SIMULIZI: JUMBA JEUSI

SIMULIZI: JUMBA JEUSI

STORY: JUMBA JEUSI
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

EPISODE 29.
ENDELEA.......

“Zote zinaweza kuwa ni sababu za msingi, kijana umefanya jambo hilo liwe nje ya mkono wangu lakini kabla ya kukufanyia maamuzi ya mwisho nataka kujua ni kwa namna gani umeweza kuniingiza kwenye kesi na waziri mpaka ayahitaji maisha yangu yaende? Anajua kama sababu ni wewe kulala na binti yangu?”

“Hapana hajui hilo ndiyo maana natakiwa kukuua kabla hajaweza kulijua hilo”
“Wewe hapo ndo unataka kuniua mimi?”
“Unahisi haiwezekani?”
“Nimekufunza mwenyewe, naijua kila sehemu ambayo ni dhaifu kwenye mwili wako, hauna hata nafasi ya kuusogelea mwili wangu. Umefanya jambo gani mpumbavu wewe?” aliongeza sauti na kuifanya kuwa kali.

“Nilitambua kwamba umejua natoka na binti yako hivyo ungekuja kunisababishia matatizo makubwa kwa hapo baadae hivyo nikaamua kukuwahi kwanza. Mimi nilikutana na baadhi ya wanasiasa wa upinzani kupitia watu wa mtaani ambao niliwalipa, watu hawa walienda pale kwa jina lako na utambulisho wako ambapo niliiba baadhi ya barua zako ambazo zina sahihi yako na kuzitumia kama ushahidi. Wana siasa hao baada ya kupata habari hiyo waliona ni fursa ya kumuangusha waziri lakini kabla ya yote kufanyika nikavujisha habari na kwake pia hivyo akajua na kuwafuata hao watu na kwa sababu yeye ni mkubwa na wanamuogopa, ikawalazimu kusema ukweli kwamba ni wewe ndiye uliwafuata.

Jambo hilo limempa hasira, hasira ambayo imetosha kufanya maamuzi ya mimi kukuua wewe bila kuacha ushahidi wowote ule. Hiyo ndiyo sababu ambayo ilinifanya leo niigize kama naondoka hapa kwa sababu nilijua kabisa kwamba kila mtu ataamini leo sitakuwepo hivyo kama wewe ukifa hakuna mtu hata mmoja ambaye atanihisi kwamba ni mimi nimehusika hivyo nitakuwa salama hata kwa mwanao ambaye naenda kumzalisha na nikijisikia nitamuoa maana hatajua na wewe hautakuwepo kuweza kumfumbua macho”
“Mtoto wa malaya wewe kijana”

“Malaya ni binti yako ambaye nilimtoa bikra mzee wa……” wakati anamalizia sentensi hiyo aliinama baada ya kuona vitu vinakuja kwa kasi, zilikuwa ni sindano zenye sumu. Aliinuka na kukutanishwa na mkuu wa kifua ambapo aliburuzika kidogo nyuma akanata kwa kukunja vidole vya mbele vya mguuni ambavyo vilikifanya kiatu kutulia kwenye smenti akasimama vyema kabisa.
“Nilijua utapaniki kwa sababu inauma kupigiwa mwanao na kijana ambaye humpendi au unaona hafai kuwa na mwanao. Umesema kwamba siwezi kukusogelea hata nguo zako ila sio kweli mzee, mimi sio mjinga mpaka kukubali kazi ya kukuua tena nikiwa mwenyewe. Kama kweli ningekuwa sikuwezi basi ningeikataa kazi na hata kama ningeifanya basi ningekuwa na watu zaidi ya mmoja”

“Umefanya nini mjinga wewe!?’’ mzee huyo aliongea huku akihisi kama mwili wake ulianza kuwa wa tofauti, alijigusa kwenye mdomo wake na kugundua kwamba alikuwa anavuja damu.
“Unaikumbuka ile dawa yako ya asili ambayo huwa unaitumia! Sasa ile dawa kabla ya kuondoka mimi nimetia sumu ndani yake, ni masaa mengi yamepita maana yake ile sumu ishaanza kufanya kazi hivyo itakulegeza. Mbali na hilo kuna jambo lingine ambalo haukuwahi kulijua kutoka kwangu mzee, nadhani nimekuambia kwamba mimi ni mtu ambaye huwa napenda kujiongeza kwenye kila jambo ambalo ninalifanya, vivyo hivyo na kwako niliamua kujiongeza pia. Wakati nakwambia kwamba nilikuwa nafanyia mazoezi chumbani nilikuwa namaanisha, binafsi baada ya kugundua kwamba hili ndilo eneo ambalo hata wewe huwa unafanyia mazoezi na ni watu kadhaa huwa wanaruhiwa kufika hapa, nilijiongeza kwa kutega kamera kwa sababu niliamini kwamba mwisho wetu unaweza usiwe mzuri.

Kupitia kamera hiyo, nilianza kujifunza mambo mengi kuhusu wewe kuanzia udhaifu wako, uimara wako uko wapi lakini pia niliweza kuona staili zako za siri za mapigano ambazo hata mimi mwanafunzi wako pendwa haukuwahi kunionyesha wala kuhitaji niweze kuzifahamu. Staili hizo niliweza kujifunza mimi mwenyewe, nilikuwa nautumia muda wa kuweza kupumzika kufanya mazoezi nikiwa ndani kwangu kwani niliamini hii siku ingekuja kuja kwa namna yoyote ile. Mimi leo kuja hapa sijaja kwa bahati mbaya, najua kila sehemu ambayo ungeweza kupitia. Kuna siri moja ambayo watu wengi walikuwa hawaijui kutoka kwako, siri ya kwamba kwenye mwili wako ulikuwa na nguvu za ajabu ambayo umeamua kuishi nazo miaka na miaka na jambo hilo pia niliweza kulitambua kupitia kamera yangu.


Baada ya kutambua hilo nilelewa kwamba licha ya kuweza kujifunza kila aina ya mazoezi bado nisingeweza kusimama na wewe na ndiyo sababu ambayo ilinifanya nikaamua kutumia sumu. Nilijua kwamba mwili wako ukiwa na sumu hautakuwa unaweza kuzitumia hizo nguvu zako kwa sababu kama ukijaribu kuzitumia basi utakuwa inaipasua mishipa ndani ya mwili wako jambo ambalo litafanya ujiue mwenyewe. Na ni simu ambayo imekufanya hata ule uwezo wa hisia zako kali kuweza kupotea ndiyo maana nimeweza kufika mpaka hapa ukiwa hauna taarifa kama nimeingia kwa zaidi ya dakika tano nikitazama ambacho unakifanya hapa. Kwahiyo kwa siku ya leo utahitajika kutumia zile nguvu zako za mazoezi tu na sio hizo za asili lakini pia utambue kwamba sumu imeanza kukuathiri tayari mpaka damu inakutoka mdomoni na kila muda utakavyo zidi kwenda ndivyo hali yako itakuwa hatari zaidi labda kama utawahi kupatiwa matibabu” maelezo marefu ya Jaden ndiyo ambayo yalihitimisha mzee huyo kujua kwamba kijana alikuwa amedhamiria kweli kuweza kuondoka na maisha yake. Alitabasamu kwa sababu kwenye maisha yake aliwahi kujiona kwamba yeye ni mtu mmoja makini, kuzidiwa na kijana tena ambaye alikuwa anazidi kumtengeneza mwenyewe kwake kilikuwa kama kichekesho.

“Sikuwahi kufikiria hata siku moja kwamba anaweza kutokea kijana wa kawaida kama wewe akaja kunifanyia mimi haya. Siku zote nimekuwa nikijiona kama mtu ambaye nipo makini kwa kila hatua ambayo nina ifanya ila sikuwa sahihi, kuna mahali nilifanya mahesabu yangu vibaya ambayo yanaenda kuniingiza matatizoni. Lakini hili jambo ilitakiwa Aimi aweze kujua na wafanyakazi wangu wote hivyo hakuna mahali bado unaenda”

“Aaaaaaah! Mzee wangu unataka ufe kwa aibu namna hiyo? Unahisi dunia itakuonaje hata kama utapona ikigundulika kwamba ulimkimbia mwanafunzi wako? Nani ataamani kwamba wewe ni yale masalia ya Samurai huku unaukimbia upanga na kwenda kulia lia mbele ya binti yako akusaidie? Naelewa vizuri historia ya Samurai, naelewa historia ya Japan lakini historia yako wewe pia. Kwenu heshima ni kitu kikubwa kuliko hata uhai hivyo unatakiwa ushike upanga wako na kujaribu kupambana na mimi hapa na sio kunikimbia. Ni muda wa wewe kuweza kujaribu bahati yako ya mwisho ili ukishindwa ufe kwa heshima kwamba ulikuwa unaipambania heshima yako kwa sababu siri zako zitazikwa na wewe hakuna mtu atakuja kujua kwamba wewe ulikuwa muuaji kama mimi ambavyo nipo kwa sasa. je utakimbia?”

“Moja kati ya makosa makubwa ambayo niliyafanya ni kukuona kama kijana wa kawaida na kama ningejua hili mapema basi nilitakiwa kuishi na wewe kwa namna nyingine”
“Kwa bahati mbaya ni kwamba muda haupo upande wako kwa sasa, muda sio rafiki kwani una dakika kadhaa za kuweza kuendelea kuishi”
“Nakuapia kijana, nitakuua na nitaishi halafu baada ya hapo nitarudi kwenye zile zama zangu hivyo naenda kumuua huyo mshenzi waziri na familia yake yote”
“Kama utakuwa na hiyo bahati ya kutoka hapa salama basi binafsi nakuruhusu ukafanye lolote ambalo unalitaka mwenyewe ila kumbuka tu huu sio usiku wangu wa mimi kuweza kufa, mpaka hapo nadhani unajua kabisa kwamba mtu ambaye anatakiwa kufa ni wewe na sio mimi” Shimamoto alichukizwa zaidi, kijana yule alikuwa anaongea bila heshima mbele yake na kumchukulia kama mtoto mwenzake, hali hiyo ndiyo ambao ilimtaka yeye kumfanyia mbaya Jaden.

Aliikunja mikono yake ambayo iliitikia kwa sauti ya mifupa ambayo ilikomaa, mikono hiyo aliikunjua lakini wakati huo alikuwa tayari anasogea kwa kujivuta mbele kuelekea mahali ambapo alikuwepo Jaden. Ujio wa mzee Shimamoto ulikuwa ni mkali ambao ulimtaka yeye kuwa makini zaidi kwa sababu vinginevyo alikuwa anakufa. Ule mkono mmoja wa kulia uliikosa shingo yake na kugusa kwenye ukuta ambapo ukuta ulibabuka kwa nguvu ambayo ilitumika. Mzee Shimamoto aligeuka kwa mguu mmoja mmoja ukiwa unaelea, Jaden alitumia mikono yake kuupangua ule mguu lakini ule mwingine ulikuwa unakuja kwa kasi ambapo ulitua kwenye mbavu yake akarudi nyuma kidogo.

Aliinua uso wake wakati ambao aliona vazi la mzee huyo linakuja kwa kuzunguka, hakuelewa mikono ipo sehemu gani hivyo kwenye kulikabili lile vazi alijikuta anapigwa kwenye shingo, alikohoa na kujinyoosha haraka kwani alitaka kumeza ulimi wake, mkono mwingine ulitua kwenye paji lake la uso hapo ndipo alitambua kwamba anafanya uzembe mwingi ambao ulikuwa unaweza kwenda na maisha yake. Aliipanga mikono yake na yeye huku akiwa anainyoosha shingo yake, mzee Shimamoto alidunda kwenye kasafu akajigeuza kama mshale, alimkosa Jaden miguu ikatua kwenye ukuta wakati huo aligeuka na mikono yake miguu ikiwa bado ukutani.

29 inafika mwisho.

FEBIANI BABUYA.
 
STORY: JUMBA JEUSI
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

EPISODE 30.
ENDELEA.......

Alikuwa ametegemea kumkita Jaden kwenye mbavu lakini haikuwa hivyo kwani mwanaume huyo alikuwa amerudi nyuma na alibetuka sarakasi ya mbele halafu akauyumbisha mguu mmoja ambao ulitua kwenye kwapa ya mzee huyo. Mguu ulikuwa umekomaa, ulimfanya mzee yule kupata maumivu makali hivyo akajigeuza na kutua akiwa anainyoosha kwapa yake kwa kukaza misuli! Alielewa kwamba aliyekuwa mbele yake hakuwa mtoto bali yale maneno yake ya kujinadi yalikuwa ya kweli kabisa. Alitembea miguu yake akiwa anaibana na kuiachia, alitua karibu na mguu wa Jaden, alimkosa mwanaume huyo ambaye alitua kwa sarakasi ya mbele.

Mzee Shimamoto aligeuka haraka na goti ambalo lilitua kwenye ardhi mpaka pakabonyea akamkosa Jaden ambaye wakati anarudi chini aliugeuza mguu wake wa kushoto ukatua kwenye shingo ya mzee huyu huku naye akimpatia maumivu kwenye mguu ambao ulimbamiza kwenye shingo yake. Ni kama ilikuwa ghafla kwake kwani kuguswa kwenye shingo kulimfanya kutapika damu kwa wingi kidogo, ile sumu bado ilikuwa inaendelea kufanya kazi, aliona sasa mambo yangeweza kuwa magumu kwa upande wake muda sio mrefu ukizingatia na aina ya mtu ambaye alikuwa anashindana naye, hakuonekana kuwa ligi ndogo, ulikuwa ni mlima mrefu kuweza kuudondosha hivyo alisogea ukutani akatoa panga mbili ambazo zilipambwa kwenye hilo eneo kama urithi wa Samurai.

Upanga mmoja aliurushia kwa Jaden na ule mmoja alibakiwa nao yeye kwenye mkono wake, aliona haikuwa sehemu salama kwake hivyo alitakiwa kujaribu njia nyingine ambayo ingemfanya kumalizia kazi yake kwa uharaka zaidi kisha aweze kuangalia namna ya kuweza kujisaidia kutoka kwenye hiyo sumu.
Upanga ulikuwa sehemu ya maisha yake, ndiyo silaha yake kubwa ambayo alikuwa akiitumia kwenye miaka yake yote hivyo aliuzungusha kwa kasi mpaka ukawa unaonekana kama kivuli tu kisha akautupa kwenda kwa jaden yeye mwenyewe akiwa anafuata kwa nyuma. Ule upanga mwanaume aliuona akaupisha ambapo ulitua kwenye ukuta ambao ulikuwa nyuma yake lakini Shimamoto alikuwa amefika, alikuwa anakuja kwa kujizungusha mithili ya tairi ya gari. Mwanaume alimuona vizuri, alimpisha kwa kujilaza ardhini kisha akanyanyuka ghafla akiwa anaurusha ule upanga ambao ulizama kwenye tumbo la Shimamoto hata yeye alimchana kwenye mkono wake.

Mzee huyo hakuwa sawa, alisimama lakini alikuwa anaonekana kuwa na maumivu makali ndani yake kwa sababu kwa wakati huo alikuwa anashindana na maumivu ya aina mbili, ya sumu lakini na huo upanga ambao ulimtoboa kwani hakuwa na uwezo hata wa kuukaza mwili tena, mishipa ilikuwa inakatika hivyo mwili ulikuwa dhaifu kwa wakati huo na kwa eneo kama hilo ambalo alikuwepo hapo, mazingira hayakuwa rafiki kwake. Alisonya na kujianza tena kutumia staili zake ambazo ndizo zilidaiwa kuwa za siri, alizunguka na ule upanga akajikunja kama ng’e na baada ya kutoka pale mwili wake ulikuwa unatembea zigzaga kama umesambaratishwa, yaani alitumia eneo kubwa kujitawanya wakati anakuja kwa kasi.

Jaden alimuona na alikuwa anaelewa kile ambacho mzee yule alikuwa anajaribu kuweza kukifanya pale, aliyafumba macho yake na kuyafumbua kwa kasi wakati ambao mzee huyo alikuwa ameruhusu upanga wake kwenda kwa bwana huyo. Yeye aliinama kwa kasi kama upepo unapita na kuzungukia upande wa pili ambapo aliurudisha ule upanga kwa nyuma tena. Ule muda ambao alizungukia pembeni ni kwamba alimkata kata mzee yule na kuligawanya tumbo lake kwenda ubavuni kisha wakati anaugeuza upanga huo aliuzamisha mgongoni ukatokezea mpaka tumboni. Hakumpa ruhusa ya kupumua kwa sababu alimzoa mzee huyo na mguu wake akiwa bado hajageuka na wakati huo mzee upanga wake ulinasa ukutani kwani alitumia nguvu kubwa kuweza kuurusha akiamini ulikuwa unatua kwenye mwili wa Jaden. Baada ya kumzoea mwanaume aligeuka na double kick ambayo ilitua kwenye kiuno kikateguka vibaya na mzee huyo akabamizwa kwenye ukuta akatua chini huku akiwa anatokwa na damu nyingi na kuhema kwa taabu.

“Wewe shetani muda wako unakuja, utakufa vibaya kuliko mwanadamu yeyote yule’
“Nitaona kama muda huo utakuja mzee wangu ila hapa naona kwamba wewe ndiye mtu ambaye unakufa vibaya” Jaden aliongea akiwa ameutupa ule upanga na kujifuta damu sehemu ambayo aliguswa na upanga huku akiwa anamsogelea mzee yule akiwa kwenye hatua zake za mwisho kabisa za maisha. Akiwa hajamfikia kabisa mzee huyo, alihisi kuna jambo halipo sawa, kuna mtu alikuwa ameongezeka hapo na mtu huyo alikuwa ameurusha upanga kwa nguvu kubwa ukamkosa kwa sababu aliwahi kugeuka akafanikiwa kuuona.

Ni mlinzi wa karibu wa mzee Shimamoto ndiye ambaye alishtukia kwamba kuna jambo halikuwa sawa kwa bosi wake baada ya kukaa kwa muda mrefu bila kujitokeza. Hali ambayo alimkuta nayo bosi wake ilikuwa inatisha na hakuamini kwamba mtu ambaye alifanya yale yote ni yule ambaye mzee huyo alijitolea kumsaidia! “Usiwaamini wanadamu” kauli hiyo ilimjia kichwani akiwa hana uwezo wa kuurudisha muda nyuma zaidi ya kulipa kisasi kwa ajili ya bosi wake.

Jaden hakutegemea kabisa kama anaweza kukutana na huyo mwanaume hayo maeneo kwa nyakati hizo. Mlinzi mkuu wa Shimamoto hakuwa anajua kuzungumza lugha ya kiingereza hivyo wawili hao walitakiwa kuzungumza zaidi kwa lugha ya mikono, lugha ambayo huwa inawakutanisha mabingwa kwenye sanaa ya mapigano. Uso wake mlinzi huyo ulionyesha kabisa kwamba alikuwa amechukizwa na jambo lile hivyo alijizoa mzima mzima kwenda kwa Jaden ambaye alikuwa tayari kumsubiria mwanaume huyo akiwa peku kabisa mguuni na mwilini mwake alivaa gauni la kuwakilisha tamaduni zao.

Ujio wake ulikuwa ni wa nguvu na kasi kubwa ambao ulijumuika na ghadhabu, Jaden alikuwa anaipimia ile kasi wakati inakuja kwake hivyo alirudi nyuma kiasi akainamia nyuma akiwa anashika ukuta kidogo kupata balansi nzuri. Mguu ulimpita na kumomonyoa sehemu ndogo ya ukuta, alijivuta ili kwenda pembeni ndipo akakutana na kiganja shingoni, alifika kwa kuyumba huku akiwa anajinyonga, ule mkono ambao ulikita kwenye shingo yake ulikuwa umekomaa. Sasa na yeye aliipanga mikono yake kwani hakukuwa na mazungumzo mengine, yule mlinzi hakuwa na muda wa kusubiri wala kuuliza zaidi ya kushambulia nyakati zote.

Alikuwa akizunguka na lile gauni lake wakati ambao hata mikono yake ilikuwa inakusanywa na kugawanyishwa kwa pamoja, alimfikia Jaden, ngumi nne zilirushwa lakini mbili zilizuiwa na mbili zilitua kwenye mbavu na kifuani. Jaden alishangaa namna mwanaume huyo alivyokuwa anakuja tu bila hata kumpa nafasi ya kupumua. Alizunguka kurudi nyuma kwa mfano wa kimbunga, akiwa anamsoma mlinzi yule wakati anakuja, alimsubiri amfikie ndipo alijifanya kama analala upande wa ukutani naye mlinzi yule akaingia kwenye mtego. Alinyanyuka na kugeuka ambapo alitua juu ya kichwa cha yule mlinzi, alijiviringisha kutaka kumtoa yule bwana kichwani akaishia kutua nyuma yake ambapo alimpa nafasi ya kugeuka.

Mlinzi yule baada ya kugeuka alikutana na ngumi mithili ya tani kadhaa za mawe, alihema na kutema damu kwa wakati mmoja, sasa ilikuwa zamu yake kuweza kulipa yale mashambulizi ambayo alikuwa ameyafanya tangu mwanzo. Ile ngumi ilikuwa nzito hivyo ilimuathiri, alihitaji kuzikunja ngumi zake ila alibaki ameduwaa baada ya kuona Jaden anazitumia zile staili za siri ambazo ni watu kadhaa walikuwa nazo, hata yeye kama mlinzi alifanikiwa kuzisoma tu ila hata siku moja hakuwahi kufundishwa. Akiwa kwenye mshangao alihisi kivuli kinakuja kwake, ni Jaden alikuwa anahesabu hatua akiwa amejiachia anakuja kwa bwana huyo.

Wakati anamfikia Jaden alihisi tumbo linamuwasha lakini wakati huo yeye mwenyewe alikilainisha kifua cha mlinzi huyo baada ya kumpiga na ngumi zote mbili zikiwa zimeunganishwa, kililainika kama mtori na mwanaume huyo akapiga goti akiwa anamwaga damu kwa wingi. Jaden naye alipo jiangalia tumboni kwake, aligundua kwamba alikuwa ametobolewa na kisu hivyo wakati anashambulia mwanaume yule hakumpakia poda bali naye alimuwajibisha ipasavyo. Alisogea hatua kadhaa akaokota upanga na kuanza kumsogelea mwanaume yule ambaye baada ya kuona ule upanga alijitahidi kunyanyuka ili aendelee na mapambano japo muda haukuwa kwake kwani hali yake tayari ilikuwa mbaya.

Jaden alitishia kurusha ule upanga ikamlazimu yule mlinzi kunyanyuka akiwa bado hayupo sawa, aliikunja mikono yake na kuukaza mwili huku akiwa anaonekana kabisa kwamba anateseka kwani alikuwa anaendelea kutapika damu kila alipo vikaza viungo vyake ila hakuonekana kuwa na namna nyingine. Jaden alimsogelea kwa nguvu kubwa, nguvu ambayo ilimfanya mlinzi yule kuhitaji kujisogeza nyuma ili apate balansi nzuri ya kuweza kushambulia ila haikuwezekana, alirusha mkono wake mmoja na kuishia kwenye miguno mikali kwani alidodosha kiganja cha mkono ambacho kilikutana na upanga. Alishuka na kupiga goti shingo yake ikiwa inamwaga damu, wakati anakatwa kwenye viganja vyake ule upanga ulizungusha na kupita kwenye shingo yake hivyo mpaka wakati huo alikuwa anahesabu sekunde tu za kuendelea kuhisi uwepo wake duniani.

Jaden baada ya kuhakikisha zoezi hilo limeenda vizuri ndipo alishtuka, alishtuka baada ya hisia za mwili wake kumpatia taarifa kwamba kulikuwa na uwezekano wa mtu mwingine kuongezeka kwenye eneo hilo hivyo aliutupa upanga na kukimbilia pale ambapo alikuwepo mwalimu wake Shimamoto. Shimamoto alishuhudia yote ambayo Jaden aliyatenda kwa mlinzi wake ila wakati huo hakuwa hata na uwezo wa kuzungumza zaidi ya kubaki ametumbua macho tu.
30 inafika mwisho.

FEBIANI BABUYA.
 
STORY: JUMBA JEUSI
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

EPISODE 31.
ENDELEA.......

“Mara ya kwanza kabisa ni bora ungechagua kuwa dhaifu ukaita msaada wa walinzi mzee wangu, nenda na safari yako tutakuja kuonana huko siku moja. Binti yako hakupaswa kukukuta kwenye hali kama hii na hivi sasa atajua kwamba ni mlinzi wako amekuua kisha nami nikamuua mlinzi wako, kwa maana hiyo mtu pekee ambaye ataenda kumuamini kwenye maisha yake ni mimi hapa na ikiwezekana kuna siku nitahama naye kabisa huku kwenda nyumbani Tanzania hivyo hakutakuwa na kumbukumbu za kizazi chako tena” Jaden aliongea akionekana kabisa kwamba alikuwa anamng’ong’a mzee Shimamoto ambaye alikuwa anasikia tu ila hakuwa na uwezo wa kuongea. Mzee huyo alikuwa anazungumza kwa ishara tu kwani alionekana kuwa na hasira ambazo zilijionyesha kwa namna alivyokuwa anaukunja uso wake ila hakuwa na jambo la kuweza kufanya.

Na muda huo ndipo kweli kama ambavyo Jaden alipata hisia, binti wa Shimamoto yaani Aimi alikuwa anaingia eneo hilo, kwenye mkono wake alikuwa ameshika kikombe cha kahawa. Kikombe kilimponyoka baada ya kuona baba yake yupo kwenye hali kama ile, alibaki ameduwaa kama sekunde thelathini akiwa haelewi kama anaota au ni kweli, na kama ilikuwa ni kweli basi hakuwa anajua kwamba anatakiwa kuchukua hatua gani kwenye jambo la kutisha kama lile. Baba yake alikuwa anaona kwa mbali, alinyoosha mkono kwa binti yake huku mdomo wake ukiwa kama unahitaji kuongea jambo lakini haukuweza na hatimae mkono wake ulilegea, safari yake ya kwenda kwenye shimo la futi sita ilikuwa imewadia.

Aimi bado alibaki ameduwaa, aligeukia upande mwingine ambapo alikutana na damu za kutosha huku mlinzi mkuu wa baba yake, mwili wake ukiwa umelala hauna uhai. Aliyarudisha macho yake kwa mpenzi wake ambaye alikuwa amemshikilia baba yake bado naye akiwa anavuja damu mkononi na kwenye tumbo lake! Bado hakuwa anaelewa kwamba ni jambo gani limetokea eneo lile.
“Nini kimetokea hapa?” aliuliza macho yake yote yakiwa kwa mpenzi wake maana ndiye mtu pekee aliyekutwa eneo lile.

“Mimi leo sikuwepo nadhani una hizi taarifa, mzee alikuwa amenituma Tokyo kwa moja ya marafiki zake ambao ndio ilikuwa sababu ya mimi kuwepo hapa. Nilipofika kule shida ambayo nilitakiwa kwenda kuitatua kwa zaidi ya siku mbili tumefanikiwa kuitatua ndani ya masaa kadhaa tu kwa sababu mhusika alikuwa Tokyo hivyo ikawa rahisi. Kwa maana hiyo ikanilazimu mimi kurudi tena nyumbani mapema na….’’ mwanaume alikuwa ameyapanga maelezo yake kimkakati ila alikatishwa akiwa anazungumza.
“Namanaanisha nini kimetokea humu ndani, sijauliza kuhusu ulikotoka na sijali kuhusu hilo’’

‘Kuna mahusiano ya moja kwa moja ndiyo maana nimeanzia hapa. Jambo hilo limenifanya mimi nirudi bila taarifa. Sasa maagizo ya mzee ilikuwa ni kwamba nikirudi tu nikutane naye kwanza, hivyo baada tu ya mimi kufika hapa nilienda kwenye ofisi yake kukutana naye ila sijampata. Tangu siku ya kwanza aliwahi kunionyesha hii sehemu kwa sababu ndiyo tulikuwa tunaitumia kwa ajili ya mazoezi na kwa maelezo yake ni kwamba ikitokea siku nimemkosa kwenye ofisi yake basi nitakuwa nampata eneo hili, kwa maana hiyo baada tu ya kuweza kufika nilikuwa na uhakika kwamba nitampata huku ili apate taarifa kwamba kijana wake nimerudi. Kwa bahati mbaya wakati nakaribia hili eneo nilihisi kama kuna sauti za panga zinasikika ikanilazimu kukimbia ili niwahi na baada ya kufika hapa ndipo nimemkuta yeye akiwa napigana na mlinzi wake, jambo hili limenishtua lakini wakati nafika tu ndipo mzee alikuwa anajeruhiwa vibaya namna hii. Hali hiyo ikanilazimu kuingilia kati ili kuweza kuyanusuru maisha yake ila nahisi tayari alikuwa amejeruhiwa vibaya. Kwa sababu mlinzi wake alikuwa hawezi kuzungumza kiingereza hatukuweza kuelewana maana ningemhoji kujua sababu ya mzee kuwa hivi, baada ya kuona nimejua ukweli kwamba yeye ndiye alikuwa amefanya haya ni kwamba hakutaka kabisa mimi nitoke nikiwa hai hapa ndipo akaanza kunishambulia kwa nguvu wakati ambao mimi nilihitaji kuwahi kumtoa mzee hapa tuone kama tunaweza kuyaokoa maisha yake na kwenye mashambulizi yetu ndiyo yametokea haya ambayo unayaona hapa” aliweka kituo mwanaume kwa uongo wake ambao alikuwa anautoa kwa hisia kali.

Yale maelezo ndiyo yalimzindua Aimi na kwenda kuukumbatia mwili wa baba yake huku akiwa analia kwa sauti kiasi kwamba muda mfupi walinzi wengi ndani ya hilo jengo walianza kufika humo ndani Jaden akiwa amejikausha kama naye ni mhanga vile vile kwani alionyesha kila dalili za kuumia kumpoteza mwalimu wake.
“Kabla ya kufa ameniambia mambo makubwa mawili. Jambo la kwanza ni kwamba ANAKUPENDA SANA lakini jambo la pili amenitaka mimi nikulinde wewe Aimi kwa maisha yangu yote, hii itakuwa kama asante kwangu kwa kuweza kunilea kwa huu muda wote kama mwanae wa kumzaa” alizidi kumtoa machozi bibie ambaye aliendelea kulia kwa maumivu huku akimkumbatia Jayden.

“Ndiye pekee ambaye nilibakiwa naye mimi, nitaenda wapi, nitakuwa mgeni wa nani kwenye huu ulimwengu”
“Usiseme hivyo kwa sababu tayari unaye mimi ambaye nipo tayari kuyatoa hata maisha yangu kwa ajili yako. Unajua kabisa ni kiasi gani nakuhitaji kwenye maisha yangu na kukupenda”
“Usije ukanikimbia na wewe Jaden tafadhali”
“Mimi nitaenda na wewe kwenye kila pembe ya dunia ambayo mimi nitaenda kwa sababu nakupenda. Ila naomba unisamehe kwa sababu kufa kwa mzee sababu ni mimi, kama ningewahi zaidi ya hapa nilikuwa ninaweza kuyaokoa maisha yake”

“Sio kosa lako hata hivi umejitahidi, nashukuru umetoa damu kwa ajili ya kuyapigania maisha ya baba yangu” walikumbatiana wawili hao ambao walionekana kabisa kwamba walikuwa ndani ya mahaba mazito.
Baada ya hilo kupita mwili wa Shimamoto ulipimwa na kugundulika kwamba ulikuwa na sumu kali ndani yake, wote waliamini kwamba lazima ndiyo ilikuwa sababu ambayo ilimfanya mlinzi wake kuwa na kiburi cha kutaka kumuua mzee huyo kwani kama angekuwa timamu asinge thubutu kufanya jambo hilo. Walihitimisha kwamba mlinzi wake alihitaji kumuua mzee huyo ili hiyo miliki ibaki kwenye mikono yake yeye ili afanye yale ambayo angeyataka mwenyewe jambo ambalo halikuwa kweli.

Msiba wake ulikuwa maarufu, ulihudhuriwa na viongozi wakubwa wa ngazi za juu akiwepo waziri mwenyewe wa mambo ya nje wa Japan ambaye alidai kwamba alikuwa anamheshimu Samurai huyo na walijuana miaka ya zamani huku ile siri ya yule Samurai ikibaki kuwa siri kama ambavyo ilikuwa mwanzo. Sasa baada ya mzee kufa binti yake ndiye ambaye alitakiwa kuwa mrithi wake ila alitakiwa kuwa na mume ambaye angesimama kama kiongozi, jambo hilo lilitakiwa kumlazimu yeye kuolewa na Mjapan mwenzake lakini aligoma kabisa, kugoma kwake ni kwa sababu alikuwa anajua ana mtu ambaye ni mweusi wangemkataa kwakuwa wangeenda nje na tamaduni.

Yeye alihitaji kuwa karibu kabisa na Jaden na baadae waje kuoana hivyo Jaden ndiye ambaye alisimamia ile nafasi ya kuweza kusimama kama mume pale japo hakukuwa na ndoa ya kuhalalisha hilo. Maisha yao yalikuwa ya furaha na walipendana haswa mpaka pale ambapo simu ilipigwa kutoka kwa mheshiwa raisi wa Tanzania, bwana Darian Julius. Simu ilipigwa Tokyo hivyo ikamlazimu huyo ambaye amepigiwa simu kusafiri usiku huo huo mpaka ndani ya jiji la Akita ambapo usiku huo Jaden hakuwa amelala, alikuwa milimani kuteleza kwenye barafu huku akiwa anafanya mazoezi makali ambayo yalimfanya asilione hata barafu lenyewe kwakuwa alikuwa anaona kama mambo yapo kawaida tu. Akiwa huko alipokea ugeni wa mtu ambaye alikuwa anamfahamu, alikuwa ni moja ya vijana wake ambao walikuwa wanaishi Tokyo.

‘Bosi anakuhitaji nyumbani”
“Lini?”
“Kesho”
“Kwamba bado hawajampata?”
“Inaonekana limekuwa zoezi gumu ndiyo maana anakuhitaji mwenyewe’
“Oooooh shiiiit!’’ alijikuta anatukana kwa sauti kwani alitakiwa kumkimbia mwanamke ambaye alikuwa amempenda na kumuaminisha kwamba yeye ni wake.
“Kwahiyo tunaondoka muda huu bosi?”
“No, wewe nenda mimi nitakuja asubuhi ila hakikisha unaandaa tiketi za watu wawili”
“Watu wawili?”
“Ndiyo kuna mwanamke ambaye anaitwa Aimi Shimamoto ila kwenye tiketi weka jina la Kitanzania kuna uwezekano nikaondoka naye”
“Huu ni uamuzi mbaya unaufanya, yule mwanamke ulitakiwa kumtumia tu na sio kuanza kumpenda”

“Fanya niliyo kwambia”
“Jaden, bosi sina imani kama atalifurahia hili jambo”
“Niamini mimi nipo makini kwenye kazi yangu kuliko mtu yeyote yule ila fanya yale ambayo nimekwambia”
“Sawa” kijana wake aliondoka na wakati huo yeye aliketi kwanza akifikiria namna ya kwenda kumuanza mwanamke huyo ili aweze kuikimbia asili yake na kukubali kurudi naye Tanzania, kwenye ardhi yake ya nyumbani ambako alikuwa anahitajika haraka kutokana na umuhimu wa kazi ambayo ilikuwa mbele yao.

31 inafika mwisho.

FEBIANI BABUYA.
 
STORY: JUMBA JEUSI
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

EPISODE 32.
ENDELEA.......


ZYRA.
“Maisha yangu mimi ni kama hadithi ya kutungwa ama ya kufikirika, hayana uhalisia, hayana ukweli kwa sababu nimeishi maisha ambayo naweza kusema kwamba sio yangu ila nilifanya haya yote ili nipate kuishi. Sehemu kubwa ya maisha ya mwanadamu imejawa na hofu na hofu ndiyo ambayo huwa inawafanya watu washindwe kuishi kwa amani, furaha na hata kuhisi lengo la kuja duniani ni kuteseka na sio kufurahia nyakati zao.

Hofu imewafanya watu wengi kupoteza tumaini hali ambayo huwa inawafanya watu kujikuta kwenye mazingira ambayo hawakuyatarajia ama kufanya vitu ambavyo hata wao hawakuwahi kuvidhania kwamba wanaweza kuvifanya. Hiyo ni tafsiri sahihi ya maisha yangu pia ila nimewazungumzia na watu wengine kwa sababu nimeishi nao na nimeona jinsi ambavyo wanayapeleka maisha yao na uhalisia ni kwamba hali ni ngumu kuliko serikali na wana siasa wanavyo wadanganya watu hususani kwenye mitandao ya kijamii.

Mimi nimedanganya mambo mengi kwenye historia yangu, maisha ambayo watu wanayajua kama mwanamke maarufu kwenye hili taifa yametawaliwa na simulizi ya uongo na kwa sababu wanaambiwa kile ambacho wanataka kukisikia basi hakuna hata mmoja ambaye amewahi kutamani japo kufuatilia jambo hilo ili aweze kuupata ukweli halisi wa mambo upoje. Mimi kuingia kwenye maisha ya Bazoka haikuwa bahati mbaya, haikuwa mapenzi ya kukutana, kutongozana na kisha kupendana kama watu wengine ambavyo huwa wanafanya. Haimaanishi kwamba yule bwana mimi sikumpenda kabisa kwa sababu nikisema hivyo nitakuwa nadanganya kwani hata mimi ni mwanadamu japo huenda nilisema sijawahi kumpenda, kwa hilo nitakuwa naudanganya moyo wangu mwenyewe.

Mimi ni binti ambaye nilizaliwa kwa mwanamke aliyekuwa anauza mgahawa, mgahawa ambao ulikuwa unafanya mwanamke yule anakula na kushiba lakini haukuwa mgahawa wa kumfanya atosheleze kupata mahitaji yake ya msingi hivyo bado kuna mambo mengi alikuwa anayakosa na ndiyo maana akawa mtu wa kujiongeza. Mama yangu naweza kusema kwa lugha rahisi kwamba alikuwa malaya kwa sababu kwa mwanaume ambaye angeahidi kumpatia pesa nzuri basi ilikuwa ni lazima amvulie nguo ili kuongeza mtaji wa biashara yake lakini pia kupata mahitaji yake mengine kama mwanamke. Hili halifanyi mama yangu tu na wala sio kwa wauza migahawa tu bali kwa wanawake wengi ambao wana hizi biashara ndogo ndogo huwa wanayafanya sana haya ila kuyajua wewe ukiwa nao mbali ni ngumu.

Sasa kwenye hilo zoezi lake la kujipatia kipato ndipo alikutana na mwanaume mmoja ambaye kwa maelezo yake ni kwamba alikuwa mfanya biashara aliyekuwa anapita na eneo hilo alikaa kwa wiki moja tu pekee. Mwanaume huyo ndiye ambaye anadaiwa kwamba alimpatia mimba na baada ya wiki moja yule bwana alipotea jumla na hakuwahi kurudi tena mpaka siku mama yangu anapoteza pumzi yake. Mimi simlaumu huyo bwana ambaye kwa asili ndiye baba yangu kwa sababu hakuwa anajua kama mama ana mimba, yeye alipita tu na wiki hiyo moja aliamua kujipa burudani kwa mwanamke mrembo ambayo alikuwa anapatikana kwa bei rahisi na baada ya hapo aliendelea na safari zake akiwa hajui kabisa kama aliacha mwanamke mwenye mimba nyuma kwa sababu kama angejua hilo huenda angerudi lakini kuondoka bila kurudi maana yake hakuwa na habari kabisa kama kulikuwa na mtoto wake anazaliwa nyuma. Ni mwanaume gani angerudi kumtafuta mwanamke malaya wakati dunia ina wanawake wengi wazuri zaidi ya huyo mwanamke? Labda kama angejua kuna mtoto nyuma.

Yeye lazima alifikiria kwamba kama yeye alifika tu ndani ya siku moja akamvua nguo kwa wiki nzima! Vipi kwa wanaume wengine ambao wanaishi naye karibu na wanaweza kumpata kila siku? Maana yake yeye alipata burudani tu na kuweza kutoweka jumla na kuendelea na maisha yake mengine na baada wiki tatu baadae ndipo mama alipo gundua kwamba alikuwa mjamzito. Alijaribu kuutoa lakini ilishindikana, alipambana mpaka mwisho wa siku akaambiwa kwamba anaweza kupoteza maisha yake hivyo alitakiwa kukubaliana na kila hali ambayo ilikuwa inamtokea kwa wakati ule na hiyo ikawa ni sababu ya mimi hapa kuzaliwa.

Mama yangu alidai kwamba alijaribu kusubiri akiamini yule bwana angerudi lakini haikuwa hivyo, wiki ziliisha, miezi ilienda na hatimae miaka ikakatika na hakukuwa na dalili za bwana huyo kurudi na kwa bahati mbaya hakuwa hata na mawasiliano naye ya kudumu kwa sababu namba ambayo alimpatia haikuwahi kupatikana tena. Simlaumu baba yangu na wala simlaumu mama yangu kwa sababu kila mtu alifanya kinacho takiwa kufanyika ili aweze kuishi. Haya yote nilikuja kuyajua siku ambayo mama yangu alikuwa kitandani akiwa anaivuta pumzi yake ya mwisho na akinipa wosia ambao bila shaka nilijua kabisa kwamba ilikuwa ni mara yangu ya mwisho kuongea na mwanamke yule ambaye nilimpenda kuliko kitu chochote hapa duniani.

Mama yangu aliniusia kwamba haya maisha ni tofauti na yanavyo onekana, maisha kwa mtazamo ni marahisi ila kwenye uhalisia maisha ni magumu kwani kuna wakati inakulazimu ufanye mambo ambayo hata wewe unayaona kabisa kwamba sio sawa ila unafanya hivyo kwa sababu hauna namna na ingefika wakati ambao hata mimi nilikuwa naenda kufanya maamuzi hayo. Aliniomba msamaha kwa kutoweka akiwa hana jambo lolote la maana ambalo alinipatia mimi mwanae wa pekee kama urithi, zawadi pekee ambayo alikuwa amenipatia ni ya maisha ya kujitahidi kunisomesha mpaka pale ambapo aliona uwezo wake umeishia.

Mama yangu alikufa mbele yangu nikiwa nipo mwaka wa kwanza chuo, ni ile ile biashara ya mgahawa na kujiuza kwake kwa kujifanya ana mahusiano na wanaume tofauti tofauti ndivyo ambavyo vilinifikisha pale ambapo mimi nilikuwepo hivyo ningeanzia wapi kumpa lawama wakati yale mambo ya kishenzi ndiyo yamenilea! Nimejifunza kutohukumu sehemu ambayo hata ningekuwa mimi ningefanya vile vile. Sasa kwa bahati mbaya kwangu ni kwamba wakati mama anakufa ndio wakati ambao naweza kusema kwamba nilikuwa namhitaji zaidi ili niweze kwenda na masomo yangu lakini pia ndio wakati ambao maisha yangu yalikuwa yamepanda bei yaani yamekuwa ya gharama na kama mwanamke nilikuwa nahitaji vitu vingi.

Anakufa huku nikiwa sina kitu na hata ule mgahawa wa kubahatisha nisingeweza kuuendesha kwani muda mwingi nilitakiwa niwe nasoma. Ule ulikuwa wakati ambao kwa mara ya kwanza niliwaza hata kuyabeba maisha yangu mwenyewe japo mimi ni miongoni mwa wanadamu wachache ambao wanayapenda sana maisha yao. Maisha yalianza kuwa magumu, pesa zilikuwa zinahitajika nikajikuta hata chuo naanza kwenda kwa kubahatisha. Ilitakiwa nitafute pesa ya chuo, kula, mavazi, kodi na matumizi ya kawaida huku pia nikitakiwa niwe nasoma kwa bidii na ukizingatia sikuwa na kitu cha kunisaidia mimi kukamilisha yote hayo na ndipo nikaingiwa na msongo wa mawazo.

Ule msongo wa mawazo nilikuwa nautumia kuweza kuainisha mambo mengi kwenye halmashauri ya ubongo wangu, nilitakiwa kufanya maamuzi magumu kwa wakati ule hata kama yangekuwa na matokeo mabaya kwa baadae ila nilitakiwa kukipita kwanza kile kipindi kisha huko baadae ningejua maamuzi gani natakiwa kuyachukua. Mawazo yangu yalinipelekea mimi kuwaza kwa umakini sehemu ambayo nilitakiwa kuwekeza ili nipate pesa, nilipiga hesabu kali lakini sikuwa na sehemu yoyote ile zaidi ya kitu kimoja tu! Mwili wangu.
Niliona hayo mawazo ni ya kipuuzi mpaka pale ambapo niligundua kwamba ilikuwa ni njia ngumu ila ndiyo ilikuwa njia pekee ya kufanya. Ni mara mia wanadamu wakulaumu kwa kupoteza heshima yako muda mwingine lakini sio kufa kwa sababu ya njaa, watu watakuona akili hauna wewe. Nilisimama kwenye kioo nikiwa najiangalia kwa umakini, niligundua kwamba mimi ni moja ya wanawake warembo, wazuri na wenye mvuto mkali. Ni aina ya wale wanawake ambao tumependelewa kupewa kila kitu kwenye miili yetu hivyo huo kwangu ulitakiwa kuwa mtaji, kivipi! Ndipo rasmi nilijiingiza kwenye biashara ya umalaya au unaweza kusema kujiuza.

Maisha ya mjini na unafuu wa maisha umewafanya watu wengi kuwakejeli baadhi ya watu kwa kuhisi hawana akili, kuwaona ni wajinga wa mwisho kwenye baadhi ya maamuzi ambayo wanayafanya ila niamini mimi, hilo jambo sio kweli hata kidogo. Kuna watu wapo mjini wanafanya mambo ya ajabu na unaweza ukaanza kuwalaumu na kuwaona ni watu walio lelewa vibaya au kukosa maadili lakini wengi ukizifunua kuraza za maisha yao ya nyuma utagundua kwamba viatu vyao hata wewe hauwezi kuvivaa. Watu wana mengi kwenye mioyo yao, watu wanaishi kwenye maumivu makali nje ya tabasamu lisilo kera ila uhalisia ni kwamba ndani yake wanaungua, hata wao wanayajutia maamuzi yao lakini kuna wakati maisha yanakufanya usiwe na chaguo lingine zaidi ya lile ambalo watu wengi wanaliona kama ni la kijinga ama halifai.

Mjini kuna malaya wengi wanajiuza, kuna mabinti wengi wanafanya shughuli ambazo kimaadili ni mbaya, siwatetei lakini wengi wao ukitaka kujua kwamba hawapo pale kwa kupenda jaribu kukaa nao halafu wakupe simulizi za maisha yao, niamini mimi utagundua kwamba hata kama ungekuwa wewe huenda lile ndilo lingekuwa chaguo pekee ambalo ungekuwa nalo kwenye ufanyaji wako wa maamuzi. Hivyo hata mimi niliamua kufanya hayo maamuzi ya kuanza kujiuza ili niweze kupata uhakika wa kula, nivae na nilipe kodi kisha baadae ningekuja kuangalia utaratibu wa mambo mengine kwa baadae.

32 inafika mwisho.

FEBIANI BABUYA.
 
STORY: JUMBA JEUSI
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

EPISODE 33.
ENDELEA.......

Biashara yangu mwanzoni niliona kama inatisha, kama unavyo jua wanaume, mimi nilikuwa mgeni hivyo nilionekana kigoli kwahiyo nilikuwa nashambuliwa kama jogoo la pasaka. Mara ya kwanza nilikuwa muoga, nilikutana na baadhi ya watu wakawa wananitapeli pesa mpaka pale ambapo nilikuja kuwa mzoefu kwenye ile biashara na niwe muwazi ni kwamba nilikuwa naingiza pesa nyingi kuliko hata baadhi ya wafanya biashara na waajiriwa wa nafasi za juu kabisa serikalini. Lengo langu kubwa ilikuwa ni kwamba niwe nafanya ile biashara usiku na baadhi ya wateja ningekuwa naenda kuwahudumia hata mchana mahotelini hususani ambao walikuwa na namba zangu ambazo nilikuwa nazisambaza kwenye baadhi ya mitandao ambayo ilikuwa ya siri na ina wateja kutoka nje wengi ambao kwa usiku kukupa hata milioni tano ni kawaida kwao ndiyo maana watu hao walikuwa wakinipata kwa urahisi na wengine walihitaji huduma muda ambao waliutaka wao halafu mchana niwe naenda chuo.

Aliyesema pesa ni mwanaharamu alikuwa sahihi kabisa, ilifika wakati nikawa nina uhakika wa kushika pesa zaidi hata ya wale ambao walikuwa wananifundisha hivyo niliona kama kusoma tena ilikuwa ni kujipotezea muda wangu kwani shida yangu kubwa kwenye maisha yangu ulikuwa ni pesa ndipo nikaamua kuipotezea kabisa elimu nikiamua kukomaa na kazi yangu ya umalaya ambayo niliona inanilipa. Hii kazi ina ubaya sehemu moja ni kama madawa ya kulevya tu vile yalivyo, kuingia huko ni rahisi lakini kutoka ni kazi ngumu kuliko kawaida, lile ni gereza ambalo linatembea.

Biashara yangu ilikuwa nzuri hivyo hata mimi nikawa najipa matunzo ya gharama na nilizidi kung’aa na kuwa na mvuto usio wa kawaida kiasi cha kuanza kuwagombanisha mpaka watu kwenye ndoa zao kwa baadhi ambao walifanikiwa kunijua lakini pia nilianza kuwapata hadi viongozi kadhaa ambao nao walikuwa wanazitumia kodi za wananchi ipasavyo kuhakikisha kwamba mtoto wa kike naweza kupata yaliyo mazuri na nafurahi. Huenda unajiuliza ni kwanini nimekwambia haya yote kuanzia siku ya kwanza kabisa, ni kwa sababu biashara yangu ya kujiuza ndiyo ambayo ilizalisha simulizi mpya ya maisha kati yangu mimi pamoja na Oliver, umalaya wangu ndiyo ambao umemfanya Oliver kuishia alipo hii leo na huenda ndiyo ilikuwa sababu kubwa ya raisi Philip kufa na Darian Julius kuingia madarakani. Sasa ilikuwaje?

Kama nilivyo kwambia mimi nimebahatika kuwa mzuri na mwenye mvuto mkali hususani kwa wanaume, ule mvuto wangu ulipelekea mpaka wanasiasa kuanza kuniparamia kwa kasi mpaka siku moja nilipo kutana na bwana mmoja ambaye nilimpatia mtandaoni. Bwana huyu yeye hakutaka kukutana na mimi hapa Tanzania hivyo alipiga simu tukutanie ndani ya jiji la Paris Ufaransa, mimi sikujali kwa sababu nilizipenda pesa kwa wakati ule nahisi kuliko hata nafsi yangu mwenyewe na ukizingatia sikuwahi kufika kwenye hilo jiji ambalo linadaiwa kuwa la starehe na matajiri wengi wa kutosha hivyo niliona ni nafasi yangu kuweza kufika huko. Nilitumiwa tiketi ya ndege na hatimaye kwa mara ya kwanza nikasafiri kwenda ulaya ambapo nilipokelewa uwanja wa ndege kama malkia vile hali ambayo ilinifanya niyapende yale maisha ya kujiuza.

Nilipelekwa kwenye hoteli ambayo sidhani kama niliwahi kufikiria kwamba hapa duniani kuna hoteli za kifahari na anasa namna ile, unajihisi upo kwenye ulimwengu wa tofauti kabisa na huu ulimwengu wa wengi hivyo nilijikuta nafurahi mno mpaka pale ambapo nilifikishwa chumbani. Baada ya kuingia ndani nilikutana na mwanaume mmoja ambaye alikuwa kwenye taulo akiwa anaangalia nje ya dirisha eneo ambalo lilikuwa linauonyesha mji na mandhari yake ya kuvutia. Nilimsalimia kwa kuibia ndipo akageuka akiwa na taulo, baada ya kumuona nilishtuka sana na hata ile hali ya kujiamini ilipotea kabisa kwani niliingiwa na hofu na maswali kwa wakati mmoja.

Alikuwa ni mtu wa karibu sana na mheshimiwa ambaye alikuwa anawania kwa ukaribu nafasi ya uraisi wa Tanzania, Darian Julius. Sikuwa mtu wa siasa kabisa lakini kuhusu kufuatilia nani anaenda kuliongoza hili taifa kiukweli sikupitwa na ndiyo sababu nilibaki natetemeka. Yule alikuwa ni mtu mkubwa mno na kuingia Ikulu lilikuwa suala la muda tu kwani mtu wake ndiye alikuwa ana nguvu kubwa ya kisiasa nchini na yeye ndiye alikuwa mkono wake wa kulia maana yake baada ya raisi ajae ni yeye upande wa pili. Bwana yule alikuja kunikumbatia huku akinivua nguo, hapo nilikuwa kama nimepigwa ganzi kwenye mwili wangu nikiwa najishauri jambo la kufanya. Hakuongea zaidi ya kunibeba na kunipeleka bafuni kwenda kuniogesha na baada ya hapo nilishtuka baada ya masaa mawili baadae ile shughuli nzito ilipo isha.

Aliniteka kwenye mawazo ya ngono na yule sikufanya naye kama najiuza bali nilifanya naye kama mpenzi wangu na naweza kukiri kwamba alikuwa ni mwanaume wangu wa kwanza tangu nianze kujiuza ambaye nilifanya naye mapenzi bila kutumia kondomu. Baada ya kumaliza zoezi lile nilijikuta nipo huru kwake, kwanza nilitambua kabisa kwamba kuwa karibu na mtu kama yule kwangu ilikuwa na faida kubwa kwani ingenifanya niwe mwanamke mwenye nguvu pia na huko mbeleni ningekuja kuwahitaji watu kama yeye kama mambo yangu yangeenda vibaya. Kule tulikaa wiki moja ambayo mimi niliona ni kama siku mbili kwani sikutamani hata kurudi tena Tanzania lakini wahenga waliwahi kusema kwamba mkataa kwao ni mtumwa siku zote na mimi sikutaka kuwa mtumwa.
Yule bwana alikuwa ananizingatia kwenye kila jambo, kuanzia namna ya kuniangalia, namna nilivyo na joto kali ambalo lilikuwa linamfanya kufika kileleni haraka huku akiwa anatoa machozi kwa utamu ambao nilikuwa nao mpaka siku moja ambapo mazungumzo yake yalibadilika na kuonekana kuwa siriasi zaidi ya vile ambavyo yalikuwa mwanzo.

‘Kuna nyakati muda huwa unatuhukumu, natamani kabisa nisingekuwa na familia ndipo nikutane na mwanamke kama wewe, binafsi ningekuoa wakati huo huo’’
“Kwanini unasema hivyo mpenzi?”
“Kwa dunia hii ambayo imejaa mambo ya ajabu kumpata mwanamke mwenye mvuto mkali kama wewe, kitandani una moto ambao unamfanya mwanaume atamani kukulilia hata ukienda kuoga tu anaogopa ataibiwa na unanipa mapenzi bila kunibania kama wapenzi wakati unafanya tu biashara, kiukweli unahitaji pongezi kubwa’’

“Sikutegemea kama ningekupa furaha mpenzi”
“Mara ya kwanza wakati naiona picha yako kwenye ule mtandao nilitamani niweze kulila tunda lako tu kisha kila mtu apite njia yake ila kwa sasa hilo naona haliwezekani tena”
“Kwanini mpenzi?”
“Kwa sababu nataka nikufanye uwe mchepuko wangu wa kudumu na kama mambo yataenda vizuri baadae naweza kukufanya ukawa mke wangu mdogo kama utakuwa tayari”
“Mimi ni nani ambaye naweza kusema hapana kwako? Kiukweli hata mimi natamani siku moja niitwe mke wa mtu, natamani kuitwa mama pia”
“Hilo linawezekana ila kwa muda ambao nimekaa na wewe hapa kuna kazi kwanza ambayo inabidi ifanyike ndipo haya maamuzi yaweze kufanyika”

“Unamaanisha kwamba kuna kazi unataka kunipa?”
“Ndiyo”
“Kazi ipi hiyo?”
“Kwanza unaweza kukaa na siri kifuani bila kwenda kuitangaza mahali kama wanawake wengine walivyo?”

“Nadhani mpaka unataka kunipa hiyo kazi umeona kabisa namna nilivyo na najua kabisa kwamba una uhakika kwamba naweza kufanya hivyo”
“Nimekuuliza hilo kwa sababu jambo ambalo naenda kukwambia hapa ni jambo kubwa na la hatari zaidi kuwahi kutokea ndani ya taifa la Tanzania”
“Mbona unanitisha tena”
“Sikutishi kwa sababu jambo lenyewe ndilo linatisha hata kwangu pia ila kama unavyo jua kwenye haya maisha kama ukiogopa kufanya mambo ambayo yanatisha basi hata wewe utaishia kuwa mtu wa kawaida tu”
“Yeah, naweza kufanya hivyo”
“Una uhakika?”
“Ndiyo”

“Kipi kinakufanya uwe na huo uhakika?”
“Kwa sababu sina cha kupoteza, jambo pekee ambalo lilibaki kwenye maisha yangu ni kuuza utu wangu na nilisha uuza tayari hivyo sioni jambo lingine lolote ambalo mimi naweza kulihofia tena kwa sasa”
“Unaweza kuua?”
“Unataka kunipa kazi ya kuua mtu?”
“Sijasema hivyo, nimekuuliza unaweza kuua?”
“Inategemea na nitakacho kipata baada ya kuua na hali ya usalama wangu baada ya kufanya hivyo”

“Safi, sasa unajua kabisa kwamba uchaguzi unakaribia na kuna majina ya watu wawili ambao ndio wana nafasi kubwa ya kufika wanapo elekea na kwenye hayo majina mawili ambayo yapo ni kwamba moja linatakiwa kupotea. Wewe na baadhi ya watu huenda mnahisi Darian anaenda kuwa raisi lakini sio kweli, Darian hawezi kushinda mbele ya Philip’’

33 inafika mwisho.

FEBIANI BABUYA.
 
STORY: JUMBA JEUSI
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

EPISODE 34.
ENDELEA.......

“Lakini mbona Darian ndiye ana nguvu zaidi?”
“Kuwa na nguvu za kupiga kelele sio kushinda, unajua huu ulimwengu ni mdogo sana kama ukipata watu sahihi ama ukawa na taarifa sahihi kwa sababu zinaweza kukuletea jambo lolote mezani kwako ama kukusafirisha popote pale duniani kwa muda ambao unautaka wewe”
“Mpenzi bado sijajua maana yako ni ipi hapo”

“Namaanisha kwamba Darian ana siri zake ambazo sio nzuri, sehemu ndogo ya siri hizo kuna watu kadhaa wanazijua na watu hao kama watazitoa nje maana yake ni kwamba maisha yake yote yataharibika na jambo hilo halitakiwi kufanyika”
“Sasa mimi nahusikaje kwenye mambo ya wakubwa huko?”
“Huku wala hauhusiki na kazi yako haipo huku juu ila najaribu kukupa akili ya uelewa wa jambo hili. Kwa sababu ndani ya chama linatakiwa kutoka jina moja, Darian anahitaji jina lake likatwe ili Philip ndiye apewe nafasi ya kugombea uraisi”
“Sijakuelewa kwamba anajikatia tamaa mapema hivi?”

“Mhhhh hakuna mtu anaweza kujikatia tamaa linapokuja suala la nafasi hizi kubwa kama kwenda ndani ya lile jumba jeupe ambalo ni ndoto ya kila mwanadamu aliye hai”
“Sasa kwanini anataka kufanya hivyo?”
“Maisha ya siasa ni tofauti na maisha ya kawaida, maisha ya kawaida unaanza kuishi wakati uliopo kisha unaenda wakati ujao lakini maisha ya siasa ni kwamba unaanza kuuishi wakati ujao kisha ndipo unarudi kwenye wakati uliopo. Hilo huwa wanalitambua watu kadhaa tu wenye akili kubwa kwa sababu kumaliza vita kwa amani sio kushindwa vita bali ni kushinda vita kwa kumfanya mpuuzi ambaye umeenda kuomba amani kwake ahisi ameshinda, sasa kinafuata nini? Siku akiwa amestarehe ndipo unamshtukiza ghafla na anapokuja kushtuka unakuwa umebeba kila kitu kutoka kwake”

“Ukiwa na maana gani mpenzi?”
“Darian anataka kukubali jina lake litolewe lakini kabla ya hapo atakutana na Philip ili wakubaliane akubali kumpa nafasi hiyo na kumuunga mkono kisha akiwa raisi anatakiwa kumteua Darian kuwa waziri mkuu wa Tanzania”
“Japo bado sijaelewa sababu ya msingi ya kufanya hivyo ila naamini kwamba hata raisi ambaye atakuwa madarakani hawezi kukubali kupangiwa mtu wa kumteua”
“Niamini mimi kwamba hapa duniani kila mtu anapangiwa cha kufanya ni kwa sababu tu wewe huwezi kuona. Yeye anajua kabisa Darian ana nguvu hivyo kama Darian akikubali kuondoka yeye basi kwake itakuwa na faida nyingi hivyo lazima ataikubali hiyo ofa na baada ya kuikubali hiyo ofa wewe kazi yako itaanzia hapo”

“Wapi?”
“Philip ni kiongozi bora lakini Darian anatakiwa kuingia Ikulu kwa namna yoyote ile hivyo tunahitaji kujua kila jambo ambalo litaendelea kwenye mzunguko wa hawa watu”
“Bado sijakuelewa”
“Iko hivi bibie Philip akiwa raisi, yule ni kiongozi bora hivyo wananchi hawatahitaji aweze kuondoka tena madarakani na uchaguzi ambao unafuata utakuwa ni rahisi kwake na hakuna mtu atakuwa na uwezo wa kumtoa pale kwa sababu wananchi watakuwa wamemkubali yeye tayari jambo ambalo litakuwa hatari kwetu”
“Kwahiyo unamaanisha kwamba mnahitaji kuja kumpindua akiwa madarakani?”

“Hapana sio kumpindua”
“Ila?”
“Atatakiwa kufa”
“Nadhani sijakusikia vizuri, mnapanga kuja kumuua raisi wa nchi?”
“Ndiyo”
“Hapana, hapana, hapana, siwezi kushiriki kwenye jambo la hatari kama hilo”
“Binafsi nimevutiwa na wewe ila kama hautakuwa tayari kuifanya hii kazi basi itanilazimu nikuue kwa sababu tayari umesha ijua siri ambayo huenda haukutakiwa kabisa kuweza kuijua”
“Lakini hayo hayakuwa makubaliano yetu”
“Kwa sababu unagoma kabla hata sijakupa kazi yako na haujui unatakiwa kufanya nini”
“Unatakiwa kuniongezea kiwango cha pesa ili tuwe kwenye mstari mmoja”
“Sasa hapo umeanza kuongea kama mwanamke ambaye umekomaa na unajielewa”
“Nakusikiliza”

“Yule akiwa madarakani tutahitaji kupata watu wa karibu ambao watakuwa wanatupatia taarifa za ndani zaidi kutoka kwake. Najua kuna taarifa ambazo tutakuwa tuna uwezo wa kuzipata ila kuna taarifa hatutaweza kwa sababu kwa historia ya yule bwana ni moja kati ya watu ambao ni wasiri mno na huwa sio rahisi kuweza kuzitoa taarifa zao kirahisi”
“Taarifa kuhusu nini?”
“Hizi hazikufai wewe kwa sasa, ukianza kazi yako utaanza kuzifahamu”
“Hivi kwanini mnaonekana kama mnaogopa sana kuhusu uchaguzi?”
“Hilo ni kweli kwa sababu huwa unakuja na mambo mengi ndani yake, kwenye uchaguzi kunakuwa na mambo mengi na unakutana na watu ambao watahitaji kuzipata kila taarifa zako sasa kama una historia mbaya inaweza kuja kukuharibia moja kwa moja”

“Ndiyo maana mnataka kuja kuingilia kati kati ili hata watu wakija kuupata ukweli Darian anakuwa tayari Ikulu?”
“Una akili ya haraka bila shaka nimempata mtu sahihi kwa hii kazi”
“Bado haujaniambia sababu ya kunichagua mimi kuwa sehemu ya hii kazi kwa sababu haunifahamu kiundani”
“Mhhhh sio kweli bibie, nimekaa na wewe wiki sasa hivyo kulipata jina lako tu kumenifanya nikujue wewe kiundani zaidi. Kuhusu sababu ya mimi kukupa wewe hii kazi wakati kuna wanawake wengi huko nje ni kwa sababu nimeona wewe ni mwanamke mwenye mvuto mkali ni rahisi kumshawishi mtu yeyote kukupenda au hata kutamani kufanya mapenzi na wewe tu hivyo utanifaa kwenye hii kazi”
“Ambayo ni?”
“Kuna mtu nahitaji umpende”
“Nimpende au niigize kumpenda?”
“Ni wewe utakavyo ona inafaa kikubwa usiathiri kazi ambayo itakuwa mbele yako”

“Usiniambie unataka nimpende raisi!”
“Hilo ni gumu kwako ila kazi yako nataka umshawishi mlinzi mkuu wa raisi awe sehemu ya maisha yako”
“Unamaanisha yule kijana ambaye huwa naona anatembea naye kila sehemu kwenye shughuli zake za kisiasa?”
“Ndiyo yule, yule bwana kwa sababu ni mtu msiri kupitiliza, ana watu wake kadhaa ambao ndio huwa anawaamini na kuwapa siri zake za ndani na moja ya watu ambao wanakuwa na taarifa zake nyingi ni yule bwana mdogo hivyo kama ukiwa karibu yake itatufanya sisi tujue mipango yake yote ambayo itatufanya sisi tufanikishe kazi yetu kirahisi”

“Hilo jambo naona kama ni gumu, kama mnamhitaji kirahisi hivyo kwanini msisubiri wakati ambao mtaona ni sahihi halafu mnamteka yule kijana na kumhojikinguvu?”
“Nadhani bado unahisi ninayo yazungumza hapa ni matani ndiyo maana unaongea kimasiara hivyo. Hapa tunayo yazungumzia ni maisha ya raisi wa taifa hili ambaye siku kadhaa zijazo anaenda kuwa raisi na mtu ambaye nataka uingie kwake ni mlinzi wake ambaye nina imani kwamba hata akipita kwenye nafasi yake lazima huyu ndiye bado anaenda kuwa mlinzi wake hivyo hata wewe maisha yako yapo hatarini muda wowote unaweza kuuawa kuanzia sasa kama ukijulikana kwamba unahusika kwenye huu mpango”

“Kwahiyo unanipeleka kwenye kifo na unajua?”
“Nisikilize binti, usione watu wanatembelea magari ya kifahari, usione watu wanaapishwa kuingia Ikulu ukahisi kwamba huwa inakuja kirahisi tu, huku nyuma ni lazima watu watoe kafara, kuna watu inabidi maisha yao yaende kama ikiwezekana ili mambo yawe sawa. Huyu kijana ambaye wewe unamtaja hapa hayupo kama ambavyo unamuona kwenye suti akiwa na raisi, ni moja kati ya vijana hatari zaidi kuwahi kuishi kwenye hili taifa na ni muuaji wa kutisha yule hivyo unapo enda kwake ni kwamba unaenda kwa mtu ambaye amekamilika kila sehemu hivyo ukifanya kosa hata moja tu basi ujue maisha yako yameishia hapo”
“Natakiwa kufanya nini?”

34 Inafika mwisho.

FEBIANI BABUYA.
 
STORY: JUMBA JEUSI
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

EPISODE 35.
ENDELEA.......

“Hilo ndilo swali ambalo ulitakiwa kuuliza tangu mwanzo, ni kwamba anatakiwa kuwa mpenzi wako. Kazi sio kuwa mpenzi wake bali inaanza baada ya yeye kuwa mpenzi wako. Mwanaume huyu mfanye akuamini wewe, mfanye awe sehemu ya maisha yako, mfanye ahisi kwamba pumziko lake ni wewe hapo. Yule anapata muda mfupi wa kuweza kupumzika hivyo anakuwa ni mtu ambaye hana furaha, hana amani na muda wote anakuwa mtu mpweke asiye na mtu wa karibu au msaada kwake kwahiyo kama ukimfanya akakuamini wewe maana yake kuna nyakati ambazo atakuwa hayupo sawa atakuwa anakuambia baadhi ya mambo kama sehemu ya kutoa ya moyoni na kila jambo ambalo atakuwa analifanya au kulisema unatakiwa uwe unanifikishia taarifa mimi kwa wakati mwafaka”

“Unamaanisha kwamba hili jambo ni la muda mrefu?”
“Ni zoezi la miaka bibie, jambo zuri huwa halitaki haraka hata siku moja. Wewe unahisi tu kwamba ataingia madarakani kisha sisi tumuue? Unahisi ni rahisi kufanikisha zoezi hilo? Inatakiwa tuijue mifumo yake, tuzijue siri ambazo huenda zinaweza kuwa hatari kwetu hata kama yeye atakuwa amekufa, tunatakiwa kujua udhaifu wake, uimara wake, tunatakiwa kutengeneza mazingira ambayo hata siku akifa watu wasije kushtuka kwamba kuna jambo limefanyika nyuma ya pazia ambalo huenda hawalijui kwamba lipo”
“Yule mtu sio rahisi kukutana naye, unahisi hiyo kazi nitaifanya nikiwa wapi?”

“Mpaka nakuja kwako ni kwamba hayo yote mimi nayajua kwamba sio rahisi kuweza kukutana naye ila inawezekana na ndiyo sababu kwa sasa unatakiwa kubadilisha maisha yako yote”
“Kivipi?”
“Unatakiwa kuingia kwenye mashindano ya miss Tanzania”
“Mimi?”
“Kwani unahisi hapa naongea na nani?”
“Kwanini iwe hivyo?”
“Ndiyo njia rahisi ya kuweza kuonana naye au kupata ukaribu angalau na huyu mtu”
“Unahisi hilo linawezekana vipi?”

“Kwa sasa akiwa raisi atahitaji zaidi kuvutia tasnia ya habari kwa sababu aliahidi hilo maana yake wanawake ambao mtaingia kwenye hiyo nafasi ya kushiriki ni lazima atawakaribisha Ikulu na hiyo itakuwa sehemu ya wewe kuanza ukaribu na huyo bwana. Sasa hapa ndipo unatakiwa kuanza kuitumia ile nguvu yako ya asili ya mvuto mkali ambao upo nao, usijionyeshe kwamba wewe ni malaya japo ni malaya kweli. Kwake kuwa mwanamke ambaye anaweza akawa na heshima kwenye jamii na kuanzia wakati huo hautakiwi kuwa na skendo mbaya yoyote ambayo inaweza kukuharibia kwa sababu kama ukipata skendo mbaya atakuacha muda huo huo, kazi yake ni mhimu kuliko mtu yeyote yule na ndiyo ambayo anatakiwa kuilinda kwa gharama zote”

“Na vipi kama siku akija kujua kwamba mimi najiuza?”
“Atajua kutoka kwa nani?”
“Kumbuka nimetoka na watu wengi wakubwa kama wanasiasa na wafanya biashara ambao wanaijua sura yangu, inaweza ikawa rahisi kumfikishia yeye taarifa”
“Nisikilize bibie, hao wanasiasa na wafanya biashara wengi ambao unawasemea wanafanya haya mambo ya kukutana na kufanya mapenzi na malaya kwa siri kwa sababu wana familia zao lakini jamii ina waamini sana hivyo kama kukiwa na taarifa zozote za kutembea na malaya kama wewe kwao ni hatari kubwa zaidi kuweza kupoteza biashara zao na hata familia zao mambo yakienda vibaya! Sasa unahisi ni nani yupo tayari kuipoteza familia yake kwa sababu ya malaya? Mpaka hapo hawawezi kuthubutu maana wao ndio wanataka usiri zaidi yako wewe hapo.

Wewe unaenda kuwa maarufu ndani ya taifa hili na ukiwa hivyo maana yake hata wale vijana ambao umewahi kufanya nao mapenzi wakidai hivyo itaonekana kama wapenda kiki tu ambao wameona umefanikiwa wanaanza kushoboka hivyo hawatakuwa na madhara yoyote yale na kama atatokea ambaye anaweza kuwa na madhara kwa baadae basi nitammaliza mwenyewe. Tukija kwa huyu mlinzi, kwa kazi yake yeye itakuwa ngumu kuruhusiwa kuwa na mwanamke wa aina yako ambaye anaenda kuwa maarufu kila kona, hawa mara nyingi huwa kama akitaka kuwa na familia basi awe na familia ambayo imetulia na haifahamiki kwa watu wengi kwa sababu za kiusalama, hivyo mpaka hapo ina maana kwamba hata ikitokea umemshawishi na yeye maana yake mapenzi yenu yatakuwa ya siri.

Sasa muda wote huo wewe kwenye mitandao ya kijamii utatakiwa kuwa mtu ambaye utakuwa na usiri mkubwa kuhusu maisha yako binafsi, maana yake mtakuwa kwenye mapenzi ya watu wawili tu na watu wa nje hakuna hata mmoja ambaye ataweza kulitambua jambo hilo. Na baada ya muda kufika ambao raisi atatakiwa kufa kuna kazi nyingine utaongezewa kwa sababu hata huyu mlinzi wake atahitajika kufa au kuuziwa kesi ya mauaji ya raisi”
“Mimi nitapata nini baada ya hapo?”

“Kwanza pesa, maisha yako yatabadilika kabisa baada ya hapo, pili utakuwa na umaarufu ambao utabadili kabisa historia yako na baada ya haya kukamilika basi utakuwa moja ya wanawake wenye nguvu zaidi ndani ya taifa hili kwani hakutakuwa na mtu hata mmoja ambaye atakuwa na jeuri ya kuweza kukugusa wewe”
“Kwanini natakiwa kukuamini juu ya haya?”
“Kwa sababu ungekuwa na chaguo lingine mpaka sasa usingekuwa hapa Paris”
“Na vipi kuhusu wewe?”
“Mimi nitakuwa nafanya mapenzi na wewe kwa muda ambao najisikia mimi”
“Nitaifanya kazi yako”
“Good”

Hayo yalikuwa ni maelezo ya mwanamke mrembo Zyra, alikuwa anampatia maelezo hayo Jessica ambaye alikuwa makini kumsikiliza mwanamke huyo kwa sababu alimhitaji ampatie taarifa zote kuanzia mwanzo mpaka walipokuwa wamefikia siku hiyo ikiwa ni kwenye harakati zake za kuweza kumtafuta Oliver Jefferson kama bado angekuwa hai mpaka wakati huo ili aweze kumpata binti wa raisi ambaye alimpoteza mbele ya watu asio wajua kule Mwl. Nyerere.

“Umenipa historia ya maisha ambayo mlikutana nyuma jambo ambalo ni zuri kwangu kwa sababu sikuwa na hizo taarifa ila halina msaada wowote ule kwangu mpaka sasa Zyra na unalitambua hilo”
“Ni wewe umesema nikupe taarifa za kuanzia mwanzo”
“Ni kweli lakini wewe unaona kwamba taarifa hizi zina msaada wowote ule kwangu?”

“Kwahiyo unataka mimi nifanye nini dada yangu?”
“Niambie namna ambayo naweza kumpata Oliver”
“Mimi sijui?”
“Haujui au hautaki kuniambia?”
“Mimi nilimpatia sumu tu na baada ya hapo sijui jambo ambalo lilifuatia baadae”
“Hiyo sumu uliyo mpatia ni sumu ya namna gani?”
“Siijui jina ila ni moja ya sumu ambazo ni hatari sana kwa sababu nilijaribu kuwapa paka na mbwa wao hawakukaa muda mrefu wakafa”
“Kwanini ulimpatia sumu?”

“Kwa sababu hata wao hawakuwa na imani kama ingekuwa rahisi kumuua hivyo walitaka sumu imuangamize na kama hilo lingeshindikana basi ingemuathiri na kwao ingekuwa kazi rahisi kuweza kuimalizia”
“Nadhani umelielewa swali swali langu ila unajifanya kama hauelewi”
“Niamini mimi mpaka sasa kuna siri nyingi ambazo mimi sizijui kabisa”
“Lazima una watu ambao watakuwa wanazifahamu kama sio wewe”
“Ndiyo nitakupatia hizo taarifa lakini naomba hili jambo lisije kujulikana kama wewe ulikuja hapa”

“Hakuna mtu atakaye jua kwa sababu wewe bado nakuhitaji ukiwa hai kwani nina kazi na wewe baadae ila nikija kugundua kwamba kuna taarifa hata moja ambayo ulikuwa unanidanganya kuniambia hapa basi utakuwa ni mwisho wako kwa sababu nitakuua mwenyewe kwa mkono wangu tena kikatili kuliko ambavyo umewahi kuona”

35 inafika mwisho.

FEBIANI BABUYA.
 
STORY: JUMBA JEUSI
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

EPISODE 36.
ENDELEA.......

“Naomba Mungu umpate kama atakuwa na bahati ya kuwa hai”
“Una uhakika unaomba Mungu kwamba unamtaka akiwa hai?”
“Sina hakika na hilo, kwani unahisi anaweza kunisamehe?”

“Nadhani moja ya makosa makubwa ambayo umeyafanya kwa miaka yote ambayo umekuwa na huyu bwana ni kushindwa kuisoma historia ya maisha yake hususani kwenye kazi yake. Hajawahi kumsamehe binadamu hata mmoja ambaye amemsaliti, labda kama utakuwa wa kwanza”
“Na vipi kama atakuwa amekufa?”
“Maana yake wewe utakuwa hauna kazi yoyote kwangu”
“Utaniua?”
“Bado sijapata maamuzi ya mwisho juu ya hatima yako”

“Binafsi nakushauri jambo hili ungeachana nalo kwa sababu lina mizizi mirefu kuliko unavyo fikiria na kuna mambo ya kutisha ndani yake ambayo yanaweza kukufikisha kwenye hatua mbaya ya maisha yako. Haya nakushauri kama mwanamke mwenzako kwa sababu nawajua hawa watu namna walivyo, kama wamemuua raisi hawaoni shida kukupoteza mtu kama wewe hapo”
“Yeah, najua ila ila inaonekana kuna mambo mengine ambayo hauniambiia hapa”
“Ni kweli”

“Basi ni vizuri ukaongea haraka kwa sababu nataka kuondoka”
“Sio kwamba mimi napenda aina ya haya maisha”
“Kwamba unapenda kurudi kwenye kujiuza?”
“Hapana”
“Ila?”
“Natamani kuishi maisha ya kawaida kama watu wengine, natamani niwe mwanamke bora kwa jamii kama walivyo baadhi ya wanawake na natamani kuwa na familia kama walivyo wanawake wengine”

“Nadhani wakati unafanya maamuzi ya mwisho ulikuwa unayajua matokeo yake na ulikuwa tayari kuyebeba kama ulivyo jitanabaisha kwenye maelezo yako”
“Upo sahihi”
“Sasa unalalamika nini?”

“Nimechoka kuwa hivi, haya maisha siyataki tena kuishi nikiwa hivi naona kama nipo gerezani bado”
“Unataka kusema nini Zyra?”
“Kuna baadhi ya siri nipo nazo ambazo zinaweza kukusaidia kupambana na hawa watu kama kweli utaamua kulibeba hili jambo kwa moyo wako kama ambavyo umesema hapa”
“Nakusikiliza”

“Mara ya kwanza wakati nafanya maamuzi nahisi sikuwa na chaguo kwa wakati ule ila kwa sasa nataka kufanya jambo jipya tofauti na lile la mwanzo”
“Siku zote huwa tuna machaguo Zyra”
“Basi huenda mimi nilifanya chaguo baya ambalo limenifanya niishi kama mfungwa kwa zaidi ya miaka minne sasa”
“Unataka kufanya nini?”
“Nina frash ndogo ambayo ina baadhi ya taarifa za mhimu kuhusu hawa watu”

“Kwamba umekuwa ukiwafuatilia kwa muda mrefu?”
“Ndiyo”
“Kwanini?”
“Kama ambavyo bwana yule aliwahi kuniambia kwamba siku zote wanasiasa huwa waangalia maisha ya baadae kwanza ndipo wanarudi kwenye yale maisha ya leo basi nilitambua kwamba ni tafsiri ya kwamba wanasiasa karibia wote ni waongo. Huwa wanatoa maneno ambayo watu wanataka kuyasikia kwa wakati huo ila kwa baadae huwa hayana maana yoyote hivyo nilitambua kwamba kipindi ikifika sina kazi kwao tena lazima wataniua kwa sababu ninajua siri zao nyingi na wakati kama huu ambao watu wanaanza kuhoji naweza kuishia pabaya”

“Kwahiyo unaniambia haya kwa sababu unahisi utakufa na hatia?”
“Nahisi hivyo”
“Nipe hiyo frash na kuhusu hatia omba Mungu Oliver awe hai na kama una bahati uje umuombe msamaha mwenyewe hata kama atakuua ila sina uhakika kama atakupa nafasi ya kuishi mwanamke kama wewe” mazungumzo yao yaliishia hapo Jessica akaondoka eneo hilo akiwa amepata taarifa nyingi ambazo mara ya kwanza hakuwahi kuzijua kabisa.




KIJIJI CHA BANZOKA
Ndicho kijiji alichokuwa yupo Bazoka, mwanaume ambaye aliponea kwenye tundu la sindano na kuendelea kuwa hai. Alikuwa anaelezea baadhi ya mambo ya kutisha wakati ambao alikuwa usingizini, ni kama alikuwa anaota ndoto lakini mambo yote ambayo alikuwa anayazungumzia kwa wakati ule hayakuwa ndoto bali ulikuwa ni uhalisia wa maisha ambayo alikuwa ameyaishi kwa miaka kadhaa ambayo ilikuwa imepita.

Ni kweli kabisa kwamba yeye alikuwa ni mlinzi wa raisi Philip, raisi ambaye alifia madarakani akiwa na miaka minne na nusu ikiwa umebakia mwaka mmoja na nusu kuweza kuingia kwenye uchaguzi kwakuwa Tanzania kwa wakati huo uchaguzi ulikuwa unafanyika kila baada ya miaka sita. Watu ambao waliamua kuibeba nafasi yake walidai kwamba haikuwa rafiki kwao kuweza kusubiri wakati wa uchaguzi tena kwani bwana huyo alikuwa ameweka mizizi mirefu na imani kwa raia wake hivyo wasingeweza kumpa mtu mwingine nafasi hiyo zaidi yake. Kuendelea kumuacha akiwa hai ilikuwa ni hatari zaidi kwao ndiyo sababu waliamua kumuua na sio yeye tu bali kila mtu ambaye alihisiwa kuwa karibu naye alitakiwa kuuawa.

Wakati anaendelea kutoa ushuhuda wa simulizi hiyo ya kutisha mbele ya watu ambao walimsaidia bila yeye kujua ndipo alifumbua macho yake na kugundua kwamba alikuwa sehemu tofauti, alikuwa sehemu ambayo hakuijua ni wapi na alikuwa anafanya nini. Watu ambao alikuwa anawaona mbele yake walikuwa wa tofauti na wale ambao aliwazoea na hata mavazi yao yalimshtua. Alikuwa amesimama mwanamke mmoja ambaye alikuwa amejifunika usoni na mbibi mmoja ambaye alikuwa na majani kadhaa kwenye mkono wake. Bazoka ni kama bado alikuwa haelewi jambo ambalo lilikuwa linaendelea pale hali ambayo ilimfanya kuhitaji kujigeuza lakini aligundua kwamba mwili wake haukuwa na nguvu za kutosha bali ulikuwa kwenye maumivu makali.

Alitambua kwamba alikuwa kitandani, kitanda ambacho kilifungwa na kamba kuonyesha wazi kwamba watu hao walikuwa wanayaishi yale maisha ya zamani, enzi za kale ambazo watu hawakuwa wameathirika na ujio wa utandawazi. Mwanaume huyo alijishangaa kuona hawezi kunyanyuka vizuri kwani kila alipo jaribu hilo mwili wake ulikuwa unauma kiasi cha kumrudisha tena kitandani hapo kuendelea kulala akiwa anawatolea macho watu hao ambao alikubali kwamba kama walikuwa watu wabaya basi wangemfanyia lolote ambalo walikuwa wanalitaka wao kwani hakuwa na uwezo wa kuweza kupingana nao kwa nyakati kama hizo.

“Nini kimenitokea, hapa ni wapi na nyie ni akina nani?” aliuliza kwa msisitizo watu hao wakiwa bado wanamwangalia yeye, yule bibi alisikitika na kutoka humo ndani kwani aliona hilo jambo walipaswa kuongea watu wawili tu hivyo aliwapa nafasi.
“Umesema wewe ni mlinzi wa raisi kwenye ndoto yako, je jambo hilo ni la kweli?” alishtuka kusikia hayo maelezo, kumbukumbu zake hazikuwa sawa kwa nyakati hizo hivyo hakumuelewa mwanamke huyo na hata kama angemuelewa basi alishangaa inakuaje raia hamjui mlinzi wa raisi wake kwamba alikuwa nje na utaratibu wa maisha ya kawaida? Ilimshangaza.

“Sina kumbukumbu hiyo kwenye akili yangu. Ni mimi nimesema hayo?”
“Ndiyo”
“Kwani nimefikaje hapa?”
“Mimi nilikuokoa kwenye kifo”
“Mimi nilikuwa nakufa?”
“Ndiyo, kuna watu walionekana kuihitaji sana nafsi yako”
“Wapi”

36 inafika mwisho.
 
STORY: JUMBA JEUSI
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

EPISODE 37
ENDELEA.......
“Kwenye kingo za kijiji hiki, sijajua ulitoka nao wapi ila wakati nakupata ulikuwa kwenye hali mbaya na ulikuwa umepoteza fahamu”
“Ulifanikiwa kuwajua hao watu ambao walikuwa wananifukuza?”
“Hapana, mimi ndiye nataka wewe unisaidie kuniambia kwamba ni akina nani hao ambao walikuwa wanaonekana kuiwinda nafasi yako kwa nguvu namna ile mithili ya mtu ambaye ulikuwa umetapeli maisha yao yote” hiyo kauli ilimfanya kufumba macho yake, aliyafumba kwa muda wa dakika kumi na tano kupata utulivu wa akili ili aweze kurejesha kumbukumbu zake. kila kitu kilianza kurudi kama kilivyo! Alitokwa na jasho jingi baada ya dakika hizo kumi na tano kuweza kuisha huku akiwa anaangalia kila upande kwa umakini mkubwa kiasi kwamba kulikuwa na watu wanamjia hapo alipo.

“Nina muda gani tangu nipo hapa?”
“Ni mwezi mmoja sasa”
“Whaaaaaat?”
“Ndiyo, umekamilisha mwezi usiku wa leo”
“No, no, noooooooo” alifoka kwa sauti kwa sababu hakuwa anaamini bado, alikuwa anajua jambo ambalo lilikuwa limetokea hivyo kukaa mwezi mzima hapo maana yake ni kwamba mambo yalikuwa yameharibika zaidi japo alimshukuru Mungu kumpa nafasi ya upendeleo kuwa hai mpaka wakati huo.

“Nadhani wewe ndiye unatakiwa kunipa historia ya maisha yako kwa sababu kukusaidia wewe hapo imekuwa hatari zaidi kwa kijiji changu” aliongea yule mwanamke akiwa anampatia kikombe kimoja ambacho kilikuwa na dawa ya kienyeji ndani yake.
“Ni sumu ya aina gani ambayo ilikuwa kwenye mwili wangu?”
“Hatujafanikiwa kuijua bado ila ilikuwa imeathiri sehemu kubwa ya mwili wako na ulitumia nguvu nyingi wakati ambao haukutakiwa kufanya hivyo kwahiyo iliathiri mishipa yako mingi ndani ndiyo maana umetumia muda mrefu kurudi kwenye fahamu zako. Hata hivi unatakiwa kumshukuru Mungu wako au mizimu yako kwa sababu sisi wenyewe tulikata tamaa tukijua kwamba ni lazima ufe”

“Inaweza kunichukua muda gani mpaka kuweza kurudi kwenye hali ya kawaida?”
“Inategemea na nguvu ya mwili wako, kama unaweza kuanza mazoezi kesho basi kuanzia wiki moja ijayo unaweza kuanza kurudi kwenye hali yako ya kawaida japo haitakuwa rahisi kwa sababu bado kwenye mwili wako kuna sumu kidogo ambayo inaendelea kutoka taratibu”
“Hawa watu hawajafika huku kunitafuta?”
“Walifika”
“Imekuaje bado mpo hai?”
“Kwa sababu huwa tunahamisha makazi kila wakati hivyo tulihamia upande mwingine na baada ya kwenda kule ambako tulikuwa mwanzo, tuligundua kwamba kuna watu walifika kule”
“Kuna mtu alikufa?”
“Hapana”
“Nyie ni akina nani?”

“Siwezi kukujibu hilo mpaka pale ambapo utaniambia wewe ni nani na umetokea wapi! Kwa sababu simulizi fupi ya kwenye ndoto yako sina imani kama ni maisha yako kweli kwa sababu mlinzi wa raisi hauwezi kuishia kwenye hali kama hii ama mahali kama hapa hivyo nina imani ulikuwa unaongea mambo ambayo uliwahi kusimuliwa ama haukuwa ukijua yale ambayo ulikuwa unayafanya”
“Kuna umbali upi kutoka hapa mpaka ndani ya jiji la Dar es salaam?”
“Umbali wa kutosha tu kuwa na amani, sina imani kama kuna mtu anaweza kujua mahali ulipo kwa sasa”
“Nitakwambia kila kitu ila kwa sasa naomba unipe nafasi nitafakari kuhusu maisha yangu kwanza. Nahitaji muda wa kuweza kupata akili mpya ili niweze kujua nini hatima ya haya mambo yote ambayo yameanzia kwenye mikono yangu”

“Sawa, mimi na wewe tutaonana hiyo kesho kama utakuwa tayari kwa ajili ya kufanya mazoezi”
“Shukrani kwa kunifanya mimi kuwa hai tena”
“Utanishukuru mimi na watu wangu siku ambayo utakuwa sawa ila kwa sasa pigania kurudisha nguvu zako kwanza” mwanaume aliitikia kwa kutikisa kichwa chake ile moyoni alikuwa na ghadhabu, mambo mengi yalitokea likiwemo la raisi kuuawa na yeye ndiye ambaye alitakiwa kuhakikisha anamlinda. Moyo wake ulikuwa unaenda mbio alipogundua kwamba watu hao walihitaji kumuua hata yeye ili kumaliza ushahidi wote lakini kitu ambacho kilimuumiza zaidi kwenye akili yake ni kusalitiwa na mwanamke ambaye yeye alimuamini kwa maisha yake yote. Mwanamke ambaye yeye alijitoa kwa ajili ya kumpigania, mwanamke ambaye alimnyanyua kwa nguvu zake zote mpaka kumfikisha pale ambapo alikuwepo akawa na mafanikio makubwa Afrika ya Mashariki huku biashara yake ya vipodozi ikiwa ni maarufu, lakini malipo yake yalikuwa ni usaliti.

Aliona kabisa kwamba mwanamke huyo alikuwa anastahili malipo ya usaliti wake, alitakiwa kufanywa mfano ili watu wa aina yake wajifunze kuhusu maisha, wajifunze namna ya kuishi na wanadamu wenzao ambao wanawatendea wema. Hakika kama angefanikiwa kumuona mwanamke huyo angemfanyia jambo ambalo lingemfanya hata akiwa ndani ya kaburi aendelee kumuogopa na kutamani kumkimbia hata wakati ambao angekuwa amelala usingizi ila kwa wakati huo alitakiwa kuwa mpole kwa sababu hakuna jambo la maana angeweza kulifanya kutokana na hali ambayo alikuwa nayo.

Kesho yake kulikucha mapema, yule mwanamke alimchukua Bazoka ambaye kwa wakati huo alikuwa anatembelea magongo kwa sababu mwili wake haukuwa na nguvu bado za kutosha. Kuzunguka naye ilikuwa ni sehemu ya kwanza ya mazoezi ya bwana huyo ili aweze kuhakikisha anakuwa sawa kama mwanzo.
“Kwanini umenisaidia mtu ambaye hata haunijui, vipi kama nitakuwa hatari kwa upande wako na watu wako?”

“Nimewahi kuwa kwenye nafasi kama yako kabla na kuna watu walinipa msaada bila kujiuliza mara mbili japo hawakuwa wakinijua, tangu siku ile nilipata elimu ya kumsaidia mtu ambaye yupo kwenye uhitaji mkubwa hususani kwenye kuokoa maisha yake. Najua kabisa kama wewe ndiye ungekuwa mwenye makosa kwa wale watu basi wasingehitaji kukuua bali wangehitaji kukupata ukiwa mzima wa afya hususani kama wangekuwa watu wa serikali lakini kukusaka namna ile ambayo ilionyesha kabisa kwamba wanayahitaji maisha yako! Nilitambua kwamba kuna jambo halikuwa sawa hivyo kuna mambo yalikuwa yanaendelea na sikujiuliza mara mbili”

“Mhhhhh unaonekana wewe na watu wako mna moyo wa kipekee sana!”
“Huenda upo sahihi japo sina uhakika na hilo kwa sasa kwani kuna wakati mazingira yanaweza kukufanya ukawafikiria watu tofauti kabisa na wao walivyo”
“Hiyo ni kweli kwa sababu hata mimi baadhi ya watu niliwahi kuwaamini lakini matokeo yake ndiyo wamekuwa sababu ya mimi kuishia hii sehemu hapa ambapo nipo”
“Ni jambo gani hasa limekutokea?”
“Nilitamani nikuulize swali hilo hilo kwamba kilitokea nini mpaka wewe na watu wako mkaishia kwenye hili eneo”
“Uzuri basi nimewahi kukuuliza mimi”

“Maisha yangu ya safari ndefu mno, safari ambayo ni ngumu hata kuweza kuielezea kirahisi. Mpaka nafika hapa basi ujue kabisa kwamba nyuma yangu kuna mambo mengi ambayo yametokea, mambo ambayo mengine ni ya kutisha, hayana usalama kwa watu wengi na kama ukifanikiwa kuyajua basi maisha yako muda wowote ule yanakuwa hatarini”
“Mpaka nakusaidia wewe tayari nimeyaweka maisha yangu na ya watu wangu kwenye hatari kubwa kiasi kwamba muda wowote kama hawa watu ambao wanakutafuta watajua basi ni lazima watahitaji kutuua sisi. Siwezi kufa kwa kitu ambacho sikijui, mimi niliamua kukuamini na kukusaidia mtu ambaye sikujua kama ni muuaji, mhalifu au umetoka wapi kwahiyo ni zamu yako kuulipa wema ambao nimekutendea” mwanaume alihema kwa nguvu baada ya kuambiwa hayo maneno.

“Ni kweli kabisa kwamba mimi nilikuwa mlinzi wa raisi, mlinzi wa mkuu wa taifa hili. Ni kweli kwamba raisi aliuawa, hakufa kwa mipango ya Mungu bali wanadamu waliamua kuyakatisha maisha yake kwa sababu hakuwa na faida kwao kuendelea kuwa hai na njia pekee ya kukamilisha mipango yao ilikuwa ni kumuua ndiyo maana haya yote ambayo yanatokea naona kama mimi ndiye napaswa kuwajibishwa, mimi ndiye natakiwa kubeba kila aina ya lawama kwa sababu huenda bila mimi basi kila kitu kingekuwa sawa.
37 inafika mwisho.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom