***SURA YA HAMSINI NA TANO***
(MSIMU WA 02)
Baada ya dakika moja Mamba akanyanyuka tena apambane. Mara hii alitaka kuifuata bunduki yake ili amalize kazi kwa wepesi, ila kabla hajaifikia Vitalis aliilenga bunduki hiyo kwa bomu, bunduki ikaenda mbali zaidi. Ile Mamba kumtizama Vitalis akashangaa mtu yupo hewani kufumba na kufumbua akazawadiwa mateke mawili kwa pigo la kisigino, chali akaachwa hoi, mdomo wazi. Vitalis akaokota bomu na kuendelea kushughulika nalo sasa muda ukiwa umebakia dakika tano tu lilipuke na kugeuza eneo lote bahari ya moto.
Kwa uangalifu mkubwa, Vitalis akafukunyua bomu hilo na kukuta waya tatu zenye rangi tofauti tofauti. Aligusa kila waya na kusikilizia kwa muda kama inapitisha moto. Baada ya muda vidole vyake vikawa vimebakia na waya rangi ya njano tu baada ya akili yake kutambua kwamba ndio waya wa kuukata ili bomu likome.
Sasa ilikuwa ni kupata ama kukosa.
Kama atakuwa amelikosea bomu litafyatuka na kutekeza wote. Kama atakuwa amefanya mahesabu yake vyema, atakuwa ameokoa watu lukuki waliomo ndani ya jengo hilo.
Alishusha kwanza pumzi ndefu alafu akafunga macho. Kwanguvu zake zote akauvuta na kuukata waya huo wa njano. Bomu likaacha kuhesabu muda. Vitalis akatabasamu kwa kujipogeza. Akaikota bunduki na kumnyooshea Mamba apate kummaliza. Ila kabla uamuazi huo haujapita, akasikia vishindo vya watu vikija.
Wanaume watatu, maafisa wa usalama, walikuwa wanaongozana wakielekea maliwatoni wakiteta. Walipokamata korido ya uchaguzi wa vyoo wakashangaa kumkuta mwanaume, Mamba, amelala chini pembeni yake kukiwa na bomu na bunduki. Walitoa bunduki zao wakapekua pekua wasimuone mtu mwingine yeyote. Walimuweka Mamba chini ya ulinzi wakamtwaa na kumpeleka kituoni.
Kukutwa na ndevu bandia, bomu na bunduki kulimweka Mamba hatiani. Taarifa za habari ziliporushwa kutangaza hatia hiyo, ushahidi wa mlinzi wa soko kuu na mtoto wa marehemu waziri akisaidiana na Sandra ukazidi kukazia kamba kwenye hukumu ya Mamba.
Hakuwa na nafasi yoyote ya kuwa huru tena.
*****
Asubuhi hiyo bahari ilikuwa na mawimbi makubwa yenye hasira yaliyochapa fukwe kwa fujo na kutengeneza sauti ya nguvu. Jua lilikuwa kali pamoja pia na upepo wa bahari.
Ilikuwa ngumu kuamini kama kuna watu ndani ya maji ya bahari yaliyoonekana tu kwa macho kwamba ni marefu na yenye nguvu mpaka pale wanaume wawili: Vitalis na Kaguta, walipotoka kwenye maji hayo baada ya nusu saa wakiwa wamevalia nguo zilizobana miili yao barabara.
Walitembea kwa ukakamavu wakielekea kwenye makazi yao huku wakichonga maneno kuhusu siku ya nanenane. Walipofika ndani walimkuta mtoto tu, Marietta, akiwa amelala, wengine wote walikuwa upande wa pili wa fukwe wakifanya mazoezi mbalimbali ya kutengeneza pumzi na kujenga stamina.
Baada ya lisaa limoja wote walikutana mezani kupata kifungua kinywa, wakawa wanaongea na kupanga yale ya kutendeka ndani ya mkoa wa Dodoma, mkoa utakaoshuhudia sherehe ya nanenane kwa mwaka huo. Tageti yao kubwa ikiwa ni kuwakamata waamerika kusini watatu: Emilio, Cruz na Santanna.
“Tunafahamu fika kutakuwepo na pacha tatu mbili kwenye hiyo shughuli. Tunatakiwa tuwe wepesi zaidi wa kufanya maamuzi kuliko kawaida. Wote hapa tunajua jinsi mapacha walivyo haraka na wenye nguvu. Inahitajika matumizi ya akili zaidi. Hakikisha unatumia vyema sindano zenye dawa kuwafanya wawe dhaifu. Hakikisha pia unakuwa kwenye mawasiliano na wenzako. Na pia hakikisha watu hawa watatu wanakufa kwa gharama yeyote ile.” Vitalis alihutubia akiwatizama wenzake machoni. Wote wakaridhia na kufanya maongezi yawe mafupi zaidi kabla ya kumaliza kula, kupumzika na kisha kwenda kufanyia mazoezi walichopanga siku hiyo ya nanenane wakitumia miti iliyochongwa kama watu.
Zilipopita siku tatu ndipo ikawadia siku ya tukio – siku ya kufa ama kupona – tarehe nane mwezi wa nane. Vitalis akiwa amevalia suti nyeusi isiyo na tai aliongozana na wenzake: Kaguta, Jombi, Sandra, Bakari na Miraji wote wakiwa ndani ya suti nyeusi wakaingia ndani ya uwanja wa sherehe na kuketi juu kabisa.
Bakari alifungua tanakilishi akajaza mtandao. Alipobonyeza vitufe mara tatu akajiona alipo na wenzake kwenye ramani. Akatikisa kichwa na kuweka earphone.
“Tayari, nawaona wote sasa. Embu jaribu na sauti.”
Sandra aligeukia upande wake wa kushoto alafu akaongea maneno kadhaa, yote yakasikika kwa Bakari. Bakari akatikisa kichwa.
“Tayari na sauti pia. Mnaweza mkaenda sasa.”
Baada tu ya hayo maneno wote wakatawanyika wakimuacha Bakari peke yake na tanakilishi yake wakawa wanawasiliana kila mtu akiwa kwenye pande yake.
Baada ya muda mfupi:
“Kuna watu watatu wanaingia ukumbini sasa hivi, nadhani ndio watu tunaowatafuta.”
Sauti ya Vitalis ilifika masikioni mwa Bakari. Punde ikaambatana na picha kwenye tanakilishi.
“Umeziona hizo picha?”
“Ndio.” Bakari alijibu.
“Embu zitizame kama ni wenyewe.”
Bakari alifananisha picha hizo alizotumiwa na zile alizozipakua kwenye mtandao kuhusu kundi la kijambazi, majibu yakaja ni zenyewe baada ya macho kufanyiwa upembuzi.
“Ndio wenyewe.”
“Sawa sawa.”
Vitalis akawasiliana na wenzake kuwataarifu upande ambao mlengwa wao yupo ili wahakikishe hawawapotezi kisha taratibu akawa anatizama saa yake kana kwamba kuna jambo analingoja litokee muda si mrefu.
Uwanja ulikuwa umejaa watu pomoni. Vikundi mbalimbali vya wakulima na washikadau wa kilimo walikuwa tayari wameshajipanga kwa ajili ya maonyesho. Kila kitu kilikuwa kimeshajipanga kwa mujibu ya ratiba, ni waziri tu wa kilimo ndiye alikuwa anangojewa ili tafrija ipate anza.
“Sandra, Miraji, muda umewadia. Fanyeni kazi yenu sasa kabla waziri hajaingia!” Vitalis aliagiza. Baada tu ya hilo agizo mlipuko mkubwa ulitokea upande wa juu kabisa ambapo hamna watu. Watu wakaanza kukimbia huku na huko wakigombania milango ya kutokea nje.
Baada tu ya dakika chache, uwanja wote ulikuwa mweupe kasoro watu wachache mno. Vitalis pamoja na wenzake, pia Emilio, Santanna na Cruz wakiwa pamoja na kundi lao lenye watu kumi na nne – mapacha ndani. Milango yote ya uwanja ikafungwa na Miraji. Alafu sauti ya Bakari ikasema kwenye kipaza:
“Leo ni mwisho wenu, wapendwa.”
Kundi lote linalowalinda waamerika kusini likakusanyika na kuwaweka wakuu wao katikati. Lakini bado hawakujua wala kuona wanaopambana nao. Uwanja mzima walijiona wenyewe tu. Si Vitalis wala wenzake walikuwa wanaonekana wapi walipojificha.
Ni ghafla mlio wa kitu kama kamshale ukavuma. Kutizama, Pacha mmoja alikuwa amedungwa sindano mkono wake wa kuume. Punde tu, pacha huyo akalegea na kudondoka chini kama mzigo.
“Upande ulee!”
Mwanaume mmoja alielekezea kidole chake ilipotokea sindano – upande wa kulia. Wanaume watano wakaanza kukimbilia huko kabla ya sindano nyingine mbili kuruka tokea upande wa kushoto, zikawachoma mapacha wengine wawili na kuwaacha chini wamelegea.
“Upande huu!”
Mwanaume mwingine akaonyeshea kidole chake upande wa kushoto. Ila kabla hawajakimbilia huko, pacha mmoja akawaonyeshea ishara ya kuwakataza kisha akawaelekeza wajigawanye kwa kila upande. Wakafanya hivyo.
Sindano zingine tatu zilirushwa, mapacha waliobakia wakazidaka kwa mikono yao kabla hazijawakuta, wakazivunja na kuzitupilia mbali. Kisha wakakimbia haraka kufuata sehemu ambapo sindano hizo zimetokea. Huko wakakutana na Miraji upande wa kulia na Jombi upande wa kushoto wakiwa wameshikilia pinde zenye sindano.
Kabla mpambano haujajiri, taa zikazima kukawa giza. Zilipowaka zikawaka kwa fujo mno na kuwapiga usoni mapacha hao ambao walishindwa kuhimili – Vinasaba vya wanyama walivyonavyo mwilini haviwezi kustahimili mwanga mkali machoni. Kabla hawajakaa vyema walishashindiliwa sindano kwenye miili yao wakaachwa hoi hawajiwezi kwa lolote kwa chochote. Mapacha wote wakawa historia. Sasa wakabakia binadamu nane wa kawaida ambao hawakuwaumiza kichwa WAGENI kupambana nao.
Vitalis alichukua wanaume wawili, vile vile Jombi, Kaguta na Miraji. Waliwasulubu wanaume hao kwa mateke na ngumi takatifu zilizowaacha wakilowea kwenye ulimwengu mchungu wa maumivu huku hakuna yeyote miongoni mwao aliyethubutu kurusha ngumi ama teke lolote lililofanikiwa kumgusa Vitalis au wenzake.
Baada ya hapo hakukuwepo tena na kizingiti kilichosimama mbele ya WAGENI. Hakuna mwanaume yeyote aliyekuwa mbele yao isipokuwa tu wale waliowafuata: Cruz, Santanna na Emilio tena wakiwa wamevaa nyuso za hofu baada ya kuona jinsi watumishi wao walivyosambaratishwa.
“What do you want from us?”
****
☆Steve