SEHEMU YA 09:
“Nawapongeza kwa kufikia uamuzi huo lakini nataka uje unitambulishe kwa mchumba wako kabla hamjafunga ndoa. Unajua sijawahi kukutana naye!”
“Basi subiri Jumapili, tutakuwa hoteli fulani nitakuita.”
“Hapahapa Ilala?”
“Ndiyo, itakuwa hapahapa Ilala.”
“Saa ngapi?”
“Itakuwa midamida ya usiku.”
“Poa. Nataka nimuone tujuane kabla ya ndoa yenu.”
“Usijali.”
SASA ENDELEA…
aada ya mazungumzo yetu na Amina tuliagana, Amina akaondoka.
Kwa kawaida kila siku ya Jumapili, kama Musa hakwenda safari huwa tunakutana katika hoteli moja pale Ilala. Tunakula chakula cha usiku na kuzungumza machache kisha anaondoka zake.
Jumapili ilipowadia Amina alinipigia simu kunikumbusha juu ya ile ahadi yetu. Nikamwambia kuwa ninaikumbuka.
“Tutakapokuwa wote nitakupigia,” nikamwambia nikimaanisha nitakapokuwa na mchumba wangu Musa nitampigia ili aje.
Saa moja usiku Musa akanipigia simu kunijulisha kuwa ameshafika hapo hotelini. Hapakuwa mbali sana na nyumbani kwetu. Na mimi nikampigia Amina.
Nikamwambia nikutane naye hapo hotelini. Baada ya kumweleza hivyo nikaanza mwendo wa miguu kuelekea huko hotelini. Nikiwa njiani nilimpigia tena Musa kumjulisha kuwa nitakuwa na rafiki yangu.
“Nani?” Akaniuliza.
“Humjui, ndiyo nataka nikutambulishe.”
“Anaitwa nani.”
“Amina.”
“Uliwahi kunitajia jina lake lakini sijawahi kukutana naye.”
“Ndiyo nataka leo umuone mjuane.”
“Sawa. Ninawasubiri.”
“Poa.”
Nikakata simu.
Wakati nafika pale hotelini nilikutana na Amina kwenye mlango.
“Eh! Shoga umekuja na bodaboda nini?” Nikamuuliza kwa mshangao.
“Kwa nini?” Akaniuliza.
“Jinsi ulivyowahi ni kama uliyekuja na usafiri.”
“Hapana nimekuja kwa miguu tu,” Amina aliniambia kisha akacheka.
“Au ni hamu ya kumuona shemeji yako?” Nikamuuliza kwa mzaha.
Amina akaendelea kucheka.
“Umejuaje?”
Aliponiambia hivyo tukacheka sote.
“Wala usiumie shoga, shemeji yako utamuona leo tena yeye ameshafika,” nikamwambia.
“Yuko wapi?”
“Yuko ndani.”
“Twen’zetu nikamuone.”
Tukaingia ndani ya hoteli. Tulimkuta Musa akiwa amekaa kwenye meza ya peke yake akitusubiri. Nilimuona akitafunatafuna, nikajua alikuwa anatafuna mirungi kisirisiri. Mezani kwake kulikuwa na chupa ya cocacola na ya maji safi.
Alipotuona alijifuta midomo yake kwa kitambaa kisha akakaa vizuri.
“Vipi unasaga?” Nikamuuliza.
“Umejuaje?”
“Si nimekuona unatafuna halafu umeweka chupa ya maji na cocacola.”
“Nilikuwa namalizia miti yangu ya mchana. Sijui hii tasnima yangu nitaiweka wapi?”
“Tasnima ndiyo nini?”
Nikavuta kiti na kuketi. Amina naye akaketi.
“Hili tonge la mirungi lililoko mdomoni,” Musa akanijibu.
“Ndiyo linaitwa tasnima?”
“Ndiyo.”
“Na ninyi mna maneno ya ajabuajabu, eti tasnima!” Nikamtazama Amina kisha nikacheka.
Nilijua Amina pia alitaka kucheka lakini alijikaza kwa kumuonea aibu shemeji yake.
“Amina shemeji yako huyo, umuone, umjue, umfahamu,” nikamwambia Amina.
“Shemeji habari za siku?” Amina akamsalimia Musa huku akimpa mkono.
“Nzuri shemeji.”
“Musa huyo ni rafiki yangu kipenzi, anaitwa Amina,” nikamwambia Musa.
“Oh! Nimefurahi kumfahamu, karibu shemeji.”
“Sasa hilo tasnima lako si uende ukalitupe nje,” nikamwambia Musa.
“Hili halitupwi, linahifadhiwa tu kisha baadaye ninalirudisha mdomoni.”
“Amina unawasikia watu wa mirungi hao?” Nikamuuliza Amina.
“Lakini si uliniambia hata wewe unakula,” Amina akaniambia.
“Nakula lakini siyo kivile.”
“Sasa ni nyote.”
“Hebu nisaidie shemeji yangu, asinisakame mimi kumbe na yeye pia yumo,” Musa akasema.
Kikafuatia kicheko.
“Hebu kalitupe bwana…” nikamwambia Musa baada ya kucheka.
Musa akainuka na kutoka.
“Naona mnapendana sana,” Amina akaniambia.
“Umeona eeeh!”
Mhudumu akatufuata na kukatiza mazungumzo yetu. Alitupa menyu. Nikaangalia orodha ya vyakula kisha nikamwambia.
“Ngoja bwana mkubwa aje.”
Mhudumu huyo akaondoka.
Musa aliporudi nikamuuliza.
“Tutakula nini?”
“Kila mtu atakula anachopenda.”
“Mimi nataka chipsi kuku,” nikasema kisha nikamtazama Amina.
“Utakula nini Amina?” Nikamuuliza.
“Nitakula hizohizo chipsi kuku.”
Je, nini kiliendelea? Usikose kufuatilia