***SURA YA THEMANINI NA MBILI***
(MSIMU WA 02)
MTUNZI: Stevie Mollel
No; 0685 758 123
Ilichukua muda mrefu sasa Kaguta hajarejea, Miraji na Bakari wakapata mashaka. Kwa mujibu wa saa ya ukutani alikuwa anatimiza masaa matano sasa akiwa nje. Sio masaa matano ya kawaida, masaa matano ya usiku tena kwenye nchi ngeni, nchi ya adui.
Waliona yapaswa Vitalis kushirikishwa. Miraji aliendea chumba alalacho Vitalis na Bernadetha akabofya kengele. Baada tu ya muda mfupi, Vitalis akafungua mlango. Alikuwa amevalia bukta fupi tu. Kifua chake cha mazoezi kilichobebelea nywele kadhaa kilikuwa wazi. Macho yake yalikuwa yamepooza ila si kwa kulala, aidha kuna kitu alikuwa anafanya ama anakitizama.
“Kaguta hayupo ndani, na hajarudi mpaka sasa hivi tokea alivyotoka jioni hii.” Alisema Miraji. Uso wake ulieleza shaka.
“Ameenda wapi?” Vitalis aliuliza. Alikuwa ametoa macho yake nje, uso wake ameukunja. Haikuwa habari njema hiyo.
“Alituaga anaenda café kubadili chakula.”
‘Café ipi?” Vitalis aliwahi kuuliza. Alionekana kupoteza subira.
“Sijui! Alisema tu café.”
Vitalis aliingia ndani ya chumba, baada tu ya dakika moja alitoka nje akiwa amevalia suruali ya jeans na raba huku akifunga vifungo vya shati.
“Acha niende. Bakia hapa hapa utizame usalama, sawa?”
“Kwanini tusiende wote?”
“Miraji, ni hatari. Nisingependa kumhatarisha ama kumpoteza yeyote kabla ya kuanza kutimiza mipango yetu. Baki hapa, huwezi jua labda ni mchezo wa kututawanya. Inabidi tuwe wa tahadhari sana.”
Kishingo upande, Miraji aliridhia. Vitalis aliondoka upesi akimuacha mwanaume huyo akimtazama anavyoyoma, hata mlango hakuufunga.
Alipopotea, Miraji alitazama ndani kwa kupitia mwanya ulioachwa na mlango akaona karatasi kubwa jeupe limelazwa mezani. Alijaribu kulivutia taswira ila hakuipata vema kutoka na umbali aliopo. Hakuingia ndani, labda alihofia anaweza mkuta mama yake ameketi vibaya. Alifunga mlango akarejea chumbani kwake alipompasha Bakari habari.
Vitalis alishuka ngazi upesi akajikuta kaunta alipotoa taarifa ya kutoka kwake. Akiwa kwenye mwendo wa kasi, alitoka nje ya hoteli.
Watu walikuwa wachache sana mtaani, pia na magari. Ungeweza kuyahesabu pasipo shida. Hali ya ubaridi bado iliendelea kutawala na kila mtu aliyeonekana basi alikuwa amevalia nguo nzito ya kumsitiri, isipokuwa Vitalis.
Vitalis aliperuzi huku na huko asione cha maana. Alimuuliza mtu mmoja aliyekutana naye barabarani kuhusu café iliyoko karibu akaelekezwa. Alikata mtaa mpaka ilipo café hiyo. Ilikuwa ndiyo ile aliyokuwamo Kaguta masaa kadhaa nyuma. Alikuta imefungwa tayari.
Alishusha pumzi ndefu akitafakuri. Hakuwa na pa kwenda wala cha kufanya zaidi. Moyo wake ulijazwa na hofu juu ya wapi alipo Kaguta, na usalama wake.
Alishika kiuno akawa anarejea alipotokea taratibu. Uso wake aliuelekezea chini akitazama sakafu iliyopokea lami pana ya njia nne. Alipofika maeneo ya supermarket akaona kitu. Ilikuwa ni bangili ipo chini. Malighafi yake ya metali iling’aa na kudaka macho ya Vitalis.
Aliinama akaiokota na kuitizama vema.
“Kaguta.”
Vitalis alijikuta akisema kwa bumbuwazi. Aliikumbuka ile bangili, ndio. Kaguta aliinunua bangili hiyo nje ya airport baada tu ya kutua. Sasa aliikuta barabarani na si mkononi mwa Kaguta. Yupo wapi?
Vitalis alitazama kushoto kwake akaona jengo la supermarket lililo gizani, lilikuwa tayari limefungwa. Hakuwepo wa kumuuliza chochote.
Alifuata barabara usawa wa eneo bangili ilipodondokea, akatizama vema. Hakuona kitu. Alitoa simu mfukoni akamulika barabarani hapo akaona alama za mchubuko wa matairi ya magari. Hapo akawa tayari amegundua jambo.
Kitu pekee alichokipata sasa ni kwamba Kaguta ametekwa. Hakukuwa na namna kwamba alidondosha bangili ile mpya aliyovutiwa nayo pindi tu alipoitizama. Hakuingia akilini pia kwamba mwanaume huyo alidondoka chini akaiacha bangili hapo. Kilichooneka kina maana kichwani mwa Vitalis ni kwamba kulikuwa na pambano, Kaguta alishindwa kwa kudondoshewa chini kisha akakwapuliwa na kuingizwa kwenye gari lililoondoka kwa kasi ya kuchubua barabara.
Alisimama akajiuliza:
“Wakina nani watakuwa wamemteka? … Kim? … Ina maana anajua tulipo? Anajua tunapoishi? … Ina mana anatufuatilia?”
Alijikuta anapata hofu. Vipi kama kule hotelini atakuwa ame …?
Alitoa macho kwa uoga.
Haraka alikimbia kwenda hotelini pasipo kuweka kituo popote. Alienda haraka chumbani kwake akafungua mlango, hakukuta mtu. Chumba kilikuwa kitupu lakini kikiwa hovyo, kila kitu kilikuwa shaghalabaghala.
Jasho lilimtoka Vitalis na moyo ulienda mbio kupita kiasi.
Aliendea milango ya bafu na choo akaifungua pasi hodi, napo hakukuta mtu. Alitoka upesi akaenda chumba cha wakina Miraji. Napo huko alikuta kama vile alivyokuta chumba chake, hakukuwa na mtu na kulikuwa hovyo hovyo. Hapo akachoka zaidi. Alihisi ‘joint’ zimepoteza nguvu ghafla.
Alizidiwa kete. Adui alimtangulia mbele hatua moja.
Aliketi kitandani akiwa kama mtu asiyeamini. Kwa muda kidogo akili iligoma kuchambua mambo. Baada ya dakika kumi ama zaidi alinyanyuka akaenda kaunta kukutana na mapokezi na wahudumu.
Aliwaulizia wenzake pasipo mafanikio, hakuna mhudumu aliyesema ameshuhudia chochote. Hata pale Vitalis alipoomba kamera zitumike, hakupewa majibu ya maana.
Haikumuwia vigumu kuelewa hali aliyomo. Kwa yale aliyoyashuhudia aliishia kutambua kwamba: yupo kwenye nchi ya adui, na si tu kwamba yupo ndani ya nchi hiyo, bali yupo ndani ya nchi iliyoshikiliwa na mikono ya adui; mikono yake ipo kila eneo; mikono yake ina nguvu ya kunyonga na kukata hata akiwa ofisini. Mikono yake ni ya chuma.
“Tuwataarifu polisi?” Mwanamapokezi aliuliza.
“Hapana.” Vitalis akajibu. Hakuwa na imani na polisi pia.
Alirejea chumbani akapekenyua kwenye mojawapo ya begi na kutoa fedha alizozitia mfukoni. Kabla hajatoka nje ya chumba hicho aliona kiasi kidogo cha damu chini ukutani, mbali kidogo na mlango. Alisogea eneo hilo akaona damu zaidi kwa chini, ila haikuwa nyingi kiasi cha kumfanya mtu aone upesi ukizingatia ilikuwa zuliani.
Vitalis alitazama damu hiyo ya ukutani akaona imechorewa jambo. Ilikuwa ni kama ka alama ka paa mbili za nyumba zikigusana.
Alitafakari alama hiyo inamaanisha nini kwa dakika moja. Alikuja kugundua baada ya kufananisha taswira ya muonekano wa jengo la Mr Kim na mchoro ule.
likumbuka mojawapo ya eneo waliloliona vema walipokuwa kwenye ile hoteli wakitazama jengo la Kim, ni majengo mawili ya mshenzi uyo yakiwa yamepakana paa. Ina maana Bernadetha na wenzake wamepelekwa huko?
Pasipo na shaka Bernadetha alipigwa kwanza kabla ya kubebwa, hii ni damu yake. Na inaelekea aliambiwa wapi anapelekwa kabla hajabebwa. Hiki alichokiandika ukutani atakuwa alikifanya kwa umakini mkubwa asionekane ili anifikishie mimi taarifa, Vitalis aliwaza.
Alisaga meno yake akikunja ndita kabla hajanyanyuka na kupotelea kusikojulikana.
***
☆Stevie