SIMULIZI YA KWELI:Niliolewa na wanaume watatu

SIMULIZI YA KWELI:Niliolewa na wanaume watatu

SEHEMU YA 20:

Wakati ule namuaga Amina nikamuona Mustafa ameinuka.
“Unaondoka?” Amina akamuuliza.
“Ndiyo, nataka kwenda nyumbani nioge nibadili nguo. Nilikuwa Kibaha tangu asubuhi.”
“Basi utampa lifti shoga yangu, umuache nyumbani kwake.”
“Hakuna tatizo. Twende Mishi,” Mustafa akaniambia kwa furaha.SASA ENDELEA
Nikanyanyuka kwenye kiti na kumuaga Shabir.
“Shabir kwaheri, tutaonana siku nyingine,” nilimwambia.
“Usijali, tutaonana,” Shabir akaniambia.
Nikaondoka na Mustafa. Tukiwa nje ya hoteli Mustafa alinipakia kwenye gari lake. Alikuwa na gari jipya aina ya Range Rover la rangi nyekundu.
Akaliwasha gari tukaondoka.
“Unaishi wapi?” akaniuliza mara tu alipoliondoa gari.
“Naishi Kimara Baruti.”
“Unafanya kazi wapi Mishi.”
Hapo nilisita kumjibu ukweli kwa vile sikuwa na kazi na nilikuwa nimeolewa. Nikaishia kumuuliza:
“Mimi…?”
“Si ndiyo.”
“Niko nyumbani tu.”
“Uko na wazazi wako?”
Ilibidi nimkubalie.
“Ndiyo, bado naishi na wazazi.”
“Unaonaje tukiwa marafiki?”
Moyo wangu ulishituka ingawa nilitarajia kuwa angeniambia hivyo.
Uso wangu ukawa umepatwa na tabasamu la fadhaa.
“Si tumeshajuana?” nikajidai kumuuliza.
“Kujuana tu haitoshi, nataka tuwe marafiki kabisa.”
Mustafa aliponiona nimesita nikifikiria kumkubalia au kumkatalia alianza kunimwagia sera.
“Unajua nilipokuona pale hotelini moyo wangu ulishituka sana ndiyo maana nilipoona unamuaga shoga yako na mimi nikainuka haraka. Nilikuwa nataka nipate nafasi ya kuzungumza na wewe.”
“Nilikuona na nilijua ulikuwa na jambo.”
Mustafa akacheka.
“Kumbe ulishanisoma?”
“Sasa kitu gani kilichokuvutia?” nikamuuliza kwa kuzuga.
“Ni wewe mwenyewe jinsi ulivyo,” Mustafa alinijibu haraka kama vile jibu hilo lilikuwa mdomoni mwake.
“Nikoje?”
“Mishi unauliza jibu? Au una bwana anakupa pesa nyingi?”
Kabla sijajibu, Mustafa akaongeza:
“Pesa si tatizo kwangu. Juzijuzi tu nilikuwa India. Nimekuja na pikipiki mia mbili.”
“Shabir alituambia wakati ulipompigia simu.”
“Huwa nashirikiana naye.”
Wakati Mustafa akiniambia hivyo mawazo yangu yalikuwa mbali. Nilikuwa kwenye mjadala mkali ndani ya moyo wangu. Upande mmoja wa akili yangu ulitaka nimkubalie kwa sababu ya tamaa ya kupata pesa. Nilijua nikiwa naye pesa ya kuweka akiba haitanisumbua, nitakuwa kama Amina.
Lakini upande mwingine wa akili yangu ulisita kumkubalia kwa sababu nilikuwa mke wa mtu, kuwa na mwanaume mwingine wa pembeni ni jambo ambalo sikulizoea.
Jambo la ajabu ni kuwa wakati nikijadiliana na akili yangu kuhusu suala hilo nilikuwa nikipata ujasiri wa ajabu wa kumkubalia. “We mkubalie tu..unaogopa nini..kwanza mume wako yuko safarini…akija akikaa siku tatu anaondoka tena, akienda huko anakaa mwezi mzima…Mustafa ana gari nzuri anakwenda nchi za nje mara kwa mara… huyo ndiye mwanaume wa kuwa naye…” niliisikia sauti ikinishawishi ndani ya moyo wangu.
Nilijaribu kuipuuza kwa hofu ya kuisaliti ndoa yangu lakini sikuweza. Nikajikuta nikimuuliza Mustafa:
“Kwani wewe huna mke.”
“Mke wangu unaweza kuja kuwa ni wewe,” akaniambia na kunizidisha tamaa.
“Yaani huna mke?” nikamuuliza tena ili nipate uhakika.
“Sijaoa bado.”
“Kwa nini?”
“Kwa sababu sijampata anayenifaa.”
“Lakini mimi nisingependa kuolewa kwa sasa.”
Nilipotoa jibu hilo nilikuwa nimeshalegea. Nilikuwa kama ngamia niliyesalimu amri nikisubiri kuchinjwa tu.”
“Hata mimi sina nia ya kuoa kwa sasa. Nahitaji tu nipate mwenzangu wa kuniliwaza.”
“Basi usijali, mimi nipo.”
“Utanionesha mtaa unaoishi.”
“Nishushe tu hapahapa.”
Sikutaka Mustafa anifikishe nyumbani kwangu na pia sikutaka aijue nyumba ninayoishi. Akasimamisha gari.
“Umeshafika nyumbani kwenu?” akaniuliza.
“Tumekaribia lakini nataka nishuke hapa, kuna rafiki yangu nataka nimuone.”
“Sasa tutakutana lini tena?” Mustafa akaniuliza.
“Niambie wewe.”
Mustafa alifikiri kidogo kisha akaniambia:
“Nipe namba yako ya simu.”
Nikampa namba yangu na yeye akanipa yake.
“Kabla ya kunipigia kwanza nitumie sms,” nikamwambia.
“Usijali.”Mustafa akanionesha kuwa alikuwa amekusudia hasa kuwa na mimi, alitia mkono mfukoni akatoa pochi yake na kunipa shilingi laki moja.
Je, nini kiliendelea?
 
SEHEMU YA 21:

Mustafa alifikiri kidogo kisha akaniambia.
“Nipe namba yako ya simu.”
Nilimpa namba yangu na yeye akanipa yake.
“Kabla ya kunipigia kwanza nitumie sms,” nikamwambia.
“Usijali.”Mustafa akanionesha kuwa alikuwa amekusudia hasa kuwa na mimi, alitia mkono mfukoni akatoa pochi yake na kunipa shilingi laki moja.
SASA ENDELEA…
“Asante,” nilimwambia huku nikizipokea pesa hizo.
“Basi wewe nenda, tutakuwa tunawasiliana,” Mustafa aliniambia.
Ajabu ni kwamba ile shilingi laki moja aliyonipa ilinifanya nianze kumpenda palepale. Lakini wasiwasi wangu mkubwa ulikuwa kwa Amina. Nilikuwa na wasiwasi kwamba Amina anaweza kuja kumueleza Mustafa kuwa nina mume na kuniharibia mpango wangu. Kitu kingine pia sikutaka Amina afahamu mapema uhusiano wangu na Mustafa.
“Kuna kitu nataka nikwambie,” nikamwambia Mustafa.
“Kitu gani?” akaniuliza.
“Nisingependa umueleze chochote Amina kwa sasa.”
“Kuhusu nini?”
“Kwani tumezungumza nini mimi na wewe?”
“Sawa. Nimekuelewa.”
Nikafungua mlango wa gari kisha nikamtupia jicho la tabasamu.
“Nakutarajia,” nikamwambia kabla ya kushuka.
Nikamuona Mustafa naye akitabasamu kisha akaliondoa gari. Nilisimama nikalitazama gari lake kwa nyuma lakini mawazo yangu hayakuwa kwenye gari, yalikuwa kwa mwenye gari.
Nilikuwa kama nimejisahau. Nilipozinduka nikaongoza njia kuelekea katika mtaa niliokuwa nikiishi.
Usiku ule mawazo yangu kwa mara ya kwanza yaliondoka kwa mume wangu yakawa kwa mwanaume mwingine ambaye nilimuona na kumjua kwa siku ileile.Sikutaka hata kupata muda wa kumjua vizuri, niliamini kuwa alikuwa ni mtu wa pesa hivyo niliona kuwa atanifaa.
Nikiwa nyumbani kwangu nilikwenda kuoga, nilipotoka bafuni nikakaanga chipsi zangu na mayai. Baada ya kula nilipumzika kidogo kisha nikaingia chumbani kwa ajili ya kulala.
Wakati nikiwa kitandani nililisevu jina la Mustafa kwa herufi moja tu ya ‘M’ kwenye simu yangu. Hapohapo nikamuona kwenye Mtandao wa WhatsApp uliokuwa kwenye simu yangu.
Niliona picha yake akiwa amependeza. Na mimi nikatafuta picha nzuri kwenye sehemu ya picha nikaiweka kwenye WhatsApp yangu kisha nikamtumia meseji.
“Nimekuona,” nilimuandikia.
Haikupita hata dakika moja akatuma jibu.
“Na mimi nimekuona.”
Nikamtumia tena.
“Umependeza.”
Akanijibu: “Asante. Wewe pia umependeza!”
Tukaendelea kutumiana sms mpaka usingizi ulipoanza kuninyemelea tukaagana. Nililala huku moyo wangu ukiwa na furaha.
Siku ya pili yake sikutaka kutangulia kumtumia Mustafa sms. Nilitaka aanze yeye. Lakini hakutuma wala hakunipigia simu. Nikakasirika. Ilipofika saa tisa alasiri ndipo nilipoona sms yake.
“Mambo?” akaniuliza.
Na mimi nikamuandikia kumjibu.
“Poa. Vipi?”
“Poa tu. Mambo yanakwendaje?” akanitumia tena.
Nikatamani kusikia sauti yake. Nikamuandikia.
“Nipigie.”
Salio nilikuwa nalo lakini sikutaka kupiga mimi.
Baada ya muda kidogo akanipigia. Nikaipokea simu yake.
“Hello!”
“Hello baby. Uko wapi?” akaniuliza.
“Niko nyumbani.”
“Unaweza kuja hapa…” alitaja jina la hoteli fulani ambayo sikufahamu ilikuwa wapi.
“Sipafahamu,” nikamwambia.
“Mwambie mwenye teksi yeyote atakuleta.”
“Unataka nije muda huu?”
“Ndiyo.”
“Subiri basi nijitayarishe.”
“Ukiwa tayari nijulishe.”
“Sawa.”
Mustafa akakata simu.
Nikaanza kujitayarisha. Mpaka saa kumi jioni nikawa tayari. Nikatoka na kufunga mlango wangu kisha nikaenda kukodi teksi. Teksi ikanipeleka kwenye hiyo hoteli iliyokuwa Ubungo.
Niliposhuka kwenye teksi nikampigia simu Mustafa. Mustafa alipopokea simu nikamuuliza.
“Uko na nani?”
“Niko mwenyewe. Amina yuko na Shabir.”
“Wao si wako kwenye ile hoteli nyingine.”
“Ndiyo, wao wako kule.”
“Usiwaambie kuwa umeniita hapa.”
“Kwani wewe uko wapi?”
“Nimeshafika, niko hapa nje ya hoteli.”
“Ingia.”
“Hapana, nifuate.”
“Subiri nakuja.”
Baada ya muda kidogo Mustafa akatoka nje ya hoteli. Alionekana wazi kuwa alikuwa ameanza kulewa.
“Mishi vipi?” akaniuliza.
“Poa,” nilimjibu nikiwa na hofu kidogo.
“Twende.”
Akanishika mkono tukaingia mle hotelini. Kama Mustafa angenitazama vizuri angegundua kuwa nilikuwa na wasiwasi na sikuwa nikijiamini lakini nilikuwa nikijikaza tu kwa sababu nilishaamua kuwa naye.
Mustafa alikuwa ameanza kunywa pombe tangu saa tisa alasiri. Akaanza kunishawishi na mimi nilewe.
 
SEHEMU YA 22:

Bila shaka Amina alimnyang’anya simu alipomuona anaanza kuropoka. Nikaisikia sauti ya Amina akisema:“Jamaa yupo njwii hapa, hajui anachokisema, poa basi.”
Aliponiambia hivyo akakata simu japokuwa mimi ndiye niliyempigia.
SASA ENDELEA…
Nikahisi kwamba Shabir alikuwa akimpa pesa nyingi Amina si kwa sababu alikuwa anazo, bali alikuwa analewa kupita kiasi. Hapo ndipo Amina anapompatia kwenye masuala ya pesa. Akimuomba kiasi chochote anampa.
Nikajiambia na mimi nikishazoeana na Mustafa nitamsubiri akilewa niwe ninamuomba pesa nyingi.
“Siwezi kuisaliti ndoa yangu burebure, lazima kuwe na masilahi ya kutosha,” nikajiambia kimoyomoyo.
Wazo kwamba nini kitatokea endapo Musa atagundua kuwa nina mwanaume wa nje halikunijia akilini mwangu. Niliona kwamba ningeweza kuitunza siri ile na kwamba Musa asingeweza kuigundua kwa vile muda mwingi anakuwa safarini.
Sikujua ni kitu gani kilichonibadili ghafla, ni tamaa ya pesa au vile ninavyomkosa mume wangu kwa muda mrefu. Sikuweza kujua.Sikukutana tena na Mustafa kwa siku tatu. Tulikuwa tukiwasiliana kwa simu tu. Asubuhi ya siku ya nne yake Amina akanipigia simu na kuniuliza kama mume wangu amerudi.
“Kwa nini unaniuliza hivyo?” nikamuuliza.
“Nataka nije nikutembelee.”
“Hajarudi, njoo tu.”
“Basi najitayarisha nije.”
“Nakusubiri.”
Baada ya kupita saa moja hivi Amina akafika nyumbani. Nilimkaribisha kwa furaha ili nipate umbeya.
“Karibu shoga, nimeku-miss…” Nilimwambia Amina alipoketi sebuleni.
“Hata mimi nimeku-miss shoga. Tangu juzi nilikuwa bize na yule mwanaume. Jana ndiyo nimerudi nyumbani.”
“Acha shoga! Mlikuwa mwatumia tu…!”
“Yule jamaa anajua kuchezea pesa halafu siyo mgumu.”
“Amekupa ngapi?”
“Kwanza zile zinazobakibaki tunaponunua vocha au anapolipia vyakula na ulevi, ninabaki nazo mimi. Mpaka naondoka jana nilikuwa na laki mbili halafu yeye mwenyewe amenipa shilingi milioni mbili. Juzi tukiwa palepale hoteli alijisahau akanipa milioni moja. Jumla nimeondoka na shilingi milioni tatu na laki mbili. Nimeshaziweka benki.”
Alipotaja benki mwili ulinisisimka. Na mimi nilikuwa mbioni kufungua akaunti. Mustafa au Musa wakinipa pesa na mimi nilitaka niziweke benki kama mwenzangu.
“Naona tangu umpate huyo bwana mambo yako yanakuwa poa,” nikamwambia.
“Wala usiniambie shoga. Hivi namlilia aniletee pikipiki.”
“Kwa nini asikuletee gari?”
“Gari bado kwanza, tumeanzana juzijuzi tu. Ataona nina tamaa.”
“Na vipi kuhusu Mustafa, hivi ana mke yule…?”
“Mbona unamuuliza, umempenda?”
Nikajidai kucheka.
“We Amina wanichekesha kweli…nimpende nini sasa wakati nina mume wangu?”
“Uliona wapi jiwe moja likainjika chungu?” Amina akaniambia.
“Hata mawili hayainjiki,” nikamjibu.
“Lakini yanakuwa afadhali kidogo.”
Nikabetua mabega yangu. Laiti Amina angekuwa na ujuzi tu wa kusoma akili ya mtu angegundua kuwa niliyabetua mabega yangu kumzuga tu.
“Mimi siko huko. Nimefundwa nikafundika. Nilikuwa nakuuliza tu.”
“Mustafa hajaoa bado.”
“Kama hajaoa atakuwa malaya sana,” nilimwambia hivyo kusudi ili anieleze tabia zake.
“Sijamjua bado, unajua hatuwi naye mara kwa mara.”
“Lakini nawaona wanapendana sana na Shabir.”
“Kawaida tu, unajua yule anatumwa na Shabir kwenda nje kumnunulia vitu na yeye anapata chake humohumo.”
Hayo ndiyo niliyokuwa nikiyataka.
“Hana shughuli nyingine?” nikamuuliza.
“Ana maduka yake mawili pale Mwenge. Duka la spea za magari na duka la vipodozi.”
“Lakini yanamtosha.”
“Si umeona ana gari lake zuri?”
“Siku ile alinipakia hadi nyumbani.”
“Hakukutongoza?”
“Labda hakunipenda. Hakuniuliza chochote.”
“Alishindwa kwa sababu aliona tunajuana.”
“Labda.”
Siku ile Amina alishinda nyumbani kwangu, kwa hiyo tuliongea mengi kumuhusu Shabir na mwenzake Mustafa. Nilikwenda sokoni na Amina. Tuliporudi tulipika ugali na nyama tukala kisha tukaendelea na mazungumzo hadi jioni ambapo Amina aliniaga na kuondoka.
Licha ya kuzungumza mengi na Amina sikuthubutu kumueleza Amina kuwa jana yake niliisaliti ndoa yangu na Mustafa. Sikutaka Amina afahamu lolote na kama atafahamu iwe ni baadaye sana.
Usiri wangu huo kwa shoga yangu ulitokana na aibu. Ndoa yangu haikuwa na muda mrefu, hivyo niliona aibu kama Amina atajua kuwa natoka na Mustafa tena baada ya yeye kututambulisha siku ile pale hoteli.
Ilipofika usiku Musa akanipigia simu. Siku zote ninapopata simu ya Musa huwa nafurahi lakini siku ile kwa mara ya kwanza nilijisikia kuchukia. Lakini sikujua ni kwa nini.
“Hello Baby!” Musa aliita kwa bashasha baada ya kupokea simu yake.
“Niambie mume wangu?” nikamwambia kwa kumzuga tu ili asijue kuwa mwenzake nimeshaota mbawa.
“Kesho nakuja mke wangu, niko mpakani.”
Kusema kweli sikutaka aje haraka. Hapohapo nikanuna.
“Unakuja kesho?” nikamuuliza nikijifanya sikumsikia vizuri.
“Kesho nakuja. Nimeku-miss sana…”
Kwa jinsi moyo wangu ulivyonywea nilitaka ninyamaze tu lakini niliona nitamgutusha, nikajidai kumwambia…
Je, nini kiliendelea?
 
SEHEMU YA 23:

Kusema kweli sikutaka aje haraka. Hapohapo nikanuna.
“Unakuja kesho?” nikamuuliza nikijifanya sikumsikia vizuri.
“Kesho nakuja. Nimekumiss sana…”
Kwa jinsi moyo wangu ulivyonywea nilitaka ninyamaze tu lakini niliona nitamshangaza, nikajidai kumwambia:
SASA ENDELEA…
“Mimi zaidi…”
“Unaniambia ukweli mpenzi?”
“Kutoka ndani ya moyo wangu.”
“Acha we…”
“Umeniletea zawadi gani?”
“Utakuja kuiona hukohuko.”
“Nitafurahi.”
Nilikuwa kama ninayeigiza sinema. Maneno yangu hayakuwa na ukweli wowote. Sikuwa nimemmiss na wala sikuwa nikihitaji zawadi yake, kwa vyovyote vile zawadi yenyewe itakuwa nguo moja au vipodozi ambavyo hata mimi mwenyewe naweza kuvinunua.
Baada ya kuzungumza machache, Musa akaniaga. Nilichofurahi siyo kwamba Musa anakuja bali kujua kama anakuja kwani angekuja ghafla bila kunifahamisha angeweza kukuta sipo nyumbani na hivyo kuanza kunitilia mashaka.
Kesho yake Musa akanipigia simu saa kumi na mbili jioni akanijulisha kuwa ameshafika Dar na yuko ofisini kwao. Nikaandaa chakula kwa ajili yake. Saa mbili usiku Musa akawasili nyumbani.
Wakati Musa anabisha mlango nilizima simu yangu. Nilihofia kwamba Mustafa anaweza kunipigia wakati Musa akiwepo.
Nilipofungua mlango nilimpokea begi lake kwa vile aliniahidi kuniletea zawadi, nikaingia nalo ndani.
“Habari za safari?” nikamuuliza.
“Nzuri, za hapa.”
“Hapa ni kwema tu.”
Wakati tunaulizana hali na Musa nilikuwa nimeshalifungua begi na kuanza kutoa vilivyokuwemo ndani.
Nikaona boksi, nikalitoa na kulifungua. Lilikuwa na viatu vizuri vya kike vya mchuchumio.
Nikahisi kwamba ilikuwa ndiyo zawadi yangu. Kile kitendo cha kupekua begi lake hakikumshangaza Musa kwani kilikuwa cha kawaida. Kama kilimkera hakuweza kuniambia kwa sababu alikuwa akinipenda sana.
“Hii ndiyo zawadi yangu?” nikamuuliza huku nikitabasamu baada ya kuona vile viatu.
“Ndiyo hiyo,” Musa akaniambia.
Hapohapo nikaanza kuvijaribu miguuni. Vilikuwa sawa kabisa. Nikanyanyuka na kujaribu kuvitembelea pale sebuleni.
“Vimekupendeza sana,” Musa akaniambia.
“Sema kweli?”
“Nakwambia kweli kabisa.”
“Siku nyingine uniletee mkoba wa kike wa rangi hiihii ili niweze kumechisha.”
“Nitakuletea na gauni lake.”
“Utakuwa umefanya jambo la maana sana.”
Baada ya kuvijaribu vile viatu nilivivua nikamwambia mume wangu aende akaoge ili tule chakula.
Musa akaingia chumbani. Alipomaliza kuoga alikuja mezani tukala chakula kisha tukakaa sebuleni kuzungumza. Muda wa kulala ulipowadia tukaenda kulala.
Asubuhi iliyofuata, Musa baada ya kunywa chai alitoka kwenda kazini kwake. Nilipoona ameondoka ndipo nilipowasha simu.
Wakati nawasha meseji ikaingia. Ilikuwa meseji ya Mustafa, aliandika:
“Mbona hupatikani?”
Nikaijibu haraka.
“Nilikuwa nachaji simu.”
Wakati naosha vyombo Mustafa akatuma meseji nyingine.
“Niko njiani naenda Arusha, nitarudi kesho.”
Na mimi nikamuuliza:
“Kuna nini?”
“Nakwenda kumjulia hali mama yake Shabir.” Hilo ndilo jibu alilotuma Mustafa. Nikamtumia meseji nyingine:
“Ukirudi utanishitua.”
Mustafa akanijibu: “Poa.”
Nilipomaliza kuosha vyombo nilikwenda kuoga kisha nikakaa sebuleni kuangalia televisheni.
Ni kweli kuwa mapenzi hayagawanyiki na mtu huwezi kupenda watu wawili kwa wakati mmoja. Mawazo yangu yote yalikuwa kwa Mustafa. Musa hakuwa na nafasi tena ndani ya moyo wangu. Tulikuwa pamoja tu kwa sababu alinioa lakini si kimapenzi.
Nilivyoanzana na Mustafa ilikuwa ni kwa sababu ya tamaa ya pesa baada ya kumuona shoga yangu Amina alikuwa akihongwa pesa nyingi na mwanaume wake. Lakini kwa sasa yalikuwa yamegeuka mapenzi. Nilikuwa nampenda sana Mustafa.
Nilikuwa natamani Musa asikae sana aondoke ili nipate nafasi ya kuwa na Mustafa. Moyo wangu tayari ulikuwa umeshaharibika. Nilikuwa namtahadharisha Musa kuhusu wasichana huko anakosafiri, sasa tatizo lilikuwa kwangu.
Kama nilivyokuwa nikitamani, Musa hakukaa sana. Baada ya siku tatu tu akaniambia anakwenda Mwanza. Nikafurahi kweli kwani wakati ule Mustafa alishanijulisha kuwa alirudi kutoka Arusha na nilikuwa sipati nafasi ya kukutana naye.
Musa alipoondoka kwenda Mwanza nikampigia simu Mustafa.
“Uko wapi baby?” Nikamuuliza kwa kumlegezea sauti.
“Niko nyumbani,” akanijibu.
“Huko nyumbani kwako utanionesha lini?”
“Siku yoyote tu utakayotaka.”
“Nataka unioneshe leo.”
“Ni wewe tu.”
“Lakini nisije nikaja kupigwa na wanawake zako!”
“Hapana. Sina mwanamke yeyote humu ndani, ondoa wasiwasi.”
“Kwani unaishi wapi?”
“Niko Mbezi.”
“Sasa tutakutana wapi. Nimekumiss baby…?”
Je, nini kiliendelea?
 
SEHEMU YA 26

ILIPOISHIA
Licha ya kufanikiwa kumdanganya Musa, nilipata wasiwasi kuwa endapo atarudi na kunitaka twende kwa shangazi halafu akakuta shangazi hakuwa akiumwa itakuwaje? Nikajiambia ataona kwamba nilimdanganya na atatafuta sababu kwa nini nilimdanganya. Atagundua kuwa nilikuwa nimekwenda sehemu! Nilipowaza hivyo nilianza kupata hofu.


SASA ENDELEA…


Hofu yangu haikunizuia nisimuwaze Mustafa ambaye nilikuwa nimempenda zaidi ya Musa. Nataka niwe sahihi kwamba mapenzi yangu kwa Mustafa yalikuwa na sababu za kiulimbukeni. Ulimbukeni wa pesa na maisha ya kifahari. Nilikuwa nikifikiria kwamba kama nitaendelea kuwa na Mustafa nitaweza kujenga nyumba yangu mwenyewe na pia kununua au kununuliwa gari. Pia nilifikiria kwamba nikiwa na Mustafa pesa haitanipiga chenga kwa sababu Mustafa kwa jinsi nilivyomfahamu hakuwa tajiri lakini alikuwa mtafutaji na niliamini msemo wa Kiswahili kuwa mkaa karibu na waridi haachi kunukia. Usiku wa siku ile niliwaza kununuliwa gari na Mustafa kama alivyoniambia. Sikujua kama maneno yake yalikuwa ya utani au ya ukweli lakini mimi niliyachukulia kuwa ni ya kweli. Hata kama yeye aliyasema kiutani mimi nitayafanya kuwa ya kweli kwani nilikuwa nimepanga kumtia mikononi vilivyo. Ufundi wote niliofundwa kwa kungwi nilipanga kuumalizia kwake ili nihakikishe kuwa Mustafa anakuwa haoni wala hasikii juu yangu. Na itakapokuwa hivyo nitajihakikishia kuwa gari ninalipata tu, Mustafa hatakuwa na ujanja! Asubuhi kulipokucha baada ya kumaliza kazi zangu za nyumbani nilimpigia simu Musa kujua kama angekuja siku ile. Nilipomuuliza kama anakuja akanijibu kuwa hakuwa na uhakika wa safari. “Kwa nini?” nikamuuliza. “Tajiri hataki gari lirudi tupu na mpaka sasa sijapata mzigo.” “Kwa hiyo kuna uwezekano usirudi leo?” nikamuuliza. “Uwezekano huo upo.” “Basi utanijulisha itakavyokuwa.” “Sawa.” Baada ya kukata simu nikampigia shoga yangu Amina. “Amina vipi?” nikamuuliza Amina baada ya kupokea simu yangu. “Poa Mishi, za kunisusa?” “Sijakususa shoga, naona wewe ndiyo uko kimya.” “Kawaida tu shoga, si unajua mishemishe?” “Mishemishe zipi hizo shoga yangu? Tuambiane.” “Hizo hizo za kuganga njaa, kwacha hakuchi.” INAENDELEA
 
SEHEMU YA 30:

Siku nyingine akaniambia anaanzisha safari zake mwenyewe lakini kwanza alitaka akanitolee posa nyumbani kwetu ili tuoane.
“Nimeona unafaa kuwa mke wangu,” akaniambia. Kauli yake ambayo sikuitarajia ilinishitua.
“Unataka tuoane?” nikamuuliza.
“Una sifa za kuwa mke wangu.”
“Mh!”
“Mbona unaguna?”
“Umenifanyia sapraizi.”
SASA ENDELEA…
“Hapana. Nadhani ulikuwa unafahamu wakati wote tulikuwa katika maandalizi ya uchumba,” Mustafa akaniambia.
“Mbona hukuwahi kuniambia.”
“Kule kukubaliana kwetu kuwa tunaishi pamoja inatosha kuwa ni taarifa kwetu sote kuwa wakati wowote tunaweza kuoana. Ulitaka nikuambie nini zaidi ya hapo?”
Nikawa sina la kusema. Kwa kweli nilishindwa kumwambia kuwa nilikuwa na mume wangu, asingenielewa na pia malengo yangu ya kuendelea kuwa naye yasingekuwepo tena.
“Niambie baby, sifai kuwa mume wako mtarajiwa?” akaniuliza baada ya ukimya mfupi.
Nikainua uso wangu niliokuwa nimeuinamisha, nikamtazama kisha nikamjibu:
“Unafaa.”
“Au una mwingine zaidi yangu?”
Nikatikisa kichwa haraka.
“Sina mwingine zaidi yako,” nilipomwambia hivyo sauti yangu mwenyewe ilinisuta kwa kusema uongo. Ilitoka ikiwa haina nguvu. Kama angekuwa na akili nzuri angegundua kama namdanganya.
Nikawa najiuliza kama kweli Mustafa amedhamiria kunioa mimi, hiyo posa yangu ataipeleka kwa nani? Kama ni kwa shangazi yangu, si atakwenda kushangaa kuona mke wa mtu anatolewa posa nyingine?
Shangazi ataniuliza imekuwaje napeleka watu wanitolee posa wakati nikijijua ni mke wa mtu? Umbeya wangu utaishia hapo. Mustafa akijua kuwa nilikuwa namtapeli ataniacha siku hiyohiyo.
Kwa hiyo nifanye nini? Nikajiuliza.
Nikapata jibu kwamba nimwambie Mustafa kuwa mimi sikuwa na wazazi, baba yangu na mama yangu walikuwa wameshakufa. Nilikuwa naishi mwenyewe tu. Na akiniuliza kuhusu ndugu yangu yeyote, nimwambie kuwa nilizaliwa peke yangu, sina ndugu. Baada ya kupanga uongo huo nikabaki nao kichwani mwangu hadi siku ambayo Mustafa alirudia tena lile suala.
“Nataka nijitokeze kwenu niwajue wazazi wako,” aliniambia
“Ndiyo unataka kupeleka hiyo posa?” nikamuuliza.
“Ndiyo lengo langu.”
“Sasa ngoja nikwambie kitu, mimi sina wazazi. Sikuwahi kukwambia jambo hilo.”
“Kwa nini huna wazazi?” akaniuliza kwa mshangao.
“Wazazi wangu walishakufa zamani.”
“Sasa unaishi na nani?”
“Naishi mwenyewe tu.”
“Pole sana. Lakini hilo si tatizo, ndugu wengine si wapo?”
“Mimi sina ndugu, nilizaliwa peke yangu.”
“Kweli?”
“Hata ndugu wa mbali pia huna?”
Nikaona nikisema sina ataona mimi ni muongo. Nikatafuta la kumjibu.
“Ndugu wa mbali hawakosekani lakini ndugu ni wale mnaopatilizana. Hao ndugu zangu hatupatilizani. Kila mmoja ana lake. Sina shida nao.”
“Ni kweli, kama ndugu hampatilizani si ndugu tena.”
“Mimi naendesha mambo yangu mwenyewe, sishirikishi ndugu kwa sababu nimeshajihisebu sina ndugu.”
“Sawa. Sasa tutafanyaje?”
“Tunaweza kuoana wenyewe tu.”
“Mahari yako nimpe nani.”
“Nipe mwenyewe. Unataka umpe nani wakati nimeshakwambia sina ndugu?”
“Kwa hiyo mipango ya harusi tutaipanga mimi na wewe tu?”
“Au wewe hupendi iwe hivyo.”
“Kama hapana budi tutafanya hivyo.”
“Kwanza itakuwa nafuu kwako, tunapanga ndoa yetu tunaoana wenyewe kwa utashi wetu vile ambavyo tunataka.” Mustafa alifikiri kidogo kisha akaniuliza:
“Ungependa nikutolee mahari ya kiasi gani?”
“Shilingi milioni mbili,” nikamjibu haraka.
“Nitakupa nusu kwanza.”
“Nataka zote.”
“Nitakupa milioni moja halafu nitakuja kukupa milioni moja nyingine.”
“Kwani ukinipa zote kabisa itakuwaje?”
“Ni makubaliano yetu. Kaka yangu alioa mke alilipa mahari nusu. Baada ya ndoa akamalizia.”
“Sasa na wewe unataka umuige kaka yako?”
“Si kumuiga, ni mipango tu Mishi. Kukupa milioni mbili kwa sasa nitaharibu mambo mengine.”
“Kwani utanipa lini hiyo nusu na hiyo nusu nyingine utanimalizia lini?”
“Naweza kukupa hata kesho, nusu nyingine nitakupa baada ya kuoana.”
“Wewe unataka tuoane lini?”
“Kwa vile tunajipangia wenyewe nataka tuoane haraka iwezekanavyo.”
Nikafikiri kidogo kisha nikamwambia:
“Unaonaje tukioana kwa siri, yaani sitaki hata Amina ajue.”
“Amina anakuhusu wewe, mimi hanihusu.”
“Anakuhusu kupitia kwa Shabir.”
“Kumbe sijakueleza kuwa mimi na Shabir kwa sasa hatuko pamoja?” Mustafa akaniambia.
 
SEHEMU YA 31:

“Unaonaje tukioana kwa siri yaani sitaki hata Amina ajue.”
“Amina anakuhusu wewe, mimi hanihusu.”
“Anakuhusu kupitia kwa Shabir.”
“Kumbe sijakueleza kuwa mimi na Shabir kwa sasa hatuko pamoja?”
SASA ENDELEA…
Tulishatengana na ninahisi fitina zilitoka kwa Amina.”
“Sema kweli.”
“Nakwambia ukweli. Mimi naendelea na biashara zangu.”
“Lakini si unaweza kumualika.”
“Nani…mimi? No! Kwanza urafiki wenyewe haupo. Alinishutumu mbele ya Amina kuwa namuibia pesa zake. Ana pesa gani za kunitambia mimi…?”
“Sasa huyo Amina alimtia fitina gani?” nikamuuliza.
“Ninahisi tu kwamba anaweza kuwa anamtia maneno kutugombanisha kwani tangu alipoanzana naye ndiyo Shabir akaanza kuwa na maneno madogomadogo.”
“Kwani utaratibu wenu wa biashara ulikuwaje?”
“Shabir anapenda pesa lakini ni mvivu wa kazi. Yeye ametoa mtaji lakini ninayefanya kazi ni mimi. Mimi ndiye ninayetafuta oda kwa wafanyabiashara halafu ninakwenda kununua bidhaa zinazotakiwa, aidha Dubai au China, wakati mwingine Japan au India.”
“Unapoleta hizo bidhaa mgawanyo wenu unakuwaje?”
“Siri ya hii biashara ninaijua mimi, wateja wetu wote niliwatafuta mimi na wananijua mimi. Shabir kazi yake ni kuuliza faida.
“Wakati mwingine dola inakuwa juu, faida yetu inakuwa ndogo. Inapofikia hapo anasema nimemuibia.”
“Sasa kama ni hivyo aendelea na biashara mwenyewe.”
“Ndiyo najipanga. Shabir nimeshamrudishia pesa zake zote, hanidai kitu. Nataka nianze kazi na pesa zangu mwenyewe. Ni mtovu wa shukrani lakini mimi ndiye niliyemtajirisha.”
“Sasa umemtajirisha mwenzako, wewe je?”
“Ninajua mwenyewe, kila mtu na akili yake. Nitafanya biashara mwenyewe, uwezo ninao.”
“Utaenda wapi?”
“Nimepanga niende Dubai.”
“Lini?”
“Baada ya kuoana na wewe. Ndiyo maana nataka tuoane haraka.”
Pakapita ukimya mfupi. Mustafa alikuwa ametulia akiwaza. Mimi nilikuwa nikimtazama huku mawazo ya ndoa ya pili yakipita kwenye akili yangu. Nilikuwa nimeshaamua kuoana naye. Nilijua ulikuwa ni utapeli lakini niliamini kuwa usingefahamika.
Baada ya kimya hicho kilichodumu kwa sekunde chache nikamwambia Mustafa.
“Sasa sikiliza, utakaponipa hiyo nusu ya mahari yangu ndiyo tutaweza kupanga harusi yetu itakavyokuwa. Kwa vile itakuwa ndoa ya harakaharaka nataka isiwe na sherehe, iwe kimyakimya tu. Sherehe zitafuatia utakapotulia. Unaonaje?”
“Sawa. Itabidi katikati ya wiki hii nikakutambulishe kwetu.”
“Wapi?”
“Bagamoyo. Baba yangu alishakufa lakini mama yangu yupo ingawa ni mzee sana.”
“Basi nitatafuta siku twende, kwani kuna ulazima wa kulala huko?”
“Tunaweza kwenda na kurudi.”
“Mimi nataka twende asubuhi turudi jioni.”
“Sawa.”
Siku ile tuliyozungumza maneno hayo, siku ya pili yake Musa akawasili kutoka Congo DR ambako alikuwa amepeleka mzigo. Kuondoka kwake kulinipa nafasi ya kutosha ya kuwa na Mustafa.
Aliporudi nikazima simu yangu ili Mustafa asije akanipigia. Usiku wa siku ile aliyorudi nikamuweka kikao Musa.
“Unajua kwamba unaposafiri unaniacha peke yangu?” nikamuuliza.
“Sasa nitafanyaje mke wangu?”
“Lakini unajua kuwa mimi ni mwanamke?”
“Ninajua ndiyo.”
“Na unajua kwamba unaposafiri wakati mwingine unakaa mwezi mzima?”
“Ndiyo ninajua. Kwani unataka kuniambia nini?”
“Nataka kukwambia kwamba, mimi ninaogopa kuishi peke yangu unapoondoka. Naona usalama wangu ni mdogo sana nikiwa hapa.”
“Sasa tufanyeje?”
“Ninataka uajiri mlinzi. Nikilala ndani, nje kuwe na mlinzi.”
“Ni wazo zuri, nitatafuta mlinzi.”
“Tena nataka wale walinzi wa makampuni ya ulinzi. Anakuja jioni anaondoka asubuhi. Mchana hakuna tatizo.”
“Sawa. Nitafanya mpango huo.”
“Yaani ikiwezekana umpate huyo mlinzi kabla hujasafiri.”
“Sawa.”
“Utasafiri lini?”
“Sijajua bado.”
“Utajua lini?”
“Ni mpaka niambiwe na tajiri.”
“Safari zenu hazieleweki, kesho tu unaweza kuambiwa kuna safari. Kwa hiyo ni vizuri uwahi kwenda kwenye hizo kampuni za ulinzi. Vile ukiondoka ujue mlinzi ameshapatikana.”
“Sawa.”
Siku ya pili yake Musa alikwenda kufuatilia suala la mlinzi. Akanipigia simu na kunijulisha kuwa ameshapeleka maombi ya kuletewa mlinzi.
“Atakuja lini kuanza kazi?” nikamuuliza.
“Atakuja kesho.”
“Sawa.”
Nilimtaka mlinzi huyo kwa akili yangu kwani nilishapanga kuhamia nyumbani kwa Mustafa pindi mume wangu awapo safarini, hivyo nilitaka nyumba yetu iwe inalindwa usiku ili wezi wasije wakatuibia.
Siku iliyofuata mlinzi akaja nyumbani. Musa alikwenda ofisini kwao akamchukua na kuja kumuonesha nyumba. Nilionana naye tukasalimiana.
Musa akamwambia kwamba mimi ndiye mama mwenye nyumba na kwamba atakuwa anawasiliana na mimi. Nikachukua namba yake na yeye akachukua yangu.
“Tuna utaratibu wa kubadilishwa mara kwa mara lakini itakapokuwa hivyo nitakujulisha,” mlinzi huyo akaniambia.
“Hakuna tatizo,” nikamjibu.
Kutoka siku ile nyumba yetu ikawa na mlinzi. Alikuwa anakuja saa kumi na mbili jioni na kuondoka saa moja asubuhi. Anapokuja ananijulisha na anapoondoka asubuhi pia ananipa taarifa.
Baada ya mlinzi huyo kuanza kazi, siku mbili zilizofuata Musa akaondoka tena kwenda Burundi.
Wakati wote Musa alipokuwepo nilikuwa nikimpigia simu Mustafa kisirisiri na kumdanganya kwamba nilikuwa nimekwenda kwenye msiba wa rafiki yangu uliotokea ghafla huko Kisarawe.
Je, nini kiliendelea?
 
SEHEMU YA 32:

Kutoka siku ile nyumba yetu ikawa na mlinzi. Alikuwa anakuja saa kumi na mbili jioni na kuondoka saa moja asubuhi. Anapokuja ananijulisha na anapoondoka asubuhi pia ananipa taarifa.
Baada ya mlinzi huyo kuanza kazi, siku mbili zilizofuata Musa akaondoka tena kwenda Burundi.
Wakati wote Musa alipokuwepo nilikuwa nikimpigia simu Mustafa kisirisiri na kumdanganya kwamba nilikuwa nimekwenda kwenye msiba wa rafiki yangu uliotokea ghafla huko Kisarawe.Siku ile ambayo Musa aliondoka nikampigia na kumwambia kuwa nimesharudi.SASA ENDELEA…
“Mmemaliza msiba?” Mustafa akaniuliza.
“Tumemaliza leo.”
“Unadhani lini tutakwenda Bagamoyo?”
“Twende kesho.”
“Nilishamfahamisha mama yangu kuhusu uchumba wetu amependa nikupeleke akakuone.”
“Sawa.”
“Kwa hiyo kesho nitakufuata asubuhi twende.”
“Nifuate saa tatu mahali petu palepale.”
“Poa.”
Nikakata simu. Siku iliyofuata niliamka mapema nikijua kuwa nina safari ya Bagamoyo. Nilifanya usafi wa nyumbani kwangu nikapika chai. Nilipoitia chai kwenye chupa nikaenda kuoga. Nilipotoka kuoga tu nikanywa chai kisha nikaenda kuvaa.
Kwa vile nilikuwa napelekwa ukweni, nilivaa nguo za heshima. Nilivaa dera la bei kubwa ambalo alininunulia Musa.
Saa mbili na nusu nikatoka nyumbani. Nilifunga mlango nikaondoka. Nilikwenda katika ule mtaa ambao mara nyingi Mustafa huniacha hapo anaponirudisha na gari.
Nilipofika hapo zilikuwa zimebaki dakika chache kuwa saa tatu kamili. Nikasimama kando ya barabara kuisubiri gari ya Mustafa. Zile dakika nilizosimama nilikuwa nikikodolewa macho na kila mpita njia.
Ili kujipa shughuli, nilitoa simu yangu nikampigia Mustafa. Simu ilichelewa sana kupokelewa mpaka nikapata wasiwasi. Nikiwa nimekata tamaa ya kupokelewa simu ndipo Mustafa alipopokea simu.
“Mbona hupokei simu?” nikamuuliza bila hata salamu.
“Unajua ninaendesha na nilikuwa sehemu mbaya, sikuweza kupokea.”
“Unakwenda wapi?” nikamuuliza tena huku sauti yangu ikinguruma.
“Ninakufuata wewe.”
Nikanyamaza. Mustafa alipoona nipo kimya akakata yeye simu.
Baada ya sekunde chache tu nikaliona gari lake linakuja. Lilisogea hadi kando ya miguu yangu likasimama.
Nilifungua mlango wa upande wa pili wa dereva nikajipakia na kukaa kando ya Mustafa.
“Umekuja muda mrefu?” Mustafa akaniuliza baada ya kuona nimekunja uso.
“Nimekuja muda mrefu ndiyo, halafu hupokei simu.”
“Kwani tulipatana tukutane saa ngapi?”
Sikujibu swali hilo kwani niliyetoa muda wa kukutana nilikuwa mimi na muda aliofika ulikuwa ndiyo huohuo.
“Kama uliwahi kuja ni wewe mwenyewe. Tulikubaliana nikufuate saa tatu na sasa ni saa tatu na dakika mbili.”
Wakati Mustafa akisema nilitoa kioo kutoka kwenye mkoba wangu nikakiweka mbele ya macho yangu na kuuweka sawa uso wangu.
Nilipoona Mustafa amenyamaza nilikirudisha kile kioo kwenye mkoba.
“Si hatutalala?” nikamuuliza.
“Sina mpango wa kulala kule. Tukimaliza mazungumzo na mama tunarudi.”
Mvua ilitunyeshea njiani. Ilianza kidogodogo, mwisho ikawa mvua kubwa.
Wakati tunaendelea na safari, mvua ikaacha. Mji huo wa Bagamoyo nilikuwa siufahamu. Niliujua siku ile nilipokwenda na Mustafa. Ulikuwa mji wa kiasili ambao tuliusoma shuleni katika masomo ya historia. Siku ile nilivutika sana kuuona.
Nilishuhudia mahoteli makubwa makubwa na maeneo mengine ya kiasili yaliyowekwa kwa ajili ya watalii.
Mustafa aliniambia kulikuwa na hoteli za bei ghali kuliko zilizoko Dares Salaam.
“Wanapangisha wazungu tu na vigogo.”
“Siku moja na sisi tuje tupangishe chumba tulale huku.”
“Ngoja nitatafuta siku tutakuja.”
Licha ya Mustafa kumiliki gari la kifahari, nyumba yao ilikuwa ya kawaida, sawa tu na ile aliyokuwa akikaa shangazi yangu.
Baada ya kulisimamisha gari, tuliingia ndani. Nilimuona mama yake. Alikuwa amekaa sebuleni. Alikuwa mwanamke mnene na mfupi. Nilimkadiria umri wake kuwa ulishafikia miaka themanini.
Alikuwa amevaa dera na alikuwa amejitanda khanga kichwani.
Baada ya kumuamkia, Mustafa alimwambia hapohapo:
“Mama nimekuletea mkwe wako umuone.”
“Ndiye huyo uliyekuja naye? Mama huyo aliuliza kisha akaongeza:
“Macho yangu siku hizi hayaoni vizuri kwa uzee. Karibu mwanangu.”
“Asante mama, unajisikiaje hali yako?’ nikamuuliza.
“Sijambo kidogo. Miili ya kizee haiachi kuumwaumwa lakini sijambo. Nashukuru.”
Mustafa akanitazama mimi na kuniuliza:
“Mishi umemuona mama yangu?”
Kabla sijajibu, sauti ya mama mkwe ikanikatiza:
“Mbona hamkai. Mustafa mkaribishe mwenzako.”
Tukakaa kwenye kochi moja. Fanicha zilizokuwa hapo sebuleni zilihitaji sana kufanyiwa ukarabati. Nilimshangaa sana Mustafa kumiliki gari zuri na kupanga katika nyumba nzuri lakini ameshindwa hata kumnunulia mama yake fanicha mpya.
Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 33:

Fenicha zilizokuwa hapo sebuleni zilihitaji sana kufanyiwa ukarabati. Nilimshangaa sana Mustafa kumiliki gari zuri na kupanga katika nyumba nzuri lakini ameshindwa hata kumnunulia mama yake fenicha mpya. Wanaume wengine wa ajabu sana.
SASA ENDELEA…
Sasa mmepanga kuoana lini?” mama mkwe akaniuliza.
“Hatujapanga siku, nimemleta kwanza muonane mjuane,” Mustafa akamjibu.
“Tumeshaonana, tumeshajuana na tutajuana zaidi, sasa swali linakuja mtaoana lini?”
Mama alikuwa mswahili kweli.
“Ndiyo tuko kwenye mipango,” Mustafa akamjibu.
“Sikiliza Mustafa, wewe ni mwanangu na mimi ni mama yako. Kama umeshapata mchumba ambaye umempenda na yeye amekupenda, nataka muharakishe kuoana. Msiendelee kuishi hivyohivyo ni haramu.”
“Mpaka nimemleta hapa ujue kuwa mambo yamekaribia. Usifikiri kwamba tunaishi hivihivi, tumepanga kuoana na tutaoana.”
“Inshaallah. Na wewe sema inshaallah.” mama mkwe akamwambia mwanaye.
“Inshaallah,” Mustafa akamfuatisha mama yake aliyeonekana kuwa mtu wa dini sana.
“Kila jambo jema linaongozwa na Mungu, lazima useme inshaallah.”
“Inshaallah,” na mimi nikatia mkazo.
“Japokuwa nimekuwa mzee lakini nitafurahi sana kama mtaharakisha kuoana na nawaombea Mungu awe nanyi katika mipango yenu.”
”Twashukuru mama, asante,” nikamwambia.
Mustafa mwenyewe alikuwa akitabasamu tu. Baada ya mazungumzo marefu na mama mkwe tulimuaga.
“Mimi nilijua mtalala hapa,” mama mkwe akauliza.
“Tutalalaje hapa mama, si unajua kazi zetu,” Mustafa akamwambia.
“Kazi zenu zina nini?”
“Yaani tukilala huku kazi zetu zitaharibika.”
“Wewe kila siku ni kazi tu, huna siku unayosema nikalale kwa mama. Kazi mpaka lini mwanangu?”
“Nitatafuta siku mama, nitakuja kulala. Usijali.”
Tukaondoka kurudi Dar. Mustafa alikuwa amefurahi kwa sababu mama yake alikuwa amempa baraka zote za ndoa yetu.
“Sitamuarifu tena, siku tukienda tena ninamwambia tumeshafunga ndoa,” Mustafa akaniambia.
“Kwa hiyo tutaoana peke yetu?”
“Watakuwepo ndugu na jamaa.”
“Lakini usisahau nilivyokwambia.”
“Vipi?”
“Tuoane hivyohivyo kimyakimya, sherehe tutafanya baadaye.”
“Kwa nini hupendi tuchanganye na sherehe pamoja?”
“Tutachelewa kuoana, mambo yatakuwa mengi. Tuoane kwanza halafu ndiyo tupange sherehe.”
“Sawa.”
Ingawa Mustafa alinikubalia, hakuelewa maana yangu hasa ya kutaka tufanye sherehe hizo baadaye na pia kutaka ndoa yetu ifanyike kimyakimya.
Tayari nilikuwa mke wa mtu na sikuwa nimeachika hivyo sikutaka ijulikane kuwa ninaolewa tena, ndiyo sababu nikataka ndoa hiyo ifanyike kimyakimya.
Na pia akili yangu ya kutaka sherehe ifanyike baadaye ni kuwa atakaponioa suala la sherehe nitalipotezea mbali. Hatutaifanya tena kwani sherehe itahusisha watu wengi, huenda wakawepo wanaonijua.
Kutoka siku ile nikawa namuhimiza Mustafa kuhusu suala la ndoa kwa vile Musa alikuwa bado yuko Burundi.
“Unasikia Mustafa, tuharakishe kufunga ndoa kwanza, ndoa haina gharama ni kupanga siku tu. Baada ya hapo ndiyo tutapanga mambo mengine, nilikuw
a nikimwambia Mustafa.
Siku moja Mustafa akanipa nusu ya mahari yangu shilingi milioni moja akaniambia kesho yake ndiyo tutaoana. Nilikwenda kuziweka benki zile pesa.
Kwa vile nyumbani kwangu kulikuwa na mlinzi, katika kipindi hicho nilikuwa nalala kwa Mustafa. Mlinzi nilikuwa nampa posho ndogondogo ili anitunzie siri.
Kwa hiyo ilikuwa rahisi kukamilisha mipango ya ndoa yetu. Ile siku ambayo Mustafa alipanga kunioa nilikwenda saluni asubuhi kutengenezwa nywele na kupambwa kisha nikarudi.
Niliporudi Mustafa akaja na shehe na mashahidi wawili.
Wakaniuliza jina langu. Nilipowaambia wakaniuliza walipo wazazi wangu.
“Wazazi wangu wameshakufa,” nikawajibu.
“Wazazi wako wote wawili wamekufa?” shehe akaniuliza tena ili apate uhakika.
“Baba na mama wameshakufa.”
“Huna ndugu wengine kama vile kaka?”
“Nilizaliwa peke yangu.”
“Sasa walii wako atakuwa nani?”
“Walii ni nani?” nikamuuliza.
“Walii ni baba atakayekutolea idhini nikuozeshe.”
“Nitajitolea idhini mwenyewe.”
“Kwani ulishawahi kuolewa chuo cha kwanza?”
Nikatikisa kichwa haraka.
“Hapana sijawahi kuolewa.”
“Itabidi upate walii. Huwezi kujiidhinisha mwenyewe.”
“Sasa nitampata wapi mimi.”
“Basi mimi nitakuwa walii wako kama utanikubali na pia ndiye nitakayewaozesha. Wewe utakuwa kama mwanangu.”
“Sawa.”
Shehe akamtazama Mustafa.
“Mimi nitakuwa walii wake wa kumsimamia, ndoa ni lazima walii. Halafu mimi nitawaozesha,” akamwambia.
“Sawa,” Mustafa akamjibu.
Baada ya hapo shehe akaniambia kuwa kutoka muda ule ninatakiwa kukaa chumbani kama mwari na nivae nguo za sitara na nijitande mtandio kama biharusi kwani saa chache baadaye atatufungisha ndoa.
Niliambiwa kuwa ndoa hiyo itafungwa msikitini lakini mimi nitabaki nyumbani. Baada ya ndoa ndiyo Mustafa angekuja kunipa mkono.
Ilikuwa kweli. Ilipofika saa mbili usiku ndoa ikafanyika. Nyumbani nilikuwa mimi na ndugu wachache wa Mustafa waliokuwa wakiishi palepale
 
SEHEMU YA 34:

Nikakata simu na kujitayarisha kutoka. Nilijitayarisha harakaharaka ili Mustafa asije akarudi na kuniambia atanipeleka kwa gari.
Nilipokuwa tayari nilitoka, nikafunga nyumba na kutafuta teksi iliyonipeleka Kimara kwa mume wangu wa kwanza.
Nilipofika tu nikampigia simu Musa.
“Baby wangu umzima?” nikajidai kumwambia kwenye simu.
“Mimi ni mzima tu, sijui wewe mke wangu?” Musa akanijibu.
SASA ENDELEA…
“Mimi pia ni mzima. Mmeshaondoka mpakani?”
“Tumeondoka tangu alfajiri.”
“Mtafika Dar saa ngapi?”
“Kila ilivyo tutaingia usiku.”
“Kwa hiyo nisikuwekee chakula?”
“Usiniwekee.”
“Poa. Safari njema mume wangu.”
“Poa.”
Baada ya kumzuga Musa na kujiona yeye ndiye kidume peke yake nilikata simu.
Hawa wanaume wamezoea kutuchezea sisi wanawake, ngoja na mimi niwachezee. Nikajiambia kimoyomoyo wakati liliponijia wazo kuwa mtindo niliokuwa nikiutumia wa kuwa na waume wawili haukuwa wa kiungwana.
Kwa vile nilikuwa sina kazi ya kufanya nikampigia simu Amina.
Amina alipopokea simu aliniambia haraka:
“Siku hizi umekuwa mswahili shoga yangu.”
“Siyo hivyo shoga, ile jana simu yangu iliisha chaji ghafla. Sijui yule fundi alinibadilishia betrii yangu!” nikampiga uongo. “Mara simu ilikuwa mbovu, mara betrii imebadilishwa, siku hizi hueleweki.”
“Aaah…niamini shoga. Mbona muda huu nimekupigia?”
“Mimi naona si bure..!”
Aliposema hivyo nilishituka nikajidai kucheka.
“Kwa nini unaniambia hivyo?” nikamuuliza ili kama amesikia jambo anieleze.
“Naona shoga si bure, iko namna. Hutaki tu kuniambia.”
“Hakuna kitu, kama kipo tungekwishaambizana. Vipi Shabir hajambo?” nikabadili ile mada ghafla.
“Hajambo.”
“Yupo au amesafiri?”
“Amejaa tele kama pishi ya mchele.”
“Rafiki yake Mustafa naye yupo?”
“Mh! Mustafa walikwishatengana, siku hizi kila mmoja ana biashara yake.”
“Unasema ukweli shoga?”
“Yule jamaa alikuwa mjanja sana, anamtia hasara mwenzake.”
“Anamtia hasara kivipi?”
“Nafikiri alikuwa anamuibia pesa.”
“Sasa utakuja lini nyumbani tuzungumze?”
“Nitakuja.”
“Niambie siku.”
“Naweza kuja hata kesho.”
“Poa. Njoo kesho. Utakuja saa ngapi?”
“Nitakuja asubuhi.”
Baada ya kuzungumza na Amina nikaiweka simu yangu pembeni na kufikiria kwenda kupika.
Siku ile nilishinda nyumbani. Mlinzi alipokuja jioni nilikutana naye.
“Leo upo?” akaniuliza.
“Nimerudi tangu asubuhi. Nilikuwa safarini,” nikamdanganya.
Nilidhani angeniuliza nilikwenda wapi lakini hakuniuliza. Nikatoa shilingi elfu kumi na kumpa.
“Asante,” akanishukuru kisha aliniambia:
“Mwenye nyumba naye sijamuona muda mrefu.”
Alikuwa akimaanisha mume wangu.
“Yupo safarini lakini atarudi leo. Unaweza kumuona usiku.”
“Sawa.”
Baada ya hapo nikarudi ndani. Nilimsubiri Musa nilipoona hatokei nikaenda kulala.
Akaja kuniamsha saa saba usiku kwa kunipigia simu. Simu iliita sana mpaka nilipozinduka nikaipokea.
Sikutazama nani aliyekuwa anapiga. Nilikimbilia kuipokea na kuuliza:
“Nani?”
“Mimi Musa, nifungulie mlango.”
“Uko nje?” Nikamuuliza.
“Ndiyo niko nje.”
“Subiri.”
Nikashuka kitandani na kujifunga khanga kisha nikatoka. Nilikwenda kwenye mlango wa mbele nikaufungua. Musa akaingia.
“Karibu,” nikamwambia huku nikimpokea begi lake.
Tuliingia chumbani. Musa akaenda kuoga. Wakati anaoga nilifungua begi lake na kuchunguza vitu vilivyokuwemo.
Nilikuta nguo zake, chupa tatu za pafyumu na vitu vyake vingine. Nilipopekuapekua zaidi nikakuta kipakiti cha kondomu kilichotiwa kwenye soksi.
“Ha!” nikashituka.
“Kondomu hizi ni za nini?” nikajiuliza.
Hapo ndipo nilipopata mawazo kuwa mume wangu naye amekuwa muasherati kama mimi. Niliichukua ile pakiti ya kondomu kisha nikarudisha vile vitu kama nilivyovikuta.
Ingawa hatua yangu ya kuolewa kwa mara ya pili ilikuwa ya kuchukiza zaidi, nilikerwa kuziona zile kondomu. Nilijua kuwa mume wangu alikuwa na wasichana wengi huko vijijini anakopita.
Maisha ya mimi na yeye yalikuwa mfano wa miguu na mikono ya nzi. Nzi anapoisugua mikono na miguu yake, waswahili wana tafsiri zao. Wanasema “Wewe ukijua hivi na mwenzako anajua hivi.”
Lakini nilishukuru kwamba Musa anajua umuhimu wa kutumia kondomu, vinginevyo tungeuana.
Pamoja na kujikaza lakini moyo wangu haukukubali kumuachia, nilimngoja kwa hamu atoke bafuni.
Nilipomuona anatoka tu nikamuonesha ile pakiti yake ya kondomu na kumuuliza.“Kondomu hizi ni za nini?”
Musa alishituka sana.
Je, nini kiliendelea?
 
Sure.. Bahati mbaya sikumbuki lilikuwa ni gazeti lipi ila no miongoni ya yanayo milikiwa na shigongo..

Na nilikuwa msomaji kipindi hicho[emoji28]
Ilikuwa ijumaa ndio walikuwa wanaandika story hii hata ukiitafuta kwenye mtandao bado ipo
 
SEHEMU YA 35:

Aliondoka asubuhi akiwa hana habari ya safari. Baadaye mchana alirudi akaniambia kuwa atakuwa na safari.
“Utaondoka saa ngapi? Nikamuuliza haraka.
“Nitaondoka usiku. Hivi sasa gari iko bandarini inapakia mzigo.”
“Hapa nyumbani utaondoka saa ngapi?”
“Nimekuja kuchukua begi langu, nikiondoka ndiyo nimeondoka. Sitarudi tena.” SASA ENDELEA…
“Poa,” nikajisemea.
Hivyo ndivyo nilivyokuwa nataka.
“Hutawahi kula chakula?” nikajidai kumuuliza.
“Kwani umeshapika?”
“Ndiyo ninapika.”
“Sitakisubiri, acha niende. Nitakula hukohuko.”
“Hao matajiri zenu wanapenda kuwapa taarifa za ghafla sana. Ilitakiwa wakwambie mapema kuwa utakuwa na safari.”
“Ndiyo kazi zetu zilivyo. Tumeshazoea.”
“Poa. Safari njema.”
Musa alichukua begi lake akatia vitu alivyovitaka kisha akaniaga. Wakati anatoka nikamuuliza:
“Kondomu zako huzihitaji tena?”
Musa aligeuka mara moja akanitazama kisha akasema:
“We’ acha mzaha wako.”
Nilisimama kunako mlango nikamtazama alivyokuwa akitembea kuelekea kwenye kituo cha daladala. Wakati namtazama mawazo ya Mustafa yakaanza kunijia.
Nikarudi ndani na kufunga mlango. Niliketi kwenye sebule nikajiambia kuwa sitapika tena. Nitakwenda kupika kwa Mustafa.
Nilisubiri yapite masaa mawili nikatia baadhi ya vitu vyangu kwenye mkoba wangu kisha nikatoka. Sikuchukua nguo. Nilikwishahamishia kwa Mustafa baadhi ya nguo zangu na viatu. Nilichukua vitu vidogovidogo tu ambavyo Mustafa asingeweza kuvizingatia.
Kabla ya kwenda Mbezi nilipitia sokoni nikanunua vitu ambavyo nilihitaji kupika. Nilipofika Mbezi Mustafa alikuwa hayupo. Kwa vile nilikuwa na funguo zangu nikafungua mlango na kuingia ndani.
Niliingia chumbani nikabadili nguo kisha nikazima simu yangu na kuiweka kwenye chaji ili Mustafa akija aone simu iko kwenye chaji. Sikutaka anipigie wala sikutaka Musa anipigie.
Baadaye nikatoka chumbani na kuelekea jikoni na kuanza kupika.
Yalikuwa majira ya saa kumi na moja Mustafa aliporudi nyumbani na kunikuta nimeketi sebuleni nikiangalia CD ya filamu ya Kihindi.
“Mbona hukunifahamisha kama umeshakuja?” akaniuliza.
“Kwani ulitaka kuleta msichana wako?”
“Mishi acha mzaha wako, una ‘surprise’ za ajabu sana. Halafu nilikupigia ukawa hupatikani.”
“Simu ilikuwa kwenye chaji. Mimi mwenyewe nilikuwa jikoni napika.”
“Kwani ulikuja saa ngapi.”
“Tangu saa sita niko hapa.”
Nilimdanganya. Muda niliofika, saa sita ilikuwa imeshapita.
“Umepika nini?”
“Nimepika wali na nyama.”
Nilipomwambia hivyo Mustafa aliinuka na kuelekea chumbani. Baadaye alirudi tena sebuleni. Alionekana alikuwa anatoka kuoga.
Tukaendelea na mazungumzo.
Kabla ya mwezi mmoja kukamilika Mustafa akaenda India. Alipoondoka tu nikarudi kwa Musa. Musa aliporudi kutoka Burundi alinikuta nipo nyumbani.
Kwa vile safari zake nyingi zilikuwa za Burundi, alipoondoka tena kwenda Burundi nikahamia Mbezi kwa Mustafa. Mustafa alikaa India kwa wiki nzima. Aliporudi alinikuta nipo nyumbani kwake.
Baada ya mwezi mmoja nikajikuta nina mimba. Sikujua ile mimba ilikuwa ni ya nani lakini nilikisia kuwa ilikuwa ya Mustafa. Nikaitambulisha mimba yangu kwa waume wote wawili. Kila mmoja akajua nina mimba na mimba ni yake.
Kwa vile waume wangu wote wawili walikuwa wakisafiri nje ya nchi na wakiwa huko hukaa kwa zaidi ya wiki. Niliendelea kutumia mtindo uleule wa kuhamia kwa mwanaume mmoja pindi mwenzake anaposafiri.
Kwa bahati njema walikuwa wakisafiri kwa nyakati tofauti hivyo kuniwezesha mimi kuweza kuwa kwa mwanaume mmoja pale mwenzake anapokuwa hayupo. Ile mimba iliendelea hadi ikatimiza miezi tisa. Hakukuwa na mwanaume wangu yeyote aliyegundua kuwa mimba hiyo ilikuwa ya watu wawili.
Kuna siku Mustafa alikuwa amekwenda China kununua bidhaa. Lakini Musa alikuwepo na nilikuwa nyumbani kwake. Musa akaniambia kwamba anataka asafiri lakini anasita kwa sababu naweza kuumwa na uchungu wakati wowote na nitakuwa peke yangu.
Wakati akiniambia hivyo Mustafa alishanipigia simu kunijulisha kuwa anarudi kesho yake.
Nikamwambia Musa kuwa anaweza kwenda safari.
“Mimi nitakwenda kwa shangazi.”
“Shangazi ataweza kukuhudumia?” akaniuliza.
“Kwa nini asiweze. Yeye mwenyewe ameniambia niende.”
“Kama ameshakwambia basi unaweza kwenda, acha mimi niende safari.”
Siku ile Musa akaondoka. Sikwenda kwa shangazi. Musa alipoondoka nikaenda Mbezi kwa Mustafa.
Mustafa alirudi siku iliyofuata na siku hiyohiyo nikaumwa na uchungu. Mustafa alinikimbiza na gari hospitali. Nikajifungua usiku mtoto wa kiume. Alikuwa amefanana sana na Mustafa.
Mustafa alikuja hospitali asubuhi akamkuta mtoto ameshazaliwa. Akampa jina hapohapo.
“Mwanangu ataitwa Amani,” akaniambia.
Nikatabasamu na kumuuliza:
“Umempa jina la nani wako?”
“Ni jina la babu yangu mzaa mama yangu,” akaniambia.
Je, nini kiliendelea?
 
Back
Top Bottom