Simulizi: Tugawane Maumivu

Simulizi: Tugawane Maumivu

Sehemu ya 39.

"Mdogo wangu kukaguliwa ndiyo sitaki, lakini kweli nilikuwa na jamaa fulani sehemu," Eliza alininong'oneza sikioni.
"Wapi?"
"Mabibo."
"Jamaa mwenyewe siyo shemeji?"
Nilimuona Eliza akijiumauma huku akishindwa kuniangalia.

"Enhe vipi?" shemeji alitokea.
Eliza na shemeji walipoangaliana macho, kila mmoja alionesha tabasamu laini. Kama dada Light angekuwepo naamini pale pale angeisoma hali fulani na pale pale ndio ingekuwa mwanzo wa uchunguzi wake.

Itaendelea.....
 
Sehemu ya 40.

Sikutaka kwenda chumbani kwangu kulala, nilichotaka ni kujua shemeji ataamuaje kuhusu tatizo la Eliza.
"Shemeji nilikuwa naomba nilale hata hapa sebuleni mpaka asubuhi nitaenda kwa ma mdogo Kimara," alisema Eliza.

Shemeji akatabasamu tena.
"Utalalaje shemeji sebuleni, kalale na Maria chumbani kwake," alisema shemeji bila kuuliza upande wa pili wa mume wa Eliza utakavyochukulia.

"Asante shemeji, kesho asubuhi naenda Kimara."
"Au nimekumbuka kitu kimoja, lala hapa sebuleni ila hata kama akija na kukukuta umelala sebuleni atajua kweli upo katika shida kuliko akikukuta umelala chumbani," alisema shemeji huku akijikunakuna mgongoni, tumboni, chini ya taulo.

Eliza alikubali, nikaingia chumbani kumchukulia shuka. Lakini wakati natoka nikasikia sauti kama ya busu. Nilipotoka nikamkuta shemeji anampa mkono Eliza eti huku akimwambia alale salama.
Na mimi nilikwenda chumbani kulala, lakini sikupata usingizi. Lawama zangu zilikuwa kwa shemeji. Kwanini anamsaliti dada kiasi kile?

Je, dada naye akiamua kufanya hivyo kwa mume wa Eliza atajisikiaje?
Kwenye saa nane usiku nikasikia mlango wa chumbani kwa dada Light ukifunguliwa. Dakika mbili na mimi nikatoka kitandani. Nilichungulia sebuleni kupita tundu la funguo.

Kwa macho yangu niliweza kumwona shemeji amekaa kwenye kochi alilolala Eliza. Hakukuwa na mwanga wa kutosha, lakini ule mdogo wa taa ya nje uliniwezesha kuona kila kitu pale sebuleni.

Nilimuona shemeji akimshikashika Eliza huku wakati mwingine akimuinamia.
Ina maana alikuwa akimpa mabusu motomoto. Dada Light yeye alikuwa amelala tu muda huo. Na hivi alishakunywa bia zake mbili tatu...!

Itaendelea.....
 
Sehemu ya 41.

Nilitamani kufungua mlango ili nijitokeze lakini nikahisi huenda kitendo hicho kingemuasha dada kule chumbani kwake kwani mlango wa chumba changu una kelele sana.

Nikamuona kama Eliza anakataa kataaa. Nikajua anahofia usalama wake. Hasa fumanizi, lakini nikamuona shemeji anamshika kama anamlazimsha Eliza akalegea.

Nikamuona shemeji anajiandaa vizuri, wakati huo Eliza naye anamvutia kwake.
Kwa kweli ubinadamu ulimshinda. Sikuwa tayari nione dada angu anasalitiwa hivi hivi. Kuendelea kufumbia macho ni sawa na kusaliti mimi.

Nilichukua simu na kumpigia dada kumwambia aende sebuleni kushuhudia kwa jicho lake.

"Namba unayopiga kwa sasa haipatikani, tafadhali jaribu tena baadaye," eti simu ya dada Light ilinijibu hivyo. Mwenye bahati habahatiki!

Niliwaza moyoni! Nikafikiria kidogo nikapata wazo. Kuipiga simu ya shemeji, ikilia itamuasha dada Light.

Wakati inaita, nilikuwa nakaza macho pale sebuleni. Ghafla! Nilimuona shemeji akikurupuka kwenda chumbani kwake. Kumbe aliisikia simu yake ikiita.

Nilirudi kitandani kulala, nikawa nasikilizia. Mara simu yangu iliita. Jina shemeji likajitokeza juu ya kioo cha simu yangu.
"Halooo," niliipokea kwa mapozi sana.
"Ulikuwa unapiga au una-beep?" aliniuliza shemeji.

"Mh! Labda imejipiga kwa bahati mbaya," nilimjibu kwa sauti iliyochoka kwa usingizi na ulevi. Pale pale alikata simu. Lakini ulipita muda mrefu sikumsikia akitoka. Huenda na mkewe alishaamka.

Mara meseji iliingia kwenye simu yangu. Nikajua shemeji aliamua kunitumia meseji.
"Vipi mtoto mzuri umelala? Mke wangu kalala kwenu au aliondoka?" alikuwa mume wa Eliza. Niliachia tabasamu laini huku nikiwaza.

"Mke bado unampenda halafu unajifanya kuja juu."
Nilimjibu amelala sebuleni. Na asiwe na wasiwasi kwani nimempa na shuka.
***

Itaendelea....
 
Sehemu ya 42.

Asubuhi na mapema Eliza aliamka na kuniamsha na mimi. Akasema anakwenda Kimara kwa ndugu yake. Kama atauliziwa na mtu yeyote akiwemo mume wake nimwambie hivyo.

Nilimtoa kumsindikiza mpaka nyumba ya tatu. Lakini wakati tunaagana nilimwambia ukweli.

Nilimwambia kwamba tabia anayoiendeleza kuwa na uhusiano wa kimapenzi na shemeji inaweza kuvunja ndoa yake au kuleta uadui mkubwa sana.

"Mbona tulishaachana tangu siku ile?"
"Mliachana wapi wakati jana huko Mabibo ulikuwa na shemeji. Kama haitoshi, usiku alikufuata kwenye kochi, kataa?" nilimwambia kwa kumkazia macho. Aibu niliiweka pembeni.

Alishindwa kuendelea kujitetea kwani nilimwambia kitu ambacho nilikuwa na uhakika nacho.

"Bwana tutaongea siku nyingine. Usiwe na wasiwasi mdogo wangu."
Eliza alijibu huku akiondoka zake.
Nilirudi nyumbani na kumkuta mume wa Eliza yuko sebuleni akiongea na shemeji. Waliniuliza kama nilikuwa na habari na alikokwenda Eliza. Niliwajibu ndio natoka kumsindikiza.

"Anakwenda Kimara kwa ndugu yake gani sijui," niliwajibu huku nikipitiliza mpaka chumbani. Wakati nafungua mlango wa chumba changu niliwageukia kuwaangalia pale sebuleni kwani nilipowajibu ulipita ukimya.

Niliwaona wote wakinitumia macho mimi. Jicho la shemeji lilikuwa ni la kunihesabia siku. Jicho la mume wa Eliza lilikuwa ni la kuhakikisha siku ile anatimiza tamaa yake kwangu.
*
*

Je, nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 43.

Walipomaliza mazungumzo yao waliagana. Baadaye shemeji na dada walitoka kwenda kazini. Mume wa Eliza siku hiyo niliendelea kumwona yupo yupo tu nyumbani.
Labda kitendo cha kutibuana na mkewe kilimuondoa kwenye 'mood'.
Saa nne, msichana wa kazi wa da' Light na Eliza walikwenda sokoni. Nyumbani nikabaki mimi na mume wa Eliza.

Ni mimi ndiye niliyeanza uchokozi. Nilimgongea mlango mume wa Eliza.
Alipofungua mlango na kuniona kidogo anikumbatie.

"Ooh, karibu Maria."
Nilijipenyeka mpaka sebuleni.
Lakini sikupenda kukaa pale maana anaweza kutokea mgeni ambaye atapata picha ya tofauti. Nilipenda twende chumbani. Nikamwambia...

"Twende chumbani kwako, hapa sebuleni mi sina amani," nilimwambia kwa sauti ya kubana. Nawajua wanaume.
Hata hakuniambia kitu zaidi ya kunishika mkono na kunikokota mpaka chumbani kwake. Kitandani puu!

Akaniwahi na busu moja kisha akajitupa na yeye. Tukawa sambamba kitandani. Umbali wa macho yake na yangu ni sawa na umbali wa kiganja cha mkono.
"Nakupenda Maria," aliniambia kwa sauti ya kukatakata. Najua kwanini sauti yake ilikuwa ikikatakata.

"Mimi sijaamua kukupenda shemeji," nilimjibu kutoka moyoni.
Alishtuka sana kisha akanikazia macho.
"Kweli Maria?"

"Kweli kabisa," nilimjibu.
"Basi naomba unipende," aliniambia.
"Itakuwa ngumu sana shemeji," nilimjibu. Mara tukasikia mlio wa gari nje ya nyumba. Mume wa Eliza aliamka haraka kitandani akatoka. Na mimi nikamfuatia kwa nyuma.

Nikiwa sebuleni, yeye akiwa anapeleka mkono kushika kitasa cha mlango ili kufungua...kabla hajakamilisha kitendo hicho, mlango huo ukafunguliwa na mtu aliyekuwa kwa nje...Ni Eliza akaingia.
"Ha! Da Eliza," nilijikuta nikitamka hivyo.
Nilimuona Eliza akinitumbulia macho mithili ya nyati aliyejeruhiwa wakati akitafuta chakula.

"Kumbe kuja kwangu kufuata nguo kumenisaidia sana kujua nani mbaya wangu katika ndoa yangu. Maria ni wewe?" Eliza alisema kwa mshangao huku bado akiendelea kunitumbulia macho.

Itaendelea....
 
Sehemu ya 44.

Mumewe aliingilia kati na kumwambia kuwa, mimi niliingia mule ndani kwa lengo la kumsalimia tu.
"Mbona siku zote sijawahi kumwona akidamkia ndani kukusalimia?" Eliza alimkong'ota swali mume wake ambalo alishindwa kulijibu.

Najua kilichomfanya Eliza ashangae. Unajua wakati nilipokuwa namsindikiza asubuhi nilikuwa ndani ya khanga moja na nilipoingia kwake bado nilikuwa na khanga moja.
Aliponikuta kwake ndiyo kwanza ile khanga ilikuwa inanivuka, nikawa naiweka vizuri.
Hata kama ni wewe ungefikiria vibaya. Niko na mumeo, wawili tu halafu khanga moja, tena inaonekana kutaka kunivuka.

Eliza aliingia kisha akafunga mlango kwa funguo na kukaa kwenye kochi kubwa.
"Maria tafadhali kaa hapo," alisema huku akinionyesha pa kukaa kwa kidole.

Nilikwenda kwenye kochi hilo na nikakaa.
Mume wa Eliza naye akakaa lakini kwenye kochi lingine tofauti na nililokaa mimi.
"Naomba mniambie ukweli, mlikuwa mnafanya nini humu ndani," Eliza aliuliza kwa sauti iliyoashiria kwamba ameumia sana lakini hana jazba.

"Nimeshakwambia kwamba alikuja kunisalimia, asa we unafikiria nini?" mume wake alisema.

Eliza alisimama na kunishika mkono kisha akanivuta kumfuata. Nilimfuata hadi chumbani. Alianza kukikagua kitanda. Nafikiri ana vigezo vyake vya kumuonyesha kwamba tulitoka kitandani kamilikamili au sivyo.

Alilishika shuka na kulinyoosha, sijui aliona nini, akaliachia na kunigeukia.
"Unataka kunisaliti katika ndoa yangu siyo?"
Nilijitetea kwa kumwambia kwamba, sikuwa na nia mbaya na mumewe na ninamuheshimu sana kama shemeji yangu aliyemuoa da' Light.
"Sasa kwanini umekuja kumsalimia ukiwa na khanga moja tu?"

"Dada Eliza khanga moja ndiyo vazi langu la kila siku asubuhi. Na kama ningetaka kutembea na mumeo ningeshatembea naye zamani sana na usingejua."
Nilimuona Eliza akishikwa na kizunguzungu cha kuongea.
"Una maana gani, alishakutaka siyo?" alitaka kuja juu.

"Siyo alishanitaka bali, ila unafikiri ningemuita sehemu na kumwambia unatembea na mume wa Light angeniacha?"
Kabla Eliza hajanijibu mume wake aliingia.
"Sasa Eliza ndiyo unafanyaje?" alifoka mumewe.
"Unakifanya chumba changu ni cha kuchezea siyo?"

Itaendelea....
 
Sehemu ya 45.

Mimi nilitumia nafasi hiyo kutoka nje na kuendelea na shughuli zangu. Watakavyomalizana watajua wenyewe.
Jioni da Light aliporudi alinikuta na mimi navaa ili nitoke.

"Lakini siendi mbali, nitakuwa Romo Green View tu," nilimwambia.
"Uko na nani au ndiyo huyu shemeji yangu?"
Sikumjibu zaidi ya kuachia tabasamu tu. Mwenye akili na afahamu!

Siku hiyo nilivaa traksuti ya pink, ndala simpo nazo za pink, nikatia glasi zangu machoni, simu kwenye kipochi kidogo cha mkononi....huyoo mpaka Romo Green View.
Sikuwa na ahadi na mtu ila nilitaka nifike pale nimpigie simu mume wa Eliza aje nimwambie ukweli kuhusu mkewe kutembea na shemeji yangu.

Atajaza mwenyewe, aamue kutengana naye au kuendelea kuwa naye. Niliamua kufanya hivyo baada ya kuona alivyonikomalia asubuhi aliponikuta na mumewe wakati anajua mimi nazifahamu dhambi zake.

Kweli mkuki ni mtamu kwa nguruwe lakini kwa binadamu mchungu.
Nilitafuta meza nzuri nikakaa, nilikuwa peke yangu kwenye kiti. Nilivuta simu yangu nikampiga mume wake Eliza.

"Mambo dear."
"Eeh, niko Rombo mpenzi wangu."
"Nataka uje nikupe ishu mpya sana ya mkeo," nilimwambia nikiwa nimeukaza uso. Liwalo na liwe!

Nilisema moyoni. Hawezi kumchukulia mume dada yangu halafu yeye kuniona niko na mumewe tu anakuja juu.

Niliendelea kusema moyoni. Ina maana anataka kututawala siyo. Nilizidi kusema.
Hata dakika kumi haikupita, mume wa Eliza akaingia kwa mikogo.

Nilimuona akinitafuta nilipokaa, ikabidi nim-beep!
Aligeuka huku na kule kunitafuta, aliponiona akaja.

Alifikia kunipa busu moja la maana sana siwezi kulisahau mpaka leo. Busu liliwashtua wateja wote waliokaa jirani na meza niliyokaa mimi.

Itaendelea...
 
Sehemu ya 46.

Sikutaka kumwambia habari ya mkewe mapema. Nilimuacha apate kama bia mbili tatu kwanza ndipo nimmwagie kila kitu. Na ushahidi ninao, wasichana wa kazi.
Inaonekana hakujua ni kitu gani ningemwambia kuhusu mkewe, kama angehisi alipofikia tu angeniuliza.

Akiwa katikati ya bia ya pili na mimi pia ya pili, ghafla nilimuona da Light akiingia kwenye baa ile ya Rombo.
"Mungu wangu, Mungu wangu," nilisema kwa mshtuko mkuu.

Mume wa Eliza naye alishtuka na kugeuka kuangalia nilikokuwa naangalia mimi. Alijua tayari kuna soo.
"Vipi kuna nini?" aliniuliza baada ya kutoona chochote.

"Da' Light," nilimwambia mume wa Eliza.
Lakini wakati huo alishafika na pia alikuwa ameniona. Sasa kuja yake alitaka kujua mwanaume niliyekaa naye.

"Nimesema ngoja nikuone, japo shemeji anipe bia moja," da Light aliniambia huku akipeleka mkono kwenye kiti.
Macho yake yalipokutana na ya mume wa Eliza alishtuka sana.

"Maria," alisema huku akikaa.
Akachukua kitambaa cha mkononi na kujifuta jasho kwanza. Mimi matumbo yalijichanganya tumboni kama ni mtu aliyeshinda bila kula halafu akaanza kwa kunywa maji.

"Bee," niliitika huku nikingoja bomu langu. Mimi sikujua kama da Light angekuja pale baa. Na kama ningejua kwamba alikuwa na mpango huo nisingemwambia nakwenda baa ile.

"Wewe ndiyo mwenyeji hapa au shemeji?"
Niliachia tabasamu laini na kumwangalia mume wa Eliza. Nafikiri alijua nina maana gani.

"Haya nasubiri unitambulishe kwa huyo shemeji au hajaja?" da' Light alisema akinikazia macho ya hamu ya kusubiri jibu. Sijui alihisi ningemwambia ni yule mume wa Eliza.

Dada naye aliagiza bia yake, akaanza kunywa. Wakati mimi na mume wa Eliza tukiwa na bia ya nne, da' Light alikuwa bia ya pili na nusu. Nafikiri alikuwa akifukuzia namba zetu.

Ilifika mahali mazungumzo yalichanganya, sasa da' Light alikuwa akiongea sana na mume wa Eliza. Kuna wakati niliwaona wanainamiana na kuzungumza kwa kunong'onezana, nikajua tayari...!
Shemeji naye akae tayari, akileta ujinga wake anachukuliwa mkewe, kama yeye anavyochukua wa mwenzake.

Itaendelea....
 
Sehemu ya 47.

Kwa upande fulani sikupenda ijitokeze hali hiyo, kwamba ifike mahali da Light atembee na mume wa Eliza. Niliona kama kinyaa fulani. Hata kama ni ugonjwa ungewaumiza sana wote.

Lakino da Light alipofikisha bia ya tatu, sasa akili zikawa si zake, aibu ikamtoka kabisa na kuanza kusema lolote lile.
"Sasa mdogo wangu huyo shemeji uliyesema unakuja kukutana naye hapa yuko wapi au ndiyo huyu shemeji yangu hapa?" aliniuliza akiwa ananiangalia usoni.

"Ilikuwa aje ila amenitumia meseji amesema amepata dharura," nilimjibu huku nikimwangalia mume wa Eliza na kumlegezea macho. Haraka sana niligundua ugonjwa alionao da Light na mimi ninao.

Kwamba mara nyingi bia mbili, tatu tunatamani kitanda. Naamini nimeeleweka.
Endapo ningesema nawaacha pale si ajabu wangerudi nyumbani saa sita, saba!
Sijui wangejieleza nini?

Nilimtumia meseji mume wa Eliza kumwambia kuwa, siku ile ndiyo nilipanga tukamalizane, lakini kwa sababu da Light yupo hakuna jinsi. Tupange siku nyingine. Cha ajabu mume wa Eliza alijibu poa tu, wakati mawazoni mwangu niliamini angeniambia yeye atatangulia mahali fulani nimfuate.

Tukiwa tunaendelea kunywa, mume wa Eliza alipokea simu. Ilitoka kwa mkewe kwa namna aliyokuwa akiongea naye.
"Kwani ulikuwa unasemaje?"
"Niko Rombo Green View hapa Shekilango."
Alipokata simu alikuwa amekasirika. Akatuambia.

"Eliza anauliza niko wapi, nimemwambia niko Rombo, kasema anakuja."
Nilimwacha da Light aseme kitu kama alikuwa nacho, lakini badala yake alimwangalia mume wa Eliza kisha akatabasamu.

Itaendelea......
 
Sehemu ya 48.

Haikupita hata nusu saa Eliza aliingia, mimi ndiye niliyetangulia kumwona akiingia, kwani nilikaa kutazama getini.

"Anakuja," nilisema, japo ilikuwa giza tayari lakini macho yangu bado imara sana.
Eliza alipofika, alisimama kwa muda bila kukaa huku akiniangalia kisha akamuangalia dada Light na kumalizia na mumewe.

"Kaa sasa," alisema mumewe akimuonyesha kiti. Kulia kwa mume wa Eliza alikaa da Light, kushoto kwake nilikaa mimi. Kwa hiyo kama mkewe angekaa angekuwa ametenganishwa na mmi na dada Light kitu ambacho wapenzi huwa hawakai hivyo hata siku moja.

Kisirani alichokionyesha Eliza siku hiyo naamini hakuwahi kukionyesha hata siku moja. Naamini hata da Light alishangaa, lakini bado ukweli ulikuwa pale pale kwamba, hata ningekuwa mimi, kuwakuta majirani wamekaa na mume wangu vile nisingependa. Kama si watu wabaya kwangu wangeniambia tuko sehemu fulani na shemeji.

Alivuta kiti na kukaa kisha akamuita mhudumu. Uzuri ni kwamba, hakuna aliyemuonyesha kwamba labda tulikuwa tumemdharau, kwani muda huo huo da Light alikumbuka kwamba, alipokaa sipo.
"Shoga angu njoo ukae hapa," alisema dada huku akiinuka na kumpisha Eliza akae jirani na mumewe. Naye alikwenda kukaa, kidogo akachangamka na kuchangamka.

Mhudumu alipofika aliagiza mchemsho wa samaki, kisha akaagiza na bia moja ya baridi.
Licha ya hali hiyo, lakini Eliza alionekana kutokuwa na amani na mimi kwani alikuwa akiniangalia kwa kuniiba lakini kwa jicho kali sana.

Imavyoonekana moyoni mwake aliamini kuwa, kwa vyovyote vile mimi na mumewe ilikuwa 'ile mbaya'. Lakini alikuwa anashindwa kusema kwa sababu na mimi nina madhambi yake.
Angesema na mimi ningesema, mbaya zaidi yeye anayemwibia alikuwa naye pale pale, angeona joto lake.

Kuna wakati niliaga nakwenda maliwatoni, nikasimama. Kumbe nyuma yangu mume wa Eliza naye akasimama, naye akaenda maliwatoni yao wanaume.

Mimi nikiwa huko simu yangu ikaita, kuangalia namba ni za mume wa Eliza, kwanza niliogopa kwani nilijua huenda ni Eliza amechukua simu ya mumewe kunipigia, lakini nikasema acha nipokee nimsikie anachosema.

Itaendelea......
 
Sehemu ya 49.

"Halo, asa, basi tukifika nyumbani wakilala wote, mimi nitatoka hata kule nyuma si tunaweza kukutana tu," alisema mume wa Eliza, kabla sijamjibu, Eliza aliingia kule chooni huku akinikazia macho.
"Maria unajua sikuelewi," Eliza aliniambia kwa kumaanisha.

"Hata mimi sikuelewi Eliza," nilimjibu nikimshangaa sana kwa kauli yake hiyo.
"Hata wewe hunielewi siyo, eee! Aaaa! Lakini hakuna lenye mwanzo likakosa mwisho wala hakuna siri ya mtu mmoja," Eliza aliniambia lakini kwa sauti ya woga fulani.

"Eliza nikitaka naimaliza ndoa yako hata sasa hivi, kama unabisha nipe ruhusa," nilimwambia. Wateja wengine wa baa ile walikuwa wakiingia na kutoka, lakini siye tuliendelea kujibizana kule chooni bila kuhofia.

"Utaimalizaje?"
"Nipe ruhusa nakwambia."
"Niambie kwanza, au ndiyo utatembea na mume wangu? Si umeshatembea naye, kwani sijui," alisema Eliza.

Sasa hapo ni pombe zilikuwa zikifanya kazi vichwani mwetu, kwani hata watu waliokuwa wakiingia tuliwaona kama watoto wadogo wasiojua lolote.

Itaendelea....
 
Sehemu ya 50.

"Ndiyo nimeshatembea naye, wewe je? Mbona unatembea na shemeji tena unajua ni mume wa shoga yako kipenzi, lakini hata haya huna! Loo we dada Eliza," nilimpasha, alipotaka kunijibu kitu, da Light alitokea na kusimama akituangalia.

Alionekana si kwamba alikuja kwa kujisaidia, bali huenda aliambiwa na majirani tuliokaa nao kwamba, sisi tunazozana chooni.
"Hivi mna akili kweli nyie? Mnachogombania ni nini tena chooni, hata hamuogopi watu au ndio pombe hizo?" da' Light alitusema. Hata yeye najua alikuwa akiongozwa na pombe, kwani ninavyomjua sio rahisi kumsema Eliza vile.

Nilitoka nikijipenyeza ukutani mpaka nilipokuwa nimekaa. Mume wa Eliza aliniangalia usoni kama vile alitaka kuniuliza kuna nini.

Eliza na da' Light nao walifika na kukaa, lakini hali ya da' Light ilikuwa ni ya kawaida. Alionekana kutaka kujua nini kilikuwa kimetugombanisha kule chooni.
"Shemeji hebu waulize wewe," dada Light alimwambia mume wa Eliza.

"Eti, kulikuwa kuna nini chooni?"
Mimi nilijiinamia bila kujibu kitu kisha nikanyanyua kichwa na kuchukua glasi yangu. Eliza alianza kudondosha machozi kiaina bila kusema kitu. Hali hiyo ilionekana kumshtuka sana da Light. Alihisi kuna jambo kubwa zaidi.

"Maria," aliniita.
"Abee."
"Kuna nini mbona siwaelewi?"
Mimi binafsi nilimshangaa sana dada Eliza kwani yeye alitakiwa kuvumilia mpaka mwisho, kwa vile alivyokuwa anafanya alikuwa akinihamasisha na mimi niweke wazi kila kitu.

"Mimi sijui dada, muulizeni yeye mwenyewe," nilijibu huku nikitegea anianze yeye mimi nimmalize.

"Eti Eliza mbona hii hali sikuwahi kuiona kabla, kuna nini leo dear?" dada alimuuliza Eliza kwa sauti ya kumbembeleza.
Eliza aliinuka na kukaa sawa kisha akapeleka makamasi ndani na kusema.

Itaendelea.....
 
Sehemu ya 51.

"Mdogo wako ameniambia ametembea na mume wangu."
Dada Light alionekana kubabaika na kauli hiyo ya Eliza. Akaniangalia kwa kunitumbulia macho kisha akamgeukia mume wa Eliza, naye akamuangalia kwa kumtumbulia macho kama mimi. Mume wa Eliza alianza kutingisha kichwa kuashiria kukataa.
"Eti Maria?" dada Light aliniuliza hivyo tu, tena kwa sauti ya chini sana.

"Dada mimi nitakuwa mwongo mkubwa kama nitakataa au nitakubali. Mumewe huyu hapa muulize. Na anavyosema nimemwambia nimetembea na mume wake si kweli ila nitasimulia kisa na chanzo," nilisema huku nikikaa vizuri.

Hasira zilinipanda mpaka kwenye kona ya kichwa, kwani niliamini Eliza ana kichaa. Si mzima, katika mazingira ya matukio yake na shemeji hakupaswa kunifanyia vile.

Hakutakiwa kuweka uwazi wa hisia zake wakati mimi si hisia, bali kwa wenyewe kukiri kwamba wanarushana roho.

Nilisimulia kila kitu kuanzia nilipokuja nyumbani kwake asubuhi ile alivyotokea Kimara kwa ndugu yake na kunikuta sebuleni kwake na mumewe.

"Lakini dada aliponiuliza nilimkatalia kwamba sijatoka kufanya mapenzi na mumewe, na alinishika mkono mpaka chumbani na kukagua kitanda, akakuta safi. Sasa wasi wasi wake unaendelea kutokana na vigezo gani?" nilihoji kwa hasira.

Nilimuona da Light akiendelea kuniangalia kisha akanisemesha kilugha, akimaanisha kwamba, ninapofika sehemu za watu nisiwe na tabia za kudandia dandia, ninaweza kujikuta ninadandia gari moja na yeye.
"Mh," niliguna kwa sauti ya kufuatia kauli hiyo. Nikajikuta kama akili zinaniruka vile.
Sikumuelewa vizuri sijui.

Nikarudia kuyasema yale maneno mwenyewe ili nione kama nitapata maana nzuri.
"Ina maana da Light ana uhusiano wa kimapenzi na mume wa Eliza?"
Nilijihoji mwenyewe.

Itaendelea......
 
Sehemu ya 52.

"Kwanini aseme nisidandie dandie gari naweza kujikuta nadandia na yeye?"
Niliumiza kichwa ili kupata maana ya kauli yake hiyo, lakini wapi. Sikutaka kuwa ni mwenye kuamini kauli hiyo ya dada.
Kama ni kweli basi wote wamekwisha. Maana kama ni ugonjwa hakuna atakayepona. Nyumba nzima watakufa. Na nyumba yenyewe wanakaa wao tu, hakuna mpangaji mwingine.

Basi, lakini mimi nilimjibu dada kwa kilugha nikiendelea kumkatalia kuwa na uhusiano na mume wa Eliza. Nilipoona kama hajanielewa kwa kilugha nikamkatalia kwa kingereza. Halafu nikaendelea kumkatalia kwa kiswahili.

Dada alimshika Eliza bega na kumpoza kwa kumwambia kuwa, ananifahamu mimi ni mtu muwazi, sana. Kama ingekuwa kweli ningekiri mbele yao bila kujua madhara yatakayotokea kufuatia kukiri kwangu. Hivyo ni kweli, ndivyo ilivyo. Mimi niko wazi sana.
Kidogo Eliza alionekana kukubaliana na maneno ya da Light. Akanishika mkono na kuniambia nimsamehe kwa tuhuma zake kwangu. Akachukua glasi na kutaka chiazi.

***
Siku ya pili toka kikao chenye matata cha pale baa ya Rombo, siku hiyo dada akiwa kazini, shemeji akiwa kazini, Eliza akiwa kazini na mumewe akiwa kazini. Nilikuwa peke yangu nyumbani. Wasichana wa kazi walienda gengeni, nikawa nawaza kauli ya dada. Kila nilipojaribu kuipeleka kwenye ukweli ulivyo, moyo wangu ulikataa. Lakini mwisho nikaona kama naanza kukubaliana nayo.

Kwani wote si binadamu inawezekana, nilisema moyoni.
Kazi ikawa moja, nitafanyaje ili kuupata ukweli wa mawazo yangu na kauli ya dada ingawa pia nilikuwa nikitaka kukubali kwamba, kauli ya dada ilikuwa inatoa mfano wa ubaya wa kudandia lakini si hali halisi ilivyo.

Jioni aliyeanza kufika ni da Light. Na mara nyingi huwa hivyo. Alinisalimia, akaingia ndani na kuvua suti aliyovaa kazini na kuvaa khanga moja tu. Kisha akaenda bafuni kuoga.

Huku nyuma mimi nikachukua simu yake na kuandika namba za mume wa Eliza, nikapiga, likatokea jina la Mwantumu.

*
*

Itaendelea.....
 
Sehemu ya 53.

"Mh!" niliguna. Nikaangalia huku na kule, hakukuwa na mtu. Sikuamini macho yangu na akili pia.

Nikazihakikisha zile namba, zilikuwa sahihi. Nikafungua kiboksi cha meseji zinazotoka, nikakuta meseji nyingi za kwenda kwa mumewe kwa jina la Honey, lakini nikakuta meseji moja ya mwisho kabisa ya Mwantumu ikisema,
"Itabidi nifike nyumbani kwanza kisha nitakuja. Lakini d, usiuweke sana, si unajua wote tupo katika ndoa?"

Baada ya hapo nikakifungua kiboksi kinachopokea meseji kutoka nje. Meseji zote zilikuwa za mumewe, zilikuwa na jina Honey. Nikajua dada alikuwa hazifugi meseji zake za siri. Hata ile si ajabu hakuwa na habari kama alisahau kuifuta.

Alipotoka kuoga alijipara barabara kisha akaniita na kusema anakwenda kwa rafiki yake mmoja, alihamia sehemu mpya kwa hiyo watakutana kituoni ili akamuoneshe makazi mapya!

Nilimuuliza kama alimuaga mumewe.
"Anajua nilishamwambia toka asubuhi," moyoni nikajikita nikisema "duh!" ama kweli hakuna ndoa miaka hii. Mtu toka asubuhi anaaga kwa mumewe kwamba anakwenda kufanya uzinzi.

Kweli moyo wa mtu ni kichaka! Na ni siri, kama kila mtu angekuwa anajua password ya moyo wa mwenzake, pangekuwa panachimbika kila sekunde.

Dakika kumi baada ya dada kuondoka, shemeji alirudi. Nusu saa akarudi Eliza. Lakini mume wa Eliza alichelewa kurudi. Nikawa nimepata picha kamili. Lakini niliwaona wajinga sana. Si waamue kila mmoja amchukue mke wa mwenzake ili waondoe zinaa hiyo? Nilijiambia moyoni.

Jioni hiyo wasichana wa kazi walitoka wote kwenda kwenye maziwa. Mimi nilikuwa nimelala tu chumbani. Mara shemeji alinigongea na kuniuliza kwanini nilikuwa nimelala muda ule.

"Shemeji kichwa kinaniuma sana, sijui ni bia za jana?" nilimjibu nikiwa bado kitandani.
Akanipa pole na kuniuliza kama nimeshakunywa dawa.

Nikamjibu sitakunywa dawa kitapona chenyewe tu. Akanitakia kupona haraka kisha akatoka, mara Eliza naye aliingia na kuniambia amesekia naumwa.
"Nani kakwambia?" nilimpachika swali. Alionekana kubabaika kunijibu, akajitahidi tu.

Itaendelea.....
 
Sehemu ya 54.

"Si bahati?" huyo Bahati ni msichana wa kazi wa dada Light. Nikajua uongo. Ni shemeji tu, kwani Bahati anajua nimelala lakini hajui kama ninaumwa na kichwa, kwani hata da Light alipokuwa anaondoka sikumwambia kama naumwa kichwa.

Akaniambia kuwa, anavyojua yeye kichwa kikiuma, halafu ukilala kwa nusu saa kinatulia chenyewe.

Moyoni nikajua kuwa alikuwa akinifundisha hivyo ili wao wapate nafasi ya kufanya mapenzi, hakuna lingine.

"Oke, basi mimi nitalala kwa saa nzima," nilimjibu huku nikigeukia ukutani. Akatoka bila kuniaga. Dakika tano mbele nikaanza kusikia minong'ono chumbani kwa Eliza. Mara vishindo, mara sauti za mahaba.

Nikaamka na kufungua mlango kutoka nje.
Nilibahatika kuukuta mlango mkubwa upo wazi. Mapenzi ni kitu cha ajabu sana, yaani waliamini kwamba ni wao tu, hakuna mtu mwingine aliyekuwa akiwaona.

Niliingia mpaka sebuleni na kutegesha sikio kwenye tundu la kitasa cha mlango wa kuingilia chumbani walikokuwa.
"Nifungue mlango niingie ndani au niache?" nilijiuliza.

"Lakini watajirekebisha lini kama si kuingia moja kwa moja," niliendelea kuwaza.
Mwishowe nilipata wazo zuri tu. Niliamua kukaa sebuleni ili watakapotoka, wajue nilikuwa nimejua kila kitu.

Niliona kitendo cha kuingia chumbani na kuwakuta wakiserebuka, ingekuwa ni kumkosea heshima shemeji yangu ambaye ni mume wa dada yangu. Nilikaa kwenye kochi sebuleni huku nikisoma magazeti.

Dakika tano tu mbele nikasikia mlango ukifunguliwa taratibu. Akatoka shemeji huku akiwa katika sura ya tahadhari kubwa.
Tulipokutana macho akasimama kwanza.

"Shemeji nakuomba nyumbani," alisema huku akiwa amebadilika sura. Niliogopa, lakini nikasimama na kumfuata. Kabla sijamaliza mlango Eliza naye alitoka huku akiwa ndani ya khanga moja tu. Tulipokutana macho tu alikunja sura kama vile aliona kinyesi kisha akaubetua mdomo.

Nikafahamu kumbe Eliza alikuwa tayari hata kuivunja ndoa ya mwenzake bila woga wala wasiwasi na ndiyo maana suala la kutembea na shemeji tena pale pale nyumbani yeye hakuona kama ni tatizo.

Basi niliendelea kumfuata shemeji mpaka ndani nikidhani kwamba atakaa sebuleni ili aongee alichonitakia, lakini akapitiliza kuelekea chumbani kwake.

Itaendelea.....
 
Sehemu ya 55.

"Ingia," aliniambia huku akiwa ameshika simu. Nikaingia sambamba naye. Kisha akakaa kitandani simu ikiwa sikioni. Mara nikamsikia akisema.

"Haloo uko wapi?" huku akinionyesha mahali pa kukaa. Si pengine, ni kitandani.
Nilikaa huku nikifuatilia maongezi yake kwenye simu. Alikuwa akiongea na dada. Maana nilimsikia akimwambia poa. Usijali sana, wala hakuna haja ya kuharakisha kurudi.

"Shemeji Maria leo nataka lazima nilale na wewe," aliniambia shemeji huku akianza kunishika shika mwilini. Nilimkazia macho kama vile nilikuwa namsuta kwa kauli yake.
"Shemeji hapa. Hapana shemeji, sipo hivyo," nilimjia juu.

"Unataka hutaki lazima tufanye," alinikazia shemeji huku sasa akianza kutunisha msuri wake kunikamata.

Lakini nilijitahidi kwa njia zote mpaka nikamshinda na kumwangusha chini na kugalagala. Nikatoa mbio sebuleni. Nilim-beep dada muda huo huo naye akaenda hewani.

"Vipi?" dada aliniuliza. Ni dhahiri kwamba dada alikuwa kwenye chumba ambacho hakitoi sauti kwani maneno yake yalisikika moja kwa moja kiasi kwamba sikuweza kusikia lolote lile jingine zaidi yake.

"Uko wapi dada angu?" nilimuuliza kwa sauti ya upole. Kabla hajanijibu shemeji alikuja mbio na kunyakua simu yangu. Tulianza kunyang'anyana huku nikimsikia dada akiongea. Lakini sikujua alikuwa akiongea nini.

Alifanikiwa kuninyang'anya simu akaingia nayo chumbani kwake huku akiizima ili kukata mawasiliano na dada.
Haikupita muda nikasikia simu yake ikiita, nikajua kwa vyovyote vile alikuwa ni dada kampigia mumewe ili kutaka kujua kulikoni napigiwa simu halafu siongei.
"Mi sijui si uongee naye mwenyewe," alikuwa akijibu shemeji.

"Nimesema mi sijui lolote, ongea naye, we vipi kwani?" shemeji aliendelea kusema kwenye simu. Jibu nikawa nalo.
Mara aliingia Eliza akiwa ameshika chanuo huku akiniimbia nyimbo za mafumbo. Akasema anaazima kibao cha nazi. Nilisimama na kwenda kumchukulia nikampa, akatoka.

Shemeji akaja sebuleni na kukaa jirani na mimi huku akiniangalia kwa umakini sana.
"Naona umepania kuvunja ndoa ya dada yako," aliniambia huku akinipa simu yangu. Niliipokea na kuiwasha, kabla sijajibu. Pale pale meseji ikaingia.

Itaendelea....
 
Sehemu ya 56.

"Unaomba kupigiwa simu halafu ukipigiwa huongei, vipi kuna tatizo mdogo wangu?"
Kisha muda huo huo simu ikapigwa. Ni dada Light. Nadhani aliona meseji 'delivadi' kwangu ndiyo maana alipiga.

"Haloo dada," nilisema nikimwambia shemeji. Aliweka mkono kifuani kuashiria kwamba anaomba nisije kusema niliyotaka kuyasema.

"Aaa nilitaka kujua uliko tu dada. Unarudi saa ngapi?" nilimuuliza nikijibalaguza.

"Oke sawa, tutaongea ukija," nilimjibu, dada akakata simu. Moyoni niliwachukia wote. Nilimchukia da' Light, nilimchukia sana shemeji, nikamchukia Eliza na mume wake.
Saa tatu na nusu nikiwa nimelala, mlango wangu uligongwa kwa nguvu sana mpaka nikaogopa.

"Nani?" niliuliza.
"Fungua," nilisikia sauti ikisema hivyo huku nikiwa sijui ilikuwa ni sauti ya nani japokuwa ilikuwa ni ya mwanamke.
Nilitoka kitandani na kwenda kufungua mlango. Alikuwa ni da' Light akionekana kuvimba sura kwa hasira.

Aliingia ndani ya chumba changu na kupanda kitandani kulala. Sikujua kwanini alifanya vile. "Inawezekana amegombana na shemeji?" nilijiuliza moyoni mwangu.
Hali ya chumba changu ilikuwa ya utulivu sana huku kila mmoja, yaani mimi na dada akionekana kuwaza yake. Sikufahamu kwa muda huo alikuwa akiwaza nini.

"Da Light kwani vipi?" nilimuuliza na hivyo kukata ukimya na utulivu uliokuwepo.
Dada Light alianza kulia huku akishikwa na kwikwi.

"Sikiliza mdogo wangu kila siku shemeji yako amekuwa akinifikiria kwamba natembea na mume wa Eliza, sasa leo nimerudi kanipiga vibao akidai nilikuwa naye."

Kwangu hayo hayakuwa mapya kwa kweli. Kwani ninavyofahamu ni kweli dada alikuwa na uhusiano na mume wa Eliza. Lakini shemeji naye alikuwa na uhusiano na Eliza.
Sasa sijui dada alikuwa anakataa nini? Kama sio unafki tu?
"Lakini ni kweli au sio kweli?" nilimuuliza bila kuhofia ukubwa wa kuzaliwa kwake.

Itaendelea....
 
Sehemu ya 57.

"Hakuna ukweli wowote mdogo wangu," alinijibu.
"Sasa unafikiri shemeji anatumia kigezo gani?"


Da Light hakujibu alibaki kimya kisha akageuka na kuangalia ukutani.
"Sijui mwenyewe asema anajua tu," alinijibu hivyo kisha akaniambia hataki tena maswali mimi siyo polisi wala mgambo wa jiji.

Nikabaki kimya tuli. Lakini nikawa nawaza sana. Nini kilimfanya shemeji aamini kuwa mkewe anajirusha mume wa Eliza. Kabla sijapata usingizi shemeji nilimsikia akisema kwa nguvu nje.

"Nakwambia nitakuua siku moja. Ohoo, we endelea tu. Unataka kuingia kaburini siku si zako," alifoka shemeji.

Kwa kutoshituka kwa dada nikagundua kuwa, alikuwa ameshalala usingizi, nikamtingisha kwa kumgusa na bega.
"Da Light, da Light," niliita.

"Mmmh."
"Hebu sikiliza shemeji anagomba huko nje."
Da Light aliinua kichwa kuachana na mto kama ishara ya kusikiliza vizuri kisha akakaa kabisa.

"Unabisha nikuchome kisu, unabisha," shemeji aliendelea kusema kwa hasira.
"Shahidi yako nani?" mume wa Eliza aliuliza naye kwa sauti iliyojaa hasira.

Da Light alikurupuka na kutoka nje huku akijifunga khanga vizuri. Na mimi nikafuatia.
Tulimkuta shemeji yuko na bukta tu, mume wa Eliza naye alikuwa katika taulo. Eliza naye alikuwa katika khanga moja ilizunguka kiunoni nyingine kifuani.
"Lakini dear huoni kama unajidhalilisha?" da Light alimwambia mumewe.

"Nyamaza, malaya mkubwa wewe," alisema shemeji. Da Light akafunga mdomo wake.
Niliamua kuingilia kati na kwenda kuwashika wote pamoja kisha nikamuuliza shemeji wanachogombania ni nini?
"Dada yako anatembea na huyu bwana," shemeji aliniambia.

"Eti, ni kweli?" nilimuuliza mume wa Eliza.
"Si kweli, lini? Aliniona wapi kwanza?"
Niliwashika wote na kuwavutia ndani kwa mume wa Eliza. Najua wote walikubali bila kuniletea tabu kwa sababu kila mmoja anajua alikuwa akinitaka. Kwa shemeji alijua ningeweza kusema kila kitu kuhusu yeye na Eliza. Na kama pangekuwa na mtu mwingine aliyekuwa akiwasikiliza angebaini kitu, kwani kelele zao hizo zote, Eliza alikuwa haongei kitu.

Tulikuwa wote watano tumekaa kwenye sebule ya Eliza. Shemeji alikuwa akihema kama swala aliyekimbizwa na simba.

Itaendelea.....
 
Sehemu ya 58.

Da Eliza yeye alikuwa ameinama chini, nadhani aibu. Mume wa Eliza alikuwa akihangaika kutuliza sura yake sehemu moja lakini akawa anashindwa. Eliza alibaki amejishika kidevu kwa mawazo.

"Nataka kuwaambia jambo moja, niko tayari kuhama hapa nyumbani kwenu kama mtaendelea kugombana," nilianza kusema...nikaendelea.

"Kati yenu shemeji wewe na shemeji wewe, nani hajatoka nje ya ndoa yake wiki hii?" niliuliza huku mapigo ya moyo yakiwa yananienda kwa kasi ya ajabu sana. Nilipaniki.

Hakuna aliyenijibu, si shemeji wa da' Light wala shemeji mume wa Eliza. Kila mmoja aliangalia chini kwa aibu. Walijijua matendo yao, kwa dhamira ikawa inawauma.

Moyoni niliwaza je, na mimi ningewakubalia ingekuwaje? Ingekuwa mchanganyiko usiokuwa na jina. Maana wenye jina unaitwa mchanyanto, ule sasa, yaani mimi Maria nitembee na shemeji mume wa dada yangu toka nitoke, halafu nitembee na mume wa shoga wa dada 'angu, halafu dada naye atembee na mume wa shoga 'ake na huyo shoga 'ake atembee na mume wa dada 'angu, loooo!

Sijui ni nini kilikuwa kimenipa ujasiri kiasi kile. Eti niliwaona wote kama watoto wadogo kwangu. Nikaamua kubwaga ukweli.

"Shemeji kwanini unamtuhumu mume wa Eliza anatembea na mumeo?" nilimuuliza shemeji, wote wakakaa kimyaa wakisubiria jibu.

"Ee siku moja nilikuta meseji ya mapenzi ya mume wa Eliza, nilipombana dada 'ako alikiri kwamba ni kweli alikuwa anamtongoza lakini alikuwa hajaona ndani. Lakini baada ya hapo nikaona kama siwaelewielewi, siku dada 'ako akisema atachelewa kurudi nyumbani na huyu bwana anachelewa kurudi.

Akisema anakwenda kwenye kipaimara cha mtoto wa rafiki yake na huyu bwana, hata jumamosi ambayo mara nyingi huvaa penzi tu, atavaa vizuri na kuondoka. Kwa vyovyote vile anatembea na mke wangu.

Leo pia dada 'ako kasema anakwenda kuona nyumbani kwa rafiki yake kule nanihi, lakini na huyu bwana nikamuona mitaa hiyo hiyo na hamsini zangu," shemeji alitoa dukuduku lake.

"Enhe shemeji pale unasemaje kuhusu tuhuma za mwenzio, tena mnakaa nyumba moja, sema ukweli," nilimgeukia mume wa Eliza.
Alisita kwa muda kisha akaanza kusema.
"Ni kweli...!" wote tukashtuka...akaendelea.

Itaendelea......
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom