Unafiki wa Sitta Ulianza kipindi cha Nyerere kakachapwa viboko
Mjumbe huyo wa NEC na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga aliyejipambanua kupiga vita ufisadi na vitendo viovu ndani na nje ya CCM, alisema historia ya Waziri Sitta inajionesha wazi kwamba ni 'mkorofi na msaliti mkubwa', kwani mwaka 1966 akiwa mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam alishiriki maandamano hadi Ikulu kupinga sheria ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT).
Alisema katika harakati zao hizo za kupinga sheria hiyo iliyotaka kila mwanafunzi wa Chuo Kikuu lazima ajiunge na Jeshi la Kujenga Taifa, Baba wa Taifa wakati huo akiwa Rais wa nchi na mkuu wa chuo hicho, alilazimika kumchapa viboko Sitta kutokana na usaliti wake huo kwa serikali.
Mgeja alisema mbali na kufanya maandamano hayo, Sitta na wenzake ambao wengine ni marehemu kwa sasa walikuwa na mabango yenye ujumbe mkali kwa serikali, ukiwemo uliosema 'Onyo kali na la mwisho kwa serikali', na kwamba alikuwa akiipinga pia Serikali ya Baba wa Taifa huku akiusifu uongozi wa kikoloni.
"Huyu Sitta ambaye leo hii anawadanganya watu, kipindi hicho akisoma Chuo Kikuu alikuwa akiipinga serikali na kudai afadhali serikali ya kikoloni. Tusipoamini leo usaliti wake huu tunasubiri hadi aje shetani atuambie usaliti wa Sitta ndipo tuamini?