JanguKamaJangu
JF-Expert Member
- Feb 7, 2022
- 3,177
- 7,472
Stendi ya makumbusho ni kati ya Stendi ambazo zimekuwa zikipokea daladala nyingi kutoka maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es salaam, lakini stendi hiyo imekuwa ikipoteza hata ubora mdogo iliyokuwanao awali, ambapo kwa sasa imechakaa na imekuwa kero kwetu madeleva wa daladala.
Licha ya daladala zinazoingia kwenye stendi hiyo kutozwa tozo ambayo kati ya matumizi yake ni pamoja na kuboresha miundombinu ndani ya Stendi, usafi na usalama, lakini kwa sasa miundombinu imekuwa chakavu na hakuna maboresho yoyote yanafanyika wala ambayo tumeshuhudia kwa kipindi cha hivi karibuni.
Stendi imejaa mashimo na hakuna mpagilio wa magari unaoeleweka, maji machafu yamejaa kwenye mashimo mpaka yanatoa harufu, stendi imekuwa kama haina wasimamizi licha ya kuingiza pesa nyingi kulingana na daladala zinazoingia.
Maeneo maalum kwa abiria kuketi wakiwa wanangojea magari nayo yamechakaa mvua ikinyesha ndio majanga kabisa, abiria wanakimbilia kwenye maduka ya watu au kwenye magari.
Sijui nani amepewa mamlaka ya kusimamia stendi hiyo ya daladala naona kama wameshindwa, lakini wito wangu kwa Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni lazima wawajibike katika hilo maana stendi hiyo ipo kwenye eneo lao la kiutawala, maana tunajiuliza tozo tunazokatwa zinaenda wapi?