SIMULIZI: Nilipanga Nyumba Moja na Majini

SIMULIZI: Nilipanga Nyumba Moja na Majini

Sasa kwa nini hakumpigia mwenye nyumba, unataka kuniambia aliingia mkataba na dalali badala ya mwenye nyumba, mhm!
 
MziziMkavu unadhani kwa mtindo huu wa kuleta hadithi nusu nusu utamfunika mjeda CHAI CHUNGU na ile riwaya yake ya binti mrembo wa ki-singida?!.humuwezi yule.jamaa alijipanga.:israel:
 
Last edited by a moderator:
Nilipanga Nyumba Moja na Majini -6

SASA ENDELEA…

Nilianza kuamini kwamba, kuna uhusiano mkubwa kati ya yule msichana na wale wapangaji wa pale ndani nilipo, inawezekana alinijua jina kwa sababu naishi nao na wana uwezo wa kujua jina la mtu kulingana na mazingira yao.

Pia niliwaza kwamba, kuna uwezekano mkubwa yule msichana alitokea baada ya maono yao kuniona mimi na yule mama wa jirani tukitaka kuwazungumzia wao kama wapangaji wenye maajabu hivyo hawakupenda iwe hivyo ndiyo maana msichana akaibuka na kusababisha mvurugano.

"Itakuwa kweli, ndiyo maana yule mama naye alisema ameshajua ni kwa nini aliugua kichwa ghafla, alijua yule msichana ni nani na kwa nini yeye kasikia maumivu ya ghafla vile."

"Lakini pia kuna wale wauza chipsi, nao niliwakumbuka hasa yule mmoja aliyesema yule msichana wanamjua, anaishi mtaani, lakini hawajawahi kubaini anaishi nyumba gani na kwa mzee nani wala anajishughulisha na nini," hayo yote niliyawaza mimi.

Nilisimama, nikachukua sabuni ya kuogea ambayo haijafunguliwa, nikaipiga chini kwenye kapeti kwa hasira huku nikisonya, nikasema kwa sauti ya chini:
"Humu ndani naishi na majini."
Kule chumbani nikasikia wakicheka.

"Si unaona, nimesema mimi, lazima naishi nao humu ndani, da! Najuta sana," nilisema. Kicheko kikasikika tena, safari hii kilikuwa cha juu zaidi kuliko kile cha awali.

Moyo ulijaa mawazo, akili ilihisi uchungu wa maisha, niliwaza fedha nilizozilipa kwa ajili ya kupanga mle ndani, nikamkumbuka dalili, niligundua alichofanya ni kunitapeli na hakuna lingine wala hakuwa msaada kwangu.
"Mimi ni mwanaume, kama niliweza kupata fedha za kupanga hapa, sishindwi kupata nyingine za kupanga sehemu nyingine tena mbali na hapa," nilisema kwa moyoni.
***

Usiku nikiwa nimelala, nilichelewa sana kupata usingizi, ghafla nikaona taswira za watu ukutani, wawili tena wakiwa wamesimama, ni mwanamke na mwanaume. Niliogopa sana, nikainua kichwa polepole kuwaangalia kwa umakini, japo kulikuwa na giza, lakini niliweza kuona vizuri lakini si kwa uwazi mkubwa kama ambavyo taa ingekuwa inawaka.

Ni kweli walikuwa watu wawili kama nilivyoona, tena weupe nikimaanisha si watu weusi. Walikuwa wakionesha vitendo vya kucheka huku wakijinyonganyonga.

Kuna wakati walitembea mpaka jirani na kitanda changu kisha wakageuza na kurudi pale ukutani. Nilipeleka mkono hadi kwenye swichi ya kitanda (bed switch), nikawasha, cha ajabu sikumwona mtu wala dalili pale ukutani.
Niliamka nikiwa nahema kwa kasi mpaka nikajishika kifuani, nikafungua mlango na kutoka nje ili nijifanye nakwenda chooni lengo langu lilikuwa kupata picha kwa wenzangu kukoje maana niliwashuku wao na wale walioonekana chumbani kwangu.

Kwa wenzangu niliwasikia wakikoroma kwa zamu. Nikajiuliza ina maana si wao waliokuja chumbani kwangu? Niliona ni utani wa hali ya juu.

Niliamua kurudi chumbani na kukatisha safari ya kwenda chooni, nikafunga mlango wangu kwa funguo na kupanda kitandani, nilizima taa ili nione kama yale mauzauza yatatokea tena.

Ukimya ulitawala kwa muda bila kujitokeza chochote, nikaanza kupitiwa na usingizi kwa kusinziasinzia, ghafla ukutani nikawaona tena wale watu wawili.

Safari hii walikuja hadi kitandani, wakakaa, wakasimama, wakaenda kwenye kabati, wakafungua, wakatoa mashuka na kujifunika, wakayarudisha, wakaenda nyuma ya mlango, wakatungua mashati yangu mawili, wakagawana na kuyavaa kisha wakayavua, mmoja mwanaume akaenda sehemu yenye redio, akapeleka mkono, nikajua anataka kuiwasha, lakini hakufanya hivyo.

Nilichoamua kukifanya akilini ni kuwasha taa kwa ghafla na kuwavamia na nilipanga kumvamia mwanamke nikiamini ndiye aliyekuja kule kwenye chipsi. Polepole nilipeleka mkono hadi kwenye swichi, nikawasha taa kwa ghafla huku macho yangu yakiwa kwao, lakini sikumwona hata mmoja! Kwangu haikuwa mapambano bali nilichukulia kama changamoto za maisha.

Asubuhi, niliamka nikiwa nimechoka sana, lakini kabla sijatoka kitandani nilisikia nje ya mlango kukiwa na hali ya watu kutembeatembea tena kwa kasi, niliinua shingo ili nione kama nitasikia zaidi, lakini kukawa kimya.
Niliamka, nikatoka, nilikwenda sebuleni kwanza kuangalia kama kuko salama.

Nilishangaa kukuta mezani kuna mfuko wa rambo uliojaa chipsi kuku kama nilivyonunua mimi, lakini zangu nilikula, sasa zile sikujua zilitoka wapi.

Niliubeba ule mfuko nikatoka nao, nilifungua mlango mkubwa wa nje nikautupia pembeni kidogo, niliporudi, nikaenda chooni, mlango ulikuwa umefungwa kwa ndani kwani hata niliposhika kitasa na kukivuta kilikuwa kigumu.

Hii iliashiria kwamba kuna mtu, kwa hiyo moyoni nilisema nisimame palepale nje ya mlango hadi atoke. Nilisimama eneo ambalo akitoka tu, uso kwa uso na mimi.

"Tuone leo, wao si wajanja, leo nimemnasa mmoja wao," nilisema moyoni. Dalili zote zilionesha kwamba mle chooni mlikuwa na mtu kwani niliweza kusikia hata kuhema kwake, mara mlio wa maji, mara alikohoa, tena kwenye kukohoa nikabaini mtu mwenyewe alikuwa ni mwanamke ndiye aliyekuwa mle.

"We kohoa mpaka utapike, lakini mimi nipo hapa mpaka utoke," nilisema moyoni. Nilikaa sana, ikafika mahali nikachoka, lakini moyoni nikasema siondoki hata iweje, lakini nilishtuka kitu, niligundua muda mrefu sijazisikia zile dalili kama maji au kuhema, nikafunguka akili. "Mh! Siyo kwamba ametoka?"

Ile namalizia kusema ‘ametoka?' nikasikia kicheko kutoka kwenye chumba chao. Vicheko vikubwa sana cha kike na kiume.

Nilirudi chumbani mwili ukinisisimka, hapo ndipo niliamini mia kwa mia kwamba, nilikuwa nadili na watu wasiokuwa wa kawaida.

Niliingia chumbani, nikampigia simu dalali.
"Haloo," niliita.
"Haloo. Halooo," nilirudia lakini sikupokelewa.
Nikiwa nimeachana na simu, mara iliita yenyewe, alikuwa ni dalali nikapokea.
"Haloo," niliita.
"Haloo," niliitikiwa lakini sauti haikuwa ya dalali.
"Mzima bwana?" nilisalimia.

"Tuone leo, wao si wajanja, leo nimemnasa mmoja wao."
Ha! Nilishtuka sana, nilisikia sauti yangu mwenyewe ikisema hivyo. Ikaendelea.

"We kohoa mpaka utapike, lakini mimi nipo hapa mpaka utoke."
Nilikata simu, nilikuwa nahema sana, mapigo ya moyo yalikuwa yakienda kwa kasi ya ajabu huku nikishindwa kuona sawasawa.
"Hii ni hatari sasa," nilisema.

Usiku wa siku hiyo sikulala kusema kweli kwani kila nilipofikiria maisha yale sikuona sababu ya kuendelea kuishi pale. Moyoni nilisema kwamba, ni afadhali ningeishi na watu ambao ni majambazi kuliko hawa, nafuu ningepanga nyumba moja na makahaba kuliko kupanga nyumba moja na majini.

Nilichoamua, asubuhi nikifika kibaruani tu niombe ruksa kisha nianze kumsaka yule dalali na pia nitafute dalali mwingine ambaye atanitafutia vyumba kwingine na si maeneo yale tena kwani niliyaona yana nuksi.

Asubuhi kulikucha salama kabisa, tena usiku wa siku hiyo sikuona mauzauza wala dalili zake. Nilikwenda kuoga bila kukagua mazingira, moyoni nilisema liwalo na liwe kwa maana kwamba, wawepo wasiwepo sawa tu.
Bafuni niligundua wameshaoga kwani kulikuwa na majimaji ya muda mfupi uliopita. Nilipomaliza kuoga, nilijiandaa na kutoka. Nje nilikutana na mtu ana mkokoteni, akanisalimia.
"Za asubuhi bwana mkubwa?"
"Salama, karibu sana."
"Asante, kuna watu fulani wanaishi humu nina shida nao."
Aliposema hivyo nilishtuka sana, niliamini yeye ni mmoja wa wale ila amejigeuza kwa kujifanya ana shughuli za mkokoteni.
"Unawajua kwa sura?" nilimuuliza huku nikiwa na wasiwasi maana alinikazia macho.
"Siwajui."
"Sasa una shida nao kivipi watu usiowajua kwa sura?"

Ni kwamba, kuna binti mmoja huwa wanamtuma niwaletee maji, nikifika hapa huyo binti anabeba madumu kupeleka ndani, sasa jana nilikutana na huyo binti nikamuuliza kuhusu malipo yangu ya mwezi sasa, akasema nije nifuatilie mwenyewe."

Nilishangaa sana kusikia hivyo. Nijuavyo mimi mle ndani mna watu wawili, mwanamke na mwanaume, sasa kama kuna binti hilo lilikuwa jipya kwangu, labda lakini.
"Huyo binti naye anaishi humu au?" nilimuuliza.
"Sidhani, inaonekana kama huwa wanamtuma tu."

"Kwa nini huamini kama anaishi humuhumu ndani? Hafanani na wao wenyewe?" hili swali niliuliza likiwa na mtego mkubwa sana, nilitaka nijue uhalisia wake.

"Siwezi kusema hafanani wakati wao siwajui kwa sura."

Hapo ndipo nilipopataka, nilidhani atasema hafanani nao, ningejua ni walewale.

"Oke, nadhani wameondoka kwenda kazini."
"Ah! Sasa mimi fedha zangu nitazipataje jamani?"
"Subiri wakirudi jioni."
"Wewe utakuwepo?"
Nililishangaa swali hilo, hakuwa akinidai mimi lakini anataka niwepo?
"Unataka niwepo?"
"Ee."
"Kwa nini?"
"Naamini utanisaidia kuzipata fedha zangu."
"Uliwahi kuja wakagoma kukupa?"
"Siyo hivyo, ila kila nikija, nikigonga mlango huwa hawafungui."
"Basi nitakuwepo."
"Asante kaka. Nije saa ngapi?"
"Saa moja nitakuwa nimerudi."
Aligeuza mkokoteni na kuondoka zake huku akisema:
"Muda huo nitakuwa nimefika kaka."

Niliondoka kwenda kazini kuomba ruksa. Lakini wakati naondoka, mfanyakazi mwenzangu mmoja aliniuliza nakwenda wapi, nikaamua kumsimulia kwa ufupi kisa changu.

"Kha! Sasa hapo tatizo liko wapi, mbona dawa ipo rahisi sana."
"Rahisi! Ni ipi hiyo?"
"Sikia, twende pembeni nikakusimulie," aliniambia yule mfanyakazi mwenzangu huku akiangalia kulia na kushoto kama mabosi watatokea.
Tulikwenda kusimama pembeni, akaanza kuniambia:

"Sikiliza, kama unaishi nyumba ya namna hiyo, unachotakiwa kufanya, kila siku asubuhi na jioni au usiku unapuliza bangi ndani ya nyumba, kama ni majini, mapepo sijui nini, utaona mambo poa kabisa."
Sikuamini maneno hayo, nikamuuliza mara mbilimbili kama ni kweli.
"Khaa! Nina mjomba'ngu aliwahi kuishi kwenye nyumba ya hivyo, akaenda sehemu akaelekezwa dawa ni hiyo, akaitumia, mpaka sasa anaishi kwa raha hakuna cha majini wala mapepo," alisema.

Nilimsikiliza nikianza kuamini kwa mbali, lakini nilifika mahali nikamuuliza hiyo bangi mimi nitavuta au nitaiwasha ili itoe moshi yenyewe?
"Ukishaiwasha, utaiweka mezani au popote ndani kwako, lakini angalia isizimike ili moshi wake usambae chumba kizima au sebule nzima."

"Hilo linawezekana," nilimwambia nikimtumbulia macho.

Kwa sababu nilikuwa nimeshaaga, ilibidi niondoke tu na kurudi baadaye. Nilikwenda mtaani, nilitafuta bangi nikapata maeneo ya Kariakoo, nikaitia mfukoni.

Nilizurura sana siku hiyo, saa tisa kamili nilikuwa njiani narudi kazini. Nilipiga hesabu za kufika kazini na kuondoka, maana muda wa kazi ni saa tisa na nusu.

Wakati napita pale Kituo cha Polisi Msimbazi, fujo zikazuka, kuna machinga wawili walikuwa wanapigana kwa sababu ya kugombea sehemu ya kufanyia biashara, katika ugomvi huo mimi nilibaini mmoja wao ndiyo mwenye kosa.

Nikampa laivu kuwa yeye ndiye mwenye tatizo, alikuja juu, akachukua boksi lenye viatu na kunirushia, likanipata kwenye bega la kulia, sikukubali, nikaokota jiwe na kumrushia, likampata mkononi.

Polisi walifika haraka sana, wakanikamata mimi, yeye na yule machinga niliyeona anaonewa, tukapelekwa Msimbazi polisi.

Tulipofika pale, afande aliyetukamata alituamuru kuvua viatu, mikanda, simu kuweka pembeni. Halafu mmoja alianza

kutusachi mifukoni. Wakati tendo hilo linaanza kwa wenzangu, ndipo nikakumbuka mimi mfukoni nina vipisi viwili vya bangi.

Nilitaka kutoka mbio kituoni hapo, lakini sehemu tuliyokaa, ningesema nitoke, nisingefika nje au hata kama ningefika ningekamatwa au kupigwa risasi kama mhalifu, nilitetemeka, mwili uliisha nguvu.

Ilipofika zamu yangu kusachiwa, askari mwenyewe alishangaa kuniona nachezesha miguu kama niliyebanwa na haja ndogo, akaniuliza:

"We vipi, unaumwa?"
Nikamjibu naumwa afande.
"Unaumwa nini?"
"Sijui, nadhani homa."

Hakunijibu, alianza kwa kutumbukiza mkono kwenye mfuko usiokuwa na kitu, akahamia wa nyuma ambao una waleti, akapeleka wa kulia kwangu ambao ndiyo wenye bangi, aliposhika, akakunja sura, alipotoa akashtuka sana na kusema:
"Haa! Hii bangi siyo?"

Sikumjibu kwani niliamini ameshaijua, wenzake waliokuwa kaunta wakaacha mambo yao na kunigeukia mimi, nao wakashangaa sana. Mmoja alikuwa amekaa juu ya stuli, akashuka huku akiniangalia kwa kunikazia macho.

"Unakuja kituo cha polisi na bangi, wewe unatutafuta nini sisi?" aliuliza yule aliyeshuka kwenye stuli.
Niliambiwa nafunguliwa kesi ya pili, ya kwanza kupigana na kujeruhi ya pili kukutwa na bangi!
Nilijitetea nikisema bangi ile si kwa ajili ya kuvuta bali nilikuwa nina shida nayo.

''Wewe usitufanye sisi watoto wadogo, tunawajua ninyi raia," alisema yule afande aliyenisachi.
Lakini afande mmoja wa kike ambaye muda wote alikuwa akiangalia tu, akawaambia wenzake:
"Lakini huyu kaka mbona hafanani na kuvuta bangi, muulizeni ana shida nayo gani?"
Wale wenzake wakanigeukia na kuniuliza:

"Haya, wewe mwananchi, raia kabisa, unaweza kuwa na shida gani na bangi mbali na kuvuta?"
Niliwasimulia kila kitu, tena nilifika mahali nikawaambia kama kuna asiyeamini, tuongozane hadi nyumbani, Magomeni akaone maajabu ambayo hayahitaji kuelekezwa sana ili kuamini kama yapo au la!
Palipita ukimya wa sekunde kadhaa, mmoja wao akaniuliza:

"Kama ni kweli au tufanye ni kweli, ni kwa nini umemuumiza huyu?"
Nilisema kilichotokea, yule chinga niliyemsaidia naye akanitetea kwa kusema hivyohivyo, lakini afande mmoja akasema nilijichukulia sheria mkononi ambapo ni kosa kisheria.

Niliomba sana wanisamehe kwa yote, nikasingizia kwamba ni kwa sababu kichwa changu hakipo sawa kwa kuishi nyumba moja na majini.

Namshukuru mmoja wao aliniambia niondoke lakini nihakikishe situmii bangi katika kujitibu kwani serikali haiamini kama bangi ni dawa.

Nilipotoka, nilikwenda kununua nyingine, lakini akili iliingia hisia kwamba, huenda yule dada wa ajabu mle ndani ndiye anayecheza michezo ili kunikwamisha kwenda na bangi ndani ya nyumba, nikasema moyoni ngoja ninunue hii nione kitakachotokea, nikanunua tena misokoto miwili.

Nilitembea kuelekea kituo cha daladala. Njiani nilimpigia simu yule mfanyakazi mwenzangu aliyenijulisha kuhusu dawa ya kutibu nyumba yenye majini, nikamwambia sitaweza kurudi kwani nilipata wakati mgumu kidogo njiani.

Alinielewa, akaniuliza kama nimepata, nikamjibu kila kitu kimekwenda sawa, lakini sikumwambia kuhusu timbwili lililojitokeza.

Nilipanda daladala nikashuka Magomeni, niliingia ATM kutoa fedha kidogo, kisha nikatoka. Wakati natafuta mwelekeo wa kwenda nyumbani, nilimkumbuka dalali, nikampigia simu.

"Halo."
"Halo habari za kazi bwana?"
"Nzuri, pole na kazi na wewe mwenzangu?"
"Nimepoa. Bwana vipi kuhusu nyumba?" nilimuuliza.
"Nyumba imefanyaje?"
"Si nilikusimulia matatizo yake, umesahau?"
"Kwani ulisema matatizo yake yakoje vile?"

Nilimwelezea kwa kirefu, nikafika mahali nikamwambia hadi nilivyompigia simu halafu ikapokelewa na sauti ya ajabuajabu, alicheka sana.

"Wewe bwana acha kunichekesha.
"Kwa nini unasema hivyo?"
"Yaani simu yangu mimi halafu apokee mtu mwenye sauti ya ajabuajabu, kwa nini sasa?"
"Mimi pia sijui."
"We ulikosea namba."
"Labda bwana mi siwezi kukazania sana," nilimjibu kwa kinyongo kwani namba yake niliisevu na ninapompigia huwa nasachi jina tu, sasa nilikosea kivipi?
"Enhe, unasemaje bwana?" aliniuliza.
"Nimeshakwambia bwana."
"Kwa hiyo unashauri nini?"
"Nataka pesa zangu nikapange kwingine."

"Da! Hilo halitawezekana kirahisi bwana, maana mpaka nimpate mpangaji mwingine atoe fedha ndipo nikulipe wewe na mpangaji atakayekuwa tayari kutoa fedha lazima akute nyumba tupu, sasa wewe utalikubali hilo?"

"Naweza kulikubali, ila tuandikishiane."
"Kwamba?"
"Kwamba unajikomiti nikiondoka, akiingia mpangaji mwingine tu unanilipa pesa zangu."
"Ngoja nitakupigia," alisema dalali na kukata simu.
Nilipokuwa nakaribia nyumbani, nikakutana na yule msukuma mkokoteni wa maji.
"Kaka za kazi?"
"Nzuri, vipi wewe?"
"Niko sawa, ndiyo unarudi?"
"Ndiyo."
"Najua jamaa hawajarudi, nitakuja muda uleule tuliopanga."
"Sawa, karibu sana."
"Asante sana."

Niliingiza funguo ili kufungua mlango, lakini nikagundua kwa ndani kulikuwa na funguo nyingine maana nilichungulia.
Nilipousukuma, ulifunguka. Hii ina maana wale watu wa ajabu walikuwa wamesharudi, wako ndani. Niliingia ndani, nikafungua mlango wa sebuleni, nikaingia humo.

Nilifikia kwenye kochi kubwa, nikajilaza. Sikuangalia kama kweli wenzangu walikuwa wamesharudi, ila nilisikia sauti ya muziki wa redio, nikajua wapo.

Mara nikasikia mlango wao mmoja ukifunguliwa, nikasikia mtu akitoka. Kwa mara ya kwanza nilisikia akisema:
"Kama utamkamata anavuta bangi apelekwe polisi, ndiyo dawa yao watu wa aina hii."
Nilishtuka, nikakaa. Nikawaza kama ninachosikia ni cha kweli au?

Huyo aliyekuwa akisema hayo ni mwanamke na ilionekana alitoka kuelekea uani. Nikatoka ghafla, nikaona kisigino cha mguu mmoja kikimalizia kuingia chooni.

Nilirudi chumbani huku najiuliza kama hawa watu walisema vile kwa sababu wamejua mimi nimenunua bangi au? Na ni kwa nini wazungumze Kiswahili kwa mara ya kwanza siku hiyo?
Baada ya dakika mbili, nilimsikia akirejea chumbani kwake huku akisema:
"Mimi mtu anayevuta bangi siku yoyote na mahali popote pale, nikimwona nampeleka polisi ajue mimi ni nani. Haiwezekani watu wawe wanavuta bangi hovyo tu.

Moyoni nikasema hata iweje, hii bangi leo lazima niichome humu ndani. Mkienda polisi msipoenda mtajua wenyewe.
"Mimi siwezi kuishi katika mazingira magumu namna hii wakati pesa ni yangu. Kwa nini ustaarabu usiwepo?" nilisema moyoni nikipeleka mkono mfukoni ili kutoa ile bangi niliyonunua mara ya pili.

Niliipata, nikaitoa. Niliiweka kwenye meza kisha nikaendelea kulala nikiusaka usingizi kwa nguvu zangu zote maana nilijisikia kuchoka sana. Hapo nilikuwa sijaenda chumbani kwangu.
Sikumbuki ni muda gani nilipitiwa na usingizi, ila nakumbuka wakati nalala ilikuwa saa kumi na moja. Nilipokuja kushtuka

ilikuwa saa kumi na mbili na nusu. Ina maana nililala kwa saa moja na nusu.
Jicho langu moja kwa moja lilitua kwenye bangi pale mezani, sikuiona.

Je, nini kiliendelea? SOMA SEHEMU YA KUMI

 
Ndio maana niliomba JUKWAA LA :MAISHA,MIKASA na USHAURI
threads nzuri za mikasa kama hii ingekuwa huko.Unasoma mpaka mwisho tujue uzoefu uliotamalaki duniani
 
Weeee humuli njoo umalizie basi mimi kule kwa mjeda kumenishinda stori haiishi alafu na pandisha mafaili ile mbaya
 
Though mimi ni mpenzi WA horror movies, for the first time in my life, I am scared reading these MziziMkavu's stories!
Hii ni kwa sababu Leo nimeshuhudia mtu anayesumbuliwa na majini kuanzia jana yanajiita makata, zainabu na mariam! I am realy so scared talking about them!

Sent from my BlackBerry 8520 using JamiiForums
 
Last edited by a moderator:
Tunakusubiri mzizi mkavu lete uhondo,mbona hata humi mmu tuna majini tunachat nayo?
 
Nilipanga Nyumba moja na Majini-10

Nilihamaki kwa kusema ha! Nani amechukua bangi yangu? Sikujibiwa na mtu, ukimya ulitawala huku akili ikiniambia wale wapangaji wenzangu watakuwa wanahusika moja kwa moja.

Baada ya muda nilitoka mle sebuleni, nikaenda chumbani. Nilifungua mlango na kusimama kwanza kabla ya kuzama ndani. Niliangaza kila kona, nikabaini kitu.

Niligundua kwamba, kuna mtu alikaa kitandani maana nilipoondoka asubuhi nilikuwa nimekitandika, muda huo kwa pembeni upande wa mbele kulikuwa na alama za makalio.

Alama hiyo ilinipa picha kuwa, aliyekaa alikuwa na makalio makubwa sana! Nilipoangalia chini kwenye kapeti nikabini kitu kingine kwamba, aliyekaa alikuwa na mafuta kwenye miguu kwani iliweka alama kuzunguka miguu yake.

Aidha, nilibaini jambo jingine kwamba, aliyekaa kitandani pia alikuwa akisimama na kutembeatembea kwani alama ya miguu yenye mafuta ilionekana sehemu mbalimbali za chumbani kwangu.

Mara nikasikia hodi ikigongwa mlango mkubwa. Niliikumbuka ile sauti kwamba ilikuwa ya yule msukuma mkokoteni wa maji.

"Nakuja," nilisema kwa sauti kupitia dirishani kwani chumba changu na sebule yangu vilikuwa upande wa mlango mkubwa wa kuingilia.

Nilitoka mpaka mlangoni, nikafungua na kumkuta yule kijana.

"Bro vipi, wapo wale watu ndiyo nimekuja hivi."

Nilimshika mkono, nikamvuta kumwingiza ndani bila kusema naye. Nilimwelekeza vyumba vya wale wapangaji wenzangu kisha mimi nikaingia chumbani kwangu.

Nilikaa kitandani na kutega sikio kitakachotokea huko. Nilimsikia yule kijana akigonga mlango. Aligonga mara tatu, kisha nikasikia mlango ukifunguliwa, sikuamini. Nilitaka kutoka, lakini nikasema nisubiri hadi mwisho nione.

Baada ya mlio wa kufunguliwa kwa mlango, ukafuatia mlio wa kufungwa halafu ukapita ukimya. Akilini nilijua wamemkaribisha na wakafunga mlango na sasa wanaongea naye.

Cha ajabu, kila nilipofuatilia ili kujua kama mlango utafunguliwa na yule kijana kutoka, sikufanikiwa kugundua hali hiyo, nikaanza kupata wasiwasi.

"Inamaana tangu wakati ule hadi sasa bado wapo ndani? Wanaongea nini sasa? Au wanapigiana mahesabu? Si yule kijana alisema anadai pesa nyingi?" maswali hayo yote yalikuwa yangu lakini majibu yake sikuyajua.

Usiku uliingia, muda ukazidi kwenda, sikusikia ishara yoyote ya yule kijana kutoka. Zaidi sana nilisikia wale wapangaji wenzangu wakipika kwa kukaangiza kitu kama nyama.

Usiku nilitoka, nikaenda kutafuta chakula, nikarudi nacho nyumbani. Nikala, nikaenda kuoga, nikarudi kitandani na kulala, sikuona dalili ya mawengewenge wala mang'amng'amu.

Asubuhi niliamka kwa kushtuka, lakini sijui nini kilinishtua ila ni kama kuna mtu alinishika mguu. Hakukuwa na kitu chochote chumbani mwangu. Nilitoka na kwenda kusimama kwenye dirisha, nikachungulia nje. Kulikuwa shwari.

Nilipotoka kuoga nikiwa navaa nguo ili kuondoka, nikasikia wenzangu wakitoka. Nilisimama tena dirishani kwani kwa mtu anayetoka kwenye nyumba ile na kwenda popote ilikuwa lazima apite mbele ya dirisha langu.

Baada ya muda walifungua mlango mkubwa, nikasikia wakiufunga, lakini baada ya hapo sikumwona mtu yeyote yule akipita mbele ya dirisha.

Na mimi nilipomaliza kujiandaa, nilitoka, nikafungua mlango na kutoka. Mbele kidogo nilikutana na watu kama kumi wamesimama wakiongea. Niliwasalimia nikawauliza kama kuna usalama.

"Usalama ni mdogo bwana, kuna kijana mmoja amepotea. Tangu jana usiku alipotoka kwa mkewe akasema anafuatilia

madeni ya biashara zake hajarudi," alisema mzee mmoja ambaye alisimama akiwa amejishika mikono kwa nyuma.
"Ni biashara gani anafanya?" niliuliza.
"Huwa anauza maji kwenye mkokoteni."
"Ha! Ni yule muuza maji?"
"Huyohuyo," alisema yule mzee.

Akili za haraka nikasema hapa ndipo pa kujua wale wapangaji ni akina nani, inabidi niseme ukweli ili waende polisi, najua
polisi watakuja kukagua ndani.

"Lakini mbona jana usiku alikuja kwangu kudai pesa yake?" nilihoji kwa uso wa wasiwasi.
"Ulipomlipa akaondoka?" mwanamke mmoja aliniuliza.
"Siyo kwangu, ila mimi ndiye niliyemfungulia mlango. Alipoingia akawaulizia wapangaji wenzangu, nikawaonesha chumba, akapiga hodi, akakaribishwa ndani."
"Hukumuona kutoka?"

"Kwa kweli sikufuatilia maana na mimi nilirudi chumbani kwangu."
Wale watu wakaniuliza kama naweza kuwapeleka pale nyumbani, nikawaambia kwa muda ule hapakuwa na mtu nyumbani, wanarudi jioni.

"Basi tunakwenda kuwaambia ndugu zake, jioni watakuja, si nyumba ile pale?"
"Ndiyo."

Nilipofika kazini na kuanza kazi, akili zangu zikawa zimefunguka kitu. Nilijiambia wale watu wakijua ni mimi niliyetoa mchoro wote, watanifanyaje?

Nilibaini nimechemsha, lakini nikasema moyoni kwamba potelea mbali, wajue wasijue sawa tu.
Kuna wakati nilipigiwa simu, namba sikuitambua, yaani ilikuwa ngeni kwenye kumbukumbu zangu. Nilijiuliza mwenyewe kwamba anaweza kuwa nani, lakini sikupata jibu.

Awali nilisita kuipokea kiasi kwamba ilikata, mpigaji akapiga tena. Nikaamua kuipokea sasa:
"Halooo," nilivuta sauti.
"Hujambo bwana?"
"Nani mwenzangu?"
"Hujambo, hata kusalimiana pia unataka kujua nani, ungeitika kwanza kisha ndipo uniulize nani."
"Sijambo, nani mwenzangu?"
"Angalia sana bwana," alisema huyo mtu bila kujitambulisha kisha akataka simu.

Nilishangaa sana, nikaanza kazi ya kuwaza kwamba anaweza kuwa nani na ni kwa nini aniambie angalia sana?
"Atakuwa jamaa wa nyumbani, kwa vyovyote vile," nilisema moyoni na kuamini hivyo kwani kwa maisha ninayoishi mimi si rahisi kuwa na maadui. Mapigo ya moyo yalianza kwenda mbio kwa wasiwasi. Nilijua nimeingia kwenye mapambano makubwa na wale wapangaji wenzangu.

Niliendelea kufanya kazi, lakini sikuwa na amani tena. Mara alitokea yule mfanyakazi mwenzangu ambaye alinipa ushauri wa kupulizia bangi ndani ya nyumba ili kuwakimbiza majini au viumbe wote wabaya.
"Vipi mambo yako, yamekwendaje?"

"Mambo gani?" nilimuuliza huku nikiwa namtazama. Kisa cha kumtazama kwanza ilikuwa kujiridhisha kama kweli ni yeye au wale wapangaji wenzangu wameamua kunifuata ‘laivu'.
"Si yale niliyokuelekeza kufanya."

Nilipomkazia macho sana, akasema ana kazi nyingi, akageuza na kuondoka. Mlango ulipojifunga tu, nikajiegemeza kwenye meza na kuwaza mambo kibao. Ilikuwa kama nataka kusinzia, lakini nikasikia sauti kichwani zikisemezana hivi:

"Halooo."
"Hujambo bwana?"
"Nani mwenzangu?"
"Hujambo, hata kusalimiana pia unataka kujua nani, ungeitika kwanza kisha ndipo uniulize nani."
"Sijambo, nani mwenzangu?"
"Angalia sana bwana."
Mara nikasikia tena zikisemazana hivi:
"Vipi mambo yako, yamekwendaje?"
"Mambo gani?"
"Si yale niliyokuelekeza kufanya."

Nilishtuka na kusimama, nikaondoka kwenda nje. Nilikutana na yule mfanyakazi tena, akaniuliza kama naondoka.

"Vipi, unaondoka saa hizi?"
"Bado nipo."

"Kwanza nilisahau kukuuliza, vipi ulifanikisha ile kitu ya kuvuta kama nilivyokwambia?"
Moyo ulishtuka, nilijua ni watu wawili kwani huyu angekuwa yule aliyenifuata muda ule, asingesema alisahau kuniuliza.
"Nilifanikiwa kupata bwana, lakini," nilisema nikimshika mkono, nikamvutia pembeni kidogo.
"Kaka mambo makubwa kule. Kwanza unajua kama nimekuona wewe mara ya pili hii leo?"
"Kivipi?" aliniuliza.

Nilianza kumsimulia kila kitu, kuanzia zile bangi hadi nusu saa kabla sijaonana naye. Alishangaa sana, akasema yeye ndiyo kwanza anaingia, alikuwa Kariakoo, pia akasema kwa siku hiyo ndiyo kwanza ameniona mimi muda ule.

"Sasa itakuwaje ndugu yangu?" aliniuliza.
"Sielewi."
"Sasa sikia, mimi ninajua nitapata wapi bangi, we usiku saa moja niambie tukutane wapi, nitakuja nayo halafu nitaiwasha na kuivuta mimi."
"Wewe huogopi?"
"Niogope nini?"
"Kufa."
"Nani ataniua?"
"Si hao watu wabaya."
"Hamna, hawawezi."

Nilimkubalia, nikamwambia nitampigia saa moja ili tukutane akiwa na hiyo bangi yake.
Akili zangu hazikukaa sawa, niliondoka kwenda kutafuta maji ya kunywa, kisha nikaenda kupumzika kwenye kibanda cha kuuza vocha za simu.

Pale, mtu yeyote anayenijua angeniona angebaini nina matatizo mazito kichwani mwangu, kwani sikuwa sawa hata usoni. Muda mwingi niliwaza maisha ya kwenye ile nyumba, hasa usiku wa siku hiyo ambapo najua wale watu wakija ndiyo balaa litakuwa kubwa zaidi.

"Halafu usiku wa leo lazima watakuja kunifanyia maajabu yao, lakini dawa yao nisilale. Oke, kumbe bangi itapulizwa leo, kidogo itakuwa nafuu," nilisema moyoni, nikashtuliwa na sauti ya kike nyuma yangu iliyoita jina langu.

NILIPOGEUKA nyuma, nikamwona dada mmoja aitwaye Mwantumu Seleman nilikuwa naishi naye Mwananyamala. Akaniuliza habari za siku. Niliamua kumsimulia janga langu, lakini ghafla likaja gari, akaingia huku akiniambia atanitafuta siku nyingine.

Baadaye nilirudi kazini huku nikiwa na hali ya wasiwasi, hata kazi zangu zikuzifanya sawasawa kama ilivyo kawaida yangu. Iliniuma sana!

Muda wa kazi ulipokwisha, niliondoka moja kwa moja hadi nyumbani. Sikutaka kupitia mahali siku hiyo, lakini nilishakubaliana na yule mfanyakazi mwenzangu aliyesema atakuja na bangi yake.

Wakati nafungua mlango mkubwa nilibaini wenzangu walisharudi maana mlango haukufungwa na funguo, nikaingia ndani. Nilipofika kwenye mlango wangu wa kuingilia sebuleni, wakati naufungua nikasikia mlango wa chooni unafunguliwa, yaani kumaanisha kwamba kuna mtu anatoka.

Ukisimama mlangoni pangu, mtu akitoka chooni unamuona bila kificho, hususan kama anakuja vyumbani. Lakini pia hata akiwa anatoka kwenda uani, utamuona kwa mgongoni. Nilisita kuingia nikiamini nitamwona mtu huyo. Nilianza kuona miguu ikitoka, moyo wangu ukashtuka, mara nikamwona mtu mwenyewe.

Nilijikuta nikisisimka mwili, niliamini naona kivuli chake na si yeye. Ni mtu mweusi, wakati nilitarajia angekuwa mweupe.
Alivyozidi kunisogelea, nikabaini kuwa, ni yule kijana muuza maji kwenye mkokoteni.

"Ha! Wewe vipi, unatafutwa sana unajua?" nilimwambia.

Badala ya kunijibu, alikata kona kuufuata mlango mkubwa. Na mimi nikamfuata kwa nyuma, nilimkuta akiwa anamalizikia

kutoka nje. Niliitupa simu kwenye kochi kisha nikatoka kumfuata, na mimi nilifungua mlango ambao ulishaanza kurudi baada ya yule kijana kutoka.

Nilishangaa kutomuona popote kule nje. Wazee wawili walikuwa wanapita, nikawauliza kama wamemuona mtu ametokea mlangoni pale, wakasema hapana, ila kuna mbwa alitokea ndani kazunguka nyumba.

"Mh! Mbwa tena?" niliwauliza wale wazee, nao wakasisitiza kuwa ni mbwa, tena mweusi.

Mapigo ya moyo yalianza kwenda mbio, wasiwasi uliongezeka kiasi cha kunifanya niishiwe nguvu. Wakati huo wale wazee walikuwa wakimalizikia kwa mbali. Niliogopa kurudi ndani, nikawa nimesimama mlangoni.

Wazo lilinijia kwamba, nimpigie simu yule mfanyakazi mwenzangu kumuomba aje mapema maana hali ni mbaya sana. Lakini simu nayo ilikuwa sebuleni kwenye kochi, nitaipataje, yaani nitaifuataje kule ndani wakati niliamini tayari kumeshakuwa ukanda wa kifo?

Niliteremka na kusimama nje kabisa, ghafla kwenye dirisha la chumbani kwangu nikaona kama mtu anachungulia nje, nilikaza macho ili kumwangalia vizuri, akapotea.

"Mh! ni kweli?" nilijiuliza mwenyewe. Ukweli ni kwamba alikuwepo mtu, tena mweusi au niseme Mwafrika kama mimi.

Nilikwenda pale dirishani, nikapanda ili kuchungulia, nikaona mlango unafunguka kuashiria kuna mtu alitoka maana mlango ule ulikuwa hauwezi kukaa wazi, ni lazima ujifunge wenyewe na mbaya zaidi mimi nilikuwa sijaufungua zaidi ya ule wa sebuleni.

Kuna jamaa mmoja alikuwa anakuja kutokea upande ninaoondokea kwenda kazini, simfahamu lakini nilimsimamisha.

"Bro kuna ishu hapa inatisha kidogo, naomba msaada wako."
"Kuna nini?" aliniuliza.
Nilimsimulia kila kitu cha siku ile tu lakini, sikugusia mambo ya nyuma.
"Du! Kwa hiyo mimi nikusaidieje?"
"Naomba tuingie wote ndani, nataka nikachukue simu yangu tu nimpigie huyo jamaa."
"Da! Itakuwa ngumu kidogo, unajua mimi nina haraka sana leo," alijitetea yule mtu ambaye kwa umbo ni bonge la mtu.

Nilijua ni uoga tu, hakuwa na kuwahi wala kuchelewa.
Alipopita, akatokea mwingine, mzee mmoja, kichwa chote kilichafuka kwa mvi. Nilimsalimia huku nikimwonesha ishara kwamba nataka kuzungumza naye.
"Mzee samahani sana."
"Bila samahani kijana."

Naye nikamsimulia tukio la siku ile, lakini wakati ananisikiliza, mara nilimwona anatupia macho dirishani na mimi nikageuka kuangalia, sikuona mtu.
"Umeona nini mzee wangu?"
"Nimeona msichana ananizomea."
"Kweli?"
"Ee. Ndiyo hayo mambo unayosema?"
"Ndiyo hayo mzee."

"Twende," alisema, nikaanza kutangulia mbele, mzee akanifuatia kwa nyuma. Hatukuwa tukiongea chochote, najua sababu. Kila mmoja alikuwa anaiwaza hatari ya mbele.
Tuliingia ndani, tukafika sebuleni, lakini sikuiona simu kwenye kochi.
"Ona sasa mzee, simu niliitupia hapa, lakini haipo."
"Au unayo mfukoni kijana?"

"Hapana, nina uhakika," nilisema huku nikijipapasa mifukoni, hakukuwa na simu.
"Nitajie namba nijaribu kuibipu," yule mzee aliniambia huku akitoa simu yake mfukoni. Nilimtajia namba zote, akawa anaziandika, kisha akapiga huku simu akiwa ameiweka kwenye sikio lake la kulia. Nilishtuka sana kusikia simu yangu

inaita kutokea kwenye chumba cha wale wapangaji wenzangu.
"Si hiyo?" yule mzee aliniambia akiniangalia kwa mshangao.
Mzee alikata kisha akapiga tena, ikaita tena kutokea kulekule, nilizidi kuogopa, nikamwambia tutoke lakini uzee kweli

dawa, aliniambia hakuna haja ya kutoka dawa ni kupambana tu.
Alinisogelea na kuniambia kwa sauti ya chini:
"Niwagongee mlango?"
"Si watakasirika?"

"Sasa kama unaogopa watakasirika, unadhani simu yako utaipataje?"
"Haya wagongee. Lakini subiri, kwa nini tusiende kwanza chumbani tukajua nani alikuwa anachungulia nje?"

"Kijana unaonekana muogamuoga sana, we mwanaume bwana, jifunze kukabiliana na hali kama hii, sawa?"
"Sawa mzee."
"Haya twende huko chumbani kwako unakotaka tukaone huyo msichana."
Tulifungua mlango wa chumbani, hakukuwa na mtu, ila shuka nililoliacha kitandani asubuhi silo, lilitandikwa jingine pia la kwangu.
"Khaa!" nilishangaa.
"Nini?"
"Hili shuka."
"Limefanyaje?"
"Silo nililolitandika asubuhi."
"Lakini la kwako?"
"Ndiyo langu."

Niliangalia mazingira mengine ya mle ndani na kubaini kwamba, kuna vitu vingi sana vilikuwa ndivyo sivyo.
"Si umeona hayupo?" yule mzee aliniuliza, nikamjibu ndiyo, akasema twende tukachukue simu yetu kwenye kile chumba ambacho ilikuwa inaita.

Moyo wangu ulikuwa mzito sana, nilihisi kizunguzungu, nilitamani kukaa chini na kumwomba yule mzee asichukue uamuzi wa kuifuata ile simu, lakini ningeipataje simu yangu wakati ina namba kibao?
"Kijana, ngoja nikuoneshe dawa moja ya hao viumbe wasiotaka kuonekana," alisema yule mzee, nikamuuliza ni ipi hiyo.
"Tulia wewe," alisema huku akiingiza mkono mfukoni na kutoa kimfuko kidogo, akakifungua akatoa kitu. Nilipomuuliza ni nini akajibu:
"Ni bangi."
"Sawa kabisa, hiyo ndiyo dawa, ngoja nikupe kiberiti."

Katika mambo yaliyonishangaza ni hilo, tulitafuta kiberiti chumbani hadi sebuleni lakini hakikuonekana, mbaya zaidi mimi nilikuwa na kawaida ya kununua viberiti bunda zima, lakini pia sikuona popote.

"Kweli una kiberiti ndani?" yule mzee aliniuliza.
"Kiberiti kipo na uzuri ni kwamba, nina bunda zima, pia silioni."
Nilimwona yule mzee akisimama wima na kunyoosha mikono juu kama mtu anayeomba dua kwa Mungu.
"Kijana nimejua sasa, ngoja kidogo," alisema huku akitoka na mimi nikimfuata kwa nyuma.

Wakati tunapita kwenye korido jirani na vyumba vile vya wenzangu, nikaisikia simu yangu ikiita.
"Mzee mzee, hiyo bwana," nilisema, mzee akasimama na mimi nikasimama nyuma yake, tukasikia sauti ya mwanaume ikipokea simu yangu:

"Haloo…Juma…Juma gani wewe? Nakuuliza Juma gani maana mimi ndiyo mwenye simu hii, huyo unayemsema simjui na wala hajawahi kumiliki simu hii," sauti ya kiume ilisema, ukapita ukimya kidogo kisha sauti hiyohiyo ikasema:
"Kama unabisha siyo simu yangu ongea na mke wangu huyu hapa."

Mara nikasikia:
"Haloo…ni kwa nini mnapenda sana kumfuatafuata mume wangu, mara mzungumzie bangi, mara mtusemee kwa watu."
Nilitamani sana kumwambia asiniache katika safari yake maana kwangu kwa muda ule palishaharibika, ningeuawa na watu wasioonekana.

"Wewe nisubiri kijana," mzee aliniambia akiendelea kwenda nje sikukubali.
"Mzee humu ndani mimi sikai, nimeshajua sasa."
"Umejua nini?"

"Huyo Juma anayetajwa hapo nafanya naye kazi na ilikuwa aje na bangi kwa ajili ya hawahawa watu wa humu ndani."
Mzee aliniangalia, akaniuliza:
"Wewe kijana unaye Mungu?"
"Ninaye."
"Huwa unakwenda kusali?"
"Sana."
"Lini umekwenda mara ya mwisho?"

"Ungeniambia tatizo ni kusali au?"
"Si hilo tu, ila una matatizo mengi. Hivi hapa tumesimama, nyuma yako nimemuona yule msichana amekuinamia akikung'ong'a kama mara tatu kwa harakaharaka."
Nilitimua mbio kuelekea kusikojulikana, nikaenda kufunga breki kwenye mtaa mmoja ambao ukienda kushoto kwangu

unakwenda kutokea kwenye barabara ya kwenda Kigogo Mbuyuni.
Baadhi ya watu walioniona nilivyo walitambua nina tatizo zito kichwani, mzee mmoja aliniuliza kama nakimbizwa nimefumaniwa.

"Sijafumaniwa mzee, lakini kwa tatizo langu afadhali ningefumaniwa."
Huyu mzee alikuwa amebeba kibegi kidogo mgongoni, alivaa suti nyeusi huku akionekana ni mzee mwenye heshima kubwa katika jamii inayomzunguka.

"Tatizo nini, hebu nisimulie kidogo tu," alisema huku akinivutia pembeni. Nilimsimulia kila kitu, alichokuwa akinishangaza sasa, kila hatua ya maelezo yangu alikuwa akiachia tabasamu hata pale nilipoamini kwamba ninachokisema kwa wakati huo asingetabasamu na uso wake ungeonesha kushtuka.

Nilipomaliza nikanyamaza na kumwangalia kwa woga, nilitaka kuamini ni yule mwanaume aliyepokea simu yangu kule nyumbani amenibadilikia ili nisiweze kumtambua.

Moyoni nilisema kuwa, kama kweli ni yeye atakapojidhihirisha tu kwangu nitoke mbio na kwenda kuingia kwenye nyumba

ya mtu yeyote mbele yangu.

"Tatizo ni hilo dogo tu?" aliniuliza.

"Ni hilo tu mzee wangu. Ukiweza kunisaidia nitashukuru sana."
"Nyumba yenyewe iko wapi?"
"Kule nyuma nyuma."

Nilimwona akiingiza mkono mfukoni na kuchomoa simu nyeusi ndogo, wengi wanaziita za tochi kisha akabonyezabonyeza na kuiweka sikioni. Moyoni nilisema yaleyale.
"Si ajabu anawasiliana na yule mwanamke wa kule nyumbani."
Nikamsikia akiuliza:
"Isdory, bado mpo hapo?"

Nadhani huyo jamaa alisema yupoyupo maana nilimsikia huyo mzee akisema: "Unaweza kuja na akina Tino hapa kwenye kibanda tulichotuma pesa asubuhi ya leo? Haya njooni."

Niligeuzageuza kichwa na kukiona kibanda cha kutuma pesa kwa kupitia mitandao mbalimbali ya simu. Nikajua amewaita watu waje pale.

Baada ya dakika kama tatu, wakafika watu kama saba, wanne wanawake, watatu wanaume akiwemo Isdory na Tino.
"Huyu bwana anaitwa," alianza kusema yule mzee akiniangalia nikajua anataka nijitambulishe jina mimi mwenyewe, nikafanya hivyo. Nilipomaliza, ndipo yule mzee akawaambia wenzake kisa chote cha kwangu, mwanzo hadi mwisho kama nilivyomsimulia awali.

"Ndugu, sisi wote walokole, kazi hiyo tunaimudu kwa vile mara nyingi huwa tunatumia jina la Bwana na Mwokozi wetu kufukuza uchafu kama huo, sasa itabidi utupeleke kwenye hiyo nyumba," alisema yule mzee.
Nilianza kutembea mimi na wao wakawa wananifuata kwa nyuma. Wale wanawake niliwasikia wakizungumzia mwanamke mmoja aliyeangushwa chini na mapepo akawa anataka kupigana na wale waliokuwa wakimwombea. Moyoni nikasema:
"Leo huko sijui."

Tulifika nje ya nyumba, kitendo cha kwanza ambacho si cha kawaida, nilimwona yule kijana muuza maji akitoka ndani. Alivaa kama siku alivyokuja nikamwingiza ndani."
Nilishtuka sana, yeye hakushtuka, ila aliponiona akaniambia:

"Bro nashukuru sana wamenilipa pesa zangu."
Sijui ni nini kilinipata nilijikuta nikisema sawa, sikuongeza neno jingine lolote lile.
"Ni humu waheshimiwa," niliwakaribisha wale watu nikiwa nimeshapishana na yule kijana.

Waliingia wote ndani, wakasimama katikati ya korido kisha wakawa wananiangalia, yule akaniuliza:

"Hivyo vyumba ni vipi?"

Sikumjibu kwa sauti, nilinyoosha mkono kuelekea kwenye vyumba vyote viwili. Vilioneshwa kufungwa kwa ndani lakini hakukuwa na sauti ya muziki wala maongezi yao.
"Baba katika jina la Yesu," yule mzee alianza ghafla.
"Amiiiin," walijibu wote aliofuatana nao, tena walijibu kwa sauti ya juu kisha wakatulia kimya.

Akaanza kusali akitaja maneno ya kutisha, nilimsikia akisema, choma moto roho mtakatifu, mara Malaika Michael shuka na panga likatalo kuwili.
Kifupi yule mzee alisema maneno ya ki-Mungu kwa jinsi nilivyoelewa mimi. Ikafika mahali akasema:
"Paaza sauti yako."

Ndipo wengine nao wakapokea kwa kila mmoja kuomba kivyake. Wengine walisikika wakisema wanaangusha na kuvunja ngome za ibilisi, wengine wanachoma moto makazi ya shetani, wengine wanamwagia damu ya Yesu pale ndani. Nilianza kuhisi amani iliyoje, niliamini ukombozi umefika tayari kwani sauti tu niliisikia ikipenya hadi kwenye mbavu zangu.

Waliomba sana, kuna wakati mimi nilihisi kuchoka lakini wao waliendelea tu hadi moyoni nikasema kweli ni watu wa Mungu.

Ghafla nilianza kuona moshi mweusi ukitoka chini ya milango yote ya wale ndugu, mlango wa sebuleni kama sikikosei na mlango wa chumbani. Moshi ulikuwa mzito kiasi kwamba, kuna wakati nilihisi kupaliwa na kukohoa kwa nguvu lakini wao hawakuonesha dalili ya kusumbuliwa na moshi huo.

Mara, milango yote miwili ikaanza kufunguka yenyewe polepole huku maombi yakiendelea kwa kasi na nguvu ya ajabu. Milango hiyo ilifunguka hadi ikafika mahali ndani kukaonekana.

Cha ajabu sasa, vyumba vilikuwa vyeupe, ndani yake hakukuwa na kitu chochote, hata karatasi. Ilikuwa kama chumba kilichopigwa deki au kufagiliwa kwa ajili ya maandalizi ya kuingia mkaaji mpya.

"Ha! Oneni jamani," nilijikuta nikisema hivyo. Nilibaini kwamba, wale watu hawakuona wakati milango inafunguka kwa vile walipokuwa wakiomba walifumba macho na walikuwa wakijipigapiga kwenye viganja kwa kutumia ngumi.

Yule mzee alipoona vile akasema:

"Katika jina la Yesu."
"Amiiin."

"Sasa tushushe uwepo wa Bwana mahali hapa, kwamba akapafanye pawe mahali salama, penye amani na utulivu wa hali ya juu, kila mmoja sasa amwombe Bwana hivyo."

Wakaanza kuomba tena, safari hii si kwa kukemea kama mwanzoni, ilikuwa sauti yenye upole na utii, mara nikasikia mlango mkubwa ukigongwa kwa nguvu.

"Ngo ngo ngo ngoo."
"Ingia," nilisema lakini huku nikienda mlangoni, nikaufungua! Mbele yangu alisimama yule dalali.
"Karibu bwana."
"Ee bwana nini umefanya sasa?" ndilo swali lake hata kabla ya salamu.
"Kwa nini?"

"We hujui umefanya nini? Si wako watu humo ndani, wamekuja kufanya nini hapa? Hujui kama kuna watu umewaumiza? Wewe ungefanyiwa hivyo ungekubali kweli?"
"Kaka unajua ukija kwangu njoo kwa heshima zako zote na hoja zenye msingi, usije kama mwendawazimu mpya, wewe unachokisema mimi sijakisema kwako? Ulichukua hatua gani wakati naumia mimi?"

Je, nini kiliendelea? Fuatilia -
SEHEMU YA 15https://www.jamiiforums.com/mahusia...ipanga-nyumba-moja-na-majini.html#post5395722
 
Back
Top Bottom