***SURA YA HAMSINI NA SABA***
(MSIMU WA 02)
Giza lilitwaa jiji la Hamilton ambalo ukiachana tu na umaarufu wake wa kuwa na fukwe za bahari zinazovutia basi utakutana na bandari yake asili inayofanya kazi usiku mchana. Meli za makampuni makubwa kama DryShips Inc, Frontline Limited na Dockwise zilikuwa zinapishana kuingia makaoni mwake.
Sauti za mawimbi ya bahari, upepo mwanana na milio ya mabasi makubwa ya abiria ambayo bado yalikuwa yanatoa huduma ndio hasa zilikuwa zinasikika zikitumia utulivu wa usiku kwa faidaze. Mbali na hapo labda sauti za watu wachache hapa na pale.
Ndani ya jengo jeupe la ghorofa kwenye uwanja mkubwa walisimama wanaume wapatao themanini kwa idadi. Walichanganyikana wanaume weusi na wazungu. Vifua vyao vilivyojengeka kimazoezi vilikuwa wazi wakivalia suruali nyeusi za jeans. Migongoni mwao walibebelea mchoro mkubwa wa kichwa cha simba.
Mbele ya wanaume hao kulikuwapo na kiti kikubwa kirefu chenye rangi ya dhahabu. Hakikuwa na mtu lakini wanaume wote walikuwa wanakitizama kana kwamba kuna mtu asiyeonekana amekaa hapo.
Kim alitokea mlango wa kushoto wa uwanja, akanyookea kitini na kuketi. Wanaume wote nao wakaketi kitako chini wakimtizama.
“Nimewaita hapa kwa dhumuni la kuwataarifu kazi iliyopo mbele yetu. Ndani ya siku nne zijazo tunatakiwa tutengeneza msiba mkubwa. Msiba wa kifalme. Msiba utakaotikisa vichwa vya habari.”
Kim alisema kwa kujiamini akikaza macho yake.
“Nitawateua wanaume watano miongoni mwenu. Wanaume hao wataenda Oman. Wataenda huko kwa dhumuni moja tu: kummaliza Sultan Absaedy Omar ama mwanawe yeyote wa kiume. Nataka damu zao hapa kwa gharama yoyote ile … kwa gharama yoyote! … Wanaume hao watakaofanikisha hilo, watazawadiwa maradufu kwa ushujaa na ufanisi wao.”
Kim alinyanyuka akaweka mikono yake nyuma. Alitembea akipita katikati ya mistari ya wanaume waliokuwa wamejipanga akiendelea kumwaga maneno.
“Hakuna nafasi ya kufanya makosa katika hili. Ni eidha kufa ama kupona. Ni eidha wao wafe ama sisi tufe. Hatujawahi kushindwa vita yoyote ile na hii siyo ya kwanza na wala haitakuwa ya mwisho. Nawaamini.”
Baada ya maneno hayo aliwateua wanaume watano kwa kuwagusa mabegani. Wanaume hao wakasimama na kwenda mbele, wengine wakasimama na kutokomea.
Katikati ya wanaume hao watano walioachaguliwa, walikuwepo pia wanaume wale wawili waliokuwa na Kim wakati anatizama televisheni, walijulikana kwa majina ya Panther na Jaguar.
Kim aliwatizama akawapa ishara huku wengine akiwaambia kwa maneno:
“Nimewachagua nyie kwasababu naamini kwa dhati mnaweza mkafanya hii kazi. Nataka damu ya kifalme ije hapa ndani ya siku tatu tu. Siku tatu! Nataka mkajadili na kupanga usiku huu. Kesho asubuhi mnieleze nini mnahitaji kukamilisha hili zoezi.”
Wanaume hao wakaondoka wakimuacha Kim mwenyewe ameketi kwenye kiti chake kikubwa. Alifikira kwa muda kisha akatabasamu akitikisa kichwa.
“Nadhani hili litakuwa kisasi kizuri dhidi ya yule mshenzi aliyeninyima fursa ya kuwekeza kwenye biashara yake ya mafuta … Sultan, nipo njiani nakuja. Ulinihukumu kwa uchotara wangu, mimi nitakuhukumu kwa ncha ya upanga.”
***
Bakari akiwa pamoja na Miraji walitizama kioo cha tanakilishi mpakato kilichokuwa kinaonesha michoro ya simba na alama za maji kwa makini kana kwamba wanatafutia suluhisho hesabu ngumu.
Bakari alitikisa kichwa chake akauliza:
“Sijui hii michoro ina maanisha nini?”
Ukimya ulikatiza kwa sekunde kabla Bakari hajaendelea kunena:
“Ina mana kuna watu wengine wenye hii michoro, sio?”
“Nadhani.” Miraji alijibu.
“Sasa tutawapataje hao watu? Au tutawangoja mpaka watushambulie?”
“Inabidi tuwagundue mapema. Tofauti na ilivyokuwa kwa kundi la nyoka, wenyewe walitutafuta. Hatujajua hawa wenye hii michoro watatutafuta ama tutawatafuta. Ila tutakuwa salama zaidi endapo tutawatafuta kabla wao hawajafanya hivyo.”
Vitalis na Kaguta waliingia wakaungana na wakina Bakari. Waliendeleza mjadala wakijaribu kufumbua fumbo ambalo lilikuwa gumu kufumbuliwa.
Marietta aliingilia mjadala huo akamuiba Vitalis. Alitaka akacheze naye fukweni kwani alimkumbuka sana tokea yupo shuleni bweni. Vitalis alishindwa kukataa. Alimnyanyua Marietta akamuweka begani wakaenda zao kuchezea maji ya fukweni.
Walirushiana maji wakikimbizana. Walioga michanga. Waliogelea wakishindana kukaa muda mrefu majini. Mwishowe walilala kwenye mchanga mlaini wa fukwe wakitizama jua la saa mbili asubuhi. Hapo Bernadetha akajitokeza na kujiunga nao baada ya kukaa muda mrefu pembeni akiwatizama pasipo wao kujua.
Macho yake yalikuwa mekundu akitabasamu. Kwa muda wakati anamtizama Vitalis akicheza na mwanae, Marietta, alimkumbuka mume wake, Malale. Kila mwisho wa juma walikuwa wanaenda ufukweni kama familia. Huko walicheza na kufurahia kisha wanarudi nyumbani jua likizama.
“Karibu!” Vitalis alimkaribisha Bernadetha.
“Ahsante.” Bernadetha alijibu akimtizama mwanae.
“Vipi, kuna tatizo?” Vitalis aliuliza.
“Hapana. Hamna tatizo!” Bernadetha alijibu akilazimisha tabasamu. Alimbeba mwanae akamuuliza:
“Mlikuwa mnafanya nini?”
“Tunacheza! … Nilikuwa nacheza na anko!” Marietta alijibu kwa maajivuno.
“Alafu mama, nimemuambia anko anifundishe ngumi!”
“Ngumi?” Bernadetha alitabasamu. “Nani kakuambia anko anapigana ngumi?”
“Nilimuona! … siku moja nilimuona akipigana na anko Kaguta.”
Baada ya kucheka, Bernadetha akauliza:
“Wewe unataka ukampige nani?”
“Kule shuleni kuna mijitu migomvi!” Marietta alijibu. “Nataka niwapige mpaka wakome!”
Wote walicheka wakaondoka kurudi kwenye makazi yao.
Siku hiyo ilikuwa ni ya kupumzika. Hakuna kazi waliyofanya zaidi ya kupika na kula kisha kufurahia mandhari ya bahari. Waliogelea, walicheza mpira mpaka jua linatuama.
Kaguta akiwa pamoja na Sandra, Miraji, Jombi na Bakari waliaga wanatoka kwenda kujirusha nje ya kisiwa. Waliahidi kurudi siku inayofuata mapema, wanahitaji kupumzisha na kubadilisha mazingira mara moja.
Baada ya mvutano wa hapa na pale, walikubaliana waende.
“Kuweni makini.” Bernadetha aliwahasa.
“Usihofu. Wapo na mimi.” Kaguta akajibu akijinyooshea kidole.
Walitumia boti yao ndogo wakakata maji kwenda jiji la Dar, wakawaacha Bernadetha, Vitalis na Marietta kisiwani.
Haukupita muda mrefu baada ya kula chakula cha usiku, Marietta akapitiwa na usingizi. Vitalis alimbeba akampeleka chumbani alipomlaza na kumfunika na shuka.
Alirudi sebuleni akamkuta Berbadetha ametulia akijikunyata. Alikuwa anafikiria jambo ambalo halikuchukua muda mrefu akamshirikisha Vitalis:
“Samahani, Vitalis. Kuna muda naona picha ya mume wangu pale ninapokutizama. Sijui kwanini inakuwa hivyo. Haijalishi mara ngapi najitahidi kujizuia lakini haisaidii katu.”
Bernadetha aliweka kituo akitizama chini, mara chozi likaanza kumshuka.
“Leo wakati nakuona na mwanangu nili …”
“Sshh! …” Vitalis alimkatiza. Alimfuta chozi akamnyanyua uso.
“Usihofu. Haina haja ya kuomba samahani, Bernadetha. Naelewa. Naelewa unachojihisi … kuna mambo yakupasa uyaache yaende ili upate amani moyoni.”
Vitalis alimbusu Bernadetha shavuni kisha akambeba akimlaza mikononi mwake.
“Nataka uwe na furaha. Sipendi kukuona ukifadhaika.”
Bernadetha alipeleka mdomo wake kwa Vitalis wakanyonyana ndimi. Walielekea chumbani wakazima taa.
****
☆Steve