bioto
JF-Expert Member
- Oct 1, 2017
- 1,261
- 2,095
IMEANDIKWA NA : SANGO
KIPOZI
*********************************************************************************
Simulizi : Kibwe Katika Safari Ya
Ajabu
Sehemu Ya Kwanza (1)
MWANA MTEULE
Ukimya wa kutisha ulitawala eneo zima, na Kibwe akahisi woga wa ajabu ukimtambaa mwilini na kuzitawala fahamu zake zote. Alikuwa na kila sababu ya kutawaliwa na woga, kwani pamoja na kwamba hapakuwa na hata mtu mmoja pamoja naye, lakini vilevile hakukusikika kwenye msitu ule mlio hata wa ndege wala wadudu kama ilivyo kawaida.
Kimya kizito! Mara, sauti za ajabu zinasikika angani. Bundi na sauti za ndege wengine zisizopendeza masikioni zilivuma ghafla na kuzidi kumuongezea hofu Kibwe. Alipoangaza huku na kule, alishangaa sana kuona majabali na milima iliyotanda kila upande, bila kuwepo dalili ya mimea wala miti! Ardhi ya eneo lile ilikuwa imekauka na katika sehemu nyingi ilikuwa imepasukapasuka.
Kijana yule aliegemea mwambaulioelekea kwenye pango moja kubwa. Hivi naota…au ni kweli niko kwenye sehemu hii isiyoeleweka? Aliwaza huku akitetemeka kama mpapai uliopigwa na kibunga. Licha ya zile sauti za bundi na zisizopendeza masikioni za ndegewa ajabu, kwa muda wote wa saa kadhaa alizokuwa pale mahali, hakusikia sauti nyingine yoyote, hata ya upepo ukivuma, isipokuwa pumzi yake mwenyewe tu!
“Nimekusubiri kwa miaka mingi mno kijana, sikudhani kama siku hii ingefika.” Kibwe alipogeuka na kuangalia pangoni, alihisi ganzi kwenye miguu yake kwahofu! Moyo wake uliacha kudunda kwa sekunde chache, akatoa macho pima kutokana na kile alichokiona! Aka! Ni kitu gani hiki mbele yangu tena? Alijiuliza, huku fahamu zakezikimshauri atimua mbio kuelekea popote pale, alimuradi tu pawe mbali kabisa na mahala pale!
Kwa sekunde kadhaa, kile alichokuwa akikiona kilimfanya ashindwe kabisa hata huko kukimbia kwenyewe. Mbele ya
macho yake, kilisimama kitu kisichoeleweka, kama kijitu kidogo sana mithili ya mbilikimo, lakini udogo wake ulizidi ule wa
mbilikimo! Kilikuwa ni kijitu chenye uso ulioshupaa kama mzee wa miaka zaidi ya tisini.
Uso ule ulipambwa kwa msitu wa ndevu nyingi za mvi tupu zilizofika hadi magotini kwake! Kibwe alianza kukimbia lakini
ghafla, pale mahali alipokanyaga wakati akiruka kwa hofu, palianza kutitia na ardhi ikajiachia na kuporomoka pamoja naye! Wakati akiporomoka, alipoangalia chini kabisa, aliona uwazi usio na mwisho! Kwa hofu kubwa mno, aliachia ukelele wamfululizo, akihangaika kutafuta sehemu ya kukamata.
“Wooooooooooooooo…! Wooooooooooooa…….!” Kwa wepesi wa ajabu, yule mtu mdogo alinyoosha juu mkono wake na kuwahi kukamata mzizi uliokuwa ukining’inia juu yake. Alikunja miguu yake akijiandaa kubembea kwa kutumia mzizi
ule, akiazimia kujirusha kuelekea katika sehemu iliyokuwa imarakidogo. Alipofanya vile, alibembea huku akimchukua Kibwe pamoja naye kwa mkono wake wa pili, na wote wawili wakabembezwa na mzizi ule na kutupwa kwa mweleka mzito kiasi cha mita kumi hivi kutoka pale walipokuwa, wakiwa salama salimini ndani ya lile pango kubwa, lakini Kibwe akiwa ameshituka sana!
“Heeeeh! Ilikuwa kidogo niporomoke shimoni na kupotelea sijui wapi tu kule!” Kibwe aliropoka, akimshukuru Mungu kwa nusura aliyoipata. Alimtazama yule mtu mdogo wa ajabu, na kushangaa kuona jinsi alivyomnyakua kwa wepesi kama
mtu aliyechukua unyoya. Alitaka sana kujua alikuwa ni kiumbe wa aina gani yule!
Wakati wote ule wa pata shika, upepo mkali ulioambatana na dhoruba ulikuwa ukivuma, huku majabali yaliyotanda eneo lile yakiyumba na kutingishika vibaya. Ilikuwa ni hali ya kuogopesha mno kwa Kibwe. Kijana yule na mwenzake yule mwenye umbile dogo kama tumbiri, waliketi kwa muda wa kutosha pale mahali walipoangukia. Kile kijitu kilinyamaza kimya, kumpa nafasi Kibwe apumue kidogo, na Kibwe naye akanyamaza kimya, akijaribu kuelewa yule alikuwa ni nani, na ni kitu gani kilichokuwa kikiendelea pale, na kwa nini?
Baada ya nusu saa hivi, muda ambao kwa Kibwe ulionekana kama siku nzima, ile hekaheka ya maporomoko ilitoweka, na polepole upepo na dhoruba vikapunguza kasi yake. Alipoangalia nje ya pango lile kubwa, kwenye upeo wa macho
yake, akaona maajabu mengine. Katikati ya majabali makubwa na milima mirefu, aliona maumbile ya watu wakubwa mno! Aliinuka na kujaribu kutoka nje kidogo ya lile pango lililotitia bila kizuizi muda mchache uliopita, akitaka kuhakikisha kuwa ni kweli aliona kile alichokiona?
Ghafla alishikwa mkono na yule mtu mdogo aliyemrudisha nyuma kwa nguvu. “Chunga hatua zako kijana! Eneo lote hili linakabiliwa na uwazi mkubwa katika kila sehemu, na kama ulivyoona, inaweza kutokea hatari kubwa upande wetu. Kwa
sababu ya kuzuia hatari hiyo, ndiyo maana nikakuambia kuwa nimekusubiri wewe Kibwe kwa miaka mia moja!” Khah!
“Imekuwaje ukafahamu jina langu? Kwani wewe ni nani?” “Jina langu ni Bunga, na ni kiumbe pekee niliyebaki katikasehemu hii…” “Kiumbe pekee uliyebaki…??” “Naam. Nilibaki mimi na raia wachache tu, tulionusurika katika
nchi ya Sabaa miaka mia moja
iliyopita.” Kile kijitu kilichojinadi
kwa jina la Bunga kilimjibu, na
Kibwe akazidi kutoelewa.
“Mi..mi…mi sikuelewi we
babau!” Alimwambia.
“Huwezi kuelewa mpaka
ueleweshwe Kibwe. Hebu kaa
chini unisikilize basi…” Bunga
alimjibu, na KIbwe hakuwa na
namna ya kufanya vinginevyo.
Ndipo kibabu/kidudu Bunga
alipomsimulia za madhila
makubwa, akimuelezea habari za
nchi ya Sabaa ambayo ilikuwa ni
moja katika nchi za falme za
Kaskazini Mashariki ya dunia
zilizotawaliwa na wanawake
waliorithi falme za baba zao.
Alimwambia kuwa miaka mingi
nyuma, ikiwa chini utawala wa
Malkia Balika, nchi ya Sabaa na
jamii yake ya ‘Wanahewa’
iliteketezwa vibaya sana na jamii
yenye asili ya ‘Wanamoto’ kutoka
katika falme za majini, kwa
kutumia mioto iliyotokana na
pumzi zao.
“Kutokana na mashambulizi yao,
hakikubaki chochote katika
utajiri mkubwa wa nchi ya
Sabaa!” Alisema, akiongezea
kuwa siku hiyo ilikuwa ni siku
ambayo ‘Wanahewa’ waliandaa
hafla maalum ya kumtoa kijana
wao mteule na kumkabidhi kwa
mwalimu maalum ambaye ndiye
angemuelekeza kijana huyo jinsi
ya kutumia vipaji vyake vya
kipekee kwa faida ya jamii ya
sayari yao.
Bunga alikumbuka kuwa katika
baraza rasmi la Malkia Balika wa
Sabaa miaka hiyo mia moja
iliyopita, ulifanyika utabiri
kuhusu Mwana Mteule
aliyezaliwa nchini mwao. “
Atakapofikia umri wa miaka
kumi na nne, kijana huyu
mwenye vipaji maalum,
atakabidhiwa kwa mwalimu
ambaye atamwelekeza jinsi ya
kuvitumia vipaji hivyo kwa faida
ya jamii ya sayari hii, kwani yeye
ndiye mwokozi wa jamii zote
duniani...!” Mzee yule wa ajabu
alimwambia Kibwe kuwa tamko
lile lilitolewa na wazee
waheshimiwa, katika lile baraza
maalum la Malkia Balika.
“Walikuwa katika maandalizi ya
kutafuta mustakabala mwema wa
taifa lao.” Alisema.
“Ama! Sasa ikawaje tena?” Kibwe
aliuliza, akionekana kuvutiwa na
maelezo yale.
Bunga alimfafanulia kuwa kitu
kilichowaponza ‘Wanahewa’
miaka mia moja iliyopita ilikuwa
ni neema kubwa na mafanikio
yao ya ajabu yaliyotokana na
rasilimali yao ya kipekee ya vito
na madini, na pia vipaji vyao
adimu walivyojaaliwa.
“Katika miaka hiyo mia moja
iliyopita, nchini Sabaa alizaliwa
mwana wa kipekee mwenye
vipaji vingi vya ajabu na uwezo
mkubwa wa kimazingaombwe.
Kuwepo kwake katika sayari ile
ilikuwa ni kwa ajili ya kuinusuru
jamii yake katika sayari yake
pamoja na kuipa matumaini.
Utabiri wa wanataaluma
ulionesha kuwa kijana yule
angeelekezwa mbinu za
kumwezesha kuvitumia vipaji
vyake kwa ajili ya kuinusuru
jamii yake pindi atakapofikisha
umri wa miaka kumi na nne.
“Lakini looh! Hili halikutimia,
kwani chuki na inda za jamii ya
majini waovu dhidi ya jamii yake
vilitimia, na kijana yule
akateketezwa na moto katika
uvamizi ule wa wanamoto’,
uvamizi uliokusudiwa kumzuia
asitekeleze kazi muhimu
iliyomleta katika sayari ya dunia.
Kazi ya kuinusuru jamii ya
Sabaa!”
“Heh! Kwa nini ilikuwa hivyo
sasa?” Kibwe aliuliza kwa
hamaniko.
Kidudu Bunga alipiga kimya kwa
muda, kisha akamweleza Kibwe
chimbuko la uhasama
ulioiangukia nchi yake ya Sabaa.
Nchi iliyoneemeka. Nchi yenye
hewa safi pasina mfano. Nchi ya
wanahewa…
***
Miaka elfu mbili iliyopita huko
nyuma, nchi ya Sabaa ilineemeka
kwa kila fani – utajiri, maendeleo
makubwa na ustaarabu wa hali
ya juu, chini ya malikia wao
Balika. Sabaa ilitegemea zaidi
madini,vito pamoja na kilimo
kutokana na ardhi yake iliyokuwa
na rutuba, na hali ya hewa yake
mwanana. Baada ya uvamizi wa
Wanamoto ambao ni majini
wachokozi, raia wachache
waliobaki chini ya Malkia mpya
bibi Sultana, mdogo wake Malkia
Balika, walijitahidi kuijenga upya
nchi yao na kuanzisha utawala
mpya. Miongoni mwa mambo
waliyoyafanya ni kuanzisha
kanuni mpya za maendeleo, na
za kuendesha mambo yao kadhaa
wa kadhaa, na kuonesha kwa kila
hali ukomo wa ustaarabu
ulionawiri upya, alioufikisha
malkia wao huyo mpya. Hata
hivyo, kukosekana kwa ile neema
ya Mwana Mteule aliyehusudiwa
awali katika utawala ule tangu
miaka mia moja iliyopita,
kuliwapa Wanahewa majonzi na
masikitiko makubwa mno. Tukio
lile lilichelewesha sana
utekelezaji wa malengo bora ya
nchi ya Sabaa kwa ajili ya jamii
yake kote ulimwenguni kwa
kipindi cha miaka mia moja,
athari ambayo ilitabiriwa kuwa
ingejidhihirisha kwa dalili
mbalimbali katika sehemu nyingi
duniani!
“Kukosekana kwa kijana mteule,
kumeondoa matumaini miongoni
mwa jamii na kuzuia nusura si
kwa raia wa Sabaa pekee, bali pia
duniani kote.” Malkia Sultana
aliyerithi kiti cha Malkia Balika
aliwaambia wazee waheshimiwa
katika baraza lake la mashauri.
Alitoa wazo kwao kwamba ni
vizuri kuitisha mkusanyiko wa
raia wa Sabaa wakiwemo
wanataaluma ya nyota na
wanajimu, ili watabiri
mustakabala wa nchi yao pamoja
na dunia nzima, kuelewa ni
matatizo gani yatakayowakabili
katika sayari yao na jinsi gani
yanaweza kutatuliwa. Wazee
wale waheshimiwa ambao ni
washauri wa Malkia Sultana
katika utawala wake, waliafiki
mawazo yake, na ndipo
ulipoitishwa mkusanyiko wa raia
wote wa Sabaa katika uwanja
maalum. Uwanja ulifurika watu
waliokuwa na hamu ya kufahamu
hatima ya sayari yao. Wakati huo
sayari ya dunia ilikwishafikia
kiwango kikubwa cha nyuzi joto
ambacho haikuwa rahisi
kukipunguza, na kilikuwa
kikiongezeka kwa kasi kubwa.
Hali ile ilitishia mno maisha ya
viumbe wote duniani!
“Kwa hakika ingawa mwana
mteule aliteketezwa na moto kwa
njama za wale viumbe waovu
kwa nia ya kutuondolea
matumaini yetu, lakini hivi
tunavyozungumza umejitokeza
uwezekano mkubwa wa kupata
ufumbuzi utakaorejesha
matumaini kwa wanahewa wote
nchini Sabaa, na jamii nyingine
duniani.” Alitabiri mmoja kati ya
wanajimu waliohudhuria,
ambaye kwa maelezo yake hayo
hakuwatosheleza raia waliokuwa
na shauku ya kupata majawabu
ya maswali waliyokuwa
wakijiuliza. Malkia Sultana
alimwangalia mzee yule kwa
makini na kisha akamuuliza.
“Unaonaje ukitufichulia kuwa ni
matumaini gani hasa
yatakayopatikana, ili kila mmoja
wetu aondokane na wasiwasi
alionao hivi sasa?” Malkia yule
alihisi kuwa mnajimu kwa
makusudi kabisa, hakupenda
kufichua ukweli wa sababu za ule
utabiri, ambazo aliamini kuwa
zilikuwa ni nzuri tu, lakini hata
hivyo bado alitaka ufafanuzi wa
namna fulani, ili kurejesha imani
kwa raia wake, na kuwaweka
katika hali ya utulivu. Raia wote
nao waliafiki hoja za Malkia wao
na wote wakamkodolea macho
mnajimu yule, wakisubiri jibu
lake la kuridhisha, lakini kabla
yule mnajimu hajafungua mdomo
kusema lolote, kishindo kikubwa,
mithili ya kile kitolewacho na
gari moshi likichemka,
kilirindima eneo lote lile.
“Aaaa! Aaach-ch-chuuuuu!
Aaaa---aaaaach-ch-chuuuuu!”
Pale uwanjani vumbi lilitimka
kama kimbunga! CHANZO: https://
deusdeditmahunda.blogspot.com/
Jamii yote iliyohudhuria
mkusanyiko ule iligutuka na
kuruka kutoka vitini mwao. Vitu
vidogo vidogo vilivyokuwepo
katika eneo la mkusanyiko ule
kama vile mazulia, viti ambavyo
havikukaliwa, makaratasi na
vinginevyo, vilirushwarushwa na
kutawanywa huku na kule.
Hamadi!
Kumbe ilikuwa ni chafya moja ya
nguvu iliyotoka miongoni mwa
raia waliohudhuria mkusanyiko
ule. Kila mmoja alitaharuki na
kugeukia upande kilipotokea
kishindo kile, kushuhudia ni nini
hasa kilichotokea.
“Hayaaa! Hayaaaa! Jamani! hebu
tulieni kidogo! Tulieni jamani!
Bila shaka baadhi yenu
mnafahamu jinsi Mzee wa Busara
anavyokuwa kila anapokuwa na
mawazo mazito, kutokana na
matatizo ya aina hii.” Alisema
mmoja kati ya wazee
waheshimiwa.
“Mara nyingi anapofanya hivi
huwa na wazo muhimu la
kuchangia! Kwa hiyo ni bora
tutulie na tumsikilize kwa makini
ndugu zangu!” Mwingine
aliafikiana na yule mzee
muheshimiwa wa kwanza.
Naam. Mzee wa Busara alikuwa
amejirundika kama kifusi
pembeni kabisa ya ule uwanja!
Kwa haraka haraka mtu
angeweza kudhani kuwa ni
kilima kidogo kilichotokana na
takataka nyingi! Mzee yule wa
ajabu alianza kujigeuzageuza na
kunyoosha nyoosha shingo yake
ambayo awali haikuonekana.
Alikuwa kama mnyama mwenye
miguu minne na mkia mnene
kama wa mamba, na ngozi yake
ilikuwa na magamba kama ya
samaki, lakini zaidi yalionekana
kama ya mamba kwani yalikuwa
mapana mno!
“Aaaa—ch---chu---!” Alianza tena
Mzee wa Busara akiwapa wahaka
mkubwa wote waliokuwa
wakimwangalia. Alichukua nafasi
ile na kuanza kuelezea jambo
lake, wakati ambapo wote
waliohudhuria walikuwa makini
kabisa, wakidhani kuwa litatoka
chafya jingine babu kubwa
liwatimulie vumbi kama awali!
“Sisi---eh! Mhh-khuu! Sisi t-tun-
nafahamu kuw wa y-yapo mat-
tumaini ma-kubwa m-mbele-
yetu! Tusub-iri tu---aaach-ch-
mhhh!” Mzee wa busara
alijitahidi kuzuia chafya yake, ili
asiwavuruge raia waliokuwa
wakimsikiliza.
“Tuv-vute s-subira, maa n-na s-si
muda mr-refu t-tutapata maj-jibu
yatakayo turudishia imani na
matumaini, pamoja na nusura
tuliyoitegge—m-eaaaaaaa----c-h---
u….....!” alisema mzee yule wa
busara huku akizuia chafya zake
kwa taabu sana, akiwa pembeni
mwa uwanja na huku shingo
yake ndefu ikizunguka zunguka
kwa madaha kama shingo ya
twiga mtoto. Alimgeukia mtu
mmoja mdogo sana ambaye kimo
chake kilikuwa mithili ya kimo
cha ngedere. Mtu yule aligubikwa
na ndevu nyeupe tupu zenye
urefu wa kama mita thelathini
hivi, zilizoburuza hadi aridhini.
“Na matumaini hayo
yatadhihirika itakapokamilika
miaka mia moja kamili tangu
nchi hii ilipovamiwa na
kuteketezwa na majini wa
bahari.” Kijitu kile kidogo
kiliongezea taarifa katika maneno
ya Mzee wa Busara. Awali kabla
ya uvamizi wa nchi ya Sabaa,
kijitu kile ndicho kilichotarajiwa
kuwa mwalimu wa yule Mwana
Mteule aliyeteketezwa na moto
wa majini, katika siku ambayo
raia wa Sabaa waliazimia
kumkabidhi kwake.
“Kwa hiyo hakuna yeyote kati
yenu atakayekuwa na ufafanuzi
wa ufuatiliaji wa jambo
litakaloturudishia matumaini
yetu?” Alidadisi Malkia Sultana,
akiwaangalia wazee wake
waheshimiwa na watabiri wake
wa mambo waliohudhuria.
Mmoja kati ya wanajimu
aliyekuwa amejiinamia kwa
muda wote wa mkusanyiko ule
alisema; “Kwa hakika hatuwezi
kufafanua zaidi kwani
tutakapofanya hivyo tutavunja
mwiko, na hivyo kuweka ugumu
zaidi katika upatikanaji wa
ufumbuzi wa mambo
yanayohusika. Ila, tunachoweza
kusema ni kwamba maelekezo ya
dalili za madhara yanayoikabili
sayari yetu na jinsi ya
kukabiliana nayo, yameandikwa
katika moja ya vidani vya fedha
vyenye umbile la kucha za Simba,
kwenye mkufu unaoning’inia
shingoni mwa sanamu la shaba la
kichwa cha Simba, katika nchi ya
milima minne myeusi ya
maangamizi, kwenye uwanda wa
jabali la kisiwa cha Baharia!”
Raia wote waliohudhuria
waliduwaa!
Kwenye milima myeusi ya
maangamizi? Ndio wapi huko?!
Ukimya mkubwa ulitawala
uwanja ule wa mikutano, kila
mmoja akitafakari kuhusu taarifa
ile mpya ambayo kwa hakika
iliwakatisha tamaa zaidi, kwani
walihisi kuwa lile ndilo lililokuwa
jukumu la Mwana mteule,
ambaye walikwisha mpoteza!
***
Naam, Kibwe alimsikiliza Bunga
kwa makini sana, akijaribu
kuhusisha taarifa ile ya kidudu
Bungan a yale na maneno yake ya
awali, kwamba ‘alimsubiri yeye
kwa kipindi cha miaka mia moja’.
Hapo akasikia mikoromo ya
kutisha nje ya lile pango
walilokuwemo. Akakumbuka yale
majitu ya ajabu aliyoyaona kule
nje muda mchache uliopita.
Alizidi kuogopa.
“Yale…ni majitu gani kule nje?”
Kibwe alimuuliza yule mzee wa
ajabu, huku akioneshea na
akichungulia nje ya lile pango
kujaribu kuyaangalia majitu yale
aliyoyaona awali. Kama hapo
awali aliogopa, basi safari hii,
aliogopa maradufu, kwani baada
ya lile giza la vumbi nene
kutoweka, aliweza kuyaona vizuri
sana yale majitu ya ajabu! Miili
yao mikubwa kama milima
ilikuwa na vichwa vyenye
mapembe vilivyofanana na
vichwa vya ng’ombe! Halafu lo!
Mikono na miguu yao ilikuwa na
makucha marefu ya shaba!
Wakati akishangaa kwa kuhofu
namna ile, aliyaona yale majitu
yakipasua majabali na
kuchimbua milima. Huku
yakikenua meno yao makubwa ya
shaba yaliyong’ara mno kwa
mwanga wa jua, Kibwe
aliyashuhudia yale majitu
yakitafuna mawe bila kizuizi
kama kwamba yalikuwa
peremende! Miguu ilimwisha
nguvu, na kumfanya kijana yule
anyong’onyee taratibu na kurudi
chini, akiwa dhofu-l-hali kwa
hofu.
“Ama hakika leo ndio kifo
changu! Hakuna uwezekano wa
kunusurika hata kidogo hapa! Na
kama ninaota, mbona siamki
mpaka sasa? Laaa! Sijui
nitanusurika vipi mimi!” Aliwaza
kijana yule kwa hofu na wahaka.
Alimwangalia Bunga
aliyeonekana kuwa hana hofu
hata chembe, na kwa sauti ya
kutetemeka, akamuuliza kwa
mara nyingine, “Aaa...eeeh…
hivi…eeeh…. wale ni kina nani
babu….? Wametoka wapi…..na
kwa nini….wanafanya vile
wanavyofanya?”
“Wale kijana ndio wala mawe.
Kila mwaka kwa muda wa miaka
mia moja sasa, watu hao wa
ajabu wamekuwa wakitokea,
wakisindikizwa na upepo mkali,
vumbi, dhoruba na matetemeko
ya majabali. Wakifika tu, huanza
kuchimbua milima na mawe na
kupasua majabali, ili kujipatia
chakula chao. Watu hao wala
mawe wataendelea kufanya hivyo
hadi kuimaliza dunia yetu yote,
wakisababisha uwazi wenye kina
kirefu kisichokuwa na mwisho!”
Bunga alimwambia, na Kibwe
akaduwaa akiwa kinywa wazi.
Bunga alizidi kumkatisha tamaa
ya nusra pale alipomweleza kuwa
hata yeye anahofu kwamba
hatimae, hata ile sehemu ya ardhi
kwenye lile pango alikokuwa
anaishi kumsubiri, pia itatoweka
pamoja naye, na kuacha uwazi
kama sehemu nyingine katika
eneo lile, ambao uliwapoteza
viumbe wengine wengi kabla
yake.
“Oooh! Haponi mtu hapa!” Kibwe
alijisemea kwa sauti huku
akijishika kichwa kwa kukata
tamaa.
“Wewe pekee ndiye
utakayesaidia kuzuia hali hii
isiendelee na labda kuirudisha
vile ilivyokuwa awali Kibwe,
kwani wewe bado ni damu
changa, hujaanza kufikia umri wa
kukata tamaa.” Bunga
alimwambia, na Kibwe
akamshangaa. Hakujiona yeye
akimuokoa yeyote kutokana na
maangamizi ya ile mijitu
inayokula mawe, lakini pia
alishangaa kwani hakuona
uhusiano baina ya kuiokoa dunia
na ule uwazi ulioikabili. Vyote
kwa vyote, hakuelewa ni vipi
yeye angeweza kuzuia ile hali ya
hatari isitokee, hasusan
akizingatia kuwa waliohatarisha
hali ile ya dunia walikuwa ni
majitu makubwa mno kwa yeye
kuyadhibiti!
Kama vile aliyekuwa akiyasoma
mawazo yake, Bunga aliendelea
kumwelezea hatua zipi achukue,
ili kuinusuru dunia.
“Wewe ndiye mteule mwenye
jukumu hilo Kibwe, pamoja na
mengine ya kuitahadharisha jamii
na kuiokoa dunia na ukame, na
uwazi ulioikabili. Hiyo ni pamoja
na matatizo ya kiafya na vifo vya
binaadamu na viumbe wengine,
na pia kuinusuru dunia na uovu
na uadui miongoni mwao,
pamoja na kuwajengea imani na
matumaini...”
“Khah! Mimi?”
“Wewe, Kibwe! Kwa hiyo, ili
ufanikishe kazi hiyo, lazima
ufanye safari ndefu na yenye
mitihani mikubwa. Safari hiyo
ndiyo itakupatia ufumbuzi wa
jambo hilo. Kwa vyovyote vile,
usikubali kabisa kukata tamaa
kwa jambo lolote litakalotokea,
kwani utakapokata tamaa, azma
yako haitatimia.” Bunga
alisisitiza, mara kwa mara
akikunja uso wake uliokomaa na
uliopambwa na zile ndevu zake
nyingi za mvi.
“Lakini bado sijaelewa jinsi
nitakavyotimiza azma hiyo babu!
Na hiyo safari nitakayoifanya ni
kuelekea wapi baada ya kutoka
hapa?” Kibwe alihoji, yote yale
yakiwa ni mazito kwake.
Maelekezo ya Bunga kuhusu
safari yake yalizidi kumtia hofu,
kwani yalimdhihirishia kuwa
hakika safari ile ingekuwa ngumu
mno na isiyo ya kawaida.
“Mara baada ya kuondoka wale
wala mawe, takriban nusu saa
kuanzia sasa, utaelekea
magharibi ya dunia hadi ufike
mahali kunakokuchwa jua, katika
makutano ya mbingu na ardhi,
ambapo jua huonekana kama
kwamba linazamia hapo. Kwenye
ufukwe wa bahari utaona
mtumbwi. Tumia mtumbwi ule
kwa safari yako ya kuelekea
kisiwa cha mazimwi, viumbe
ambao nusu;yaani kuanzia
kuanzia tumboni kwenda
miguuni ni wanyama, na kuanzia
tumboni kwenda kichwani ni
wanadamu. Katika kisiwa hicho
utakuta ngome moja imara, na
ndani ya ngome hiyo, huishi hao
mazimwi ambao hulinda upanga
wa radi. Jitahidi uupate upanga
huo ili ukusaidie katika
mapambano ya kuzuia vitendo
vitakavyozidi kueneza uwazi
mkubwa katika dunia hii.
Utakapofanikiwa kuupata upanga
wa radi na kuondoka katika
kisiwa cha mazimwi salama
salimini, utaelekea katika nchi ya
Azarbajan iliyoko kaskazini ya
mbali ya dunia, baina ya milima
miwili mirefu sana. Ili kuupata
upanga wa radi kwenye kisiwa
cha mazimwi, lazima uwe
mwangalifu mno, uhakikishe
kuwa unaingia kwenye ngome
yao wakati ukiwa na hakika
kuwa wote wamelala usingizi
kwani….”
“Sasa, nitahakikisha vipi kwamba
mazimwi hao wamelala ili niweze
kuingia kwenye hiyo ngome?”
Kibwe alimkatisha kwa
mshangao. CHANZO: https://
deusdeditmahunda.blogspot.com/
“Utakapo sikia kelele nyingi na
zogo kutoka ndani ya ngome
kama vile unazomewa na kundi
kubwa la watu, hapo ndio
utaanza kuingia ndani polepole,
na utakapofika ngomeni,
utawakuta mazimwi hao
wamelala sesa; fo-fo-fo! Humo
ngomeni utaona mnara wa
dhahabu, na juu ya mnara huo
wa kipekee, utauona upanga wa
radi uliowekwa nje ya ala yake na
unang’ara kama jua.” Bunga
alitoa maelekezo yale
yaliyomshangaza mno Kibwe,
aliyestaajabu sana kusikia kuwa
eti zinaposikika kelele nyingi za
mazimwi, ndio ishara kuwa
wamelala! Alijiuliza sana moyoni
mwake kama mambo yote yale
aliyokuwa akisikia yalikuwa
katika ndoto, au kweli yalikuwa
alivyokuwa akiyasikia!
Wakati Kibwe anahoji uhakika
wa mambo mengi yaliyomtokea
katika kipindi kifupipale kwenye
ule mji wa wala mawe, alimsikia
tena Bunga akisema; “Ingawa
utafaulu kuwakimbia mazimwi
wa ngomeni, hutaweza kuvuka
mpaka wa nchi hiyo ili kuendelea
na safari yako, kwani njiani
utazuwiliwa na kiongozi wa
mazimwi hao, zimwi ‘Nyalile’
mwenye jicho moja. Kwa bahati
nzuri icho hilo moja la zimwi
‘Nyalile’ halioni vizuri. Na kama
atajaribu kukuzuia usipite, lazima
umuimbie wimbo mzuri
utakaomvutia na kumlaghai, ili
asiweze kujua kama wewe ni
mwanaadamu!” Lo! Hapo Kibwe
akazidi kuhofu, na kuzidi
kumaizi kuwa kazi iliyokuwa
mbele yake, kamwe haikuwa
rahisi! Aliogopa sana kusikia
maelezo ya Bunga, na akakosa
imani kabisa ya kuendelea na
jukumu lile la kuiokoa dunia
isikumbwe na janga la uwazi
ulioikabili, pamoja na majanga
mengine.
Bunga alifahamu wahaka na
taharuki ya Kibwe baada ya
kumpa maelezo ya jinsi safari
yake itakavyokuwa, hivyo akazidi
kumpa moyo akiongea naye kwa
upole, na kumuhakikishia kuwa
hatapata tatizo lolote katika safari
hiyo, kama atatumia busara na
kufuata maelekezo yake.
“Nimekuambia tokea mwanzo
kuwa wewe ndiwe mteule wa
jukumu hilo, kwa hiyo kabla
hujaondoka kuelekea kwenye
safari hii ya aina yake, nitakupa
silaha mbalimbali, ambazo
utazitumia kadiri inavyostahili.”
Baada ya kusema hivyo, Bunga
alijisogeza ndani ya pango lake
na kutoa mfuko mmoja mkubwa
wa gunia na kumkabidhi Kibwe.
“Humu ndani kuna silaha nyingi
utakazozitumia utapozihitaji……”
Bunga alizitoa zile silaha moja
baada ya nyingine, akielezea kazi
zake taratibu na kwa makini,
Kibwe alisikiliza maelezo hayo
kwa umakini mkubwa. Bunga
akamuuliza iwapo ameelewa
maelekezo yote. Kibwe akaafiki
kuwa ameelewa.
“Haya kijana, hebu fumba macho
kidogo….” Hatimaye Bunga
alimuamuru, na Kibwe akafanya
alivyoambiwa. Wakati macho
yake yakiwa yamefumba, alihisi
mtikisiko na akasikia mvumo
ulioambatana na mtikisiko ule
mithili ya mtu aliyekuwa kwenye
gari moshi. Naam, hapo ndipo
ilipoanza safari ndefu na ya ajabu
ya Kibwe. Alipofumbua macho
kuelewa ni jambo gani lililokuwa
likiendelea, alijikuta ufukweni,
na mbele yake ulikuwepo
mtumbwi!!
***
Kibwe aliendelea na safari ile
kama alivyoelekezwa na Bunga.
Kwa muda mrefu mno aliendesha
mtumbwi alioukuta ufukweni,
hadi akachoka sana na kuanza
kusinzia kwa uchovu.
Alipokaribia kile kisiwa cha
mazimwi, Kibwe alianza kusikia
sauti nyororo na nzuri zikiimba
wimbo ulioburudisha kupita
kiasi! Alipotupia macho mbele
kabisa ya kisiwa, akawaona
mabinti saba wazuri, waliovalia
mavazi ya hariri yaliyometameta
juani, na waliovutia kupita kiasi.
Lakini zaidi ya uzuri wao, sauti
zao ndizo zilizomvutia Kibwe
zaidi. Alitega sikio na kusikiliza
kwa makini. Lo! Sauti zilikuwa si
za kawaida! Kibwe akazidi
kusinzia kwa burudani ilepamoja
na uchovu aliokuwa nao. Mara
akakumbuka maneno ya Bunga!
“Karibu na kisiwa cha mazimwi,
kuna mabinti saba laghai wenye
sauti nyororo za
kimazingaombwe. Ukizisikiliza
sauti zao nzuri kwa mfululizo,
lazima utawafuata walipo, na
ukifika kule watakuwekea ulozi
kwenye kinywaji chako na
kukufanya usahau kabisa
kutekeleza malengo yako!
“Kwa hiyo nitafanyaje kujinusuru
na ulaghai wao?” Kibwe aliuliza
“Utachukua hii ‘nta’ na kuziba
masikio yako ili usiweze kuzisikia
sauti zao.”
Haa! Sijui kwa nini Kibwe alitaka
kusahau jambo lile muhimu
kabisa. Haraka akatoa ile ‘nta
aliyowekewa kwenye mfuko wa
gunia na kuyaziba barabara
masikio yake, kisha akaendelea
na safari yake kwa amani hadi
alipofika kisiwa cha mazimwi.
Kibwe alianza kuangalia huku na
huko akitafuta sehemu ya kivuli
aweze kupumzika kabla ya
kuanza kutekeleza ile kazi
iliyompeleka kule. Alipata
sehemu yenye mti wenye matawi
marefu sana yaliyokuwa
yakiburuza hadi chini, na hapo
akaketi na kutumia yale matawi
kwa kujificha, ili asionekane.
Baada ya kunywa maji
aliyowekewa na Bunga kwenye
ule mfuko mkubwa wa gunia,
Kibwe alipata lepe zuri la
usingizi, kutokana na upepo
mwanana uliopuliza sehemu ile.
Alilala kwa muda mrefu
akapumzika vya kutosha, ili
apate nguvu ya kuanza kuelekea
kwenye ngome ya mazimwi,
kuchukua upanga wa radi, kama
alivyoelekezwa na Bunga.
Baada ya mapumziko yake, Kibwe
alianza ufuatiliaji wa kazi
iliyompeleka kule. Alikumbuka
maneno ya Bunga. “Itakubidi
kwanza uende kwenye mlima
ambao chini yake kuna shamba
kubwa la ufuta.” Alifahamishwa
kuwa sehemu ile ilikuwa karibu
na makazi ya wale mazimwi
hatari wafuasi wa Zimwi
mkubwa aliyeitwa ‘Nyalile’ na
ambao kwa pamoja, wakati fulani
waliwateketeza wakazi wa kisiwa
hicho kwa kuwatafuna. “Lazima
upande mlima huo hadi kileleni,
na huko utakuta jumba
wanamoishi mazimwi hao,
lililozungushiwa ngome
madhubuti.” Aliambiwa kuwa
lazima akachukue upanga wa radi
unaotoa cheche za moto kila
unapotumiwa, na kumpa ushindi
yule anaye utumia. Aliambiwa
kuwa ile ndiyo silaha pekee
ambayo ingemsaidia kupambana
na mitihani mikubwa iliyokuwa
mbele yake, akiendelea na safari
yake kuelekea matokeo ya jua,
baina ya mashariki na magharibi.
Kibwe alipita kwenye shamba
kubwa la ufuta na kuanza safari
yake ngumu ya kupanda mlima
akielekea kileleni kwenye jumba
la mazimwi. Katika jitihada zake
hizo, mara kwa mara kijana yule
aliteleza na kuporomoka, lakini
alizidi kuupanda mlima bila
kuchoka wala kukata tamaa.
Mchana kutwa Kibwe aliendelea
na safari ile ya kupanda mlima,
na ilimchukua takriban siku mbili
njiani akila matunda ya porini
kujinusuru na njaa. Kila
alipokutana na wanyama wakali
kama simba, chui , faru, mbogo
na wengine, Kibwe aliwakwepa
kwa kujificha vichakani. Hadi
kufikia saa kumi jioni siku ya tatu
jua lilipoanza kuchwa, kijana yule
aliona ngome ndefu mno,
iliyosimama kwenye upeo wa
macho yake katikati ya msitu!
Taratibu, huku akiangalia huku
na kule, Kibwe alisogea karibu na
ngome ile. Alipokaribia zaidi
alistushwa na kelele na zogo
kutoka ndani ya ngome ile
madhubuti! “Huyooooo! Anakuja
kuchukua upanga wetu! Haraka
mkamateni! Mfuateni mumlete
haraka kabla hajaingia ndani!
Hayaaa! Kamataaa! Chinjaaaa!
Uwaaaa! Nyongaa!” La haulaa!
Kibwe alianza kukimbia kwa hofu
ya kukamatwa na kutafunwa na
mazimwi wale hatari, na kusahau
kabisa usia aliopewa na Bunga!
“Utakapo sikia kelele nyingi na
zogo kutoka ndani ya ngome
kama vile unazomewa na kundi
kubwa la watu, hapo ndipo
utaanza kuingia ndani polepole,
na utakapofika ngomeni
utawakuta mazimwi hao
wamelala sesa, fo-fo-fo !
Kutakapokuwa kimya basi
tahadhari sana, kwani mazimwi
hao watakuwa wako macho!”
Hilo lilikuwa ni onyo la Bunga
kwa Kibwe.
Haa! Ilikuwaje akasahau jambo
jingine muhimu kama lile?
Hamadi! Palepale alipokumbuka
onyo lile na taarifa ya Bunga
kuhusu maajabu ya wale
mazimwi, Kibwe aligeuka na
kupiga mbio kuelekea kule
ngomeni. Alipofika langoni huku
akipumua kwa kasi, Kibwe
alichunguli ndani kwa uangalifu
na umakini mkubwa kuona kama
wale mazimwi walikuwa
wamelala. Hakuona dalili ya mtu
au kitu chochote katika upeo wa
macho yake. Taratibu aliingia
ndani akinyata polepole na
alipoangalia mbele zaidi, akaona
eneo kubwa la wazi lenye bustani
nzuri ya maua. Aliambaa na
ukuta, huku polepole akinyanyua
mguu mmoja mmoja, akishikilia
pumzi yake kwa hofu ya kusikika
na madude yale hatari
aliyoambiwa na Bunga. Mwisho
kabisa wa eneo lile la wazi,
Kibwe aliona lango jingine kubwa
lenye mbao za marembo
marembo. Alinyata taratibu na
alipogundua kuwa lango lile
lilikuwa wazi, alilisukuma na
kuchungulia uwani. Hamadi!
Kibwe hakuamini macho yake
kwa kile alichokiona! CHANZO:
https://
deusdeditmahunda.blogspot.com/
Macho ya kijana yule yalikutana
na kundi zima la madude
makubwa kupita kiasi yaliyokuwa
nusu ni watu, yaani kutoka
tumboni kwenda kichwani na
nusu, katika sehemu ya tumboni
kwenda miguuni walikuwa kama
sokwe! Kundi lile la madude yale
ya ajabu na ya kutisha, lililala
sesa kwenye nyasi za eneo lile, na
huku kelele zao za kuzomea
zikiendelea! Wakati sauti zao
zikimbabaisha Kibwe, miili yao
ilimtisha sana kwani ilikuwa na
manyoya marefu kupita kiasi
yakiburuza hadi chini kama
ufagio! Viumbe wale walikuwa
na midomo iliyojaa meno yenye
ukubwa mithili ya pembe za
ndovu! “Lo….. ndiyo maana
ilikuwa rahisi sana kwa madude
haya kuwatafuna na
kuwateketeza mara moja watu
wa kisiwa chote hiki, kutokana
na urefu na wingi wa meno yao
makali!” Kibwe aliwaza, akiwa na
woga na wahaka mkubwa usio
mfano.
Haraka Kibwe alifuata yale
maelekezo ya Bunga, akianza
kuwatambuka taratibu wale
mazimwi waliolala huku
wakipiga kelele na kuzomea
kama kwamba walikuwa macho,
hali iliyomfanya Kibwe azidi
kuhofu, kwani muda wote alihisi
kuwa huenda ghafla wakamrukia
na kumshambulia. Hiyo Ilikuwa
ni kazi ngumu mno kwa kijana
yule na muda wote wa zoezi lile,
jasho lilikuwa likimtiririka na
mara nyingine alihofu kuwa
huenda jasho lile likawadondokea
na kuwaamsha wale mazimwi, na
huo ukawa ndio mwisho wake!
MAJANGA YA SAYARI
Wakati Kibwe akiwa katika
jitihada za kutekeleza malengo
yake ya kuinusuru jamii kule
machweo ya jua katika kisiwa cha
mazimwi, katika sehemu
nyingine iliyo baina ya mashariki
na magharibi mbali kabisa
kutoka kisiwa kile cha mazimwi,
katika milki ya Sultani Bashar,
majini yalitawala sehemu kuu
iliyowapatia maji raia wa nchi ya
Shamsi mjini Majabali. Jambo
hilo lilisababisha shida kubwa ya
maji na ukame uliathiri maeneo
mengi ya nchi ile, iliyokosa
chakula cha kutosha kwa watu
wake. Ili kuwanusuru raia wake
na shida ile ya maji, kila mwaka
Sultani Bashar wa nchi ya Shamsi,
alimtoa kafara binti yake kwa
joka moja kubwa ambalo
lilimchukua binti yule na kuzama
naye kwenye mto Sakara ulioko
kati ya majabali mawili na
kumpeleka kwa jini ‘Makattani,’
mfalme wa majini yote. Mpaka
kufikia wakati ule Kibwe
alipokwenda kisiwa cha
mazimwi, tayari Sultani Bashar
wa nchini Shamsi alikwisha
watoa kafara watoto wake sita,
binti mmoja kila mwaka na kila
mara akiwapatia raia wake
mwaka mmoja wa kuchota maji
kutoka mto Sakara. Hatimae
Sultani yule alibaki na binti
mmoja tu, Bhaduri binti sultani
ambaye kwa bahati mbaya
kwake, alitakiwa kumtoa kafara
wiki mbili zilizofuata kwenye mto
uleule Sakara, ili kuwapatia raia
wake mwaka mmoja zaidi wa
kutumia maji yake!
“Ama kweli hali hii ni ya
kusikitisha na kusononesha
mno,” Malkia wa Shamsi
amlalamikia mumewe Mfalme
Bashar, huku akilia bila kizuizi!
“Haya ni maonezi makubwa na
ni unyanyasaji wa aina yake, wa
kuwalazimisha mabinti zetu
wajitowe mhanga, eti kwa ajili ya
kunusuru raia wako! Hili si
jambo la kibinaadamu hata
kidogo.” Malkia yule alisema kwa
masikitiko makubwa. “Sasa mke
wangu unadhani tungefanya nini
kulitatua tatizo hili sugu
linalotukabili kila mwaka?”
Sultani Bashar alimuuliza mkewe
kwa upole.” Hata mimi nina
majonzi makubwa kuhusu
mabinti zetu, lakini hii ndiyo njia
pekee ya suluhu kwa jambo hili.”
Katika mji ule mkuu wa Majabali
nchini Shamsi, baada ya Suitani
kufanya maandalizi ya
kumpeleka kitindamimba wake
Bhaduri kule mtoni Sakara kwa
ajili ya kafara, aliketi kwenye kiti
chake cha enzi na kujiinamia kwa
fikira na majonzi ya kumpoteza
binti yake mwengine! Ama kweli
Sultani yule alikuwa mtawala wa
aina yake! Eti kudiriki kuwatoa
kafara mabinti zake saba! Si
jambo la kawaida asilani!
Kule Azarbajan nako kwa Sultani
Kash Kash kaskazini ya mbali ya
dunia, ingawa chini kabisa ya
bahari, i jini ‘Makatta’na
wenzake walikuwa wakiandaa
vichafuzi vya hewa safi
iliyowasaidia watu kuishi, na
kuigeuza hewa ile kuwa
hatarishi, lakini Mfalme wa nchi
ile hakutambua hivyo. Hakujua
kama hewa ile iliyogeuka kuwa
moshi mnene ilipoanza kuzizima
na kisha kuwazingira watu katika
himaya yake, ndipo walipogeuka
kuwa mawe ya theluji! Kwa kuwa
hawakuelewa chanzo hasa cha
janga lile, watu wote wa kule
waliingia hofu kubwa na Mfalme
wao alikuwa akimtafuta
mkombozi atakaye wanusuru raia
wake kutokana na janga lile!
“La mgambo! La mgamboooo!
Likilia lina jamboo! Asiye mwana
a eleke jiwee!” Kijumbe wa
Mfalme Kash Kash alipita mitaani
akiwatangazia raia wa Azarbajan
kama kawaida wakati inapotokea
dharura ama ya raha, au ya
karaha, akianza kwa kupiga goma
lake kubwa alilolibeba kifuani, na
lililofungwa kwa kamba iliyopita
mabegani na kuzungukia
makwapani.
Kwa kupiga ile ngoma kijumbe
yule aliwavutia watu na
kuwasogeza karibu, ili waende
kumsikiliza. “Jamani eeeh!
Kuhusu janga linalotukabili la
raia wengi kugeuka mawe ya
theluji, mpaka hivi sasa bado
haujapatikana ufumbuzi wa
tatizo hilo, na wala bado
hajapatikana mkombozi atakaye
saidia kunusuru maisha ya raia
wa nchi hii. Hivi sasa wazee wa
baraza la Mfalme, wako mbioni
kutafuta njia ya haraka ya
ufumbuzi wa tatizo hilo. Kwa
hiyo yeyote atakaye kuwa na
mawazo tafadhali asisite
kujitokeza na kuchangia, ili
kulipiga vita janga hili la
kihistoria nchini kwetu…..! La
mgambooooo! La mgambooooo!
Likilia lina jamboooooo!”
Kijumbe yule alihitimisha
tangazo lake na kisha kuendelea
katika maeneo mengine ya mji
wao mkuu. Tangazo lile
lilitangazwa mara kwa mara
katika miji mbalimbali ya
Azarbajan, lakini hakujitokeza
mtu yeyote aliyeweza kutoa
ushauri kuhusu utatuzi wa tatizo
lile.
Katika ngome ya jumba la
mazimwi kwenye kisiwa chao,
Kibwe alitumia muda ule ambao
mazimwi wale walikuwa
wakipiga kelele, kwa kuendelea
kuwatambuka mmoja mmoja,
hadi alipofika kwenye ule mnara
wa dhahabu. Pale alipumua
kidogo kabla ya kuanza kupanda
mnara huo ambao juu yake
ulikuwepo upanga wa radi
alioutaka. Kelele za mazimwi
zilizidi kuliko awali, kama
kwamba walihisi kuwa kuna mtu
karibu ya hazina yao.
“Naomba Mungu majitu haya
yasiamke ama sivyo sitanusurika
asilani!” Kibwe aliwaza.
Alikumbuka kuwa mara tu, kelele
zitakapokoma, ndio utakuwa
wakati wa hatari kubwa kwake!
“Na kutakapokuwa kimya basi
tahadhari kwani watakuwa wako
macho!” Bunga alimwambia.
Ingawa aliogopa sana na kuhofu,
lakini kijana yule shujaa alipanda
juu ya ule mnara mrefu akafika
kileleni, na kwa uangalifu
akauchukua ule upanga na kuutia
kwenye ala yake, na kisha
akaupachika kiunoni kwake na
kuanza kuteremka chini kwa
uangalifu! Alipofika chini,
akarudia lile zoezi la wasiwasi la
kuyatambuka yale mazimwi
yaliyolala! Lo! Kwa bahati mbaya,
alipokuwa akimalizia zoezi hilo,
alilikanyaga zimwi la mwisho
lililolala karibu na lango kuu la
kutoka ngomeni, na hivyo,
lilipokuwa kimya tu, kwa ishara
ya kuamka, na menzake yote
yakawa kimya! Masikini wee!
Mazimwi yote yakawa macho!
Kabla hayajataharuki na
kugundua kuwa alikuwepo mtu
ngomeni mwao na amechomoka
na kupenyeza getini wakati
mmoja wao akiamka, Kibwe
alipiga mbio kama mshale!
Alikimbia kuelekea mpakani
mwa nchi ile kama alivyoambiwa
na Bunga, akiazimia kupita katika
njia kati ya mashariki na
magharibi!
Walipoangalia mnarani na kukuta
upanga wa radi umetoweka,
mazimwi wote walitaharuki na
kuwa na hasira nyingi “Bila shaka
alikuwepo mtu humu ngomeni.
Afuatwe haraka kabla
hajaondoka na upanga wetu!”
Baada ya kusema hivyo, wote
walitimua mbio, huku vumbi
likitanda kwa heka heka hiyo, na
baadhi ya miti ikikatika kwa
vikumbo vyao! Alipoangalia
nyuma, kibwe aliona vumbi
lililotanda hadi mawinguni! “Leo
ndio hatima yangu mimi! Sijui
kwa nini nilifika huku!” Kibwe
alisema kwa majuto. Mazimwi
yalipoanza kumkaribia alihisi
miguu yake ikiwa inalegea mno
na kukosa nguvu kwa hofu! Moyo
wake ulienda kwa kasi mno!
Alikumbuka maneno ya Bunga.
“Wakikaribia kukufikia, watupie
kichupa kimoja kati ya vichupa
hivi vidogo vya mazingaombwe,
ili uwacheleweshe.” Kibwe
haraka alitoa kichupa kimoja na
kukitupia nyuma yake kwa yale
mazimwi. Lo! Mara ukatokea
msitu mnene kupita kiasi.
Mazimwi yalianza kuhangaika
kukata miti ya msitu ule uliozuka!
Kutokana na ukubwa wao, muda
si mrefu yalifaulu kukanyaga
kanyaga miti midogo na kuipiga
vikumbo miti mikubwa, na kisha
kuendelea kumkimbiza Kibwe,
ambaye alipoona hivyo, alirusha
kichupa cha pili, na mara
zikazuka mbigili nyingi mno
nyuma yake! Mazimwi
yaliumiaumia miguu yao, na
wengi wakaachwa nyuma. Kibwe
aliyaona baadhi ya mazimwi
yakizidi kumfuata, huku yeye
akiwa amechoka mno kukimbia.
Alipatwa na wasiwasi mkubwa,
“Sasa nikishindwa kukimbia na
madude hayo yanazidi kunifuata,
itakuwaje?” alijiuliza huku
akipapasa papasa kwenye fuko
lake, kutoa kichupa kingine
miongoni mwa vichupa
alivyopewa na Bunga. CHANZO:
https://
deusdeditmahunda.blogspot.com/
“Kwa kuwa mazimwi hupenda
sana kula ufuta, utakapo watupia
kichupa cha ufuta, wote wataketi
chini na kuanza kula, na hivyo
utapata nafasi ya kuwakimbia.”
Kibwe alikumbuka maneno hayo
ya Bunga! Mara moja akarusha
kichupa cha ufuta, na hapohapo
ukazuka mlima mkubwa wa
ufuta, na kuwafanya mazimwi
wote kuchanganyikiwa kwa
uchu! ”Aaaaa! Ufutaaaa! Ufuta
mtamuuuu! Nakula ufutaaa!”
Wakawa wanajisemesha maneno
hayo, kila mmoja akifurahia
chakula kile akipendacho, na
kumsahau kabisa Kibwe na
upanga wa radi! Waliketi chini na
kuanza kuushambulia ufuta!
Kibwe naye aliongeza kasi ya
mbio zake, akiruka mabonde na
kuangukia kwenye makorongo na
mito, misitu na nyika hadi
kwenye mpaka kuelekea
kaskazini ya mbali, kulikozizima
baridi ya ajabu, iliyowagandisha
watu na kuwageuza mawe! Pale
mpakani alisimama ghafla
akitahamaki na kuona moshi
mwingi uliotanda mbele yake, na
umbile la dude kubwa
lililofichwa na giza la moshi huo,
likiashiria kuwepo kwa jitu
kubwa likishughulika chini ya mti
mkubwa kupita kiasi! Muda wote
aliokuwa akiwakimbia wale
mazimwi, alimsahau kabisa
kiongozi wao, aliyeitwa Nyalile!
Kibwe alitaka kufahamu ule
moshi uliotanda vile ulitokana na
nini. Huku akihofu, lakini kwa
moyo wa kishujaa, taratibu
alisogea kule kulikotoka moshi
ule, akiangalia huku na kule kwa
wasiwasi hadi akafika karibu
kabisa na sehemu ile. Aliona
kuwa ule moshi ulitokea bondeni,
wakati yeye akiwa juu kidogo
kwenye uwanda. Aliposogea na
kukodoa macho yake vizuri ili
aweze kuona kama kwenye ule
utando wa moshi kulikuwa na
nini, alihisi kama vile anaangalia
umbile kubwa sana la jitu la
miraba minne, likishugulika
kufanya kazi fulani. Alipozidi
kutazama kwa makini aliona
kuwa lile halikuwa jitu la miraba
minne tu, bali lilikuwa ni kitu
kama mtu, na vilevile kama
mnyama, likishugulika kuandaa
chakula chake chini ya mti
mkubwa sana! Lo! Kumbe
alikuwa akiliangalia dude moja la
kutisha mno, lililokuwa na
manyoya mwili mzima, meno
marefu kama pembe za tembo
lakini yaliyojaa kinywa tele, na
kuanzia tumboni kwenda
miguuni, Kibwe alikuwa
akiangalia mwili wa binaadamu
mithili ya sokwe, isipokuwa
ulikuwa mkubwa kupita kiasi!
Uso wa dude hilo uliokuwa
kwenye kichwa kilicho fanana na
cha tembo, na katika paji la uso
wake, kulikuwa na jicho moja tu!
Naam, kwenye bonde
lililozungukwa na msitu wenye
miti mirefu kupita kiasi,
alikuwemo zimwi Nyalile, na juu
ya bonde hilo, alikuwepo Kibwe
akimwangalia! Utakisia
mwenyewe hali ya Kibwe
ilivyokuwa, mara alipotahamaki,
akagundua jinsi alivyokuwa
karibu kabisa na kubwa la
mazimwi wote, ambalo sifa zake
alizipata kutoka kwa Bunga!
“Mama yangu weee! Sasa kweli
niko hatarini!” Kibwe aliwaza.
Alijibanza kwenye miti mirefu
kabisa, huku jasho likimtoka, na
hofu iliongezeka kila sekunde,
wakati kijana yule alipoyaona
yale aliyoyaona mle bondeni!
Kwenye mafiga makubwa sana
kupita kiasi, Nyalile alikua
ameinjika jungu kubwa mno.
Wakati likichemka, alimkamata
ng’ombe mzima na kumnyonga
na kisha kumtumbukiza ndani ya
lile jungu. Pamoja na ng’ombe
huyo Nyalile alichukua kama
gunia mbili za mchele na kuutosa
kwenye lile jungu lililokuwa
likichemka kwa mchemko wa
kelele kubwa za ngurumo pale
msituni! Shughuli iliendelea na
muda wote lile zimwi lilikuwa
likichochea mapande ya miti
mikubwa mafigani, kukoleza
moto wake ili chakula kichemke
vizuri. Kitendo kile kilisababisha
moto mkubwa sana kuwaka ,
ulioambatana na moshi mnene,
ikawa kama msitu wote ulikuwa
unawaka moto!
Pale alipokuwa Kibwe,
ukilinganisha ukubwa wa miti
iliyomzunguka, alionekana kama
kidege kidogo mno. Aliwaza na
kukumbuka maneno ya Bunga,
kwamba akitaka kuvuka mpaka
kuelekea kaskazini ya mbali bila
kukamatwa na Nyalile, lazima
amliwaze kwa wimbo mzuri
utakaomburudisha na
kumfurahisha, kwani
atakapofanya hivyo lile zimwi
litadhani kuwa ni kidege
kinachoimba! Vilevile, Bunga
alimwambia kuwa lile jicho moja
la Nyalile halioni vizuri. Habari
yote hiyo ilimpa moyo Kibwe,
akahisi kuwa angeweza
kufanikiwa kulikwepa zimwi lile,
kama akijitahidi kufanya vile
alivyaelekezwa na Bunga. Lakini
imani yake ilipungua wakati lile
zimwi lilipomaliza kupika na
kisha kuketi chini ya mti
mkubwa, na kuanza kufuta jasho
lililotiririka kama mfereji wa
maji! Maajabu yale yalimfanya
Kibwe aduwae kabisa na hofu
yake kuongezeka upya! Hakujua
afanye nini! Je, akimbie?
Akimbilie wapi na njia ni ile
moja tu! au arudi alikotoka
walikokuwa wale mazimwi wala
ufuta? Aliona kuwa hapana budi
afanye alivyoambiwa na Bunga,
kwani hakuona njia nyingine!
Hivyo, kwa sauti iliyojaa
mawimbi kwa wingi wa hofu,
Kibwe alianza kuimba wimbo,
kwa maneno yaliyomjia katika
mawazo yake wakati ule…..!
Nyaalileee! Nyaalileee, Nyaali…
Nyaalileee, Nyaali……
Nyaalileeee! X2
Babu zimwi nipe motooo,
Nyaali Nyaalileee,
Niikapikie waanaanguuu,
Nyaalii Nyalileee,
Niipate viijunguuu namiii,
Nyaali nyaalileee,
Chaa wali naa cha mchuuzi ii,
Nyaali Nyaalileee!
Nyaaliileee! Nyaaliileee! Nyaalii
Nyaaliileee! Nyaalii Nyaalileee!
Kibwe alipomaliza wimbo wake
ule, alimchungulia zimwi Nyalile,
ili atambue hisia zake baada ya
kusikia ule wimbo. Alimuona
Nyalile akiinua kichwa na
kuangalia juu ya lile bonde
kwenye miti mingi mirefu
alikokuwa yeye Kibwe! Lo! Kijana
yule alianza kutetemeka na jasho
likazidi kutoka! Ni dhahiri Nyalile
hakuona kitu chochote huko,
kwanza kwa kuwa Kibwe alikuwa
ni mdogo sana na miti
iliyomficha ilikuwa ni mikubwa,
na pili, jicho moja la Nyalile
halikuwa likiona vema! Kibwe
akapata faraja kidogo,
alipomuona nyalile kiogo kidogo
akianza kutabasamu, na hatimae
kutoa kicheko cha aina yake na
halafu akisema;
“Weee kidege weee! Uko wapi?
Wimbo wako ni mzuri sana.
Hebu imba tena nisikiye!” Kibwe
alizidi kujibanza mitini, akihisi
wakati wowote ule, Nyalile
angeweza kumuona! Pamoja na
hofu yake, Kibwe alijitahidi
kurudia kuimba ule wimbo wa
Nyalile, ili kumfurahisha. Na
halafu lo! Kwa jinsi zimwi
alivyofurahia wimbo ule, alikariri
maneno katika kiitikio, “Chaa
walii naa cha mchuziii, Nyaalii
nyaaliileee………!” Na kisha weee!
Zimwi Nyalile liliinuka na
kujikung’uta, huku likizidi
kutabasamu kusikia jina lake
likitajwa, na pia likifurahia uzuri
wa kiitikio cha wimbo ule. Basi
ikawa tena ni:
“Chaa wali na cha mchuchiiii,
Nyaalii Nyaaliileee! Chaa walii na
cha mchuuchiii, Nyaliii
nyaaliileee…….!”
Alipokua akirudia rudia kiitikio
hicho, zimwi Nyalile alikuwa
akicheza hatua mojamoja,
akifuatisha wimbo ule, na
kuitikia vile alivyoelewa yeye!
Alivyonogewa zaidi, akawa
anapiga hatua za haraka haraka
na kuendelea na kiitikio chake;
na hatimae likatimka mbio huku
likiitikia;
“Chaa wali na cha mchuchiiii,
Nyaalii Nyaaliileee! Chaa walii na
cha mchuuchuuchii, Nyaliii
nyaaliileee a!
Moja kwa moja zimwi Nyalile
likayoyoma na wimbo wake huku
likitimua vumbi na kuangusha
miti kwa kuikumba lilipopiga
mbio, huku likiimba. Hiloooo!
Likayoyoma, msitu na nyika
mguu nipe, hadi likafika mbali
mno, bila kujielewa, likielekea
kusini mwa dunia! Kibwe naye,
haraka alishuka bondeni na bila
kupoteza muda…… akaanza
kupiga mbio bila kusimama, hadi
alipovuka ule mpaka
uliotofautisha eneo la kule
kunako kuchwa jua, ambako ni
magharibi ya dunia, na kaskazini
ya mbali ya dunia. Kibwe alikuwa
akielekea kwa mzee wa busara
aliyeelekezwa na Bunga, ili
kupata maelekezo kuhusu
maendeleo ya safari yake ya
ajabu.
MZEE WA BUSARA.
Safari yake ikamfikisha mahali
kati ya milima miwili mirefu,
kwenye mazingira mazuri sana,
yenye mianguko na maporomoko
ya maji, mahali palipojaaliwa
ardhi iliyorutubika mno. Kule,
Kibwe alikuta miti ya matunda ya
makomamanga iliyostawi vizuri
sana. Aliona ndege wakirukaruka
na kuimba kwa furaha juu ya miti
hiyo, ambayo chini yake vilipita
vijito venye maji safi na ya
baridi, vikitokea juu ya milima.
Kibwe alifarijika mno na hali ile,
hususan baada ya kuona maeneo
mengi yaliyoathirika na ukame,
na pia yaliyokabiliwa na uwazi
uliotokana na mashambulizi ya
majabali na ardhi, baada ya
kuteketezwa na wala mawe.
Alishangaa kuona jinsi sehemu
ile ndogo ilivyotofautiana na
maeneo yale ya awali!
Mara Kibwe akakumbuka!
CHANZO: https://
deusdeditmahunda.blogspot.com/
“Ahaaaaa! Sijui kwanini nilitaka
kusahau! Hapa ndipo Bunga
aliposema kuwa nitamkuta mzee
wa busara, ili nipate maelezo
kuhusu safari yangu! Sijui huyo
mzee wa busara ni nani? Lakini
nitafahamu baadae, kama kweli
hapa ndipo mahali penyewe.”
Hata hivyo kwa uchovu na njaa
aliyokuwa nayo, kijana yule
aliamua kuketi chini ya
mkomamanga , akawa anaokota
makomamanga yaliyoiva na
kudondoka chini, na kuanza kula.
Aliendelea kuketi chini ya ule mti
akipumzika, ili kupata nguvu
mpya. Alikuwa akitafakari
kuhusu hatima ya safari yake
wakati aliposikia mlio kama wa
pikipiki iliyokua ikianza
kuondoka! Alihisi kama mlio ule
ulikuwa ukitokea chini bondeni
hatua chache kutoka alipokuwa
ameketi, na alipotafakari kuhusu
mlio huo, akahisi kuwa ulikuwa
ni kama kikohozi cha jitu kubwa
sana! “Sijui ni kitu gani hicho
tena?” Kibwe aliwaza, na kwa
mara nyingine akaanza kupata
hofu. Alianza kujuta kwa nini
alikuwa kule mbali mno na
wazazi wake, ambao hata
hakukumbuka walikokuwa! Hata
hivyo, taratibu alinyanyuka na
kuanza kuangaza angaza,
akisogea bondeni uliposikika ule
mlio. Alitaka sana kufahamu ni
kitu gani kilichotoa mlio wa
labda tuseme….pikipiki? ……
Trekta……..?
Kila alipoangaza, hakuona kitu
chochote! Alisogea na kuzidi
kuchungulia chini bondeni, lakini
hakuona kitu licha ya ardhi ya
tope jeusi ambalo liliotesha
majani marefu, na pia
kulikuwepo lundo la kifusi
kilichoinuka mithili ya kilima
kidogo. Juu ya kilima hicho,
Kibwe aliona uyoga pori
umestawi vizuri sana. Taratibu
alisogea zaidi na kukichungulia
kile kilima, kuona kama
angeweza kushuka bondeni kwa
kurukia juu ya kilima hicho. Kwa
hiyo kutoka juu alikokuwa, kijana
yule alijirusha na kuangukia juu
ya hicho kilima. Hapo aliweza
kuangaza vema sehemu zote za
bondeni, ingawa bado alishindwa
kuona kitu chochote ambacho
kingeweza kutoa mlio wa
kustusha kama ule aliousikia
muda si mrefu uliopita.
Kibwe alishangaa sana, kwani
alikuwa na uhakika mkubwa
kuwa sauti aliyoisikia ilitokea
bondeni.
“Haya sasa ni maajabu makubwa!
Hivi ndio kusema kuwa labda
huo mlio sikuusikia? Au tuseme
haukutokea humu bondeni?”
Alijiuliza kwa mshangao mkubwa
juu ya muujiza ule wa aina yake.
Lakini kabla hajazidi kudadisi,
alisitushwa tena na mlio ule
usiofahamika, ila safari hii
alijikuta akirushwa hadi ng’ambo
kabisa juu ya bonde.
“Aaaaaaaaaaaaaaaaghh! Mama
yangu weeeeeeeeaaaagh…!” Alilia
kwa taharuki wakati alipokuwa
akielea hewani kabla ya
kuangukia kwenye matawi ya
mti, mbali na pale alipokuwa
awali.
Kijana aligwaya vibaya sana
akiwa ananing’inia juu ya mti
kama popo. Alikuwa akitweta na
kupumua kwa kasi, huku macho
yametoka pima, bila kufahamu
kilichomsibu! Halafu, kabla
hajatulia vema, kilisikika kitu
kama chafya ya nguvu
iliyoambatana na upepo mkali
kama wa gari moshi likifoka, na
hapohapo yeye alizolewa na huo
upepo na kujikuta akielea tena
hewani, na kisha akatupwa mbali
zaidi juu ya bonde kulikokuwa na
miti ya mikomamanga, akawa
amebanwa na matawi ya mmoja
kati ya mikomamanga ile!
Walisindikizwa na raia wa
Azarbajan kwa shangwe na
hoihoi hadi bandarini, na kule
wakaagana kwa upendo mkubwa,
na kisha merikebu ikaanza safari
nyingine ya ajabu ya Kibwe,
kumuokoa Bhaduri binti Sultani
Bashar wa Mashariki ya mbali ya
dunia!
Merikebu ya Mfalme KashKash
iliyoyoma usiku na mchana, na
hali ya bahari ilikuwa shwari
kabisa, kwa muda wote huo.
“Tuna bahati kubwa, kwani
mpaka sasa bado hali ni shwari
sana.” Hanga alimwambia
mwenzake Kibwe. “Kwa kawaida
mimi hutapika sana baharini,
lakini leo niko salama kabisa,”
Alieleza. Kibwe alimwambia
kuwa kwa kuwa bado safari ni
ndefu asijiamini sana. Kwa
maneno hayo, wote wawili
walicheka kwa pamoja. Meli hiyo
iliyowabeba vijana hao wawili,
wahudumu wakutosha wa meli
na manahodha, ilizidi kuyoyoma
hadi kufika katikati ya bahari,
halafu jambo la ajabu likatokea!
Ile meli ilisimama ghafla, kama
kwamba ilinasa mahali. Kibwe
alipomuuliza nahodha aliyekuwa
kwenye usukani ni nini
kilichotokea, akajibiwa kuwa
hakuelewa ni nini
kimeikwamisha meli yao.
“Huenda majani ya mwani
yamenasa kwenye pangaboi
linalozungusha maji huko chini
ya meli,” alisema nahodha.
Alipoambiwa hivyo kijana yule
alijitolea kwenda kuangalia kule
chini ya meli, ingawa wenzake
walimzuia sana.
“Ni hatari kwenda peke yako.
Labda tufuatane pamoja .” Hanga
na baadhi ya wahudumu wa
ndani ya meli walimwambia.
Ingawa Kibwe alipinga kufuatana
nao, lakini wenzake walishikilia
tu, hadi yule kijana akakubali
waende wote.
Naam, karibu watu wanne
walishuka na kuogelea kwenda
chini ya ile merikebu, kuangalia
hicho kilichonasa kwenye
pangaboi la meli yao. Wote
waliogelea, na Kibwe alikuwa
mbele zaidi, hivyo alitangulia
kuwasili pale lilipokuwa hilo
pangaboi. Lakini lo! Pangaboi
lenyewe lilikuwa limeshikiliwa
madhubuti na mtu mmoja
mwembamba kupita kiasi, na
mrefu kuliko utakavyofikiria!
Macho ya mtu yule yalikuwa
pembeni mwa sura yake,
iliyofanana na chura!
“Ahaa! Kumbe! Tunakutana tena
siyo?” Kibwe aliwaza, na bila
kupoteza muda, na haraka kama
mwendo wa mshale, kijana yule
alitoa rungu lililokuwa kwenye
mfuko alioubeba mgongoni, na
kulirusha kwa nguvu zake zote,
kumtupia yule mtu wa ajabu,
akilenga ule mkono ulioshikilia
lile panga boi! Kwa kishindo
kikubwa, lile rungu likamfikia
kwenye mkono wake huo, na
palepale akaachia lile panga boi,
na kama umeme, akapotelea
chini kabisa ya bahari!
Naam kwa mara nyingine, Kibwe
alikutana na mmoja kati ya jamii
ya majini wa bahari, jamaa zake
‘Makatta wa Makattani.’ Wakati
hayo yakitokea, wenzake wengine
waliokuwa wakija kuangalia chini
ya merikebu, walifika na
kumkosa yule jini wa bahari kwa
sekunde tu!
“Kwani kuna nini?” waliuliza, na
wakati huohuo, ile meli ikawa
inasogea mbele!
“Ilikuwa ni mwani tu, ulioshikilia
pangaboi! Nimekwisha uondoa ,
na ndio maana mnaona meli
inaondoka. Twendeni tuwahi!”
Kibwe alidanganya, akichelea
kuwatia hofu watu na hadithi za
majini wa bahari! Wote
wakarejea melini, na kuendelea
na safari.
Kibwe na wenzake waliendelea
na safari yao huko mashariki ya
katikati ya dunia, kwenye
majabali yaliyouzingira mto
mkubwa wa maji, mto Sakara,
ambako Bhaduri binti Sultani
kitinda mimba na mwana wa
saba wa Sultani Bashar, alikuwa
ameketi juu ya uwanda wa jabali
moja, akisubiri kutolewa kafara!
Kwa moyo wa ushujaa, na utiifu
kwa amri ya baba yake, mrembo
Bhaduri binti Sultani aliketi juu
ya jabali kwenye kiti kimoja
kizuri cha enzi, akiwa
amepambwa kwa sundusi za
hariri, mikufu, hereni na vikuku
vya dhahabu na vito vya
thamani, huku akinukia utuli
mchanganyiko kama udi, miski
na ambari, akisubiri wakati wake
wa kuchukuliwa na hicho
kitakachokuja kumchukua!
Kibwe na msafara wake ndani ya
merikebu yao ya fahari,
waliyoyoma kuelekea huko
mashariki ya katikati ya dunia,
wakati huo zikiwa zimebaki siku
chache tu, kuwasili mwisho wa
safari yao. Usiku mmoja
alipokuwa amelala na mwenzake
Hanga kwenye chumba chao,
Kibwe alimuota Bunga, akimpa
maelekezo ya safari yao hiyo.
“Lazima msafara huu usitishwe
haraka iwezekanavyo, mara tu
mtakapowasili kwenye bandari
yoyote ya jirani,” alisema Bunga.
Aliendelea kumwambia kuwa
itabidi wasubiri kwenye bandari
hiyo kwa siku mbili zaidi, kabla
ya kuanza tena safari yao. “Katika
muda huo mtakapo kuwa
mkisubiri kwenye bandari hiyo,
mtakuwa mmejinusuru na hatari
ya kupambana na mwamba wa
barafu majini, na pia
mtanusurika na tufani kubwa
itakayotokea mnamo saa ishirini
na nne zijazo.” Kibwe alimsikiliza
Bunga, aliyeonekana akielea
hewani kama ndege, na maneno
yake yakisikika kwa kukatika
katika, kwa sentensi
zisizokamilika!
Ndotoni Kibwe alikuwa
akimcheka Bunga, na
akimshangaa sana kwani kwa
mara hii alimuona ni wa ajabu
kabisa. Hakuamini maneno yake
hata kidogo, “Usinitanie mzee
Bunga! Unajua kwamba msafara
huu lazima uwahi nchini Shamsi
mashariki ya kati kati. Sasa
mbona unataka
kutuchelewesha?” Kibwe alianza
kulumbana na kile kijitu cha
ajabu.
“Tutaendelea tu……..na-
safa-”Lakini kabla hajamalizia
maneno yake, Kibwe akaona
ukuta uliokuwa mbele yake
ukipasuka, na maji mengi
yakianza kumwagika kama
mafuriko, na kumzoa Kibwe
kutoka pale alipokuwa, akajikuta
akitapatapa kujinusuru asizame!
Ingawa alikuwa anajitahidi
kuogelea, lakini alishindwa, na
hivyo akaanza kuzama---!
Akazama—akienda moja kwa
moja hadi chini kabisa ya dimbwi
la maji---! Pumzi zikamwishia
kabisa! Halafu ghafla, akajiibua
juu, na kutoa kichwa chake nje ya
dimbwi la maji, na kisha palepale
akasituka na kuamka, huku moyo
wake ukienda kwa kasi mno!
Aliinuka na kuketi kitako, akiwa
anapumua haraka haraka mno!
CHANZO: https://
deusdeditmahunda.blogspot.com/
Mwenzake Hanga aliyekuwa
karibu yake, naye aliamka na
kumuona Kibwe akiwa katika hali
isiyo ya kawaida. “Vipi kibwe,
mbona uko hivyo, umeota ndoto
mbaya nini?” Kimya! Kibwe
hakujibu kitu, bali alizidi
kupumua kwa haraka haraka,
huku macho yake yakiangalia
mbele zaidi ya pale alipokuwa
mwenzake, kama kwamba
hakumuona wala kumsikia
Hanga! Haraka Hanga alichukua
gilasi ya maji na kumpa
mwenzake huyo anywe, akihisi
huenda akajisikia nafuu kidogo.
”Hebu kunywa maji kidoga, labda
yatakusaidia.” Kibwe aliyapokea
yale maji bila kumwangalia
mwenzake, na akanywa funda
mbili, na halafu akajilaza
kitandani. “Unajisikiaje hivi sasa
Kibwe? Ni ndoto gani uliyoota?”
Hanga aliuliza, akiwa na wasiwasi
na jinsi alivyomuona mwenzake.
Kibwe alikohoa kidogo, na kisha
akaanza kuongea.
ITAENDELEA
KIPOZI
*********************************************************************************
Simulizi : Kibwe Katika Safari Ya
Ajabu
Sehemu Ya Kwanza (1)
MWANA MTEULE
Ukimya wa kutisha ulitawala eneo zima, na Kibwe akahisi woga wa ajabu ukimtambaa mwilini na kuzitawala fahamu zake zote. Alikuwa na kila sababu ya kutawaliwa na woga, kwani pamoja na kwamba hapakuwa na hata mtu mmoja pamoja naye, lakini vilevile hakukusikika kwenye msitu ule mlio hata wa ndege wala wadudu kama ilivyo kawaida.
Kimya kizito! Mara, sauti za ajabu zinasikika angani. Bundi na sauti za ndege wengine zisizopendeza masikioni zilivuma ghafla na kuzidi kumuongezea hofu Kibwe. Alipoangaza huku na kule, alishangaa sana kuona majabali na milima iliyotanda kila upande, bila kuwepo dalili ya mimea wala miti! Ardhi ya eneo lile ilikuwa imekauka na katika sehemu nyingi ilikuwa imepasukapasuka.
Kijana yule aliegemea mwambaulioelekea kwenye pango moja kubwa. Hivi naota…au ni kweli niko kwenye sehemu hii isiyoeleweka? Aliwaza huku akitetemeka kama mpapai uliopigwa na kibunga. Licha ya zile sauti za bundi na zisizopendeza masikioni za ndegewa ajabu, kwa muda wote wa saa kadhaa alizokuwa pale mahali, hakusikia sauti nyingine yoyote, hata ya upepo ukivuma, isipokuwa pumzi yake mwenyewe tu!
“Nimekusubiri kwa miaka mingi mno kijana, sikudhani kama siku hii ingefika.” Kibwe alipogeuka na kuangalia pangoni, alihisi ganzi kwenye miguu yake kwahofu! Moyo wake uliacha kudunda kwa sekunde chache, akatoa macho pima kutokana na kile alichokiona! Aka! Ni kitu gani hiki mbele yangu tena? Alijiuliza, huku fahamu zakezikimshauri atimua mbio kuelekea popote pale, alimuradi tu pawe mbali kabisa na mahala pale!
Kwa sekunde kadhaa, kile alichokuwa akikiona kilimfanya ashindwe kabisa hata huko kukimbia kwenyewe. Mbele ya
macho yake, kilisimama kitu kisichoeleweka, kama kijitu kidogo sana mithili ya mbilikimo, lakini udogo wake ulizidi ule wa
mbilikimo! Kilikuwa ni kijitu chenye uso ulioshupaa kama mzee wa miaka zaidi ya tisini.
Uso ule ulipambwa kwa msitu wa ndevu nyingi za mvi tupu zilizofika hadi magotini kwake! Kibwe alianza kukimbia lakini
ghafla, pale mahali alipokanyaga wakati akiruka kwa hofu, palianza kutitia na ardhi ikajiachia na kuporomoka pamoja naye! Wakati akiporomoka, alipoangalia chini kabisa, aliona uwazi usio na mwisho! Kwa hofu kubwa mno, aliachia ukelele wamfululizo, akihangaika kutafuta sehemu ya kukamata.
“Wooooooooooooooo…! Wooooooooooooa…….!” Kwa wepesi wa ajabu, yule mtu mdogo alinyoosha juu mkono wake na kuwahi kukamata mzizi uliokuwa ukining’inia juu yake. Alikunja miguu yake akijiandaa kubembea kwa kutumia mzizi
ule, akiazimia kujirusha kuelekea katika sehemu iliyokuwa imarakidogo. Alipofanya vile, alibembea huku akimchukua Kibwe pamoja naye kwa mkono wake wa pili, na wote wawili wakabembezwa na mzizi ule na kutupwa kwa mweleka mzito kiasi cha mita kumi hivi kutoka pale walipokuwa, wakiwa salama salimini ndani ya lile pango kubwa, lakini Kibwe akiwa ameshituka sana!
“Heeeeh! Ilikuwa kidogo niporomoke shimoni na kupotelea sijui wapi tu kule!” Kibwe aliropoka, akimshukuru Mungu kwa nusura aliyoipata. Alimtazama yule mtu mdogo wa ajabu, na kushangaa kuona jinsi alivyomnyakua kwa wepesi kama
mtu aliyechukua unyoya. Alitaka sana kujua alikuwa ni kiumbe wa aina gani yule!
Wakati wote ule wa pata shika, upepo mkali ulioambatana na dhoruba ulikuwa ukivuma, huku majabali yaliyotanda eneo lile yakiyumba na kutingishika vibaya. Ilikuwa ni hali ya kuogopesha mno kwa Kibwe. Kijana yule na mwenzake yule mwenye umbile dogo kama tumbiri, waliketi kwa muda wa kutosha pale mahali walipoangukia. Kile kijitu kilinyamaza kimya, kumpa nafasi Kibwe apumue kidogo, na Kibwe naye akanyamaza kimya, akijaribu kuelewa yule alikuwa ni nani, na ni kitu gani kilichokuwa kikiendelea pale, na kwa nini?
Baada ya nusu saa hivi, muda ambao kwa Kibwe ulionekana kama siku nzima, ile hekaheka ya maporomoko ilitoweka, na polepole upepo na dhoruba vikapunguza kasi yake. Alipoangalia nje ya pango lile kubwa, kwenye upeo wa macho
yake, akaona maajabu mengine. Katikati ya majabali makubwa na milima mirefu, aliona maumbile ya watu wakubwa mno! Aliinuka na kujaribu kutoka nje kidogo ya lile pango lililotitia bila kizuizi muda mchache uliopita, akitaka kuhakikisha kuwa ni kweli aliona kile alichokiona?
Ghafla alishikwa mkono na yule mtu mdogo aliyemrudisha nyuma kwa nguvu. “Chunga hatua zako kijana! Eneo lote hili linakabiliwa na uwazi mkubwa katika kila sehemu, na kama ulivyoona, inaweza kutokea hatari kubwa upande wetu. Kwa
sababu ya kuzuia hatari hiyo, ndiyo maana nikakuambia kuwa nimekusubiri wewe Kibwe kwa miaka mia moja!” Khah!
“Imekuwaje ukafahamu jina langu? Kwani wewe ni nani?” “Jina langu ni Bunga, na ni kiumbe pekee niliyebaki katikasehemu hii…” “Kiumbe pekee uliyebaki…??” “Naam. Nilibaki mimi na raia wachache tu, tulionusurika katika
nchi ya Sabaa miaka mia moja
iliyopita.” Kile kijitu kilichojinadi
kwa jina la Bunga kilimjibu, na
Kibwe akazidi kutoelewa.
“Mi..mi…mi sikuelewi we
babau!” Alimwambia.
“Huwezi kuelewa mpaka
ueleweshwe Kibwe. Hebu kaa
chini unisikilize basi…” Bunga
alimjibu, na KIbwe hakuwa na
namna ya kufanya vinginevyo.
Ndipo kibabu/kidudu Bunga
alipomsimulia za madhila
makubwa, akimuelezea habari za
nchi ya Sabaa ambayo ilikuwa ni
moja katika nchi za falme za
Kaskazini Mashariki ya dunia
zilizotawaliwa na wanawake
waliorithi falme za baba zao.
Alimwambia kuwa miaka mingi
nyuma, ikiwa chini utawala wa
Malkia Balika, nchi ya Sabaa na
jamii yake ya ‘Wanahewa’
iliteketezwa vibaya sana na jamii
yenye asili ya ‘Wanamoto’ kutoka
katika falme za majini, kwa
kutumia mioto iliyotokana na
pumzi zao.
“Kutokana na mashambulizi yao,
hakikubaki chochote katika
utajiri mkubwa wa nchi ya
Sabaa!” Alisema, akiongezea
kuwa siku hiyo ilikuwa ni siku
ambayo ‘Wanahewa’ waliandaa
hafla maalum ya kumtoa kijana
wao mteule na kumkabidhi kwa
mwalimu maalum ambaye ndiye
angemuelekeza kijana huyo jinsi
ya kutumia vipaji vyake vya
kipekee kwa faida ya jamii ya
sayari yao.
Bunga alikumbuka kuwa katika
baraza rasmi la Malkia Balika wa
Sabaa miaka hiyo mia moja
iliyopita, ulifanyika utabiri
kuhusu Mwana Mteule
aliyezaliwa nchini mwao. “
Atakapofikia umri wa miaka
kumi na nne, kijana huyu
mwenye vipaji maalum,
atakabidhiwa kwa mwalimu
ambaye atamwelekeza jinsi ya
kuvitumia vipaji hivyo kwa faida
ya jamii ya sayari hii, kwani yeye
ndiye mwokozi wa jamii zote
duniani...!” Mzee yule wa ajabu
alimwambia Kibwe kuwa tamko
lile lilitolewa na wazee
waheshimiwa, katika lile baraza
maalum la Malkia Balika.
“Walikuwa katika maandalizi ya
kutafuta mustakabala mwema wa
taifa lao.” Alisema.
“Ama! Sasa ikawaje tena?” Kibwe
aliuliza, akionekana kuvutiwa na
maelezo yale.
Bunga alimfafanulia kuwa kitu
kilichowaponza ‘Wanahewa’
miaka mia moja iliyopita ilikuwa
ni neema kubwa na mafanikio
yao ya ajabu yaliyotokana na
rasilimali yao ya kipekee ya vito
na madini, na pia vipaji vyao
adimu walivyojaaliwa.
“Katika miaka hiyo mia moja
iliyopita, nchini Sabaa alizaliwa
mwana wa kipekee mwenye
vipaji vingi vya ajabu na uwezo
mkubwa wa kimazingaombwe.
Kuwepo kwake katika sayari ile
ilikuwa ni kwa ajili ya kuinusuru
jamii yake katika sayari yake
pamoja na kuipa matumaini.
Utabiri wa wanataaluma
ulionesha kuwa kijana yule
angeelekezwa mbinu za
kumwezesha kuvitumia vipaji
vyake kwa ajili ya kuinusuru
jamii yake pindi atakapofikisha
umri wa miaka kumi na nne.
“Lakini looh! Hili halikutimia,
kwani chuki na inda za jamii ya
majini waovu dhidi ya jamii yake
vilitimia, na kijana yule
akateketezwa na moto katika
uvamizi ule wa wanamoto’,
uvamizi uliokusudiwa kumzuia
asitekeleze kazi muhimu
iliyomleta katika sayari ya dunia.
Kazi ya kuinusuru jamii ya
Sabaa!”
“Heh! Kwa nini ilikuwa hivyo
sasa?” Kibwe aliuliza kwa
hamaniko.
Kidudu Bunga alipiga kimya kwa
muda, kisha akamweleza Kibwe
chimbuko la uhasama
ulioiangukia nchi yake ya Sabaa.
Nchi iliyoneemeka. Nchi yenye
hewa safi pasina mfano. Nchi ya
wanahewa…
***
Miaka elfu mbili iliyopita huko
nyuma, nchi ya Sabaa ilineemeka
kwa kila fani – utajiri, maendeleo
makubwa na ustaarabu wa hali
ya juu, chini ya malikia wao
Balika. Sabaa ilitegemea zaidi
madini,vito pamoja na kilimo
kutokana na ardhi yake iliyokuwa
na rutuba, na hali ya hewa yake
mwanana. Baada ya uvamizi wa
Wanamoto ambao ni majini
wachokozi, raia wachache
waliobaki chini ya Malkia mpya
bibi Sultana, mdogo wake Malkia
Balika, walijitahidi kuijenga upya
nchi yao na kuanzisha utawala
mpya. Miongoni mwa mambo
waliyoyafanya ni kuanzisha
kanuni mpya za maendeleo, na
za kuendesha mambo yao kadhaa
wa kadhaa, na kuonesha kwa kila
hali ukomo wa ustaarabu
ulionawiri upya, alioufikisha
malkia wao huyo mpya. Hata
hivyo, kukosekana kwa ile neema
ya Mwana Mteule aliyehusudiwa
awali katika utawala ule tangu
miaka mia moja iliyopita,
kuliwapa Wanahewa majonzi na
masikitiko makubwa mno. Tukio
lile lilichelewesha sana
utekelezaji wa malengo bora ya
nchi ya Sabaa kwa ajili ya jamii
yake kote ulimwenguni kwa
kipindi cha miaka mia moja,
athari ambayo ilitabiriwa kuwa
ingejidhihirisha kwa dalili
mbalimbali katika sehemu nyingi
duniani!
“Kukosekana kwa kijana mteule,
kumeondoa matumaini miongoni
mwa jamii na kuzuia nusura si
kwa raia wa Sabaa pekee, bali pia
duniani kote.” Malkia Sultana
aliyerithi kiti cha Malkia Balika
aliwaambia wazee waheshimiwa
katika baraza lake la mashauri.
Alitoa wazo kwao kwamba ni
vizuri kuitisha mkusanyiko wa
raia wa Sabaa wakiwemo
wanataaluma ya nyota na
wanajimu, ili watabiri
mustakabala wa nchi yao pamoja
na dunia nzima, kuelewa ni
matatizo gani yatakayowakabili
katika sayari yao na jinsi gani
yanaweza kutatuliwa. Wazee
wale waheshimiwa ambao ni
washauri wa Malkia Sultana
katika utawala wake, waliafiki
mawazo yake, na ndipo
ulipoitishwa mkusanyiko wa raia
wote wa Sabaa katika uwanja
maalum. Uwanja ulifurika watu
waliokuwa na hamu ya kufahamu
hatima ya sayari yao. Wakati huo
sayari ya dunia ilikwishafikia
kiwango kikubwa cha nyuzi joto
ambacho haikuwa rahisi
kukipunguza, na kilikuwa
kikiongezeka kwa kasi kubwa.
Hali ile ilitishia mno maisha ya
viumbe wote duniani!
“Kwa hakika ingawa mwana
mteule aliteketezwa na moto kwa
njama za wale viumbe waovu
kwa nia ya kutuondolea
matumaini yetu, lakini hivi
tunavyozungumza umejitokeza
uwezekano mkubwa wa kupata
ufumbuzi utakaorejesha
matumaini kwa wanahewa wote
nchini Sabaa, na jamii nyingine
duniani.” Alitabiri mmoja kati ya
wanajimu waliohudhuria,
ambaye kwa maelezo yake hayo
hakuwatosheleza raia waliokuwa
na shauku ya kupata majawabu
ya maswali waliyokuwa
wakijiuliza. Malkia Sultana
alimwangalia mzee yule kwa
makini na kisha akamuuliza.
“Unaonaje ukitufichulia kuwa ni
matumaini gani hasa
yatakayopatikana, ili kila mmoja
wetu aondokane na wasiwasi
alionao hivi sasa?” Malkia yule
alihisi kuwa mnajimu kwa
makusudi kabisa, hakupenda
kufichua ukweli wa sababu za ule
utabiri, ambazo aliamini kuwa
zilikuwa ni nzuri tu, lakini hata
hivyo bado alitaka ufafanuzi wa
namna fulani, ili kurejesha imani
kwa raia wake, na kuwaweka
katika hali ya utulivu. Raia wote
nao waliafiki hoja za Malkia wao
na wote wakamkodolea macho
mnajimu yule, wakisubiri jibu
lake la kuridhisha, lakini kabla
yule mnajimu hajafungua mdomo
kusema lolote, kishindo kikubwa,
mithili ya kile kitolewacho na
gari moshi likichemka,
kilirindima eneo lote lile.
“Aaaa! Aaach-ch-chuuuuu!
Aaaa---aaaaach-ch-chuuuuu!”
Pale uwanjani vumbi lilitimka
kama kimbunga! CHANZO: https://
deusdeditmahunda.blogspot.com/
Jamii yote iliyohudhuria
mkusanyiko ule iligutuka na
kuruka kutoka vitini mwao. Vitu
vidogo vidogo vilivyokuwepo
katika eneo la mkusanyiko ule
kama vile mazulia, viti ambavyo
havikukaliwa, makaratasi na
vinginevyo, vilirushwarushwa na
kutawanywa huku na kule.
Hamadi!
Kumbe ilikuwa ni chafya moja ya
nguvu iliyotoka miongoni mwa
raia waliohudhuria mkusanyiko
ule. Kila mmoja alitaharuki na
kugeukia upande kilipotokea
kishindo kile, kushuhudia ni nini
hasa kilichotokea.
“Hayaaa! Hayaaaa! Jamani! hebu
tulieni kidogo! Tulieni jamani!
Bila shaka baadhi yenu
mnafahamu jinsi Mzee wa Busara
anavyokuwa kila anapokuwa na
mawazo mazito, kutokana na
matatizo ya aina hii.” Alisema
mmoja kati ya wazee
waheshimiwa.
“Mara nyingi anapofanya hivi
huwa na wazo muhimu la
kuchangia! Kwa hiyo ni bora
tutulie na tumsikilize kwa makini
ndugu zangu!” Mwingine
aliafikiana na yule mzee
muheshimiwa wa kwanza.
Naam. Mzee wa Busara alikuwa
amejirundika kama kifusi
pembeni kabisa ya ule uwanja!
Kwa haraka haraka mtu
angeweza kudhani kuwa ni
kilima kidogo kilichotokana na
takataka nyingi! Mzee yule wa
ajabu alianza kujigeuzageuza na
kunyoosha nyoosha shingo yake
ambayo awali haikuonekana.
Alikuwa kama mnyama mwenye
miguu minne na mkia mnene
kama wa mamba, na ngozi yake
ilikuwa na magamba kama ya
samaki, lakini zaidi yalionekana
kama ya mamba kwani yalikuwa
mapana mno!
“Aaaa—ch---chu---!” Alianza tena
Mzee wa Busara akiwapa wahaka
mkubwa wote waliokuwa
wakimwangalia. Alichukua nafasi
ile na kuanza kuelezea jambo
lake, wakati ambapo wote
waliohudhuria walikuwa makini
kabisa, wakidhani kuwa litatoka
chafya jingine babu kubwa
liwatimulie vumbi kama awali!
“Sisi---eh! Mhh-khuu! Sisi t-tun-
nafahamu kuw wa y-yapo mat-
tumaini ma-kubwa m-mbele-
yetu! Tusub-iri tu---aaach-ch-
mhhh!” Mzee wa busara
alijitahidi kuzuia chafya yake, ili
asiwavuruge raia waliokuwa
wakimsikiliza.
“Tuv-vute s-subira, maa n-na s-si
muda mr-refu t-tutapata maj-jibu
yatakayo turudishia imani na
matumaini, pamoja na nusura
tuliyoitegge—m-eaaaaaaa----c-h---
u….....!” alisema mzee yule wa
busara huku akizuia chafya zake
kwa taabu sana, akiwa pembeni
mwa uwanja na huku shingo
yake ndefu ikizunguka zunguka
kwa madaha kama shingo ya
twiga mtoto. Alimgeukia mtu
mmoja mdogo sana ambaye kimo
chake kilikuwa mithili ya kimo
cha ngedere. Mtu yule aligubikwa
na ndevu nyeupe tupu zenye
urefu wa kama mita thelathini
hivi, zilizoburuza hadi aridhini.
“Na matumaini hayo
yatadhihirika itakapokamilika
miaka mia moja kamili tangu
nchi hii ilipovamiwa na
kuteketezwa na majini wa
bahari.” Kijitu kile kidogo
kiliongezea taarifa katika maneno
ya Mzee wa Busara. Awali kabla
ya uvamizi wa nchi ya Sabaa,
kijitu kile ndicho kilichotarajiwa
kuwa mwalimu wa yule Mwana
Mteule aliyeteketezwa na moto
wa majini, katika siku ambayo
raia wa Sabaa waliazimia
kumkabidhi kwake.
“Kwa hiyo hakuna yeyote kati
yenu atakayekuwa na ufafanuzi
wa ufuatiliaji wa jambo
litakaloturudishia matumaini
yetu?” Alidadisi Malkia Sultana,
akiwaangalia wazee wake
waheshimiwa na watabiri wake
wa mambo waliohudhuria.
Mmoja kati ya wanajimu
aliyekuwa amejiinamia kwa
muda wote wa mkusanyiko ule
alisema; “Kwa hakika hatuwezi
kufafanua zaidi kwani
tutakapofanya hivyo tutavunja
mwiko, na hivyo kuweka ugumu
zaidi katika upatikanaji wa
ufumbuzi wa mambo
yanayohusika. Ila, tunachoweza
kusema ni kwamba maelekezo ya
dalili za madhara yanayoikabili
sayari yetu na jinsi ya
kukabiliana nayo, yameandikwa
katika moja ya vidani vya fedha
vyenye umbile la kucha za Simba,
kwenye mkufu unaoning’inia
shingoni mwa sanamu la shaba la
kichwa cha Simba, katika nchi ya
milima minne myeusi ya
maangamizi, kwenye uwanda wa
jabali la kisiwa cha Baharia!”
Raia wote waliohudhuria
waliduwaa!
Kwenye milima myeusi ya
maangamizi? Ndio wapi huko?!
Ukimya mkubwa ulitawala
uwanja ule wa mikutano, kila
mmoja akitafakari kuhusu taarifa
ile mpya ambayo kwa hakika
iliwakatisha tamaa zaidi, kwani
walihisi kuwa lile ndilo lililokuwa
jukumu la Mwana mteule,
ambaye walikwisha mpoteza!
***
Naam, Kibwe alimsikiliza Bunga
kwa makini sana, akijaribu
kuhusisha taarifa ile ya kidudu
Bungan a yale na maneno yake ya
awali, kwamba ‘alimsubiri yeye
kwa kipindi cha miaka mia moja’.
Hapo akasikia mikoromo ya
kutisha nje ya lile pango
walilokuwemo. Akakumbuka yale
majitu ya ajabu aliyoyaona kule
nje muda mchache uliopita.
Alizidi kuogopa.
“Yale…ni majitu gani kule nje?”
Kibwe alimuuliza yule mzee wa
ajabu, huku akioneshea na
akichungulia nje ya lile pango
kujaribu kuyaangalia majitu yale
aliyoyaona awali. Kama hapo
awali aliogopa, basi safari hii,
aliogopa maradufu, kwani baada
ya lile giza la vumbi nene
kutoweka, aliweza kuyaona vizuri
sana yale majitu ya ajabu! Miili
yao mikubwa kama milima
ilikuwa na vichwa vyenye
mapembe vilivyofanana na
vichwa vya ng’ombe! Halafu lo!
Mikono na miguu yao ilikuwa na
makucha marefu ya shaba!
Wakati akishangaa kwa kuhofu
namna ile, aliyaona yale majitu
yakipasua majabali na
kuchimbua milima. Huku
yakikenua meno yao makubwa ya
shaba yaliyong’ara mno kwa
mwanga wa jua, Kibwe
aliyashuhudia yale majitu
yakitafuna mawe bila kizuizi
kama kwamba yalikuwa
peremende! Miguu ilimwisha
nguvu, na kumfanya kijana yule
anyong’onyee taratibu na kurudi
chini, akiwa dhofu-l-hali kwa
hofu.
“Ama hakika leo ndio kifo
changu! Hakuna uwezekano wa
kunusurika hata kidogo hapa! Na
kama ninaota, mbona siamki
mpaka sasa? Laaa! Sijui
nitanusurika vipi mimi!” Aliwaza
kijana yule kwa hofu na wahaka.
Alimwangalia Bunga
aliyeonekana kuwa hana hofu
hata chembe, na kwa sauti ya
kutetemeka, akamuuliza kwa
mara nyingine, “Aaa...eeeh…
hivi…eeeh…. wale ni kina nani
babu….? Wametoka wapi…..na
kwa nini….wanafanya vile
wanavyofanya?”
“Wale kijana ndio wala mawe.
Kila mwaka kwa muda wa miaka
mia moja sasa, watu hao wa
ajabu wamekuwa wakitokea,
wakisindikizwa na upepo mkali,
vumbi, dhoruba na matetemeko
ya majabali. Wakifika tu, huanza
kuchimbua milima na mawe na
kupasua majabali, ili kujipatia
chakula chao. Watu hao wala
mawe wataendelea kufanya hivyo
hadi kuimaliza dunia yetu yote,
wakisababisha uwazi wenye kina
kirefu kisichokuwa na mwisho!”
Bunga alimwambia, na Kibwe
akaduwaa akiwa kinywa wazi.
Bunga alizidi kumkatisha tamaa
ya nusra pale alipomweleza kuwa
hata yeye anahofu kwamba
hatimae, hata ile sehemu ya ardhi
kwenye lile pango alikokuwa
anaishi kumsubiri, pia itatoweka
pamoja naye, na kuacha uwazi
kama sehemu nyingine katika
eneo lile, ambao uliwapoteza
viumbe wengine wengi kabla
yake.
“Oooh! Haponi mtu hapa!” Kibwe
alijisemea kwa sauti huku
akijishika kichwa kwa kukata
tamaa.
“Wewe pekee ndiye
utakayesaidia kuzuia hali hii
isiendelee na labda kuirudisha
vile ilivyokuwa awali Kibwe,
kwani wewe bado ni damu
changa, hujaanza kufikia umri wa
kukata tamaa.” Bunga
alimwambia, na Kibwe
akamshangaa. Hakujiona yeye
akimuokoa yeyote kutokana na
maangamizi ya ile mijitu
inayokula mawe, lakini pia
alishangaa kwani hakuona
uhusiano baina ya kuiokoa dunia
na ule uwazi ulioikabili. Vyote
kwa vyote, hakuelewa ni vipi
yeye angeweza kuzuia ile hali ya
hatari isitokee, hasusan
akizingatia kuwa waliohatarisha
hali ile ya dunia walikuwa ni
majitu makubwa mno kwa yeye
kuyadhibiti!
Kama vile aliyekuwa akiyasoma
mawazo yake, Bunga aliendelea
kumwelezea hatua zipi achukue,
ili kuinusuru dunia.
“Wewe ndiye mteule mwenye
jukumu hilo Kibwe, pamoja na
mengine ya kuitahadharisha jamii
na kuiokoa dunia na ukame, na
uwazi ulioikabili. Hiyo ni pamoja
na matatizo ya kiafya na vifo vya
binaadamu na viumbe wengine,
na pia kuinusuru dunia na uovu
na uadui miongoni mwao,
pamoja na kuwajengea imani na
matumaini...”
“Khah! Mimi?”
“Wewe, Kibwe! Kwa hiyo, ili
ufanikishe kazi hiyo, lazima
ufanye safari ndefu na yenye
mitihani mikubwa. Safari hiyo
ndiyo itakupatia ufumbuzi wa
jambo hilo. Kwa vyovyote vile,
usikubali kabisa kukata tamaa
kwa jambo lolote litakalotokea,
kwani utakapokata tamaa, azma
yako haitatimia.” Bunga
alisisitiza, mara kwa mara
akikunja uso wake uliokomaa na
uliopambwa na zile ndevu zake
nyingi za mvi.
“Lakini bado sijaelewa jinsi
nitakavyotimiza azma hiyo babu!
Na hiyo safari nitakayoifanya ni
kuelekea wapi baada ya kutoka
hapa?” Kibwe alihoji, yote yale
yakiwa ni mazito kwake.
Maelekezo ya Bunga kuhusu
safari yake yalizidi kumtia hofu,
kwani yalimdhihirishia kuwa
hakika safari ile ingekuwa ngumu
mno na isiyo ya kawaida.
“Mara baada ya kuondoka wale
wala mawe, takriban nusu saa
kuanzia sasa, utaelekea
magharibi ya dunia hadi ufike
mahali kunakokuchwa jua, katika
makutano ya mbingu na ardhi,
ambapo jua huonekana kama
kwamba linazamia hapo. Kwenye
ufukwe wa bahari utaona
mtumbwi. Tumia mtumbwi ule
kwa safari yako ya kuelekea
kisiwa cha mazimwi, viumbe
ambao nusu;yaani kuanzia
kuanzia tumboni kwenda
miguuni ni wanyama, na kuanzia
tumboni kwenda kichwani ni
wanadamu. Katika kisiwa hicho
utakuta ngome moja imara, na
ndani ya ngome hiyo, huishi hao
mazimwi ambao hulinda upanga
wa radi. Jitahidi uupate upanga
huo ili ukusaidie katika
mapambano ya kuzuia vitendo
vitakavyozidi kueneza uwazi
mkubwa katika dunia hii.
Utakapofanikiwa kuupata upanga
wa radi na kuondoka katika
kisiwa cha mazimwi salama
salimini, utaelekea katika nchi ya
Azarbajan iliyoko kaskazini ya
mbali ya dunia, baina ya milima
miwili mirefu sana. Ili kuupata
upanga wa radi kwenye kisiwa
cha mazimwi, lazima uwe
mwangalifu mno, uhakikishe
kuwa unaingia kwenye ngome
yao wakati ukiwa na hakika
kuwa wote wamelala usingizi
kwani….”
“Sasa, nitahakikisha vipi kwamba
mazimwi hao wamelala ili niweze
kuingia kwenye hiyo ngome?”
Kibwe alimkatisha kwa
mshangao. CHANZO: https://
deusdeditmahunda.blogspot.com/
“Utakapo sikia kelele nyingi na
zogo kutoka ndani ya ngome
kama vile unazomewa na kundi
kubwa la watu, hapo ndio
utaanza kuingia ndani polepole,
na utakapofika ngomeni,
utawakuta mazimwi hao
wamelala sesa; fo-fo-fo! Humo
ngomeni utaona mnara wa
dhahabu, na juu ya mnara huo
wa kipekee, utauona upanga wa
radi uliowekwa nje ya ala yake na
unang’ara kama jua.” Bunga
alitoa maelekezo yale
yaliyomshangaza mno Kibwe,
aliyestaajabu sana kusikia kuwa
eti zinaposikika kelele nyingi za
mazimwi, ndio ishara kuwa
wamelala! Alijiuliza sana moyoni
mwake kama mambo yote yale
aliyokuwa akisikia yalikuwa
katika ndoto, au kweli yalikuwa
alivyokuwa akiyasikia!
Wakati Kibwe anahoji uhakika
wa mambo mengi yaliyomtokea
katika kipindi kifupipale kwenye
ule mji wa wala mawe, alimsikia
tena Bunga akisema; “Ingawa
utafaulu kuwakimbia mazimwi
wa ngomeni, hutaweza kuvuka
mpaka wa nchi hiyo ili kuendelea
na safari yako, kwani njiani
utazuwiliwa na kiongozi wa
mazimwi hao, zimwi ‘Nyalile’
mwenye jicho moja. Kwa bahati
nzuri icho hilo moja la zimwi
‘Nyalile’ halioni vizuri. Na kama
atajaribu kukuzuia usipite, lazima
umuimbie wimbo mzuri
utakaomvutia na kumlaghai, ili
asiweze kujua kama wewe ni
mwanaadamu!” Lo! Hapo Kibwe
akazidi kuhofu, na kuzidi
kumaizi kuwa kazi iliyokuwa
mbele yake, kamwe haikuwa
rahisi! Aliogopa sana kusikia
maelezo ya Bunga, na akakosa
imani kabisa ya kuendelea na
jukumu lile la kuiokoa dunia
isikumbwe na janga la uwazi
ulioikabili, pamoja na majanga
mengine.
Bunga alifahamu wahaka na
taharuki ya Kibwe baada ya
kumpa maelezo ya jinsi safari
yake itakavyokuwa, hivyo akazidi
kumpa moyo akiongea naye kwa
upole, na kumuhakikishia kuwa
hatapata tatizo lolote katika safari
hiyo, kama atatumia busara na
kufuata maelekezo yake.
“Nimekuambia tokea mwanzo
kuwa wewe ndiwe mteule wa
jukumu hilo, kwa hiyo kabla
hujaondoka kuelekea kwenye
safari hii ya aina yake, nitakupa
silaha mbalimbali, ambazo
utazitumia kadiri inavyostahili.”
Baada ya kusema hivyo, Bunga
alijisogeza ndani ya pango lake
na kutoa mfuko mmoja mkubwa
wa gunia na kumkabidhi Kibwe.
“Humu ndani kuna silaha nyingi
utakazozitumia utapozihitaji……”
Bunga alizitoa zile silaha moja
baada ya nyingine, akielezea kazi
zake taratibu na kwa makini,
Kibwe alisikiliza maelezo hayo
kwa umakini mkubwa. Bunga
akamuuliza iwapo ameelewa
maelekezo yote. Kibwe akaafiki
kuwa ameelewa.
“Haya kijana, hebu fumba macho
kidogo….” Hatimaye Bunga
alimuamuru, na Kibwe akafanya
alivyoambiwa. Wakati macho
yake yakiwa yamefumba, alihisi
mtikisiko na akasikia mvumo
ulioambatana na mtikisiko ule
mithili ya mtu aliyekuwa kwenye
gari moshi. Naam, hapo ndipo
ilipoanza safari ndefu na ya ajabu
ya Kibwe. Alipofumbua macho
kuelewa ni jambo gani lililokuwa
likiendelea, alijikuta ufukweni,
na mbele yake ulikuwepo
mtumbwi!!
***
Kibwe aliendelea na safari ile
kama alivyoelekezwa na Bunga.
Kwa muda mrefu mno aliendesha
mtumbwi alioukuta ufukweni,
hadi akachoka sana na kuanza
kusinzia kwa uchovu.
Alipokaribia kile kisiwa cha
mazimwi, Kibwe alianza kusikia
sauti nyororo na nzuri zikiimba
wimbo ulioburudisha kupita
kiasi! Alipotupia macho mbele
kabisa ya kisiwa, akawaona
mabinti saba wazuri, waliovalia
mavazi ya hariri yaliyometameta
juani, na waliovutia kupita kiasi.
Lakini zaidi ya uzuri wao, sauti
zao ndizo zilizomvutia Kibwe
zaidi. Alitega sikio na kusikiliza
kwa makini. Lo! Sauti zilikuwa si
za kawaida! Kibwe akazidi
kusinzia kwa burudani ilepamoja
na uchovu aliokuwa nao. Mara
akakumbuka maneno ya Bunga!
“Karibu na kisiwa cha mazimwi,
kuna mabinti saba laghai wenye
sauti nyororo za
kimazingaombwe. Ukizisikiliza
sauti zao nzuri kwa mfululizo,
lazima utawafuata walipo, na
ukifika kule watakuwekea ulozi
kwenye kinywaji chako na
kukufanya usahau kabisa
kutekeleza malengo yako!
“Kwa hiyo nitafanyaje kujinusuru
na ulaghai wao?” Kibwe aliuliza
“Utachukua hii ‘nta’ na kuziba
masikio yako ili usiweze kuzisikia
sauti zao.”
Haa! Sijui kwa nini Kibwe alitaka
kusahau jambo lile muhimu
kabisa. Haraka akatoa ile ‘nta
aliyowekewa kwenye mfuko wa
gunia na kuyaziba barabara
masikio yake, kisha akaendelea
na safari yake kwa amani hadi
alipofika kisiwa cha mazimwi.
Kibwe alianza kuangalia huku na
huko akitafuta sehemu ya kivuli
aweze kupumzika kabla ya
kuanza kutekeleza ile kazi
iliyompeleka kule. Alipata
sehemu yenye mti wenye matawi
marefu sana yaliyokuwa
yakiburuza hadi chini, na hapo
akaketi na kutumia yale matawi
kwa kujificha, ili asionekane.
Baada ya kunywa maji
aliyowekewa na Bunga kwenye
ule mfuko mkubwa wa gunia,
Kibwe alipata lepe zuri la
usingizi, kutokana na upepo
mwanana uliopuliza sehemu ile.
Alilala kwa muda mrefu
akapumzika vya kutosha, ili
apate nguvu ya kuanza kuelekea
kwenye ngome ya mazimwi,
kuchukua upanga wa radi, kama
alivyoelekezwa na Bunga.
Baada ya mapumziko yake, Kibwe
alianza ufuatiliaji wa kazi
iliyompeleka kule. Alikumbuka
maneno ya Bunga. “Itakubidi
kwanza uende kwenye mlima
ambao chini yake kuna shamba
kubwa la ufuta.” Alifahamishwa
kuwa sehemu ile ilikuwa karibu
na makazi ya wale mazimwi
hatari wafuasi wa Zimwi
mkubwa aliyeitwa ‘Nyalile’ na
ambao kwa pamoja, wakati fulani
waliwateketeza wakazi wa kisiwa
hicho kwa kuwatafuna. “Lazima
upande mlima huo hadi kileleni,
na huko utakuta jumba
wanamoishi mazimwi hao,
lililozungushiwa ngome
madhubuti.” Aliambiwa kuwa
lazima akachukue upanga wa radi
unaotoa cheche za moto kila
unapotumiwa, na kumpa ushindi
yule anaye utumia. Aliambiwa
kuwa ile ndiyo silaha pekee
ambayo ingemsaidia kupambana
na mitihani mikubwa iliyokuwa
mbele yake, akiendelea na safari
yake kuelekea matokeo ya jua,
baina ya mashariki na magharibi.
Kibwe alipita kwenye shamba
kubwa la ufuta na kuanza safari
yake ngumu ya kupanda mlima
akielekea kileleni kwenye jumba
la mazimwi. Katika jitihada zake
hizo, mara kwa mara kijana yule
aliteleza na kuporomoka, lakini
alizidi kuupanda mlima bila
kuchoka wala kukata tamaa.
Mchana kutwa Kibwe aliendelea
na safari ile ya kupanda mlima,
na ilimchukua takriban siku mbili
njiani akila matunda ya porini
kujinusuru na njaa. Kila
alipokutana na wanyama wakali
kama simba, chui , faru, mbogo
na wengine, Kibwe aliwakwepa
kwa kujificha vichakani. Hadi
kufikia saa kumi jioni siku ya tatu
jua lilipoanza kuchwa, kijana yule
aliona ngome ndefu mno,
iliyosimama kwenye upeo wa
macho yake katikati ya msitu!
Taratibu, huku akiangalia huku
na kule, Kibwe alisogea karibu na
ngome ile. Alipokaribia zaidi
alistushwa na kelele na zogo
kutoka ndani ya ngome ile
madhubuti! “Huyooooo! Anakuja
kuchukua upanga wetu! Haraka
mkamateni! Mfuateni mumlete
haraka kabla hajaingia ndani!
Hayaaa! Kamataaa! Chinjaaaa!
Uwaaaa! Nyongaa!” La haulaa!
Kibwe alianza kukimbia kwa hofu
ya kukamatwa na kutafunwa na
mazimwi wale hatari, na kusahau
kabisa usia aliopewa na Bunga!
“Utakapo sikia kelele nyingi na
zogo kutoka ndani ya ngome
kama vile unazomewa na kundi
kubwa la watu, hapo ndipo
utaanza kuingia ndani polepole,
na utakapofika ngomeni
utawakuta mazimwi hao
wamelala sesa, fo-fo-fo !
Kutakapokuwa kimya basi
tahadhari sana, kwani mazimwi
hao watakuwa wako macho!”
Hilo lilikuwa ni onyo la Bunga
kwa Kibwe.
Haa! Ilikuwaje akasahau jambo
jingine muhimu kama lile?
Hamadi! Palepale alipokumbuka
onyo lile na taarifa ya Bunga
kuhusu maajabu ya wale
mazimwi, Kibwe aligeuka na
kupiga mbio kuelekea kule
ngomeni. Alipofika langoni huku
akipumua kwa kasi, Kibwe
alichunguli ndani kwa uangalifu
na umakini mkubwa kuona kama
wale mazimwi walikuwa
wamelala. Hakuona dalili ya mtu
au kitu chochote katika upeo wa
macho yake. Taratibu aliingia
ndani akinyata polepole na
alipoangalia mbele zaidi, akaona
eneo kubwa la wazi lenye bustani
nzuri ya maua. Aliambaa na
ukuta, huku polepole akinyanyua
mguu mmoja mmoja, akishikilia
pumzi yake kwa hofu ya kusikika
na madude yale hatari
aliyoambiwa na Bunga. Mwisho
kabisa wa eneo lile la wazi,
Kibwe aliona lango jingine kubwa
lenye mbao za marembo
marembo. Alinyata taratibu na
alipogundua kuwa lango lile
lilikuwa wazi, alilisukuma na
kuchungulia uwani. Hamadi!
Kibwe hakuamini macho yake
kwa kile alichokiona! CHANZO:
https://
deusdeditmahunda.blogspot.com/
Macho ya kijana yule yalikutana
na kundi zima la madude
makubwa kupita kiasi yaliyokuwa
nusu ni watu, yaani kutoka
tumboni kwenda kichwani na
nusu, katika sehemu ya tumboni
kwenda miguuni walikuwa kama
sokwe! Kundi lile la madude yale
ya ajabu na ya kutisha, lililala
sesa kwenye nyasi za eneo lile, na
huku kelele zao za kuzomea
zikiendelea! Wakati sauti zao
zikimbabaisha Kibwe, miili yao
ilimtisha sana kwani ilikuwa na
manyoya marefu kupita kiasi
yakiburuza hadi chini kama
ufagio! Viumbe wale walikuwa
na midomo iliyojaa meno yenye
ukubwa mithili ya pembe za
ndovu! “Lo….. ndiyo maana
ilikuwa rahisi sana kwa madude
haya kuwatafuna na
kuwateketeza mara moja watu
wa kisiwa chote hiki, kutokana
na urefu na wingi wa meno yao
makali!” Kibwe aliwaza, akiwa na
woga na wahaka mkubwa usio
mfano.
Haraka Kibwe alifuata yale
maelekezo ya Bunga, akianza
kuwatambuka taratibu wale
mazimwi waliolala huku
wakipiga kelele na kuzomea
kama kwamba walikuwa macho,
hali iliyomfanya Kibwe azidi
kuhofu, kwani muda wote alihisi
kuwa huenda ghafla wakamrukia
na kumshambulia. Hiyo Ilikuwa
ni kazi ngumu mno kwa kijana
yule na muda wote wa zoezi lile,
jasho lilikuwa likimtiririka na
mara nyingine alihofu kuwa
huenda jasho lile likawadondokea
na kuwaamsha wale mazimwi, na
huo ukawa ndio mwisho wake!
MAJANGA YA SAYARI
Wakati Kibwe akiwa katika
jitihada za kutekeleza malengo
yake ya kuinusuru jamii kule
machweo ya jua katika kisiwa cha
mazimwi, katika sehemu
nyingine iliyo baina ya mashariki
na magharibi mbali kabisa
kutoka kisiwa kile cha mazimwi,
katika milki ya Sultani Bashar,
majini yalitawala sehemu kuu
iliyowapatia maji raia wa nchi ya
Shamsi mjini Majabali. Jambo
hilo lilisababisha shida kubwa ya
maji na ukame uliathiri maeneo
mengi ya nchi ile, iliyokosa
chakula cha kutosha kwa watu
wake. Ili kuwanusuru raia wake
na shida ile ya maji, kila mwaka
Sultani Bashar wa nchi ya Shamsi,
alimtoa kafara binti yake kwa
joka moja kubwa ambalo
lilimchukua binti yule na kuzama
naye kwenye mto Sakara ulioko
kati ya majabali mawili na
kumpeleka kwa jini ‘Makattani,’
mfalme wa majini yote. Mpaka
kufikia wakati ule Kibwe
alipokwenda kisiwa cha
mazimwi, tayari Sultani Bashar
wa nchini Shamsi alikwisha
watoa kafara watoto wake sita,
binti mmoja kila mwaka na kila
mara akiwapatia raia wake
mwaka mmoja wa kuchota maji
kutoka mto Sakara. Hatimae
Sultani yule alibaki na binti
mmoja tu, Bhaduri binti sultani
ambaye kwa bahati mbaya
kwake, alitakiwa kumtoa kafara
wiki mbili zilizofuata kwenye mto
uleule Sakara, ili kuwapatia raia
wake mwaka mmoja zaidi wa
kutumia maji yake!
“Ama kweli hali hii ni ya
kusikitisha na kusononesha
mno,” Malkia wa Shamsi
amlalamikia mumewe Mfalme
Bashar, huku akilia bila kizuizi!
“Haya ni maonezi makubwa na
ni unyanyasaji wa aina yake, wa
kuwalazimisha mabinti zetu
wajitowe mhanga, eti kwa ajili ya
kunusuru raia wako! Hili si
jambo la kibinaadamu hata
kidogo.” Malkia yule alisema kwa
masikitiko makubwa. “Sasa mke
wangu unadhani tungefanya nini
kulitatua tatizo hili sugu
linalotukabili kila mwaka?”
Sultani Bashar alimuuliza mkewe
kwa upole.” Hata mimi nina
majonzi makubwa kuhusu
mabinti zetu, lakini hii ndiyo njia
pekee ya suluhu kwa jambo hili.”
Katika mji ule mkuu wa Majabali
nchini Shamsi, baada ya Suitani
kufanya maandalizi ya
kumpeleka kitindamimba wake
Bhaduri kule mtoni Sakara kwa
ajili ya kafara, aliketi kwenye kiti
chake cha enzi na kujiinamia kwa
fikira na majonzi ya kumpoteza
binti yake mwengine! Ama kweli
Sultani yule alikuwa mtawala wa
aina yake! Eti kudiriki kuwatoa
kafara mabinti zake saba! Si
jambo la kawaida asilani!
Kule Azarbajan nako kwa Sultani
Kash Kash kaskazini ya mbali ya
dunia, ingawa chini kabisa ya
bahari, i jini ‘Makatta’na
wenzake walikuwa wakiandaa
vichafuzi vya hewa safi
iliyowasaidia watu kuishi, na
kuigeuza hewa ile kuwa
hatarishi, lakini Mfalme wa nchi
ile hakutambua hivyo. Hakujua
kama hewa ile iliyogeuka kuwa
moshi mnene ilipoanza kuzizima
na kisha kuwazingira watu katika
himaya yake, ndipo walipogeuka
kuwa mawe ya theluji! Kwa kuwa
hawakuelewa chanzo hasa cha
janga lile, watu wote wa kule
waliingia hofu kubwa na Mfalme
wao alikuwa akimtafuta
mkombozi atakaye wanusuru raia
wake kutokana na janga lile!
“La mgambo! La mgamboooo!
Likilia lina jamboo! Asiye mwana
a eleke jiwee!” Kijumbe wa
Mfalme Kash Kash alipita mitaani
akiwatangazia raia wa Azarbajan
kama kawaida wakati inapotokea
dharura ama ya raha, au ya
karaha, akianza kwa kupiga goma
lake kubwa alilolibeba kifuani, na
lililofungwa kwa kamba iliyopita
mabegani na kuzungukia
makwapani.
Kwa kupiga ile ngoma kijumbe
yule aliwavutia watu na
kuwasogeza karibu, ili waende
kumsikiliza. “Jamani eeeh!
Kuhusu janga linalotukabili la
raia wengi kugeuka mawe ya
theluji, mpaka hivi sasa bado
haujapatikana ufumbuzi wa
tatizo hilo, na wala bado
hajapatikana mkombozi atakaye
saidia kunusuru maisha ya raia
wa nchi hii. Hivi sasa wazee wa
baraza la Mfalme, wako mbioni
kutafuta njia ya haraka ya
ufumbuzi wa tatizo hilo. Kwa
hiyo yeyote atakaye kuwa na
mawazo tafadhali asisite
kujitokeza na kuchangia, ili
kulipiga vita janga hili la
kihistoria nchini kwetu…..! La
mgambooooo! La mgambooooo!
Likilia lina jamboooooo!”
Kijumbe yule alihitimisha
tangazo lake na kisha kuendelea
katika maeneo mengine ya mji
wao mkuu. Tangazo lile
lilitangazwa mara kwa mara
katika miji mbalimbali ya
Azarbajan, lakini hakujitokeza
mtu yeyote aliyeweza kutoa
ushauri kuhusu utatuzi wa tatizo
lile.
Katika ngome ya jumba la
mazimwi kwenye kisiwa chao,
Kibwe alitumia muda ule ambao
mazimwi wale walikuwa
wakipiga kelele, kwa kuendelea
kuwatambuka mmoja mmoja,
hadi alipofika kwenye ule mnara
wa dhahabu. Pale alipumua
kidogo kabla ya kuanza kupanda
mnara huo ambao juu yake
ulikuwepo upanga wa radi
alioutaka. Kelele za mazimwi
zilizidi kuliko awali, kama
kwamba walihisi kuwa kuna mtu
karibu ya hazina yao.
“Naomba Mungu majitu haya
yasiamke ama sivyo sitanusurika
asilani!” Kibwe aliwaza.
Alikumbuka kuwa mara tu, kelele
zitakapokoma, ndio utakuwa
wakati wa hatari kubwa kwake!
“Na kutakapokuwa kimya basi
tahadhari kwani watakuwa wako
macho!” Bunga alimwambia.
Ingawa aliogopa sana na kuhofu,
lakini kijana yule shujaa alipanda
juu ya ule mnara mrefu akafika
kileleni, na kwa uangalifu
akauchukua ule upanga na kuutia
kwenye ala yake, na kisha
akaupachika kiunoni kwake na
kuanza kuteremka chini kwa
uangalifu! Alipofika chini,
akarudia lile zoezi la wasiwasi la
kuyatambuka yale mazimwi
yaliyolala! Lo! Kwa bahati mbaya,
alipokuwa akimalizia zoezi hilo,
alilikanyaga zimwi la mwisho
lililolala karibu na lango kuu la
kutoka ngomeni, na hivyo,
lilipokuwa kimya tu, kwa ishara
ya kuamka, na menzake yote
yakawa kimya! Masikini wee!
Mazimwi yote yakawa macho!
Kabla hayajataharuki na
kugundua kuwa alikuwepo mtu
ngomeni mwao na amechomoka
na kupenyeza getini wakati
mmoja wao akiamka, Kibwe
alipiga mbio kama mshale!
Alikimbia kuelekea mpakani
mwa nchi ile kama alivyoambiwa
na Bunga, akiazimia kupita katika
njia kati ya mashariki na
magharibi!
Walipoangalia mnarani na kukuta
upanga wa radi umetoweka,
mazimwi wote walitaharuki na
kuwa na hasira nyingi “Bila shaka
alikuwepo mtu humu ngomeni.
Afuatwe haraka kabla
hajaondoka na upanga wetu!”
Baada ya kusema hivyo, wote
walitimua mbio, huku vumbi
likitanda kwa heka heka hiyo, na
baadhi ya miti ikikatika kwa
vikumbo vyao! Alipoangalia
nyuma, kibwe aliona vumbi
lililotanda hadi mawinguni! “Leo
ndio hatima yangu mimi! Sijui
kwa nini nilifika huku!” Kibwe
alisema kwa majuto. Mazimwi
yalipoanza kumkaribia alihisi
miguu yake ikiwa inalegea mno
na kukosa nguvu kwa hofu! Moyo
wake ulienda kwa kasi mno!
Alikumbuka maneno ya Bunga.
“Wakikaribia kukufikia, watupie
kichupa kimoja kati ya vichupa
hivi vidogo vya mazingaombwe,
ili uwacheleweshe.” Kibwe
haraka alitoa kichupa kimoja na
kukitupia nyuma yake kwa yale
mazimwi. Lo! Mara ukatokea
msitu mnene kupita kiasi.
Mazimwi yalianza kuhangaika
kukata miti ya msitu ule uliozuka!
Kutokana na ukubwa wao, muda
si mrefu yalifaulu kukanyaga
kanyaga miti midogo na kuipiga
vikumbo miti mikubwa, na kisha
kuendelea kumkimbiza Kibwe,
ambaye alipoona hivyo, alirusha
kichupa cha pili, na mara
zikazuka mbigili nyingi mno
nyuma yake! Mazimwi
yaliumiaumia miguu yao, na
wengi wakaachwa nyuma. Kibwe
aliyaona baadhi ya mazimwi
yakizidi kumfuata, huku yeye
akiwa amechoka mno kukimbia.
Alipatwa na wasiwasi mkubwa,
“Sasa nikishindwa kukimbia na
madude hayo yanazidi kunifuata,
itakuwaje?” alijiuliza huku
akipapasa papasa kwenye fuko
lake, kutoa kichupa kingine
miongoni mwa vichupa
alivyopewa na Bunga. CHANZO:
https://
deusdeditmahunda.blogspot.com/
“Kwa kuwa mazimwi hupenda
sana kula ufuta, utakapo watupia
kichupa cha ufuta, wote wataketi
chini na kuanza kula, na hivyo
utapata nafasi ya kuwakimbia.”
Kibwe alikumbuka maneno hayo
ya Bunga! Mara moja akarusha
kichupa cha ufuta, na hapohapo
ukazuka mlima mkubwa wa
ufuta, na kuwafanya mazimwi
wote kuchanganyikiwa kwa
uchu! ”Aaaaa! Ufutaaaa! Ufuta
mtamuuuu! Nakula ufutaaa!”
Wakawa wanajisemesha maneno
hayo, kila mmoja akifurahia
chakula kile akipendacho, na
kumsahau kabisa Kibwe na
upanga wa radi! Waliketi chini na
kuanza kuushambulia ufuta!
Kibwe naye aliongeza kasi ya
mbio zake, akiruka mabonde na
kuangukia kwenye makorongo na
mito, misitu na nyika hadi
kwenye mpaka kuelekea
kaskazini ya mbali, kulikozizima
baridi ya ajabu, iliyowagandisha
watu na kuwageuza mawe! Pale
mpakani alisimama ghafla
akitahamaki na kuona moshi
mwingi uliotanda mbele yake, na
umbile la dude kubwa
lililofichwa na giza la moshi huo,
likiashiria kuwepo kwa jitu
kubwa likishughulika chini ya mti
mkubwa kupita kiasi! Muda wote
aliokuwa akiwakimbia wale
mazimwi, alimsahau kabisa
kiongozi wao, aliyeitwa Nyalile!
Kibwe alitaka kufahamu ule
moshi uliotanda vile ulitokana na
nini. Huku akihofu, lakini kwa
moyo wa kishujaa, taratibu
alisogea kule kulikotoka moshi
ule, akiangalia huku na kule kwa
wasiwasi hadi akafika karibu
kabisa na sehemu ile. Aliona
kuwa ule moshi ulitokea bondeni,
wakati yeye akiwa juu kidogo
kwenye uwanda. Aliposogea na
kukodoa macho yake vizuri ili
aweze kuona kama kwenye ule
utando wa moshi kulikuwa na
nini, alihisi kama vile anaangalia
umbile kubwa sana la jitu la
miraba minne, likishugulika
kufanya kazi fulani. Alipozidi
kutazama kwa makini aliona
kuwa lile halikuwa jitu la miraba
minne tu, bali lilikuwa ni kitu
kama mtu, na vilevile kama
mnyama, likishugulika kuandaa
chakula chake chini ya mti
mkubwa sana! Lo! Kumbe
alikuwa akiliangalia dude moja la
kutisha mno, lililokuwa na
manyoya mwili mzima, meno
marefu kama pembe za tembo
lakini yaliyojaa kinywa tele, na
kuanzia tumboni kwenda
miguuni, Kibwe alikuwa
akiangalia mwili wa binaadamu
mithili ya sokwe, isipokuwa
ulikuwa mkubwa kupita kiasi!
Uso wa dude hilo uliokuwa
kwenye kichwa kilicho fanana na
cha tembo, na katika paji la uso
wake, kulikuwa na jicho moja tu!
Naam, kwenye bonde
lililozungukwa na msitu wenye
miti mirefu kupita kiasi,
alikuwemo zimwi Nyalile, na juu
ya bonde hilo, alikuwepo Kibwe
akimwangalia! Utakisia
mwenyewe hali ya Kibwe
ilivyokuwa, mara alipotahamaki,
akagundua jinsi alivyokuwa
karibu kabisa na kubwa la
mazimwi wote, ambalo sifa zake
alizipata kutoka kwa Bunga!
“Mama yangu weee! Sasa kweli
niko hatarini!” Kibwe aliwaza.
Alijibanza kwenye miti mirefu
kabisa, huku jasho likimtoka, na
hofu iliongezeka kila sekunde,
wakati kijana yule alipoyaona
yale aliyoyaona mle bondeni!
Kwenye mafiga makubwa sana
kupita kiasi, Nyalile alikua
ameinjika jungu kubwa mno.
Wakati likichemka, alimkamata
ng’ombe mzima na kumnyonga
na kisha kumtumbukiza ndani ya
lile jungu. Pamoja na ng’ombe
huyo Nyalile alichukua kama
gunia mbili za mchele na kuutosa
kwenye lile jungu lililokuwa
likichemka kwa mchemko wa
kelele kubwa za ngurumo pale
msituni! Shughuli iliendelea na
muda wote lile zimwi lilikuwa
likichochea mapande ya miti
mikubwa mafigani, kukoleza
moto wake ili chakula kichemke
vizuri. Kitendo kile kilisababisha
moto mkubwa sana kuwaka ,
ulioambatana na moshi mnene,
ikawa kama msitu wote ulikuwa
unawaka moto!
Pale alipokuwa Kibwe,
ukilinganisha ukubwa wa miti
iliyomzunguka, alionekana kama
kidege kidogo mno. Aliwaza na
kukumbuka maneno ya Bunga,
kwamba akitaka kuvuka mpaka
kuelekea kaskazini ya mbali bila
kukamatwa na Nyalile, lazima
amliwaze kwa wimbo mzuri
utakaomburudisha na
kumfurahisha, kwani
atakapofanya hivyo lile zimwi
litadhani kuwa ni kidege
kinachoimba! Vilevile, Bunga
alimwambia kuwa lile jicho moja
la Nyalile halioni vizuri. Habari
yote hiyo ilimpa moyo Kibwe,
akahisi kuwa angeweza
kufanikiwa kulikwepa zimwi lile,
kama akijitahidi kufanya vile
alivyaelekezwa na Bunga. Lakini
imani yake ilipungua wakati lile
zimwi lilipomaliza kupika na
kisha kuketi chini ya mti
mkubwa, na kuanza kufuta jasho
lililotiririka kama mfereji wa
maji! Maajabu yale yalimfanya
Kibwe aduwae kabisa na hofu
yake kuongezeka upya! Hakujua
afanye nini! Je, akimbie?
Akimbilie wapi na njia ni ile
moja tu! au arudi alikotoka
walikokuwa wale mazimwi wala
ufuta? Aliona kuwa hapana budi
afanye alivyoambiwa na Bunga,
kwani hakuona njia nyingine!
Hivyo, kwa sauti iliyojaa
mawimbi kwa wingi wa hofu,
Kibwe alianza kuimba wimbo,
kwa maneno yaliyomjia katika
mawazo yake wakati ule…..!
Nyaalileee! Nyaalileee, Nyaali…
Nyaalileee, Nyaali……
Nyaalileeee! X2
Babu zimwi nipe motooo,
Nyaali Nyaalileee,
Niikapikie waanaanguuu,
Nyaalii Nyalileee,
Niipate viijunguuu namiii,
Nyaali nyaalileee,
Chaa wali naa cha mchuuzi ii,
Nyaali Nyaalileee!
Nyaaliileee! Nyaaliileee! Nyaalii
Nyaaliileee! Nyaalii Nyaalileee!
Kibwe alipomaliza wimbo wake
ule, alimchungulia zimwi Nyalile,
ili atambue hisia zake baada ya
kusikia ule wimbo. Alimuona
Nyalile akiinua kichwa na
kuangalia juu ya lile bonde
kwenye miti mingi mirefu
alikokuwa yeye Kibwe! Lo! Kijana
yule alianza kutetemeka na jasho
likazidi kutoka! Ni dhahiri Nyalile
hakuona kitu chochote huko,
kwanza kwa kuwa Kibwe alikuwa
ni mdogo sana na miti
iliyomficha ilikuwa ni mikubwa,
na pili, jicho moja la Nyalile
halikuwa likiona vema! Kibwe
akapata faraja kidogo,
alipomuona nyalile kiogo kidogo
akianza kutabasamu, na hatimae
kutoa kicheko cha aina yake na
halafu akisema;
“Weee kidege weee! Uko wapi?
Wimbo wako ni mzuri sana.
Hebu imba tena nisikiye!” Kibwe
alizidi kujibanza mitini, akihisi
wakati wowote ule, Nyalile
angeweza kumuona! Pamoja na
hofu yake, Kibwe alijitahidi
kurudia kuimba ule wimbo wa
Nyalile, ili kumfurahisha. Na
halafu lo! Kwa jinsi zimwi
alivyofurahia wimbo ule, alikariri
maneno katika kiitikio, “Chaa
walii naa cha mchuziii, Nyaalii
nyaaliileee………!” Na kisha weee!
Zimwi Nyalile liliinuka na
kujikung’uta, huku likizidi
kutabasamu kusikia jina lake
likitajwa, na pia likifurahia uzuri
wa kiitikio cha wimbo ule. Basi
ikawa tena ni:
“Chaa wali na cha mchuchiiii,
Nyaalii Nyaaliileee! Chaa walii na
cha mchuuchiii, Nyaliii
nyaaliileee…….!”
Alipokua akirudia rudia kiitikio
hicho, zimwi Nyalile alikuwa
akicheza hatua mojamoja,
akifuatisha wimbo ule, na
kuitikia vile alivyoelewa yeye!
Alivyonogewa zaidi, akawa
anapiga hatua za haraka haraka
na kuendelea na kiitikio chake;
na hatimae likatimka mbio huku
likiitikia;
“Chaa wali na cha mchuchiiii,
Nyaalii Nyaaliileee! Chaa walii na
cha mchuuchuuchii, Nyaliii
nyaaliileee a!
Moja kwa moja zimwi Nyalile
likayoyoma na wimbo wake huku
likitimua vumbi na kuangusha
miti kwa kuikumba lilipopiga
mbio, huku likiimba. Hiloooo!
Likayoyoma, msitu na nyika
mguu nipe, hadi likafika mbali
mno, bila kujielewa, likielekea
kusini mwa dunia! Kibwe naye,
haraka alishuka bondeni na bila
kupoteza muda…… akaanza
kupiga mbio bila kusimama, hadi
alipovuka ule mpaka
uliotofautisha eneo la kule
kunako kuchwa jua, ambako ni
magharibi ya dunia, na kaskazini
ya mbali ya dunia. Kibwe alikuwa
akielekea kwa mzee wa busara
aliyeelekezwa na Bunga, ili
kupata maelekezo kuhusu
maendeleo ya safari yake ya
ajabu.
MZEE WA BUSARA.
Safari yake ikamfikisha mahali
kati ya milima miwili mirefu,
kwenye mazingira mazuri sana,
yenye mianguko na maporomoko
ya maji, mahali palipojaaliwa
ardhi iliyorutubika mno. Kule,
Kibwe alikuta miti ya matunda ya
makomamanga iliyostawi vizuri
sana. Aliona ndege wakirukaruka
na kuimba kwa furaha juu ya miti
hiyo, ambayo chini yake vilipita
vijito venye maji safi na ya
baridi, vikitokea juu ya milima.
Kibwe alifarijika mno na hali ile,
hususan baada ya kuona maeneo
mengi yaliyoathirika na ukame,
na pia yaliyokabiliwa na uwazi
uliotokana na mashambulizi ya
majabali na ardhi, baada ya
kuteketezwa na wala mawe.
Alishangaa kuona jinsi sehemu
ile ndogo ilivyotofautiana na
maeneo yale ya awali!
Mara Kibwe akakumbuka!
CHANZO: https://
deusdeditmahunda.blogspot.com/
“Ahaaaaa! Sijui kwanini nilitaka
kusahau! Hapa ndipo Bunga
aliposema kuwa nitamkuta mzee
wa busara, ili nipate maelezo
kuhusu safari yangu! Sijui huyo
mzee wa busara ni nani? Lakini
nitafahamu baadae, kama kweli
hapa ndipo mahali penyewe.”
Hata hivyo kwa uchovu na njaa
aliyokuwa nayo, kijana yule
aliamua kuketi chini ya
mkomamanga , akawa anaokota
makomamanga yaliyoiva na
kudondoka chini, na kuanza kula.
Aliendelea kuketi chini ya ule mti
akipumzika, ili kupata nguvu
mpya. Alikuwa akitafakari
kuhusu hatima ya safari yake
wakati aliposikia mlio kama wa
pikipiki iliyokua ikianza
kuondoka! Alihisi kama mlio ule
ulikuwa ukitokea chini bondeni
hatua chache kutoka alipokuwa
ameketi, na alipotafakari kuhusu
mlio huo, akahisi kuwa ulikuwa
ni kama kikohozi cha jitu kubwa
sana! “Sijui ni kitu gani hicho
tena?” Kibwe aliwaza, na kwa
mara nyingine akaanza kupata
hofu. Alianza kujuta kwa nini
alikuwa kule mbali mno na
wazazi wake, ambao hata
hakukumbuka walikokuwa! Hata
hivyo, taratibu alinyanyuka na
kuanza kuangaza angaza,
akisogea bondeni uliposikika ule
mlio. Alitaka sana kufahamu ni
kitu gani kilichotoa mlio wa
labda tuseme….pikipiki? ……
Trekta……..?
Kila alipoangaza, hakuona kitu
chochote! Alisogea na kuzidi
kuchungulia chini bondeni, lakini
hakuona kitu licha ya ardhi ya
tope jeusi ambalo liliotesha
majani marefu, na pia
kulikuwepo lundo la kifusi
kilichoinuka mithili ya kilima
kidogo. Juu ya kilima hicho,
Kibwe aliona uyoga pori
umestawi vizuri sana. Taratibu
alisogea zaidi na kukichungulia
kile kilima, kuona kama
angeweza kushuka bondeni kwa
kurukia juu ya kilima hicho. Kwa
hiyo kutoka juu alikokuwa, kijana
yule alijirusha na kuangukia juu
ya hicho kilima. Hapo aliweza
kuangaza vema sehemu zote za
bondeni, ingawa bado alishindwa
kuona kitu chochote ambacho
kingeweza kutoa mlio wa
kustusha kama ule aliousikia
muda si mrefu uliopita.
Kibwe alishangaa sana, kwani
alikuwa na uhakika mkubwa
kuwa sauti aliyoisikia ilitokea
bondeni.
“Haya sasa ni maajabu makubwa!
Hivi ndio kusema kuwa labda
huo mlio sikuusikia? Au tuseme
haukutokea humu bondeni?”
Alijiuliza kwa mshangao mkubwa
juu ya muujiza ule wa aina yake.
Lakini kabla hajazidi kudadisi,
alisitushwa tena na mlio ule
usiofahamika, ila safari hii
alijikuta akirushwa hadi ng’ambo
kabisa juu ya bonde.
“Aaaaaaaaaaaaaaaaghh! Mama
yangu weeeeeeeeaaaagh…!” Alilia
kwa taharuki wakati alipokuwa
akielea hewani kabla ya
kuangukia kwenye matawi ya
mti, mbali na pale alipokuwa
awali.
Kijana aligwaya vibaya sana
akiwa ananing’inia juu ya mti
kama popo. Alikuwa akitweta na
kupumua kwa kasi, huku macho
yametoka pima, bila kufahamu
kilichomsibu! Halafu, kabla
hajatulia vema, kilisikika kitu
kama chafya ya nguvu
iliyoambatana na upepo mkali
kama wa gari moshi likifoka, na
hapohapo yeye alizolewa na huo
upepo na kujikuta akielea tena
hewani, na kisha akatupwa mbali
zaidi juu ya bonde kulikokuwa na
miti ya mikomamanga, akawa
amebanwa na matawi ya mmoja
kati ya mikomamanga ile!
Walisindikizwa na raia wa
Azarbajan kwa shangwe na
hoihoi hadi bandarini, na kule
wakaagana kwa upendo mkubwa,
na kisha merikebu ikaanza safari
nyingine ya ajabu ya Kibwe,
kumuokoa Bhaduri binti Sultani
Bashar wa Mashariki ya mbali ya
dunia!
Merikebu ya Mfalme KashKash
iliyoyoma usiku na mchana, na
hali ya bahari ilikuwa shwari
kabisa, kwa muda wote huo.
“Tuna bahati kubwa, kwani
mpaka sasa bado hali ni shwari
sana.” Hanga alimwambia
mwenzake Kibwe. “Kwa kawaida
mimi hutapika sana baharini,
lakini leo niko salama kabisa,”
Alieleza. Kibwe alimwambia
kuwa kwa kuwa bado safari ni
ndefu asijiamini sana. Kwa
maneno hayo, wote wawili
walicheka kwa pamoja. Meli hiyo
iliyowabeba vijana hao wawili,
wahudumu wakutosha wa meli
na manahodha, ilizidi kuyoyoma
hadi kufika katikati ya bahari,
halafu jambo la ajabu likatokea!
Ile meli ilisimama ghafla, kama
kwamba ilinasa mahali. Kibwe
alipomuuliza nahodha aliyekuwa
kwenye usukani ni nini
kilichotokea, akajibiwa kuwa
hakuelewa ni nini
kimeikwamisha meli yao.
“Huenda majani ya mwani
yamenasa kwenye pangaboi
linalozungusha maji huko chini
ya meli,” alisema nahodha.
Alipoambiwa hivyo kijana yule
alijitolea kwenda kuangalia kule
chini ya meli, ingawa wenzake
walimzuia sana.
“Ni hatari kwenda peke yako.
Labda tufuatane pamoja .” Hanga
na baadhi ya wahudumu wa
ndani ya meli walimwambia.
Ingawa Kibwe alipinga kufuatana
nao, lakini wenzake walishikilia
tu, hadi yule kijana akakubali
waende wote.
Naam, karibu watu wanne
walishuka na kuogelea kwenda
chini ya ile merikebu, kuangalia
hicho kilichonasa kwenye
pangaboi la meli yao. Wote
waliogelea, na Kibwe alikuwa
mbele zaidi, hivyo alitangulia
kuwasili pale lilipokuwa hilo
pangaboi. Lakini lo! Pangaboi
lenyewe lilikuwa limeshikiliwa
madhubuti na mtu mmoja
mwembamba kupita kiasi, na
mrefu kuliko utakavyofikiria!
Macho ya mtu yule yalikuwa
pembeni mwa sura yake,
iliyofanana na chura!
“Ahaa! Kumbe! Tunakutana tena
siyo?” Kibwe aliwaza, na bila
kupoteza muda, na haraka kama
mwendo wa mshale, kijana yule
alitoa rungu lililokuwa kwenye
mfuko alioubeba mgongoni, na
kulirusha kwa nguvu zake zote,
kumtupia yule mtu wa ajabu,
akilenga ule mkono ulioshikilia
lile panga boi! Kwa kishindo
kikubwa, lile rungu likamfikia
kwenye mkono wake huo, na
palepale akaachia lile panga boi,
na kama umeme, akapotelea
chini kabisa ya bahari!
Naam kwa mara nyingine, Kibwe
alikutana na mmoja kati ya jamii
ya majini wa bahari, jamaa zake
‘Makatta wa Makattani.’ Wakati
hayo yakitokea, wenzake wengine
waliokuwa wakija kuangalia chini
ya merikebu, walifika na
kumkosa yule jini wa bahari kwa
sekunde tu!
“Kwani kuna nini?” waliuliza, na
wakati huohuo, ile meli ikawa
inasogea mbele!
“Ilikuwa ni mwani tu, ulioshikilia
pangaboi! Nimekwisha uondoa ,
na ndio maana mnaona meli
inaondoka. Twendeni tuwahi!”
Kibwe alidanganya, akichelea
kuwatia hofu watu na hadithi za
majini wa bahari! Wote
wakarejea melini, na kuendelea
na safari.
Kibwe na wenzake waliendelea
na safari yao huko mashariki ya
katikati ya dunia, kwenye
majabali yaliyouzingira mto
mkubwa wa maji, mto Sakara,
ambako Bhaduri binti Sultani
kitinda mimba na mwana wa
saba wa Sultani Bashar, alikuwa
ameketi juu ya uwanda wa jabali
moja, akisubiri kutolewa kafara!
Kwa moyo wa ushujaa, na utiifu
kwa amri ya baba yake, mrembo
Bhaduri binti Sultani aliketi juu
ya jabali kwenye kiti kimoja
kizuri cha enzi, akiwa
amepambwa kwa sundusi za
hariri, mikufu, hereni na vikuku
vya dhahabu na vito vya
thamani, huku akinukia utuli
mchanganyiko kama udi, miski
na ambari, akisubiri wakati wake
wa kuchukuliwa na hicho
kitakachokuja kumchukua!
Kibwe na msafara wake ndani ya
merikebu yao ya fahari,
waliyoyoma kuelekea huko
mashariki ya katikati ya dunia,
wakati huo zikiwa zimebaki siku
chache tu, kuwasili mwisho wa
safari yao. Usiku mmoja
alipokuwa amelala na mwenzake
Hanga kwenye chumba chao,
Kibwe alimuota Bunga, akimpa
maelekezo ya safari yao hiyo.
“Lazima msafara huu usitishwe
haraka iwezekanavyo, mara tu
mtakapowasili kwenye bandari
yoyote ya jirani,” alisema Bunga.
Aliendelea kumwambia kuwa
itabidi wasubiri kwenye bandari
hiyo kwa siku mbili zaidi, kabla
ya kuanza tena safari yao. “Katika
muda huo mtakapo kuwa
mkisubiri kwenye bandari hiyo,
mtakuwa mmejinusuru na hatari
ya kupambana na mwamba wa
barafu majini, na pia
mtanusurika na tufani kubwa
itakayotokea mnamo saa ishirini
na nne zijazo.” Kibwe alimsikiliza
Bunga, aliyeonekana akielea
hewani kama ndege, na maneno
yake yakisikika kwa kukatika
katika, kwa sentensi
zisizokamilika!
Ndotoni Kibwe alikuwa
akimcheka Bunga, na
akimshangaa sana kwani kwa
mara hii alimuona ni wa ajabu
kabisa. Hakuamini maneno yake
hata kidogo, “Usinitanie mzee
Bunga! Unajua kwamba msafara
huu lazima uwahi nchini Shamsi
mashariki ya kati kati. Sasa
mbona unataka
kutuchelewesha?” Kibwe alianza
kulumbana na kile kijitu cha
ajabu.
“Tutaendelea tu……..na-
safa-”Lakini kabla hajamalizia
maneno yake, Kibwe akaona
ukuta uliokuwa mbele yake
ukipasuka, na maji mengi
yakianza kumwagika kama
mafuriko, na kumzoa Kibwe
kutoka pale alipokuwa, akajikuta
akitapatapa kujinusuru asizame!
Ingawa alikuwa anajitahidi
kuogelea, lakini alishindwa, na
hivyo akaanza kuzama---!
Akazama—akienda moja kwa
moja hadi chini kabisa ya dimbwi
la maji---! Pumzi zikamwishia
kabisa! Halafu ghafla, akajiibua
juu, na kutoa kichwa chake nje ya
dimbwi la maji, na kisha palepale
akasituka na kuamka, huku moyo
wake ukienda kwa kasi mno!
Aliinuka na kuketi kitako, akiwa
anapumua haraka haraka mno!
CHANZO: https://
deusdeditmahunda.blogspot.com/
Mwenzake Hanga aliyekuwa
karibu yake, naye aliamka na
kumuona Kibwe akiwa katika hali
isiyo ya kawaida. “Vipi kibwe,
mbona uko hivyo, umeota ndoto
mbaya nini?” Kimya! Kibwe
hakujibu kitu, bali alizidi
kupumua kwa haraka haraka,
huku macho yake yakiangalia
mbele zaidi ya pale alipokuwa
mwenzake, kama kwamba
hakumuona wala kumsikia
Hanga! Haraka Hanga alichukua
gilasi ya maji na kumpa
mwenzake huyo anywe, akihisi
huenda akajisikia nafuu kidogo.
”Hebu kunywa maji kidoga, labda
yatakusaidia.” Kibwe aliyapokea
yale maji bila kumwangalia
mwenzake, na akanywa funda
mbili, na halafu akajilaza
kitandani. “Unajisikiaje hivi sasa
Kibwe? Ni ndoto gani uliyoota?”
Hanga aliuliza, akiwa na wasiwasi
na jinsi alivyomuona mwenzake.
Kibwe alikohoa kidogo, na kisha
akaanza kuongea.
ITAENDELEA