JOTO LA MOTO
JF-Expert Member
- Apr 11, 2018
- 766
- 562
SCRIPT ZA IMA.
MTUNZI:MSANII JOTO LA MOTO.
SEHEMU YA KWANZA.
NYUMBANI KWA MKWERE CHUMBANI-ASUBUHI.
Mkwere, kijana, 30, yupo kitandani amelala, pembeni kwenye kochi wapo Erin,mtoto, binti wa miaka 7,na Roda,mdada wa miaka 27, wameketi kwenye sofa wakipata kifungua kinywa, Erin akiwa amevaa sare za shule, Roda anainua kikombe na kumnywesha Erin kumalizia chai kidogo iliyopo kwenye kikombe, “haya inuka twende” Roda anasema huku anainuka na kumuinua Erin, Erin anachukua begi lake na wanatoka.
Zinapita dakika kadhaa, mlango unagongwa, Mkwere bado yupo kitandani amelala, mlango unagongwa mara kadhaa, anashtuka na kuinua kichwa, mlango unagongwa tena, anainuka na kushuka kitandani, anachukua T shirt iliyotundikwa kwenye msumari ukutani na kuivaa kisha anaenda mlangoni na kuufungua mlango, mlangoni yupo Mama Tufe, mama wa makamo, wa miaka 67 hivi, Mkwere anashtuka, “mama shikamoo” anasalimu, “pesa yangu” anasema Mama Tufe kwa sauti ya chini lakini inayoashiria shari, Mkwere anashusha pumzi, “sasa ni hivi..naomba mtoe vitu vyenu nje kuna Mpangaji namleta sasa hivi” anasema Mama Tufe kisha anaondoka, Mkwere anabaki ameduwaa kwa muda, kisha anafunga mlango na kwenda kuketi kwenye kochi, zinapita sekunde kadhaa, mlango unafunguka anaingia Roda, Mkwere ameketi kochini kinyonge huku amejishika tama, “kulikoni baba Erin?” Mkwere anainua kichwa, “kwa nini hukuniamsha?” anauliza Mkwere, “lini nimekuamsha na ukaamka kwa wakati huo huo Baba Erin?” anauliza Roda, Mkwere anabaki kimya, anashusha pumzi,“Mama Mwenyenyumba amekuja amenikuta” anasema Mkwere, “dawa ya deni ni kulipa Baba Erin..sio kukimbia” anasema Roda, Mkwere anabaki kimya, “kwa hiyo amesemaje?” anauliza Roda,“amesema tutoe vitu nje” anasema Mkwere huku Roda akiketi pale kochini, “Mungu wangu” anasema Roda na kushuhsha pumzi “kwa hiyo sasa tunafanyaje?” anauliza Roda, “itabidi tufungashe” anasema Mkwere kwa sauti ya kukata tamaa, Roda anashusha pumzi na kutulia kwa muda, “Baba Erin..tukifukuzwa tena na hapa..namchukua Erin tunarudi zetu shamba” anasema Roda, “umeanza” anasema Mkwere kwa mshtuko huku akigeuka kumuangalia Roda, “habari ndio hiyo Baba Erin” anasema Roda, wanabaki kimya kwa muda, “ulijigamba umepata kazi mambo mazuri..kumbe”, anasema Roda na kutulia, “kila siku ni kulalama tu” Roda anaendelea kusema, “kama hilo gari bovu unang’ang’ania hiyo kazi ya nini?” anasema Roda, wanabaki kimya kwa muda, Mkwere anashusha pumzi, “mimi ni Mwanaume..sitakosa ufumbuzi” anasema Mkwere huku anainuka, “na hilo la kurudi Shamba utarudi wewe mwenyewe mwanangu haondoki hapa” anasema Mkwere huku anachukua mswaki na taulo na kutoka, “tutaona” anasema Roda baada ya Mkwere kutoka nje.
NYUMBANI KWA BONGE-ASUBUHI.
Mkwere akiwa juu ya bodaboda wanafika mbele ya geti, anashuka kutoka kwenye boda boda na kwenda kugonga geti, geti linafunguliwa na Mzee Matata,mzee wa miaka 70, “Shikamoo Mzee” Mkwere anamsabahi Mzee Matata huku anaingia getini,“marahaba kijana wangu..vipi leo mbona unaonekana mnyonge?” anauliza Mzee Matata huku akitoa Daftari na kumpatia Mkwere, “achana na madaftari yako kwanza..bosi yupo?” anasema Mkwere bila kupokea lile daftari, “ameshatoka..kwani vipi?” anauliza Mzee Matata, “Mke wake?” anauliza tena Mkwere, “yupo ndani..kuna nini mbona sikuelewi” anauliza Mzee Matata, “kazi yao siitaki tena” anasema Mkwere huku anaketi kwenye kiti kilichopo pale getini, “namsubiri Mkewe hapa nimwambie” Mzee Matata anabaki anamuangalia Mkwere kwa mshangao, “ningeamua kuishia huko huko lakini maisha kuna leo na kesho..acha niwaage tu vizuri” “kwa hiyo nikupe maagizo aliyoacha Mzee ama niache tu?”, “maagizo gani?” anauliza Mkwere, “alisema leo utumie hiyo Premior mpya ya Mama” Mkwere anashtuka na kumuangalia Mzee Matata, kisha anageuka kuiangalia ile Toyota Premior mpya ya silva yenye usajili wa DDM kwenye plate number, “ndio alivyosema?” anauliza Mkwere kwa mshangao, “na kasema ukiikwaruza hata kwa kucha unarudia kwenye ule mkweche wako” anaongeza Mzee Matata huku akimpatia Mkwere ufunguo wa gari, Mkwere anapokea ule ufunguo huku akionekana bado ana butwaa, “uwe makini..si unamjua huyu Mama mtiti wake?” anasema Mzee Matata huku wanaelekea ilipo gari, “na ukipata trip ya madongo kuinama achana nayo”, “usinifundishe kazi wewe mzee..maana unaongea sana kama redio ya kijiji” anasema Mkwere huku anafungua mlango na kuingia kwenye gari, anapiga moto, “hujasaini” anasema Mzee Matata huku akimpa Mkwere daftari, Mkwere anapokea daftari, anasaini na kumrudishia Mzee Matata lile daftari kisha anafunga mlango na kutoa simu na kuibofya, “Mama Erin” Mkwere kwa bashasha na tabasamu kubwa anaongea na simu, “nenda kwa Mama mwenye nyumba mwambie pesa yake ipo tayari” anasema Mkwere, “imekuwaje kwani?” anauliza Roda kwenye simu, “leo nimeanza kazi rasmi” anasema Mkwere, “umepata kazi mpya?” anauliza Roda, “kazi ni ile ile gari ndio mpya” anasema Mkwere, “bado sijakuelewa Baba Erin”, anasema Roda, “napita hapo muda si mrefu utanielewa tu” anasema Mkwere, “mmh” anaguna Roda, “baadae ngoja nikapige kazi” anasema Mkwere na kuitoa simu sikioni, anashusha kioo “fungua geti wewe Mzee” Mkwere anapayuka, “usinifundishe kazi wewe Mtoto” Matata anasema huku akienda getini na kufungua geti na gari inatoka.
HOTELI MNAZI MMOJA-NDANI-ASUBUHI
Idd Riss, kijana wa miaka 27 hivi, mtanashati aliyevalia maridadi, anafika mapokezi huku akiwa amebeba jaketi mkononi na mkoba mdogo wa ngozi, anaangalia saa yake ya mkononi, “Watu wa Arusha utawajua tu” anashtushwa na maneno ya Adela, dada mrembo wa pale mapokezi “narudi nyumbani ooo” Idd Riss anaimba huku akisogea na kuweka mkoba na jaketi juu ya meza ya mapokezi, “lete bili yangu” anasema Idd Riss, “ndio safari?” anauliza Adela, “sio kitu ya kuuliza” anajibu Idd Riss huku akipokea bili kutoka kwa Adela, anaingiza mkono mfukoni na kutoa waleti, anatoa bunda la noti na kumpatia Adela, Adela anapokea na kuanza kuhesabu “keep chenji” Idd Riss anasema huku akiinua mkoba na jaketi lake na kuondoka, Adela anabaki akiwa na tabasamu kubwa usoni, “safari njema” anasema Adela kwa sauti ya juu iliyojaa bashasha huku Idd Riss akitoka mlangoni.
HOTELI BLUE SEA KARIAKOO-NDANI-ASUBUHI
Adamuu, jamaa,27 aliyevalia maridadi nguo zenye gharama, yupo mapokezi akiwa na jaketi mkononi, anatoa pesa na kumpatia bwana aliyepo pale mapokezi, kisha anachukua mkoba ulio juu ya meza ya mapokezi, anaelekea mlangoni na kutoka.