Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

Sasa kama Wageni baadhi wametekwa itakuwa shida maana wanabip faya
 
***SURA YA THEMANINI NA TATU***




(MSIMU WA 02)



MTUNZI: Stevie Mollel




No: 0685 758 123









Ilikuwa asubuhi sasa ya saa mbili, jiji la Hamilton lilikuwa bize magari na watu wakipishana.
Miongoni mwa watu walioujaza mji, alikuwamo Vitalis. Alikuwa amevaa koti refu jeusi na kofia ‘cowboy’. Mikono yake aliidumbukiza mfukoni kama mtu anayehisi baridi akitembea kuelekea upande wake wa kaskazini.
Aliona taksi akainyooshea mkono, taksi ikasimama. Aliingia ndani ya taksi hiyo akampa maelekezo dereva ampeleke nje kabisa ya jiji, huko vijijini. Dereva, mwanaume mzee mweusi aliyevalia kapelo iliyochoka na shati la bluu iliyopauka, alimtazama mteja wake huyo kwa mashaka. Alimuuliza:
“Una pesa ya kunilipa kukupeleka kote huko?”
Vitalis alitoa pesa kwenye koti lake, noti kadhaa za dola za kimarekani akamuonyesha dereva, dereva akatikisa kichwa akitabasamu. Alipangua gia akakanyaga mafuta.
Kwa muda wa dakika kama ishirini ama zaidi walitembea pasipo yeyote kuongea. Dereva alimtazama mteja wake kwa kupitia kioo kilicho juu ya kichwa chake mara mbili akamuona mteja wake huyo akitazama nje. Alionekana kuboreka. Alipomtazama kwa mara ya tatu kiooni na kumuona yu vile vile, alimuongelesha.
“Pasipo mashaka, wewe ni mgeni, sio?”
Vitalis alimtazama mzee huyo akatikisa kichwa kukubali.
“Nilivyokuona tu ukinielekeza nikajua wewe ni mgeni. Kama ungekuwa mwenyeji ungepanda basi na si taksi. Ila sio mbaya, umemsaidia mzee wako kuona siku njema leo.”
Vitalis hakusema kitu. Aliendelea kutazama nje.
“Kwanini umeamua kwenda huko?” Dereva aliuliza akimtazama Vitalis kiooni. “Hakuna kitu cha utalii huko zaidi tu ya mashamba.”
“Najua.” Vitalis alijibu kiufupi akiendelea kutazama nje.
Dereva alilazimisha kutabasamu, akaendelea kuongea:
“Kama ukitaka nikutembeze sehemu za utalii, nitakufanyia kwa bei poa sana. Najua sehemu zote za kuvutia ndani ya hii nchi. Umeona namba yangu nyuma ya kiti nilichokaa? Ukintafuta muda wowote siku yoyote nitakufanya ufurahi sana kuwepo hapa.”
“Ahsante.” Vitalis alijibu akitazama nje.
Dereva alibinua mdomo wake akapandisha mabega. Alikaa kimya kwa dakika kama tatu kisha akaanza kuongea tena:
“Kwanini umeamua kwenda huko kijijini? Sio salama sana. Muda si mrefu kuna watu wawili waliuwawa huko. Mmojawao aliuwawa kwa risasi.”
Vitalis kimya.
“Ni tahadhari tu.” Dereva alijitetea kisha akafunga mdomo wake. Baada ya dakika moja, Vitalis aliuliza:
“Watu hao waliofanya mauaji wamekamatwa?”
Bado uso wake ulikuwa unatazama nje.
“Wakamatwe wapi!” Dereva alihororoja. “Tokea mamlaka haya ya nchi yaingie kwenye dola, hakuna muuaji yeyote aliyewahi kukamatwa nchi hii. Hakuna! Tunafanya tu kusikia watu wameuwawa huku na kule. Lakini hakuna aliyewahi kutiwa nguvuni. Hata pale wananchi wanapotoa taarifa, inakuwa kazi bure. Sana sana huyo aliyetoa taarifa naye hatochukua zaidi ya siku moja kuuwawa.”
Hapo Vitalis alihamisha uso wake kutoka nje akamtazama dereva. Macho yake yalionyesha amevutwa hisia.
“Sio kwamba nakutisha.” Dereva alijitetea, “Ila nakupa hali halisi ya nchi hii. Kwa miaka kadhaa tumekuwa tukihofia sana usalama wetu.”
Walikuwa sasa nje ya jiji. Waliacha majengo mazuri marefu mbali wakishika njia kuelekea kijijini.
Dereva bado alikuwa anaongea, Vitalis asitie neno bali tu kumsikiliza.
Haikumchukua muda mrefu baada ya kuacha jiji, Vitalis akagundua wanafuatiliwa. Nyuma yao kulikuwa kuna gari ‘cadillac’ nyeusi ‘tinted’ inakuja kwa kasi. Aliitazama gari hiyo kwa macho makini akitumia vioo vya gari.
Gari hiyo ilipunguza mwendo ilipokaribia taksi, kisha vioo vya viti vya nyuma vikashuka chini wakatoka wanaume wawili kila pande wakiwa wamebebelea bunduki kubwa nzito. Walikuwa wamevalia suti na miwani nyeusi.
“Inama chini!”
Vitalis akamuamuru dereva. Dereva asijue linaloendelea, aliuliza:
“Niiname? Sasa nitaendeshaje?”
Alipomaliza tu hiyo kauli, risasi zilizorushwa hovyo kulenga gari zilimpasua bongo. Gari liliyumbayumba. Vitalis alinyoosha mikono yake akashika usukani, akajaribu kulimudu gari hilo lililozidi kumiminiwa risasi za kutosha.
Alimvutia dereva kiti cha kando, akapata kukaa nafasi nzuri aliyoweza kulimudu gari vema. Mkono wake mmoja ulishikilia usukani huku mwingine ukikanyagia mafuta.
Wanaume wale waliokuwa wanamimina risasi waliacha hilo zoezi wakaingia ndani ya gari na vioo vikafungwa. Sasa gari liliongeza kasi likagonga taksi kwa nyuma kwanguvu. Taksi lilienda mbele mputa mputa. Vitalis alijitahidi sana kulibakiza barabarani. Haraka alijivuta toka nyuma akakaa kwenye kiti cha dereva. Vioo vya pembeni vya gari vilikuwa tayari vimeondolewa na risasi. Vitalis alikuwa anatumia kioo pekee kilicho juu yake kuwatizama maadui.
Alikanyaga mafuta kwanguvu, taksi ikapepea. Nyuma yake ‘cadillac’ nayo iliongeza kasi maradufu ikawa inamfukuzia.
Ilibidi akili itumike sasa. Alikuwa mwenyewe pia akiwa hana silaha. Silaha pekee aliyokuwa nayo ni akili kichwani ambayo kwa muda huo ilikuwa inahangaika kutafuta jibu la jinsi gani atajinasua kwenye janga hilo. Hakukuwa na muda, ilibidi akili ifanye kazi mara mbili ya kawaida.
Kwa kasi kubwa, cadillac ilisogelea taksi. Ilibakia kaumbali kadogo sana gari hilo kubwa libamize taksi. Vitalis alitazama kiooni kwa makini kana kwamba kuna kitu anangojea.
Cadillac ilipomsogelea zaidi, akasema:
“Tayari.”
Ghafla alisogeza taksi pembeni kidogo upande wa kulia kwa kasi ya ajabu kisha akapiga breki kali.
Bodi ya pembeni ya taksi ilimezwa na gari kubwa la Cadillac ambalo liliparamia bodi hiyo na tairi lake moja la kulia. Kutokana na kasi lilikuwemo, cadillac lilinyanyuka juu juu na kupinduka vibaya likibiringita mara sita. Hakuna aliyetoka hai.
Vitalis alikanyaga mafuta ndani ya taksi akaisogelea hiyo cadillac. Alisimamisha kando yake akalitizama kwa kinyaa.
Alitema mate nje ya gari, ptuuh!, akasema akibinua mdomo:
“Wasalimie kuzimu.”
Kisha akatia moto taksi na kutimka zake.
Ilimchukua dakika chache tu kuwasili eneo alilokuwa analihitaji – lile aliloliona kwenye taarifa ya habari.
Kwa msaada wa maelekezo ya hapa na pale aliyopewa na wenyeji, hatimaye alifika mbele ya nyumba ya marehemu Kelly na Johnny.
Ilikuwa pweke kwa kuitazama tu hata kwa nje.
Vitalis aliitazama kisha akashusha pumzi ndefu kabla hajaanza kuchukua hatua kusogea mlangoni.
Pasipo kugonga hodi wala kuhangaika na mlango huo uliokuwa umefungwa, alichambua mazingira. Kwa haraka akaona mkanda wa njano uliosomeka – Police, don’t cross the line, ukiwa kando kando umeachwa pasipo mashiko. Haukuwa na maana tena, ndivyo ambavyo ungesema kutokana na kutokuwepo kwake mahala husika wakati husika.
Vitalis alibinua mdomo wake akijisogeza dirishani mwa nyumba hiyo na kuchungulia ndani.
Sebule ilikuwa shaghalabaghala. Hakukuwa na dalili yoyote ya binadamu.
Vitalis alikunja shingo yake akatazama kushoto mwa nyumba hiyo alipoona nyumba iliyokuwa karibu zaidi zikiwa zinatazamana madirisha ya pembeni.
Alisogelea nyumba hiyo akagonga mlango. Punde akatoka mwanamama mfupi mzee. Nywele zake zilikuwa nyeupe pe uso wake ukikunjamana vilivyo.
Alimtazama Vitalis na macho yake ndani ya miwani kubwa kama vile anajitahidi kuing’amua sura hiyo aliyowahi kuiona hapo nyuma.
Vitalis alitabasamu kidogo kabla hajamsalimu kwa kumpa mkono.
Bibi huyo asipokee mkono wa Vitalis, aliuliza kwa sauti yake kavu:
“We ni nani? Mbona kama nakujua?”
Vitalis akatabasamu zaidi, ila akiwa na uso wa tahadhari.
“Kweli?”
“Ndio. Kwani wewe haunijui?”
“Mama, umeanza!”
Sauti nyembamba ya kike iliita tokea ndani.
Mlango ulifunguliwa akatokea mwanamama mwekundu mnene kiasi. Nywele zake ndefu za kahawia na mwenye macho ya ukali. Alikuwa amevalia gauni refu la maua maua lililobanwa kiunoni na kamba ya nguo hiyo.
Alitabasamu kumtazama Vitalis, akasalimu.
“Tafadhali, karibu ndani. Samahani kwa usumbufu wa mama yangu, kila mtu akija hapa lazima amwambie maneno hayo hayo.”
“Usijali.”
Alisema Vitalis akipiga hatua kuingia ndani wakati yule bibi akitokomea kufuata ngazi na mwendo wake wa kinyonga.
Ilimchukua Vitalis dakika mbili kumtambua yule mwanamke aliyekamrimu ndani. Alikuwa ni mmojawao wa wale waliotua ushuhuda wao kwenye televisheni juu ya kifo cha Kelly na mumewe.
Jambo hilo lilimpa afueni, uso wake ukawa mwepesi zaidi.
“Samahani sana kwa usumbufu, naitwa Vitalis. Nimekuja hapa kwa ajili ya kupata taarifa zaidi juu ya kifo cha majirani zako. Naomba ushirikiano wako.”
“Wewe ni mwandishi wa habari?” Aliuliza mwanamke yule akimtazama Vitalis na macho yaliyoboreka punde tu kusikia.
“Yah! Ni mwandishi wa habari, ila ni wa upelelezi.” Alijibu Vitalis kwa kujiamini lakini mama yule hakuonyesha kushtushwa na hilo.
“Unajua wamekuja waandishi wengi sana wa habari hapa, na mapolisi pia wakitaka kufahamu yaliyotukia. Ila ninachokijua ni kwamba hakuna lolote litakalotokea. Ni upepo tu utakaopita kama pepo zingine. Sioni kama kuna haja ya mimi kuongea tena na tena kila siku kwa kitu ambacho hata kama nikiongeaje hakitaleta mabadiliko yoyote.”
“Lakini muda huu haitokuwa tena kama huko mwanzoni.” Vitalis alisema akimtazama mwanamke anayeongea naye. Macho yake yalionyesha ni namna gani anamaanisha kile kilichotoka mdomoni.
Hapo mwanamke yule akavutiwa. Macho yake yaliwaka hamu ya kutaka kufahamu.
“Una maanisha nini?”
“Sasa hivi wauaji watakamatwa. Nao watauwawa.”
Kwa muda mfupi kidogo kukawa kimya wakitazamana.
“Nakuhakikishia hiki ninachokuambia. Maneno yako hayataenda bure.” Vitalis alitia msisitizo.
Ni kama vile alimpa nguvu fulani mwanamke yule aliyekuwa anatazamana naye. Mwanamke huyo alimtazama Vitalis machoni kisha akaurushia uso wake chini na kuanza kueleza yote kwa pande ambayo aliliona tukio.
Sauti yake yembamba ilikuwa nyembamba zaidi akisimulia. Ila haikusita pia kukwaana na kilio pale palipokuwa pagumu kueleza. Mpaka anamaliza kusema yote uso wake ulikuwa umelowana machozi na sauti yake ilikuwa imefifia zaidi.
Vitalis aliweka mkono wake kwenye bega la mama huyo, akamuuliza:
“Unadhani kwanini Kelly na hao watu walienda uelekeo huo?”
Mwanamke yule akavuta kwanza makamasi mara mbili. Akiwa anaminyaminya vidole vyake, alijibu:
“Sijui ni kwanini. Ila huko walipokuwa wanaelekea ni njia karibu na bahari, itakuwa aliwatoroshea huko.”
Alijifuta pua na mgongo wa kiganja chake, kisha akaendelea:
“Walitumia boti ya Kelly kutoroka nayo maana polisi walisema hawakuikuta hiyo boti huko ufukweni.”
“Kelly alikuwa ana boti?”
“Ndio, alikuwa nayo. Si tu boti bali pia nyumba japokuwa amefariki ameiacha bado haijakamilika … Unajua Kelly alikuwa na wakati mgumu sana kuishi na mumewe, Johnny. Mume wake hakuwa mtu wa kuwaza maendeleo bali pombe na wanawake. Kidogo alichokuwa anapata kwenye kilimo alikuwa anawekeza pasipo mumewe kujua.”
Kuna kitu kikagonga kichwani mwa Vitalis.
“Unaweza ukanielekeza hiyo nyumba yake ilipo?”
Mwanamke alisita.
Alimtazama Vitalis machoni kama mtu anayewazua jambo. Baada ya muda mfupi, akatua zigo lake la hofu.
“Ndio, naweza.”
Vitalis akatabasamu.
Mwanamke huyo alimuelekeza Vitalis akitumia mikono yake kama ramani. Kwa muda wa kama dakika tatu, alifanya tukio hilo kufanikiwa pasipo kujua kama Vitalis ni mgeni nchini.
Kwa kutazama na kusikiliza kwa makini, Vitalis aliweka maelezo kichwani, akamuaga mwenyeji wake kabla ya kujirudisha kwenye gari alilokuja nalo lililokuwa na majeraha karibia kila pande na kuondoka eneo hilo.
Alichukua takribani masaa mawili na nusu kufika alipolenga.
Ilikuwa ni nyumba yenye ukubwa wa kati ikiwa haijamaliziwa kupakwa rangi wala kuezekwa paa. Ilikuwa imekaa mbali kidogo na shurba za watu – sehemu tulivu ambapo pangekuhitaji sababu kubwa kukufanya uende hapo.
Nyumba ilikuwa imezingirwa na majani marefu ambayo yalichora njia zinazotumika kuingilia ndani ya nyumba. Njia hizo nazo hazikuwa safi kama tujuavyo, zilikuwa na majani pia lakini yakiwa mafupi kuliko ya kando kando.
Vitalis alipekua eneo hilo na macho upesi. Hakuona dalili ya yeyote kuishi hapo. Aliegemea gari akaendelea kupekua eneo hilo kwa dakika kama mbili ama zaidi kabla hajaanza kuchukua hatua kwenda ndani.
Alifika sebuleni pasipo kuona kitu. Alipita vile vile chumba cha kwanza, pili na tatu pasipo kuona mtu.
Lakini baada ya muda mfupi akaona alama za unyayo wa kiatu koridoni. Hakukuwa na sakafu. Ardhi ilikuwa rafu na ngumu hivyo kuona jambo kama hilo ilihitaji umakini mno kwenye utazamaji.
Vitalis alichuchumaa akatazama alama hiyo kwa karibu. Alirusha macho yake aone kama ataona nyingine, hakufanikiwa.
Kabla hajajua achukue hatua gani ya pili, alishituka kusikia kishindo nyuma yake. Aligeuka upesi akakutana na teke lililokita chini ya taya bila huruma na kumrushia mbali.
Kabla hata hajafungua macho alishaamriwa ageukie ukutani na anyooshe mikono juu kabla hajalipuliwa na risasi. Haraka aliusogelea ukuta akipeleka mikono yake juu.
“Mimi sio adui yenu!”
Vitalis alijitetea.
Kivuli cha mwanaume aliyemnyooshea bunduki kilijongea kumfuata.
Mwanaume huyo alisimama nyuma yake, akamuuliza akiwa ameweka mdomo wa bunduki kisogoni.
“Wewe ni nani na unafanya nini hapa?”
Sauti haikuwa ngeni.
Ilikuwa na ka-lafudhi ka-kihindi ndani yake japokuwa ilisema kwa mkazo usio na tone la utani.
Likiwa jibu langojewa, mdomo wa bunduki uliendelea kushindiliwa kwenye kichwa cha Vitalis kwanguvu.
“Naitwa Vitalis – Vitalis Byabata toka Tanzania.”
Vitalis alijieleza. Alikuwa anatota jasho.
Muda mfupi mdomo wa bunduki uliondolewa kichwani kwake swali likiulizwa:
“Vitalis?”
“Ndio.” Vitalis akajibu akitikisa kichwa.
“Umekuja kufanya nini huku?”
“Kumuua Kim.”
Kimya.
“Umejuaje kama tupo hapa? Nani kakuambia?”
“Nilifuatilia kwa Kelly. Jirani yake alinambia ana nyumba yake maeneo haya nikajua fika mtakuwa huku.”
“Hakuna mtu anayekufuatilia?”
Rajul aliuliza akiangazaangaza.
“Hamna mtu yoyote. Nilihakikisha nipo mwenyewe.”
Rajul alirudisha bunduki kiunoni akamtaka Vitalis anyanyuke.
Alikuwa amevalia suruali nyeusi ya kadeti pamoja na shati jeupe, miguuni alikuwa peku. Kichwa chake kilichozoeleka kutokuwa na nywele, kilikuwa kimeshamiri kedekede pamoja pia na ndevu.
Ni macho na sauti yake ndivyo bado vingekufanya umgundue. Tena baada ya kumfanyia uchambuzi yakinifu.
Aliongozana na Vitalis kwenda chumba cha kwanza kabisa ambapo alijongea karibu na kona ya dirisha akakanyaga chini kwanguvu mara tatu na mara kukafunguliwa.
Ilikuwa ni kama andaki. Mlango wake ulikuwa ngumu kutambuliwa kwasababu ya kutandazwa udongo juu yake ambao haukonyesha tofauti yoyote na wa kando kando.
Waliingia ndani wakamkuta Stanis. Alikuwa kifua wazi akiwa amevalia suruali pekee. Mwili wake ulikuwa na makovu mengi kama kenge ila lisionekane jeraha hata moja. Alikuwa anamimina jasho jingi. Kwa hali ya joto mule ndani ya handaki halikuwa la kushangaza hilo.
Kwa chini kulikuwa kumetandazwa jamvi na ndilo hilo lilikuwa linatumika kama kitanda. Kwenye jamvi hilo konani pia kulikuwa na kofia la nywele, na pasipo shaka lilikuwa ni mahususi kwa ajili ya Stanis kujifichia uso asijulikane.
Rajul alivua nywele na ndevu zake za bandia, akamwambia Stanis:
“Tumepata ugeni kutoka kwa wageni.”
Stanis alimtazama Vitalis kwa macho ya kutafuta. Rajul alimsogelea karibu akamwambia:
“Anaitwa Vitalis, toka Tanzania. Nafikiri hilo si jina geni kwako.”
“Vitalis?” Stanis alishangaa akimtazama Vitalis. Ni kana kwamba alikuwa anajaribu kuvuta kumbukumbu yake juu ya hilo jina.
“Ndio, Vitalis. Amemsumbua sana mkuu wako, Kim, huko Tanzania. Kim alikuwa akiniambia sana habari za huko nyumbani kwake kwa pili. Sasa amekuja Bermuda kumaliza biashara yake aliyoianza.”
“Nini kinakufanya udhani utafanikiwa, Vitalis?” Stanis aliuliza.
Vitalis alimtazama na macho yaliyoonyesha hamu ya damu. Aliminya lips zake akasema:
“Sina kitu wala kazi nyingine kwa sasa zaidi ya Kim. Alichonipotezea hakiwezi kurejeshwa kwa njia yoyote ile na moyo wangu hautotulia kamwe mpaka pale nitakapohakikisha hayupo tena duniani.”
Kulikuwa kimya kidogo kama vile kuna kitu kimepita. Stanis na Rajul walimtazama Vitalis na ni wazi waliona jinsi kiu yake ya kisasi ilivyo kali usoni.
“Amepoteza familia yangu. Amepoteza rafiki zangu. Amepoteza kazi yangu. Amepoteza na anaendelea kupoteza watu kila kukicha kwenye nchi yangu aidha kwa madawa, ama kafara. Amekuwa mchango mkubwa wa kudorora kwa serikali na maendeleo ya nchi yangu. Hastahili kuishi kwa amani. Hastahili kuwepo duniani. Kuendelea kwake kuvuta pumzi ni mzigo na adhabu kwa wengi.”
Stanis na Rajul walitazamana. Ni kama kuna jambo waliteta na macho yao kabla ya Rajul kuuliza:
“Wenzako wapo wapi? Najua haupo peke yako.”
“Wametekwa wote na Kim.” Vitalis alijibu upesi. “Alinitangulia hatua moja mbele, akafanikiwa kunizidi kete.”
“Vitalis.” Rajul aliita. Uso wake ulikuwa na miale ya huruma.
“Huku si Tanzania. Kim anajua kila sehemu ya nchi hii, kila sehemu. Hakuna mahali ambapo hana mtu wake wa kumuangalizia jambo. Iliwapasa kuwa makini sana. Si tu kwamba ana ushawishi kila Nyanja, lakini pia ana mkono kila mahali. Ni ngumu sana kupambana naye.”
Akamshika Vitalis bega la kuume.
“Ila ujio wako umenipa nguvu. Sitosita kusaidia nguvu ama akili kwenye kulifanikisha hili. Nimetenda makosa makubwa sana huko nyuma kwa kumsaidia. Nadhani ni wakati sasa wa mimi kulinywa nililolikoroga.”
Kimya kidogo.
“Pumzika kwa sasa, uso wako unaonyesha umepitia mengi. Tutajadili zaidi baadae.”
Aliposema hayo alipanda juu na baada ya muda mfupi akarejea na majani fulani aliyoanza kumkanda nayo Stanis mgongoni.
Japokuwa hakuwa na majeraha, Stanis alikuwa analalamika kwa maumivu.
Aidha bado alikuwa ana maumivu ya ndani kwa ndani.
Vitalis aliyekuwa amekaa kandokando alitazama zoezi hilo likifanyika akiwa na macho ya maswali.
Labda alikuwa anajiuliza nini kilijiri kwenye mgongo ule uliokuwa hautamaniki kwa makovu. Ila hakuuliza.
‘Tutajadili zaidi baadae’ ya Rajul labda itahusisha na hilo jambo, aliwaza.

***


☆Steve
 
***SURA YA THEMANINI NA NNE***




(MSIMU WA 02)



MTUNZI: Stevie Mollel



No: 0685 758 123








Joto kali la ndani ya Handaki lilimbughudhi Vitalis na kumfanya aamke. Alitazama pembeni yake lakini hakuona mtu, alikuwa peke yake.
Haraka alinyanyuka akifikicha macho.
Akiwa anajinyoosha mwili, alisikia kelele za kiume toka juu, akajawa na tahadhari.
Taratibu aliusukuma mlango wa handaki akatoka ndani.
Ilikuwa ni jioni sasa. Kwa macho ilikuwa ni kama saa kumi na moja ama kumi na mbili. Kwa nje kulikuwa kuna kaubaridi ukilinganisha na ndani ya handaki kulimokuwa kama tanuru.
Vitalis akiwa na sura ya mashaka, alifuata sauti aliyokuwa anasikia ikampeleka mpaka nyuma kabisa ya jengo. Huko alikuta wenyeji wake wakijipasha kwa mazoezi.
Aliketi akawatazama kwa muda kabla hawajamuona na kumtaka ajiunge nao.
Baada ya kufanya hilo zoezi kwa muda wa kama nusu saa ama zaidi, walishitushwa kuona kivuli cha nyumba kinasongeshwa na mwanga ambao waliujua ni wa gari baada ya kusikia sauti ya mngurumo.
Walitazamana kwa mshangao. Ni kana kwamba walikuwa wanajiuliza nini cha kufanya na wakina nani hao wamekuja maskani mwao.
Haraka Rajul aliwaonyesha upande wa kwenda. Ilikuwa ni kwenye nyasi ndefu zilizosimama wima. Pasipo kupoteza muda, wakaeleka huko na kujificha.
Walisikia milango ya gari inafunguliwa na wanaume wakiteta. Punde wakasikia vishindo vikizama ndani. Kisha kukawa kimya kidogo.
“Tunafanyaje sasa?” Stanis alinong’oneza.
“Tatizo hatujajua wapo wangapi na wana nini.” Vitalis alimjibu kisha kimya kikatawala kwa dakika kadhaa. Sauti tu za mioyo yao iliyokuwa inaenda mbio ikivuma.
“Wamejuaje tulipo lakini?” Rajul aliuliza kana kwamba haitaji jibu.
Kulikuwa kimya kwa sekunde kadhaa, Vitalis akasema:
“Itakuwa wameifuatilia ile taksi niliyokuja nayo.”
“Kivipi?” Stanis aliuliza.
“Wakati naelekea kule kwa Kelly walikuwa wananifuatilia ili nilifanikiwa kuwamaliza wote. Itakuwa walitoa taarifa kuhusu lile gari kabla sijawamaliza na labda baada ya kuona kimya kirefu, wakaanza kufuatilia.”
Milio ya risasi ikavuma.
“Inabidi tufanye jambo, hatuwezi tukakaa hapa muda wote!” Alisisitiza Rajul.
Kupambana na watu wenye silaha, tena bunduki, yahitaji uangalifu mkubwa. Ndani ya jengo walikuwepo wanaume watatu waliovalia suti na kubebelea bunduki aina ya SMG mikononi mwao. Miongoni mwa wanaume hao alikuwepo mwanaume mmoja wa kazi. Mwili wake uliojaa ulibana suti. Walikuwa wanatazama huku na kule wakiwa na sura za kazi.
Vitalis alijongea akachungulia mlangoni, akawaona wanaume hao wakiingia kwenye chumba kimoja kabla ya sauti kusikika muda mfupi:
“Kuna handaki!”
Wanaume wawili waliingia kwenye handaki hilo kwa tahadhari ya kutosha mmoja akabakia juu.
Ndani ya muda mfupi yule aliyebakia alivunjwa shingo na Vitalis pasipo kusema chochote. Kabla hajadondoka na kusababisha sauti ambayo ingeweza kuwagutua wenzake, Vitalis alimdaka na kumlaza taratibu kabla hajafunga mdomo wa handaki na kuwashitua wenzake kwa mluzi, wakafika ndani ya muda mfupi.
“Wamo ndani!”
Alisema Vitalis aliyekuwa amebebelea bunduki sasa mkononi.
Mara milio ya bunduki ikaanza kurindima. Mdomo wa handaki ulikuwa unapokea risasi mfululizo zikitoka kwa wale waliofungiwa humo.
Rajul alimtazama Vitalis akamshika mkono.
“Nadhani ni muda wa kuondoka. Tutatumia usafiri wao.”
“Kwanini tuondoke kabla hatujawamaliza?” Vitalis aliuliza.
“Bado hatujajiandaa vya kutosha.” Rajul akajibu akimvutia Vitalis nje ya chumba.
Vitalis hakuelewa kilichokuwa kinaendelea na kwa namna moja ama nyingine alishangazwa kuona wameridhia kile alichokisema Rajul kwa wepesi.
Waliingia ndani ya gari la maadui wakakuta hamna funguo. Stanis alikata waya alizoziunganisha gari likawaka. Ila kabla chombo hakijaondoka, walisikia sauti kubwa ya kushtua. Haikuwa ya mlio wa bunduki, la hasha! Ilikuwa ni sauti ya kishindo kilichoashiria kufunguliwa kwa mdomo wa handaki.
Tena kwa nguvu mno.
Rajul alimtazama Stanis aliyekuwa amekalia kwenye kiti cha dereva, akamuamuru:
“Ondoa gari!”
Stanis alikanyaga mafuta gari likatimka likiacha vumbi jingi.
Hawakufika mbali gari likaanza kulengwa na risasi kwa pupa. Alikuwa ni yule mwanaume wa kazi akiwa anakimbiza gari hilo kwa hatua zake pana na ndefu. Mkono wake wa kuume alikuwa amebebelea bunduki aliyokuwa anaifyatua pasipo kukosea. Kwa shabaha yake hiyo, vioo vyote vya gari walilokuwemo Vitalis na wenzake vilitawanywa na kumwagwa.
Mwanaume huyo alikimbia kwa mwendo mkali akajiweka karibu na gari. Alimiminia risasi gari hilo dereva asipate muda wa kuzingatia barabara kwa umakini, gari likawa linaenda kwa pupa huku na kule. Watu wote ndani ya gari walikuwa wameinama kujificha dhidi ya risasi.
Endapo kama mwanaume yule wa kazi angeendelea kushambulia gari hilo basi si muda mrefu angekuwa amemaliza kazi yake, ila zoezi lake hilo lilikwamishwa pale risasi zilipokauka bundukini.
Alisimama akaitazama na kuikagua bunduki kabla hajaivunja na mikono yake kwa hasira. Kwa muda huo gari likajichanua kumuacha. Alilitazama gari likiyoyoma, mara akaanza tena kukimbia ila mara hii akielekea upande tofauti na ule gari lilipoelekea.
Hakuonekana mwehu, hapana, uso wake ulionyesha anajua anachokifanya japo kwa namna moja ama kingine kingekustaajabisha kama Vitalis.
“Anaenda wapi?”
Vitalis aliuliza. Hakuna aliyemjibu. Aidha hawakuwa na majibu ama bado walikuwa katika ombwe la mshangao kwa namna gani wamepona.
“Yule mtu ni nani? – si wa kawaida!” Vitalis aliongezea swali.
Hapo Rajul akamjibu upesi:
“Ndio mana nilikwambia bado hatujajiandaa.”
Kimya kidogo.
“Ni bahati yetu alikuwa mmoja, kama wangelikuja wote basi tusingelikuwa na nafasi ya kuishi leo hii.” Rajul aliendelea kuongea.
“Wapo watano na wana nguvu ya ajabu. Wote nyota zao ni simba. Wamepewa madawa yaliyojumuisha damu ya mtawala wa kifalme. Ni ngumu sana kuwazuia kwa uwezo wa binadamu wa kawaida.”
“Kwanini nyota ya simba?” Vitalis aliuliza.
Rajul akashusha pumzi ndefu.
“Kwasababu ni mojawapo ya alama ya nguvu aliyobakiwa nayo Kim mbali na ile ya maji. Watu waliotakiwa kupewa nguvu hiyo ni wale tu wenye nyota hiyo, si vinginevyo.”
Rajul alimaliza kwa kumtazama Stanis.
Vitalis alikumbuka ile michoro waliyoiona na wenzake kule kisiwani kwenye ukuta wa yule mganga.
“Kwahiyo? Hakuna lolote la kufanya kuwakabili?”
“Lipo, ila linataka muda, nguvu naa … wizi vilevile.”
“Wizi?”
“Ndio. Kupata mkabala wa kuwakabili kuna ulazima wa kuiba jambo fulani sehemu fulani. Kama tusipofanikiwa hatuwezi kumpata Kim.”
“Tunaiba sehemu ga …”
Waliona kitu mbele yao!
Alikuwa ni yule mwanaume wa kazi. Hawakujua amefikaje pale ila sasa ilikuwa na mantiki kusema na kuamini kwamba alikuwa amewapitia njia denge. Njia ile waliyokuwa wanaitumia ilikuwa na kona kadha wa kadha na mwanaume huyo alionekana kufahamu kwa undani ramani ya eneo hilo.
Stanis alikanyaga moto zaidi. Kabla mwanaume yule wa kazi hajazolewa, aliruka juu akanasa paa la gari. Vidole vyake vilitoa kucha ndefu zikang’ang’ania paa kwanguvu. Haikujalisha ni kwa kiasi gani Stanis aliyumbisha gari, mwanaume huyo hakuachia paa sembuse kutetereka.
Vitalis alifyatua bunduki kulenga paa. Risasi za mfululizo zikamtoboa mwili wa mwanaume huyo lakini asikome. Sasa alikuwa anapiga ngumi paa na imebakia kidogo tu alitoboe. Vitalis alichomoza dirishani upesi akamfyatulia risasi kadhaa mwanaume huyo kabla bunduki haijapigwa kofi ikarukia mbali.
Mwanaume huyo alituma teke lake kumzoa Vitalis akiwa amejishikiza na mkono mmoja. Vitalis alikwepa teke hilo kisha akalidaka na kulivuta. Hakufua dafu. Aligeuziwa kibao kwa kukandamizwa mateke mawili ya haraka. Ilikuwa ni wakati ameshika mguu ule uliorusha teke, mwingine ulimuadhibu kisha akaachia ule wa awali ambao nao pia ukamsigina.
Isingekuwa Rajul basi angelidondoka toka kwenye gari lile lillokuwa linaenda kwa kasi, muhindi huyo aliwahi kumdaka Vitalis na kumvutia ndani kwa kutumia nguvu zake zote. Vitalis hakuwa hata na muda wa kujiuguza maumivu, paa la gari lilichanwa kama karatasi mkono wa mwanaume yule ukapenya kushika kichwa cha dereva – Stanis. Vidole viliziba uso wa dereva huyo na kumpotezea uwezo wa kuona.
Gari likawa linaenda alimradi laenda.
Rajul alidaka usukani kusaidia kubaki barabarani pia kukwepa magari mengine.
Stanis akiwa anahangaika kujikomboa, alikamata mkono wa adui akaujeruhi kwa kuuachana na bati la paa baada ya kuugandamizia hapo. Mwanaume yule wa kazi akauvuta mkono wake na kuutazama kwa ghadhabu. Ulikuwa unachuruza damu toka kwenye jeraha kubwa.
Breki kali ilikanyagwa, akarushiwa mbali.
Isingelikuwa alizingatia mkono wake zaidi ni wazi asingelirushwa. Kucha zake ndevu ziling’ata paa ya gari vizuri. Na kama tu zingepata msaada wa akili yake nzima, kubanduka hapo ilikuwa ni ndoto isiyotekelezeka.
Mwanaume huyo alibiringita mara mbili tu kabla viganja vyake havijakita juu ya lami kucha zikazama. Alijisogeza kando upesi kupisha gari la wakina Vitalis kisha akafanya jitihada ya kupata usafiri mwingine, akapata pikipiki.
Vitalis alipogundua wanafuatwa na usafiri huo, aliomba akalie yeye usukani, Stanis akampatia hiyo fursa. Kitu cha kwanza alichokifanya ni kutazama kioo cha juu akiwa anasaga meno yake na kubinua lips. Kinyume na matarajio akapunguza mwendo kwa kiasi fulani. Pikipiki ikajongea karibu zaidi.
Baada ya kujihakikishia pikipiki ipo karibu na kingo ya bampa la gari, taratibu Vitalis akaongeza kasi ya gari. Ilikuwa bado kidogo mwanaume wa kazi aitie gari mkononi. Pikipiki nayo ikaongeza kasi.
Baada ya dakika kama moja likatokea jambo haraka sana!
Ni baada ya kuona gari lingine, Noah rangi ya silver, laja kwa nyuma na kusonga karibu, ndipo Vitalis akakata kona ghafula akiwa amekamata breki. Kama fagio, gari likamzoa mwanaume juu ya pikipiki na chombo chake kwa pamoja wakamwagiwa mbele ya Noah.
Mwanaume yule alitupwa kando na pikipiki yake ikamfuata pia kumkanyagia juu. Noah iliyomgonga ilisimama dereva akiwa na nyuso ya huruma na mshangao. Alikuwa anatetemeka asijue la kufanya.
Tusijue hata kama mwanaume yule aliyegongwa amepona ama ameenda, Vitalis alirudisha gari nyuma akampanda mwanaume huyo kana kwamba mlima. Alifanya zoezi hilo mara nne, akikanyaga mafuta kwenda na kurudi, kabla hajajiweka sawa na kuondoka kwa kasi.
Dereva wa Noah kushuhudia hayo, alizirai. Barabara ilitapakaa damu mhanga akiwa ameachwa amepasuka kichwa na viungo vimevunjwa kwanguvu.
Kwa muda kukawa na foleni eneo hilo.
Vitalis alifuatisha maelezo aliyopewa na Rajul baada ya muda mfupi akawasilisha gari karibu na eneo la ‘temple’. Rajul alitazama eneo hilo kwa haraka akashusha pumzi.
“Ni hapa.” Alisema. “Ni hapa ndipo tunatakiwa kuiba kitu fulani.”
“Utahitaji msaada wowote?” Stanis aliuliza.
“Hapana.” Rajul akajibu. “Tangu walipovamiwa na kuuwawa kwa ajili yangu, sidhani kama kutakuwa na watu wengi. Naweza nikafanikisha hili mwenyewe.”
Alipomaliza kusema hilo alifungua mlango akatoka ndani.
“Nipatieni kama nusu saa hivi.”
Alielekea nyuma ya temple alipodandia ukuta na kujimwagia ndani. Kwa uangalifu mkubwa akiwa amebonyea alitembea haraka kuliendea jengo. Alijibanzia ukutani akachungulia korido kama ina watu, akaona hewara.
Alitembea upesi upesi, aliposikia sauti za watu alijifichia kwenye kuta ama kwenye vyoo kisha akaendelea na safari mpaka alipofika kwenye mlango fulani mkubwa uliokuwa unaong’aa kwa matirio yake ya mbao yenye polishi. Alijaribu kuufungua akashindwa, ulikuwa umebanwa na komeo. Funguo atatoa wapi?
Alisaga meno yake kabla hajatwanga kiganja chake na ngumi nzito kisha kuendea ngazi apande juu. Ilibidi sasa aende chumba kinachotunza funguo. Alifika hapo baada tu ya sekunde chache. Ndani ya chumba hicho kulikuwamo na mwanaume mmoja mzee aliyekuwa amevalia shuka la kahawia na cheni ya madunguli meusi. Alikuwa ameketi akisoma kitabu kikubwa chenye jarada jeupe. Macho yake ndani ya miwani kubwa ya macho yalikuwa yanaenda kushoto na kurudi kulia, kulia yakirudi kushoto.
Hakukuwa na muda wa kupoteza kwa Rajul, lakini pia hilo halikutosha kumfanya asiwe muangalifu. Korido haikuwa na mtu ila si kwamba itakuwa hivyo milele hivyo ilibidi achakate akili yake kwa upesi.
Akigonga mlango ataambiwa karibu. Akiingia uso wake ukionekana atajulikana, si ndio? Hakutaka kujulikana. Alibisha hodi mara tatu, mzee yule aliyekuwemo ndani akapaza sauti yake kumkaribisha pasipo kutazama mlangoni.
Mtu hakuingia.
Mzee alibandua macho yake kitabuni akatazama mlangoni. Baada ya dakika moja ya kutosikia tena hodi alinyanyuka akauendea mlango. Alipoufungua tu, Rajul aliusukuma mlango kwanguvu ukamgonga mzee huyo na kumlaza hajitambui. Aliingia ndani akufuata ubao wa funguo na kuchukua ufunguo anaouhitaji na kutokomea eneo hilo akifunga mlango na kumuacha mzee huyo chini.
Alirejea mlango ule akaufungua na kuingia ndani. Humo ndani hakuchukua muda mrefu akatoka na bilauri refu la kioo.
Kitendo tu cha kuufunga mlango huo, sauti kubwa ya king’ora ikaita! Jengo zima lilikuwa kelele ghafula.
Tayari mzee yule aliyeziraishwa kule ofisi ya utunzwaji funguo alikuwa ameonekana. Ni punde tu baada ya Rajul kutoka, watu wawili walikuja na kumkuta katika hali ile. Kutokana na kitendo cha kuvamiwa kwa jengo hilo siku za nyuma na kupelekea mauaji, hali ya usalama ilikuwa imeimarishwa zaidi mahali hapo. Wanaume waliobebelea silaha mathalan jambia, marungu na mapanga walitapakaa kuitikia wito wa king’ora kile.
Rajul akiwa amebebelea bilauri lake alikimbia kurejea njia yake aliyoingia nayo jengoni humo, bahati mbaya akakuta tayari maeneo yale yashatwaliwa na walinzi. Alirudi upesi kwenda upande mwingine ila huko kabla hajafikia ukuta aliamriwa na sauti nyuma yake asimame la sivyo atatapanywa!
Walikuwa wanaume watatu waliobebelea mapanga mikononi. Nyuso hazikuwa rafiki hata kidogo. Vichwa vyao havikuwa na nywele na walivalia mashuka ya kahawia. Walikuwa wanamsogelea Rajul taratibu.
Rajul alisimama akiwa hajui la kufanya. Macho yalikuwa yamemtoka na mdomo ulikuwa umeachama. Alitazama bilauri alilobebelea akameza mate ambayo hayakuwepo hata mdomoni. Mdomo wake ulitetema mambo ambayo hayakusikika.
Ghafla, geti lililokuwa karibu yake lilivunjika likaingia gari lililowabebelea Vitalis na Stanis kwa kasi kubwa!
Gari hilo likiwa linaendeshwa na Vitalis liliwafyagia wanaume wale wenye silaha kisha likajitenga mbele ya Rajul.
“Ingia fasta!” Vitalis alimuamuru Rajul.
Rajul aliingia ndani ya usafiri, gari likatimka upesi!
Baada ya masaa mawili walikuwa fukweni mwa bahari ila fukwe iliyojitenga na purukushani za dunia. Kulikuwa kimya upepo ukipuliza. Mawimbi yalikuwa yanapiga taratibu na yakivutia kutazama.
Walikuwa wameegemea gari wakitazama jua likizama. Anga lilikuwa jekundu. Kulikuwa kimya kana kwamba walipeana tahadhari ya kutoongea. Wakati jua likiwa jekundu mno na limebakiza punde ndogo ili lipate kupotea kwenye uso wa dunia, Rajul alijikuta anakohoa kusafisha koo lake kisha akasema:
“Kesho ni siku muhimu sana.”
Aliposema hivyo kulikuwa tena kimya kwa dakika kama mbili. Jua lilizama kukawa na kakiza kepesi.
“Ni siku yangu ya kubeba adhabu halisi ya yale yote niliyoyatenda. Ila nafurahi mana nitakuwa huru. Nafurahi maana nitakuwa nimelinywa nililolikoroga.” Alisema Rajul.
“Naomba nirudie kuuliza, ina maana hamna njia nyingine kabisa?” Stanis alivuma. Sauti yake ilikuwa ya kuguswa.
“Hamna njia nyingine. Endapo kama sitofanya hivyo si tu kwamba nitakuwa nimekimbia jukumu langu, bali itawawia vigumu kushinda” Rajul akajibu kwa sauti kakamavu kisha akanyooshea kidole baharini. “Mtanitupia kule mkiwa mmenifunga jiwe kubwa shingoni.”
Alishusha kidole chake akasisitiza:
“Naomba mfanye hivyo maana sitakuwa binadamu wa kawaida tena. Nitakapokunywa hizo dawa nitauchukua uovu wote nilioupandikiza na hivyo nitakuwa shetani haswa. Sitakuwa namjua wala kumkumbuka yoyote yule mbele yangu, nitakuwa hatari. Hivyo muwe mmenifunga na kunijaladia vema.”
Hakuna tena aliyesema kitu. Ni upepo tu ulipuliza.
Na hapo ndipo tuliporudi nyuma kwa lisaa limoja kushuhudia mabaki ya damu ya mwanaume yule wa kazi yakipatikana ndani ya gari mahali pale alipokatwa mkono, yakachanganywa na damu ya Rajul ndani ya bilauri kabla ya kufungwa upesi na kuchimbiwa chini ya bahari.
Ilitosha kupata na kutumia damu ya mwanaume yule kama alama ya kumuwakilisha Kim, utawala na mabadiliko yake, wakati damu ya Rajul ikitumika kumwakilisha aliyechagiza mabadiliko hayo.
Tayari bilauri hilo lilikuwa linatetemeka ndani ya ardhi ya bahari kana kwamba simu iliyonyimwa mlio. Ila muda wake wa kuopolewa ulikuwa bado. Ni siku inayofuata majira ya tatu asubuhi.

***

☆Steve
 
Ndugu, tatizo dozi yako ni kama chanjo ya surua.

Embu tupia hata nne nne.
 
Duuuu hatimae nmemaliza,Steve hadithi nzuri sanaaaa
 
Huyu bwana atakuwa kapoteza kamera kwenye maji akifuatilia utoswaji wa mhindi baharini.

Amenitext kazamia kuifuta.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom