dhehebu hilo na waumini wote waliitikia Ameni!
Hawakutaka kupoteza muda taratibu zote ziliandaliwa, mabasi mawili yalikodishwa pamoja gari dogo aina ya Landcruiser pickup lililokuwa mali ya mmoja wa waumini yalipeleka waumini kwenda nyumbani kwa Anne!
Ukimya uliokuwepo nyumbani hapo wakati wanaingia uliwashangaza waumini wote hapakuwa na dalili yoyote ya kuwepo mtu, milango yote ya nyumba ilifungwa na hapakuwa na kelele yoyote, mchungaji aliteremka katika gari lake aina ya Musso na kwenda mlangoni kuanza kugonga lakini hakuna mtu aliyeitikia.
“Labda walisafirisha?”
“Hapana nilivyosikia mimi Anne alikuwepo hapa na maiti za watoto wake!” Alijibu muumini mwingine.
“Sasa atakuwa wapi?”
“Sifahamu!”
Karibu kila muumini aliyekuwepo mbele ya nyumba ya Anne aliziba pua yake, sababu ya harufu kali iliyokuwepo mahali pale, iliyowafanya waendelee kuamini ni lazima maiti za watoto wa Anne zilikuwemo ndani!
“Huyu huku nyumba!” Ilikuwa ni sauti ya mmoja wa waumii aliyezunguka nyuma ya nyumba waumini wote walitembea harakaharaka hadi nyuma ya nyumba wakiongozwa na mchungaji Aaron!
Anne alikuwepo nyuma akichimba shimo ardhini, shimo lilishafika kiunoni mwake na alikuwa akilia machozi, alitia huruma sana.
Anne alishajua kulikuwa na watu nyumba yake lakini hakuonyesha kujali, aliendelea kuchimba huku akilia machozi, alionekana kama mtu aliyekata tamaa kabisa, mchungaji alimfuata na kumgusa begani lakini hakugeuka, aliweka jembe lake chini na kukaa ndani ya shimo akilia.
“Mwanangu Anne unafanya nini hapa?” Mchungaji aliuliza.
“Ni..na…chi…mba…kaburi….la…watoto..wa..ngu!” Aliongea Anne huku kwikwi ya kulia imemkaba!
Jibu hilo la Anne liliwafanya waumini wote waliokuwepo waanze kulia na hata mchungaji Aaron alishindwa kuvumilia akamwaga machozi.
“Acha mwanangu nyanyuka na utoke shimoni, maombi yako Mungu ameyasikia!”
Anne alijitahidi na kusimama waumini wakamsaidia kutoka shimoni akasimama nje ya kaburi na kusadiwa kuingia ndani ya nyumba yake ambako harufu ilizidi na kuwafanya hata baadhi ya waumini kushindwa kuvumilia kakaa ndani ya kutoka nje!
Miili ya watoto wake ilikuwa imelazwa kitandani chumbani ikiwa imevimba na kuharibika vibaya, hakuna mtu aliyekuwa tayari kuamini kama binadamu wanaweza kufanya binadamu mwenzao kitendo cha kinyama kiasi kile!
“Huu si ubinadamu hata kidogo na kwanini hukuja kwetu kututaarifu?”
“Niliogopa!”
‘Uliogopa nini mwanangu?”
‘Nilijua msingenisaidia kabisa!”
“Kwanini?”
”Sababu niliacha kuja kanisani!”
Baadaye wakati waumini wengine waliondoka kwenda makaburini kuchimba makaburini, mchungaji alipata nafasi ya kumhoji Anne suala lililopelekea mpaka majirani zake wagome kuzika watoto wake! Annne alisimulia kila kitu mpaka kilichopelekea mume wake kukimbia nyumbani kwake na kuhamia nyumbani kwa kahaba, mchungaji alipigwa na butwaa!
“Kwa hiyo kila mtu anaamini kuwa wewe ndio umeshirikiana na mama yako kuwaua watoto wako siyo?”
“Ni kweli mchungaji lakini jambo hilo si kweli hata kidogo, ila mama yangu amefanya hivyo yeye peke yake, kama njia ya kunishinikiza mimi nikubali kurudi tena katika ushirikina kitu ambacho sipo tayari kukifanya ingawa hivi sasa nipo nje ya kanisa!”
“Unajua kwanini lakini mama yako amefanikiwa kuua watoto wako?”
“Hapana mchungaji!”
“Kwa sababu wewe na mumeo mliacha kumtumaini Mungu! Kwanini unafikiri hakulifanya hili siku za nyuma?”Anne alikaa kimya kwa sababu alijua kilichosemwa na mchungaji kilikuwa kweli tupu!
“Unasikia?”
”Nimekuelewa mchungaji!”
Baadaye watu waliokwenda makaburini kuchimba kaburi walirejea na kutoa taarifa kazi hiyo ilikuwa tayari, mchungaji na watu wengine kama watano hivi waliingia ndani wakiwa wamevaa mipira mikononi na kusafisha miili ya Frank na William ilikuwa ni kazi ngumu lakini ulikuwa ni wajibu wao.
Baada ya hapo kazi hiyo ibada fupi ilifanyika na miili ikachukuliwa kwenda makaburini kwa mazishi ambako mchungaji Aaron pia aliongoza ibada! Muda wote huo Anne alikuwa akilia, maisha yake tangu utotoni yalikuwa ni ya mateso mengi na kutengwa na jamii, hali iliyosababishwa na mama yake.
“Sasa tunamwomba mama wa marehemu hawa aje mbele aweke mchanga kama ishara ya kuwaaga wapendwa wake!”
Anne alishikwa mikono na akinamama wawili waliomwongoza hadi kaburini lakini kabla hajaweka mchanga alilegea na kuanguka chini, alikuwa amezimia, ilibidi ndoo ya maji iletwe haraka na kumwagia maji ili azinduke lakini haikuwa hivyo, ikabidi apakiwe katika gari na kurudishwa nyumbani akiacha mazishi yakiendelea, nyumbani pia alimwagiwa maji lakini hakuzinduka ikabidi achukuliwa na kupelekwa hospitali ya TMC iliyokuwa karibu na nyumbani kwao ambako alipewa matibabu ya kuzimia ikiwemo kuongezewa maji na kuzinduka masaa mawili baadaye.
Alipozinduka kwa mara ya kwanza alifikiria yupo makaburini, hakujua mara moja kuwa alikuwepo hospitali.
“Nipeni mchanga! Nipeni mchanga niwaage watoto wangu!” Watu wote waliokuwa karibu yake wakiwemo manesi walisikitishwa sana na kitendo hicho na walimhurumia sana Anne.
“Hapa ni wapi?” Aliuliza fahamu zilipomrudia kichwani.
“Hapa ni Hospitali ya TMC!”
“Nimekukuja hapa saa ngapi?”
“Ulizimia makaburini!”
“Kweli haya nirudisheni makaburini upesi!”
“Makaburini wameshatoka labda tukupeleke nyumbani!”
”Hapana nataka makaburini nataka niyaone makaburi ya watoto wangu!”
Mchungaji Aaron na waumini wengine waliokuwepo hospitali walijaribu kumshauri waende nyumbani kwanza lakini Anne alikataa na kuendelea kusisitiza apelekwe makaburini, hapakuwepo na njia ya kulikataa hilo ikabidi watoke hospitali na kumpakia hadi makaburini.
“Watoto wako tumewalaza kwenye kaburi hili!”
Anne alianguka juu ya kaburi hilo na kuanza kulia akiita majina ya watoto wake.
“Frank na William kweli mmekwenda? Kweli mmeniacha? Kwa sababu yenu mimi nitamuua mama yangu!”
“Acha Anne acha usiseme hivyo tafadhali mwachie Mungu kila kitu!”
“Mchungaji inauma sana!”
Walimnyanyua kutoka kaburini na kumwomba waondoke, Anne hakutaka kuendelea kukataa huku akilia alitembea hadi kwenye gari nakupanda, alikuwa amekonda sana sababu ya kulia na kutokula.
“Mchungaji sijui jinsi ya kukushukuru wema na waumini wa kanisa, Mungu atanilipia ila mmenisaidia katika wakati mgumu sana!”
****
Walipofika nyumbani walikuta waumini wengi wakiendelea na shughuli za msiba, wengine wakipika chakula na wengine wakipasua kuni na wanakwaya wakiimba nyimbo mbalimbali za kumsifu Mungu, ilikuwa ni faraja kubwa sana kwa Anne, majirani walikuwa wamemtenga walishangazwa sana na kitendo kile, wengi walipita na kuchungulia na kutokuamini kama hatimaye watoto wa Anne walikuwa wamezikwa, wao pia walishukuru kwa kitendo hicho kwani walikuwa na mateso makali sana ya harufu nyakazi za usiku.
****
Mchungaji Aaron na waumini wengine walikaa na Anne wiki moja wakimfariji siku ya nane nao walilazimika kumwaga ili warudi nyumbani kwao na kuendelea na shughuli zao, siku zote alizokaa nao zilikuwa za faraja kubwa kwa Anne mpaka wakati huo alishindwa kuelewa bila waumini hao mwisho wa tatizo lake lingekuwa nini? Ndiyo angezika halafu baadaye kingefuata nini, hakuwa na jibu la moja kwa moja.
Shukrani zake kwa mchungaji na waumini wengine wote zilikuwa kubwa mno na hakujua jinsi ya kuzielezea kwa maneno, asingependa sana Frank na William waendelee kuishi naye lakini isingewezekana ilikuwa ni lazima sasa apambane na maisha peke yake!
Katika siku zote waumini waliokaa kwake, hakuwahi kumwona Huggins akija nyumbani pale wale wazazi wake na watoto wake wawili Patrick na Nancy roho ilimuuma sana kujikuta katika hali hiyo, angependa kumbadilisha na kuirejesha tena katika wakati wa zamani alipokuwa na maisha bora lakini aliona kama ilikuwa si rahisi kabisa jambo hilo kutokea.
Hapakuwa na njia ya kuwazuia waumini wasiondoke, ilibidi waondoke na kumwacha Anne peke yake, nyumba kubwa aliyoishi ilimtisha sana na ilimfanya asikie ukiwa zaidi.
Siku hiyo alilala peke yake ndani na siku hiyo hiyo majira kama ya saa tisa hivi usiku alisikia dirisha la chumba alikokuwa amelala likigongwa alishtuka sana ana hakufahamu ni nani aliyekuwa akigonga usiku huo, baadaye alisikia sauti ya kiume ikiita dirishani, alipoisikiza vizuri sauti ile ilikuwa ni sauti ya Huggins, furaha kubwa ilimrejea moyoni na kujua kipenzi chake alikuwa amerejea kwake, hakutaka kuchelewa alisimama na kutembea hadi dirishani na kufungua.
Alipofungua alishangaa kukutana na sura ya mama yake! Mwili wake ulitetemeka alikataa kufungua dirisha lakini alishindwa
“Karibu mama!”
“Unamkaribisha nani? Na bado nimekwishachukua watoto wawili sasa nimebakiza kuwajia hao wawili ulionao ndio utaelewa kuwa mimi nimekasirika mpaka utakapokubali kuwa upande wangu ndipo nitakapokuacha, umeuniudhi sana!” Mama yake alisema maneno hayo kabla Anne hajajibu kitu alishtukia kitu kama maji yenye harufu kali yakimwangika kuingia ndani na kumlowanisha mwili mzima!
“Huo tayari ni mkosi watu watakuona kama mavi kuanzia leo!” Mama yake alisema na kupotelea katikati ya migomba.
Anne alirudi na kuanguka kitandani kwao na kuanza kulia alishindwa kuelewa ni kwanini mama yake alikuwa akimfanyia unyama ule!
“Watoto wangu hawaui nitawapeleka kwa mchungaji Aaron na halafu mimi nianze kazi ya kumtafuta mama hadi nimuue tu!”Asubuhi kulipokucha Anne alitoka ndani baada tu ya kunywa chai na kuanza kutembea kwenda nyumbani kwa wazazi wake na Huggins kabla hajafika alipita kwanza nyumbani kwa Delila kumwona Huggins!
Aligonga mlango na mlango ulifunguliwa na Huggins mwenyewe.
“Wewe mchawi umefuata nini hapa? Tokaa vinginevyo nitakua!” Alisema Huggins.
“Huggins wewe ni baba wa watoto wangu acha kusema maneno hayo!”
“Toka hapa kwanini umeua watoto wangu?”
“Sio mimi Huggins nimekwisha kueleza juu ya jambo hilo!”
Huggins alimwacha Anne mlangoni na kuingia ndani alipotoka alikuwa na panga mkononi na kuanza kumkimbiza Anne, watu waliokuwa wakiangalia walishangilia na kumzomea Anne! Kweli Anne aliamini mama yake alikuwa amempaka mkosi, kila alipopita watu walipishana nae hawakutaka akae karibu yao, harufu ya mwili wake haikuwa nzuri.
“NITAMUUA MAMA!” Alisema kwa sauti alipofika nyumbani kwa wakwe zake walishangaa kwa harufu aliyokuwa nayo. Siku iliypfuatia, akaamua kuwapeleka watoto wake kwa mchungaji Aaron.
Kwa mwaka mzima aliishi mbali na watoto wake na hakuona jambo lolote lililowapata Patrick na Nancy alimshukuru Mungu mama yake hakuja tena usiku.
****
Januari 23 saa tisa ya usiku ikiwa ni miezi miwili tangu watoto wake wafariki alizinduliwa usingizini na sauti ya mtu akiongea dirishani ilikuwa ni sauti ya mama yake.
“Kwa sababu umewaweka watoto wako kwa mchungaji sasa nitakupa adhabu nyingine, itabidi kila siku maisha yako yote!”
Dakika mbili tu tangu asikie sauti hiyo alishangaa kusikia nguo zake za ndani zikilowa damu ilikuwa ikitoka kama maji!
“Mungu wangu!” Alisema Anne kwa mshangao, hakuamini kama hali hiyo ingeendelea siku zote lakini alishangaa alipomaliza miezi sita ikivuja damu usiku na mchana wakati mwingine alilazimika hata kwenda kuongezewa damu na kupewa vidonge vya kuongezwa damu, nyumba yake ilijaa makopo ya vidonge vya Fero B’ alivyopewa hospitali kuongeza damu! Aliishi kwa mateso, inzi walimfuata kila alikokwenda, watu hawakumkaribia, kila mara alishindwa kukaa kitini sababu kila alipokaa alilowanisha kiti alichopewa katika daladala alisimama hata kama kulikuwa na viti.
Hakuweza kumudu kununua ‘Always’ badala yake akawa anatumia taulo lakini nazo zilioza pia, yalikuwa mateso makubwa sana kwa Anne alilia na kumwomba Mungu amsaidie, hasira ya kumuua mama yake ilipanda kila siku.

Je nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 12


Anne alizidi kukimbia huku akilia machozi, Huggins alizidi kumfuata nyuma yake, akimpiga na ubapa wa panga! Watu wote walioshuhudia walizidi kupiga kelele wakishangilia kitendo kile na wengine walizomea!
Taarifa za Huggins kuhama nyumbani kwake na kutoshiriki katika mazishi ya watoto wake kwa kile kilichoaminika kuwa ni mkewe kuwatoa sadaka watoto wake mwenyewe wafe kichawi!
Wengi walimchukia Anne, hakuna mtu hata mmoja aliyekuwa tayari kumsaidia Anne akipigwa na Huggins, hata alipoangushwa chini na kuanza kuchaniwa nguo watu wote walishangilia na kupiga mayowe.
“Ua mchawi huyo! Ua mchawi huyo!” Wananchi walipiga kelele.
Huggins alizidi kushusha kipigo kwa Anne huku watu wakizidi kushangilia, mwisho kabisa Huggins alilinyanyua panga lake na kumkata nalo Anne begani, damu nyingi sana ilimtoka, watu walipoona kitendo kile waliogopa na kuanza kukimbia kuondoka eneo lile, baadaye Huggins naye aliondoka.
Anne alijitahidi akanyanyuka lakini alishindwa kwa sababu alikuwa nusu uchi, watu waliendelea kukusanyika wakimshangaa, baadhi ya akinamama walimhurumia lakini wengine walimlaani kwa kitendo chake cha kuwaua watoto.
Baaaye alishtukia akifunikwa na khanga mwili mzima! Alishangaa ni mtu gani mwenye huruma, alinyanyua uso kuangalia juu, aliitambua sura yake!
“Anne vipi?”Aliuliza
“Mume wangu kanipiga dada!”
“Kwanini?”
“Wewe ni nani na unaishi wapi hujayasikia yaliyonipata?”
“Mimi naitwa Victoria kama utakumbua tulisoma wote Ngaza!”
Aliposema hivyo kweli Anne alikumbuka msichana huyo alikuwa miongoni mwa wasichana waliosoma katika shule ya wasichana ya Ngaza, ila Anne alikuwa mbele yake, msichana yule alimsaidia Anne kusimama wima.
“Twende nikusindikize hospitali!”
“Lakini nilikuwa nakwenda ukweni kwangu kuwafuata watoto wangu, baba mkwe aliwachukua!”
“Hapana huwezi kwenda katika hali hii ya kuvuja damu twende kwanza polisi ukatoe taarifa kisha twende hospitali ukatibiwe, baada ya hapo ndipo utaweza kwenda ukweni kwako!”
“Twende tukatoe taarifa wapi?”
“Polisi!”
“Hapana Vicky siwezi kwenda polisi!”
“Kwanini?”
“Sitaki kumshitaki mume wangu, Huggins ni baba wa watoto wangu, akifungwa watoto wangu watakuja kuniuliza!”
“Mh!” Vicky aliguna.
“Kama ni hospitali twende lakini polisi sitakwenda, nisaidie kunifikisha basi!”
“Hospitali hawawezi kukutibu bila PF3!”
“Hilo nalifahamu lakini wee twende tu!”
Walianza kutembea taratibu kuelekea hospitali ambako pia hapakuwa mbali sana na mahali tukio hilo lilipotokea, watoto wengi waliwafuta nyuma wakati wakitembea na watu wengine wakubwa walizidi kuwashangaa.
****
“Binti kimetokea nini?”Daktari aliuliza.
“Nimeangukia kisu jikoni!”
“Pole sana na hayo majeraha usoni je?”
“Ni jengo la jiko limebomoka ndiyo likasababisha niangukie kisu!’
“Aisee pole tena!” Daktari alimpa pole Anne.
“Itabidi tukushone kiasi cha nyuzi zisizopungua kumi na tano, sababu umeumia sana, itakugharimu shilingi elfu kumi na tano na baada ya hapo tutakuandikia sindano za PPF tano na chanjo ya pepopunda sawa, kwa hiyo gharama na matibabu yote itakuwa shilingi eflu ishirini na moja na mia tano!”
“Daktari mie sina pesa kabisa!” Alisema Anne huku akilia.
“Mimi nitalipa!” Vicky alisema na palepale alianza kufungua mkoba wake kutoa pesa!
“Subiri kwanza basi utalipia pale dirishani kwa keshia!”
Baada ya kulipia Vicky alirudi kwenye benchi na kukaa akimsubiri Anne amalize kuhudumiwa muda wa dakika thelathini baadaye, Anne alitoka chumba cha upasuaji akiwa amefungwa bandeji kubwa begani! Alishachomwa tayari sindano za PPF na Pepopunda.
****
Walipotoka hospitali, Anne alimuomba Vicky waongozane kwenda ukweni kwake kuwachukua watoto, Vicky alikubali na walikwenda hadi nyumbani kwa mzee Martin.
Walipowasili nyumba ilikuwa kimya kama vile hapakuwa na watu, Anne aligonga na mlango ukafunguliwa na mama yake Huggins!
“Karibuni sana!”
“Ahsante shikamoo mama” wote wawili waliitikia na baada ya salamu wote waliingia ndani ambako walikaa vitini na muda mfupi mzee Martin aliungana nao na wote wakamwamkia!
“Vipi binti zangu?”
“Baba nimekuja kuwafuata watoto, hawatakiwi kabisa leo kulala hapa, najua kitakachowapata!” Alisema Anne akikumbuka kitisho kilichotolewa na mama yake.
“Nini kitawapata?”
“Watakufa?”
“Watakufa vipi?”
“Mama amesema anawafuata!”
“Sasa unataka kuwapeleka wapi kwenye usalama kuliko hapa nyumbani?”
“Nataka niwapeleke kwa mchungaji Aron akakae nao, leo mama anakuja kuwadhuru watoto wangu!”
“Hilo mwanangu haliwezekani, watoto hawaondoki hapa, baba yao amekataa kabisa!” mama yake Huggins aliweka mgomo.
“Hapana mama nipeni watoto wangu, niondoke nao!”
“Haiwezekani labda tumwite baba yao aje hapa umuombe!”
“Sitaki kuonana na Huggins kabisa, kwani ni yeye aliyenifanyia hivi!”
“Sawa na pole sana lakini sisi hatuwezi kuacha uondoke na watoto bila yeye kukubali!”
Wakati maongezi yakiendelea, Patrick na Nancy waliokuwa wakicheza chini walimfuata Anne na kusimama mbele yake! Ikabidi Anne awapakate miguuni pake, alijisikia vizuri kuwa na watoto wake tena! Hakutaka kabisa kutenganishwa nao! Aliwapenda na hakutaka wapatwe na matatizo yaliyosemwa na mama yake!
“Baba siwezi kuwaacha watoto wangu!” Alisema Anne huku akiwawekea watoto wake matiti mdomoni ili wanyonye! Watoto walionyesha furaha.
“Mimi naondoka!”
“Tafadhali waache watoto!” Baba yake Huggins alisema kwa sauti.
“Hapana baba ni lazima niondoke nao
Ulitokea mzozo mkubwa sana wa kunyang’anyana watoto hatimaye Anne alinyang’anywa Patrick na Nancy walilia kupita kiasi wakimlilia mama yao.
“Ondoka hapa vinginevyo nitakuitia polisi”
“Siondoki nipeni watoto wangu upesi!” alisema Anne huku akilia machozi.
“We binti!” Mzee Martin alimwita Vicky!”
“Naam mzee!”
“Hebu mwondoe huyu mchawi hapa sisi hatuwezi kumpa watoto akawaue, ondokeni kabla sijawaita wezi!”
Vicky aliogopa na kujikuta akimwomba Anne waondoke, Anne alikataa lakini Vicky alimbembeleza hatimaye alikubali na wote walianza kuondoka, watoto wakimlilia mama yao lakini mzee Martin na mkewe hawakujali walizidi kumfokea Anne kwa maneno machungu yaliyomuumiza moyo.
****
Kwa msaada wa Vicky huku akilia machozi Anne alikwenda hadi nyumbani kwake , baada ya kufika Vicky aliaga na kuondoka kwenda nyumbani kwake, aliishi kwenye majengo ya shule ya Isamilo ambako alifanya kazi kama mwalimu!
“Ahsante kwa msaada wako Vicky!” alisema Anne akitoa shukrani.
****
Saa tatu usiku Anne akiwa amelala kitandani kwake alisikia sauti ya watoto wakilia nje ya nyumba yake, alishituka zaidi kusikia mlango ukigongwa! Aliogopa kwenda kuufungua lakini baadaye aliposikia sauti ya watu wakiongea na kuitambua sauti ya mama mkwe wake alinyanyuka harakaharaka kwenda mlangoni.
Alisikiliza kwa muda na kugundua kweli waliokuwa nje walikuwa wakwe zake pamoja na watoto wake, ingawa aliogopa na hakujua kilichowaleta alifungua mlango, alishangaa kukuta Huggins na Delila pia wapo.
“Karibuni ndani!”
“Unamkaribisha nani ndani? Nani aingie nyumbani kwa mchawi” Delila alisema kwa nyodo.
“Jamani ingieni ndani!”
“Sisi ndani hatuingii, tangu umeondoka watoto wanalia tu na hawataki kula sijui umewaroga, sasa dawa ya mchawi ni kumpa mtoto alee! Tumekuletea watoto wako ili uwaue vizuri!”
Baada ya kusema hayo tu waliwabwaga watoto chini na kuondoka, Anne alimshukuru Mungu na alichofanya pale kikawa ni kuwachukua watoto wake na kuanza safari ya kwenda nyumbani kwa mchungaji.
Hapakuwa mbali sana ulikuwa kama umbali wa robo kilometa hivi, alipofika aligonga na kufunguliwa.
“Nimewaleta watoto wangu mkae nao hapa nyumbani!”
“Mchungaji na mke wake hawakutaka kuuliza kwanini bali waliwapokea watoto wale na kuagana na Anne, watoto walilia lakini hapakuwa na njia ilibidi wabaki kwa usalama wa maisha yao, Anne alikuwa na uhakika pale walikuwa salama kuliko nyumbani kwake.
Aliporudi nyumbani aliendelea kulia akimfikiria mama yake na jinsi alivyomtesa tangu utotoni! Alikosa raha ya maisha na thamani ya kuwa na mama mzazi.
Mpaka saa tisa ya usiku Anne alikuwa bado yupo macho, bila kupata hata lepe la usingizi, ghafla alishitukia kimbunga kikubwa nje na mwanga mkali ukafuata, alilifananisha tukio hilo na tukio la siku Frank au Henry, jina alilopewa na babu yake baada ya kuzaliwa na William walipokufa!
“Ahaa! Umejifanya mjanja siyo, umewahamisha watoto eh! Sasa ni kazi kwako! Nakuambia tangu sasa utalowanisha hizo nguo zako hadi mwisho wa uhai wako!”
Baada ya sauti hiyo tu, Anne alishitukia kitu kama maji mengi yakitoka sehemu zake za siri na nguo zake za ndani zililowa, alifikiri ni mkojo lakini hali ilipotulia na kuangalia vizuri aligundua haukuwa mkojo bali damu nzito iliyotiririka kushuka chini miguuni kwake!
“Hili ni pigo jingine lakini ni heri hali hii kuliko watoto wangu kufa na ugomvi wangu na mama hautakwisha mpaka nimwondoe duniani!” aliwaza Anne.
****
Asubuhi kulipokucha nguo zote alizovaa zililowa damu, damu iliyokuwa ikimtoka ilikuwa nyingi mno kiasi cha kushindwa kuvaa ‘pedi’ ili kuzuia isilowanishe nguo zake alilazimika kuchukua taulo ya kuogea na kulikunja akaivaa katika ya miguu yake lakini nalo muda mfupi tu lililowa!
Pamoja na shida hiyo Anne alijitahidi kutembea hadi nyumbani kwa Mchungaji kuwaangalia watoto wake, aliwakuta wakinyweshwa uji aliwabeba na kuanza kuwanyonyesha.
Walimweleza kila kitu kilichotokea usiku, kimbunga na mwanga mkali huku sauti za watu wakiwataka Nancy na Patrick, Anne alielewa kilichoendelea.
“Ilibidi mimi na mchungaji tuanze maombi ndipo hali ikatulia!” Mke wa mchungaji alisema.
*****
Hayo ndiyo yakawa maisha ya Anne kila siku ilikuwa ni lazima aende kwa mchungaji kuwanyonyesha watoto wake, damu iliendelea kumtoka kila siku, kila alikokwenda kwa sababu ya harufu alifuatwa na inzi wengi, harufu hiyo ilimfanya atengwe na watu, kila alipokaa watu walimkimbia!
“Aliishiwa damu mara tano katika kipindi cha miezi sita, safari zote alilazwa hospitali na kuongezwa damu chupa kadhaa! Madaktari walijaribu kumpa tiba lakini haikusaidia, ikabidi ajaribu tiba za jadi lakini nazo hazikusaidia, maisha yalimtesa na hakuona haja ya kuendelea kuishi alitamani kufa lakini aliwahurumia watoto wake Patrick na Nancy alijua bila yeye wangepata taabu kubwa maishani.
“NITAMUUA MAMA HAWEZI KUNITESA HIVI” Anne aliwaza na siku hiyohiyo alichukua kalamu na karatasi kumwandikia mama yake barua akimweleza kuwa aliamua kuuacha Ukristo na kurudi tena katika uchawi ili awe mrithi wa mzimu wa Lutego.
Mama yake alipoipokea barua hiyo alifurahi mno na kuisoma usiku mbele ya wanachama wenzake, walipiga makofi na kushangilia wakajua Anne alikuwa amenyooka.
“Hivyo nitakwenda mimi na wengine wawili na tutakwenda kama binadamu wa kawaida!”
“Lini?” wanachama wengine waliuliza!
“Kesho asubuhi!”
****
Ulikuwa mchana wa joto kali, Anne alikuwa amechoka sasa alidhamiria kumwondoa mama yake duniani! Hakuwa na kitu kingine cha kufanya, mateso aliyopata yalitosha kabisa hakutaka mengine zaidi, akiwa katika mawazo hayo ghafla alishitukia mlango wa nyumba yake ukigongwa, alikwenda moja kwa moja kufungua mlango, alikutana na sura ya mama yake na bibi vizee wengine wawili, alipowaangalia aliwafahamu walikuwa bibi vizee wa kijijini kwao.
Hasira ilimkaba Anne kooni lakini hakutaka kuionyesha, aliazimia kuwaua wote watatu
****
Anne alikuwa akitetemeka kwa hasira, tayari alishamchoma mama yake kwa kisu kifuani tena kwenye titi la mkono wa kushoto na alipohakikisha kuwa amekufa alikichomoa na kutembea hadi chumba cha pili ambako bibi kizee mwingine muumini wa Ushirikina aliyeongozana na mama yake alilala, huko nako aliikamilisha kazi yake kwa kukizamisha kisu kilekile kifuani kwa bibi yule naye akaaga dunia.
Alikuwa amebakiza mtu mmoja tu ili alikamilishe zoezi zima, bibi kizee wa tatu aliyelala katika chumba kilichokuwa mkono wa kulia pembeni mwa chumba chake cha kulala, ni huyo ndiye aliyekuwa amesimama mbele yake!
Tofauti na mama yake pamoja na bibi kizee mwingine aliyekwishawaua, bibi kizee huyo alikuwa macho amesimama katikati ya chumba huku tunguli mbili kubwa zikiwa mikononi mwake! Anne alitetemeka hali iliyokuwepo ilikuwa ni tofauti kabisa na picha aliyoitegemea, kwa hasira aliyokuwa nayo moyoni hakusita wala kuiruhusu hofu imtawale.
“Nakuua! Amini usiamini wewe bibi kizee pamoja na uchawi wako mimi nakuua uwafuate wenzako kwanini mmenitesa kiasi hiki?”
“Mimi huwezi kuniua, utajiua mwenyewe tu!”
“Nakuambia wazi utakufa!”
“Huwezi na jaribu uone!”
Akiwa na hasira kali na uchungu pamoja na nia ya kuua ambayo hakutaka kabisa izuiliwe, Anne aliruka juu huku kisu chake chenye ncha kali kikiwa mkononi, lengo lake likiwa kumchoma bibi kizee shingoni lakini kabla hajamfikia bibi alizirusha tunguli zake juu na zilipodondoka chini zilipasuka!
Moshi mkubwa ulikifunika chumba na kumfanya Anne ashindwe kuona mbele baadaye mwanga mkubwa ulimulika kila kona ya chumba, Anne aliona kitu kama moto ukiwaka chumbani lakini cha kushangaza hakuhisi maumivu wala kuungua.
Anne aliendelea kuzunguka chumbani akimtafuta bibi kizee lakini hakufanikiwa kumpata sehemu yoyote ya chumba! Ghafla alihisi kuanza kulewa na kupoteza fahamu na hatimaye akajikuta akianguka sakafuni, hakuelewa tena kilichoendelea na alipozinduka alishangaa kujikuta akiwa amelala nje ya nyumba yake akiwa uchi wa mnyama! Alishindwa kuelewa nini kilitokea mpaka akajikuta nje!

Je nini kitaendelea?
Je Anne ataweza kuwaua wengine?
Je watoto wake watabaki salama?
 
SEHEMU YA 13


Ilikuwa ni saa kumi na mbili kasorobo na hapakuwa na mtu yeyote aliyekuwa ameingia ndani ya nyumba ya Anne asubuhi ile, alichofanya baada ya kuzinduka ni kukiokota kisu chake kilichokuwa pembeni na kujikongoja taratibu kuingia ndani ambako alizunguka akamtafuta bibi kizee yule lakini hakumuona mahali popote! Alishindwa kuelewa mahali alipokuwa lakini alihisi ni lazima aliondoka kichawi.
Alipoingia katika chumba alicholala mama yake aliikuta maiti ikiwa imelala sakafuni ikiwa imezungukwa na damu nyingi iliyoganda, huruma ilimshika Anne! Alikuwa amemuua mama yake aliyemzaa.
“Shauri yake si alinianza mwenyewe, kanitesa sana!” Alisema Anne kwa hasira huku akilia alijua wazi alilolifanya lilikuwa kosa.
“Sikuwa tayari Nancy na Patrick wafe halafu mama aendelee kuishi! Ni heri mimi niendelee kuteseka na hii damu mpaka mwisho wa maisha yangu lakini mama afe na sijutii nilichokifanya!” Aliendelea kusema peke yake Anne.
Ghafla kumbukumbu za tangu utoto wake zilimwijia, alikumbuka jinsi mama yake alivyompenda, alishindwa kuelewa ni kitu gani kilitokea kiasi cha kumfanya mama yake ampe mateso makubwa kiasi kile!Yaliyompata shuleni yalimuumiza zaidi moyo wake, alipokumbuka kifo cha Dio mvulana wa kwanza kumpenda hasira yake ilizidi kumpanda zaidi.
“Kwa kweli aliyonifanyia mama ulistahili kifo! Hakuna mtu angeweza” Alipaza sauti Anne.
Alitoka chumbani na kwenda moja kwa moja hadi chumba alicholala bibi kizee mwingine aliyemuua, hakuamini alipokuta maiti ya bibi kizee aliyemuua haipo! Alishindwa kuelewa ilikuwa wapi na ghafla alisikia sauti ikitoka darini lakini hakumuona mtu aliyekuwa akiongea, ilikuwa sauti nzito na ya kutisha.
“Tunakuachia mzoga wa mama yako sisi tunaondoka zetu! Usingeweza kutuua kwani sisi si damu yako!”
Baada ya sauti hiyo Anne alishuhudia kimbunga kikubwa kikiitingisha nyumba yake na paa la juu ya chumba alichokuwa amesimama liliezuliwa mabati kama matano yakatupwa pembeni Anne akauona mwanga kutoka nje.
“Bahati yao!” Anne alitamka akijua bibi vizee wengine walikuwa wameondoka kichawi.
Anne alikuwa amebaki na maiti ya mama yake, alianza kufikiria ni kitu gani angefanya na maiti hiyo na alikuwa na uhakika kabisa hapakuwa na mtu yeyote aliyefahamu nini kilichotokea ndani ya nyumba yake na hakutaka mtu yeyote aelewe.
Alijua wazi kuwa hakuna mtu angekuwa kumsaidia kuzika mwili wa mama yake na alijua ni lazima watu wangehoji kilichomuua, akili ilimzunguka kichwani kwani hakutaka kubaki na maiti ndani kama ilivyotokea kwa watoto wake.
“Nafunga mlango na ninatoka kwenda kwa mchungaji Aaron kuwanyonyesha watoto wangu, simwambii mtu yeyote juu ya jambo hili, nikirudi usiku nitaibeba maiti kwenda kuitupa barabarani halafu nitatangaza mama yangu amepotea!” aliwaza Anne.
Alichofanya baada ya mawazo hayo ni kuingia ndani ya nyumba yake na kuvaa nguo safi, akachukua taulo nyingine nzito akaikunja na kuvaa katikati ya miguu yake ili kuzuia damu iliyokuwa ikitoka isimchafue zaidi.
**********
Ali funga mlango wa nyumba yake na kuondoka taratibu kwenda nyumbani kwa mchungaji Aaron kunyonyesha watoto wake ndani ya moyo wake alijawa na huzuni, moyo wake ulikuwa mzito kupita kiasi kwa sababu ulibeba siri kubwa ya mauaji.
Pamoja na kuua na maiti kuwa ndani Anne alikuwa ameamua kuonyesha ushujaa, hakutaka kuonyesha dalili yoyote juu ya mauaji aliyoyafanya.
“Anne, una matatizo gani leo?” Mke wa mchungaji alimuuliza Anne baada ya kugundua tofauti katika tabia yake.
“Hapana mama mchungaji najisikia kichwa kinauma sana, nafikiri ni sababu ya mawazo!”
“Mh! Lakini nahisi kuna tatizo linalokusumbua!”
“Hapana mama na lingekuwepo lazima ningekueleza!”
Muda wote akiwanyonyesha watoto wake mawazo yake yalikuwa chumbani ilipolala maiti ya mama yake ni hicho ndicho kilifanya mke wa mchungaji agundue! Alipomaliza kuwanyonyesha watoto aliwakabidhi kwa mama mchungaji akawabusu usoni na kuaga kurudi nyumbani kwake.
Njiani wazo jipya lilimwijia, hakuelewa wazo hilo lilianzia wapi, ghafla alijikuta akitamani kupita nyumbani kwa Delila ili aonane na Huggins! Aliogopa kwenda alipoyakumbuka mambo aliyofanyiwa na Huggins mara ya mwisho, kwa sababu moyoni mwake bado alijisikia kumpenda Huggins alijipa moyo na kuamua kupita tena ingawa moyo wake ulijaa hofu.
Alijipa moyo na kuanza kutembea kuelekea nyumbani kwa Delila lakini alipokaribia akiwa umbali kama wa mita mia moja na hamsini alishangazwa na umati wa watu uliokuwepo, kulikuwa na magari mengi sana yaliyoegeshwa mbele ya nyumba ya Delila!
Alipoangalia vizuri alilitambua gari la baba yake na Huggins! Moyo uliruka ghafla na ghafla aliona wanawake wengi wakijishughulisha na kusomba maji huku wengine wakipasua kuni.
Anne alishindwa kuelewa kilichokuwa kimetokea nyumbani kwa Delila mpaka kuwa na idadi kubwa kiasi kile ya watu, wazo lililomwijia kwanza kichwani mwake lilikuwa ni harusi! Alihisi uwezekano wa Huggins kufunga ndoa na Delila kama njia ya kumkomoa na kumuumiza moyo.
Alijaribu kusikiliza sauti ya muziki ambayo aliamini ingekuwa ishara ya harusi hakusikia lakini alipotulia zaidi alisikia sauti ya vilio vya watu! Moyo wake ulishituka ikabidi asogee karibu zaidi.
Aliposimama katikati ya uwanja wa nyumba ya Delila kilio kiliongezeka, watu walizidi kulia kuliko hata mwanzo, maneno yenye kumuumiza yalitamkwa katikati ya vilio vya akina mama na alilisikia jina lake likitajwa akilalamikiwa kusababisha kifo cha Huggins.
“Bila Anne kuwaua watoto wake Huggins asingeondoka nyumbani kwake kuja kwa huyu malaya na hivyo asingekufa!”
Maneno hayo yalizidi kumchanganya akili Anne na alishindwa kuamini kama Huggins alikuwa amekufa! Afe vipi wakati alionekana mzima siku aliyomkimbiza na kumkata panga!
“Haiwezekani! Huggins haweza kufa” alisema Anne akitembea kuelekea jikoni walikokuwa akina mama wengi alipowakaribia alishangaa kuona wanawake wote wakianza kusambaa na wengine kumkimbia, Anne alijisikia vibaya.
Anne alikumbuka kilichokuwa kikiendelea watu waliogopa kuongea naye sababu ya vitu viwili, cha kwanza ni amri iliyotolewa na uongozi wa mtaa lakini cha pili kilikuwa ni mkosi aliomwagiwa na mama yake dirishani mara tu baada ya mazishi ya watoto wake!
Alijaribu kuwasogelea akinamama lakini walizidi kumkimbia, kabla hajaondoka eneo hilo vijana watatu walimfuata wakamkatama na kuanza kumvuta kwa nguvu kumwondoa nyumbani pale.
“Jamani mnieleze tu kimetokea nini?”
“Mumeo Huggins amekufa!”
“Haiwezekani amekufa vipi mume wangu wakati alikuwa mzima?”
“Amenyweshwa sumu na Delila inaaminika alikuwa akimpa dawa ya mapenzi, hakujua kumbe ilikuwa sumu hivi sasa Delila ametoroka!”
“Sasa kwanini mnanitoa kwenye msiba wa mume wangu?”
“Haiwezekani wazee wamesema hawataki kukuona msibani sababu wewe ni mchawi!” Vijana wale walipomfikisha barabarani tu walimwacha na kuondoka zao kurudi nyumbani kwa Delila
Anne alilala barabarani akilia alikuwa akimlilia Huggins, alimpenda na aliamini ni matatizo yake Anne ndiyo yaliyochangia sana kifo cha mumewe, alimlaumu mama yake kwa kila kitu.
“Tena afadhali nimemuua !” alisema Anne huku akisimama, machozi yalikuwa yakimmwagika mfululizo.
****
Muda mfupi baadaye akiwa amesimama barabarani alishuhudia sanduku likibebwa na kuingizwa katika moja ya magari, watu wengi walipanda kwenye magari na msafara mrefu ulianza kuondoka nyumbani kwa Delila.
Ilivyoonekana ndugu wa Huggins walikwenda nyumbani kwa Delila kuichukua maiti ya Huggins kuirudisha nyumbani kwa baba yake kwa ajili ya mazishi!
Gari lenye jeneza lilipopita karibu yake Anne alianza kulikimbilia jambo hilo lilionyesha ni kiasi gani Anne alimpenda mumewe pamoja na kutengana! Baadhi ya akina mama ndani ya gari walimuonea huruma na kumwomba dereva asimamishe gari ili Anne apande lakini dereva alikataa na kuendelea na safari, Anne aliendelea kulifukuza gari hilo bila kuchoka.
“Hivi huyu dada ni kichaa?” Aliuliza mmoja wa wanawake aliyekuwa ndani ya moja ya magari.
“Kichaa? Hapana huyu ni mke wa marehemu!”
“Sasa ni kwanini hapandi kwenye gari badala yake anakimbia kwa miguu?”
“ Ametengwa na kijiji baada ya kuua watoto wake wawili na ni yeye anayedaiwa kusababisha Huggins afe, wazazi wa marehemu hawataki hata kumwona kwenye mazishi!”
Mbele zaidi Anne alichoka na kuanguka chini, magari yalipita yakimwacha amelala chini, hakuna aliyeonyesha kumjali baadaye alinyanyuka na kuanza kutembea taratibu kuelekea nyumbani kwao na Huggins, alipania kuhudhuria mazishi ingawa alijua asingeruhusiwa.
Alipofika nyumbani kwao na Huggins alishangaa kukuta hakuna gari hata moja, ikabidi awaulize watu waliokuwepo na kuambiwa mwili wa Huggins ulisafirishwa kwenda Musoma kwa mazishi, Anne aliishiwa nguvu na kukaa chini na kuendelea kulia, hakuliona kosa lake mpaka azuiliwe kuuona mwili wa marehemu mume wake mara ya mwisho!Kwa mara nyingine tena alimlaumua marehemu mama yake.
****
Alifika nyumbani kwake saa nne ya usiku akiwa na wazo moja tu la kuuchukua mwili wa marehemu mama yake na kwenda kuutupa njia panda ili kupoteza ushahidi kuwa ni yeye aliyefanya mauaji!

Je nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 14


Ilikuwa ni siku ya Februari 14, Siku ya Wapendano au Valentine Day kama ilivyojulikana na watu wengi, siku ambayo kabla ya Anne na Huggins kuingia katika migogoro yao ya ndoa, walisherehekea kushinda hata walivyofanya kwa Sikukuu ya Krismasi na mwaka mpya.
Ni siku waliyoonyeshana upendo mkubwa sana kati yao, walikwenda sehemu ambayo hawakuwahi kufika kabla na kula chakula pamoja, kucheza muziki na walipigana mabusu mbele ya watoto wao, ilikuwa ni siku nzuri na ya furaha kwa familia yao.
Valentine ya siku hiyo ilikuwa tofauti sana na miaka ya nyuma, Huggins hakuwepo tena na si kuwepo nyumbani tu bali alikuwa amekufa, watoto wake wawili Frank na William nao pia walikuwa kaburini na Patrick na Nancy watoto wake waliobaki aliwahifadhi kwa mchungaji Aaron ili kuwaepusha na nguvu za kichawi.
Anne alikuwa peke yake ndani ya nyumba kubwa ambayo awali aliishi na familia yake yenye furaha, ukubwa wa nyumba yake ndiyo uliifanya itishe zaidi na ilikuwa kimya, alitamani hali ingekuwa tofauti.
Alikuwa amekaa mbele ya maiti ya mama yake mzazi akilia machozi, maisha yake yalikuwa yamebadilika tena na kumrudisha alikotokea, kwenye maumivu na mateso makali ya maisha, yote hayo kwa sababu ya mama yake.
Anne alimlaumu mama yake aliyekuwa amemuua kwa mkono wake mwenyewe kwa yote yaliyotokea, kila alipoiona maiti ya mama yake mbele yake hasira ilizidi kuongezeka, alitamani achukue tena kisu achome mama yake ingawa tayari alishakufa, alihisi akili yake haikuwa sawa, alihisi kuchanganyikiwa na kuwa mwehu!
“Ni lazima nitoe hii maiti hapa ndani nikaitupe barabarani, baadaye nitoe taarifa polisi nikijifanya mama yangu amepotea, polisi wakimtafuta lazima wataikuta maiti yake imetupwa hapo kila mtu ataamini mama ameuawa na majambazi!” Alisema Anne moyoni mwake.
Moyoni mwake aliogopa na alihisi kutetemeka mwili lakini pamoja na hali hiyo hakuwa na la kufanya ili kujiepushia matatizo ilikuwa ni lazima aiondoe maiti ya mama yake ndani.
“Vinginevyo kama ikikutwa humu ndani mambo yataniharibikia!” Aliwaza Anna.
Alipoangalia saa yake ya ukutani ilimwonyesha tayari ilikuwa saa tano kasoro dakika kumi na sita! Anne alinyanyuka na kutembea kinyonge hadi chumbani kwake ambako aliwasha taa na kuchukua suruali na koti jeusi lililotumiwa na marehemu mume wake, Huggins na kuvaa wakati akitoka chumbani alipitia kofia kubwa nyeusi iliyokuwa ukutani nayo pia akaivaa, alisimama mbele ya kioo na kugundua ni kiasi gani alikuwa amebadilika.
“I’m going for the last mission!”(ninakwenda kwa shughuli ya mwisho) Alijisemea mwenyewe moyoni mwake.
Alinyoosha moja kwa moja hadi chumbani ilikokuwa maiti ya mama yake mama yake alikuwa mnene sana na Anne alijua maiti yake ingekuwa nzito lakini hakuhitaji msaada wa mtu mwingine, alijipa moyo na bila kujua zilikotokea nguvu nyingi mwilini mwake aliunyanyua mwili wa mama yake na kuuweka begani, akatoka nao nje ya nyumba yake ambako aliuweka chini na kukimbia nje kuangalia usalama kwani hakutaka mtu yeyote hasa majirani waigundue kazi aliyokuwa akiifanya usiku huo.
Alipohakikisha hapakuwa na mtu yeyote akipita Anne alirudi mbio hadi uwani ambako aliubeba mwili wa mama yake begani kwa mara nyingine na kuanza kutoka nao nje, ambako aliingia katikati ya migomba na kuanza kutembea kuelekea darajani, hakutaka kutumia barabara kwa kuhofia angeweza kukutana na watu ambao wangetaka kujua nini alichobeba.
Usiku ulikuwa wa giza nene na manyunyu ya mvua yaliendelea kudondoka taratibu, siku hiyo ya Valentine ilionekana ya kutisha sana lakini Anne hakuogopa alikuwa ameamua kutimiza kazi yake kikamilifu.
Kutoka nyumbani kwake hadi darajani ulikuwa umbali wa mita kama mia tatu hivi, ulikuwa ni umbali mrefu sana kwa uzito wa mzigo ambao Anne alikuwa nao begani kwake ukizingatia alikuwa msichana, kwa mara mbili mfululizo alilazimika kuishusha chini maiti ya mama yake alipolemewa sana na uzito.
Ghafla alishtukia radi ya ajabu ikianza kupiga katikati ya migomba, mwanga mkali ulionekana kila sehemu aliyopita, alijua ni nini kilitaka kutokea! Ni wazi ulikuwa uchawi wa mzimu wa Lutego, Anne aliogopa sana na kujikuta akishindwa kuendelea na safari yake na kuitupa maiti ya mama yake chini.
Alianza kukimbia haraka kurudi alikotokea sauti nene na nzito ilimfuata nyuma yake, ilikuwa ni kama sauti ya binadamu lakini hakuwa binadamu wa kawaida!
“Umemuua Malkia wetu ni lazima na wewe ufe, tena kifo cha mateso!” Iliendelea kusema sauti hiyo na kumtisha zaidi Anne.
Radi ilizidi kupiga na muungurumo uliongezeka ghafla mvua kubwa tena ya mawe iliyoambatana na upepo ilianza kunyesha, Anne alishindwa kuelewa mvua ile ilitokea wapi kwa sababu hapakuwa na mawingu mazito na makubwa jioni ya siku hiyo, hakuwa na uhakika wa kufika salama nyumbani kwake.
“Ni heri mniue mimi niliyewakosea kuliko kuwaua watoto wangu wasio na hatia!” Alipiga kelele Anne huku akikimbia katikati ya migomba, mawazo yake yote yakiwa kwa watoto wake, alijua ni lazima naye angekufa kabla ya kufika nyumbani, alijua yote yaliyokuwa yakitokea yalifanywa na bibi vizee waliotoroka mauaji yake.

****
Gongo ilikuwa ni pombe haramu na ilipigwa vita kila siku iliyokwenda kwa Mungu, lakini pamoja na vita hiyo bado watu waliendelea kuitumia, ilionekana kama hapakuwa na njia yoyote ya kuwafanya wananchi wasinywe pombe hiyo.
Bernard au Bernie Killer kama alivyojulikana na wengi maeneo ya Isamilo mjini Mwanza alikuwa ndiye mpikaji maarufu wa pombe hiyo na alishafungwa mara mbili mfululizo kwa kosa la kujishughulisha na pombe haramu ya gongo lakini hata alipotoka gerezani hakukoma, bado aliendelea kupika gongo kazi iliyomfanya aishi na hata kusomesha watoto wake!
Alifanya kazi hiyo usiku wa manane wakati watu wote wamelala, alifanya hivyo ili kujiepusha na maaskari na alifanyia katikati ya migomba, alifanya kazi hiyo yeye na mke wake pamoja na vijana wengine wanne waliowaajiri.
Usiku wa siku hiyo ya Valentine, Bernard na mke wake pamoja na wafanyakazi wao walikuwa katikati ya migomba wakiendelea na kazi ya kupika gongo, walishangaa kuona mtu aliyevaa nguo nyeusi akitokea upande wa kulia katikati ya migomba! Wote walishtuka na kufikiri labda ni polisi waliokuwa katika msako wa wapika gongo, waliingiwa na hofu na kulala chini pembeni ya mtambo wao.
Mtu huyo alionekana amebeba kitu mabegani kwake na alipita eneo walilokuwa bila kufanikiwa kuwaona, mbele aliutupa mzigo huo chini na kuanza kukimbia kurudi alikotoka na hapo hapo mvua kubwa ilianza kunyesha na radi ilitanda kila mahali, hali ilibadilika ghafla.
“Sijui ametupa nini?”Bernard alimwambia mke wake.
“Hata mimi sijui, isije kuwa ni pesa?”
“Acha nikaangalie, vijana twendeni lisije kuwa bomu halafu linilipukie peke yangu!” Alisema Bernard huku akiwaita vibarua wake na wote waliongozana kwenda mahali ulipotupwa mzigo ule.
“Mh! Huyu siyo mtu kweli?” Alisema Bernard!
“Tumfunue mzee!”
“Mfunueni!” Bernad aliwaruhusu vijana wake na kweli walifunua mwili ule na Bernard akaumulika kwa tochi.
“Masikini huyu si ni mama yake na yule jirani yetu Anne, tena alikuja juzi tu kuhani msiba wake kimempata nini?” Alisema Bernard kwa sauti ya chinichini!
“Ni yeye kweli au umemfananisha!”
“Ni yeye namfahamu vizuri sana huyu mama ni mama mkwe wake na marehemu Huggins aliyefariki jana!”
“Sasa tufanye nini?”
“Hata mimi sijui ila najaribu kufikiria ni nani aliyemtupa hapa?” Alizidi kuuliza Bernard na baadaye kuanza kumulika pembeni ni huko ndiko alikokiona kiatu kimoja!
“Mh! Hiki kiatu mbona ni cha Anne? Ina maana Anne ndiye ametupa maiti ya mama yake hapa, haiwezekani hii ni njama ya kumwigiza matatani binti wa watu, hebu tufungashe vifaa vyetu tuondoke eneo hili tayari limekwishaingiwa na gundu polisi wanaweza kufika hapa wakati wowote!”
Walianza kufungua mitambo yao na kuifunga tayari kwa kuondoka kila mmoja wao alikuwa na hofu, lilikuwa tukio la kwanza katika historia ya kazi yao ya kupika gongo waliyoifanya kwa miaka kumi na tano.
Kabla hawajaanza kuondoka eneo hilo walishtukia mtu akitokea katikati ya migomba huku akinyata, mtu huyo alikuwa na tochi yenye mwanga mkali mkononi mwake na alimulika kila mahali kuzunguka eneo ilipolala maiti.
“Huyu si ndiye aliyekimbia au?” Alionong’ona Bernard akiongea na mmoja wa wafanyakazi wake.
“Ni yeye alivaa nguo nyeusi hivihivi!”
“Hebu tulieni mimi nimchunguze vizuri ni nani hasa?” Alisema Bernard na kuweka mizigo yake chini, akaanza kutembea kwa tumbo kuelekea nyuma ya mahali ilipolala maiti.
“Masikini sijui kile kiatu kipo wapi jamani, kitaniponza ni lazima watajua ni mimi ndiye nimemuua mama!” Alisikika akisema mtu huyo, Bernard aliitambua sauti ile, haikuwa sauti ngeni masikioni mwake ingawa hakuweza kuitambua mara moja ni ya nani.
“Hiki hapa!! Yes, afadhali, kisingepatikana ningefanya nini mie?” Sauti ile ilimfikia tena Bernard na kumpa jibu la uhakika, ilikuwa ni sauti ya Anne asilimia mia moja.
Bila kugundua kuwa palikuwa na mtu akimchunguza Anne alianza kutimua mbio kwa kutumia tochi yake na kutokomea katikati ya migomba na kupotea.
“Ni Anne amemuua mama yake!” Alisema Bernard mwili wake ukitetemeka.
“Nani?” Mkewe aliuliza kwa mshangao.
“Ni Anne!”
“Kweli?”
“Ndiyo na ni lazima suala hili niitaarifu polisi!” Alisema Bernard!
*****
Alipofika nyumbani kwake Anne aliingia moja kwa moja hadi ndani na kujitupa kitandani, nguo zake zote zililowa na maji lakini hakujali, alianguka hivyo hivyo na kuyalowanisha mashuka yote alikuwa amechoka kupita kiasi, kazi aliyokuwa amefanya ilikuwa ngumu sana.
Aliendelea kuwa na uhakika hapakuwa mtu aliyemwona akitimiza azma yake, aliamini zoezi zima lilikuwa limekwenda kama alivyopanga! Kilichokuwa kimebaki mbele yake wakati huo ni kwenda kituo cha polisi na kutoa taarifa juu ya kupotea kwa mama yake mzazi.
Hakutaka kupoteza muda zaidi, bila kuchelewa ingawa ilikuwa ni usiku wa manane alitoka na kuanza kutembea akielekea kituo cha polisi, Anne hakuogopa kitu kwani ilikuwa ni lazima atoe taarifa polisi ili kuficha ukweli wa tukio zima.
Alipofika kituoni kabla hajaingia ndani, mlangoni alikutana na Bernard aliyeshuhudia Anne akilia na machozi.
“Vipi jirani?”Bernard aliuliza.
“Mama yangu amepotea tangu jana na nimemtafuta bila mafanikio au umemwona mahali?”
“Hapana sijamwona, pole sana kwa hiyo umekuja kutoa taarifa siyo?” Alisema Bernard ingawa alifahamu kila kitu na alishatoa taarifa polisi!
“Ndiyo!”
“Sawa basi mimi naondoka polisi watakusaidia!”
Alipoingia ndani kabla hajasema kitu chochote Anne alishtukia anapigwa pingu mikononi.
“Vipi jamani mbona mnanifunga pingu?”
“Muuaji mkubwa wee!”
“Nimemuua nani?”
“Umemuua mama yako halafu unajifanya mjanja!” Alisema Askari na kumpiga Anne kwa rungu kichwani damu ilianza kumtoka.
“Mimi nimemuua mama yangu kwa makosa gani?”
Alizidi kujitetea Anne lakini hakuna mtu aliyemsikiliza.
“Mpakieni ndani ya gari mwende naye nyumbani kwake mkapekue haraka!” Mkuu wa kituo aliamuru na Anne alianza kuvutwa na kutupwa ndani ya gari, Anne alishindwa kuelewa ni nani aliiitoa taarifa hiyo polisi, aliamini kwa hali ilivyokuwa ndani ya nyumba yake hapakuwa na jinsi ya kujitetea juu ya mauaji ya mama yake kwani damu zilikuwa bado zimo vyumbani na alishindwa kuelewa ni maelezo gani angeyatoa juu ya damu hizo, ili aaminike kuwa hakumuua mtu.
“Sijui niseme nilichinja kuku! Lakini pia hawataamini!” aliwaza Anne.
Walipofika nyumbani kwake waliingia moja kwa moja hadi ndani na kuanza kupekua nyumba nzima, wote hawakuamini walipopambana na damu iliyogandamana sakafuni katika baadhi ya vyumba vya nyumba yake.
“Hii damu ni ya nini?”
“Kuku!”
“Kuku? Unatufanya sisi watoto, hebu sema ukweli!”
Alisema mmoja wa maaskari na kuanza kumshushia mvua ya virungu Anne kichwani mpaka akaanguka chini na kupoteza fahamu, alipozinduka damu nyingi zilikuwa zikimtoka mwili na baadaye aliendelea kupewa mateso makali sana ili aeleze ukweli.

Je nini kitaendelea?
Je Anne ataweza kusema ukweli?
 
SEHEMU YA 15


Anne alikuwa chini akiwa amepoteza fahamu kwa kipigo alichokipata lakini hakuna mtu aliyekuwa na muda wa kuchukua maji na kummwagia ili azinduke, polisi walimchukua hivyohivyo na kwa harakaharaka walimpakia ndani ya gari lao akiwa na pingu zake mkononi kwenda naye kituoni, walishakuwa na uhakika asilimia mia moja kuwa Anne ndiye alimuua mama yake mzazi na kwenda kumtupa porini.
Alipofikishwa kituoni alipelekwa moja kwa moja hadi mahabusu ambako lango lilifunguliwa na kutupwa ndani na kuwaangukia mahabusu wengine waliokuwemo ndani.
Alilala chini akiwa hajitambui lakini kwa ubaridi uliokuwepo sakafuni uliotokana na mikojo ya mahabusu Anne alirejewa na fahamu zake saa sita ya usiku na kujikuta yupo kwenye chumba kidogo chenye giza! Aliangalia huku na kule ndani ya chumba hicho na kushindwa kuelewa mahali alipokuwa.
Alihisi yupo katikati ya watu na aliposikiliza vizuri alisikia watu wakihema na kukoroma pembeni yake, alizidi kuingiwa na hofu na kuchanganyikiwa alishindwa kuelewa ni mahali gani alipokuwa, moyo wake ulizidi kwenda mbio, hakuwa na kumbukumbu juu ya tukio lolote lililotokea mpaka kumfanya awe pale.
Alipojigusa usoni juu ya jicho lake la kulia mkono wake ulikutana na uvimbe mkubwa! Ghafla kumbukumbu zilimiminika kichwani mwake juu ya kipigo kibaya alichokipata kutoka kwa polisi na pia aliyakumbuka mauaji ya mama yake aliyoyafanya siku hiyo.
“Hivi hapa nipo wapi hasa? Au Nipo mochwari nini? Labda polisi walifikiri nimekufa wakaniweka chumba cha maiti?” Aliwaza Anne lakini sauti za watu wakikoroma zilimfanya aelewe mahali pale hapakuwa kama alivyopafikiria!
Alipata nguvu na kunyanyuka akaanza kujikongoja kutembea mahali kulikoonekana kuwa na mwanga kidogo, alihisi kuwakanyaga watu waliolala sakafuni, alitembea hadi getini, ambako alimkuta mwanamke mmoja amesimama wima akiimba wimbo wa dini ulioonekana kuwa pambio.
“Dada shikamoo!”
“Marahaba mdogo wangu hujambo?”
“Sijambo! Hivi hapa ni wapi?” Anne aliuliza.
“Mdogo wangu hapa hupafahamu?”
“Ndiyo dada!”
“Hapa ni mahabusu!”
“Dada nimeletwa hapa saa ngapi?”
“Usiku lakini umefanya nini mdogo wangu?”
“Sijafanya kitu dada wananionea!”
“Hapana haiwezekani ukaletwa hapa hivihivi!”
“Kwani wewe imekuwaje mpaka ukaingia humu?”
“Nimeua watoto wangu mwenyewe!”
“Umeua watoto wako? Kwanini?”
“Kwa bahati mbaya nilikuwa napika mboga jikoni wakati huohuo nikawa napaka dawa ya kunguni kwenye magodoro sijui ile dawa iliingia vipi katika mboga watoto wangu watatu walipokula wote wakafa, ikagundulika ni sumu ndiyo iliwaua nikakamatwa ndiyo maana nipo hapa! Sasa niambie na wewe kitu gani kimekupata mdogo wangu?”
“Dada ni siri nakueleza wewe tu, kwa kweli nimemuua mama yangu mzazi!”
“Mdogo wangu kimetokea nini mpaka ukafikia hatua hiyo? Nini kilikuudhi?”
“Mama yangu alinitesa sana tena kwa muda mrefu, aliwaua watoto wangu wawili, alisababisha kifo cha mume wangu na bado alitaka kuwaua watoto wangu wawili waliobaki! Nilipokataa akanipiga mimi na ugonjwa wa kupatwa na hedhi kila siku, nikawa nanuka na watu wakanitenga, hapakuwa na njia nyingine yoyote ya kumzuia asiendelee kunitesa zaidi ya kumuondoa duniani, sikufichi dada nimeua lakini mahakamani sitakubali jambo hilo, najua nitanyongwa! Kifo cha mama yangu hakinisikitishi hata kidogo mama alistahili kufa, kitu kimoja tu kinanitia huzuni nacho ni watoto wangu nimewaacha wakiwa na miaka miwili tu nani atawalea?” Alimaliza Anne na kuanza kulia.
“Usilie pole sana mdogo wangu hebu nielezee umemuuaje mama yako?”
“Anne alieleza kila kitu kilivyotokea, alimchoma mama yake kisu na kwenda kutupa mwili wake porini ambako hakuelewa ni nani alimwona na kutoa taarifa polisi hatimaye akakamatwa, alimweleza pia mateso mengine mengi yaliyompata maishani mwake ambayo yalisababishwa na mama yake.
“Lakini kesi hiyo unaweza kushinda tena kirahisi kabisa!”
“Inawezekanaje dada wakati mimi nimeua?”
“Mimi ni mwanasheria, hakuna ushahidi wa kutosha kukubana!”
“Mbona damu wameikuta ndani?”
“Hiyo siyo sababu damu inaweza kuwa ya ng’ombe, mbuzi au hata kunguni!”
“Nitashinda vipi kesi hii?”
“Omba Mungu mimi nitoke hapa mahabusu, ndugu wananishughulikia nikitoka naweza kukusaidia bure ili ushinde!”
“Kweli?”
“Ndiyo wala usiwe na wasiwasi, hii siyo kesi kabisa, mimi pia nitashinda kwa sababu sikuua kwa kukusudia, nisingeweza kuua watoto wangu mwenyewe niliowapenda!”
“Unaitwa nani?” Anne alimuuliza dada yule.
“Mimi naitwa Lydia Ishengoma ni mwanasheria mashuhuri sana hapa mjini, wewe unaitwa nani?”
“Mimi naitwa Anne nakuomba sana ukitoka hapa kabla yangu nisaidie dada yangu, watoto wangu! Watoto wangu nawapenda sana nimewaacha wadogo mno watateseka!” Anne alianza kulia tena.
“Usilie binti utatoka tu ingawa inaweza kukuchukua muda mrefu kidogo lakini mwisho ni lazima uwe huru!”
Waliongea mengi hadi mwanga wa asubuhi ulipoanza kuonekana na baadaye ndugu wengi walianza kuja kufuatilia masuala ya ndugu zao, maaskari waliwaita baadhi ya mahabusu mmoja baada ya mwingine wakawa wanatoka nje na wengine walipelekwa mahakamani, mahabusu wote walitoka wakabaki Anne na Lydia peke yao.
“Nyie wauaji hamuwezi kutoka kaeni humo ndani msubiri kupelekwa Butimba!” Alisema askari mmoja wa kike.
Mpaka saa nne asubuhi ilipotimu Anne na Lydia walikuwa bado wako mahabusu, wahalifu wengine zaidi walizidi kuongezwa katika chumba hicho kidogo. Ghafla Anne akiwa katikati ya mawazo alisikia sauti ya watoto wakilia na aliposikiliza vizuri aligundua zilikuwa ni sauti ya watoto wake! Alisimama wima na kuchungulia kaunta, huko aliwaona mchungaji Aaron na mkewe wakiwa wamewabeba Patrick na Nancy mikononi, watoto wakilia kwa sauti ya juu!
“Jamani watoto wangu! Watoto wangu jamani” Anne alianza kupiga kelele, aliumia kuwaona watoto wake wakilia, alijua asingeishi nao tena maishani mwake alijua ilikuwa ni lazima anyongwe.
“Kelele!” Askari mmoja aliongea kwa sauti akimuamuru Anne anyamaze.
“Nawataka watoto wangu jamani, nataka niwaage kwa mara ya mwisho!” Alisema Anne.
“Umeambiwa unakwenda kufa?” Alijibu askari
“Ningejua nisingemuua mama, lakini kama nisingemuua ni lazima angewaua watoto wangu, ni heri mimi nikateseka gerezani lakini Patrick na Nancy wawe salama!” Anne aliwaza.
Alipotupa tena macho yake kaunta aliwashuhudia polisi wakiwasukuma mchungaji Aaron na mkewe kuwatoa nje ya kituo, aliendelea kuwaona watoto wake wakilia na roho ilimuuma sana! Aliwahurumia watoto wake na alijua kwa yeye kupelekwa gerezani wangeishi kama yatima duniani kwa sababu baba yao alikuwa amekufa!
*****
Muda mfupi baadaye Anne na Lydia walitolewa mahabusu na kuanza kusukumwa kwenda nje ambako gari lilikuwa tayari kuwapeleka gerezani Butimba, alipofika nje Anne alitupa macho kulia kwake na kuwaona mchungaji Aaron na mkewe wakiwa na watoto wake mikononi!
Alishindwa kuvumilia na kujikuta akitimua mbio kuwafuata akiwa na pingu zake mikononi, askari aliyekuwa akiwalinda alifikiri Anne anatoroka, bila kuchelewa alilenga bunduki yake tayari kumfyatulia risasi, lakini kabla hajaachia hata risasi moja alimwona Anne akisimama mbele ya watu wawili wenye watoto.
“Nisogezeeni watoto wangu niwabusu!” Anne alisema kwa sauti kubwa iliyomfikia askari aliyenyosha bundiki yake kwa lengo la kumpiga Anne.
“Ana bahati vinginevyo ningemmalizia mbali!” Alisema askari huyo aliyeonekana si mwepesi kutumia bunduki.
Watoto walisogezwa karibu yake na Anne alianza kuwamwagia mabusu kibao usoni kwao.
“Watoto wangu Patrick na Nancy bakini salama nawapenda na nimemuua bibi yenu kwa sababu ya kuwalinda nyinyi,bibi yenu alitaka kuwaua bila hatia!” Alisema Anne na kuwafanya mchungaji na mke wake ambao hawakuwa na habari juu ya mauaji aliyoyafanya washangae.
“Anne umemuua mama yako?” Mchungaji Aaron aliuliza kabla Anne hajajibu swali hilo maaskari walimvamia na kuanza kumpiga kwa virungu kichwani akaanguka chini tena.
“Nyanyuka twende muuaji wewe!” Alifoka mmoja wa maaskari.
“Mchungaji nitunzieni watoto wangu, ninajua sitatoka gerezani leo wala kesho, wafundisheni kumcha Mungu na mara kwa mara waelezeni kuwa mimi mama yao nipo ili wasinisahau, waleteni gerezani mara kwa mara kuniona!” Anne alisema maneno huku virungu vingi vikizidi kumwangukia chini alipolala.
Baada ya kusema hayo alijikongoja na kunyanyuka ardhini alipoanguka ni kweli aliwatia huruma watu wote waliokuwepo kituoni, uso wake wote ulivimba, na nguo zake zote zilijaa damu, ilikuwa si rahisi hata kidogo kuamini kuwa mwanamke yule alikuwa Anne!
****
Alivutwa na kupelekwa moja kwa moja hadi kwenye gari, ambako alitupwa sehemu ya nyuma na kumkuta wakili Lydia Ishengoma akiwa amekaa!
“Anne tulia watakuumiza hawa hawana huruma!” Wakili alisema.
Anne alinyanyuka na kuanza kuwapungia mchungaji na mke wake waliokuwa bado wamesimama mahali alipowaacha wakiwa watoto wakilia mikononi mwao, mlango wa gari kubwa aina ya Scania walilopanda ulifungwa baada ya kuingia askari mwenye bunduki mikononi.
“Una bahati wewe! Pale nilishaamua kukumiminia risasi kwani nilijua unatoroka, mshukuru Mungu wako!” Askari yule alisema na gari lilianza kuondoka kutoka kituo cha polisi.
Kutoka mjini Mwanza hadi gereza la Butimba ilikuwa ni mwendo wa kama kilometa kumi na tano lakini iliwachukua muda wa saa nzima kwa sababu ya ubovu wa barabara za Mwanza mjini! Walipofikishwa gerezani wote walishushwa na kuingizwa ndani ya gereza walipekuliwa na kuingizwa chumba maalum cha mahabusu wa mauaji ambako walikaa wawili tu.
****
Miaka miwili tu baada ya kuingia gerezani wakili Lydia Ishengoma aliachiwa kutoka gerezani ilipogundulika hakuua kwa kukusudia, kazi yake ya kwanza kama alivyoahidi alipotoka gerezani ilikuwa ni kumtetea Anne! Akijua shida alizokuwa nazo gerezani hasa tatizo la upungufu wa damu ambalo Anne alilolipata mara kwa mara wakili Lyidia alianzisha harakati za kumtetea Anne mahakamani.
Siku wakili Lydia aliyoondoka gerezani Anne alilia kama mtu aliyefiwa na ndugu yake kwa sababu hakuwa na rafiki mwingine yeyote zaidi yake, mahabusu wengine wote walimtenga kwa sababu ya harufu aliyotoa kutokana na hedhi ya kila siku, ni wakili Lydia peke yake katika gereza zima aliyemvumilia, alishindwa kuelewa maisha yake yangeendeleaje baada ya hapo, lilikuwa pigo kubwa!
Huo ndio ukawa mwanzo wa Anne kuingia gerezani, ambako alikaa kwa muda wa miaka kumi akipelekwa mahakamani mara moja kila mwezi ambako kesi yake iliendelea kutajwa na baadaye kuanza kusikilizwa! Alishangaa siku aliyomkuta wakili Lydia amevaa mavazi ya Uwakili akimtetea mahakahami, Anne aliamini ipo siku angekuwa huru.
Anne aliendelea kusota gerezani, nguo alizokuwa nazo zilichakaa damu ziliendelea kumtoka mfululizo, jambo hilo lilimkera sana, alinuka na inzi wengi walimfuata kila alikokwenda! Hali hiyo ilisababisha mahabusu wenzake wamfukuze katika kila chumba alichopangiwa kulala, mwisho akawa analala barazani kwenye baridi na mbu wengi.
Yalikuwa ni mateso makali mno, lakini lawama zote hizo alimtupia mama yake mzazi aliyempa ugonjwa huo wa ajabu.
“Mama alistahili kufa, na sijui ni kwanini alinizaa, inakuwaje mtoto umzae mwenyewe halafu umtese kiasi hiki? Na ninasema siku nikinyongwa huko kuzimu nikimkuta mama ni lazima nimuue tena!” Alilia Anne.
****
Kama alivyowaomba mchungaji Aaron na mke wake walilazimika kuwapeleka Nancy na Patrick gerezani kumwona mama yao kila mwezi, walikuwa ni watoto wazuri waliokuwa na kulelewa katika familia ya Kikristo, walimpenda mama yao pamoja na kuwa alikuwa gerezani. Patrick alifanana sana na marehemu baba yake Huggins lakini Nancy alimfanana Anne kwa kila kitu.
“Mama usijali ipo siku utatoka tu gerezani, tunakupenda mama, wewe ni mama yetu hata kama ni mfungwa!” Hayo ndiyo yalikuwa maneno ya watoto wake walipotimiza umri wa miaka minane.
Katika umri huo walikwisha kuwa watoto wakubwa wenye kuyafahamu mema na mabaya, walikwenda mahakamani kila siku ya kesi ya mama yao ilipofika, ni kama walikulia mahakamani wazee wa mahakahama na Mahakimu wote waliwafahamu Patrick na Nancy!

Je nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 16


MIAKA KUMI BAADA YA KUINGIA GEREZANI

Kesi ilikuwa imepamba moto wakili Lydia Ishegoma alikuwa amedhamiria kumtoa Anne gerezani, kila mara alimtembelea na kufanya naye mahojiano.
“Haupo ushahidi wa kukufunga Anne!”
“Lakini niliua mheshimiwa!”
“Pamoja na hayo lakini nitahakikisha unatoka gerezani kwa sababu uliyofanyiwa na mama yako yalikuwa ya kukulazimisha ufanye ulichokifanya!”
“Nitashukuru kama nitatoka gerezani naomba ujifahidi sana na Mungu atakusaidia, watoto wangu ndio wanaonifanya nihuzunike sana!”
“Kwani kwa hivi sasa wanaishi na nani?”
“Wanaishi na Mchungaji wa kanisa letu, niliwapeleka kwake kabla ya kukamatwa!”
“Hebu nieleze vizuri, unafikiri kuna mtu yeyote aliyekuona wakati ukiibeba maiti ya mama yako kwenda kuitupa?”
“Hapana ilikuwa ni usiku mno na watu wengi walikuwa wamelala isitoshe ilikuwepo dalili ya mvua kubwa kunyesha!”
“Sasa nani aliwaeleza polisi?”
“Hata mimi nashangaa!”
“Kuna watu waliofahamu kuwa wewe na mama yako mlikuwa hamuelewani?”
“Hapa mjini hapana, lakini kijijini kwetu Kome wapo watu wanaoelewa jambo hili!”
“Je, kuna watu walielewa kuwa mama yako alikuja hapa mjini?”
“Ndiyo lakini sio wengi!”
“Baada ya kufanya kitendo hicho ulipiga kelele kuita watu kuwaeleza kuwa mama yako amepotea?”
“Hapana ila nilikwenda moja kwa moja kituo cha polisi kutoa taarifa”
“Na huko ndiko ulikamatwa?”
“Ndiyo!”
“Unahisi nani anaweza kuwa alitoa taarifa polisi?”
“Kwa kweli sifahamu na si rahisi kuelewa na nilishangaa polisi walijuaje”
“Uliushika maiti ya mama yako kwa mikono yako?”
“Ndiyo, kwani vipi?”
“Ilipopimwa haikuonyesha alama za vidole!”
“Labda kwa sababu mvua ilinyesha sana usiku ule!”
“Anne!” Aliita wakili Lydia.
“Naam mheshimiwa!”
“Nitahakikisha unashinda kesi hii!”
“Nitashindaje mheshimiwa wakati niliua?”
“Hiyo kazi niachie mimi! Wamepanga siku ya hukumu iwe Januari 21, leo ni tarehe ngapi?”
“Ni tarehe 15, bado wiki moja tu ninyongwe! Dada Lydia utanisaidia kuwalea watoto wangu?”
“Anne nimekuambia huwezi kunyongwa, kwani hakuna ushahidi wa kutosha kukutia hatiani, mtu mwingine yeyote angeweza kumuua mama yako na kwenda kumtupa porini!”
****
Sifa ya Anne kuwa mwanamke muuaji ilisambaa kwa kasi mjini Mwanza na vitongoji vyake, kwa kitendo cha kumuua mama yake mzazi aliyemleta duniani Anne alionekana ni mwanamke mwenye roho mbaya pengine kuliko binadamu wote! Alilaaniwa na kila mtu na watu wote walitamani ahukumiwe kifo na kunyongwa!
Ni kweli Anne aliua hata yeye hilo alilikubali lakini hakuwa na mtu hata mmoja aliyeufahamu ukweli ni kwanini alifikia uamuzi wa kumuua mama yake aliyemzaa. Alitamani kuueleza ukweli Ulimwengu mzima ili asafishe jina lake lakini hakuwa na nafasi ya kuongea na watu wote! Mtu pekee aliyeufahamu ukweli alikuwa ni wakili wake.
Siku ya Januari 21, 1998 mamia ya watu walifurika mahakama kuu ya Mjini Mwanza kuisikiliza kesi ya Anne, alipoteremshwa tu kutoka katika gari lililombeba kutoka gerezani Butimba akiwa na mahabusu wengine, watu waliokuwa nje ya mahakama walianza kunong’onezana na wengine kusema kwa sauti bila hata uoga kuwa Anne alistahili kifo.
“Mnyongeni tu! Hafai kuishi huyu kwanini amuue mama yake kinyama kiasi kile?” Alisema mama mmoja wakati Anne akipitishwa, maaskari waliokuwa wakimlinda walicheka lakini maneno yale yalimuumiza sana moyo Anne na kumfanya atokwe na machozi, alimhurumia mama yule kwa sababu hakuujua ukweli.
Alitembea kwa shida akiwa amefungwa pingu mikononi na miguuni, nguo zake zilikuwa chafu kupita kiasi na mwili wake ulijaa ukurutu na ulikuwa mweusi kwa sababu ya kutokuoga, alionekana muuaji kuliko wauaji wengine wote waliotangulia.
Anne alitupa macho yake pembeni na kuwaona watoto wawili wakilia huku wakijaribu kujitoa mikononi mwa mwanamke aliyewashikilia, Anne alipomwangalia mwanamke huyo alimkumbuka, alikuwa ni mdogo wake yaani mtoto wa baba yake mdogo, Suzzane na alipotupa macho yake kuwaangalia watoto hao aliwatambua, walikuwa ni Nancy na Patrick watoto wake.
“Watoto wangu! Watoto wangu! Wale pale!” alipiga kelele Anne huku akijaribu kugeuka na kuanza kutembea kuelekea mahali walipokuwa Patrick na Nancy watoto wake mapacha waliobaki, waliosababisha amuue mama yake mzazi ili kuokoa maisha yao.
“Mama! Mama! Mama! ninakupenda mama, pole mama!” Alisema Patrick.
“Niachie! Niachie! Niachie niende kwa mama yangu!” Alilia Nancy huku akimuuma mama yake mdogo mkono ili amwachie lakini aliendelea kumshikilia kwa nguvu asimponyoke.
Anne aliumia sana moyoni mwake kushuhudia kitendo kile cha watoto wake, alitamani kuwasogelea watoto wake lakini alishindwa kwani kabla hajasogea umbali mrefu maaskari walimshika na kumbeba juu akatupwa katika mahabusu ndogo iliyokuwepo karibu na mahakama hiyo, ilikuwa ni mahabusu chafu iliyonuka mikojo na kinyesi.
“Ipo siku mama yangu atakuwa huru na nitamsaidia!” Alisema Patrick.
Katika maisha yao Nancy na Patrick hawakuwahi kuishi na mama yao, kwani kwa mara ya kwanza alipokamatwa walikuwa na umri wa miaka miwili na mpaka siku hiyo alikuwa amekaa gerezani miaka kumi, tayari walikuwa na umri wa miaka kumi na mbili! Lakini pamoja na kutokuishi na mama yao bado walimpenda na waliamini siku moja angekuwa huru na kurejea tena kwao.
****
Muda wa mahakama kuanza kazi uliwadia na watu walianza kuingia mahakamani na kuchukua viti vyao. Patrick, Nancy na mama yao mdogo nao waliingia na kuketi, wote walikuwa wakilia machozi ya uchungu ni kwa sababu walijua siku hiyo ndiyo ilikuwa siku ya hukumu ya mama yao na lolote lingeweza kutokea, kifo ama maisha.
Watu wengi walishindwa kuingia mahakamani kwa sababu ya ufinyu wa nafasi iliyokuwepo na kusimama nje ya mahakama na wengine kukaa chini ya miti wakisubiri mahakama ianze. Mawakili wote walikuwa ndani.
Kesi ya Anne ilipangwa kuwa ya kwanza, Anne alitolewa mahabusu na kuingizwa moja kwa moja hadi mahakamani, alipoingia tu hali ya hewa ndani ya chumba cha mahakama ilibadilika! Inzi waliongezeka na harufu mbaya ilitanda, watu walishindwa kuelewa hali hiyo ilitokana na nini lakini inzi walivyozidi kumfuata Anne wengi walianza kuhisi huenda alikuwa amejisaidia ndani ya nguo zake.
Jaji Raphael Mpoki aliyekuwa maarufu kwa kuhukumu watu miaka mingi katika historia ya Tanzania tena bila huruma alipoketi kitini minong’ono yote iliyokuwepo ndani ya mahakama ilikwisha na mahakama ilianza bila kupoteza hata dakika moja.
Karani wa mahakama alisimama na kuanza kutaja namba ya kesi na baadaye muendesha mashtaka alisimama na kusoma historia nzima ya kesi na baadaye kumwomba Jaji Mpoki amhuhuku Anne kwa sababu ulikuwepo ushahidi wa kutosha kuonyesha ni kweli alimuua mama yake kwa kumchoma visu.
Anne alisimama kizimbani akilia akiwa amewaangalia watoto wake Patrick na Nancy ambao pia waliendelea kulia, roho yake ilimuuma sana kujua ni lazima angehukumiwa kifo na kuwaacha watoto wake wakiteseka peke yao duniani, kuna wakati alijilaumu ni kwanini alimuua mama yake lakini alipokumbuka kuwa mama yake alitaka kuwaua watoto wake alisita kujilaumu na kuona alichokifanya kilikuwa sahihi.
Mahakama iliendelea kuwa kimya wakati mwendesha mashtaka akiendelea kumueleza Jaji Raphael Mpoki sababu za kuitaka mahakama imhukumu mshtakiwa kunyongwa.
“Mheshimiwa Jaji ushahidi wa kutosha upo na hivyo naiomba mahakama yako Tukufu imhukumu mshtakiwa kifo ili iwe fundisho kwa wengine wenye tabia kama hizo!”
****
Jaji Mpoki aliinamisha kichwa chake chini na kuanza kutafakari hiyo ndiyo ilikuwa kawaida yake kabla hajamhukumu mtu kifo! Watu wote walijua baada ya kunyanyuka pale ni lazima angemhukumu Anne kunyongwa.
“Anne!” Jaji Mpoki aliita baada ya kunyanyua kichwa chake lakini Anne hakuitika aliendelea kulia machozi akiwa amewaangalia watoto wake waliokuwa wakilia kwa sauti na kusababisha kelele mahakamani.
“Wanangu Patrick na Nancy leo nakufa kwa ajili yenu!” Badala ya kumwitikia hakimu Anne aliwaita watoto wake.
“Hapana mama usife, bado tunakuhitaji sana usituache!” Patrick alipiga kelele mahakamani na kuchomoka mikononi mwa mama yake mdogo akakimbia na kumfuata mama yake lakini kabla hajakifikia kizimba alikamatwa mkono na askari na kuanza kuvutwa kupelekwa mahali alipokuwa amekaa.
“Anne tafadhali nijibu nakuita!” Jaji Mpoki aliita tena
“Na.a..am mhe...sh..i..mi..wa ja..ji!”
“Sema Anne, sema usiogope unataka nikufanye nini? Kwani maisha yako hivi sasa yapo mikononi mwangu!” Aliuliza Jaji Mpoki, wakili Lydia Ishengoma alijua nini alichomaanisha Jaji Mpoki kwa kuuliza swali hilo kwani haikuwa kawaida yake kuuliza maswali wakati wa hukumu na ilipotokea akauliza swali hilo alikuwa ameingiwa na huruma na kulikuwa na uwezekano mkubwa wa kumwachia huru mshtakiwa.
Wakili Lydia alitegemea Anne angeomba msamaha na alijua wazi angeachiwa huru! Moyoni alijawa na furaha kupindukia alijua ushindi ulikuwa umewadia, hakutaka kabisa Anne ahukumiwe kifo kwa sababu aliua kwa kulazimishwa na mazingira.
“Mheshimiwa Jaji ninajua mimi ni muuaji na ninastahili kifo na siwezi kukataa ninakuruhusu unihukumu kifo nife lakini.....!” Anne alianza kuongea, mahakama nzima ilikuwa kimya kumsikiliza yeye, wakili Lydia alishangaa ni kwanini Anne alianza kujitetea kwa kauli hiyo lakini moyoni mwake alijua ingebadilika.
Baadaye Anne aliendelea“.... ni kweli niliua lakini mheshimiwa Jaji naomba niseme maneno yafuatayo kwa watu waliokuwepo hapa mahakamani ili wapate kuelewa ni kwanini nifanya hivyo! Ni wengi wananyongwa na ni wengi wameua lakini kwa kweli hawakutakiwa kufanya hivyo, mimi si muuaji ila nililazimika kuua kwa sababu sikuwa na njia yoyote ya kuwalinda watoto wangu! Mama yangu aliyenizaa na kunileta duniani alitaka kuwaua wanangu ingawa tayari alikwishaua watoto wangu wengine wawili William na Henry”
Mahakama ilikuwa kimya watu wote wakisikiliza maneno ya Anne aliyoyaongea huku akilia.
“Nilipokataa kumpa watoto wangu alinipiga na ugonjwa wa kupata hedhi kila siku na hivi mnavyoniona hapa niliposimama nguo zangu zote zimelowa na nimekuwa katika hali hii kwa muda wa miaka kumi na moja!”
Anne alieleza kila kitu na kila mtu mahakamani alishikwa na huzuni wengi walinong’ona taratibu wakidai hata wao wasingeweza kuvumilia mateso aliyofanyiwa Anne! Wengi walimwaga machozi na hata Jaji mwenyewe alishindwa kujizuia na kujikuta akilia mbele za watu.
“Nimemaliza mheshimiwa naomba unihukumu kifo ili ninyongwe nimfuate huko mama huko aliko na nikimkuta ni lazima nimuue tena kwa sababu amenitesa sana na mara kwa mara najiuliza ni kwanini alinizaa!” Alimaliza Anne huku akilia.
Watu wote walikaa kimya kumsubiri Jaji Mpoki atoe hukumu yake, walipomwangalia alikuwa akijifuta machozi kwa kitambaa chake na alipomaliza kufanya hivyo alimwangalia Anne kwa huruma.
“Uta....kwenda jela mia...ka mitano!” Jaji Mpoki alijikuta akitoa hukumu ambayo hakuna mtu mahakamani aliitegemea na maaskari walimuongoza Anne kumtoa mahakamani, aliondoka huku akilia na alisindikizwa na vilio vya watoto wake.
“Msiwe na wasiwasi muda si mrefu nitakuwa pamoja na nyinyi watoto wangu!” Anne aliwaaambia watoto wake kabla hajatolewa ndani ya mahakama.
Wakili Lydia aliruka na kushangilia kwa furaha alijua miaka mitano haikuwa mingi na ilikuwa bora kuliko kunyongwa, aliwakumbatia Patrick na Nancy pamoja na mama yao mdogo, kila mtu alikuwa na furaha.
“Masikini kumbe msichana huyu ameteseka kiasi hiki?”
“Aisee kwa aliyofanyiwa alikuwa na haki ya kuua!” Walisikika wakiongea watu waliotoka mahakamani.
Wakili Lydia,Patrick, Nancy na mama yao mdogo walisimama nje ya mahakama wakisubiri Anne atolewe na kupakiwa ndani ya gari kwa safari ya kwenda gerezani, machozi yalishapungua usoni na nyuso zao zilionyesha furaha.
“Mnasoma?” Wakili aliuliza.
“Ndiyo!” Patrick na Nancy waliitikia.
“Darasa la ngapi?”
“Darasa la sita!”
“Mlishika nafasi ya ngapi darasani?”
“Mimi nilishika nafasi ya pili dada yangu akashika nafasi ya kwanza!”
“Ah! Hongereni sana, wewe unataka kuwa nani ukiwa mkubwa?” Wakili alimuuliza Patrick.
“Ninataka kuwa Mchungaji! Lakini dada yangu anapenda kuwa mwanasheria!”
“Kweli?” Wakili alimuuliza Nancy
“Ndiyo mama!”
Walikaa mahakamani mpaka saa saba mchana mahakama ilipokwisha na walishuhudia Anne akitolewa mahabusu na kupakiwa ndani ya lori kubwa lililokuwa maalum kwa ajili ya kubeba mahabusu kuwarudisha gerezani.
Alikuwa amekonda sana na nguo kama sketi aliyovaa ilionekana kulowa kwa damu! Inzi wengi walimfuata, Patrick na Nancy waliumia mioyo yao kumwona mama yao katika hali hiyo na walitamani mambo yangekuwa tofauti.
Pia mambo waliyoyasikia mahakamani siku hiyo yaliwaumiza moyo, waliumia kujua mama yao aliua lakini walifarijika kujua aliua kwa sababu ya kuwatetea wao! Huo ulikuwa upendo mkubwa mno kwa mama kuuonyesha, mama yao alikuwa amekubali kuteseka gerezani kwa sababu yao! Jambo hilo liliwafurahisha sana.
“Tutaoanana watoto wangu! Miaka mitano si mingi kama nitabaki gereza la hapa Butimba tafadhali mje kunitembelea mara kwa mara lakini kama nikihamishwa basi tutaonana Mungu akipenda!”
“Sawa mama, tunakupenda mama!”
“Mchungaji Aaron na mkewe wako wapi? Na wewe Suzzane umekuja lini?”
Alipouliza swali hilo Patrick na Nancy walianza kulia machozi tena.

Je nini kitaendelea?
Je Anne ataweza kushinda kesi hiyo?
 
SEHEMU YA 17


Miezi sita kabla ya hukumu hiyo mchungaji Aaron na mkewe walipata uhamisho kwenda nchini Kenya katika jiji la Nairobi ambako mchungaji Aaron alitegemea kuongezea elimu zaidi ya mambo ya dini, alitakiwa kusoma Digrii ya kwanza ya Teolojia katika chuo kikuu cha Nairobi Theological University
Yalikuwa ni masomo ya miaka mitatu kamili, yeye na mke wake walisikitika sana kuwaacha Patrick na Nancy ambao tayari walishaanza kuwahesabu ni watoto wao, lakini kikubwa kilichowaumiza zaidi kilikuwa ni Anne aliyekuwa gerezani, hawakujua wangemwona tena lini kwani waliamini angehukumiwa kifo na si ajabu kunyongwa bila wao kuwepo.
Taarifa za kwenda Nairobi zilikuja ghafla mno kiasi kwamba hawakupata kabisa nafasi ya kwenda gerezani kumuaga Anne! Kitu kikubwa walichokifanya ni kumtafuta Suzanne, msichana aliyekwenda nyumbani kwao mara kwa mara kuwaona Patrick na Nancy, akidai walikuwa ni watoto wa dada yake yaani yeye na Anne walikuwa watoto wa baba mkubwa na mdogo.
Suzanne aliwaeleza kuwa alikuwa ameolewa hapohapo mjini Mwanza maeneo ya Capripoint, iliwachukua siku kama tatu kumtafuta Suzanne kwa sababu hakuwahi kuwaachia namba yake ya simu, siku ya nne wakiwa wamekata tamaa kabisa wakifikiria kuwapeleka Patrick na Nancy Ustawi wa Jamii, walifanikiwa kumpata baada ya kumuulizia kwa jina la mume wake Anorld aliyekuwa mfanyabiashara maarufu mjini Mwanza.
Suzanne alikuwa ni miongoni mwa watu waliofanikiwa kimaisha kwani kulikuwa na nyumba kubwa na magari kadhaa ndani ya ngome yake! Nyumba yake ilipambwa vizuri na kila aina ya samani zilizofanya ivutie kupita kiasi. kifupi Suzanne na mumewe walikuwa na pesa!
Tatizo pekee alilokuwa nalo Suzanne ni bahati mbaya ya kutozaa watoto! Akiwa kidato cha tatu bahati alipata ujauzito uliotaka kuhatarisha maisha na masomo yake, ilibidi yeye na mvulana aliyempa mimba washirikiane kutafuta mitaani daktari wa kuitoa, kazi hiyo ilifanyika lakini bahati mbaya haikufanyika vizuri kwani mabaki mengine ya mimba hiyo ya miezi mitatu hayakutoka, yalibaki ndani ya mfuko wa uzazi hivyo kusababisha mfuko wa uzazi kuoza.
Ili kuokoa maisha ya Suzanne madaktari walilazimika kumfanyia operesheni na kuutoa mfuko wake wa uzazi uliooza! Suzanne akawa amepoteza uwezo wake wa kuzaa.
Kwa uzuri wa sura Suzanne alikuwa ni mwanamke mzuri wa kumvutia kila mtu aliyemwangalia, alipata bahati ya kusoma hadi chuo kikuu na kuhitimu digrii mbili za uchumi, elimu hiyo ilimwezesha kupata kazi nzuri sana katika shirika lililojishughulisha na uchimbaji wa visima kanda ya ziwa, Hesawa na Suzanne ndiye alikuwa bosi katika shirika hilo lililofadhiliwa na wazungu.
Ni kweli Suzanne na Anne walikuwa ndugu, baba zao walikuwa ni mtu na mdogo wake. Suzanne akiwa Mwanza alisikia habari za Anne na matatizo aliyoyapata, alisikitika sana kusikia alikuwa gerezani na alianza juhudi za kuwatafuta Patrick na Nancy ili aishi nao nyumbani kwake kwani alikuwa na kila kitu isipokuwa watoto!
Mchungaji Aaron na mkewe hawakuwa tayari kwa jambo hilo, sababu hata wao waliwapenda sana watoto hao hivyo walimkatalia Suzanne kuwachukua, lakini walipotakiwa kwenda kusoma Nairobi hawakuwa na chaguo jingine zaidi ya kumtafuta tena Suzanne ili awachukue watoto na kuishi nao.
“Ninakwenda kusoma kwa muda wa miaka mitatu!”
“Wapi?”
“Hapa jirani tu Kenya!”
“Aisee hongera sana!”
Suzanne alifurahi mno kukabidhiwa watoto, aliowatamani kuwa nao kila siku, kitu cha kwanza alichokifanya baada ya kuwachukua Patrick na Nancy ni kuwahamisha kutoka shule ya Nyakabungo waliyosoma na kuwapeleka shule ya kimataifa ya Green Garden iliyokuwa maarufu kwa watoto wa watu wenye uwezo, wakawa wanafuatwa asubuhi na gari la shule na kurudishwa nyumbani jioni na walipewa chakula cha kutumia na walinunuliwa nguo mpya!
Hata mume wake Suzanne nae pia aliwapenda sana Patrick na Nancy na alitamani wangekuwa watoto wake! Alilifahamu tatizo la mke wake kutokuwa na uwezo wa kuzaa mtoto lakini alimpenda Suzanne na hakuwa tayari kumwacha Suzanne kwa sababu hiyo.
Siku zote Anorld alitamani kuwa na mrithi wa mali zake na alimtamani sana Patrick, alitamani sana kuwa na mtoto kama yeye lakini alijua isingewezekana tena na hakutaka kabisa kuzaa nje ya ndoa yake, Anorld alikuwa mwanaume mwaminifu pengine kuliko wanaume wote mjini Mwanza ingawa alikuwa na mali nyingi.
Nyumbani kwa Suzanne Patrick na Nancy walipewa kila kitu na mwisho wa wiki ilikuwa ni lazima wapelekwe kisiwa cha Saa nane kuogelea! Maisha yalibadilika na kuwa ya raha, pamoja na hayo bado hawakumsahau mama yao kila siku walimfikiria na kabla ya kwenda kulala ilikuwa ni lazima wapige magoti na kumuombea.
Waliamini muda si mrefu mama yao angetoka gerezani na kuwachukua kwenda kuishi nao pamoja, walikuwa tayari kuacha kila kitu ili mradi wawe na mama yao hata kama wangetakiwa kulala chini na kulala bila kula kwao ilikuwa sawa kwa sababu walimpenda sana mama yao!
Watu wengine ambao Patrick na Nancy hawakuwa tayari kabisa kuwasahau walikuwa ni mchungaji Aaron na mkewe, waliokuwa tayari chuoni Nairobi, kila siku waliukumbuka wema wao na walimweleza hata Suzanne na mumewe jinsi familia hiyo ilivyompenda Mungu! Walijaribu pia kumshauri Suzanne na mumewe wamgeukia Mungu na kumtegemea yeye katika maisha yao.
*****
Mchungaji Aaron na mkewe wako wapi na wewe Suzanne umekuja lini?”
“Mimi dada? Mbona nipo hapa Mwanza muda mrefu tu shikamoo kwanza!”
“Marahaba! Kweli?”
“Ndiyo!”
“Na hawa watoto wangu ulikutana nao wapi na vipi na Mchungaji Aaron na mkewe wako wapi?”
“Mchungaji Aaron na mkewe hivi sasa hawapo wamekwenda Nairobi kimasomo, kabla ya kuondoka sababu nilishakwenda kwao kujitambulisha mimi ni nduguyo walikuja hapa kuniomba nikae na watoto mpaka utakapotoka gerezani,kwa hivi sasa ninao kwa miezi sita sasa, wanasoma vizuri na ninaishi nao kama watoto wa ndugu yangu!”
“Ahsante sana hivi sasa una watoto wangapi Suzanne?”
“Sijajaliwa bado!”
“Kweli?”
‘Ndiyo!”
“Usijali lakini! Watoto hutoka kwa Mungu!”
“Mbona una hali hii Anne? Mbona nguo zako zimelowa sana?” Aliuliza Suzanne akimwangalia Anne kwenye sketi yake aliyovaa.
“Ni mama!Ni mama aliyenifanyia kitu hiki kibaya kila siku ninapata hedhi, kwa muda wa miaka karibu kumi sasa!”
“Mungu wangu kweli? Ulishakwenda hospitali?”
“Ndiyo lakini siponi haya ni mambo ya Lutego, ili nipone ninahitaji kuombewa na mchungaji au mtumishi yeyote wa Mungu!”
“Usijali mama Ipo siku utapona tu na sisi pia tutaendelea kukuombea!” Nancy alimwambia mama yake.
“Suzanne nitunzie vizuri watoto wangu Mungu atakubariki!”
“Mama usiwe na wasiwasi anti ni mtu mzuri sana anatupatia kila kitu!” Patrick aliongea kabla Suzanne hajasema neno
“Nakushukuru sana Suz….!”Kabla Anne hajamaliza alivutwa kwa nyuma na kuanza kupelekwa moja kwa moja hadi kwenye gari la kupakia wafungwa kwenda mahabusu.
“Kwaherini mwanangu, ninawapenda sana ipo siku tu tutakuwa pamoja!”
“Hakuna shida tunakupenda mama na tunakuombea na tunasubiri urudi!”
Baadaye wote walilishuhudia gari likipakia wafungwa na mahabusu likaanza safari ya kuondoka mahakamani kwenda gerezani Butimba, Patrick na Nancy walibaki wakilia machozi kwa ajili ya mama yao, walimpenda sana Anne na walitaka sana kuwa naye maishani mwao!
Gari lilipopotea machoni pao, Suzanne alifungua mlango wa gari lake na Patrick na Nancy waliingia ndani safari ya kuelekea nyumbani ilianza!Njia nzima Patrick na Nancy walilia machozi wakilitaja jina la mama yao! Katika maisha yao hawakuwa na kumbukumbu za kuishi na mama yao kwani alipotiwa nguvuni walikuwa na umri wa miaka miwili.
*****
Jioni ya siku hiyo Patrick na Nancy wakiwa wamelala usingizi, maongezi mazito na ya hatari yaliendelea chumbani kwa Suzanne na mume wake maongezi ambayo hawakutaka kabisa watoto wayasikie.
“Najua unataka sana watoto Anorld lakini mimi uwezo wa kuzaa sina, unataka sana mrithi wa mali zetu lakini sina la kufanya kusaidia!”
“Sasa tutafanya nini mke wangu? Natamani kuwa na mtoto kama Patrick ili angalau nikifa aweze kurithi mali zetu!”
“Lakini si Patrick yupo hapa na dada yake pia, hawa wanaweza kuwa watoto wetu au unaonaje?”
“Mama yao je? Mimi nataka watoto wangu mwenyewe!”
“Sasa tutawapate wapi?”
Suala la watoto lilimsumbua sana Anorld, siku zote alikuwa mtu mwenye mawazo juu ya jambo hilo na alishindwa angelitatua vipi! Mara nyingi alimshawashi mke wake Suzanne angalau wanunue mtoto wa wizi na kujifanya ni wao lakini Suzanne aliukataa mpango huo.
Usiku huo walivutana sana juu ya suala la watoto mpaka wakafikia mahali wakashindwa kuelewana, baada ya majadiliano walifikia uamuzi wa kuwachukua Patrick na Nancy moja kwa moja wawe kama watoto wao wa kuzaa.
“Nauliza mama yao je?”Anorld aliuliza tena.
“Mama yao pamoja na kuwa ni ndugu yangu,furaha katika ndoa yetu ni watoto, hivyo hakuna njia nyingine zaidi kama unakubali tuhakikishe Anne anafia huko huko gerezani, hatoki na haonani na watoto wake tena sisi ndio tutakuwa wazazi wao!”
“Tutalifanyaje hilo?”
“Tutamuua huko huko gerezani!”
“Tutawezaje kumuua mtu gerezani na ulinzi wote ulipo kule?”
Wote wawili walikaa kimya kwa muda wakijaribu kutafakari ni kipi kingefanyika ili kuhakikisha Anne anakufa gerezani, na Suzanne na Anorld wanawachukua watoto wake, Suzanne alikuwa ndugu kabisa wa Anne lakini alikuwa ameamua kumuua ndugu yake ili amnyang’anye watoto wake wazuri waliompenda.
“Hilo la tutamuuaje hebu tuliache kwanza tulale kesho tutakuwa tumeshalifikiria vizuri!”
*****
Asubuhi kulipokucha Suzanne aliwaamsha watoto na kuwatayarisha kwa kwenda shule, hiyo ndiyo ilikuwa kawaida yake kila siku, hakuonyesha dalili yoyote ya maongezi yaliyofanyika kati yake na mumewe usiku, alikuwa na furaha na mapenzi kwa Patrick na Nancy kama kawaida na alizidi kuwatamani watoto wale maradufu.
“Nimeshajua cha kufanya Anne atakufa kirahisi sana, tutatafuta msichana yeyote mteja wa madawa ya kulevya, tutampa pesa ili afanye kosa lolote na afungwe akiwa gerezani tutamwambia amtafute Anne mpaka ampate, akishampata tutampa sindano ya sumu ya ‘Heart stopper’amchome usiku akiwa amelala na kufa, hakuna mtu atakayegundua!”
Aliwaza Suzanne bila kujali mtu aliyekuwa akipanga kumuua alikuwa ndugu yake kabisa.
“Mimi sijali ni lazima afe na Anorld akija jioni nitamweleza mpango wangu!” Aliendelea kuwaza Suzanne.
Jioni mumewe aliporudi kutoka kazini watoto wakiwa wamelala Suzanne alimweleza mpango wake aliokuwa ameupanga, Anorld alicheka sana.
“Mbona unacheka?”
“Nimeamini kweli wewe ni komandoo!”
“Kwanini?”
“Una mawazo kama yangu!”
“Na wewe ulikuwa unawaza hivyo?”
“Ndiyo na tayari nimeshampata msichana wa kufanya hiyo kazi, anaitwa Zena atafanya vurugu yoyote ile leo na akitiwa ndani tutapigiwa simu!”
“Kweli?” Suzanne alieleza bila huruma.
“Wewe subiri alisema baada ya vurugu zake kwenye ukumbi wa disko wa Deluxe kesho lazima atapelekwa polisi, atatupigia simu!”
Waliongea mengi juu ya Patrick na Nancy lakini baadaye walipitiwa na usingizi na kulala fofofo! Walizinduka saa 12 asubuhi kengele ya simu pembeni mwa kitanda chao ilipoita, Anorld alinyoosha mkono akainyanyua na kuiweka sikioni.
“Ndiyo! Anorld hapa, nani mwenzangu?”
“Mh! Kituo cha polisi kati hapa?”
“Kuna nini tena ndugu yangu?”
“Kuna dada mmoja kakamatwa baada ya kupigana na polisi na kumchania shati lake Deluxe!”
“Haya nakuja sasa hivi!” Alijibu Anorld alishafahamu msichana huyo ni nani na ni kwanini alikuwa akiitwa kituoni!
“Suzanne! Suzanne! Suzanne!” Alimwita mkewe aliyeonekana kuwa katikati ya usingizi mzito.
“Vi...pi?”
“Tayari! Kazi imekwishaanza kutekelezeka!”
“Kweli?Umejuaje?”
“Nimepigiwa simu sasa hivi na polisi amka twende!”
Wote wawili walijiandaa na kutoka nje ambako walichukua gari na kukimbia haraka hadi kituoni ambako walipata nafasi ya kuongea na Zena!
“Naingia kazini hiyo milioni yangu niikute!”
“Usiwe na wasiwasi tutakuwa tumekuja kukutembelea gerezani kila Jumapili, ukishampata tu utuambie tutatumia ujanja wetu wote kukuletea hiyo sindano ya kumchoma nayo! Sawa?”
“Hakuna tatizo kabisa kaka Anorld kazi nitaifanya vizuri na kwa uangalifu!” Zena aliwaondolea wasiwasi.
Baadaye waliondoka haraka kurudi nyumbani kwenda kuwatayarisha Patrick na Nancy kwenda shule! Watoto hawakuwa na habari kabisa juu ya mpango uliokuwa unaendelea juu ya kumuua mama yao! Walijua kila kitu kiliendelea vizuri.
“Anti lini tutakwenda kumuona mama gerezani?”
“Jumapili!” Alijibu Suzanne akijua ni siku hiyo ndiyo yeye na mumewe wangekwenda kumwona Zena gerezani Butimba!
“Kweli?”
“Ndiyo!”
Gari la shule lilipokuja liliwachukua watoto na kuwapeleka shuleni, Suzanne na mumewe nao muda mfupi baadaye waliondoka kwenda kazini kwao.
****
Kijua kilikuwa kikichoma hali ya Mwanza siku hiyo ya Jumapili ilikuwa ya joto kidogo, ilikuwa rahisi kuifanananisha na Morogoro, siku hiyo Anorld, Suzanne, Patrick na Nancy waliondoka kuelekea gerezani Butimba ndani ya gari dogo la Anorld aina ya Cadillac! Watoto waliamini walikuwa wakienda gerezani kumwona mama yao kumbe Anorld na mkewe walikuwa na mpango tofauti kabisa vichwani mwao, walikuwa wakienda kumwona Zena na kumuuliza kama alifanikiwa kumpata Anne gerezani ili wakamilishe mpango wa kumuua.
Kitu cha kwanza kilichofanyika baada ya kufika gerezani Butimba kilichowashangaza pia watoto ni kuitwa kwa mwanamke mwingine badala ya mama yao ambaye hawakumtambua na Anorld kwenda kuongea naye pembeni kwa muda mrefu!
“Anti mbona mama humwiti? Muda wa kuona ndugu si utakwisha?” Patrick alimuuliza Suzanne lakini hakujibiwa kitu.
****
“Vipi Zena umefanikiwa kumpata?” Anorld alimuuliza Zena!
“Hapana tangu niingie hapa nimemtafuta lakini sijampata , nimejaribu hata kuulizia jina lake lakini sijampata si anaitwa Anne?”
“Aisee, basi subiri hapahapa kwani mwanamke atakayetoka sasa hivi kuongea na sisi ndiye huyo! Akija nitakuita nikutambulishe nikidai wewe ni dada yangu ili iwe rahisi wewe kuzoeana naye! Sitaongea na wewe tena ila Jumapili ijayo nitakuletea sindano ya sumu ndani ya ugali ambao hutatakiwa kuula kabisa! Cha kufanya kuanzia leo jaribu kumzoea sana ili nikileta sindano ukamilishe kazi!”
“Hiyo wewe usijali nionyeshe kwanza huyo marehemu mtarajiwa mwenyewe! Alisema Zena aliyeonyesha sura ya mtumiaji halisi wa madawa ya kulevya na pombe kali!”
Anorld aliondoka na kujiunga tena na familia yake, akamwacha Zena akiwa amesimama peke yake akisubiri kutambulishwa kwa Anne!’
“Anko mbona mama hatoki?”
“Subirini nilikuwa nasalimiana na anti yenu mwingine!”
“Mbona na sisi hatusalimiani nae?” Watoto walizidi kudadisi.
“Atakuja sasa hivi!” Alisema Anorld na kuondoka kwenda kuandikisha jina la Anne ili wamwone, haikuchukua muda Anne akatoka, watoto wake walimkimbilia na kumkumbatia kwa furaha! Kama ilivyokuwa kawaida yake Inzi wengi walikuwa nyuma yake na harufu mbaya ilisikika mara tu alipofika baadhi ya watu walianza kuhama eneo hilo!
Nguo zake zote zililowa na kugandamana na damu! Anne alisikitisha, pamoja na hali hiyo watoto wake hawakudiriki kumwacha walimkumbatia mpaka wakaangushana naye chini! Watu wote walishangaa na Anne alicheka kwa mara ya kwanza baada ya muda mrefu!
Hali ilipotulia waliketi chini na kusalimiana, Anne aliendelea kumshukuru sana Suzanne kwa wema aliokuwa akimfanyia kwa kuwalea watoto wake waliongea pia mengi juu ya maisha katika siku zilizopita kati yao!
“Huyu ndiye shemeji yako anaitwa Anorld ni mfanyabiashara hapa mjini!”
“Aisee nafurahi kukufahamu shemeji, huyu ni ndugu yangu kabisa ishi naye vizuri!”
“Hakuna tatizo shemeji pole na matatizo yaliyokupata!”
“Ulisema hujabarikiwa mtoto?” Anne aliuliza tena.
“Bado lakini Patrick na Nancy wanatufariji sana, tunajisikia vizuri kuishi nao nyumbani kwetu na tunasubiri umalize muda wako ili tuungane wote nyumbani kwetu!”
“Ahsanteni sana na kwa sababu kifungo kinahesabiwa usiku na mchana siku mbili tofauti nitakaa hapa kama miaka mitatu hivi!”
“Siyo muda mrefu utatoka tu!” Patrick alimwambia mama yake, Anne alishangazwa na busara iliyokuwemo ndani ya mtoto wake! Alikuwa ni marehemu mume wake tupu.
Waliongea kwa karibu saa nzima, wakamkabidhi zawadi walizomletea na kuondoka zao, Patrick na Nancy walisikitika kumwacha mama yao tena, lakini hivyo ndiyo ilivyokuwa.
****
Jumapili iliyofuata Anorld alinunua chupa ya sumu ya ‘heart stopper’ sumu kali ya kusimamisha moyo, aliinyonya na kuiweka ndani ya bomba la sindano, mkewe alipiga ugali mzuri na sindano hiyo ikazamishwa katikati ya ugali huo uliopozwa ili kuzuia bomba lisiyeyuke!
Anorld aliwasha gari na kwenda moja kwa moja hadi gerezani ambako alifanya mpango getini na kutoa kitu kidogo kwa maaskari akamkabidhi Zena chakula kile bila kukaguliwa.
“Humo ndani ndiyo ipo hiyo sindano baada ya kumchoma nayo, atakauka! Hapohapo usichelewe kimbia chooni ulitupe bomba la sindano! Si tayari mmeshazoeana?”
“Tayari na tunalala pamoja!”
“Fanya kweli basi!”
“Usiwe na wasiwasi tayarisha pesa yangu tu!”

Je nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 18


“Utajiri bila watoto ni hasara, kumbe basi kipi bora? Watoto au mali?” Hilo ndilo swali alililojiuliza Anorld kila siku kichwani mwake! Alikuwa na kila kitu, mke mzuri mwenye mguu wa kuvutia, mwanya, rangi nzuri ya ngozi alikuwa mzuri pengine kuliko wanawake wote duniani.
Anorld alipata kila starehe iliyopo chini ya jua, kila mwaka wakati wa sikukuu za Krismasi ilikuwa ni lazima yeye na mke wake waende Canada kupumzika na kurudi mwanzoni mwa mwaka mpya! Kwao safari za visiwa kama Shelisheli, Comoro, Zanzibar kwenda kupumzika lilikuwa jambo dogo na la kawaida! Waliweza kufanya hivyo mara tano au sita kwa mwaka! Pesa ilikuwepo kilichotakiwa ni namna gani itumike.
Kifupi Suzanne na mume wake walikuwa na kila kitu kasoro kitu kimoja tu! Nacho ni mtoto, Suzanne kutokuwa na uwezo wa kuzaa ndio kuliwafanya wakose raha kidogo ya maisha katika ndoa yao pamoja na kuwa na kila kitu!
Mrithi wa mali ndiye alikuwa tatizo sababu wote walifahamu ilikuwa ni lazima siku moja wafe! Nani angebaki mrithi wa mali yao? Hilo ndilo swali liliwaumiza vichwa vyao kila siku, hivyo kuja kwa Patrick na Nancy katika maisha yao kulionekana kutoa jibu la tatizo hilo!
uzuri wa watoto hao uliwachanganya sana akili Suzanne na Anorld, Patrick na Nancy walikuwa watoto wazuri mno na hiyo ilitokana na mchanganyiko wa damu ya marehemu baba yao Huggins, walitamani watoto wale wawe wao! Roho ya dhuluma ilishawaingia mioyoni mwao, dhuluma ya watoto, viumbe hai, binadamu! Ilikuwa ni dhuluma kubwa lakini Suzanne na Anorld walikuwa wamedhamiria kuifanya bila uoga.
Ilikuwa si rahisi kuwapata watoto hao kama mama yao angetoka gerezani baada ya miaka mitano! Hivyo ili wawapate njia pekee ilikuwa ni kumwondoa Anne duniani akiwa hukohuko gerezani, walifahamu pengine baada ya Anne kufa wazazi wa marehemu Huggins au ndugu zake wengine wangeweza kujitokeza na kudai kuwachukua watoto, ni hilo pekee ndilo liliwatia hofu lakini walijua jinsi ya kulishughulikia.
“Pesa haishindwi kitu ni lazima watoto hawa wawe wetu, isitoshe sisi ni kama tumewasaidia katika maisha ni watoto wenye bahati kubwa sana hawa! Utajiri wote huu tuwaachie?’ Aliongea Anorld kwa uchungu!”
“Kwa kweli tumewasaidia!” Suzanne aliitikia.
Wakati maongezi hayo yakiendelea chumbani kwao Suzanne na Anorld waliaamini kabisa kuwa Patrick na Nancy walikuwa wamelala usingizi! Haikuwa hivyo kwani Patrick alikuwa macho akiendelea kumlilia mama yake, aliyoyaona gerezani siku hiyo yalimtia simanzi kubwa sana moyoni mwake.
Hali ya mama yake ilivyokuwa, alivyotoa harufu, alivyofuatwa na Inzi wengi kila alikokwenda, alivyokonda ilimuumiza sana moyo na kumfanya akose kabisa usingizi!Dada yake Nancy alikuwa tayari usingizini lakini Patrick hakupata hata lepe la usingizi mawazo yalikuwa mengi mno kichwani mwake, alishindwa kuelewa ingekuwaje siku ambayo mama yake angetoka gerezani. Aliamini hiyo ndiyo ingekuwa siku ya furaha kuliko zote maishani mwake.
Ghafla akiwa katika mawazo hayo alisikia maneno kutoka katika chumba cha Suzanne na Anorld hakuyaamini masikio yake ikabidi asikilize tena kwa makini zaidi lakini maongezi yaliendelea kubaki yaleyale!
“Watoto hawa watakuwa wetu tu! Si Anne anakufa usiku huuhuu! Ile sindano atakayochomwa itamkausha kama samaki!”
“Masikini Anne lakini inaniuma sana ndugu yangu kufa! Sina jinsi ya kuzuia hili lisitokee kwa sababu ninawataka sana Patrick na Nancy!”
Moyo wa Patrick uliruka mapigo mawili mfululizo, alisikia kama moyo wake unataka kusimama kufanya kazi.
“Ha! Mama yangu anakufa? Anakufa kwa nini?” Alijiuliza Patrick na kumwamsha dada yake aliyekuwa amelala fofofo!’
“Nancy!Nancy!Nancy! Tafadhali amka upesi!” Aliongea taratibu huku akimtingisha dada yake.
“Nini tena Patrick?”
“Amka usikilize wanavyoongea anko na anti Suzanne!’
“Wanaongea kitu gani?”
“Wasikilize tu!” Patrick alimwambia dada yake.
Wote wawili walisimama na kusogea dirishani na kuanza kusikiliza jinsi Anord na Suzanne walivyokuwa wakirufahia kifo cha Anne usiku huo, kifo cha sindano ya sumu aina ya Heartstopper ambayo Anne angechomwa na Zena usiku huo gerezani.
Wote wawili walimkumbuka dada zena waliyemwana gerezani siku hiyo, Nancy alishindwa kujizuia na kuanza kulia machozi tena kwa sauti ya juu, sauti hiyo iliwafikia Anorld na Nancy chumbani kwao na kutoka mbio kukimbilia chumbani kwa akina Nancy.
“Usithubutu kuwaonyesha kuwa tumeyasikia maongezi yao umenisikia?”Patrick alimwambia dada yake kabla hajafungua mlango kuruhusu Anorld na Suzanne waingie ndani.
“Vipi watoto wangu?” Suzanne aliuliza.
“Hakuna kitu ni Nancy alikuwa anaota ndoto ya kutisha!” Patrick alijibu wakati dada yake akiwa amelala kitandani na kujifunika na shuka hadi kichwani.
“Nancy!Nancy!Nancy! Vipi mwanangu?”
‘Mh!Mh!” Nancy aliguna na kuendelea kulia machozi chini ya shuka hakutaka kujifunua, alitii alichoambiwa na kaka yake. Baadaye Anorld na Suzanne waliondoka kurejea chumbani kwao ambako waliingia kitandani na kulala.
“Sijui wamesikia maongezi yetu hawa?” Anorld aliuliza.
“Ah! Wapi, haiwezekani!”
****
Nancy na Patrick hawakulala tena, waliendelea kulia wakimlilia mama yao! Walijua mama yao angekufa usiku huohuo kwa kuchomwa na sindano ya sumu, walijua wasingekuwa na mama tena duniani kuanzia asubuhi iliyofuata, walikuwa yatima tayari, walipoamka macho yao yalikuwa yamevimbiana kwa sababu ya kulia. Siku hiyo hawakujiweka tayari kwa shule kama ilivyokuwa kawaida yao jambo lililowapa Anorld na Suzanne wasiwasi kidogo.
“Mbona macho yenu yamevimba kiasi hiki?”
“Sababu ya kulia!”
“Kwanini mlie sana watoto wangu wazuri?”
“Kumbukumbu ya jana, mama alituumiza sana moyo!” Alijibu Patrick.
“Vaeni basi mwende shule sasa hivi au?”
“Mimi sijisikii hata kidogo kwenda shule anti, labda Nancy ajiandae!” Alijibu tena Patrick.
Nancy alipoulizwa naye alikataa walishapanga kutokwenda shule siku hiyo,walitaka kutoroka kwenda gerezani kuangalia kama kweli mama yao alikuwa amekufa.
“Haya chukueni hii pesa mtanununua soda mnywe sawa? Sisi tunakwenda kazini!” Alisema Suzanne na kuwakabidhi Patrick na Nancy noti ya shilingi 500.
“Ahsante anti!’ Aliitikia Nancy baada ya kuipokea noti hiyo mkononi mwake.
Suzanne na Anorld waliingia ndani ya gari na kuondoka kwenda kazini, nyuma Patrick na Nancy hawakutaka hata kupoteza dakika moja walichofanya ni kuvaa viatu na kuchomoka hadi nje ambako kabla ya kutoka mlinzi aliwauliza walikuwa wakienda wapi.
“Tunakwenda dukani kununua miswaki!”
“Ok! Nendeni basi lakini msichelewe kurudi!”
“Sawa babu!” Patrick aliitikia.
Walipofika nje walitembea hadi kituo cha daladala cha Nera ambako walipanda basi lililowapeleka hadi kitu cha mabasi ya kwenda Butimba karibu na kampuni ya Kauma, asubuhi hiyo walikuta basi moja likiwa limeegeshwa kituoni, wao ndio walikuwa abiria wa kwanza kupanda basi hilo na kusubiri abiria wengine walioanza kuingia mmoja baada ya mwingine mpaka likajaa na kuanza kuondoka.
Njiani Patrick na Nancy waliendelea kulia machozi wakimlilia mama yao, waliamini kabisa kuwa tayari Anne alikuwa maiti! Kwa maongezi waliyoyasikia kutoka chumbani kwa suzanne na Anorld ilikuwa si rahi si kuamini kuwa mama yao angekuwa hai.
“Sindano ya sumu! Yaani wamemuua mama yetu kwa sindano ya sumu? Huu ni unyama, kama walitutaka sisi ni kwanini wasingeongea tu na mama badala ya kumuua?’ Kwani mama angekataa kusema watuchukue, wakati hata uwezo wa kututunza kama mama angetoka gerezani hangekuwa nao?” Aliendelea kuwaza Patrick.
Watu wote ndani ya basi walishangazwa na kitendo cha watoto hao wawili kuendelea kulia , mzee mmoja alitaka kufahamu nini kilikuwa chanzo.
“watoto mbona mnalia tangu tuondoke kituoni?’
“Mama yetu amekufa!”
“Amekufa wapi?”
“Gerezani Butimba?’
“Nani amewapa taarifa hizo?”
Patrick na Nancy walishindwa kujibu swali hilo na kujikuta wakiendelea kulia machozi tu.
“Nielezeni basi?”Mzee yule aliendelea kuwabembeleza waseme lakini hawakufanya hivyo!
Gari lilipofika gerezani Butimba Patrick na Nancy waliteremka na kunyoosha hadi gerezani lengo lao likiwa ni kufahamu kama kweli mama yao alikuwa amekufa au la! Watu wa kwanzakukutana nao walikuwa ni maaskari walinzi wa gereza.
“Nyie watoto mnakwenda wapi asubuhi hii?’
“Tumekuja kumwona mama yetu!”
“Mama yenu nani?”
“Anne!”
“Ni mfungwa wa mahabusu!”
“Amefungwa miaka mitano!”
“Leo siyo siku ya kuona wafungwa, njooni jumamosi au Jumapili siyo leo mnasikia?”
“Hapana tunataka kumwona mama yetu, tunataka kujua yupo hai au amekufa!”
“Kwani mmeambiwa amekufa?”
“Ndiyo tunafahamu amechomwa sindano ya sumu!”
“Sindano ya sumu nani kamchoma?”
“Mfungwa mwenzake anaitwa Zena! ”
“Nyie watoto mbona siwaelewi, mnaongea jambo kubwa sana hilo hebu jaribuni kunieleza vizuri!” Askari huyo aliwachukua na kuwapeleka pembeni ambako walianza kumsimulia kila kitu kilichotokea na jinsi walivyosikia sauti ya Suzanne na Anorld wakiongea, pia jinsi sindano hiyo ilivyoingizwa gerezani ndani ya ugali.
“Mh! Jambo hilo linawezekana kweli?” Alihoji askari wakati bado akijaribu kutafakari jambo hilo lango la gereza lilifunguliwa na maiti ya mtu ikiwa imefungwa ndani ya shuka jeupe ilipitishwa mbele yao na kupakiwa ndani ya gari.
“Haya maafande waliochanguliwa kwenda kuzika maiti hii pandeni haraka ndani ya gari tuondoke!” aliamuru askari magereza mmoja mwenye V tatu begani. Maaskari kama kumi hivi walipanda ndani ya garini haraka tayari kwa kuondoka.
Tayari Patrick na Nancy walikuwa na uhakika kabisa kuwa maiti iliyopakiwa ndani ya gari ilikuwa ni mama yao,walianguka chini na kuanza kulia machozi, wakiliita jina la mama yao na kuwatupia lawama Suzanne na Anorld kwa kitendo chao cha kinyama!
Kelele hizo ziliwafanya maaskari wangine zaidi washtuke na kulazimika kuwafuata Patrick na Nancy na kuwadadisi zaidi, maelezo yao yalitosha kuwafanya maaskari waamini kweli aliyekufa alikuwa ni mama yao.
“Wapandisheni ndani ya gari wakalione kaburi la mama yao ili kama wakitaka kuwapeleka ndugu zao wawapeleke baadaye!” Alisema dereva.
Patrick na Nancy walipandishwa ndani ya gari na safari ya kwenda eneo la Mkolani nje kidogo ya mji wa Mwanza kwa mazishi ilianza, njia nzima waliendelea kulia, katika maisha yao hawakuwahi kuishi na mama yao kwa muda mrefu lakini walimpenda na alikuwa kila kitu kwao.
Walimtegemea baada ya miaka michache tu baadaye angekuwa huru pamoja nao lakini sasa maisha ya kipenzi chao yalikuwa yamekatishwa kinyama na Anorld na Suzanne sababu tu ya kutaka kumdhulumu watoto alizaa mwenyewe!
“Huu ni ukatili na Mungu atawalipia anti na anko!” Nancy alisema kwa uchungu.
“Na sitaki tena kurudi nyumbani kwao ninakwenda mwenyewe nitakako! Nitakuwa hata chokoraa lakini sipo tayari kurudi kwao tena wauaji wakubwa wale!” Alifoka Patrick.
Walipofika makaburini shimo lilishachimbwa tayari na bila hata kuruhusiwa kutoa heshima zao za mwisho au kuiona sura ya mama yao kwa mara ya mwisho, maiti ilitupwa shimoni na kuanguka kama mzigo! Shimo likaanza kufukiwa na udongo, Patrick na dada yake walilia hadi sauti zao kukauka lakini hawakuubadili ukweli kuwa mama yao alikuwa amekufa.
Baada ya mazishi walipakiwa ndani ya gari na safari ya kurudi gerezani ilianza tena ambako waliachiwa na kuingia mitaani, hawakurudi tena nyumbani kwa Anorld na Suzanne kama walivyokuwa wameamua, waliwaona ni wauaji ambao wangeweza kuwachinja hata wao wenyewe.
****
Jioni ya siku hiyo Suzanne aliwahi kurudi kutoka kazini kabla ya Anorld na dakika kama ishirini tu tangu aingie ndani ya nyumba yake, maaskari watatu walibisha hodi mlangoni aliwakaribisha sebuleni lakini hawakukakaa sana kabla hawajamwambia shida yao.
“Mama sisi ni maafisa wa polisi na hivi tunavyoongea na wewe upo chini ya ulinzi unahitajika kituoni mara moja!”
“Nimefanya nini?” Aliuliza Suzanne.
“utaelezwa hukohuko, mumeo yupo wapi?”
“Yupo kazini bado hajarudi!”
“Tutamfuata baadaye!”
“Labda nimjulishe arudi upesi?”
“Hapana!” Alijibu askari mmoja na kumpiga pingu za mikononi Suzanne akaanza kusukumwa kumtoa nje ya nyumba yake!
Alipelekwa moja kwa moja hadi kituo cha polisi ambako alifahamishwa wazi kuwa yeye na mumewe walikuwa wakituhumiwa kuingiza sumu gerezani na kusababisha kifo cha mfungwa mmoja!
Ndugu na marafiki waliofika baadaye polisi kutaka kujua sababu ya kukamatwa kwa Suzanne waliporudi majumbani kwao walimpigia simu Anorld ambaye alishapata taarifa na kujificha eneo la Nyamanoro kwa rafiki yake na kumjulisha sababu ya kukamatwa kwa mkewe na sababu iliyopelekea hilo!
“Nendeni kwanza mkaangalie nyumbani kama wale watoto wapo?” Anorld alishauri.
“Sawa!” Alijibu Jesca dada yake Anorld na bila kuchelewa alichukua gari la mama yake na kwenda nalo moja kwa moja hadi nyumbani kwa Anorld.
Alipofika nyumbani kwa kaka yake ilikuwa tayari yapata saa sita na nusu ya usiku na kukutana na mlinzi wa nyumba hiyo.
“Vipi babu akina Patrick na Nancy wamerudi?”
“Hata mimi nashangaa sijui wapo wapi siyo kawaida yao hata siku moja kukaa nje hadi saa hizi za usiku, sijui nao wamekamatwa?” Alihoji mlinzi.
“Hapana! Sijui mahali walipo! askari wamekuja tena?” Jesca aliuza.
“Nafikiri kila baada ya dakika kumi hivi wanafika na ninaona ni heri uondoke sababu wakikukuta hapa halafu itakuwa taabu!”
*****
Jesca aliondoka kurejea nyumbani ambako alimpigia tena simu Anorld na kumtaarifu hali halisi ilivyokuwa.
“Ninajua wazi hao ni Patrick na Nancy tu hakuna mwingine na nitawatafuta usiku huu huu hadi niwapate! Wamenichomea polisi watanitambua watoto hawa!” Alisema Anorld na baada ya kukata simu alimpigia msaidizi wake ambaye alitayarisha magari madogo kumi kwa ajili ya msako wa kuwatafuta watoto usiku huo.
“Je kama wamelala nyumbani kwa mtu?”
“Hawana ndugu yeyote hapa jijini na jua watakuwa wamelala sehemu fulani mitaani na ninafikiri maeneo ya hukohuko Butimba, mkikosa huko jaribuni kwenye makaburi ya Mkolani ambako wafungwa huzikwa kwa uchungu walionao ni lazima watakuwa wamelala juu ya kaburi la mama yao!”
*****
Usiku huohuo wa baridi kali huku manyunyu ya mvua yakidondoka, Patrick na Nancy walilala juu ya kaburi waliloamini ni la mama yao! Walikuwa bado wakimlilia mama yao kwa uchungu sana na kukilaani kitendo cha Suzanne na Anorld.
Hawakuwa na ufahamu wa jambo lolote lililoendelea mjini Mwanza kwa wakati huo, wala hawakuwa na hisia za kusakwa ili wauawe.
Patrick na Nancy wakiwa hawana hili wala lile mara ghafla walisikia muungurumo wa gari na kuona mwanga mkali wa taa za gari ukikatisha kutoka barabarani kuelekea makaburini kila mmoja wao alishtuka.
“Mh!nini tena? Lakini hawa wanaweza kuwa majambazi au watu wamekuja kufanya uchawi wao makaburini!”
“Sasa tufanye nini?” Nancy alimuuliza kaka yake wakati gari likizi kukaribia zaidi!
“Njooni huku tujifiche!” Patrick alisema huku akimvuta dada yake kuelekea Kwenye nyasi ndefu zilizokuwepo jirani yao wakiwa katika nyasi hizo walishuhudia gari likiegeshwa na watu watano kushuka, pamoja na kuwa giza walipojaribu kuziangalia sura za watu wale waliitambua sura ya mtu mmoja na hata sauti ilikuwa ya Anorld!Moyo wa Patrick ulilipuka, watu wote walikuwa na bunduki mikononi!
“Tafuteni kaburi la leo! Watakuwa wamelala hapohapo!” iliamrisha sauti ya Anorld.
Tochi zilimulika kila mahali hatimaye wakalifikia kaburi la siku hiyo.
“Hili hapa!” Alipiga kelele mtu mmoja!”
“Wapo?”
“Hawapo? Ila kuna miguu ya watoto hii hapa juu! Inavyoonekana walikuwa hapa muda si mrefu!”
“Inaeelekea wapi?”
“Porini!”
“Fuatilieni huko huko porini na mkivipata hivyo vitoto ueni kabisa ili kupoteza ushahidi, maana hivyo vitajidai vishahidi maana ndivyo vilisikia maneno yangu!” Aliamuru Anorld.
“Sawa bosi!”
****
mauaji yalivyotokea gerezani:
Usiku wa manane Anne akiwa amelala fofofo, Zena aliyekuwa pembeni yake alipohakikisha kuwa asingeweza kushtuka alinyanyuka na kwenda hadi chooni ambako alilificha sufuria lililokuwa na ugali darini, alilichukua na kushuka nalo hadi chini ambako alianza kuusambaza ugali na kulitoa bomba la sindano.
“Yes! Kazi imekamilika mwisho wa maisha yake umefika! NI lazima nimuue nikachukue pesa yangu” alisema Zena.
Aliliangalia bomba la sindano na kuona lilikuwa limejaa vizuri sumu ambayo ingeukausha mwili wa Anne kama alivyokuwa ameambiwa na Anorld.
“Mimi sijali kuondoa maisha ya mende kama Anne ili mradi nimepewa pesa!” Alinong’ona Zena.

Je nini kiliendelea?
Je Nancy na Patrick walipatikana?
 
SEHEMU YA 19


Kama ilivyo kawaida ya gereza lolote chakula huwa kidogo na mara nyingi hakifai wala hakiwezi kulinganishwa na chakula cha nyumbani na kwa kawaida wafungwa hula mara moja kwa siku, hivyo siku zote huwa ni watu wenye njaa!
Akiwa na bomba la sindano mkononi Zena alianza kupiga hatua kuelekea mahali alipolala Anne, alikuwa amedhamiria kuyakatisha maisha yake kwa sababu ya pesa! Hatua kama tano mbele aliikumbuka sufuria la ugali aliloliacha chini, aligeuka kuliangalia na kukuta liko palepale.
“Hili sufuria na ugali wake litaniletea taabu wacha nilirudishe kwanza darini ndiyo nije niendelee na kazi yangu!” Aliwaza Zena na kumwangalia Anne aliyekuwa amelala sakafuni akiendelea kukoroma taratibu.
Bila kuchelewa wala kusita Zena alikata kona akiwa na bomba lake mkononi kulifuata sufuria la ugali, alilibeba na kuanza kutembea kuelekea nalo chooni! Mbele kidogo hisia za ajabu zilimwijia, mate yakaanza kumdondoka! Alijisikia njaa ya ajabu, hakuwa kusikia njaa namna hiyo katika maisha yake, aliutamani ugali aliokuwa ameubeba na kujikuta akiyapuuzia maneno aliyoambiwa na Anorld kuwa asiutie mdomoni ugali huo.
Aliuangalia ugali ule na kuzidi kuutamani mdomo wake ulitaka sana aule lakini akili yake ilishindana sana na mawazo hayo. Zena alijikuta njia panda bila kujua la kufanya, ghafla alijikuta akiliweka bomba la sindano chini na pamoja na kuwepo harufu kali chooni alianza kuula ugali huo kwa juujuu bila kuingia ndani ambako bomba la sindano lilifukiwa kabla hajalitoa.
“Hata kama ni sumu huku juu haiwezi kuwa imefika ni lazima itakuwa humohumo ndani lilipokuwa bomba!” Alijipa moyo Zena na kuendelea kula ugali huo lakini dakika tano baadaye alianza kusikia kizunguzungu na baadaye macho yake yalianza kuona kiza, misuli ikaanza kukamaa na kubana kama ambavyo hutokea kwa mcheza mpira, maumivu ya misuli yalikuwa makali mno kabla hajaanza kulia alianguka chini na kupoteza fahamu hakujua tena kilichoendelea.
Saa kumi na moja alfajiri Anne alizinduka usingizini na kuanza kumwamsha mfungwa aliyelala jirani yake akidhani ni Zena.
“Mimi sio Zena!”
“Zena yuko wapi?”
“Aliondoka usiku wakati wewe umelala na hakurudi tena sijui yuko wapi?”
Kabla hawajaendelea sana na maongezi yao mara walisikia kelele za mtu kutoka chooni, wote wawili walishtuka wakanyanyuka na kukaa.
“Jamani!Jamani!Jamani! Mtu kafia chooni!” Alipiga kelele mtu huyo akikimbia kutoka chooni kwenda katika ukumbi waliolala wafungwa.
Baada ya kusikia kelele hiyo wafungwa wote walinyanyuka sakafuni walikokuwa wamelala na kuanza kumfuata mwanamke aliyekuwa akipiga kelele ili kumuuliza vizuri juu ya jambo alilokuwa akilisema.
“Yuko wapi huyo mtu aliyekufa?” Anne aliuliza hakuwa na wasiwasi kuwa mtu huyo angeweza kuwa Zena.
“Yupo chooni ingieni wenyewe mkaone!”
Anne aliongoza kundi la wafungwa kuingia ndani ya choo, hakuyaamini macho yake kukuta aliyenguka chini ni Zena!
Bomba la sindano na sufuria la ugali vikiwa pembeni mwake, hakuamini kama alikuwa amekufa palepale alipiga magoti chini na kuanza kumtingisha akimwita jina lakini Zena hakushtuka alipogusa moyo wake pia ulikuwa umesimama kabisa ni hapo ndipo alipoamini Zena alikuwa amekufa!
Kila mfungwa alihisi Zena alikuwa amejiua mwenyewe kwa kujichoma sindano ya madawa ya kulevya lakini walipoliangalia bomba la sindano lilikuwa limejaa dawa mpaka juu jambo lililoonyesha wazi kuwa alikuwa bado hajajichoma kwa sindano ile.
Anne aliangua kilio, alilia mpaka akaanguka chini na kuzimia! Ikabidi wafugwa wenzake wamtoe nje na kummwagia maji ndipo akazinduka tena, alikuwa akimlilia rafiki yake mpendwa Zena waliyekutana naye hapohapo gerezani.
Hakuwa na habari hata kidogo juu ya jambo ambalo Zena alipanga kumfanyia usiku wa siku hiyo, bila Zena kuula ugali ni lazima yeye Anne ndiye angekuwa marehemu wakati huo! Aliendelea kumlilia Zena mpaka mkuu wa gereza alipokuja na kuamuru mwili wa Zena uondolewe chooni na kupelekwa zahanati ambako ulihifadhiwa.
Pia ugali na bomba la sindano vilivyokutwa pembeni kwa Zena viliondolewa na kuhifadhiwa kwa uchunguzi asubuhi ya siku hiyo, kila mtu alichanganyikiwa na kifo cha Zena, mkuu wa gereza na daktari wa gereza walishindwa kuelewa ni dawa gani iliyokuwa ndani ya bomba la sindano alilokutwa nalo Zena na walishindwa kuelewa alilipata wapi akiwa kama mfungwa.
Kulipokucha asubuhi bomba la sindano pamoja na ugali vilichukuliwa na kupelekwa moja kwa moja hadi hospitali ya Bugando ambako vyote vilifanyiwa uchunguzi na kugundulika kuwa bomba la sindano pamoja na ugali vilikuwa na sumu aina ya ‘Heartstopper’ ambayo kazi yake ni kuusimamisha moyo kufanya kazi!
Kila mtu aliamini Zena alikuwa ameamua kujiua mwenyewe kwa sumu hiyo mbaya, hakuna mtu hata mmoja aliyehisi kuwa sumu ile iliingizwa gerezani kwa lengo la kumuua Anne na si Zena.
Nani aliingiza sumu ile gerezani ndilo lilibaki kuwa swali la kila mtu, mkuu wa gereza alichanganyikiwa na kuamuru kufuatilia ni nani aliyeingia ugali ule ndani ya gereza. Kwa sababu ya umaarufu wa Anorld haikuchukua muda mrefu kugundua kuwa ni yeye ndiye aliyeleta chakula hicho.
Mkuu wa gereza alitoa taarifa hiyo polisi ambao bila kuchelewa walianza msako wa kumtafuta Anorld kama mtuhumiwa namba moja wa mauaji hayo! Polisi walipokwenda kwake hawakumkuta na kulazimika kumkamata mke wake Suzanne na kumweka mahabusu wakati msako wa kumtafuta Anorld ukiendelea.
Mipango ya mazishi kwa taratibu za gereza ilianza kuandaliwa ili mwili wa Zena uzikwe lakini mara tu baada ya maiti yake kupakiwa ndani ya gari watoto wawili mapacha Patrick na Nancy waliwasili gerezani, habari waliyoitoa kuwa waliwasikia Anorld na mkewe wakipanga jinsi ya kumuua mama yao ili wamdhulumu watoto wake ilizidi kuwahakikishia kuwa ni Anorld na Suzanne ndiyo waliofanya mauaji hayo.
*****
Msako wa Patrick na Nancy porini:

“Fuatilieni hukohuko porini na mkivipata hivyo vitoto viueni kabisa ili kupoteza ushahidi, maana hivyo ndivyo vitajidai ni mashahidi mahakamani sababu ndivyo vilisikia maneno yangu!” Aliamuru Anorld.
Maneno hayo yalimfikia Patrick moja kwa moja mahali alipokuwa amejificha, hofu kubwa ilimwingia moyoni mwake alijua mwisho wao ulikuwa umefika kama tu wangeingia mikononi mwa watu waliokuwa wakiwatafuta. Alishindwa kuelewa ni kwanini Anorld na mama yao mdogo Suzanne walikuwa wameamua kuwageuka kiasi hicho.
Hawakuwa na mahali pa kukimbilia walijua kwa vyovyote vile wangekamatwa tu! Kwani miale ya kurunzi za majambazi ilimulika kila mahali, mahali walipolala katikati ya nyasi hapakuwa mbali sana na makaburi na kama wangejaribu kusimama wima ni lazima wangeonekana.
Nancy alijua pia kuwa yeye na kaka yake walikuwa katikati ya hatari, walikuwa katikati ya kifo na maisha! Kama mtoto wa kike hakuna alichokijua zaidi ya kulia na kuzidi kumkumbatia kaka yake akimuuliza kipi wangefanya ili kujiokoa.
“Patrick! Patrick!Patrick!” Aliita lakini kaka yake hakumwitikia.
Alianza kumtingisha lakini Patrick hakuonekana kushtuka wala kujibu kitu chochote!Alikuwa kimya kabisa na mwili wake ulikuwa wa baridi kupita kiasi, Nancy alishindwa kuelewa ni nini kilimpata kaka yake, alishindwa kuyazuia machozi yalianza kumiminika huku tochi zikimulika kuelekea mahali walipokuwa wamejificha.
“Patrick!Patrick!Amka twende, mbona umekaa kimya?” Alizidi kusema Nancy lakini Patrick hakushtuka wala kuongea kitu chochote alionekana kama mtu aliyekufa na Nancy alishindwa kuelewa alikuwa hai au la!
“Patrick usife kaka yangu! Usiniache peke yangu ninakuhitaji tutoroke pamoja! Bila baba, bila mama, bila wewe nitaishije mimi?” Alisema Nancy huku akibubujikwa na machozi.
Tochi zilizidi kumulika katikati ya nyasi walipojificha, hofu ilizidi kumwingia Nancy na mwili wake ulikufa ganzi kabisa, alijikuta akiwa tayari kwa kifo au lolote ambalo lingetokea.
“Nasikia minong’ono sehemu hizi sijui viko wapi? Mara mbili nimesikia sauti ikiita Patrick!Patrick sijui tuko wapi hutu tutoto!” Alisema mmoja wa majambazi.
“Mulika sehemu ambako umesikia minong’ono inatokea! Ni lazima hawa watoto wauawe!” Anorld alizidi kuamuru na majambazi walizidi kuzikanyaga nyasi ndefu katika kuwatafuta Patrick na Nancy.
Patrick aliendelea kuwa kimya na Nancy aliendelea kutetemeka mwili mzima, dakika chache baadaye wazo lilimwijia kichwani mwake akaamua kusogea mbele, kwa sababu hakuwa na uwezo wa kumbeba kaka yake aliamua kumvuta katikati ya nyasi ni kelele za nyasi zilizowashtua majambazi mpaka wakagundua mahali walipokuwa wamejificha.
“Hivi huku!” Alipiga kelele mmoja wa majambazi baada ya kusikia mlio wa kitu kikivutwa katikati ya nyasi na majambazi wote walikimbia kuelekea eneo hilo na tochi zao.
*****
Ilikuwa ni saa tisa alasiri siku hiyo baada ya kazi ya kupasua kuni, Anne na wafungwa wenzake walikaa ndani ya gereza wengine wakiimba nyimbo za kumsifu Mungu, mpaka wakati huo Anne alikuwa bado akilia machozi sababu ya kifo cha Zena, alikuwa bado hajauelewa ukweli, mara ghafla askari magereza wa kike alisimama mlangoni.
“Kuna mfungwa anaitwa Anne humu ndani?” Aliuliza askari huyo.
“Ndiyo! Ni mimi afande!” Anne aliitikia.
“Unaitwa ofisini kwa mkuu wa gereza mara moja!”
Anne alisimama na kuanza kukimbia kutoka nje ya gereza na kwenda moja kwa moja hadi ofisini kwa mkuu wa gereza. Mkuu wa gereza alikuwa mzee wa makamo kati ya miaka 45-50, mweusi na kichwa chake kilijaa mvi nyingi, alikuwa ni mwenyeji wa Kigoma na sura yake ilitisha kidogo.
Hakuna mtu aliyemuogopesha Anne katika maisha yake kama mkuu huyo wa gereza! Hakutaka hata kumwona na kwa kuitwa kwake ofisini siku hiyo alijua wazi kulikuwa na tatizo kubwa sana ambalo kwa vyovyote lingepelekea kuongezwa kifungo, ilikuwa si kawaida kwa mfungwa kuitwa ofisini kwa mkuu wa gereza.
“Sijui nimekosa nini tena mie? Sijui wamebadilisha tena kifungo changu?” Anne alijiuliza maswali mengi kabla hajafika ofisini kwa mkuu wa gereza.
“Unaitwa nani?”
“Mimi?”
“Wewe ndiyo!”
“Ninaitwa Anne!”
“Unatakiwa kuhama gereza hili na utapelekwa gereza la Keko jijini Dar es Salaam! Hivyo utaondoka hapa Butimba kesho asubuhi!” Mkuu wa gereza alisema.
Anne alikaa chini na kuanza kulia machozi akimwomba Mkuu wa gereza abadilishe uamuzi huo kwa sababu alikuwa na watoto ambao wangependa kumwona mara kwa mara.
“Mungu wangu watoto wangu watanionaje huko Dar es Salaam baba? Nihurumie tafadhali” Alisema Anne, hakujua jambo lolote lililokuwa likiendelea nje ya gereza juu ya watoto wake.

Je, nini kitatokea?
Anne atakubaliwa kubaki gerezani Butimba?
Na je huko porini Patrick kafa au yupo hai?
Na je watakamatwa?
 
SEHEMU YA 20


Suzanne aliwekwa maabusu kwa karibu masaa mawili akihojiwa mahali alipokuwa mumewe Anorld, mahojiano hayo yaliambatana na mateso makali akilazimishwa kusema ukweli, Alivumilia kwa muda lakini baadae alishindwa na kutoboa mahali ambako alifikiri mumewe angeweza kuwa amejificha.
Kilichofanywa na polisi ni kumchukua ndani ya gari hadi nyumbani kwa dada yake ambako waliwachukua watu watatu akiwemo dada yake na Anorld na kwenda kufanya nao mahojiano kituoni, nao waliteswa sana mpaka kufikia mpaka wakataja kila kitu kilichoendelea.
“Wamekwenda kuwatafuta wale watoto ili wawaue kwa sababu wanaamini ni wao ndio waliowaeleza nyinyi juu ya mpango wa kumuua mama yao!” Dada yake Anorld aliyasema maneno hayo mbele ya Suzanne baada ya kubanwa mikono na koleo!
“Wewe uliufahamu vipi mpango huo?”
“Nilimsikia kaka akisema kwa hasira baada ya kusikia mmemkamata mke wake, alisema ni lazima Patrick na Nancy wafe kwani ndio waliotoboa siri hiyo nilipomuuliza juu ya siri hiyo alinieleza kila kitu!”
“Kwa hiyo wamekwenda kuwatafuta wapi?”
“Taarifa nilizonazo wamekwenda katika makundi mawili, moja linazunguka mitaani na jingine limekwenda makaburini ambako mwili wa marehemu umezikwa wanaamini watoto hao watakuwa huko!”
“Yeye Anorld amekwenda na kundi gani?”
“Amekwenda na kundi lililokwenda makaburini!”
“Ok ahsante!” Alijibu mkuu wa kituo na kuwaamuru maaskari waliokuwa karibu kuwaweka Suzanne na watu wengine waliowakamata mahabusu!
“Tunaondoka kwenda makaburini Sawa, fanyeni hivyo haraka!” Aliendelea kusema Mkuu wa kituo cha Polisi cha kati mjini Mwanza.
“Sawa Afande!” Waliitikia Maaskari wote.
Mkuu wa kituo na Maaskari wengine kumi na tano waliingia ndani ya magari matatu ya polisi na safari ya kwenda makaburini kumsaka Anorld na kundi lake lilianza.
Walipolikaribia eneo la makaburini Mkuu wa kituo alisimamisha gari lake na kushuka.
“Vijana tumekaribia eneo lenyewe, tafadhali wekeni silaha zenu tayari na taa za magari yote zizimwe!”
“Sawa afande!”
“Si mnayafahamu makaburi yenyewe?”
“Ndiyo tunayafahamu!”
“Ok!”
Baada ya kusema maneno hayo safari iliendelea kuelekea makaburini, taa za magari zikiwa zimezimwa na magari yakiendeshwa kwa mwendo wa taratibu ili sauti ya miungurumo yake isisikike, mita kama mia nne hivi kutoka makaburini magari yote yalisimamishwa na maaskari wote wakashuka na bunduki zao mikononi.
“Magari yote yabaki hapa na maaskari watano wazunguke upande huu na wengine watano wapite upande huu na tutakaobaki twende moja kwa moja, nafikiri kama wapo hapa tutawakamata sababu tutakuwa tumewaweka kati!”
“Ni lazima tuwakamate kabla hawajawaua watoto! Askari mwingine aliitikia na wote walisonga mbele.
******
Makaburini

Tochi zilizidi kumulika kila upande wa msitu wa nyasi ambamo Patrick na Nancy walijificha, majambazi waliwatafuta ili wawaue watoto wale wasio na hatia, Anorld huku akitetemeka kwa hasira alizidi kuamrisha juhudi za kuwatafuta ziongezeke! Nancy aliisikia sauti ya Anorld na kuzidi kuogopa, alizidi kulala juu ya mwili wa kaka yake bila kujua la kufanya.
Alijua ni lazima wangekamatwa na kwa uhakika hata yeye angekufa kama alivyokuwa kaka yake! Aliamini asilimia mia moja Patrick hakuwa hai! Roho ilimuuma sana na kujikuta akitokwa machozi ya huzuni.
Alishindwa kuelewa kama Anorld aliyewatunza na kuwalea akiwapa kila kitu ndiye aliyekuwa akiwatafuta ili awaue, lilikuwa si rahisi kulikubali na mpaka wakati huo Nancy alikuwa haamini juu ya mambo yaliyomtokea, alifikiri ilikuwa ni ndoto.
Patrick alikuwa bado amelala akiwa kimya kabisa kama mfu. Nancy alijua tayari kaka yake alikuwa maiti, hivyo alikuwa amebaki peke yake duniani ilikuwa ni lazima apambane na maisha mwenyewe na akujua angeyaanza vipi mapambano hayo! Alipoliwaza hilo ndio alizidi kububujikwa na machozi zaidi, hakujua maisha yangeendeleaje baada ya siku hiyo bila kaka yake na pacha wake Patrick.
Hakuwa na mama, hakuwa na baba na kwa historia aliyopewa ndugu zake wawili walifariki dunia katika mazingira ya kutatanisha ni bibi yao aliyedaiwa kufanya uchawi kuwaua na alipotaka kuwaua wao Patrick na Nancy kwa uchawi huo huo mama yao Anne aliamua kumuua kabla hajatekeleza nia yake ni jambo hilo ndilo lilimfanya aingie gerezani.
Wakati akiyawaza hayo huku akilia, tochi zilizidi kuelekea mahali alipokuwa, mwili wake wote ulikufa ganzi na hakujua angefanya nini kuokoa maisha yake kwa sababu ndugu yake tayari alishakufa!
“Vitoto hivi vipo wapi jamani?” Aliuliza mmoja wa majambazi
“Vipo maeneo haya haya tu!” jambazi mwingine alijibu.
Ghafla lilimwijia wazo kichwani mwake akiwa katika kutafuta kujiokoa, alianza kumvuta kaka yake katikati ya nyasi kutafuta mahali pengine pa kujificha, ni kelele ya nyasi ndiyo iiyowashtua majambazi na kujikuta mmoja wao akipiga kelele.
“Jamani wale watoto hawa hapa!” Alipiga kelele mmoja wa majambazi na kelele hiyo ilisababisha majambazi wengine wote wakimbilie eneo hilo, kwa hofu bila kufikiria mara mbili Nancy alijikuta akinyanyuka na kuanza kukimbia katikati ya nyasi akiwa ameinama.
Risasi kama tano hivi zilimfuata nyuma yake lakini bahati ya Mungu zote zilimkosa! Akazidi kutokomea katikati ya nyasi, ni milio hiyo ya risasi ndiyo iliyowafanya maaskari waliokuwa karibu na eneo hilo waweke tayari silaha zao, ilikuwa ni milio ya bunduki aina ya SMG wakati wao walikuwa na bunduki aina ya RPG! Walijua wazi kuwa milio ile haikuwa ya bunduki za zao.
Majambazi wakiongozana na Anold walizidi kumkimbiza Nancy porini, lakini mbele kidogo Nancy alijikuta akitumbukia ndani ya shimo refu lililoonekana kuwa ni kaburi ambalo halikutumika, shimo hilo lilikuwa katikati ya nyasi nyingi kiasi kwamba majambazi hawakufanikiwa kumwona alipotumbukia.
“Kakimbilia wapi?”
“Sijui!”
“Lakini si vilikuwa vitoto viwili?”
“Ndiyo lakini kitafuteni tu ndiyo hicho kimoja kimalizeni kwanza halafu tukitafute kingine, sawa?” Anorld aliendelea kutoa amri.
“Hakionekani tena!” Alijibu mmoja wa majambazi.
Nancy aliyasikia maneno hayo akiwa ndani ya shimo lenye urefu kama futi 5 hivi yalizidi kumuogofya. Alitetemeka sababu ya hofu na baridi kali iliyokuwepo, alizidi kulia machozi na hali ya kukata tamaa iliutawala moyo wake, hakujua ni kitu gani kingeendelea dakika chake baadae! Kwa mara nyingine alimkumbuka mama yake
Alipomfikiria Patrick na mahali alipomwacha roho ndiyo ilizidi kumuuma zaidi, alitamani kutoka shimoni ili nae auawe kama alivyokufa kaka yake, lakini alishindwa kutoka shimoni kwa sababu hapakuwa na mahali popote pa kushika kama msaada wa yeye kutoka nje.
Kilichofuata Nancy akiwa shimoni ni milio mingi ya risasi, alishindwa kuelewa ni kitu gani kilikuwa kikiendelea. Alisikia sauti za watu wakilia na vishindo vya watu wakikimbia huku na kule vilisikika, Nancy hakupata jibu la kilichokuwa kikiendelea juu ya shimo hilo! Alihisi kulikuwa na mapigano makali sana yakiendelea.
Dakika kama arobaini na tano hivi baadae hali ilitulia kukawa na ukimya wa ajabu, alisikia kitu kama mizigo ikiburuzwa juu ya ardhi na watu ikivutwa na watu waliokuwa wakinong’ona .
“Tumewamaliza na kama Anorld asingenyoosha mikono juu naye tungemmaliza pia!” Nancy aliwasikia watu hao wakiongea.

******
Mapigano kati ya polisi na majambazi aliokuwa nao Anorld yalikuwa makali kupita kiasi, majambazi wote isipokuwa Anorld walipigwa risasi na kufa papo hapo, kilichomuokoa Anorld ni kujisalimisha mbele ya polisi, maiti za majambazi aliokuwa nao zilichukuliwa na polisi kupelekwa chumba cha maiti cha Bugando ambako ziihifadhiwa .
Hakuna askari hata mmoja aliyepoteza maisha yake katika mapambano hayo, maaskari waliuona huo kama ushindi mkubwa na hakuna askari hata mmoja aliyekumbuka kuwepo kwa watu wengine zaidi ya majambazi katika makaburi hayo, wote walisahau kuwa majambazi waliwafuata Patrick na Nancy.
*****
Asubuhi kulipokucha taarifa za kuuawa kwa Anorld zilishasambaa mji mzima wa Mwanza, redio na televisheni zilitangaza juu ya mauaji hayo yaliyounganishwa na mauaji yaliyotokea gerezani Butimba ambayo Anorld alihusishwa nayo moja kwa moja!
Majira ya saa mbili hivi asubuhi Nancy kwa msaada mzizi uliokuwemo ndani ya shimo hilo alifanikiwa kutoka hadi nje, alishangazwa na hali iliyokuwepo juu, nyasi zililala na damu ilitapakaa sehemu mbalimbali katika nyasi.
Kitu cha kwanza alichofanya Nancy baada ya kusimama juu ya ardhi ni kwenda moja kwa moja hadi mahali alipouacha mwili wa kaka yake ukiwa umelala. Hakuyaamini macho yake alipokuta mwili huo haupo! Alianguka chini na kuanza kulia alijua majambazi waliuchukua na kuondoka nao, ilikuwa huzuni kubwa kwa Nancy.
*****
Milio mengi ya risasi iliyotawala makaburini ndiyo iliyomzindua Patrick kutoka katika hali ya kuzimia aliyoipata sababu ya hofu! Kwanza hakukumbuka mahali alipokuwa lakini muda mfupi baadae fahamu zake zilimrejea akamkumbuka kila kitu kilichotokea na pia dada yake Nancy!
Aliangaza huku na kule lakini hakumwona dada yake mahali popote, kwa jinsi risasi zilivyolitawala anga Patrick alijua kwa vyovyote majambazi walishamuua! Naye alianza kulia akimlilia dada yake.
Hali ilipozidi kuwa mbaya zaidi makaburini aliamua kuokoa maisha yake bila kujali kitu gani kingempata, alinyanyuka na kuanza kukimbia mbio kuelekea kwenye nyasi ndefu zaidi, alifanikiwa kutokomea bila kuonekana mbele aliendelea kutembea kwenda mbali zaidi.
Alitembea usiku mzima kulipokucha alikuwa barabarani eneo la Usagara, njia panda ya kwenda Bukumbi! Mwili wake wote ulikuwa ukimwasha kwa sababu ya kupita kwenye nyasi zilizowasha! Mawazo yake yote yalikuwa kwa dada yake Nancy! Mpaka wakati huo hakuelewa alikokuwa na kama alikuwa hai au alikuwa amekufa!
“Jamani Nancy dada yangu umekufa kweli?” Patrick aliongea peke yake huku akilia.
Alijiona mtu asiye na thamani yoyote duniani bila dada yake! Hakuwa na mama, baba wala mtu yeyote aliyemfahamu kama ndugu, mtu pekee aliyemtegemea alikuwa Anti Suzanne lakini nae tayari alishawasaliti na kuamua kumuua mama yao na sasa alikuwa akitaka kuwaua wao.
“Naondoka sirudi tena Mwanza hata shule kusoma tena sitaki mie! Nitakwenda mahali popote hata kama nikifa hukohuko sawa!” Alisema Patrick kwa uchungu.
Siku hiyo nzima alishinda hapo hapo Usagara akifikiria akifikiria mahali pa kwenda tena bila kuwa na pesa yoyote mfukoni mwake, mchana aliosha vyombo kwa mama ntilie na kupewa ukoko akala! Watu wengi waliomuona walishangaa ni kwa nini alikuwa akilia muda wote, walipomuuliza hakuwa tayari kueleza kila kitu kwa kila mtu! Lakini alifanya hivyo kwa mzee mmoja wa Kisomali aliyemkuta ndani ya Hoteli iliyoitwa Bismillah, mzee huyo alimnunulia Patrick chakula cha usiku baada ya kumwona akilia nje ya hoteli hiyo.
“Kwa hiyo lengo lako ni kuondoka mkoa wa Mwanza siyo?”
“Ndiyo, nisipoondoka wataniua!”
“Unataka kwenda wapi?”
“Mimi?”
“Ndiyo”
“Nataka kwenda Dar es Salaam! Nataka nipotee kabisa sitaki kubaki Mwanza, sitaki kuona vitu vitakavyonikumbusha mama na ndugu zangu hasa dada yangu Nancy nilimpenda mno!”
“Mimi ni dereva wa lile gari aina ya Fiat pale nje ninasafiri kwenda Dar es Salaam, leo ninalala hapa kesho alfajiri naendelea na safari yangu, nitakusaidia kufika huko Dar es Salaam, lakini una ndugu yeyote katika jiji hilo?”
“Yupo shangazi yangu!” Patrick alimdanganya ili yule mzee azidi kumwamini zaidi.
Mzee yule ambaye baadae Patrick aligundua aliitwa Bashir alimchukulia chumba katika hoteli aliyopanga yeye akalala, alfajiri saa 11 siku iliyofuata alimwamsha tayari kwa safari kuelekea Dar es Salaam iliyotegemewa kuwachukua karibu siku nne.
Siku hiyo hiyo jioni walifika Nzega walichukuwa vyumba na kulala tayari kwa safari tena siku iliyofuata! Mawazo na akili yote ya Patrick ilikuwa kwa dada yake Nancy! Hakuwa na uhakika kama alikuwa hai mpaka wakati huo, safari yote hadi Nzega aliimaliza akilia.
Dereva na utingo walijaribu kila waliloweza kumfariji lakini haikuwezekana , alinyamaza dakika thelathini na kulia masaa mawili na kila alivyolia alilitaja jina la Nancy!

******
Pamoja na Anne kulia machozi akiomba abaki gerezani Butimba kumalizia kifungo chake, alishindwa kumshawishi mkuu wa gereza kukubaliana naye hivyo jioni ya siku iliyofuata alipakiwa ndani ya treni la abiria kutoka Mwanza kuelekea Dar es Salaam.
Muda wote alilia watoto wake, alishindwa kuelewa angewaona vipi maishani mwake, alikuwa na uhakika kabisa kuwa halikuwa jambo rahisi kwa watoto wake kupata nauli za kuwafikisha Dar es Salaam, moyo wake uliumia sana.
Aliondoka gereza la Butimba bila kuelewa ni kitu gani hasa kilichompelekea rafiki yake Zena kujiua kwa kujidunga sindano, hakuwa na ufahamu wowote juu ya kuhusika kwa ndugu yake Suzanne na mume wake Anorld katika jambo hilo na hakujua ni yeye aliyetakiwa kufa badala ya Zena !
Aliendelea kulia akililia watoto wake pamoja na rafiki yake Zena.
Nasikitikia sana uamuzi wa wa Zena kujiua, nilikaa nae muda mfupi sana nikamzoea!” Aliwaza Anne akiwa ndani ya treni akilindwa na maaskari jela watatu.
Miongoni mwa watu waliopanda treni ya abiria siku hiyo ni Nancy tena bila tiketi, alikuwa ameamua kutoroka ili kuokoa maisha yake, alikuwa na uhakika asilimia mia moja kuwa kama angeendelea kukaa Mwanza ni lazima angeuawa kama alivyokuwa imepangwa! Akiwa ndani ya treni daraja la tatu alijificha chini ya kiti ili asionekane.

Je, nini kitatokea?
Je, Anne na Patrick watakutana?
Na nini kitatokea ndani ya treni?
 
SEHEMU YA 21


Tofauti na wengi walivyoamini baada ya vyombo vya habari kutangaza kuwa Anorld alikufa katika mapigano makali kati ya majambazi na polisi makaburini, Anorld alikuwa hai na kutiwa nguvuni na polisi na yeye na mke wake Suzanne walifikishwa mahakamani wakishitakiwa kwa makosa ya mauaji ya Zena ndani ya gereza kwa kumpa chakula chenye sumu na pia mauaji ya watu wengine waliouwawa makaburini.
Watu wengi waliomfahamu Anorld walisikitika sana kusikia Anorld alishiriki katika kitendo hicho na wengi hawakuamini, Anorld aliaminiwa sana na watu kwa sababu ya utoaji wake wa misaada kwa wasiojiweza.
Mahakamani hawakutakiwa kujibu kitu chochote na walipelekwa mahabusu gerezani Butimba.
Suzanne alifika gerezani akilia na kichwani mwake alifikiria kitu kimoja tu nacho ni kumuomba Anne msamaha kwa mabaya yote aliyoyafanya! Alijua wazi kitendo cha kuamua kumuua ili awachukue watoto wake hakikuwa chema na alijua bila Mungu kuepusha Anne angekuwa marehemu!
Tayari mambo yalishawaharibikia Anorld na mke wake, yote hayo sababu ya tamaa ya kupata watoto! Wakiwa ndani ya gari la kuelekea gerezani wakiangaliana na hawakusema lolote, kila mtu alimuonea aibu na huruma mwenzake.
Walipofika gerezani kila mmoja alishuka na kuongozwa kuelekea gerezani, Anorld alipelekwa upande wa wanaume na Suzanne alipelekwa upande wa wanawake.
Kitu cha kwanza alichokifanya Anne baada ya kuingia gerezani ni kuanza kumtafuta Anne, alikuwa akijuta moyoni mwake kwa kitu alichokifanya! Aliulizia kwa muda mrefu bila kufanikiwa kumpata. Jioni ya siku hiyo hiyo alikutana na mama mmoja na kumuulizia yeye alionekana kumfahamu Anne vizuri!
“Si yule rafiki yake na marehemu Zena?”
“Ndiyo!”
“Amehamishiwa gereza la Segerea Dar es Salaam na aliondoka jana tu hapa gerezani”
“Eh ungu wangu eh! Nitamwona wapi Anne? Sitaki kufa bila kumuona ninajua nitafungwa lakini kabla ya hilo nataka kwanza nikutane na Anne!” Alisema Suzanne huku akilia.
“Kwani kuna nini?” Mama aliuliza.
“Nimemkosea sana!”
“Umemkosea nini?”
“Mama hayo tuyaache ila ahsante sana kwa kunisaidia” Alisema Anne na kuanza kuondoka sehemu hiyo huku akilia na kumwacha mama huyo akishangaa!
Siku hiyo pia kama siku mbili zilizopita alilala safarini, aliumwa na kunguni na kupigwa na baridi kali! Suzanne aliumia sana moyoni na kujutia uamuzi ambao yeye na mume wake waliufikia.
“Pesa tulikuwa nayo tungeweza hata kuzaa watoto wa kwenye chupa! Sasa maisha yetu yameishia gerezani hata Patrick na Nancy wenyewe hatukuwapata!”
****************************
Lori aina ya Fiat lililoendeshwa na dereva Kisomali lilikuwa likiingia mjini Dodoma, Patrick akiwa amechoka hoi bin taban, ilikuwa ni mara ya kwanza kwake kusafiri safari ndefu kiasi hicho, njiani alishalia machozi mengi yakakauka na hatimaye kuyaona yote yaliyotokea kuwa ni sehemu ya maisha!
Ilikuwa ni mara yake ya kwanza kuingia Dodoma usiku huo, alishangazwa na wingi wa taa alizozifananisha kabisa na mji wa Mwanza aliotoka! Zilimkumbusha mengi kuhusu nyumbani, zilimkumbusha marehemu mama yake, zilimkumbusha mengi kuhusu Mchungaji Aron na mke wake na Patrick alijua bila wao kuondoka kwenda Nairobi kisha yeye na dada yake kuhamia nyumbani kwa Suzanne yaliyotokea yasingetokea!
Patrick alikuwa ameyaacha maisha yake yote nyuma yake, alikuwa akienda katika nchi ya ugeni ambako hakumjua mtu yeyote, hofu ilimuingia moyoni kila alipolifikiria jiji la Dar es Salaam na sifa alizopewa juu yake! Madawa ya kulevya, machangudoa, vibaka, majambazi kwa upande mwingine aliamini alikokuwa amekwenda alikuwa anafuata matatizo kama si kifo chake mwenyewe.
Siku hiyo walilala Dodoma kama ilivyokuwa kawaida yake hakuacha kusali kabla ya kulala, dereva aliwaacha yeye na Tingo na kwenda kulala hotelini ingawa alilala kwa tabu kubwa alipata usingizi na katika usingizi wake siku hiyo aliota ndoto aliyomrejeshea faraja zake, katika ndoto hiyo alikuwa na mama yake pamoja na dada yake Nancy lakini hawakuwa watoto tena, mama yao alikuwa mzee sana na Nancy alikuwa mwanamke tajiri na yeye Patrick alikuwa mtumishi wa Mungu!
Alifurahi sana lakini alipozinduka na kukuta ilikuwa ni ndoto aliumia na kujikuta akilia machozi.
Hakulala tena mpaka asubuhi akilia na dereva alipokuja saa kumi na mbili asubuhi, waliendelea na safari yao kuelekea Dar es Salaam.
“Hivi kutoka hapa mpaka Dar es Salaam ni kama kilometa ngapi?”
“Ni kama kilometa 450 hivi, tumebakiza miji ya Morogoro, Mlandizi, Chalinze, Kibaha na Dar es Salaam yenyewe, leo hii hii saa mbili ama saa tatu usiku tutakuwa tayari tupo Dar!”
“Mtakaa muda gani Dar es Salaam?”
“Hatukai sana tukifika tutateremsha mzigo huu na kupakia mwingine kwenda Congo Braziville!”
Jibu hilo lilimtisha sana Patrick aliyetegemea dereva na utingo wangebaki Dar es Salaam angalau kwa siku kadhaa wakati akijaribu kutafuta utaratibu wowote wa kuishi! Lakini yote hayo alimwachia Mungu.
“Si ulisema kuna shangazi yako Dar?”
“Ndiyo!”
“Una namba zake za simu ili tukifika tumpigie aje kukuchukua?”
“Namba zake?”
“Ndiyo!”
“Hapa sina ila nikizifikiria vizuri naweza kuzikumbuka!” Alisema Patrick na kujifanya kufumba macho kama mtu aliyekuwa akikumbuka kitu fulani wakati hakuwa na namba yoyote ya kukumbuka wala huyo shangazi yake pia hakuwepo!
“Aisee mzee sikumbuki kabisa!”
“Sasa utafanyaje maana sisi tunaweza kuondoka usiku wa leo hii hii kwenda Congo!”
“Hiyo usijali mtaniacha tu hapo hapo Dar es Salaam nitajua la kufanya ili asubuhi niende kutafuta shangazi yangu!”
“Anafanya kazi wapi?”
“Anafanyakazi uhimbili hospitali” Patrick alitaja jina lililokuwa karibu yake.
*****************************
Tatizo la Anne kutokwa na hedhi kila siku lilikuwa bado linaendelea na yeye kama mfungwa hakuweza kujitunza vizuri, ndani ya behewa alilokaa hapakukalika abiria wote waliokuwa katika viti vya karibu na kiti alichokikalia Anne walivikimbia viti vyao! Hali ya hewa iliwashinda maafande wa magereza tu ndiyo walibaki walishindwa kuondoka kwa sababu ilikuwa kazi yao lakini hata kwao pia yalikuwa mateso.
Anne alikaa kwenye kiti chake akilia machozi ya uchungu wa mateso aliyokuwa akiyapata, pia aliwalilia watoto wake na hakujua angekutana nao vipi! Mikono yake ilifungwa pingu! Aliyafikiria maisha yake tangu utotoni na kugundua yalijaa maumivu na machozi, hakuwahi kupata furaha yoyote katika maisha yake!
Mume wake alikufa! Watoto wake wawili nao pia na bado mapacha wake Patrick na Nancy aliobakiza pia alikuwa ametenganishwa nao na alikuwa akisota kifungoni na ugonjwa wa ajabu uliomfanya atengwe na watu kwa sababu ya harufu aliyotoa! Alimlaumu mama yake kwa yote haya na muzimu wa uchawi aliokuwa nao!
“Kweli mama alistahili kufa! Ni heri nilimuua!” Aliwaza Anne huku akilia.
Wakati akiwaza hayo tayari treni ilikuwa ikiingia stesheni ya Saranda, watu wengi waliteremka na kwenda chini kununua pilau na wali na vyakula vingine vilivyouzwa stesheni hapo! Anne alibaki ndani ya treni akilalamika njaa, askari aliteremka na kwenda chini kununua chakula kwa ajili ya Anne!
Aliporudi askari alikuwa na sahani ya pilau na glasi ya maziwa, walimfungua na kuzifunga miguuni kisha akamkabidhi sahani ya chakula alikifakamia chakula hicho na kukila kwa fujo.
“Wamepika pilau nzuri sana hawa watu! Utafikiri ya nyumbani!” Alisema Anne na baada ya kumaliza kula alichukua glasi ya maziwa na kuimimina mdomoni na akajisikia vizuri, ni mara ya kwanza alikunywa maziwa katika muda wa miaka karibu kumi na tatu aliyokaa gerezani.

*****************************
Nancy chini ya kiti:
Kwa siku mbili mfululizo Nancy alijificha chini ya kiti cha treni akiogopa kugunduliwa na wakaguzi wa tiketi kwa sababu hakuwa nayo, hakuna mtu aliyegundua kulikuwa na mtu chini ya kiti, hata abiria waliokikalia kiti hawakugundua kuwa kulikuwa na mtu chini ya kiti chao, Nancy alijibana vizuri katikati ya maboksi mawili na kulala kimya!
Njaa ilimsumbua kupita kiasi lakini hakuwa na la kufanya ilibidi avumilie, alikuwa amedhamiria kujificha chini ya kiti hicho mpaka treni ifike Dar es Salaam! Hakuwahi kufikiria Dar es Salaam ilikuwa ni umbali mrefu kiasi gani kwa treni, alikuwa amesafiri kwa muda mrefu sana lakini bado hawakufika, mwisho alichoshwa na maumivu ya njaa kali aliyokuwa nayo!
Mpaka treni lilipofika stesheni ya Saranda, Nancy alikuwa akilia kwa njaa kali chini ya kiti na alishindwa kuvumilia zaidi hasa alipoanza kusikia harufu ya wali kutoka kwa abiria wengine! Aliamua kujitokeza na kupambana na sura za watu mbalimbali waliomwangalia na kumshangaa!
“Wewe binti umekaa hapo chini ya kiti tangu saa ngapi mbona hatujakuona?”
“Tangu mwanzo wa safari!”
“Mh! Kwanini lakini? Una matatizo gani?”
“Nina njaa! Nisaidieni chakula kwanza!” Nancy alisema bila woga.
“Chakula? Mbona nimemaliza hebu njoo huku!” Mama yule alijibu huku akiondoka na Nancy.
Walishuka hadi chini ambako mama huyo alimnunulia Nancy chakula akaanza kula, kasi yake ya kula ilimshangaza sana, alionekana kuwa na njaa kali kupita kiasi.
Kabla hata Nancy hajamaliza chakula chake vizuri katika sahani, treni lilipiga honi.
“Malizieni tu hiyo ni honi ya kwanza!”
“Kweli?” mama aliyemnunulia Nancy chakula aliuliza.
“Ndiyo” Mama muuza aliitikia.
Baadae treni ilianza kusogea mbele taratibu na Nancy aliendelea kula chakula na hiyo ilikuwa ni sahani ya pili ! Baada ya chakula wote wawili walipanda ndani ya treni kwa haraka kabla halijazidisha mwendo.
“Lo kumbe walikuwa wanatudanganya!” Alisema mama yule wakati wakikaa vitini, Nancy alianza kujikunja ili aingie tena chini ya kiti!
“Hapana kaa tu hapa juu ili unieleze wewe ni nani na umetoka wapi?”
“Sina tiketi nitakamatwa!”
“Wee kaa tu usiwe na shaka, wakikukamata sisi tutalipa!”
Nancy alikaa kitini na kuanza kumsimulia mama huyo kila kitu kilichotokea maishani mwake, alimweleza ni kwanini alikuwa akisafiri kwenda Dar es Salaam, mama yule alisikitika sana na machozi yalimtoka bila kutegemea, hakudhani Nancy angekuwa na matatizo makubwa kiasi hicho! Kila mtu aliyesikia habari hiyo alisikitika.
“Hiyo habari niliisoma magazetini na ilidaiwa wewe na kaka yako mlikuwa mmekufa!”
“Hapana mimi sikufa ila kaka yangu ndiye amefariki dunia!”
“Pole sana”
“Ahsante!”
“Usiwe na shaka tutakusaidia tutafika Dar es salaam mimi na mume wangu tunafanyakazi chuo kikuu cha Dar es Salaam tunatoka nyumbani Bukoba, huko ndiko nyumbani kwetu na hawa wawili ni watoto wetu Lilian na Rugarabamu” Alisema mama huyo na kumtambulisha Nancy kwa mume wake!
**********************************
Usiku wa saa sita treni lilingia Kilosa mkoani Morogoro, lakini hali ya Nancy haikuwa nzuri, tumbo lake lilikuwa linauma sana na hakuwa yeye tu aliyeumwa na tumbo ni pamoja na mama aliyemnunulia chakula na watoto wake pia waliumwa sana na matumbo, kila mtu alikitilia shaka chakula walichokula!
Kabla hawajaondoka Kilosa wote walianza kuharisha na baadae kutapika! Waliharisha maji meupe sana kama maji ya mchele na kuchafua behewa! Minong’ono kuwa walikuwa na kipindupindu ilianza kujitokeza, taarifa zilitolewa kwa kiongozi wa treni na Nancy, mama Isabela, Rugarabamu na mume wake walichukuliwa na kupelekwa zahanati iliyomo ndani ya treni ambako daktari alithibitisha kuwa wote walikuwa na kipindupindu!
Hakuwa na maji ya kutosha kuwawekea katika mishipa yao, aliwawekea chupa moja moja lakini haikusaidia kitu hali zao zilizidi kudhoofika, waliharisha na kutapika maji mengi mno! Watoto wa yule mama katika muda wa masaa mawili wakawa hawawezi hata kuongea.
Wakati wanaingia Morogoro watoto wote wawili wa mama yule walishafariki na hali ya Nancy ilikuwa mbaya mno! Walikimbizwa haraka hospitali ya mkoa wa Morogoro ambako walilazwa na kutundikiwa dripu za maji ili kuyarejesha maji yote yaliyopotea na walipewa madawa aina ya tetracycline!
Hali ya Nancy ilikuwa mbaya mno na hakuna mtu aliyekuwa na matumaini kuwa angepona kwa hali aliyokuwa nayo.
Alilazwa kitanda cha kwanza kabisa katika chumba alichopewa na mama Isabela na mume wake waliwekwa chumba cha pili, ingawa hali yake ilikuwa mbaya sana Isabela akiwa katika chumba hicho alimwona mgonjwa mwingine akiingizwa yeye naye hali yake ilikuwa mbaya mno na pamoja na kuwa hoi mgonjwa huyo alikuwa na pingu mkononi na nyuma yake walikuwepo maaskari magereza watatu.
“Huyu ni nani?” Muuguzi aliuliza.
“Ni mfungwa amehamishwa gereza la Segerea kutoka Butimba baada ya kutoka Kilosa ghafla alianza kuharisha nafikiri ni chakula alichokula Saranda!” Alijibu askari magereza mmoja.
Macho ya Nancy yalikuwa yamelegea na midomo ilikuwa mizito kupita kiasi, giza lilishaanza kuyaingilia macho yake, alijua huo ndio ulikuwa mwisho wake, lakini aliposikia kwa mbali maneno ya askari Magereza juu ya mgonjwa aliyeingizwa ndani ya chumba alijitahidi kufumbua macho yake ili amuone mgonjwa mwenzake! Hakuyaamini macho yake alipokuta ni mama yake na kujikuta akitamka kwa shida.
“Ma....ma!” Aliita kwa taabu kama mara tatu lakini alizidi kuishiwa nguvu na kulegea, hakusema neno tena.
Anne alisikia sauti ikiita mama, ingawa haikusikika vizuri lakini sauti hiyo aliifananisha na sauti aliyozoea kuisikia kabla, ilifanana na ya Nancy! Ingawa hakuwa na uhakika sana wa jambo hilo Anne aligeuza macho yake na kuangalia pembeni, alimwona mwanae Nancy katika hali mbaya.
“Ja...ma...ni mwa...na...ngu!” Alisema Anne kwa shida na kunyoosha mkono wake, Nancy nae alinyoosha wa kwake mpaka wakashikana waliamini huo ulikuwa ndiyo mwisho wao baada ya hapo walianza kuharisha mfululizo bila kusitisha!
“Patr..ic...yupo wa...pi!?” Aliuliza Anne kwa shida huku akiendelea kuharisha.
“Ali...ku...fa!”
Ingawa alikuwa mgonjwa taabani aliposikia Patrick alikufa Anne alimwaga machozi! Lakini alishukuru Mungu kukutana na mwanae angalau mmoja.
Je, nini kitaendelea?
Nini kitampata Patrick jijini?
Je, Nancy na mama yake watapona au ndiyo mwanzo wa Patrick kuwa peke yae duniani?
 
SEHEMU YA 22


Global outreach Mission lilikuwa ni shirika la kidini lililohubiri dini Duniani kote na liliongozwa na Mwijilisti wa Kimataifa Karl Heinz Schroden, Mjerumani mwenye mwenye umri usiopungua miaka hamsini hivi!
Mwinjilisti huyu alizunguka dunia nzima akihubiri Injili, na kazi yake watu wengi waliokoka na kumrejea Mungu! Lengo lake lilikuwa ni kuwafikia watu milioni 200 katika muda wa miaka thelathini. Alikuwa amefanya kazi hiyo kwa miaka karibu ishirini bila kurudi nyumbani kwao Ujerumani.
Heinz hakuwa na mke wala mtoto wala familia iliyomtegemea, kwa sababu hiyo aliamua kutumia kila alichokuwa nacho kuikamilisha kazi ya Mungu kabla ya kulala mauti.
Watu wengi walidai Mwinjilisti Heinz alikuwa na kasoro kimaumbile ndiyo maana aliweza kuifanya kazi hiyo kwa muda mrefu bila kukumbwa na kashfa yoyote! Yeye Heinz alilikanusha sana jambo hilo kwa kudai aliitwa na Bwana kwa ajili ya kazi ya Mungu na ni yeye Mungu aliyemwezesha kufanya yote aliyoyafanya.
Shirika lake lilikuwa kwa kasi ya ajabu, katika miaka mitano ya kuwepo kwake lilikua na kuwa shirika kubwa la Kidini kuliko mashirika mengine ya dini duniani! Mikutano aliyofanya ilijaza maelfu kwa maelfu ya watu na hapakuwa na utaratibu wa kukusanya sadaka bali ni yeye aliyegawa nguo na msaada kwa wasiojiweza waliofika mkutanoni.
Heinz alifungua Makanisa katika kila nchi aliyokwenda, nayo pia yalikua kwa kasi kubwa! Alimiliki ndege tatu, magari ambayo hata yeye hakujua idadi yake, meli za kusafiria, kifupi Heinz alikuwa Mwinjilisti tajiri kuliko wafanyabiashara wengi na watu walishindwa kuelewa alipata wapi utajiri huo.
Mwinjilisti Heinz aliingia Tanzania akitokea Kenya baada ya kuhubiri katika nchi za Msumbiji,Zambia, Zimbabwe, Botswana na Afrika ya Kusini, matangazo ya kuingia kwake Tanzania yalianza miezi mitatu kabla, Redio na vituo mbalimbali vya televisheni vilijipatia mamilioni ya shilingi kwa matangazo yake peke yake!
Vituo vingine vilifikiria hata kubadili vipindi vya taarifa za habari ili kutangaza matangazo ya Mwinjilisti Heinz kwa sababu yalilipiwa pesa nyingi zaidi.
Msafara alioingia nao nchini kupitia Namanga uliwashangaza watu wengi, alikuwa na magari aina ya Scania ya tani ishirini yasiyopungua thelathini ambayo yalibeba mizigo yake, alikuwa na magari mengine madogo ishirini yaliyobeba wafanyakazi wa shirika lake na waimbaji wa Kwaya mbalimbali alizotembea nazo kila alikokwenda duniani.
Hiyo peke yake ilikuwa haitoshi kwani ndege mbili zilimfuata katika kila nchi aliyoingia zikileta mizigo yake mingine, mizigo hiyo iliyodaiwa kuwa misaada iliteremshwa usiku na kwa uangalizi na usiri mkubwa! Hakuna mtu hata mmoja katika watu waliosafiri nao aliyebahatika kujua mizigo hiyo ilikuwa nini na mara nyingi usiku huohuo baada ya kupakuliwa ilipakiwa ndani ya magari madogomadogo na kupelekwa kusikojulikana.
Kila Mwinjilisti alipoulizwa jibu lake lilikuwa moja kuwa “Ilikuwa misaada kwa wenye shida!” ambalo lilitosha kuwafanya wafuasi wake waamini na kutohoji tena.
Siku alipoingia Arusha na msafara wake hoteli zilikodiwa na shirika lake, wageni walioingia Arusha siku hiyo walilala stendi za mabasi na wengine walilazimika kwenda kulala mjini Moshi! Sifa za Mwinjilisti Heinz zilisambaa Arusha nzima katika muda wa masaa mawili!
Alifanya mikutano kwa wiki nzima mjini Arusha akaondoka na kuelekea Moshi ambako alifanya tena mkutano kwa wiki nzima na baadaye kuingia Dar es Salaam, katika mikutano yake watu walipokea miujiza ya ajabu na aliwashangaza watu kwa uwezo wake wa kuwagusa puani kwa mikono yake wakaanguka chini na kupoteza fahamu na kusikia raha ya ajabu mioyoni mwao.
Kilichowashangaza wengi baada ya baada ya kuguswa puani siku iliyofuata walitaka kuguswa tena na walipoguswa walisikia raha ileile kama waliyosikia siku moja kabla hatimaye wengi wakawa hawawezi chochote mpaka wameguswa puani na Mwinjilisti Heinz! Wengi waliamini hiyo ilikuwa nguvu ya Roho Mtakatifu!
Ni siku hiyohiyo aliyoingia Dar es Salaam ndiyo pia Patrick aliingia ndani ya jiji hilo la maraha akitokea Bara, gari alilokuja nalo kwa msaada wa dereva wa Kisomali liliteremsha mizigo usiku huohuo likapakia mizigo mingine na kuondoka kuelekea Kongo kupitia Tunduma! Patrick alisikitika sana lakini alimshukuru sana dereva wa gari hilo kwa msaada wake!
Ingawa alikuwa mgeni jijini usiku wa siku hiyo Patrick alilazimika kutembea hadi ufukweni ambako alilala ndani ya mtumbwi mbovu huku akiumwa na mbu na kupigwa na baridi kali! Usiku mzima Patrick hakupata usingizi akijaribu kuyafikiria maisha yake tangu utotoni na mateso aliyoyapata!
Alipomkumbuka mama yake Anne pamoja na dada yake Nancy alishindwa kujizuia na kujikuta akilia machozi! Mpaka wakati huo Patrick hakujua kuwa aliyekufa gerezani hakuwa mama yake bali Zena, aliamini mama na dada yake hawakuwa hai na alikuwa peke yake duniani!
Mawazo hayo yalimfanya Patrick aumie sana moyoni mwake na kuona alikuwa ni mtu asiye na thamani duniani, aliichukia Tanzania na kuwaona watu wote hawafai.
“Hakuna ninaloweza kufanya hapa duniani zaidi ya kumfuata Yesu Kristo peke yake! Ni yeye ndiye anayeweza kuwa mfariji na rafiki yangu wa kweli, sina mwingine wa kurejesha furaha yangu isipokuwa yeye!’ Aliwaza Patrick huku akilia.
*****
Asubuhi ya kwanza jijini
Dar es Salaam:
Kulipokucha asubuhi Patrick alitoka ndani ya mtumbwi mchafu aliolala na kuamua kuingia mitaani kutafuta lolote! Ilikuwa ni mara ya kwanza kwake kuwa katika mji mkubwa kama Dar es Salaam alishangaa karibu kila kitu alichokiona hasa maghorofa marefu yaliyokuwepo maeneo ya posta!
Hakujua mtu yeyote ndani ya jiji hilo na hakujua aanzie wapi kwa sababu kila sehemu zilifanana! Asubuhi hakuwa na uhakika wa kufungua kinywa chake lakini bado aliamini asingeweza kufa katika nchi ambayo watu walikula na kusaza, alijua lazima ilikuwepo njia ya yeye kuishi ambayo Mungu pekee aliijua!
Ilipofika saa saba ya mchana alikuwa maeneo ya Kariakoo, kila kitu kilishamchanganya hakuelewa ni wapi kulikuwa Mashariki,Magharibi, Kaskazini wala Kusini! Hakuelewa alikokuwa akitoka wala alikokuwa akielekea! Alikwenda tu kama kitu kilichosukumwa na upepo.
Baada ya kuzunguka sana ghalfa alijikuta amesimama kwenye mnara wa askari, Patrick aliiangalia sanamu ya askari yule kwa muda mrefu na hakuona taabu wala aibu kwa jinsi watu ndani ya magari yaliyopita kwenye mzunguko wa mnara huo walivyomshangaa kwani aliamini alikuwa akijaribu kulizoea jiji la Dar es Salaam taratibu!
Huku njaa ikimuuma alipotoka kwenye mnara wa askari alinyoosha moja kwa moja kupitia barabara za Azikiwe na Maktaba na kujikuta kwenye makutano ya barabara ya Maktaba na Bibi Titi, kwa muda aliyashangaa mataa ya kuongozea magari yaliyokuwepo katika makutano ya barabara hizo lakini baadaye alikata kushoto na kuelekea Akiba!
Alipofika kwenye makutano ya barabara ya Bibi Titi na Morogoro alisimama chini ya mti mkubwa nje ya chuo cha Ufundi Dar es Salaam na kuanza kuwaza ni wapi angepata chakula cha mchana huo kwani njaa ilikuwa ikimsumbua kupita kiasi!
“Nitajikaza sababu mimi ni mwanaume isitoshe riziki ya mbwa ipo miguuni mwake!” Patrick alijisemea moyoni na kusonga mbele kufuata barabara ya Morogoro akielekea kituo cha mabasi cha Faya!
“Hivi hapa ndipo kwenye ofisi ya umoja wa vijana? Hapa kumbe ndipo zilipo ofisi za Nchimbi? Nikishindwa kabisa nitamtafuta hata yeye anisaidie hela ya kula! Ingawa hanifahamu, nitajieleza kwake nafikiri hataninyima hata mia mbili!” Patrick alijisemea moyoni mwake wakati akilipita jengo la Umoja wa vijana kulia kwake.
Alipofika kituo cha Faya alikuta watu wengi wakisubiri usafiri wa daladala kuwarudisha majumbani kwao!
“Haya, Sinza, Sinza! Sinza wahi gari!” Mpiga debe alipiga kelele kuwaita abiria wakati gari lake likiegeshwa.
“Ndiyo niliwahi kusikia hapa Dar es Salaam kuna Sinza tena na yule mwanamuziki Remmy anakaa hukohuko!” Aliwaza Patrick na hakusimama kituoni hapo alizidi kusonga mbele na kuzipita taa za kuongozea magari za Faya.
Mbele alishangaa kuona makundi makubwa ya watu wakitembea kwa miguu kuelekea bondeni wengi wakiwa akinamama na watoto!
“Masikini sijui hawa wamekosa nauli?” Aliwaza Patrick lakini alipowaangalia mikononi mwao aliwaona wakiwa na Biblia.
“Nafikiri wanakwenda kanisani, lakini leo mbona siyo Jumapili?” Alijiuliza Patrick.
Ghafla mawazo yake hayo yaliingiliwa na sauti ya kipaza sauti kikiongea kwa sauti ya juu! Alisikia sauti za watu wakiimba nyimbo za kumsifu Mungu!
“Njoo kwa Kristo, Kristo anaokoa!” Patrick aliyasikia maneno hayo ndani ya wimbo ulioimbwa.
“Namshukuru Mungu hiki ndicho kitu nilichokuwa nakitaka!” Patrick alisema na bila hata kusita alianza kuwafuata watu waliotembea katika makundi kuelekea bondeni.
“Karibuni katika viwanja vya Jangwani mmsikilize mtumishi wa Mungu Karl Heinz kutoka Ujerumani, leo yupo hapa! Njooni nyote mpokee uponyaji yaleteni matatizo yenu yote kwa Bwana!” Sauti ilisikika kwenye kipaza sauti.
Bila hata kutegemea Patrick alisikia furaha ya ajabu moyoni mwake alitembea na kujichanganya katikati ya watu na kusogea mbele zaidi ingawa ilikuwa ni kwa taabu kubwa! Aliimba nyimbo za mapambio na kurukaruka pamoja nao.Siku hiyo alijisikia kuutua mzigo uliokuwa kifuani mwake.
Baadaye Mwinjilisti Karl Heinz alisimama na kulihubiri neno la Mungu, karibu kila alichokiongea katika mahubiri yake kiliyagusa maisha ya Patrick moja kwa moja na alipoongea juu ya kifo na mauti Patrick alijikuta akiwakumbuka mama na dada yake.
Patrick alipiga magoti chini na kusali huku akilia machozi, akiwaombea mama na dada yake kwa Mungu ili awaweke mahali pema mpaka siku ambayo angekutana nao tena!
Ilikuwa ni huzuni kubwa sana kwa Patrick lakini alipokumbuka kuwa tayari alikuwa ndani ya Kristo alijisikia amani na furaha ikirejea kubwa moyoni mwake.
Mkutano ulipokwisha Patrick alisikia msukumo wa kutaka kumwona Mwinjilisti Karl Heinz, ingawa alijua ilikuwa kazi ngumu lakini aliamini kama angefanikiwa ni lazima angemwonyesha ni kwa jinsi gani angeweza kuwa mtumishi wa Mungu jambo alilotamani kulifanya!
“Nitamwona tu!” Alisema Patrick na kuanza kujongea mbele kuzunguka nyuma ya jukwaa ambako alikutana na mmoja wa shemasi waliohudumia katika mkutano huo.
“Bwana asifiwe mpendwa?” Patrick alimsalimia shemasi huyo.
“Ameeeni! hujambo mpendwa?”
“Sijambo!”
“Unauonaje mkutano huu?”
“Kwa kweli nimebarikiwa sana na ninatamani kuonana na mtumishi wa Mungu Heinz kwani ameyagusa sana maisha yangu!”
“Kweli?”
“Ndiyo!”
“Basi subiri, ingawa najua ni shida sana kumwona, hivi sasa bado anafanya maombi kwa wagonjwa!”
“Una kalamu na karatasi hapo mpendwa?” Partick aliuliza.
“Ndiyo!”
Shemasi alinyoosha mkono na kumpatia Patrick kalamu na karatasi pamoja na Biblia kugandamizia, akaanza kuandika ujumbe wa Kiingereza kwa mwinjilisti Karl Heinz.
“Ninaitwa Patrick Huggins, ni kijana mdogo na Mungu amesema na mimi jambo ambalo ni muhimu sana niongee na wewe!
Ni mimi.
Patrick
Patrick alimaliza kuandika barua hiyo na kumkabidhi shemasi.
“Tafadhali mpendwa mkabidhi tu barua hiyo mimi nasubiri huku nyuma!”
“Sawa!”
Shemasi aliondoka kwenda jukwaani ambako aliikabidhi barua hiyo kwa mchungaji mwenyeji wa mkutano ambaye alikaa nayo mkononi akisubiri Mwinjilisti Heinz amalize kuombea wagonjwa ndipo akamkabidhi barua akaanza kuisoma!
“Where is this boy?”(Mvulana huyu yupo wapi?)
“Behind the Platform!”(Nyuma ya jukwaa)
“Bring him forward I want to talk to him!”(Mleteni mbele, nataka kuongea naye)
Mchungaji mwenyeji aliteremka akikimbia na kwenda nyuma ya jukwaa kumwangalia Patrick.
“Wewe ndiyo Patrick?”
“Ndiyo!”
“Tafadhali njoo mtumishi wa Mungu anataka kuongea na wewe!”
Patrick hakuamini ingekuwa rahisi kiasi hicho kuonana na mhubiri mkubwa kama Kart Heinz.
Patrick alipandishwa jukwaani na kupewa kiti akakaa na kusubiri Mwijilisti Karl Heinz amalize kuhubiri, njaa yote aliyokuwa nayo Patrick iliyeyuka alijisikia kushiba bila kujua chakula kilitokea wapi!
“Are you Patrick?”(Wewe ni Patrick?) Mtumishi wa mungu Kart Heinz alimuuliza Patrick alipomfikia.
“Yes I’m, I cant believe I’m talking to the great servant of God!”(Ndiyo ni mimi na siamini kama ninaongea na wewe mtumishi wa Mungu!)
“ Can we talk here?Or you need more Privacy?”(Unataka tuongee hapa au unahitaji faragha zaidi?)
“I need to talk to you alone!”(Nataka kuongea na wewe peke yako)
“Sure!”(Hakika?)
“Yes!”Ndiyo)
“Then come inside with me!”(Basi nifuate ndani) Kart Heinz alimwambia Patrick na wote wawili waliteremka jukwaani na kwenda moja kwa moja ndani ya hema moja lililokuwa na kila kitu kilifanya liitwe ofisi.
“This is my temporally office!”(Hii ni ofisi yangu ya muda)
“Oh it is very nice office!”(Oh! Ni ofisi nzuri)
“Sure?Thanks God!(Hakika? Ninamshukuru Mungu)
Baada ya kujitambulisha kwa Mwijilisti Patrick alianza kumsimulia kila kitu kilichotokea maishani mwake, kufiwa na wazazi wake ndugu zake na baadaye dada yake mpendwa Nancy! Na alieleza nia yake ya kutaka kumtumikia Mungu na kuokoa roho za watu wengi waliopotea, alimwomba Mwijilisti Heinz amsaidie kutimiza ndoto yake.
“I’m very poor, but I always wanted to be an Evangelist and save people’s lives! Please help me!”(Mimi ni masikini lakini siku zote nimetaka kuwa Mwijilisti nihubiri neno la Mungu na kuokoa maisha ya waliopotea, tafadhali nisaidie kutimiza ndoto hiyo) Alisema Patrick Mwijilisti Kart Heinz alitokwa na machozi.
“So you are an orphan?”(Kwa hiyo wewe ni yatima?)
“In the world I’m an orphan, but in Heaven I’m not because I have Jesus Christ!”(Hapa duniani mimi kweli ni yatima lakini mbinguni mimi si yatima kwa sababu ninaye Yesu Kristo)
“So where do you stay in the city?”(kwa hiyo hapa jijini unaishi wapi?)
“I have no where to stay! I arrived yesterday and slept at the beach in a decaying boat!”(Sina mahali pa kuishi hapa jijini, niliingia jijini jana na nililala ufukweni kwenye moja ya boti inayooza)
Mwijilisti Karl Heinz alichukua kitambaa chake na kufuta machozi yaliyokuwa yakimtoka na kulowanisha usoni, alikuwa ameumizwa sana na habari ya Patrick! Aliguswa sana na kujisikia kumsaidia Patrick.
“Patrick I will help you fulfil you dream! will make sure you have a Passiport,and will be travelling with you wherever I go” (Patrick nitakusaidia kutimiza ndoto zako, nitashughulikia hati yako ya kusafiria na tangu sasa nitasafiri na wewe kila ninakokwenda)
“Thanks! Thanks!Thanks!”(Ahsante! Ahsante! Ahsante!) Patrick alisema huku akilia kwa furaha.
*****
Anne, Nancy hospitalini:
Hali za wagonjwa zilikuwa bado mbaya,Anne na Nancy walikuwa bado wakiharisha na kutapika sababu ya kipindupindu! Dawa za kutibu ugonjwa huo zilikuwa zimekwisha hospitali ya Mkoa wa Morogoro na ziliagizwa kutoka jijini Dar es Salaam na kuwaacha Anne na Nancy katika hali mbaya na bila dawa, walilala vitanda jirani mikono yao ikiwa imeshikana na kung’ang’aniana! Hakuna aliyeongea kati yao wote walijua kifo chao kilikuwa kimefika.

Je kweli Anne na mwanae wataokoka?
Nini siri kubwa iliyopo katika kazi ya Mwinjilisti Karl Heinz?
Je, nini kitampata Patrick?
Je, ipo siku familia hii itakutana?
 
SEHEMU YA 23


Ngozi zao zilikuwa nyembamba na zilichukua muda mrefu sana kurudi zilipominywa wauguzi, nyama zao zilikakamaa mwilini kupita kiasi.
“Wapo dehydrated mno na sijui tutaokoaje maisha yao sababu kila tunapowapatia ORS wanatapika!” Alisema muuguzi akimwambia mwenzake aliyekuwa jirani alimaanisha kila walipowapa maji ya chumvi walitapika.
“Waliofuata dripu Dar es Salaam nao wamechelewa mno sijui kifanyike kitu gani kuokoa maisha ya wagonjwa hawa!”
“Tunahitaji dripu zenye sodium chloride ziingie katika mishipa yao hapo watapona kama wangekuwa na pesa tungekwenda kuwanunulia kwenye duka la dawa wakati tukisubiri dawa zetu zifike bila hivyo watakufa tu!” Muuguzi mwingine alijibu.
“Kwani wale wenzao wawili mtu na mke wake wako wapi?”
“Si unaamanisha yule mama aliyekuwa akiongea kihaya?”
“Ndiyo!”
“Amefariki muda mfupi uliopita!”
“Kwa hiyo wote wamefariki maana watoto wao pia walifariki hapahapa hospitalini muda mfupi baada ya kufika!”
Nancy aliyasikia maongezi hayo ya wauguzi kwa mbali sana, mwili wake haukuwa na nguvu kabisa na macho yake yalifunikwa na giza nene, kitu pekee alichokikumbuka kilikuwa ni mkono wake wa kushoto uliokuwa umekamatana na mkono wa mama yake wote walikuwa katika hali ya kufa!
Mwili wa Nancy ulikuwa umelegea kupita kiasi, alishindwa hata kujigeuza kitandani akisubiri dakika yake ya mwisho ifike! Aliamini hapakuwa na njia ya kuyaokoa maisha yake na mama yake hasa aliposikia kuwa mama Rugarabamu na mumewe tayari nao walishafariki dunia!
Alitamani sana kupona ili ajue ni kitu gani kilitokea mpaka mama yake akawa hai wakati hata kaburi lake waliliona, lakini haikuwepo tena nafasi ya kulijua jambo hilo kwani alitakiwa kufa wakati wowote
“Mimi na mama tunamfuata Patrick, familia yetu yote imekwisha duniani!” Aliwaza Nancy.
*****
Mafia Drug Traffikers:

Lilikuwa kundi maarufu la uuzaji wa madawa ya kulevya na mauaji duniani, lilianzishwa miaka ya 1900 huko Mirano, Italia. Lilikuwa na matawi sehemu nyingi sana duniani ikiwemo Ujerumani, Uingereza, Marekani, Nigeria, Tunisia, Brazil, Chile na katika nchi hizo walichaguliwa wawakilishi walioitwa Presdento! Ni hao ndio waliohakikisha madawa yanaingia katika nchi zao na kuyasambaza kisirisiri bila mtu yoyote kugundua, Mapresdento wa nchi nyingine walikuwa ni viongozi kama Mawaziri, Makatibu wakuu na hata Maraisi wa nchi zao.
Biashara ya madawa ya kulevya ilikuwa ni biashara haramu iliyopigwa vita karibu kila pembe ya dunia, katika nchi za Kiarabu watu wote waliofanya biashara hiyo walipigwa risasi ama kuchinjwa hadharani walipokamatwa lakini pamoja na hali hiyo watu hawakuacha kuifanya biashara hiyo ingawa kila siku walikamatwa na kupigwa risasi hiyo yote ilikuwa ni kazi ya kundi la Mafia drug Traffikers.

Heinz Luminie, Berlin 1947

Heinz Luminie alikuwa Presdento wa Mafia nchini Ujerumani, baada ya njia nyingi za kusafirishia madawa kugundulika na wafuasi wengi kukamatwa, kufungwa na wengine kuuawa Heinz alibuni mpango wa kuyasafirisha madawa haya kupitia mkondo wa kofia ya dini! Alielewa mizigo ya Wamisionari haikukaguliwa bandarini au katika viwanja vya ndege na wala haikutozwa ushuru.
Ulikuwa ni mpango wa muda mrefu sana kuutekeleza lakini ilikuwa ni lazima afanyike baada ya miaka mingi. Heinz alikuwa baba wa watoto wawili wa kike na mwingine wa kiume, wa kike aliitwa Patricia na wa kiume aliitwa Karl ni huyo ndiye aliyetegemewa kuja kuwa mrithi wa maliz zote za Heinz Luminie.
“Nitahakikisha siku moja Karl anakuwa mfanyabiashara wa madawa kwa kupitia kofia ya dini!” Aliwaeleza wanachama wa Mafia katika mikutano yao.
“Utalifanyaje hilo?”
“Nitamlea katika mzingira ya kidini, nitampeleka katika shule za Biblia ili aje kuwa mhubiri maarufu duniani ni yeye atayesafirisha mizigo yetu yote kokote duniani na hakuna mtu atakayegundua jambo hilo!” Aliongea kwa uhakika Heinz.
“Inawezekana fanya basi!”
****
Katika umri wa miaka 12 tu Karl alipelekwa katika chuo cha Berlin Theological Institute kusomea mambo ya dini, yote hayo yalifanyika kumwandaa kuja kuwa mwinjilisti wa kimataifa. Karl aliwashangaza walimu wake kwa uwezo aliokuwa nao darasani, alisoma kwa bidii kubwa na kufanya vizuri sana katika masomo yake yote.
Pamoja na hayo Karl hakupenda kuwa Mwinjilisti, katika maisha yake alitaka sana kuwa Mwanasheria au daktari lakini sababu baba yake alimlazimisha kusoma masomo ya Uinjilisti hakuwa na la kufanya zaidi ya kukubali na kila siku aliyakumbuka maneno ya baba yake.
“Unasoma Uinjilisti si kuwa Mwinjilisti bali kutimiza kazi fulani ambayo nitakuja kukupatia baadaye maishani, kazi ambayo siku zote itakufanya kuwa tajiri kuliko binadamu yeyote!”
“Sawa baba lakini kazi gani hiyo?”
“Siwezi kukuambia sasa hivi soma kwanza na ni lazima uifanye vinginevyo utauawa!”
“Nitauawa? Kazi gani hiyo baba mimi napaswa kuifahamu!”
“Haiwezekani kuifahamu sasa hivi!”
Maongezi hayo kila siku yalimsumbua Karl akilini mwake na kwa sababu ya kuogopa kuuawa alisoma kwa bidii.
****
Akiwa na umri wa miaka 23 Karl alifanikiwa kumaliza masomo yake ya teolojia na kupata digrii zake tatu, jina lake likabadilika akawa Dr Karl Heinz!
Ilikuwa ni furaha kubwa mno kwa baba yake, alijua mtoto wake kumaliza masomo hayo kulimaanisha kazi yake kukamilika, alikuwa na uhakika dawa za kulevya aina ya Cocaine, Heroine na Mandrax ambazo kundi la Mafia lilisambaza zingefika mbali sana duniani bila mtu kukamatwa au kutiliwa mashaka na hivyo wangetajirika kupita kiasi.
****
Ulikuwa ni wakati wa kiangazi katika jiji la Berlin, jua la kawaida lilitawala angani na kuufanya mji kutokuwa na baridi hata kidogo, hali hiyo ilimfurahisha karibu kila mkazi wa jiji hilo lenye baridi. Jioni hiyo Karl alikaa na baba yake ndani ya chumba kidogo chenye mwanga duni, walikuwa wawili tu ndani ya chumba hicho! Dada yake Patricia alikuwa shuleni na mama yake alishafariki miaka kumi kabla ya siku hiyo kwa kuzama na boti baharini alikokwenda kuogelea wakati wa Sikukuu ya pasaka.
Mzee Heinz alimwita mtoto wake ili kumweleza ni kwanini alimlazimisha kwenda kusomea Uinjilisti! Karl pia alikuwa na nia sana ya kulifahamu jambo hilo kwani kwa muda mrefu alimuuliza baba yake lakini hakupewa jibu hiyo ilikuwa siku aliyoisubiri kwa hamu kubwa!
“Mwanangu Karl!” Alianza mzee Heinz na maongezi yao yalifanyika katika lugha Kijerumani.
“Ndiyo baba!”
“Leo nataka nikueleze kitu ambacho hukuwahi kukisikia na kama ulishakisikia basi haukuwa na uhakika, nataka nikueleze ni kwanini niliamua usomee Uinjilisti!!”
“Nakusikia baba!” Karl Aliendelea kumwitikia baba yake.
“Tafadhali niahidi kuwa siri nitayaokueleza hapa hautaisema mahali popote!”
“Nakuahidi baba!”
”Mwanangu mimi ni mwanachama wa Mafia na biashara yangu ni madawa ya kulevya!”
Moyo wa Karl ulipasuka paa na mapigo kubadilika, alianza kuhisi jasho likimtoka kwani hakuwahi hata siku moja kufikiri kuwa baba yake aliyeonekana mpenda dini angeweza kuwa mwanachama wa kundi hilo hatari la wauaji.
“Baba unasema kweli?”
“Ndiyo mwanangu na hutakiwi kusema kwa mtu yoyote ukisema tu utauawa wanachama wenzangu watakunywa damu yako!”
“Ndiyo nimekusikia baba sasa ni kwanini ulinipeleka kusoma Uinjilisti?”
“Nilitaka uje kufanya hii kazi ninayoifanya!”
‘Kazi ya kuuza madawa?”
“Ndiyo!”
“Siwezi baba mimi sasa namfahamu Mungu siwezi kufanya biashara hiyo!”
“Karl!Karl! Karl! Unakaidi maagizo yangu?” Alisema mzee Heinz akiwa amepandisha hasira yake kupita kiasi.
“Siyo hivyo baba nasema ukweli wangu!”
Hapakuwa na maelewano kati yao na walitoka chumbani bila kufikia muafaka. Jioni ya siku iliyofuata Karl akitembea mjini alikamatwa na watu wasiojulikana akafungwa kitambaa machoni na kupelekwa mahali kusikojulikana ambako alipewa mateso ya kutikiswa na umeme kwa usiku mzima na kulipokucha asubuhi baba yake alifika na kuongea naye tena, Karl alikubali kuifanya kazi hiyo.
Wiki mbili baadaye shirika la Global Outreach Mission lilianzishwa nchini Ujerumani, mwinjilisti kijana Karl Heinz mwenye umri wa miaka 23 akawa kiongozi wake, kwa siri kubwa shirika hilo lilifadhiliwa kila kitu na kundi la mafia! Lengo la kundi hili kwa nje lilikuwa ni kuzunguka dunia nzima kuhubiri dini lakini kwa ndani lilikuwa shirika la kusambaza madawa ya kulevya duniani.
Ratiba za safari za shirika hilo zilipangwa na kundi la Mafia, Karl Heinz alisafiri kwenda katika nchi ambazo Mafia walitaka kupeleka madawa yao. Hakuipenda kazi hiyo lakini ilibidi aifanye kwa sababu aliogopa kuuawa! Alifundishwa jinsi ya kuushika unga wa Cocaine katika mikono na kuwagusa watu puani wakati wa maombi ili walewe madawa na kuamini alikuwa na miujiza ya Mungu.
Alifundishwa pia kuchukua kitambaa na kukipaka unga wa dawa aina ya Heroine kalina alipompiga mtu na kitambaa hicho usoni alilewa na kuanguka chini na aliponyanyuka alikuwa na furaha isiyo kifani sababu ya madawa hayo kulevya.
Mambo hayo yalimpa sifa kubwa Mwinjilisti kijana Dr.Karl Heinz na kufahamika dunia nzima, kila alikokwenda kuhubiri maelfu ya watu walikusanyika kumsikiliza, katika kila nchi aliyokwenda ilikuwa ni lazima ndege mbili za madawa ya kulevya zimfuate na kushusha mizigo usiku, hakuna mtu aliyetilia mashaka wala kufuatiliwa wengi waliamii ilikuwa ni misaada aliyogawa kwa wasiojiweza.
Karl Heinz aliheshimiwa mpaka na viongozi wa serikali katika nchi nyingi duniani, alikaribishwa Ikulu katika kila nchi aliyokwenda na kula chakula na Marais, aliwapa viongozi wa Afrika pesa nyingi kwa ajili ya maendeleo lakini hakuna mtu aliyeijua siri ya utajiri wake.
Kilichowashangaza watu waliosafiri naye ni kitendo cha kila mtu aliyeteuliwa kuwa msaidizi wake kuchanganyikiwa na kuwa mwehu baada ya kufanya kazi kwa kipindi kirefu na baadaye kukutwa amekufa! Hapakuwepo na maelezo ya kutosha kuhusu vifo vyao, wasaidizi karibu wanne walishakufa kwa mtindo huohuo na Patrick ndiye msaidizi wake wa tano!
Siri ya vifo hivyo vya wasaidizi hao hakuna aliyeielewa isipokuwa Mwinjilisti Karl Heinz mwenyewe, ukweli ni kwamba aliwaua baada ya kuigundua siri yake ya madawa na kuanza kuhoji! Aliwapulizia dawa aina ya Pedraxone iliyowachaganya akili na kuwatia wehu na baada ya hapo aliwatilia sumu katika chakula na kuwaua! Karl Heinz hakutaka hata siku moja siri yake igundulike.
*****
“Nimefurahi sana kukutana na wewe mtumishi wa Mungu!” Alisema Patrick huku akitabasamu na alisema hayo kwa kutokujua ubaya wa Dr Karl Heinz, alikuwa mnyama na mkatili lakini dunia haikuelewa na haikuwa rahisi hata siku moja kulifahamu jambo hilo kwa sababu Mwinjilisti Karl alijificha chini ya mwavuli wa dini!
“Unaweza kutunza siri lakini kijana?”
“Naweza mtumishi wa Mungu!”
“Tafadhali kumbuka hutakiwi kusema chochote cha ajabu utakachokiona sawa?”
“Sawa mtumishi wa Mungu!” Aliitikia Patrick.
*****
Wodini:
“Blandina hivi hauna pesa kidogo tukanunue angalau chupa kadhaa za dripu wakati tunasubiri dawa zetu zifike?” Muuguzi alimuuliza mwenzake.
“Ninayo shingili 5000 na tunaweza kuitumia tu!”
“Basi acha mimi nikaongee na daktari ili tununue maji kwenye duka la dawa vinginevyo hata hawa nao watakufa!’
Baada ya kusema maneno hayo muuguzi alitoka mbio kuelekea ofisini kwa daktari lakini kabla hajafika alikutana na wauguzi wengine wakikimbia kuelekea katika chumba alichotoka muuguzi huyo.
“Vipi hali za wagonjwa?”
“Ni mbaya sana sista, nilikuwa nakwenda kumwomba daktari tukanunue angalau maji ya dripu kwenye duka la dawa!”
‘Hapana twende tu wodini dawa zimeshakuja!”
Walisaidiana na kuanza kutembea kwa haraka kurudi tena wodini ambako walimkuta Nancy na Anne katika hali mbaya kupita kiasi, walitundika chupa za maji na kuzichomeka katika mshipa yao ya damu zikaanza kutiririka kwa kasi kubwa ili kufifia maji yaliyopotea miilini mwao.
Kila chupa ilipoisha ilibadilishwa na dawa walizopewa kwa mdomo na kuzitapika zilianza kupitishwa katika mishipa ya damu, kwa masaa arobaini na nane ya kutumia maji na dawa hali zao zilianza kubadilika na kuwa nzuri, ngozi zao zilianza kupendeza na kujaa badala ya kusinyaa! Fahamu zilianza kuwarejea akilini.
Siku ya tatu Nancy alipopata nguvu vizuri alijigeuza na kuagalia upande wa pili wa kitanda chake, alikutanisha macho na sura ya mama yake akimwangalia na kutabasamu!”
“Nancy mwanangu!”
“Naam mama!”
“Tumenusurika na kifo kwa uwezo wa Mungu!”
“Kweli mama, wenzetu wote wamekufa!”
“Umejuaje?”
“Nilisikia kwa mbali manesi wakiongea!”
Hawakuweza kuongea sana siku hiyo sababu miili yao haikuwa na nguvu za kutosha lakini siku ya tano wakiwa wodini walikuwa wazima kabisa, hawakuharisha wala kutapika tena, kila mtu hospitali alishangazwa na muujiza uliotokea.
*****
Mama ilikuwaje ukawa mzima wakati hata kaburi lako tuliliona nani alikufa?”
“ Sikufa mimi alikufa rafiki yangu Zena, alijichoma sindano ya sumu!”
Pamoja na kuwa Anne kufurahi sana kutana na Nancy, bado alitaka kufahamu ni wapi alikokuwa mtoto wake wa kiume Patrick, alipojibiwa kuwa Patrick alikufa, alidondosha machozi ya huzuni.
******
Siku ya sita maaskari wa magereza walimfunga Anne pingu zake mikononi na safari ya kuelekea gereza la Segerea iliendelea, Nancy ilibidi aungane nao katika safari moja. Walipoingia Dar es Salaam Anne alipelekewa moja kwa moja gerezani Segerea, ambako alipokelewa kama mfungwa lakini kote huko Nancy alifuata kwa nyuma.
“Mwanangu Nancy utakwenda wapi sasa?”
“Sitaki kuondoka nataka nikae na wewe mama!” Alisema Nancy huku akilia machozi.
“Huwezi kukaa na wewe mimi gerezani mwanangu!” Alijibu Anne na kuanza kuvutwa na maaskari kuingizwa gerezani.
“Mama!Mama! Mama!” Aliita Nancy.
Nancy alikaa chini na kuanza kulia hakujua aende wapi baada ya kutoka gerezani, alitembea hadi barabarani ambako alisimama na kuanza kulia machozi, njaa ilimuuma kupita kiasi na hakujua angepata wapi chakula cha mchana huo.
Ghafla aliona gari dogo aina ya Pickup likija mbele yake, Nancy alisogea hadi katikati ya barabara na kuanza kulisimamisha,gari hilo.
“Shikamoo dada!” Nancy alimwamkia mwanamke aliyekuwa akiendesha gari hilo liliposimama na baadaye alimwamkia mwanaume aliyekaa upande wake wa kushoto!
“Naomba shilingi mia nikale nina njaa dada!”
“Baba Teddy una mia tano hapo?” Mama huyo alimuuliza mwanaume aliyeonekana kuwa mumewe aliyekaa pembeni akisoma gazeti la Amani.
“Sina darling nina kubwakubwa tu!”
“Ingia kwenye gari twende pale mbele ukale hotelini!” Mama yule alisema na Nancy alianza kupanda nyuma ya gari hilo.
“Hapana njoo ukae huku mbele!” alisema mwanaume huyo na kufungua mlango, Nancy akaingia na kukaa katikati yao.
“Mimi naitwa mama Teddy na huyu ni mume wangu anaitwa Kidubo wewe unaitwa nani binti!”
“Ninaitwa Nancy!”
“Jina zuri sana unakaa wapi hapa Segerea?”
“Mimi ni mgeni!”
“Mgeni kutokea wapi?”
Alipoulizwa swali hilo Nancy alianza kulia machozi na baadaye kusimulia kila kitu kilichotokea katika maisha yake, hakusahau kueleza juu ya mama yake aliyeingia siku hiyo hiyo gerezani Segerea.
“Pole sana, je umeokoka?”
“Hapana ila natamani sana kuwa hivyo!”
“Twende basi ukale tutakusubiri twende kwenye mkutano wa dini, kuna mhubiri mmoja anaitwa Karl Heinz kutoka Ujerumani anahubiri vizuri na tukitoka huko tutakuja nyumbani kwetu utaishi na sisi sawa?”
“Sawa dada!”
Walimpeleka hotelini akala na baadaye wakaondoka kwenda jangwani kwenye mkutano, watu walikuwa wengi sana siku hiyo kwa sababu ndiyo ilikuwa siku ya mwisho ya mkutano! Mama Teddy, Kidubo na Nancy walisimama nyuma kabisa na haikuwepo nafasi ya kusogea mbele zaidi! Walianza kusikiliza mkutano hadi mwisho mambo yote yalioongelewa katika mkutano huo yalimgusa Nancy na alilia karibu muda wote wa mahubiri hayo.
“We have only three minutes to be in Dar es Salam, let me introduce to you my new tour assistant, I met this boy here yesterday and I’m going to be travelling with him wherever I go, his name is Patrick!”(Tuna dakika tatu tu za kuwa hapa Dar es Salaam, acha nimtambulishe kwenu msaidizi wangu mpya wa safari, ni kijana niliyekutana naye hapa jana na nitasafiri naye kila niendako jina lake anaitwa Patrick!)
Patrick alipunga mkono wake hewani na sekunde chache baadaye wote walianza kuteremka jukwaani na kuingia katika magari tayari kwa safari ya kuelekea Zambia.
Nancy aliposikia jina Patrick alishtuka na kuacha kulia, alipoangalia mbele yake jukwaani, hakuamini macho yake alipomwona Patrick akipunga mkono hewani.
“PATRIIIIIIIICK!” Alipiga kelele na kuchomoka akaanza kukimbia kwenda mbele akipita katikati ya watu lakini alipofika kwa Anne magari tayari yalishaanza kuondoka, alipaza sauti akiita jina la Patrick huku akiyakimbiza magari hayo!

Je nini kitaendelea?
Je, Nancy atafanikiwa kumpata kaka yake?
Na je nini kitampata Patrick kwa Mwinjilisti karl?
 
Back
Top Bottom