***SURA YA THEMANINI NA TATU***
(MSIMU WA 02)
MTUNZI: Stevie Mollel
No: 0685 758 123
Ilikuwa asubuhi sasa ya saa mbili, jiji la Hamilton lilikuwa bize magari na watu wakipishana.
Miongoni mwa watu walioujaza mji, alikuwamo Vitalis. Alikuwa amevaa koti refu jeusi na kofia ‘cowboy’. Mikono yake aliidumbukiza mfukoni kama mtu anayehisi baridi akitembea kuelekea upande wake wa kaskazini.
Aliona taksi akainyooshea mkono, taksi ikasimama. Aliingia ndani ya taksi hiyo akampa maelekezo dereva ampeleke nje kabisa ya jiji, huko vijijini. Dereva, mwanaume mzee mweusi aliyevalia kapelo iliyochoka na shati la bluu iliyopauka, alimtazama mteja wake huyo kwa mashaka. Alimuuliza:
“Una pesa ya kunilipa kukupeleka kote huko?”
Vitalis alitoa pesa kwenye koti lake, noti kadhaa za dola za kimarekani akamuonyesha dereva, dereva akatikisa kichwa akitabasamu. Alipangua gia akakanyaga mafuta.
Kwa muda wa dakika kama ishirini ama zaidi walitembea pasipo yeyote kuongea. Dereva alimtazama mteja wake kwa kupitia kioo kilicho juu ya kichwa chake mara mbili akamuona mteja wake huyo akitazama nje. Alionekana kuboreka. Alipomtazama kwa mara ya tatu kiooni na kumuona yu vile vile, alimuongelesha.
“Pasipo mashaka, wewe ni mgeni, sio?”
Vitalis alimtazama mzee huyo akatikisa kichwa kukubali.
“Nilivyokuona tu ukinielekeza nikajua wewe ni mgeni. Kama ungekuwa mwenyeji ungepanda basi na si taksi. Ila sio mbaya, umemsaidia mzee wako kuona siku njema leo.”
Vitalis hakusema kitu. Aliendelea kutazama nje.
“Kwanini umeamua kwenda huko?” Dereva aliuliza akimtazama Vitalis kiooni. “Hakuna kitu cha utalii huko zaidi tu ya mashamba.”
“Najua.” Vitalis alijibu kiufupi akiendelea kutazama nje.
Dereva alilazimisha kutabasamu, akaendelea kuongea:
“Kama ukitaka nikutembeze sehemu za utalii, nitakufanyia kwa bei poa sana. Najua sehemu zote za kuvutia ndani ya hii nchi. Umeona namba yangu nyuma ya kiti nilichokaa? Ukintafuta muda wowote siku yoyote nitakufanya ufurahi sana kuwepo hapa.”
“Ahsante.” Vitalis alijibu akitazama nje.
Dereva alibinua mdomo wake akapandisha mabega. Alikaa kimya kwa dakika kama tatu kisha akaanza kuongea tena:
“Kwanini umeamua kwenda huko kijijini? Sio salama sana. Muda si mrefu kuna watu wawili waliuwawa huko. Mmojawao aliuwawa kwa risasi.”
Vitalis kimya.
“Ni tahadhari tu.” Dereva alijitetea kisha akafunga mdomo wake. Baada ya dakika moja, Vitalis aliuliza:
“Watu hao waliofanya mauaji wamekamatwa?”
Bado uso wake ulikuwa unatazama nje.
“Wakamatwe wapi!” Dereva alihororoja. “Tokea mamlaka haya ya nchi yaingie kwenye dola, hakuna muuaji yeyote aliyewahi kukamatwa nchi hii. Hakuna! Tunafanya tu kusikia watu wameuwawa huku na kule. Lakini hakuna aliyewahi kutiwa nguvuni. Hata pale wananchi wanapotoa taarifa, inakuwa kazi bure. Sana sana huyo aliyetoa taarifa naye hatochukua zaidi ya siku moja kuuwawa.”
Hapo Vitalis alihamisha uso wake kutoka nje akamtazama dereva. Macho yake yalionyesha amevutwa hisia.
“Sio kwamba nakutisha.” Dereva alijitetea, “Ila nakupa hali halisi ya nchi hii. Kwa miaka kadhaa tumekuwa tukihofia sana usalama wetu.”
Walikuwa sasa nje ya jiji. Waliacha majengo mazuri marefu mbali wakishika njia kuelekea kijijini.
Dereva bado alikuwa anaongea, Vitalis asitie neno bali tu kumsikiliza.
Haikumchukua muda mrefu baada ya kuacha jiji, Vitalis akagundua wanafuatiliwa. Nyuma yao kulikuwa kuna gari ‘cadillac’ nyeusi ‘tinted’ inakuja kwa kasi. Aliitazama gari hiyo kwa macho makini akitumia vioo vya gari.
Gari hiyo ilipunguza mwendo ilipokaribia taksi, kisha vioo vya viti vya nyuma vikashuka chini wakatoka wanaume wawili kila pande wakiwa wamebebelea bunduki kubwa nzito. Walikuwa wamevalia suti na miwani nyeusi.
“Inama chini!”
Vitalis akamuamuru dereva. Dereva asijue linaloendelea, aliuliza:
“Niiname? Sasa nitaendeshaje?”
Alipomaliza tu hiyo kauli, risasi zilizorushwa hovyo kulenga gari zilimpasua bongo. Gari liliyumbayumba. Vitalis alinyoosha mikono yake akashika usukani, akajaribu kulimudu gari hilo lililozidi kumiminiwa risasi za kutosha.
Alimvutia dereva kiti cha kando, akapata kukaa nafasi nzuri aliyoweza kulimudu gari vema. Mkono wake mmoja ulishikilia usukani huku mwingine ukikanyagia mafuta.
Wanaume wale waliokuwa wanamimina risasi waliacha hilo zoezi wakaingia ndani ya gari na vioo vikafungwa. Sasa gari liliongeza kasi likagonga taksi kwa nyuma kwanguvu. Taksi lilienda mbele mputa mputa. Vitalis alijitahidi sana kulibakiza barabarani. Haraka alijivuta toka nyuma akakaa kwenye kiti cha dereva. Vioo vya pembeni vya gari vilikuwa tayari vimeondolewa na risasi. Vitalis alikuwa anatumia kioo pekee kilicho juu yake kuwatizama maadui.
Alikanyaga mafuta kwanguvu, taksi ikapepea. Nyuma yake ‘cadillac’ nayo iliongeza kasi maradufu ikawa inamfukuzia.
Ilibidi akili itumike sasa. Alikuwa mwenyewe pia akiwa hana silaha. Silaha pekee aliyokuwa nayo ni akili kichwani ambayo kwa muda huo ilikuwa inahangaika kutafuta jibu la jinsi gani atajinasua kwenye janga hilo. Hakukuwa na muda, ilibidi akili ifanye kazi mara mbili ya kawaida.
Kwa kasi kubwa, cadillac ilisogelea taksi. Ilibakia kaumbali kadogo sana gari hilo kubwa libamize taksi. Vitalis alitazama kiooni kwa makini kana kwamba kuna kitu anangojea.
Cadillac ilipomsogelea zaidi, akasema:
“Tayari.”
Ghafla alisogeza taksi pembeni kidogo upande wa kulia kwa kasi ya ajabu kisha akapiga breki kali.
Bodi ya pembeni ya taksi ilimezwa na gari kubwa la Cadillac ambalo liliparamia bodi hiyo na tairi lake moja la kulia. Kutokana na kasi lilikuwemo, cadillac lilinyanyuka juu juu na kupinduka vibaya likibiringita mara sita. Hakuna aliyetoka hai.
Vitalis alikanyaga mafuta ndani ya taksi akaisogelea hiyo cadillac. Alisimamisha kando yake akalitizama kwa kinyaa.
Alitema mate nje ya gari, ptuuh!, akasema akibinua mdomo:
“Wasalimie kuzimu.”
Kisha akatia moto taksi na kutimka zake.
Ilimchukua dakika chache tu kuwasili eneo alilokuwa analihitaji – lile aliloliona kwenye taarifa ya habari.
Kwa msaada wa maelekezo ya hapa na pale aliyopewa na wenyeji, hatimaye alifika mbele ya nyumba ya marehemu Kelly na Johnny.
Ilikuwa pweke kwa kuitazama tu hata kwa nje.
Vitalis aliitazama kisha akashusha pumzi ndefu kabla hajaanza kuchukua hatua kusogea mlangoni.
Pasipo kugonga hodi wala kuhangaika na mlango huo uliokuwa umefungwa, alichambua mazingira. Kwa haraka akaona mkanda wa njano uliosomeka – Police, don’t cross the line, ukiwa kando kando umeachwa pasipo mashiko. Haukuwa na maana tena, ndivyo ambavyo ungesema kutokana na kutokuwepo kwake mahala husika wakati husika.
Vitalis alibinua mdomo wake akijisogeza dirishani mwa nyumba hiyo na kuchungulia ndani.
Sebule ilikuwa shaghalabaghala. Hakukuwa na dalili yoyote ya binadamu.
Vitalis alikunja shingo yake akatazama kushoto mwa nyumba hiyo alipoona nyumba iliyokuwa karibu zaidi zikiwa zinatazamana madirisha ya pembeni.
Alisogelea nyumba hiyo akagonga mlango. Punde akatoka mwanamama mfupi mzee. Nywele zake zilikuwa nyeupe pe uso wake ukikunjamana vilivyo.
Alimtazama Vitalis na macho yake ndani ya miwani kubwa kama vile anajitahidi kuing’amua sura hiyo aliyowahi kuiona hapo nyuma.
Vitalis alitabasamu kidogo kabla hajamsalimu kwa kumpa mkono.
Bibi huyo asipokee mkono wa Vitalis, aliuliza kwa sauti yake kavu:
“We ni nani? Mbona kama nakujua?”
Vitalis akatabasamu zaidi, ila akiwa na uso wa tahadhari.
“Kweli?”
“Ndio. Kwani wewe haunijui?”
“Mama, umeanza!”
Sauti nyembamba ya kike iliita tokea ndani.
Mlango ulifunguliwa akatokea mwanamama mwekundu mnene kiasi. Nywele zake ndefu za kahawia na mwenye macho ya ukali. Alikuwa amevalia gauni refu la maua maua lililobanwa kiunoni na kamba ya nguo hiyo.
Alitabasamu kumtazama Vitalis, akasalimu.
“Tafadhali, karibu ndani. Samahani kwa usumbufu wa mama yangu, kila mtu akija hapa lazima amwambie maneno hayo hayo.”
“Usijali.”
Alisema Vitalis akipiga hatua kuingia ndani wakati yule bibi akitokomea kufuata ngazi na mwendo wake wa kinyonga.
Ilimchukua Vitalis dakika mbili kumtambua yule mwanamke aliyekamrimu ndani. Alikuwa ni mmojawao wa wale waliotua ushuhuda wao kwenye televisheni juu ya kifo cha Kelly na mumewe.
Jambo hilo lilimpa afueni, uso wake ukawa mwepesi zaidi.
“Samahani sana kwa usumbufu, naitwa Vitalis. Nimekuja hapa kwa ajili ya kupata taarifa zaidi juu ya kifo cha majirani zako. Naomba ushirikiano wako.”
“Wewe ni mwandishi wa habari?” Aliuliza mwanamke yule akimtazama Vitalis na macho yaliyoboreka punde tu kusikia.
“Yah! Ni mwandishi wa habari, ila ni wa upelelezi.” Alijibu Vitalis kwa kujiamini lakini mama yule hakuonyesha kushtushwa na hilo.
“Unajua wamekuja waandishi wengi sana wa habari hapa, na mapolisi pia wakitaka kufahamu yaliyotukia. Ila ninachokijua ni kwamba hakuna lolote litakalotokea. Ni upepo tu utakaopita kama pepo zingine. Sioni kama kuna haja ya mimi kuongea tena na tena kila siku kwa kitu ambacho hata kama nikiongeaje hakitaleta mabadiliko yoyote.”
“Lakini muda huu haitokuwa tena kama huko mwanzoni.” Vitalis alisema akimtazama mwanamke anayeongea naye. Macho yake yalionyesha ni namna gani anamaanisha kile kilichotoka mdomoni.
Hapo mwanamke yule akavutiwa. Macho yake yaliwaka hamu ya kutaka kufahamu.
“Una maanisha nini?”
“Sasa hivi wauaji watakamatwa. Nao watauwawa.”
Kwa muda mfupi kidogo kukawa kimya wakitazamana.
“Nakuhakikishia hiki ninachokuambia. Maneno yako hayataenda bure.” Vitalis alitia msisitizo.
Ni kama vile alimpa nguvu fulani mwanamke yule aliyekuwa anatazamana naye. Mwanamke huyo alimtazama Vitalis machoni kisha akaurushia uso wake chini na kuanza kueleza yote kwa pande ambayo aliliona tukio.
Sauti yake yembamba ilikuwa nyembamba zaidi akisimulia. Ila haikusita pia kukwaana na kilio pale palipokuwa pagumu kueleza. Mpaka anamaliza kusema yote uso wake ulikuwa umelowana machozi na sauti yake ilikuwa imefifia zaidi.
Vitalis aliweka mkono wake kwenye bega la mama huyo, akamuuliza:
“Unadhani kwanini Kelly na hao watu walienda uelekeo huo?”
Mwanamke yule akavuta kwanza makamasi mara mbili. Akiwa anaminyaminya vidole vyake, alijibu:
“Sijui ni kwanini. Ila huko walipokuwa wanaelekea ni njia karibu na bahari, itakuwa aliwatoroshea huko.”
Alijifuta pua na mgongo wa kiganja chake, kisha akaendelea:
“Walitumia boti ya Kelly kutoroka nayo maana polisi walisema hawakuikuta hiyo boti huko ufukweni.”
“Kelly alikuwa ana boti?”
“Ndio, alikuwa nayo. Si tu boti bali pia nyumba japokuwa amefariki ameiacha bado haijakamilika … Unajua Kelly alikuwa na wakati mgumu sana kuishi na mumewe, Johnny. Mume wake hakuwa mtu wa kuwaza maendeleo bali pombe na wanawake. Kidogo alichokuwa anapata kwenye kilimo alikuwa anawekeza pasipo mumewe kujua.”
Kuna kitu kikagonga kichwani mwa Vitalis.
“Unaweza ukanielekeza hiyo nyumba yake ilipo?”
Mwanamke alisita.
Alimtazama Vitalis machoni kama mtu anayewazua jambo. Baada ya muda mfupi, akatua zigo lake la hofu.
“Ndio, naweza.”
Vitalis akatabasamu.
Mwanamke huyo alimuelekeza Vitalis akitumia mikono yake kama ramani. Kwa muda wa kama dakika tatu, alifanya tukio hilo kufanikiwa pasipo kujua kama Vitalis ni mgeni nchini.
Kwa kutazama na kusikiliza kwa makini, Vitalis aliweka maelezo kichwani, akamuaga mwenyeji wake kabla ya kujirudisha kwenye gari alilokuja nalo lililokuwa na majeraha karibia kila pande na kuondoka eneo hilo.
Alichukua takribani masaa mawili na nusu kufika alipolenga.
Ilikuwa ni nyumba yenye ukubwa wa kati ikiwa haijamaliziwa kupakwa rangi wala kuezekwa paa. Ilikuwa imekaa mbali kidogo na shurba za watu – sehemu tulivu ambapo pangekuhitaji sababu kubwa kukufanya uende hapo.
Nyumba ilikuwa imezingirwa na majani marefu ambayo yalichora njia zinazotumika kuingilia ndani ya nyumba. Njia hizo nazo hazikuwa safi kama tujuavyo, zilikuwa na majani pia lakini yakiwa mafupi kuliko ya kando kando.
Vitalis alipekua eneo hilo na macho upesi. Hakuona dalili ya yeyote kuishi hapo. Aliegemea gari akaendelea kupekua eneo hilo kwa dakika kama mbili ama zaidi kabla hajaanza kuchukua hatua kwenda ndani.
Alifika sebuleni pasipo kuona kitu. Alipita vile vile chumba cha kwanza, pili na tatu pasipo kuona mtu.
Lakini baada ya muda mfupi akaona alama za unyayo wa kiatu koridoni. Hakukuwa na sakafu. Ardhi ilikuwa rafu na ngumu hivyo kuona jambo kama hilo ilihitaji umakini mno kwenye utazamaji.
Vitalis alichuchumaa akatazama alama hiyo kwa karibu. Alirusha macho yake aone kama ataona nyingine, hakufanikiwa.
Kabla hajajua achukue hatua gani ya pili, alishituka kusikia kishindo nyuma yake. Aligeuka upesi akakutana na teke lililokita chini ya taya bila huruma na kumrushia mbali.
Kabla hata hajafungua macho alishaamriwa ageukie ukutani na anyooshe mikono juu kabla hajalipuliwa na risasi. Haraka aliusogelea ukuta akipeleka mikono yake juu.
“Mimi sio adui yenu!”
Vitalis alijitetea.
Kivuli cha mwanaume aliyemnyooshea bunduki kilijongea kumfuata.
Mwanaume huyo alisimama nyuma yake, akamuuliza akiwa ameweka mdomo wa bunduki kisogoni.
“Wewe ni nani na unafanya nini hapa?”
Sauti haikuwa ngeni.
Ilikuwa na ka-lafudhi ka-kihindi ndani yake japokuwa ilisema kwa mkazo usio na tone la utani.
Likiwa jibu langojewa, mdomo wa bunduki uliendelea kushindiliwa kwenye kichwa cha Vitalis kwanguvu.
“Naitwa Vitalis – Vitalis Byabata toka Tanzania.”
Vitalis alijieleza. Alikuwa anatota jasho.
Muda mfupi mdomo wa bunduki uliondolewa kichwani kwake swali likiulizwa:
“Vitalis?”
“Ndio.” Vitalis akajibu akitikisa kichwa.
“Umekuja kufanya nini huku?”
“Kumuua Kim.”
Kimya.
“Umejuaje kama tupo hapa? Nani kakuambia?”
“Nilifuatilia kwa Kelly. Jirani yake alinambia ana nyumba yake maeneo haya nikajua fika mtakuwa huku.”
“Hakuna mtu anayekufuatilia?”
Rajul aliuliza akiangazaangaza.
“Hamna mtu yoyote. Nilihakikisha nipo mwenyewe.”
Rajul alirudisha bunduki kiunoni akamtaka Vitalis anyanyuke.
Alikuwa amevalia suruali nyeusi ya kadeti pamoja na shati jeupe, miguuni alikuwa peku. Kichwa chake kilichozoeleka kutokuwa na nywele, kilikuwa kimeshamiri kedekede pamoja pia na ndevu.
Ni macho na sauti yake ndivyo bado vingekufanya umgundue. Tena baada ya kumfanyia uchambuzi yakinifu.
Aliongozana na Vitalis kwenda chumba cha kwanza kabisa ambapo alijongea karibu na kona ya dirisha akakanyaga chini kwanguvu mara tatu na mara kukafunguliwa.
Ilikuwa ni kama andaki. Mlango wake ulikuwa ngumu kutambuliwa kwasababu ya kutandazwa udongo juu yake ambao haukonyesha tofauti yoyote na wa kando kando.
Waliingia ndani wakamkuta Stanis. Alikuwa kifua wazi akiwa amevalia suruali pekee. Mwili wake ulikuwa na makovu mengi kama kenge ila lisionekane jeraha hata moja. Alikuwa anamimina jasho jingi. Kwa hali ya joto mule ndani ya handaki halikuwa la kushangaza hilo.
Kwa chini kulikuwa kumetandazwa jamvi na ndilo hilo lilikuwa linatumika kama kitanda. Kwenye jamvi hilo konani pia kulikuwa na kofia la nywele, na pasipo shaka lilikuwa ni mahususi kwa ajili ya Stanis kujifichia uso asijulikane.
Rajul alivua nywele na ndevu zake za bandia, akamwambia Stanis:
“Tumepata ugeni kutoka kwa wageni.”
Stanis alimtazama Vitalis kwa macho ya kutafuta. Rajul alimsogelea karibu akamwambia:
“Anaitwa Vitalis, toka Tanzania. Nafikiri hilo si jina geni kwako.”
“Vitalis?” Stanis alishangaa akimtazama Vitalis. Ni kana kwamba alikuwa anajaribu kuvuta kumbukumbu yake juu ya hilo jina.
“Ndio, Vitalis. Amemsumbua sana mkuu wako, Kim, huko Tanzania. Kim alikuwa akiniambia sana habari za huko nyumbani kwake kwa pili. Sasa amekuja Bermuda kumaliza biashara yake aliyoianza.”
“Nini kinakufanya udhani utafanikiwa, Vitalis?” Stanis aliuliza.
Vitalis alimtazama na macho yaliyoonyesha hamu ya damu. Aliminya lips zake akasema:
“Sina kitu wala kazi nyingine kwa sasa zaidi ya Kim. Alichonipotezea hakiwezi kurejeshwa kwa njia yoyote ile na moyo wangu hautotulia kamwe mpaka pale nitakapohakikisha hayupo tena duniani.”
Kulikuwa kimya kidogo kama vile kuna kitu kimepita. Stanis na Rajul walimtazama Vitalis na ni wazi waliona jinsi kiu yake ya kisasi ilivyo kali usoni.
“Amepoteza familia yangu. Amepoteza rafiki zangu. Amepoteza kazi yangu. Amepoteza na anaendelea kupoteza watu kila kukicha kwenye nchi yangu aidha kwa madawa, ama kafara. Amekuwa mchango mkubwa wa kudorora kwa serikali na maendeleo ya nchi yangu. Hastahili kuishi kwa amani. Hastahili kuwepo duniani. Kuendelea kwake kuvuta pumzi ni mzigo na adhabu kwa wengi.”
Stanis na Rajul walitazamana. Ni kama kuna jambo waliteta na macho yao kabla ya Rajul kuuliza:
“Wenzako wapo wapi? Najua haupo peke yako.”
“Wametekwa wote na Kim.” Vitalis alijibu upesi. “Alinitangulia hatua moja mbele, akafanikiwa kunizidi kete.”
“Vitalis.” Rajul aliita. Uso wake ulikuwa na miale ya huruma.
“Huku si Tanzania. Kim anajua kila sehemu ya nchi hii, kila sehemu. Hakuna mahali ambapo hana mtu wake wa kumuangalizia jambo. Iliwapasa kuwa makini sana. Si tu kwamba ana ushawishi kila Nyanja, lakini pia ana mkono kila mahali. Ni ngumu sana kupambana naye.”
Akamshika Vitalis bega la kuume.
“Ila ujio wako umenipa nguvu. Sitosita kusaidia nguvu ama akili kwenye kulifanikisha hili. Nimetenda makosa makubwa sana huko nyuma kwa kumsaidia. Nadhani ni wakati sasa wa mimi kulinywa nililolikoroga.”
Kimya kidogo.
“Pumzika kwa sasa, uso wako unaonyesha umepitia mengi. Tutajadili zaidi baadae.”
Aliposema hayo alipanda juu na baada ya muda mfupi akarejea na majani fulani aliyoanza kumkanda nayo Stanis mgongoni.
Japokuwa hakuwa na majeraha, Stanis alikuwa analalamika kwa maumivu.
Aidha bado alikuwa ana maumivu ya ndani kwa ndani.
Vitalis aliyekuwa amekaa kandokando alitazama zoezi hilo likifanyika akiwa na macho ya maswali.
Labda alikuwa anajiuliza nini kilijiri kwenye mgongo ule uliokuwa hautamaniki kwa makovu. Ila hakuuliza.
‘Tutajadili zaidi baadae’ ya Rajul labda itahusisha na hilo jambo, aliwaza.
***
☆Steve