Sehemu ya 48.
Haikupita hata nusu saa Eliza aliingia, mimi ndiye niliyetangulia kumwona akiingia, kwani nilikaa kutazama getini.
"Anakuja," nilisema, japo ilikuwa giza tayari lakini macho yangu bado imara sana.
Eliza alipofika, alisimama kwa muda bila kukaa huku akiniangalia kisha akamuangalia dada Light na kumalizia na mumewe.
"Kaa sasa," alisema mumewe akimuonyesha kiti. Kulia kwa mume wa Eliza alikaa da Light, kushoto kwake nilikaa mimi. Kwa hiyo kama mkewe angekaa angekuwa ametenganishwa na mmi na dada Light kitu ambacho wapenzi huwa hawakai hivyo hata siku moja.
Kisirani alichokionyesha Eliza siku hiyo naamini hakuwahi kukionyesha hata siku moja. Naamini hata da Light alishangaa, lakini bado ukweli ulikuwa pale pale kwamba, hata ningekuwa mimi, kuwakuta majirani wamekaa na mume wangu vile nisingependa. Kama si watu wabaya kwangu wangeniambia tuko sehemu fulani na shemeji.
Alivuta kiti na kukaa kisha akamuita mhudumu. Uzuri ni kwamba, hakuna aliyemuonyesha kwamba labda tulikuwa tumemdharau, kwani muda huo huo da Light alikumbuka kwamba, alipokaa sipo.
"Shoga angu njoo ukae hapa," alisema dada huku akiinuka na kumpisha Eliza akae jirani na mumewe. Naye alikwenda kukaa, kidogo akachangamka na kuchangamka.
Mhudumu alipofika aliagiza mchemsho wa samaki, kisha akaagiza na bia moja ya baridi.
Licha ya hali hiyo, lakini Eliza alionekana kutokuwa na amani na mimi kwani alikuwa akiniangalia kwa kuniiba lakini kwa jicho kali sana.
Imavyoonekana moyoni mwake aliamini kuwa, kwa vyovyote vile mimi na mumewe ilikuwa 'ile mbaya'. Lakini alikuwa anashindwa kusema kwa sababu na mimi nina madhambi yake.
Angesema na mimi ningesema, mbaya zaidi yeye anayemwibia alikuwa naye pale pale, angeona joto lake.
Kuna wakati niliaga nakwenda maliwatoni, nikasimama. Kumbe nyuma yangu mume wa Eliza naye akasimama, naye akaenda maliwatoni yao wanaume.
Mimi nikiwa huko simu yangu ikaita, kuangalia namba ni za mume wa Eliza, kwanza niliogopa kwani nilijua huenda ni Eliza amechukua simu ya mumewe kunipigia, lakini nikasema acha nipokee nimsikie anachosema.
Itaendelea......