Simulizi ya Uwanja wa Mauaji

Chachasteven

JF-Expert Member
Jul 4, 2014
1,878
1,849
SEHEMU YA 1
Nilikamatwa na maaskari majira ya saa sita mchana kwenye mgahawa wa ENO. Nilikuwa nakula mayai huku nikinywa kahawa. Unaweza kuita kifungua kinywa kilichochelewa, kwa sababu ndiyo kwanza nilikuwa natia kitu mdomoni kwa hivyo sio sahihi kusema ni chakula cha mchana. Nilikuwa nimelowa tepe tepe na mchovu baada ya kutembea kwa mwendo mrefu kwenye mvua kubwa nikitokea kati kati ya mji hadi nje kidogo ya jiji.
Mgahawa wenyewe ulikuwa mdogo, lakini mwanga uliokuwa mule ndani ulipafanya pang’ae na kupendeza. Nilikadiria ungekuwa umejengwa muda sio mrefu sana. Meza za kulia vyakula vikiwa mbele, pembeni kulia na kushoto na jiko likiwa kwa nyuma.

Mimi nilikuwa nimekaa dirishani kushoto, nikisoma gazeti nililolikuta pale mezani kipindi naingia lililokuwa likinadi kampeni za Rais ambaye sikumpigia kura wakati wa uchaguzi mkuu uliopita na sikuwa na mpango wa kumpigia kura wakati huu pia. Nje, mvua ilikuwa tayari imeshakata ila vioo vilikuwa vimefunikwa na manyunyu na ukungu kiasi lakini haikuzuia macho yangu kuziona gari mbili za polisi zilipowasili mgahawani hapo na kuegeshwa. Muda kidogo tu baada ya gari hizo za polisi kuegeshwa, milango ikafunguka na polisi wawili wawili wakatoka kwenye kila gari kwa kasi na wepesi huku silaha zao zikiwa tayari. Bunduki mbili kubwa mkononi, bunduki mbili ndogo mkononi. Hizi zilikuwa ni silaha nzito ukiniuliza. Mwenye bunduki ndogo mmoja akajiunga na mwenye bunduki kubwa mmoja wakakimbilia upande wa mlango wa nyuma wa Mgahawa.

Nikabaki nimekaa nawatazama tu. Nilikuwa najua kila aliyekuwemo Mgahawani mule. Mpishi mmoja nyuma jikoni. Wahudumu wa kike wawili. Wazee wawili. Na mimi. Hivyo ilikuwa wazi kuwa Operesheni ambayo ilikuwa ifanyike na maaskari hawa Mgahawani hapo haikuwa ya mtu mwingine bali ya kwangu. Ni mimi ndiye nilikuwa nimeingia hapo Mgahawani muda sio mrefu nikitokea mjini. Hawa wengine, pengine nusu ya uhai wao wameitumia wakiwa ndani ya mgahawa huu na kama Askari polisi wangekuwa na shida na mmoja kati yao, basi ujio wa askari ungekuwa ni ule wa kistaarabu na upole. Wasingekuja wamebeba mabunduki. Wangekuja wakamchukuwa yule ambaye wanamuhitaji kimya kimya bila silaha. Kwa hivyo zile kasi za wale askari na mabunduki vilikuwa ni kwaajili yangu. Hilo lilikuwa halina ubishi.
Nilichukua yai langu lililokuwa limebaki nikalibugia lote mdomoni halafu nikatoa noti ya shilingi elfu 5 nikaiweka mezani. Nikalikunja kunja lile gazeti nililokuwa nalisoma nikalidumbukiza kwenye mfuko wa jaketi langu. Niliinywa kahawa iliyokuwa imebaki kwenye kikombe changu halafu nikaweka mikono yangu juu ya meza.

Wale askari wawili waliopitia mlango wa mbele wakagawana majukumu. Yule mwenye bunduki kubwa akasimama mlangoni. Akaielekeza bunduki yake usawa wa kichwa changu.Yule mwenye bunduki ndogo akawa ananisogelea karibu. Kimuonekano walionekana ni wazee wa kazi. Na nyendo zao zilikuwa makini kama tu inavyoelekezwa kwenye vitabu vya mafunzo ya mapigano na matumizi ya silaha. Ile bunduki ya mlangoni ingeweza kuhakikisha inapiga popote ndani ya kile chumba cha mgahawani. Na ile ambayo ilikuwa inakuja karibu yangu ingeweza kusanisambaratisha ubongo wangu ukatapakaa kwenye vioo vya madirisha ya mgahawani humo. Pia upande wa nyuma usingekuwa sahihi kutumia ili kukimbia. Lingekuwa ni kosa. Ile bunduki ndogo ingenikosa lakini bunduki kubwa isingeniacha salama, risasi moja tu ingeua watu wawili. Mimi na yule afisa aliyesogea kuniweka chini ya ulinzi. Mpaka hapo walikuwa wanafanya vizuri. Hakuna ubishi juu ya hilo. Bahati ilikuwa upande wao. Hakuna ubishi juu ya hilo pia. Udogo wa ule mgahawa haukuwa unaniruhusu kufanya jambo lolote hivyo niliituliza mikono yangu mezani. Yule askari alikuwa amefika karibu yangu.

“Tulia! Polisi!” Aling’aka.

Alikuwa ni kama anaepiga kelele kwa nguvu kadri alivyoweza. Nadhani ili kuondoa uwoga ndani yake na kwa wakati huo huo kunitishia nishtuke. Miondoko ya kwenye vitabu. Kelele nyingi ili umtulize na kumtisha mhalifu. Nilinyoosha mikono yangu juu. Yule askari akasogea karibu. Karibu sana. Kosa lao la kwanza. Kama ningetaka, Ningempiga mkono na kuuelekeza juu. Risasi moja ingepiga ceiling board halafu akiwa anazubaa ningemchapa kiwiko cha uso, kufumba na kufumbua bunduki yake ingekuwa mikononi mwangu. Yule askari wa mlangoni asingefanya chochote kwa sababu alikuwa ameshusha kidogo bunduki yake kwa hivyo hata ningefanya hayo yote asingeruhusu risasi itoke kwenye bunduki yake kwani ingeishia tu kumdunda mwenzie. Siku yao ingeisha vibaya sana. Lakini licha ya hayo yote, nilikaa tu hapo nikiwa nimenyoosha mikono juu. Huyu jamaa mwenye bunduki ndogo alikuwa bado anapiga makelele yake.

“Inuka ulale sakafuni” Alinishtua.

Nilitoka taratibu nilipokuwa nimekaa nikainyoosha mikono yangu kuelekea alipo. Sikuwa tayari kulala chini tena mbele ya viaskari polisi. Isingetokea kwa bahati mbaya hata kama wangekuja na idara yao nzima ya mapigano na mabunduki juu.

Jamaa alielewa, hivyo akaichomoa pingu iliyokuwa kwenye mkanda wake akanifunga mikono. Wale askari wawili waliokuwa nyuma wakaingia ndani punde tu baada ya mimi kufungwa pingu. Wakatembea hadi nyuma yangu na kuanza kunipiga parapata. Nikamuona Askari aliyenifunga pingu akitingisha kichwa kama kukubaliana nao jambo kuwa sikuwa na silaha. Akili yangu ikaniambia Askari yule ndiye alikuwa kiongozi wao.
Alikuwa fiti. Umri kama wa kwangu. Baji aliyokuwa amevaa kwenye shati yake ilimtambulisha kwa jina la PUGU. Alinizunguka halafu akanitazama machoni.

“Upo chini ya ulinzi kwa kosa la mauaji,” Aliniambia “Unayo haki ya kubaki kimya. Jambo lolote utakalolisema linaweza likatumika kama ushahidi dhidi yako. Pia unayo haki ya wakili. Kama utashindwa kumudu gharama za wakili binafsi, serikali itakupatia mmoja wa kukuwakilisha bila ya gharama zozote. Umenielewa??”

Njia nzuri ya kufikisha ujumbe. Aliongea kwa ufasaha. Hakuwa anayasoma maneno hayo kutoka kwenye karatasi. Aliyaongea ni kama mtu aliyekuwa anajua anamaanisha nini na yana umuhimu kwa kiasi gani kwake na kwangu. Sikujibu chochote.

“Umezielewa haki zako?” Alirudia tena kuuliza.

Kama mwanzo, Mimi pia sikujibu chochote. Uzoefu wa muda mrefu ulikuwa umenifundisha kitu muhimu sana maishani. Ukimya ndiyo njia sahihi. Ropoka jambo, watu wanaweza wakusikie vibaya. Usieleweke. Utafsiriwe ndivyo sivyo. Inaweza ikufanye uonekane una hatia. Na mbaya zaidi inaweza ikasababisha ukauliwa. Hata hivyo, kukaa kimya huwa kunawakera sana askari. Ni wajibu wake kukuambia kuwa unayo haki ya kukaa kimya lakini anachukia pindi unapoitumia hiyo haki yako. Mimi nilikuwa nimewekwa chini ya ulinzi kwa kosa la mauaji lakini sikuwa tayari kusema chochote.
“Unazielewa haki zako?” jamaa mwenye jina la Pugu aliniuliza tena. “Unaongea Kiswahili?”

Sikusema chochote. Akatulia. Alitulia kama mtu ambaye wakati wake wa hatari ulikuwa umekwisha kupita. Kwanza kwanini ajali, maana angenipakia kwenye gari tukaenda kituoni halafu nikawa mzigo wa mtu mwingine. Aliwaangalia wenzie.

“OK, andika hajasema chochote,” Alilalama. “tuondoke”.

Tulianza kutembea kuelekea ulipokuwa mlango. Tuliunda mstari mmoja ili tupite vizuri kulingana na udogo wa mlango. Alianza Pugu. Halafu jamaa mwenye bunduki kubwa, akawa anatembea kinyume nyume huku bunduki yake akiwa kaiweka tayari kunifyatua kichwa. Baji yake ilimtambulisha kama Stevenson. Alikuwa fiti. Mweupe. Nyuma yangu walisimama wale askari wawili waliokuwa nyuma ya mgahawa. Ghafla nikasukumwa kwa nguvu kutoka nje ya mlango.

Nje, eneo la maegesho joto lilikuwa juu. Lazima mvua ingekuwa imenyesha usiku wote na asubuhi yote. Ni sasa hivi jua ndiyo lilikuwa linachomoza na ardhi ilikuwa inatoa mvuke. Kikawaida, hapa pangekuwa na vumbi sana. Lakini leo palikuwa panatoa mvuke baada ya mvua kunyesha na kusafisha mazingira na kuyafanya yawe ya kuvutia sana. Nililiangalia jua halafu nikavuta hewa nyingi sana kwenda ndani. Nilijisikia vizuri. Kumuona Stevenson bado yupo mbele yangu na bunduki yake kuliirejesha akili yangu kwenye tukio lililokuwa mbele yangu. Nilishtukia kichwa changu kinabonyezwa kwenda ndani ya mlango wa gari wa nyuma halafu nikasukumwa kuingia ndani. Miondoko ya kwenye vitabu. Si ajabu sana kwa sababu kwenye mji ulio mbali na sehemu yoyote ya mjini, unategemea kuona nini zaidi ya nadharia nyingi kuliko vitendo.?

Milango ililokiwa nikawa mwenyewe nyuma ya gari. Pugu na Stevenson walikuwa siti za mbele. Stevenson akageuka ili kunitazama kwa ukaribu. Hakuna aliyemuongelesha mwenzake. Pugu alianza kuendesha gari. Nyuma yetu gari la wale askari wengine wawili nao walianza kutufuata. Gari zilikuwa mpya. Safi na nzuri kwa ndani. Hakukuwa na alama au viashiria kuwa watu wengi sana walikuwa wamekwishaipanda na kukalia kiti nilichokuwa nimekalia.

Niliangalia nje ya dirisha. Geita. Niliiona ardhi tajiri. Ardhi nyekundu iliyozungukwa na vichaka na miti miti kama katani. Yalikuwa mananasi au majaruba ya mchele labda. Si mengi sana, ila naamini yana manufaa sana kwa mpandaji au mmiliki. Ni watu ndiyo walikuwa wamiliki halali wa ardhi? Au makampuni? Sijui.

Safari yetu haikuwa ndefu sana kuelekea mjini. Baada ya dakika kama 20 nilianza kuona majengo mawili makubwa mapya. Moja likiwa ni kituo cha polisi na lile la pili likiwa ni makao makuu ya zima moto kwa mkoa. Yalikuwa yanavutia. Majengo mazuri katika bajeti ndogo. Bara bara zilikuwa zinavutia. Takribani kama hatua thelathini kusini niliona jengo jeupe kama kanisa kwa sababu lilikuwa na msalaba kwa juu. Nyuma yake kulikwa na majengo kadhaa. Kila kitu kilivutia kutazama. Jamii iliyoendelea iliyojengwa kutokana na kodi za wananchi. Safi.

Stevenson alikuwa bado ananiangalia kipindi ambacho Pugu alikuwa analiingiza gari kwenye maegesho ya kituoni hapo. Niliangalia kushoto nikaona ubao mpana uliosomeka : Kituo Kikuu Cha Polisi Geita. Nikajikuta nawaza: Hivi natakiwa kuogopa? Nipo chini ya ulinzi kwenye mji ambao sijawahi kuwepo hapo kabla katika maisha yangu yote. Tena kwa kosa la mauaji. Ila nikiwa nawaza nikajifariji tena. Kwanza, hawawezi kuthibitisha kuwa jambo limetokea na wakati halijatokea. Na pili, Sikuwa nimeua mtu kwa muda mrefu sasa.

Kusoma sehemu ya pili bonyeza HAPA.
 
Kama wewe msomaji ni mpenzi wa riwaya usijaribu kujitupia kusoma riwaya za humu. Utasikia itaendelea ndio mazimaaa
 
SEHEMU YA 2



Baada ya gari zote kusimama. Pugu alishuka na wale askari wa gari la nyuma yetu walishuka pia kuja lilipokuwa gari lililokuwa limenibeba. Stevenson naye alishuka akasimama karibu na Pugu na kuelekezea bunduki yake dirishani nilipokuwa nimekaa. Ushirikiano mzuri. Pugu alifungua mlango wangu.

“Haya, twende, twende.” Aliniambia kwa sauti ya chini kama mtu anayenong’ona jambo. Nilijivuta kidogo halafu nikatoka ndani ya gari. Wale askari wawili wakaja nyuma yangu na kuniongoza pa kwenda kama vile nilikuwa sioni. Tulipofika kwenye mlango, Pugu aliuvuta ukafunguka. Nikaingizwa ndani halafu akaufunga baada ya kuingia.

Ndani palikuwa pazuri. Taa zilizomulika chumba kizima na kukifanya king’ae. Hiki kituo hakikuwa kinafanana na mara ya mwisho nilipotembelea kituo cha polisi miaka 14 iliyopita. Hiki kilikuwa na muonekano kama wa benki au taasisi kubwa ya kifedha. Kulikuwa na maru maru. Askari wa zamu alikuwa amesimama nyuma ya dawati la mapokezi. Kwa jinsi mule ndani palivyoonekana alipaswa kuniuliza: Nikusaidiaje, mheshimiwa?? Lakini hakusema jambo. Alikuwa ananitazama tu. Nyuma yake kulikuwa na nafasi kubwa iliyo wazi isipokuwa kulikuwa na askari wa kike ambaye muda wote alikuwa bize na Kompyuta yake kama mtu anayeingiza taarifa f’lani. Stevenson alizunguka hadi nyuma ya dawati la mapokezi huku bunduki yake akiwa bado kaielekeza kwangu. Pugu alikuwa kasimama tu ananiangalia. Yule askari wa nyuma ya dawati la mapokezi naye alikuwa bado ananiangalia. Kidogo hivi na yule askari wa kike pia akaanza kuniangalia. Hakuna aliyemsemesha mwingine. Na mimi nilianza kuwaangalia.

Ghafla wale askari wawili waliniongoza kuelekea kwenye chumba jirani mkono wa kushoto. Pugu alifungua mlango halafu nikasukumwa kuelekea ndani na yeye aliingia. Kilikuwa ni chumba cha mahojiano. Hakuna madirisha. Kulikuwa hakuna kitu zaidi ya meza moja nyeupe, viti vitatu na kamera moja kwenye kona moja ya ukuta. Hali ya hewa ya kwenye chumba hicho iliwekwa kuwa ya baridi. Mimi pia nilikuwa bado nimelowa mwili kwa ile mvua.

Nilisimama huku Pugu akinikagua kwenye kila aina ya mfuko kwenye nguo zangu. Kila kitu kilichokuwa mifukoni mwangu kilichukuliwa kikawekwa juu ya ile meza. Pesa kidogo za noti na vichenji chenji. Tiketi za mabasi na uchafu mwingine. Pugu aliliangalia lile gazeti nililokuwa nimelikunja kunja akarirudisha mfukoni mwangu. Aliitazama saa yangu niliyokuwa nimevaa akaiacha kama ilivyo. Hakuwa na shida nayo! Vingine vyote alivyoviweka juu ya meza alivikusanya na kuvipakia kwenye mfuko. Mfuko uliokuwa umetengenezwa maalum kwaajili ya watu ambao hubeba vitu zaidi ya nibebavyo mimi. Kulikuwa na kikaratsi cheupe kwenye ule mfuko ambapo Pugu alichukua kalamu akaandika namba f’lani.

Pugu aliniambia nikae chini. Baada ya kukaa chini, yeye na wale askari wawili waliondoka na ule mfuko ambao waliwekea vitu vyangu humo. Waliufunga mlango kwa nguvu halafu nikasikia sauti ya ufunguo ukizungushwa ili kuweka loki.

Nikajua nimekwisha. Kuachwa mpweke kwenye chumba bila chochote ni hatari. Mara nyingi huwa inakuwa hivyo. Upweke husababisha utake kuongea. Kuongea kutasababisha utake kukiri kosa. Kama umekamatwa kwa ukali wa makelele halafu ukaachwa mpweke kwa muda wa saa moja ni njia nzuri ya kukufanya uropoke. Hatari sana!

Lakini nilikuwa nimekosea. Hawakuwa wamepanga kuniacha mpweke kwa muda mrefu. Kwangu mimi nililiona kama kosa lao lingine ukijumlisha na lile la Pugu kunisogelea karibu kule ENO. Pugu alifungua mlango akaingia ndani akiwa kashika kikombe cha kahawa halafu akawa katoa ishara ya kumruhusu yule askari wa kike niliyemuona nyuma ya dawati kipindi nimefika aingie ndani. Pugu aliufunga mlango akabaki amesimama ananiangalia.

Yule askari wa kike alitembea kuja nilipokuwa huku amebeba kiboksi kama mkebe wa hisabati japo kilikuwa kikubwa sana. Alipofika karibu na mimi alikiweka mezani halafu akakifungua. Ndani yake kulikuwa na vikaratasi vyenye namba juu yake. Alikitoa kimoja na kunipatia huku akiniangalia kwa jicho la huzuni. Jicho ambalo manesi huwatazama wagonjwa wanaowapenda. Nilikipokea kwa taabu kwa sababu mikono yangu ilikuwa bado ina pingu. Alinipa ishara nikiweke usawa wa kumuangalia wakati akiwa anachukua kamera yake ili kunipiga picha.

Akiwa anatafuta pozi zuri la kuweka kamera ili apate picha nzuri mimi nilikuwa bize naangalia kifua chake. Ni mwanamke wa kupendeza. Nywele zake nyeusi, macho ya mvuto. Nilimwangalia usoni halafu nikatabasamu. Mwanga wa kamera ukawaka. Alikuwa ameshapiga picha yangu na kabla hajasema chochote nilikuwa nimegeuka ubavu ili apige picha ya ubavuni. Mlio wa kamera ukalia na ghafla mwanga ukawaka akawa keshapiga picha ya ubavu pia. Niligeuka kumwangalia nikampatia kikaratasi chake. Alikipokea huku akiguna ule mguno ambao unasema: Ni kweli hili suala linakera lakini ni muhimu na lazima.

Halafu alitoa mashine ya kuchukulia alama za vidole. Pingu zilifanya zoezi liwe gumu kidogo. Pugu alijikausha akajifanya hajui pingu zinaleta shida. Yule askari wa kike alichukua wino na kunipaka vidoleni kisha nikavipachika kwenye karatasi. Baada ya zoezi alinisaidia kufuta wino uliokuwa umebaki vidoleni. Mikono yake ilikuwa laini sana. Na hakuwa na pete ya aina yoyote, Acha ya ndoa. Hata ya urembo hakuwa nayo.

Baada ya kumaliza alirudisha ile mashine na kamera kwenye mkebe wake na kuufunga kama ulivyokuwa kipindi anaingia mwanzo. Pugu alifungua mlango. Yule askari wa kike alichukua mizigo yake na kuanza kuelekea ulipokuwa mlango. Hakuna aliyemwongelesha mwenzake. Yeye akaondoaka tukabaki mimi na Pugu mle ndani ya kile chumba cha mahojiano. Pugu aliufunga mlango halafu akauegemea akawa ananiangalia.

“Mkuu wangu anakuja,” Alisema “tuna tatizo ambalo linahitaji utatuzi na utatakiwa uzungumze naye.”

Sikujibu chochote. Kwanza, Kuzungumza na mimi kusingeweza, kwa namna yeyote ile, kutatua tatizo la mtu yoyote mahali popote duniani. Lakini kwakuwa nilimuona anakuwa mpole na fasaha kidogo basi nikampa mtego. Nilinyoosha mikono yangu kuelekea alipokuwa. Lilikuwa ni ombi bila ya kuzugumza la kumuomba anifungulie pingu. Alisita kidogo lakini akasogea karibu akatoa funguo na kunifungulia na kuzirudisha kwenye mkanda wake. Sikuonesha shukrani yeyote. Sikujifuta mikono yangu pahala popote. Sio kwa sababu nilikuwa sitaki. Hapana! Ni kwa sababu sikutaka mahusiano yeyote na huyu askari. Lakini niliongea

“Sawa,” Nilisema “Twende nikaonane na huyo mkuu wako.”

Kwa mara ya kwanza tokea muda nilioagiza kifungua kinywa kule ENO nilikuwa nimeongea. Pugu alitabasamu kama mtu aliyekuwa anasema Ahsante. Aliufungua mlango akanipa ishara nitoke nje. Nilimuona Stevenson akiwa kasimama nje ya mlango. Sasa hivi hakuwa na bunduki lake. Hata wale askari wawili sikuwaona popote. Mambo kidogo yalikuwa yameanza kuwa shwari. Pugu na Stevenson walijipanga kulia na kushoto kwangu kisha wakaongoza tulipotakiwa kuelekea huko kwa mkuu wao. Tulitembea kuvuka vyumba kama vitatu na hatimaye tulifika. Stevenson aliufungua mlango tukaingia. Kulikuwa na mapambo mengi ya maua. Kwa sekunde kadhaa nilihisi nimeingia duka la mapambo ya ndani.

Jamaa mmoja bonge bonge alikuwa amekaa nyuma ya meza ya mbao iliyokuwa kati kati ya hiko chumba. Nyuma yake kulikuwa na rundo la bendera mbali mbali. Ukutani kati kati ya rundo la zile bendera kulikuwa na saa kubwa ya mshale. Kwa muda mfupi nilioitazama nilihisi itakuwa ina muda mrefu tokea siku walipoinunua kwa mara ya kwanza. Lakini akili nyingine ikaniambia labda mbunifu wa hili jengo aliamua iwe hivyo ili kutia muonekano ambao nilikuwa nauona mbele yangu – Kuamsha hisia ya historia ya jeshi la polisi - na sio kwamba hii saa ilikuwa ya muda mrefu sana tokea inunuliwe. Macho yangu yalibaini kuwa tayari ilikuwa imefika saa sita na nusu.

Yule jamaa bonge alinitazama kadri nilivyokuwa nikizidi kupiga hatua kuelekea ndani. Uso wako ulionesha mshtuko ingawa alijaribu kuuficha lakini haikuwa shida kwangu kulitambua hilo. Alinitazama tena kwa umakini na ukaribu, halafu akaongea kwa mshtuko.

“Kaa chini na ufunge mdomo wako,”

Huyu bonge alikuwa mtu wa ajabu sana. Alionekana kama tahira tu mbele yangu. Tofauti kabisa na kile nilichokiona kwa Pugu na timu yake iliyonikamata kule mgahawa wa ENO. Hata yule askari wa kike aliyenipiga picha na kunichukua alama za vidole alikuwa makini sana. Huyu bonge alikuwa anamaliza nafasi tu. Nywele zake zilikuwa zimekaa hovyo. Alikuwa anavuja jasho, licha ya hali ya kiyoyozi mule ofisini. Alikuwa na uzito uliopitiliza na manyama uzembe. Kwangu, sikuwa namuona kama anafaa kukalia hicho kiti alichokuwa amekalia.

“Jina langu naitwa Simon,” Alinong’ona. Mimi sikuwa nahitaji kumfahamu na wala sikumuuliza. Nilikaa kimya tu kama sijamsikia. “Mimi ndiye Askari kiongozi mkuu hapa Geita. Na wewe ni mjinga mmoja unaevamia mji na kuanza kuua watu hovyo. Umekuja kwenye mji wangu na umeharibu tayari kwenye mali binafsi ya Mzee. Chacha. Lakini sheria huwa haimuachi mtu salama, utatakiwa uonane na mkuu wa upelelezi wa kituo changu na ukiri kila ulichokifanya.”

Baada ya kuongea aliinuka alipokuwa amekaa na kuanza kuniangalia tena kwa ukaribu. Ni kama vile alikuwa ananifananisha au pengine alikuwa anataka nimpatie jibu. Lakini hakuambulia neno lolote kutoka kwangu. Nilikaa kimya tu. Alininyooshea kidole chake.

“Na baada ya hapo unaenda jela,” aliendelea. “Halafu utaninginizwa kwenye kitanzi na mimi nitakuja nijisaidie juu ya kaburi lako.”

Alipomaliza akakaa chini akatazama pembeni kidogo.

“Hili suala ningelifanyia kazi mwenyewe,” alisema tena. “Lakini mimi ni mtu ambaye nipo bize kidogo.”

Alipomaliza kunitisha akanyanyuka tena kutoka kwenye kiti chake, akaja hadi nilipokuwa nimesimama. Uso wake ulikuwa bado unaonesha kuwa kuna kitu cha ajabu alikiona kwangu.

“Nimewahi kukuona mahala,” hatimaye alisema. “Ni wapi vile?”

Alianza kuwaangalia Pugu na Stevenson kama mtu aliyekuwa anataka wamkumbushe.

“Kuna pahala nimewahi kumuona huyu jamaa,” Aliwaambia halafu akatoa ishara nirudishwe kwenye chumba cha mahojiano nilimokuwa kabla sijaletwa kwake.



Mlango wa kile chumba cha mahojiano ulibamizwa kwa nguvu nikabaki mule ndani nikiwa nimekaa namsubiri aliyekuwa mkuu wa upelelezi kituoni hapo. Haukupita muda mrefu ule mlango ukafunguliwa tena. Jamaa mmoja ambaye sikumuona hapo kabla akaingia ndani. Alikuwa mweusi tii na mrefu, sio mzee sana, ila upaa ulikuwa tayari umeanza kumnyemelea. Muonekano wake wa kimavazi ulikuwa upo vizuri. Alikuwa kalamba suti iliyonyooshwa vizuri, na viatu vilivyopigwa kiwi vikapigika. Alisogea akakaa kwenye kiti kilichokuwa upande wa pili wa meza tukawa tunaangaliana.

Akafungua kikabati kilichoungwa na ile meza akavuta kinasa sauti. Akakiinua juu. Akafungua na kupachika kikanda. Akakiwasha halafu akabonyeza record huku akikipiga piga. Akabonyeza tena kitufe cha record akafuatisha na kile cha play. Sauti za vidole vyake vikiwa vinapiga piga ile recorder vikasikika. Akatingisha kichwa kuashiria ameridhika na alichokuwa anakisikia. Akakata halafu akabonyeza tena record. Muda wote huo nilikuwa namuangalia tu.

Kwa sekunde kadhaa kukawa na ukimya. Masikio yangu na akili vikaanza kusikia milio ya mishale ya saa. Ilikuwa inaenda taratibu. Ni kama vile muda ulikuwa unaniambia wenyewe utaendelea kwenda tu haijalishi nini nitafanya. Macho yangu na ya huyu mkuu wa upelelezi wa mkoa yalikutana. Akavikunja vidole vyake vikalia “ka ka.”

“Sawa,” akaanzisha mazungumzo. “Tuna maswali kadhaa hapa.”

Sauti yake ilikuwa nzito. Haikuwa lafudhi ya kisukuma. Mwonekano na lafudhi yake vikaniambia jamaa ni mzaliwa wa Dar Es Salaam.

“Jina langu naitwa Lazaro,” aliendelea. “Mimi ni mkuu wa kitengo cha upelelezi mkoa wa Geita. Naelewa umeambiwa kitu kuhusu haki zako baada ya kukamatwa na maaskari lakini haujathibitisha kwa namna yeyote kama umezielewa. Kwahivyo kabla sijaendelea ingekuwa vyema tuliweke sawa hilo pia.”

Nilikuwa nimekosea. Hakuwa mtu wa Dar. Lafudhi yake ilikuwa ya kichaga, labda Dar alienda kusoma tu na akawa analazimisha aongee lafudhi ya Dar.

“Nazielewa haki zangu.” Nilimjibu.

Alitikisa kichwa.

“Safi,” alisema. “Nafurahi kusikia hivyo. Na vipi kuhusu wakili?”

“Sihitaji wakili….” Nilijibu tena.

“Una kesi ya mauaji,” alinikatisha “Lazima utahitaji wakili. Sisi tutakupatia mmoja tena bila wewe kugharamika. Je ungependa tukupatie?”

“Hapana. Sihitaji wakili,” Nilisimamia msimamo wangu.

Lazaro akabaki ananishangaa kwa kile nilichokuwa nakisema.

“Sawa,” hatimae aliongea baada ya sekunde kadhaa. “Kwakuwa umekataa wakili utatakiwa uweke sahihi kuthibitisha maneno yako kuwa hauhitaji wakili, sawa?”

Nilitikisa kichwa kama ishara ya kukubaliana na pendekezo lake. Alifungua ile kabati tena na kutoa karatasi kadhaa halafu akajaza tarehe na muda. Alipomaliza akazisukuma kuja kwangu. Kulikuwa na mstari mkubwa ambao bila shaka ndipo nilipotakiwa kutia sahihi yangu. Nikiwa naiangalia ile karatasi akanirushia kalamu. Niliichukua nikaweka sahihi halafu nikazisukuma karatasi na kalamu kurudi kwake. Aliziangalia kwa muda kidogo halafu akazidumbukiza kwenye jarada lilikuwa mezani hapo.

“Nimeshindwa kuielewa sahihi yako,” alianzisha mazungumzo tena. “Kwahivyo, ili nijiridhishe zaidi tutaanza na jina lako, mahali unapoishi na tarehe yako ya kuzaliwa.”

Chumba kikaingiwa na ukimya. Nikabaki namuangalia tu. Jamaa alikuwa mkorofi. Umri wake pia nilianza kuukadiria ni miaka 45 au zaidi ya hapo. Ni kweli kwa sababu sio rahisi kuwa mkuu wa kitengo cha upelelezi kwa mkoa kama wewe sio mkorofi na una umri chini ya miaka 45. Kwa hivyo hakuna haja ya kujifanya mjuaji sana. Nilivuta pumzi.

“Naitwa Michael Kichaka,” nilisema “Sina jina la babu. Sina mahali ninapoishi.”

Alinitazama kisha akaandika nilichokuwa nimemwambia. Hayakuwa maneno mengi hivyo alitumia muda mchache sana kuyaandika. Alipomaliza nilimwambia tarehe, mwezi na mwaka wangu wa kuzaliwa.

“Sawa bwana Kichaka,” Alizungumza baada ya kumaliza kuandika. “Kama nilivyokuambia mwanzo. Leo tutakuwa na maswali kibao sana mbele yetu. Nimeshatazama vitu ulivyochukuliwa kwenye mifuko yako. Sijaona kitambulisho cha aina yoyote. Hakuna hata leseni ya dereva, wala kadi ya benki, wala chochote kinachokutambulisha. Na sasa hivi unasema huna anuani ya mahali unapoishi. Unaniacha na maswali mengi sana, yule ni nani?”

Hakuwa anataka jibu lolote kutoka kwangu. Kabla sijajibu akaendelea.

“Huyu mtu aliyekuwa amenyoa upaa ni nani?”

Sikujibu chochote. Nilikuwa naitazama saa yangu ya mkononi, nikisubiri muda uishe niachiwe niondoke.

“Niambie nini kilitokea,” Alinishtua.

Sikuwa najua anaongelea nini. Ila ilikuwa bayana kuwa kuna jambo baya lilikuwa limemtokea mtu na huyo mtu sio mimi. Kwa hivyo sikujibu chochote.

“Uhuru na umoja ina maanisha nini?” Aliniuliza tena.

Nilimwangalia nikatikisa mabega halafu nikaongea.

“Ni wito wa taifa, Ni maneno yapo kwenye Nembo ya Tanzania iliyoubuniwa na Bw. Jeremiah Wisdom Kabati mwaka 1961 huko Mwanza, au??”

Aliniangalia tu halafu akaguna. Na mimi nikabaki namwangalia machoni kwa jicho kavu. Nikagundua huyu ni mtu ambaye anaweza akajibu maswali ambayo mimi pia nilikuwa nayo.

“Kwanini nipo hapa?” Nilimuuliza

Aliniangalia halafu kimya kikatawala tena. Nilimuona ni kama mtu aliyekuwa anawaza ama anijibu au aache.

“Kwanini nipo hapa?” Nilimuuliza tena ili kumshtua kutoka kwenye chaguzi la kukataa kunijibu. Alishtuka halafu akaegemea kiti chake. Akavikuja tena vidole vyake vikatoa sauti ya “ka kaa” halafu akanijibu.

“Unafahamu fika kwanini upo hapa,” Alitulia kama mtu aliyekuwa akitafuta neno zuri la kuyasema maneno yaliyokuwa yanafuata halafu akaendelea. “Mauaji ambayo ni ya ajabu sana. Mwili wa maiti umekutwa ukiwa kwenye Go down la mzee Chacha. Mashahidi ambao tumewapata wametoa taarifa kuwa walimuona mtu akitembea kutokea eneo la tukio mida ya saa mbili asubuhi. Maelezo yao juu ya muonekano wa huyo mtu ni kwamba, ni mrefu, mweupe, hakuwa na nywele nyingi kichwani, alikuwa amevaa koti kubwa jeusi, hakuwa na kofia wala mzigo wowote.”

Kimya kikatawala tena. Mimi ni mrefu. Mweupe. Sikuwa na nywele nyingi kichwani. Asubuhi ya hiyo siku ni kweli nilikuwa nimevaa koti kubwa jeusi. Sikuwa na kofia. Sikuwa na mzigo wowote. Mbaya zaidi, ni kweli nilipita hiyo njia kwa takribani masaa manne. Kuanzia saa mbili asubuhi hadi saa tano na dakika arobaini na tano.

“Kwani kuna umbali gani kutoka huko Go down mpaka ENO?” Hatimaye nilivunja ukimya.

“Sina uhakika ila nakadiria maili 14.” Alijibu.

“Sawa,” Nilianza kujitetea. “Asubuhi nimetembea kutoka huko mjini hadi nje kidogo ya jiji. Hakuna shaka kuwa watu wengi watakuwa wameniona. Na hio haimaanishi nimefanya kitu chochote kwa mtu yeyote.”

Hakunijibu. Alikuwa ni kama anasubiri nijikaange mwenyewe kwenye mafuta.

“Hapo ni jirani yako?” Niliuliza tena.

“Ndiyo,” alijibu. “Mzee Chacha aliijenga hiyo Go down miaka mitano iliyopita. Unamfahamu?” halafu akaongeza swali.

Nilitikisa kichwa kukataa.

“Nitamjua vipi na sijawahi kufika Geita maisha yangu yote.”

“Okay! Ni mtu muhimu sana hapa,” Lazaro alianza kunifafanulia. “Shughuli zake zinachangia kodi na pato kubwa, anatusaidia sana. Pia ameajiri vijana wengi lakini leo asubuhi kumetokea mauaji kwenye eneo lake. Kwa faida alizonazo kwenye jamii, ndugu yangu una kesi kubwa ya kujibu kwa sababu wewe ndiye mhusika wa mauaji yenyewe.”

Kusema kweli, Jamaa alikuwa anafanya kazi yake, lakini alikuwa ananipotezea muda wangu.

“Poa Lazaro,” Hatimaye nilizungumza. “Nitatoa maelezo ya kila nilichokifanya tokea nilipokanyaga kwenye mji wako hadi nilipotiwa mikononi na ndugu zako nikiwa nakunywa kahawa yangu. Kama utafanikiwa kupata chochote cha kunifanya nionekane muuaji kwenye maelezo yangu, nitakupa zawadi. Kwa sababu kitu pekee nilichokifanya ni kuhakikisha mguu wangu mmoja unakuwa mbele ya mwingine kwa takribani masaa manne ya mvua kali kwa urefu wa maili kumi na nne.”

Haya yalikuwa ni maneno mengi niliyowahi kuyaongea kwa muda wa takribani miezi sita iliyopita. Lazaro alibaki ananitazama tu. Nilimuona akiwa amekwama kama wapelelezi wengine wanavyokwama kati ya kuamini ninachokisema au kuamini alichoelezwa. Hisia zake zilikuwa zinamwambia mimi sikuwa mtu wake. Lakini nilikuwa nimekaa mbele yake. Angefanya nini. Nikaamua kumuacha atafakari kidogo. Akiwa kati kati ya kutafakari nikawaza nirushe bomu litakalommaliza. Nimtie wasi wasi kwa kumwambia alikuwa anapoteza muda wake kwangu, wakati mtu wake alikuwa uraiani anaponda raha. Lakini kabla sijafungua mdomo wangu aliniwahi. Aliniwahi kubaya.

“Hakuna maelezo,” alisema. “Mimi tu ndiyo nitauliza maswali na kazi yako itakuwa ni kuyajibu tu. Wewe ni Michael Kichaka. Hauna jina la babu. Hauna anuani. Hauna kitambulisho. Wewe ni nini, omba omba au?”

Niliguna kwa mshtuko. Kwanza ilikuwa ni ijumaa. Hii ilimaanisha kadri ambavyo Lazaro angezidi kunipotezea muda ndiyo kadri ambavyo nafasi za mimi kulala kituoni mwisho wa juma lote zilivyokuwa zikiongezeka.

“Mimi sio omba omba, Lazaro.” Nilisema hatimaye. “Mimi ni wale wanawaita hobo kwa kiingereza. Kuna tofauti mkubwa sana kati ya hobo na vagrant.”

Alitikisa kichwa, halafu akatabasamu.

“Usijifanye mwerevu, Kichaka,” alisema. “Upo kwenye tatizo kubwa. Mambo mabaya yametokea huko Go Down. Mashahidi tulionao wamekuona ukiondoka eneo la tukio. Wewe ni mgeni tu hapa, huna kitambulisho. Huna chochote. Usijifanye mwerevu.”

Ni kweli tena, alikuwa anafanya kazi yake, lakini alikuwa ananipotezea muda wangu.

“Sikuwa naondoka eneo la tukio,” nilisema. “Nilikuwa natembea barabarani. Kuna tatizo mtu akitembea barabarani?? Huoni utofauti, Watu wanaoondoka maeneo ya matukio huwa wanakimbia, huwa hawatembei. Kuna tatizo gani kutembea barabarani ilihali watu huwa wanatembea muda wote??”

Lazaro aliinama kidogo, akatikisa kichwa chake tena.

“Hapana,” Alisema. “Hakuna mtu amewahi kutembea umbali huo wote tangu zilipovumbuliwa gari. Pia, kwanini hauna anuani ya mahali unapoishi. Jibu hilo swali tumalize hii ishu.”

“Sawa, Lazaro, Ngoja tumalize hii ishu,” Nilisema. “Sina anuani kwa sababu siishi popote. Labda siku moja nitapata pahala pa kuishi halafu nitapata anuani na nitakutumia barua ya mimi kupata anuani, kwa sababu inaonesha una shida sana na anuani yangu.”

Lazaro alinitazama tena huku akifikiria machaguo yake. Akaamua achague kuwa mvumilimu. Uvumilivu wenye uchokozi ndani yake.

“Unatokea wapi?” Aliniuliza. “Anuani yako ya sehemu ya mwisho ulipokuwa ni ipi?”

“Una maana gani ukiuliza mimi natokea wapi?” Niliuliza pia.

Uso wake ulianza kujikunja. Nilikuwa nimeanza kumfanya akasirike kama nilivyokuwa nimekasirika. Lakini bado alichagua kuwa mvumilivu.

“Sawa,” alisema. “Naona hauelewi swali langu, ngoja nijaribu kulifanya lieleweke kwako. Namaanisha ulizaliwa wapi, au makuzi yako yalikuwa wapi?”

Nilibaki nimemuangalia tu.

“Nitakupa mfano,” aliendelea. “Mimi nimezaliwa Arusha, nikasoma Arusha elimu ya msingi na sekondari. Masomo ya ngazi za juu nilienda kuyafanyia Dar Es Salaam, na nina imani utakubaliana na mimi kuwa nimezaliwa Arusha.”

Ni kweli nilikuwa sahihi. Huyu Lazaro alikuwa ni mzawa wa Arusha ila kama bahati tu alitokea kusomea Dar Es Salaam na kuibia ibia lafudhi ya kule.

“Sawa,” nilisema. “Umeuliza maswali yako na nitayajibu. Lakini nikupe onyo kuwa mimi sio mtu unaemtafuta. Kufikia Jumatatu utakuwa umeshajua kuwa ulikuwa unatupotezea muda, mimi na wewe. Kwa hivyo usibweteke na mimi. Endelea kuchunguza.”

Lazaro alitikisa kichwa kukubaliana na nilichokuwa nakisema.

“Nashukuru kwa ushauri wako,” Alisema. “Na kwa kujali kazi yangu.”

“Unakaribishwa.” Nilisema.

“Sawa. Endelea.” Alisema.

“Ok,” Nilianza kuongea. “Kutokana na mfano ulionipa, Mimi sijatokea popote isipokuwa sehemu yeyote ambayo inaitwa jeshi. Nilizaliwa kwenye kambi ya Jeshi Kigoma kusini mwa Tanzania. Baba yangu alikuwa mwanajeshi wa majini na mama yangu alikuwa raia wa kawaida tu aliyekutana naye huko Rwanda. Walifunga ndoa yao Korea.!”

Lazaro alitikisa kichwa tu. Akaandika kitu.

“Mimi ni mtoto wa jeshi,” niliendelea. “Nionyeshe orodha ya kambi zote za jeshi la wananchi Tanzania, ndani na nje ya nchi, huko ndipo nyumbani kwangu. Nimesoma elimu yangu nchi tatu tofauti.”

“Endelea.” Lazaro alisema.

“Nimekaa jeshini,” Niliendelea. “Nimelitumikia jeshi na nimeishi kambi mbali mbali ndani na nje ya nchi. Nenda rudi, nenda rudi. Halafu, Lazaro, baada ya miaka thelasini na sita ya kuwa mtoto wa mwanajeshi na mimi mwenyewe kuwa mwanajeshi, hakuna tena uhitaji wa jeshi kubwa kwa sababu nchi na dunia ina amani. Ni safi, amani kuwepo ambapo kwako inamaanisha wananchi watalipa ushuru utapata mshara, ila kwangu inamaanisha ni askari wa wanajeshi mstaafu na nina miaka telathini na sita na sina ajira, halafu naitwa omba omba na askari polisi wa raia wa kawaida ambaye nina uhakika asingeweza kudumu kwa dakika tano tu kwenye ulimwengu niliodumu kwa miaka thelathini na saba.”

Nilinyamaza. Lazaro alibaki anafikiria kile nilichokisema. Hakuwa ameridhishwa na maelezo yangu.

“Endelea,” Alisema.

“Kwahivyo sasa hivi nafurahia maisha nilivyo sina kazi,” Niliendelea. “Labda, muda sio mrefu nitapata kitu cha kufanya, au labda sitapata. Labda nitakaa pahala nitulie, labda sitakaa nitulie. Lakini kwa sasa hivi sina mpango wa kufanya hivyo.”

Alitikisa kichwa. Akaandika kitu tena kwenye daftari lake.

“Uliachana na jeshi lini?”

“Miezi sita iliyopita,” Niilisema. “Ilikuwa Aprili.”

“Kwahivyo, hujafanya kazi yoyote tokea hiyo Aprili?” Aliuliza tena.

“Una masihara sana,” Nilisema. “Mara ya mwisho umejaribu kutafuta kazi ilikuwa lini?”

“Aprili,” Aliniiga. “Miezi sita iliyopita ndiyo nilipata hii kazi.”

“Basi, bahati ipo na wewe, Lazaro.” Nilimwambia halafu nikakaa kimya. Sikuweza kufikiria neno lingine la kuongezea. Lazaro alinitazama kwa muda kidogo.

“Kwa hivyo umekuwa ukiishi vipi bila kazi,” alivunja ukimya. Aliuliza baada ya ukimya kidogo. “Na ulikuwa na nafasi gani jeshini.”

“Meja,” Nilisema. “Huwa wanakupa pesa nzuri sana wakikutema. Bado ninayo nyingi kiasi na ninajitahidi idumu.”

Kimya kirefu tena kikatawala. Lazaro aliiweka kalamu yake mdomoni kama anainyonya.



“Hebu tuongelee masaa 24 yaliyopita,” alisema.

Niliguna. Nilijua tunaelekea kwenye tatizo.

“Nilikuja na basi za Greyhound,” nilisema. “Nikashukia Mwatulole. Saa mbili asubuhi leo. Nikaanza kutembea mpaka nje kidogo ya mji, hadi nilipofika mgahawa wa ENO, nikaagiza kifungua kinywa changu na wakati nakula ndiyo wakati askari wako walikuja na kunitia nguvuni.”

“Una biashara yeyote huku,” Aliuliza.

“Sifanyi kazi yoyote,” Nilisema. “Sina biashara yeyote mahala popote.”

Aliandika nilichokisema kwenye karatasi yake.

“Ulipandia gari wapi kipindi unakuja huku??” Aliniuliza tena.

“Mwanza, Nyegezi,” Nilijibu. “Asubuhi mapema leo.”

Aliniangalia halafu akafungua tena kabati lililokuwa kwenye ile meza akatoa karatasi yenye ratiba za magari yote. Alikuwa mtu makini sana. Alipitisha vidole halafu akanitazama.

“Hiyo ni basi kubwa,” alisema. “Inatoka moja kwa moja hadi Geita na haisimami popote hadi ifike stendi. Kwa kawaida inafika hapa saa mbili na dakika arobaini na tano. Kwanini ulifika saa mbili kamili.?”

Nilitikisa kichwa.

“Nilimwomba dereva asimamishe gari,” nilianza kujitetea. “Aliniambia hapaswi kusimamisha gari lakini alisimamisha na kuniruhusu nishuke.”

“Umewahi kuwepo hapa kabla?” Aliniuliza.

Nilitikisa kichwa changu kuonesha hapana.

“Una familia popote,” Aliniuliza tena.

“Ndiyo. Ninae kaka yupo Dar Es Salaam,” nilisema “Anafanya kazi kwenye wizara ya fedha na mipango, idara ya hazina.”

“Hapa Geita je. Huna marafiki?” Aliniuliza tena.

“Hapana.” Nilisema.

Lazaro aliandika tena maelezo niliyokuwa nimempatia. Halafu kukawa na ukimya tena. Nilijua kwa hakika ni swali gani lilikuwa linafuata hapo.

“Sasa kwanini,” Aliuliza. “Kwanini ulishuka kwenye gari kwenye kituo ambacho sio rasmi na ukatembea kwa miguu umbali wa maili kumi na nne kwenye mvua ukielekea sehemu ambayo hukuwa na ishu yoyote unayoenda kufanya??”

Hilo swali ndilo lilikuwa mauji. Lazaro alikuwa amelichagua kwa umakini mkubwa sana. Ni kitu ambacho angekifanya hakimu pia. Sikuwa na jibu halisi la swali hilo.

“Sijui nikuambie nini,” hatimaye niliongea. “Ulikuwa ni uamuzi wa ghafla. Nilitakiwa niwe sehemu lakini sikua najua wapi.”

“Kwanini hapa sasa,” aliuliza. “Na sio sehemu nyingine?”

“Sijui,” Nilijibu. “Kuna jamaa alikuwa amekaa pembeni yangu alikuwa ameshikilia ramani, nikamuomba nikaiona hili eneo nikachagua nishukie hapo. Ingawa ningeweza kusubiri hadi tufike stendi.”

“Ulilichagua hili eneo kwa sababu ya ramani aliyokuwa nayo mtu kwenye basi,” Alisema. “Acha kunilisha matango pori. Lazima ulikuwa na sababu.”

Nilitikisa kichwa kukubali.

“Ndiyo. Nilikuja kutafuta taarifa za Abdul Naseeb,” Nilijibu.

“Abdul Naseeb??” Aliuliza kwa mshangao. “Ni nani huyo.”

Nilitulia kidogo nikawa namuangalia akiwa anapiga hesabu zake kama wacheza chess wanavyopiga hesabu kabla ya kusukuma kete. Maswali yaliyokuwa kichwani mwake lazima yalikuwa, Huyo Abdul Naseeb alikuwa ni rafiki yangu, Adui yangu, au mdaiwa wangu.

“Abdul Naseeb alikuwa mwanamuziki,” Nilisema. “Alishafariki miaka sitini na tano iliyopita, inasemekana aliuliwa kwa bunduki. Kaka yangu alinitumia barua ya kunitaarifu kuhusu taarifa hizo. Niliona nije kupata taarifa kidogo tu kuhusu kifo chake kwa sababu sikuwa na kitu cha kufanya.”

Lazaro alibaki amepigwa butwaa. Labda suala lilikuwa dogo upande wake, hata kwangu pia lilikuwa dogo.

“Yaani ulikuja huku kutafuta taarifa za msanii ambaye alishafariki miaka sitini na tano iliyopita? Wewe ni mwanamuziki?” Aliuliza kwa sauti kavu kidogo.

“Hapana.”

“ Ulisema huna anuani, Kaka yako alikutumia vipi barua?”

“Aliiandika kwenda kwenye kitengo changu cha zamani,” Nilisema. “Wao wakaifowadi kwenda benki, ambako nililipiwa hela yangu baada ya kuachishwa kazi. Ndiko nilipoipata huko.”

Alitikisa kichwa chake halafu akaandika.

“Umesema ulipanda basi za GreyHound kutokea mwanza, sio?” Aliuliza.

Nilitikisa kichwa kama ishara ya kukubali.

“Unayo tiketi ya basi?” Aliuliza tena

“Ndiyo,” Nilijibu. “Nina uhakika itakiwa kwenye mizigo yangu niliyokaguliwa.”

“Unahisi dereva atakumbuka?” Lazaro aliuliza.

“Labda,” Nilisema. “Nilimwomba asimamishe akasimamisha.”

Hali ilionesha kama vile mimi na Lazaro tulikuwa tumekuwa tunashughulikia kesi moja na wala sio mshukiwa tena.

“Kwanini hufanyi kazi?” Lazaro aliuliza.

Nilijikuta nakosa namna nzuri ya kujibu.

“Kwa sababu sihitaji kufanya kazi,” Hatimaye nilisema. “Nimefanya kazi kwa miaka zaidi ya ishirini na tano. Nahisi nimefanya vya kutosha namna ambavyo watu wengine wanatamani nifanye sasa ni wakati wa kufanya vile ninavyojisikia kufanya.”

Lazaro alibaki ananishangaa tena.

“Ulikuwa na usumbufu wowote jeshini?” Aliuliza baada ya ukimya kidogo.

“Ndiyo. Lakini sidhani kama ni zaidi ya usumbufu uliokuwa nao wewe huko chuoni.” Nilimjibu.

Alishtuka kidogo.

“Una maanisha nini??” Aliniuliza hatimaye.

“Umekaa zaidi ya miaka ishirini Dar Es Salaam,” Nilisema. “Ndivyo ulivyoniambia, Lazaro. Sasa kwanini upo hapa ulipo sehemu ambayo haieleweki. Ungetakiwa uwe unakula pensheni yako. Au labda unajiachia baharini kwenye boti. Historia yako inasemaje??”

“Hilo halikuhusu,” Alisema. “Nijibu swali langu.”

Nilitikisa kichwa.

“Iulize serikari na jeshi,” Nilimwambia.

“Nitafanya hivyo,” aliniambia. “Lakini nataka nijue kama uliagwa kwa heshima au ulitoroka?”

“Kama nilitoroka unahisi ningepewa pesa?”

“Kwanini niamini ulipewa pesa wakati unaishi maisha kama vile omba omba. Ulitoroka?? Ndiyo au hapana?”

“Hapana,” Nilisema hatimaye.

Aliandika jambo kwenye karatasi yake.

“Ulijisikiaje walipokutimua.” Aliuliza tena.

“Sikujisikia chochote,” Nilijibu. “Nilijisikia kama sekunde moja iliyopita nilikuwa mwanajeshi, na sasa hivi siyo mwanajeshi.”

“Hukuhisi uchungu?” Aliuliza tena.

“Hapana,” Nilisema. “Kwani ni lazima nihisi uchungu.”

“Una uhakika.” Aliniuliza. Ilikuwa ni kama lazima nihisi kitu.

Nilianza kuona kama sijampa jibu zuri. Mimi nilikuwa nikitumikia Jeshi tokea siku ya kwanza nilipozaliwa. Sasa hivi sikuwa Jeshini. Nilijisikia faraja. Ni kama vile nilikuwa nimepewa uhuru. Ni kama vile maisha yangu ya zamani yalikuwa ni maumivu ya kichwa na sasa nilikuwa nimesha meza tende na nimepona. Tatizo langu lilikuwa moja tu. Namna ya kutengeneza pesa. Namna ya kutengeneza pesa uraiani hakikuwa kitu ambacho nilikuwa nimekizoea. Ukweli ni kwamba sikuwa nimetengeneza hata senti moja kwa miezi sita iliyopita. Hilo tu ndiyo lilikuwa tatizo langu. Lakini sikuwa tayari kumwambia Lazaro chochote kuhusu tatizo hilo. Angeliona kama chanzo na sababu ya mimi kuwateka na kuwaua watu kwenye Go Down za watu.

Alikuwa bado anatafakari jibu nililompatia.

“Kwanini wewe,” Alisema. “Uliamua mwenyewe kutoka jeshini.”

“Hapana,” Nilimjibu. “Sheria ya kwanza ya mwanajeshi ni kusikiliza tu na sio kuamua.”

Kimya kikatawala tena.

“Ulikuwa umekubuhu kwenye chochote,” Aliniuliza tena.

“Ishu za jumla, mwanzoni,” Nilisema. “Ndiyo utaratibu. Halafu nikafanya Usalama wa taifa kwa miaka mitano. Miaka sita baadae, nikapewa majukumu tofauti kidogo.”

Nilisema hivyo maksudi ili aulize majukumu gani. Ni kweli aliuangukia mtego.

“Majukumu gani?” Aliuliza.

“Uchunguzi wa mauaji,” Nilijibu.

“Sawa,” Alisema. “Nitacheki na jamaa nijue. Kwa kuwa tunazo alama zako za vidole naamini hata Jeshini zitakuwepo. Nitajua mbivu na mbichi ni zipi? Tutaangalia ulivyolitumikia jeshi na rekodi zako, Tutaangalia tiketi ya basi na kila kitu.”

Alitulia kidogo akavuta pumzi halafu akaendelea.

“Sikia,” Aliendelea. “Kwa maelezo yako unaoneka kama wewe ni Omba omba. Usiyekuwa na mahala pa kukaa wala historia yeyote. Hio stori uliyonipa inaweza ikawa ni upuuzi mtupu tu. Labda kweli wewe unahusika na vifo vya watu kibao. Siwezi nikakupa nafasi ya huruma. Kwa sasa hivi unakaa ndani hadi hapo nitakapojiridhisha na taarifa ulizonipatia.”

Ndicho nilichokuwa nategemea kusikia. Na kama ningekuwa kwenye nafasi yake, maneno aliyoyaongea ndiyo ambayo ningeyasema.

“Ni kweli,” Nilisema. “Wewe ni mtu makini.”

Alibaki ananiangalia.

“Kama nitabaini hauhusiki nitakununulia chakula cha mchana Jumatatu kama fidia,” Alisema.

Nilitikisa kichwa changu.

“Sipo huku kwaajili ya kutengeneza marafiki,” Nilisema.

Lazaro alitikisa mabega. Akabonyeza kitufe cha record kuashiria kiache kunasa sauti. Akaitoa kanda halafu akaandika maneno ambayo sikuweza kuyasoma juu yake. Akaita na ghafla mlango wa kile chumba ukafunguka. Pugu akaingia ndani. Nilikuwa kimya muda wote. Nikaanza kuhisi baridi.

Pugu akanichukua na kunielekeza zilipokuwa selo. Nikiwa bado nimesimama nikamuona Lazaro akitingisha kichwa kama ishara ya kuniambia: Ikibainika ni ukweli, ujue nilikuwa nafanya kazi yangu. Na mimi nikatingisha kichwa kilichosema: Wewe poteza muda wako wakati muuaji yupo uraiani huko anakula maisha!
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom