Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

haaah mkuu steve bado mpka muda huu!! au ndio unamalizia viroba vya mwishomwisho kwa usongo
 
***SURA YA SITINI NA MBILI***





(MSIMU WA 02)






Ukiwa ni usiku wa saa saba, boti ndogo nyeupe inayosukumwa na mashine ilisogelea kisiwa cha wakina Vitalis kwa mwendo wa taratibu.
Kwenye boti hiyo walikuwepo wanaume wanne waliovalia nguo nyeusi juu mpaka chini. Kati yao watatu walikuwa wazungu huku mmoja akiwa mtu mweusi.
Boti hiyo ilizunguka kisiwa hiko mara mbili alafu mashine ikazimwa. Mwanaume mmoja akasema:
“Hakuna kumuacha mtu yeyote hai.”
Baada tu ya hiyo kauli, wanaume watatu waliopewa maagizo walirukia ndani ya maji wakaogelea kama samaki. Punde tu walishika nchi kavu na kuanza kusogelea nyumba pekee hapo kisiwani.
Baada ya sekunde kadhaa, sauti kali ya kiume ilisikika, Vitalis akashituka usingizini. Alitulia kwa sekunde tatu akisikilizia, akajikuta akisema:
“Jombi! … Jombi!”
Akili yake ilimuambia hiyo sauti ni ya Jombi. Upesi alifungua dirisha akachungulia nje, kwa mbali akaona kitu cheupe baharini.
Kama vile haitoshi, alisikia sauti ya kishindo nje ya chumba chake. Haraka akanyanyuka na kutwaa bunduki yake aliyoiweka chini ya godoro. Aliikoki bunduki hiyo akatoka ndani kwa kupitia dirishani.
Taratibu alinyata akifuatisha sauti mojawapo ya kiume iliyokuwa inafoka ikimuamuru mtu atoke alipojificha.
Alipofika karibu na sauti hiyo alichungulia dirishani akamuona Bernadetha anatoka ndani ya kabati pamoja na mwanaye, Marietta. Mikono yao waliiweka juu nyuso zao zikitandazwa hofu.
Pasipo kusubiri, Vitalis alipitisha mkono wake dirishani akafyatua risasi ikambanjua adui kichwani. Kufumba na kufumbua alitokea adui mwingine akaingia ndani ya chumba hiko kwa pupa. Alifyatua risasi ikamkita Marietta kifuani na kumwaga chini. Kabla hajafyatua nyingine Vitalis alimuwahi kwa kumlenga risasi ya mkono kisha akarukia ndani upesi kwenda kumjulia hali Marietta.
Alikuwa hapumui. Damu zilikuwa zimemjaa kifua kizima. Macho yake yalikuwa wazi pamoja pia na mdomo. Alikuwa amekufa, Marietta. Lakini mama yake hakuamini hilo, aliendelea kumuita akilia. Alimtikisa tikisa kama kibuyu cha maziwa.
Chozi likamshuka Vitalis. Alimfunika macho Marietta akamshika bega Bernadetha. Aliogopa hata kumbembeleza. Aliishia tu kumtizama kana kwamba amepigwa na butwaa. Alisahau ya kwamba hakumuua yule adui aliyemfyatulia risasi zaidi tu ya kumjeruhi mkono, maeneo ya begani. Adui huyo aliyekuwa nyuma yao alisogeza bunduki yake akawanyooshea pasipo wao kutambua.
Kabla hajafyatua, alifumuliwa ubongo na risasi iliyotokea nyuma yake, mlangoni, habari yake ikaishia hapo. Alitokeza Kaguta akibebelea bunduki anaongozana na Miraji na Bakari.

***

“Walikuja wanaume wanne na boti. Hatujajua ni kwa njia gani wamefahamu tunapoishi. Hatupo salama tena hapa!” Alisema Kaguta kimsisitizo wote wakimtizama.
Macho ya Bernadetha bado yalikuwa mekundu. Alikuwa makini akitazama bahari kupitia dirishani. Alitizama huko kana kwamba anamuona mwanae Marietta juu ya uso huo wa bahari ya bluu uliokuwa unamulikwa vema na jua la mchana. Mtoto wake pekee aliyebakia, Miraji, alikuwepo pembeni yake akimuwekea mkono begani kwa kumbembeleza. Pembeni zao walikuwapo Bakari, Kaguta na Sandra. Mbele zao wote alikuwepo Vitalis.
“Nini kingine umekipata?” Vitalis aliuliza. Bakari akasafisha koo lake.
“Kama unavyojua, wavamizi wote walikufa kwahiyo hakuwepo hata mmoja wa kutupa taarifa. Mmoja tuliyekuwa tunamtegemea ni yule ambaye alipigwa risasi ya mguu na Kaguta, tukimfunga kamba kwa kutegemea atakuwa rasilimali baadae ila naye tulipotoka tu ule upande wenu tukamkuta amejiua kwa kujibamiza kichwa chini.”
Bakari alisema kisha akaweka kituo. Wote walikuwa wanamtizama.
“Tulipofuatilia huko tulipotoka, tumegundua watu hao walikodisha boti kwenye kampuni ya Suleiman Fishing, wakipatana kuirejesha muda si mrefu. Walitoa pesa za kutosha hivyo kampuni ikashindwa kuwakatalia kwani hata kama wangetokomea nayo wangeweza kupata nyingine mpya …”
“Kwahiyo wametokomea nayo?” Vitalis alimkatisha Bakari.
“Ndio, wameondoka nayo. Ila itakuwa ahueni kwetu kuwapata kwa urahisi.”
“Kivipi?”
“Tutatumia tracking device ya kampuni. Suleiman Fishing huwa wanaweka vifaa kwenye kila chombo chao ili hata pale vinapopotea ama kuibwa basi inakuwa rahisi kuvipata. Tutatumia mwanya huo kuwapata.”
“Kwanini wameondoka na boti hiyo?” Vitalis aliuliza kisha akang’ata ngumi yake akitizama pembeni.
“Labda watakuwa na matumizi nayo hapo baadae.” Sandra alijibu. “Na hayo matumizi yanaweza yakawa mabaya zaidi upande wetu.” Akaongezea.
“Hatuna budi kufanya upesi kabla hawajafanya wao.” Vitalis alisema. “Hiyo ndio itakuwa njia nzuri kuenzi wapendwa wetu waliotutoka wakati bado tunawahitaji na kuwapenda.”
Aliweka kituo akawatizama wenzake wote usoni. Alifumba macho kwanguvu akayafumbua akisema:
“Muda umewadia. Twende tukafanye sala.”
Walizunguka matuta mawili makubwa yaliyokuwa umbali mchache toka yalipo makazi yao. Walitulia hapo kwa muda wakiwa kimya nyuso zao zikitizama chini.
Hawakudumu sana, Bernadetha akaanza kulia. Alidondoka chini akipiga yowe. Machozi yalimmiminika kama maji. Japokuwa alibembelezwa, hakunyamaza abadani. Uchungu aliokuwa nao ulizidi matumaini na pole alizopewa.
“Nitawaua tu na mimi … hak’ya Mungu!” Bernadetha aliapa kilioni.

***


☆Steve
 
***SURA YA SITINI NA TATU***






(MSIMU WA 02)






Hamilton, Bermuda.

Walikusanyika wote kwenye uwanja wao kama walivyofanya hapo awali. Wanaume kama themanini kwa kuhesabu kwa macho wakiwa vifua wazi na wamevalia suruali za jeans nyeusi waliujaza uwanja. Mbele yao hakuwepo mtu yeyote bali viti viwili vikubwa ambavyo kimoja wacho kilijazwa dakika moja mbele na Kim Salvatore.
Alikuwa amevalia suti nyekundu na tai nyeusi. Mgongo wake ulikuwa umefunikwa na joho kubwa la manyoya lenye vidoti doti vyeusi. Kiatu chake cheusi kilikuwa kinameta meta kama nyota. Nywele zake za mchanganyiko wa mweupe na mweusi zilikuwa zinang’aa kwa kupakwa na kushiba mafuta. Ndevu zake zilichongwa vema huku nyusi zake zikiwekwa sawia na wanja.
Kwa mbali mdomo wake ulikuwa unameta mithili ya saa yake ya dhahabu aliyoivaa mkononi. Pete yake rangi ya fedha yenye kito cha almasi, aliivalia kidole cha mwisho. Alikuwa anatumia kidole hicho kugongea gongea mkono wa kiti taratibu kana kwamba anajaribisha kipaza sauti cha sherehe.
Kwa mazingira tu yaliyopo yalionyesha siku hiyo haikuwa ya kawaida. Sio tu uwepo wa viti viwili ulisema hivyo, bali hata mavazi na maandalizi. Uwanja mzima ulipambwa na bendera nyekundu zenye mchoro mweusi – mchoro wa mikono iliyopishana ikitengeneza umbo la ‘x’ – mchoro wa mikono ya chuma.
Kila nguzo ndani ya uwanja huo ulifunikwa na kitambaa chekundu kirefu, sakafu ikifunikwa na zulia jeusi.
Kim alitoa ishara kwa kuinamisha kichwa chake, wanaume wote wakaketi kana kwamba wapo masjid – mkao mmoja. Kulikuwa kimya, tuli. Kim akanyanyuka akatizama pande zote na kusema:
“Vema!”
Akatikisa kichwa kimakubaliano.
“Naona vyote vimekuwa vema. Na hivyo ndivyo inatakiwa iwe.”
Alitabasamu akatizama upande wake wa kushoto. Huko akatokea Rajul akibebelea kibakuli kidogo cha mbao. Alivalia nguo nyeupe ndefu ikimfunika miguu kabisa. Shingoni mwake alikuwa amevalia cheni yake ya madunguli ya mbao. Kichwa chake kisicho na nywele kilikuwa kimechorwa michoro miwili meupe zigzag.
Alitembea kwa umakini akifuata kiti kitupu. Aliketi akipakata kibakuli chake, akamtazama Kim na kumpa ishara ya kuinamisha kichwa. Kim akawatazama wafuasi wake.
“Leo ndio ile siku maalum. Siku adhimu kabisa. Leo ni siku ya kurudi utotoni. Leo ni siku ya kuzaliwa upya!”
Kim alisema kisha akaweka kituo. Akatabasamu.
“Nitakaowaita watakuja hapa mbele. Watakunywa damu ya kifalme, damu ya baraka, damu ya uongozi, damu ya nguvu. Punde tu damu hiyo itakapoingia kwenye mishipa yao, hawatokuwa binadamu tena bali simba kamili. Si panga wala risasi, si mikuki wala mishale zitawamaliza.”
Alipomaliza kusema hayo akaita majina ya wanaume watano. Kati ya wanaume hao watano, wanne walikuwa ni miongoni mwa wale wanaume watano waliotumwa Muscat, Oman, kuteka damu ya mfalme.
Mwenzao mmoja hakuitwa. Aliachwa akiwa ameketi, uso wake ukibeba ndita ametoa macho kana kwamba haamini. Alikunja ngumi yake akisaga meno. Alijikuta akinong’oneza akiwatizama wenzake wakinywa walichopewa kwenye kibakuli.
“Kwanini? … Kwanini?”
Alijaribu kukumbuka yote yaliyotukia Muscat, Oman. Jinsi alivyojituma akijifanya mwanamke. Jinsi alivyowaokoa wenzake kwa shuka la Wadhaab. Na jinsi alivyorusha mateke na ngumi za adabu kwa wanajeshi wa Oman.
Kote huko hakuona kosa alilolifanya. Kwanini hajaitwa na yeye? Aliwaza.
Mkutano ulidumu kwa dakika ishirini na tano kabla watu hawajatawanyika. Kim na Rajul waliongozana wakaelekea ofisini. Nyuso zao zilikuwa na furaha, zilipambwa na matabasamu. Waliketi wakawa wanapongezana kwa kupeana mikono na kutikisa vichwa vyao.
“Sasa yamekwisha, bwana Kim. Unaweza ukatawala ulimwengu tena kwa kuwasambaratisha maadui zako.” Alisema Rajul akitabasamu.
“Ahsante sana, Rajul. Nafikiria nikulipeje lakini nakosa majibu kabisa.”
“Hamna shida kabisa bwana Kim una …”
Mlango uligongwa.
“Nani?” Kim aliuliza kwa kupaza sauti.
“Stanis!”
Sauti ikamjibu toka mlangoni.
“Ingia!”
Mlango ulifunguliwa akaingia mtumishi wa Kim. Mtumishi aliyeona amenyiwa fursa ya kuitwa na kutunukiwa kama wenzake.
“Karibu, Stanis. Naweza kukusaidia?”
Kabla Stanis hajajibu, Rajul alisimama akamtizama Kim.
“Naomba niende. Nitakuja siku nyingine tuongee zaidi.”
Kim akampa ishara ya kuinamisha kichwa, Rajul akaondoka zake. Stanis akaketi alipokuwa amekaa Rajul.
“Nimekuja kuuliza, mkuu.”
“Kuuliza nini?”
“Kwanini umenibagua wakati nami nilitumia akili na nguvu zangu zote kukutumikia. Kwanini?”
Kim alitabasamu na shavu la upande mmoja. Aligonga meza yake mara mbili akaja mwanamke mrembo ndani ya sare nyeusi na nyeupe akibebelea chupa ya mvinyo na glasi. Alimmiminia Kim kinywaji kisha akaenda zake. Kim alikunywa mafundo mawili akimtizama Stanis. Aliweka glasi yake chini akauliza:
“Ulivyorudi toka Muscat, sikukupa mifuko miwili ya dhahabu?”
“Ulinipa.”
“Sikukupa wanawake watano warembo toka Brazil ukalale nao?”
“Ulinipa.”
“Sikukupatia nafasi ndani ya mamlaka yangu?”
“Ulinipa lakini …”
“Lakini nini? Unadhani yale niliyoyafanya pale yalikuwa ni zawadi tena?”
“Ni nini?”
“Stanis! … labda umesahau wewe ni nani na mimi ni nani. Naweza nikafanya lolote lile ninalolitaka, wewe ni nani uniulize na kutilia mashaka ninachokifanya? Wewe ni mtumishi tu. Huna haki yoyote ya kutaka mimi nifanye unavyotaka. Wewe ndio unafanya mimi ninavyotaka.”
Kim alisema kwa sauti ya chini yenye mkazo. Alijimiminia mvinyo kwenye glasi yake akanywa mafundo matatu.
Stanis alinyanyuka akataka kwenda. Kim akamuita.
“Unaenda wapi Stanis? … kaa hapo, bado tuna mengi ya kuongea.”
Stanis alirudi akaketi.

***


☆Steve
 
***SURA YA SITINI NA NNE***




(MSIMU WA 02)






Baada ya kutembea kwa takribani dakika tatu akitoka kwenye jumba la Kim, Rajul alifika kwenye kituo cha mabasi. Kwakuwa ni muda wa mchana, hakukuwa na watu wengi kituoni. Eneo hilo hujaa haswa muda wa asubuhi na jioni – watu wakienda na kurudi makazini.
Rajul aliketi kungojea usafiri papo. Ilipita dakika moja basi likaja. Rajul alinyanyuka taratibu kufuata basi hilo, alipokaribia mlangoni kondakta alimnyooshea mkono akimkataza kupanda, basi lilijaa.
Rajul alitikisa kichwa chake akarudi kungojea. Aliketi hapo sasa akiwa na mtu mmoja tu, wengine walipata nafasi ya kukwea basi lililopita.
Mtu huyo aliyeketi naye alikuwa ana nywele nyeusi za singa. Hakuwa mweupe wala mweusi – maji ya kunde. Alivalia shati jeupe na kikoi cheusi. Hakuonekana kama muongeaji wala sura yake haikuwa karimu. Alikuwa ameufumba mdomo akiuvuta kana kwamba anambusu mtu.
Rajul alimtizama akampuuzia. Aliendelea kutazama tazama barabara akingojea basi. Alionekana ana haraka na swala la kungoja lilimbughudhi.
Baada ya dakika tatu, basi lingine liliwasili. Rajul alinyanyuka upesi akimtangulia mwenzake kana kwamba yu mashindanoni. Aliingia kwenye basi moja kwa moja akaenda kuketi kwenye kiti kando na dirisha. Hakujali wala kutizama nyuma kama yule mwenzake aliyekuwa naye kituoni amepanda ama lah. Hakujali alimradi yeye keshapata nafasi.
Ila yule mwanaume aliyekaa naye kituoni, naye alipanda basi hilo hilo. Alikuwa nyuma yake upande huo huo wa karibu na dirisha.
Basi lilipotembea kwa muda wa dakika sita, Rajul akabonyeza kengele kuashiria anashuka kituo kinachofuata. Alishuka akashika njia nyembamba inayopanda juu palipo na maghorofa kadhaa.
Alitembea taratibu na mwendo wake wa kizee.
Nyuma yake yule mtu mwenye nywele singa alikuwa anamfuatilia taratibu. Kila Rajul alipogeuka, mwanaume huyo alijibanza aidha kwenye jengo ama beneti na mtu mwingine, Rajul akaendelea kusonga mbele.
Alisonga hatua kadhaa, alipowadia kwenye kona ambayo aliikata ghafula akitizama nyuma, alimuona mwanaume yule anayemfuatilia. Hakujali sana. Alipuuzia akaendelea na safari yake. Ila alipata hofu zaidi pale alipokata kona mbili na zote akimuona mwanaume huyo nyuma yake akiigiza anafanya shughuli fulani kana kwamba hana muda naye.
Rajul aliongeza mwendo maradufu. Asifike mbali, akakabwa katikati ya kichochoro alichojaribu kukatiza awahi aelekeapo. Mwanaume yule mwenye nywele singa alitokea mbele yake akamziba pumzi na kitambaa.
Gari dogo aina ya Volkswagen lilijiri haraka, mwanaume yule mwenye nywele za singa akambeba Rajul na kumwagia ndani ya gari hilo. Wakatokomea.

***

Bakari alitandaza ramani ya Dar es Salaam juu ya meza akanyooshea kidole sehemu palipotiwa alama nyekundu, akasema:
“Boti ipo Whitesands hotel.” Alisema kwa uhakika akiwatizama wenzake. “Kwa mujibu wa tracker ya kampuni, boti ipo hapo, ila hatujajua haswa wahusika watakuwa eneo gani.”
“Twende!” Vitalis alitoa agizo.
Akiwa ameongozana na Jombi na Kaguta walielekea kwenye boti ndogo iliyokuwa imepaki baharini. Vitalis aliwasha mashine ya boti wakaanza safari kwa mwendo wa kasi.
Walikata mawimbi mithili ya papa upepo ukiwapuliza zaidi ya viyoyozi.
Bakari akitumia tanakilishi yake alikuwa anawaona kwenye ramani kwa mtindo wa kidoti cha bluu kilichokuwa kinasonga kwa kasi kuitafuta Whitesands hotel. Alitumia radio call kuwaelekeza upande upi waelekee, nao wakafuata.
Walipoitia machoni Whitesands hotel, mafuta yalikwisha kwenye boti. Kwa mahesabu ya haraka haraka bado walikuwa wana kama kilomita moja na nusu kuingia eneo la Whitesands hotel. Walitumia mikono yao kama mapakuo wakapakua maji mpaka ufukweni walipoificha boti yao kisha wakabadili nguo wakivalia za kuogelea.
Vitalis aliwasiliana na Bakari kupata taarifa zaidi juu ya eneo walilopo na wanapoelekea. Alipopata taarifa za kukidhi haja aliacha hapo redio call kwenye boti wakaanza kutembea kwa miguu kuifuata hotel.
Walipokaribia kwakuwa hawakuwa na tiketi wala kuponi ya kuingilia ndani ilibidi watumie njia mbadala, waliogelea wakaibukia ndani ya eneo la bahari ya hotel wakachangamana na wateja.
Kama samaki walizamia wakitumia vema pumzi zao zilizojaza vifua. Hakuna aliyechomoza kichwa nje ya maji mpaka pale walipoibuka. Hapo taratibu wakaanza kujongea kuifuata fukwe. Hawakusahau kuhakikisha macho yao yanatizama usalama kwa kuwaweka karibu walinzi na macho yao.
Walipokanyaga fukwe, Vitalis alijigawa akamfuata mlinzi mmojawapo aliyemtambua kwa sare yake. Akamuuliza akinyooshea kidole boti iliyoegeshwa kwa mbali kidogo.
"Ile boti ni ya nani, afande?" Aliongea kwa lafudhi ya kiswahili cha Kenya.
Mlinzi alitizama kule alipoelekezwa akauliza:
"Kwani kuna nini?"
"Naihitaji nikodishe!" Vitalis alijibu.

***


☆Steve
 
Doooh..!!
Mkuu Leo kazamia kambi ya beast itakuwa ,

haaah mkuu steve bado mpka muda huu!! au ndio unamalizia viroba vya mwishomwisho kwa usongo

Tuendeleee steve

muite muite mama akija nistue

Wayaaaa daaah mambo yanazidi kuwa mambo hongera mkuu

Hili balaa sasa
Nimekuja wakuu. Nipo hapa.


☆Steve
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom