Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

Hii hali nanikumbusha kipindi cha nyuma kule bushi,
Jamaa alikuwa anaonye mikanda ya kichona kwenye godauni la lijiji kila siku saa nane mcha
Baaaaasi bana bana weeeee,

Unakuta toka asubuhi unahaha upate shilingi hamisimi, mishale ya saa tano hivi za asubuhi unakuwa unazunguuka zunguuka godauni ili wakifungua ukae siti za mbele,

Aseee mapaka ije ifike saa nane ushapiga miselee ya kutosha ukihesabiwa kilomita unazo za kumwaga.

Kilicho nikuta siku moja nimeuza mayai nishaiotea shilingi hamsini yangu niko napiga misele miguu peku, pensi haijulikani na hamsini yangu nimeweka kwenye kopo la mafuta ya raisi iliyoisha mafuta mwishowee ikafika saa nane jamaa haonekani, saa tisa jamaa haonekani

Mpaka ikafika saa kumi jamaa ndio huyooo kaja na taarifa mbaya eti genereta imeloga,
Bana bana weeee, ilibidi aambiwe ipone akawasha kakawaka kidogo kakazima jamani tuliumia mnoooo


Sasa hali kama hiyo imenirudia teeeeeena
 
***SURA YA HAMSINI NA MOJA***






(MSIMU WA 02)









Baada ya kupata chakula cha usiku, WAGENI wakiwa wamekaa kwenye mkeka walianza kuteta juu ya nini cha kufanya. Karatasi kubwa ilikuwa imetandazwa chini Bakari akiwa ameshikilia marker pen. Wote walikuwa wametulia kwa utulivu na baada ya kusali, Vitalis akaanzisha mjadala.
“Hatuna muda wa kupoteza ndugu zanguni. Nini ambacho mlikipata kwenye upembuzi wenu mpaka mkafahamu tulipohifadhiwa?”
“Tulichambua zile namba na kugundua zina maanisha neno BEAST. Sandra akatuamabia anafahamu jengo la mateso na mateka linaloenda kwa hilo jina, ndipo tukawapata.” Bakari alidadavua.
“Kwahiyo ina maanisha hili kundi la BEAST lina maeneo yake ya kufanyia unyama wao.” Kaguta alieleza alafu akauliza: “Kwahiyo lile eneo la kwanza litakuwa ni nini?”
“Bila shaka itakuwa ni ofisi.” Vitalis alijibu. “Na vipi kuhusu alama ya nyoka na visu?”
Kimya kikawashika kwa muda kabla Vitalis hajafungua mdomo wake kuuliza:
“Ujanja wa nyoka upo kichwani kwake, sio?”
“Ndio.” Wote wakamjibu.
“Sasa kidogo napata picha. Nyoka tuliyemuona kwenye kuta, ni mwenye vichwa vitatu, kwanini? … Kwasababu BEAST wana viongozi watatu.” Vitalis alijibu alichojiuliza na kuendelea:
“Nakumbuka wakati tupo kule kwenye lile jumba, mmoja wao alisema kwakuwa wao wamepoteza triple yao, ambayo ni wale mapacha, Emilio atalamba miguu ya Cruz na Santanna. Kwahiyo ina maanisha kuna watu watatu hapa: Emilio, Cruz na Santanna. Na wale mapacha watatu, yani triple, waliokufa walikuwa ni wa Emilio. It means kuna mapacha wengine watatu mara mbili, wa Cruz na wa Santanna, ndio kwa jumla wanaunda idadi ya visu tisa juu ya vichwa vile vitatu vya nyoka. Kwahiyo sasa hivi kwenye vichwa vya nyoka hawa watatu kuna visu tisa tu.”
“Na kwanini ni visu si risasi wala mabomu juu ya vichwa vya nyoka hao?” Miraji aliuliza.
“Nadhani pia hapo pana siri ya kuifunua.” Vitalis alitanabahi. “Watu watatu ambao walikuwa wanahusika na kututesa, wote walikuwa na kovu za kisu sehemu mbalimbali, hasa za vichwa vyao. Kwanini si za risasi ama kitu kingine?”
Kimya kilitawala kwa muda kidogo. Jombi akachangia:
“Ila mnakumbuka wakati tunaenda kuwaokoa wenzetu tulitumia silaha gani?” Aliwatizama Sandra, Bernadetha na Miraji.
“Tulitumia visu kwasababu ya kutowashtua wenzao.” Sandra alijibu.
“Kuna kitu gani kilitokea tulipotumia visu hivyo?” Jombi aliuliza. Bernadetha akajibu:
“Waliwahi kuwa wa baridi baada tu ya muda mfupi kisu kugusa nyama na damu zao.”
“Sasa kwanini wawe na makovu ya visu wao wenyewe?” Vitalis aliuliza.
“Itakuwa ndio mtindo wao wa kiapo.” Sandra akajibu. “Kwenye kila kundi wana miiko na taratibu zao. Kile kinachowekwa kwenye tattoo lazima kiwe kina mahusiano na viapo. Na pale wanapovikiuka, ni hivyo viapo ndivyo vitawahukumu.”
“Yani kumaanisha nyoka kama vile ilivyokuwa jitu?” Kaguta aliwahi kuuliza.
“Ndio!” Sandra akajibu.
“Kwahiyo kwa sasa tuna shetani mpya wa kuhangaika naye, sio?” Vitalis akauliza kama mtu asiyetegemea jibu. Kisha akatabasamu utadhani ni mazuri.

****

Baada ya kuvuta sigara aliumeza moshi akautolea puani. Akaagiza tena kinywaji kingine kikali na kuendelea kujipa huduma taratibu akiwaza jinsi gani atawatia mikononi mateka wake waliotoroka. Hakutaka kushindwa kabisa – hiyo si asili ya Mamba. Yeyote atakayeingia kwenye maji basi ni halali yake na hakuna cha salia mtume. Alinyonya tena sigara yake akarusha moshi juu, mara hii akadidimiza mkono mfukoni akatoa simu ndogo nyeusi akaweka namba na kuipachika sikioni.
“Upo wapi? … Fanya upesi ni pakti ya sigara sasa namaliza na bado hujafika.”
Alirudisha simu mfukoni akabeba kinywaji amwagie mdomoni. Baada ya dakika chache akawasili mwanaume mwenye kovu kichwani, Bode. Alikuwa amevalia shati la kitenge linaloendana na suruali yake. Huwezi ukabashiri ya kwamba ni muuaji mkubwa ndani ya nguo hizo nadhifu zenye rangi zisizoita macho kwa ukaribu.
“Umepata nini?”
Mamba alimpokea mgeni wake na swali. Bode akashusha pumzi kwanza.
“Hakuna kipya, mzee. Nimejaribu sana kuulizia kwa kutumia picha lakini sijafanikiwa.”
Kimya kikakatiza katikati yao mpaka pale mhudumu alipokuja kumuuliza Bode angependelea huduma gani, akaagiza pombe yoyote kali.
“Kuna haja ya kurudi ofisi ya taarifa?” Bode aliuliza.
“Hapana.” Mamba akajibu kisha akatulia kwanza akichakaza kichwa. Mhudumu akaja akiambatana na kinywaji alichoagizwa, akakiweka mezani na kukifungua, alipoondoka Mamba akasema:
“Nadhani kuna njia nzuri zaidi ya kuwatafuta watu wetu. Hatutohangaika tena, bali wao ndio watakaotutafuta.”
Bode akapiga fundo moja na kutabasamu kana kwamba kinywaji kimegusa penyewe.
“Hapo ndipo nakukubali, Mamba. Upo fasta kuchonga mawazo. Embu nishirikishe hilo wazo lako. Njia gani hiyo?”
Mamba akajibu huku akikuna kidevu.
“Tutakachokifanya sasa hivi ni kuvamia shule na kuwateka wanafunzi kadhaa. Kwa kuwa wale wapumbavu wanataka sifa, watajaribu kuwaokoa na hapo ndipo watakaporudi mikononi mwangu na sitawaletea tena mzaha, nitawapa usafiri mzuri wa kwenda kuzimu.”
Bode akatikisa kichwa kuafiki wazo. Akanywa chupa yote ya pombe na kuagiza nyingine ambayo nayo aliinywa kwa pupa ingali kichwa ki chepesi. Baada ya dakika kadhaa mbele pombe zilianza kumgonga kichwa akasahau ya kwamba yupo bar na wanaongelea mambo ya hatari, sauti yake ikapanda. Mamba kuepusha adha alilipa bili akamnyanyua Bode na kuondoka naye kuelekea garini akimkokota. Waliwasha chombo wakayeya. Ila punde tu akatokea mwanamke aliyevalia nguo za wahudumu akaitizama gari lile likitokomea. Alikuwa ni Bhoke. Hakubanduka kando ya barabara mpaka pale taa za gari lile zilipopotelea. Lakini pia Mamba alimuona mwanamke huyo kwa kutumia kioo cha gari kilichoketi juu ya paji lake la uso. Alipata walakini lakini haukumkonga sana moyo wake, labda mhudumu yule alikuwa anataka kumrudishia chenji yake, aliwaza.




***

☆Steve
 
***SURA YA HAMSINI NA MBILI***






(MSIMU WA 02)




Bhoke alirejea ndani ya bar akiwa ametwaliwa na uso wa fikra. Mkononi mwake alikuwa amebebelea chenji ya mteja ambaye badala ya kumuita na kumpatia alibakia akimsikiliza kwa butwaa. Wanataka kumuua nani? Wanataka kuvamia shule? Kwanini? Hawa watu ni wakina nani? Kichwa cha Bhoke kilivuma. Mwishowe aligongana na mteja kwasababu ya mawazo. Aliomba radhi haraka akakimbilia kaunta. Alishika simu yake akitaka kumpigia mtu amwambie, ila ampigie nani sasa? Alimuita mwenzake karibu akamshirikisha, hapo akapata wazo.
“Si umpigie yule bwana ‘ako mwanajeshi?”
Haraka Bhoke akatafuta namba ya Kaguta na kuipigia.
“Samahani, namba ya mteja unayempigia haipatikani kwa sasa.” Alikatishwa hamu na ujumbe huo. Uso akaukunja.

***

Haikuwa usiku wala mchana mazoezi yasifanyike ndani ya kisiwa kando na Mafia. WAGENI walikuwa wanajinoa haswa ndani ya maji na nchi kavu wakijifua zaidi namna ya kutumia silaha, kutunza pumzi ndani ya maji, kuongeza pumzi mapafuni na kutafuta ustahimilivu. Waliamka saa kumi na moja alfajiri wakilala saa saba ya usiku. Walitota jasho wakati wa mchana jua likiwa kali huku miili ikisinyaa wakati wa usiku baridi likipiga. Lakini hiyo ikawa haitoshi kwa Kaguta na Vitalis ambao waliendelea kujifua hata pale wenzao walipopumzika. Mara kadhaa walikuwa hawalali kabisa wakishinda wakikimbia ama kuogelea, au wakipambana wenyewe kwa wenyewe. Vita iliyokuwa mbele yao ilikuwa ni kubwa – halikuanduka hilo kichwani mwao.
Wakati sasa yapata kuelekea jioni ndani ya siku ambayo haikuonyesha dalili zozote za mvurugo, Kaguta alikuwa anajiandaa apate kwenda mjini Mafia kuchukua mahitaji ya kuwasogeza siku kadhaa mbele. Mwili wake uliojaza ulikuwa umeshikwa na shati la kijani lililombana huku miguu yake ikifichamwa na kombati na buti la jeshi. Kichwani alikuwa amevalia pama ikiwa na maandishi … can you suck me?
Haikupita hata dakika nyingi Kaguta akawa tayari yupo ndani ya kamji kadogo ka Mafia. Hakuonekana kama mtu mwenye wasiwasi wowote mpaka pale alipotikiswa na mngurumo wa simu mfukoni mwake. Hakuzoea hiyo hali, kukaa sana kisiwani kusipo na mtandao kulimfanya asahau kidogo simu. Alipoitoa na kuitizama, akasonya.
“Huyu Bhoke anataka nini lakini?” Alilaumu akisoma ujumbe toka kwa Bhoke ukimtaka aonane naye haraka iwezekanavyo. Alipuuzia akarudisha simu mfukoni na kuendelea na mambo yake. Kabla ya jua kuzama alisharejea kisiwani. Bahati nzuri ama mbaya, Sandra akashika simu ya Kaguta na kuukuta ujumbe wa Bhoke. Alifura. Moja kwa moja alidhani Kaguta alienda kuonana na malaya huyo.
Alipanua kifua chake kwa kuficha jambo hilo kifuani. Kesho yake akatoroka na kwenda mjini Mafia, akampigia simu Bhoke. Baada ya kubishana kwa sekunde kadhaa juu ya Kaguta, Bhoke akampasha habari Sandra.
“Kuna majambazi wawili wanataka kuvamia shule ya Kwembe kesho wawateke wanafunzi. Walikuja hapa bar juzi wakaongea hayo mambo. Naomba umfikishie Kaguta hizi habari. Umesikia?” Bhoke aliuliza kwa nyodo kisha akakata simu. Sandra hakuamini, aliona ni janja tu ya Bhoke kukwepa mashtaka ya kudandia wanaume wa watu. Alisonya na kulaani kana kwamba Bhoke anamsikia. Alirudi zake kisiwani akajitahidi kukaa na hilo jambo kwa dakika chache tu kabla ya kufunguka kwa hofu ya usalama. Aliweka aibu yake ya kuchukua simu ya Kaguta bila ya taarifa, akafikisha habari.
“Hili si jambo la kupuuza. Watakuwa ni wana BEAST sasa wanatutafuta kwa njia mbadala. Nadhani wametupa sehemu nzuri ya kuanzia.” Vitalis aliwika. “Kaguta, nenda ukutane na Bhoke. Hakikisha anakupa kila elezo muhimu.”
Sandra hakufurahishwa sana na hayo maamuzi. Labda alitamani aende yeye na si Kaguta. Ama waende wote basi.

***

Mida ya jioni ndiyo bar hufurika wateja wakiwa wametoka vibaruani. Wahudumu wanakuwa wapo bize wakizunguka huku na huko na sketi zao fupi zinazotekenya mapaja. Mbali na kufungua vizibo vya vinywaji walikuwa pia wanafungua matabasamu na kutembea kwa madaha wang’oe wanaume ama wahongwe bia mbili tatu.
Miongoni mwa wateja hao alikuwamo Kaguta. Alikuwa ameketi mwenyewe kando kando ya bar, juu ya meza chupa ya Grants ikiwa imesimama wima pasipo na glasi. Macho yake yalikuwa lindo akitizama huku na huko. Baada ya muda Bhoke alijiunga naye.
“Sina muda wa kukaa sana hapa, si unaona wateja ni wengi.” Bhoke alijibaraguza. Kaguta akatabasamu kisha akanywa fundo moja la Grants.
“Punguza hasira na mimi, mama. Nambie kinagaubaga nini ambacho ulikiona na kukisikia.”
“Nimeshamwambia hawara ‘ako. Hajakuambia?” Bhoke alibetua mdomo.
“Bhoke, ndio mana nimekuja hapa. Najua kuna mengi ya kupata toka kwako. Kama basi hunipendi, fikiria kidogo kuhusu usalama wa watoto hao watakaoenda kudhuriwa.”
Baada ya nyodo za hapa na pale, Bhoke akaeleza yote aliyoyaona.
“Unaweza ukaniambia plate number ya hiyo gari waliloondoka nalo?”
“Sikumbuki. Ila lilikuwa ni gari jeusi lenye vioo vyeusi. Na limeandikwa be-a-st kwenye kioo cha nyuma.”
“Sura zao je?”
“Mmoja ambaye ndiye aliyetangulia, ana kovu kando ya sikio na macho yake ni makali mno na ya kutisha. Mwenzake ana kovu kubwa kichwani, ana mwili wa kawaida.”
“Kipi ulisikia?”
“Baada ya kupeleka kinywaji cha pili kwa yule mwanaume mwenye kovu kichwani, muda mfupi tu akaanza kuropoka ropoka mwenzake akijitahidi kumnyamazisha. Alisema hakuna wa kuwazuia huko Kwembe na watamuonyesha mkubwa wao kwamba wao ni wa maana pia.”
Baada ya maelezo hayo, Kaguta alimaliza kinywaji chake akaaga akimtaka Bhoke awe makini mno maana hao watu ni hatari. Na atakapowaona tena popote atoe taarifa hata polisi.
“Sasa huniachii hata tip?” Bhoke alimuuliza Kaguta kabla hajayoyoma.

****

Shule ya Kwembe ilikuwa imejitenga kidogo na purukushani za jiji la Dar es Salaam. Kwa mtu kupata kuifikia ilimpasa aache barabara ya lami kwa umbali usiopungua kilomita tatu alafu akatishe kwenye barabara iliyofunikwa na miti mbalimbali na kutengeneza kiza hata pakiwa mchana. Upande wake wa mashariki ilikuwa imepakana na maji ya bahari ya hindi. Kaskazini imepakana na misitu ya mikoko huku magharibi vijumba hoi vya wavuvi. Si bure wadhalimu walichagua hiyo shule. Ni rahisi kutoweka. Sehemu za kupotelea zi kedekede pia ni ngumu kwa msaada kupatikana kwa wahanga. Japokuwa shule ina wanafunzi wa msingi na upili bado haikuonekana kufurika. Watoto walikuwa wengi maeneo ya ufukweni na baharini wakivua samaki na kuogelea kuliko wale waliopo madarasani.
Wakati kengele ikitangaza kikomo cha mapumziko na kuwataka wanafunzi warejee madarasani, gari nyeusi aina ya van ilitokeza ikiwa katika mwendo wa kawaida usiomshangaza yeyote. Ndani walikuwemo wanaume wanne wa kazi: Mamba, Bode, Shaziri – mwanaume kijeba aliyenyoa ‘kiduku’ akiendesha gari na Yosso, mwanaume mwembamba aliyejichora chora mwilini. Waliposhika barabara ya kuelekea shuleni hapo kwa mbele kidogo wakakutana na gogo kubwa katikati ya barabara. Gari likasimama, Shaziri akashuka. Baada ya muda kidogo Mamba na wenzake wakaona kimya, Shaziri hakurudi na gogo bado lilikuwa barabarani.
Mamba akiwa na uso wa mashaka alimuamuru Bode pamoja na Yosso washuke kutizama usalama. Wakashuka wakiwa wamebebelea bunduki. Walitizama kushoto na kulia kwao pasipo kuona mtu yeyote, walipotizama juu ya mti ikawa kosa. Walimwagiwa unga rangi ya manjano usoni wakapiga mayowe ya maumivu wakirusha silaha kando. Kufumba na kufumbua mwili wa Shaziri ukadondoka toka juu ya mti alafu wakashuka wanaume watatu wakiwa wamevalia nguo za jeshi na kofia za kuficha nyuso wakaanza kumiminia risasi van kwa fujo. Kwa pupa van ikarudi nyuma na kuondoka kwa kasi mno ikiwaacha watu iliokuja nao mahututi. Kabla watu hawajajaa eneo la tukio likaja gari ‘defender’ likiendeshwa na Bakari, wanaume wale watatu wakapanda pamoja na mateka zao wakapotea haraka.
Ila Mamba bado alikuwa hai!


***

☆Steve
 
***SURA YA HAMSINI NA TATU***





(MSIMU WA 02)






Hilo jambo lilimuumiza sana Vitalis. Alijihukumu kushiriki uzembe wa kumruhusu mshenzi kama yule atoroke mbele ya macho yake. Alijua fika uhai wa mamba ni vifo vya wasio na hatia. Hakuna yeyote anayejua ataenda kufanya nini baada ya jaribio lake la kuteka wanafunzi kushindikana. Ni lazima atiwe mikononi haraka! Afunzwe adabu! Mwili wake uvunjwe vunjwe na umeze risasi si chini ya tano! Aliwaza Vitalis mwenyewe akiwa amebinua mdomo wake na amekunja sura kama mtu aliyekunywa dawa chungu.
Sasa ni fursa ya kuvamia ofisi yao na kuisambaratisha. Tusimpe muda wa kupanga mambo yake zaidi.

****

Baada tu ya muda mchache baada ya tukio la utekaji wa wanafunzi kushindikana, Mamba alishakuwa mtu tofauti kwa kubadilisha mavazi na hata usafiri – haikuwa tena van wala mark X aliyokuwa anaendesha bali range rover nyekundu aliyoisogeza mpaka eneo la bar. Uso wake ulikuwa umebeadilika kwa kupachikwa ndevu za bandia na macho kufunikwa na miwani meusi.
Alishuka akatembea taratibu mpaka ndani ya bar, punde akatoka na Bhoke akiwa kamkamatia kiuno wakitabasamu na kuongea. Alimfungulia mwanamke huyo mlango akaingia ndani, gari likang’oa nanga.
Baadae mida ya saa kumi na moja jioni, Bhoke akakutwa akiwa mfu ndani ya Limpopo guest house, Sinza, kifua chake kikiwa kimetobolewa na risasi tatu. Mdomo wake umeachama na macho yapo wazi. Shuka limetapakaa damu. Si mapokezi wala yeyote aliyesikia milio ya risasi wala kelele zozote, zaidi maelezo yalisema mwanaume aliyeingia na marehemu aliondoka baada tu ya dakika chache walipoingia chumbani.
Habari hizo zilisambaa kwa kasi kwenye mitandao ya kijamii. Na hata zikachukua nafasi kwenye taarifa za habari. WAGENI walifahamu fika ni nani aliyefanya huo unyama. Kukaa kwao kimya kungeendeleza matukio hayo ya umwagaji damu. Siku inayofuata ilikuwa ni alhamis – siku adhimu kwa shambulizi la ofisi ya BEAST. Sandra akishirikiana na Kaguta na Vitalis walitega gari lao pembeni kidogo ya barabara umbali wa kilomita moja tokea ofisi za BEAST zilipo. Punde wakiwa hapo wakaona gari la kusambaza sigara laja, wakaliteka na kwenda nalo mpaka mbele ya uzio wa jengo hilo lenye ulinzi mkali. Wakiwa wamevalia nguo za wahudumu, ilikuwa ngumu kugundulikana. Walitumia bunduki zao zenye viwamba vya kumeza sauti wakawamaliza walinzi wote wa nje kisha wakagonga geti na kuingia ndani ya uzio kwa urahisi mno.
Ndani ya sekunde kumi tu, walinzi wote wakawa wamelala chini wakivuja damu waliokuwemo ndani wasijue kinachoendelea huko nje. Vitalis na wenzake wakajigawa mmoja akaenda upande wa kushoto, mwingine kulia na mmoja katikati. Ufahamu wao juu ya hilo eneo kwa kutumia teknolojia ya google map uliwasaidia kunyambua mazingira vema. Mikono yao mepesi iliyokomaa kwa mazoezi na mateke yao mazito yenye nguvu yalirahisisha sana kazi – haikuonekana ngumu hata kidogo ukilinganisha na mazoezi yao wanayoyafanya kila uchwao. Mpaka wanaingia kwenye chumba cha mkuu, hawakuwa hata na mchubuko. Walisimama wima mbele ya mwanaume wa kilatini aliyelaza nywele zake nyuma kwa ustadi mkubwa, mdomoni mwake akiwa ana sigara kubwa. Macho yalikuwa yamemtoka kwa butwaa – wazi hakutegemea watu kuvamia ngome yake na kuingia kwa urahisi hivyo, tena bila hata ya kutambua.
“Who are you?” Mlatini aliuliza kwa uso uliokuwa unajitahidi kufichama hofu. Alitoa sigara yake akailaza kisosini.
“We are your angels of death.” Vitalis alijibu kwa kebehi kisha akamuamuru mlengwa wake asimame upesi kabla hajammwaga ubongo. Mlatini akawa mkaidi kidogo, alijaribu kufungua droo yake atwae bunduki, kabla droo haijasogea risasi ikapiga kando yake na kumshtua.
“Don’t even dare to try!” Kaguta alisema na uso wa kazi ‘uso wa mbuzi’ kisha akamtwaa Mlatini huyo na kutangulia naye nje pamoja na Sandra, Vitalis akibakia kidogo ofisini macho yake yakitembea tembea huku na huko.
Juu ya ukuta mdogo wa ubao wa matangazo, Vitalis aliona picha kadhaa za mifuko ya mbolea na matangazo ya biashara hiyo. Aliposogea na kutizama kwa ukaribu picha hizo za mbolea, chini yake akaona tarehe 8/8/2014 – Ilikuwa siku ya nanenane! Siku ya wakulima! Bila shaka BEAST walikuwepo kwenye maadhimisho ya sherehe hiyo wakitangaza bidhaa yao. Na pasipo kujua wakulima wakanunua bidhaa zao – mabaki ya binadamu wenzao waliouwawa na kuzikwa kimakundi kisha kuchanganywa na kemikali mbalimbali.
Bila shaka BEAST watakuwepo tena kwenye maadhimisho ya sherehe hiyo karibuni. Vitalis aliwaza. Bado wiki moja tu sikukuu ya nanenane ifikie kilele. Huo ndio muda muafaka sasa wa kuwatia wadhalimu hawa mikononi na kumsaidia Mungu kuwahukumu.

***

Hali ya utulivu na pilikapilika za hapa na kule zilimeza jiji la Dar es Salaam. Maduka yalifurika watu wakikatiza kule na kule katika mitaa ya Kariakoo. Kama kawaida kila mtu alikuwa ameshika yake, ukitizama kwa juu unaweza ukasema ni sisimizi wamemwagwa eneo hilo, kumbe ni watu! Katikati ya watu hao alikuwemo mwanaume mmoja aliyevalia suti nyeusi mkononi amebebelea briefcase. Alikuwa yu nadhifu mno. Kichwa chake kilikingwa jua na kofia safi nyeusi yenye ufito mwekundu. Macho yalizibwa na miwani nyeusi huku mdomo ukiwa umezungukwa na ndevu nyingi. Hakuwa mwingine, bali Mamba. Lakini kumfahamu ilihitaji uchambuzi wa hali ya juu. Dhahiri shairi alikuwa ana tukio la kufanya eneoni hapo. Laiti kama wananchi wangelikuwa wanafahamu wangelikimbia kuokoa pumzi zao.
Alitembea kwa wima pasi na hofu. Alikata mitaa akiwa anapiga mluzi taratibu kama njiwa pori. Kichwani kwake alikuwa amelaza ramani nzima ya tukio analotaka kulifanya – kulipua soko kuu! Alizama ndani ya jengo hilo mpaka chini kabisa kana kwamba ni mteja. Akiwa anatembea tembea na kutizama tizama hali ya usalama, mwanaume mmoja alimsimamisha, alikuwa ni mlinzi. Mamba alipata shaka lakini hakuruhusu hilo jambo liteke uso wake. Alitabasamu akauliza:
“Kuna shida afande?”
Huku mkono wake ukiwa tayari umeshakakamaa kufanya tukio lolote litakaloamuliwa na akili yake iliyokuwa inachemka.
“Vipi, wewe ni mgeni humu?” Mlinzi aliuliza. Mamba akatabasamu, alijua mlinzi alimuona wakati anayasoma mazingira. Japokuwa yeye ni mwenyeji huwezi mdanganya lolote kuhusu Dar, aliamua kujifanya mjinga.
“Ndio, mimi ni mgeni.” Alisema na sauti yenye mkandamizo wa kisukuma kwa mbali. Hilo likatosha kumfanya mlinzi ajue ni mtu toka kijijini.
“Nimekuja natafauta mbolea nzuri ya mahindi yangu.”
“Oooh! Nenda mbele kidogo alafu ukunje kushoto, utaona duka la mbolea na madawa ya shambani. Sawa mzee?”
“Sawa. Nashukuru gete!” Alisema Mamba kasha akafuatisha ushauri aliopewa. Alinyookea dukani hapo akajifanya mteja anayeulizia bidhaa. Aliweka mkoba wake chini kisha akaondoka kama mtu anayejinasibu kuusahau mzigo huo. Alitembea kwa kasi mno akielekea kutoka nje. Mlinzi aliyemuelekeza duka la mbolea alimuona mtu wake huyo akitembea haraka huku mkononi akiwa mtupu – akapata shaka. Eidha ameibiwa na watoto wa mjini – aliwaza. Haraka alianza kumfukuzia Mamba huku akijaribu kumuita. Mamba alizidi kusonga asigeuke nyuma kabisa ingawa alisikia sauti ya mlinzi ikimuita. Alipoacha jengo la soko nyuma kwa hatua kadhaa mlipuko mkubwa ukamrusha mbele akadondokea kwenye gari. Jengo lote la soko lilikuwa linawaka moto kama vile tanuru. Taharuki ilikamata watu wakakimbia huku na huko. Hakuna mtu yeyote aliyekuwa ndani ya soko akatoka mzima. Mlinzi pekee aliyekuwa anamkimbiza Mamba ndiye aliyepona. Aliamka akarusha uso wake kwa mbali akamuona Mamba akiyoyoma katikati ya umati wa watu unaokimbia. Alinyanyuka akamkimbilia lakini hakumuona abadani. Mamba alikuwa tayari ameshavua na kutupa kofia yake na ndevu zake bandia zilikuwa tayari zimeshatupwa kando. Ilikuwa ni ngumu tena kudhani kama ni yuleyule aliyekuwa amebeba mkoba awali. Alikuwa ni mtu mwingine akiwa tayari ameshawateketeza watu 250 ndani ya dakika, sasa akiwa tayari yupo ndani ya taksi akisepa. Huo ulikuwa ni ujumbe maridhawa sana kwa WAGENI. Wameuwa watu wake watatu na kumteka mkuu wake, sasa yeye ameua watu 250. Nani zaidi? Alijikuta akitabasamu.

***

Zilipita siku tatu za vuguvugu la tukio la ugaidi Dar es Salaam, Kariakoo. Bado watu wa Dar hawakuwa na amani, maongezi yao yalitawaliwa sana na hilo tukio la kutisha mno kuwahi kutokea katika nchi ya Tanzania. Japokuwa jeshi la polisi lilitoa tamko lake likijinasibu kufuatilia na kumtia mikononi mhalifu aliyeshiriki, bado haikutosha kuondoa ukakasi wa hofu uliowaganda wananchi waliokuwa kwenye maombolezo. Mbona siku zazidi kuyoyoma na mtuhumiwa hajakamatwa? Hilo swali lilihukumu kazi ya polisi.
Kando kando ya bahari ya hindi iliyokuwa inapuliza kwa mawimbi madogomadogo, Vitalis aliketi akiwa ana mawazo. Kwa mara ya kwanza alijihisi hana mchango wowote kwa wananchi wa Tanzania. Kama watu 250 wanakufa na yeye yupo hai, ana faida gani sasa? Alijiuliza. Alijihisi si lolote si chochote. Alijiona ngoma yake ya kitoto haswa.
Mawazo yake yalitambaa juu ya maji ya bahari. Upepo mkali uliokuwa unampuliza haukusaidia chochote kuondoa zigo la tafakuri alilonalo kichwani. Alijikuta akisaga meno yake huku akikunja ngumi kakamavu. Alitamani Mamba atokee ili apate kumtia adabu na kumvunja vunja bila huruma. Aliishia tu kutamani na kutamani, hakujua wapi atampata adui wake huyo – hawezi akakaa tena na kule kiwandani – anajua yupo mtaani kuonyesha umwamba wake dhidi ya mapacha watatu, ila haswa ni wapi aende ili amkamate baradhuli huyo amuonjeshe kifo? Alibaki anawaza mpaka pale aliposhtuliwa na mkono begani.
“Usiwaze sana, Vitalis.” Sauti ya Bernadetha ilimkarimu. Alinyanyua uso wake akamtizama mwanamke huyo mwenye sura tamu. Akajikuta anatabasamu kwa mbali. Bernadetha aliketi karibu na Vitalis, akamshika mkono.
“Unadhani huyu muuaji ndiye Yule aliyemuua Waziri?” Bernadetha aliuliza.
“Bila shaka ndiye yeye akiwa ametumwa na mkuu wake tuliyemkamata.” Vitalis akajibu kisha akaongezea: “Kwa mujibu wa maelezo ya mlinzi wa soko, kimo cha mtuhumiwa na sifa za mwili wake ni sawa na zile za yule aliyemuua waziri kutokana na maelezo ya mtoto wa marehemu. Ametusakizia kifo cha waziri na sasa anachokifanya ni kuzidi kuwafanya wananchi waamini kile walichokianzisha, uongo. Pia kututaabisha.”
Bernadetha alitizama maji ya bahari akisema:
“Ndiye yeye pia aliyemuua Bhoke … Ila si ulisema umepata nafasi nzuri ya kuwakamata?”
“Ndio, sikukuu ya nanenane, ila naona mbali. Mpaka pale siku hiyo itakapowasili atakuwa kaua wananchi wangapi wasio na hatia?”
Walinyamaza kwa muda, Bernadetha akasema:
“Labda nina wazo.”


***

☆Steve
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom